Sura ya 28
Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
USITAWI na ukuzi wa tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova umetia ndani hali mbalimbali ambazo zimetahini sana imani ya watu mmoja-mmoja. Kama vile ambavyo kupura na kupepeta hutenganisha ngano na makapi, ndivyo hali hizo zimetumika kutambulisha wale ambao ni Wakristo halisi. (Linganisha Luka 3:17.) Watu wanaoshirikiana na tengenezo wamelazimika kudhihirisha yale yaliyo mioyoni mwao. Je, walikuwa wakitumikia tu kwa manufaa za kibinafsi? Je, walikuwa wafuasi wa binadamu fulani tu asiye mkamilifu? Au walikuwa wanyenyekevu, wenye hamu ya kujua na kufanya mapenzi ya Mungu, wakiwa kamili katika ujitoaji wao kwa Yehova?—Linganisha 2 Mambo ya Nyakati 16:9.
Wafuasi wa Yesu Kristo wa karne ya kwanza walitahiniwa imani yao pia. Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba ikiwa wangekuwa waaminifu, wangeshiriki pamoja naye katika Ufalme wake. (Mt. 5:3, 10; 7:21; 18:3; 19:28) Lakini hakuwaambia ni lini wangepokea zawadi hiyo. Iwapo wanakabiliwa na ubaridi wa umma, hata uhasama, kuelekea kuhubiri kwao, je, wangeendelea kwa uaminifu-mshikamanifu kufanya faida za Ufalme huo ziwe hangaikio lao la kwanza maishani mwao? Si kila mtu aliyefanya hivyo.—2 Tim. 4:10.
Njia ambayo Yesu mwenyewe alifundisha ilitokeza mtihani kwa wengine. Mafarisayo walikwazwa alipokataa mapokeo yao waziwazi. (Mt. 15:1-14) Hata wengi waliodai kuwa wanafunzi wa Yesu waliudhika na njia yake ya kufundisha. Katika pindi moja, alipokuwa akizungumzia umaana wa kudhihirisha imani katika thamani ya mwili na damu yake mwenyewe ikitolewa kuwa dhabihu, wengi wa wanafunzi wake walishangaa kwa sababu ya usemi wa ufananisho aliotumia. Bila kungoja wapate maelezo zaidi, “wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma wakawa hawatembei tena pamoja naye.”—Yn. 6:48-66, NW.
Lakini si wote waliogeukia mbali. Kama vile Simoni Petro alivyoeleza, “Bwana, tutaenda zetu kwa nani? Wewe una semi za uhai udumuo milele; na sisi tumeamini na tumekuja kujua kwamba wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.” (Yn. 6:67-69, NW) Walikuwa wameona na kusikia mambo ya kutosha kuweza kusadikishwa kwamba Yesu alikuwa yule ambaye kupitia kwake Mungu alikuwa akidhihirisha kweli kuhusu yeye mwenyewe na makusudi yake. (Yn. 1:14; 14:6) Hata hivyo, kutahiniwa kwa imani kuliendelea.
Baada ya kufa na kufufuliwa kwa Yesu, yeye alitumia mitume na wengine kuwa wachungaji wa kutaniko. Hao walikuwa wanaume wasio wakamilifu, na nyakati nyingine kutokamilika kwao kulikuwa jaribu kwa wale waliokuwa nao. (Linganisha Matendo 15:36-41; Wagalatia 2:11-14.) Kwa upande ule mwingine, kulikuwa na watu mmoja-mmoja waliokosa usawaziko katika kuwaheshimu Wakristo mashuhuri na kusema: “Mimi ni wa Paulo,” hali wengine walisema: “Mimi ni wa Apolo.” (1 Kor. 3:4, NW) Wote walihitaji kuwa macho ili wasikose kupata maana ya yale yaliyomaanishwa na kuwa mfuasi wa Yesu Kristo.
Mtume Paulo alitabiri kuhusu matatizo mengine makubwa, akieleza kwamba hata katika kutaniko la Kikristo watu ‘wangeinuka na kusema mambo yaliyopotoka ili kuvuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.’ (Mdo. 20:29, 30, NW) Na mtume Petro alionya kwamba walimu bandia miongoni mwa watumishi wa Mungu wangetafuta kuwapotosha wengine kwa “maneno bandia.” (2 Pet. 2:1-3, NW) Bila shaka, mitihani yenye kupekua moyo na uaminifu-mshikamanifu ilikuwa mbele.
Kwa hiyo, kutahiniwa na kupepetwa ambako ni sehemu ya historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova hakushangazi. Lakini wengi wameshangaa kuhusu wale waliojikwaa na sababu ya wao kukwazwa ni nini.
Je, Walithamini Fidia Kikweli?
Wakati wa miaka ya mapema ya 1870, Ndugu Russell na washiriki wake walikua katika ujuzi na uthamini wa kusudi la Mungu. Huo ulikuwa wakati wa kuburudishwa kwao kiroho. Lakini, katika 1878, walikabiliwa na mtihani mkubwa wa imani yao na uaminifu-mshikamanifu wao kwa Neno la Mungu. Suala lilikuwa juu ya thamani ya dhabihu ya mwili na damu ya Yesu—fundisho lilelile ambalo wengi wa wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza walijikwaa kwalo.
Ilikuwa miaka miwili tu kabla ya hilo, katika 1876, kwamba C. T. Russell alikuwa ameingia katika uhusiano wa kikazi na N. H. Barbour wa Rochester, New York. Vikundi vyao vya funzo viliungana. Russell alikuwa ameandaa fedha ili kufufua uchapaji wa gazeti la Barbour Herald of the Morning, Barbour akiwa mhariri na Russell akiwa mhariri-msaidizi. Walikuwa pia wametokeza pamoja kitabu chenye kichwa Three Worlds, and the Harvest of This World.
Kisha jambo la kushtusha likatukia! Katika toleo la Agosti 1878 la Herald of the Morning, Barbour aliandika makala fulani ambayo alijulisha kuwa maandiko kama vile 1 Petro 3:18 na Isaya 53:5, 6, pia Waebrania 9:22, hayana maana na akajulisha kuwa wazo lote kwamba Kristo alikufa ili alipie dhambi zetu lilichukiza sana. Russell baadaye aliandika: “Kwa mshangao wetu wenye kutia uchungu, Bw. Barbour . . . aliandika makala katika Herald akikataa fundisho la kulipia—akikataa kwamba kifo cha Kristo kilikuwa bei ya fidia ya Adamu na jamii yake, akisema kwamba kifo cha Kristo hakingeweza kulipia adhabu ya dhambi ya mwanadamu kama vile kuchomelea pini katika mwili wa inzi na kufanya ahisi uchungu na afe kusingefikiriwa na mzazi wa kidunia kuwa malipo yanayostahili kwa kosa la mwanae.”a
Hilo lilikuwa jambo la maana sana. Je, Ndugu Russell angeshikamana kwa uaminifu-mshikamanifu na yale ambayo Biblia ilikuwa imesema waziwazi kuhusu uandalizi wa Mungu kwa ajili ya ukombozi wa wanadamu? Au angeongozwa na falsafa za kibinadamu? Ingawa Russell alikuwa mwenye miaka 26 tu wakati huo na Barbour alikuwa mwanamume mwenye umri mkubwa zaidi, Russell aliandika kwa ujasiri makala moja kwa ajili ya toleo lililofuata la Herald ambalo kwalo alitetea sana thamani ya damu ya Kristo yenye kulipia dhambi, ambayo alirejezea kuwa “mojawapo mafundisho yaliyo ya maana zaidi ya Neno la Mungu.”
Kisha, alimwomba J. H. Paton, mhariri-msaidizi mwingine wa Herald, aandike makala moja kwa kuunga mkono imani katika damu ya Kristo ikiwa msingi wa kulipia dhambi. Paton aliandika makala hiyo, na ilitangazwa katika toleo la Desemba. Baada ya jitihada za kurudia zisizofanikiwa za kutoa sababu juu ya jambo hilo na Barbour kwa kutumia Maandiko, Russell aliacha kushirikiana naye na akaacha kutegemeza gazeti lake kifedha. Katika Julai 1879, Russell alianza kutangaza gazeti jipya—Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence—ambalo kuanzia mwanzoni lilikuwa mtetezi wa pekee wa fidia. Lakini matatizo hayakuishia hapo.
Miaka miwili baadaye, Paton, aliyekuwa akitumikia akiwa mwakilishi anayesafiri wa Watch Tower, pia alianza kuasi tengenezo, na baadaye akatangaza kitabu (chake cha pili chenye kichwa Day Dawn) ambacho kwacho alikataa itikadi ya kuanguka kwa Adamu katika dhambi na hivyo kukawa hakuna uhitaji wa kuwa na mkombozi. Alitoa sababu kwamba Bwana mwenyewe alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu ambaye kwa maisha yake alionyesha tu wengine jinsi ya kusulubisha maelekeo yao ya dhambi. Katika 1881, A. D. Jones, mshiriki mwingine, alianzisha gazeti (Zion’s Day Star) lililofanana na Watch Tower lakini lenye wazo kwamba lingezungumza juu ya mambo rahisi zaidi ya kusudi la Mungu. Mwanzoni ilionekana kana kwamba mambo yote yalikuwa sawa. Na bado, katika muda wa mwaka mmoja, gazeti la Jones lilikuwa limekataa dhabihu yenye kulipia ya Kristo, na katika muda wa mwaka mwingine mmoja, lilikuwa limekataa Biblia yote. Ni nini kilichokuwa kimewapata watu hao? Walikuwa wameruhusu nadharia za kibinafsi na mavutio ya falsafa za wanadamu zinazopendwa na wengi ziwakengeushe kutoka kwenye Neno la Mungu. (Linganisha Wakolosai 2:8.) Gazeti lililotangazwa na A. D. Jones liliendelea kwa muda mfupi tu na kisha likafifilia mbali. J. H. Paton aliamua kutangaza gazeti ambalo kwalo aliandika gospeli kama alivyoiona, lakini usambazaji walo ulikuwa mdogo.
Ndugu Russell alihangaishwa sana kuhusu matokeo ya hayo yote juu ya wasomaji wa Watch Tower. Aling’amua kwamba hilo lilitahini imani ya kila mmoja. Alijua vema kwamba wengine walifikiri uchambuzi wake wa mafundisho yasiyo ya kimaandiko ulisababishwa na roho ya ushindani. Lakini Ndugu Russell hakujitafutia wafuasi. Kuhusu yale yaliyokuwa yakitukia, yeye aliandika: “Kusudi la kutahini na kupepeta huku kwa wazi ni kuteua wote ambao tamaa zao za moyoni si za kichoyo, ambao wamejitakasa kabisa kwa Bwana bila masharti, ambao wanahangaikia sana kuona mapenzi ya Bwana yakifanywa, na ambao uhakika wao kwa hekima yake, njia yake, na Neno lake ni mkubwa sana, hivi kwamba wanakataa kuvutwa kutoka kwenye Neno la Bwana, ama kwa madanganyo ya wengine, ama kwa mipango na mawazo yao wenyewe.”
Je, Mungu Alikuwa Akitumia Mfereji Unaoonekana?
Bila shaka, kuna matengenezo mengi ya kidini, na idadi kubwa ya walimu hutumia Biblia kwa kiasi fulani. Je, Mungu alikuwa akimtumia Charles Taze Russell kihususa? Ikiwa ndivyo, je, Mungu aliacha kuwa na mfereji unaoonekana wakati Ndugu Russell alipokufa? Hayo yalikuja kuwa masuala ya maana, ambayo yaliongoza kwenye kutahiniwa na kupepetwa zaidi.
Bila shaka haingetazamiwa kwamba Mungu angemtumia C. T. Russell ikiwa hangeshikamana kwa uaminifu-mshikamanifu na Neno la Mungu. (Yer. 23:28; 2 Tim. 3:16, 17) Mungu hangemtumia mwanadamu ambaye alijizuia kwa woga asihubiri yale aliyoona yameandikwa waziwazi katika Maandiko. (Eze. 2:6-8) Wala Mungu hangemtumia mtu ambaye angetumia ujuzi wake wa Maandiko ili kujiletea utukufu. (Yn. 5:44) Kwa hiyo, mambo ya hakika yanaonyesha nini?
Mashahidi wa Yehova leo wanapopitia kazi ambayo alifanya, mambo aliyofundisha, sababu ya yeye kuyafundisha, na matokeo yayo, hawana shaka kwamba Charles Taze Russell alitumiwa kikweli na Mungu kwa njia ya pekee na katika wakati wa maana.
Maoni hayo hayategemei tu msimamo imara ambao Ndugu Russell alichukua kuhusu fidia. Yanatia ndani pia uhakika wa kwamba yeye bila kuogopa alikataa mafundisho ambayo yalitia ndani baadhi ya itikadi za msingi za Jumuiya ya Wakristo, kwa sababu hizo zilipingana na Maandiko yaliyopuliziwa. Itikadi hizo zilitia ndani fundisho la Utatu (ambalo shina lalo lilikuwa katika Babiloni wa kale na halikutumiwa na wale waitwao eti Wakristo hadi muda mrefu baada ya uandikaji wa Biblia kukamilishwa) pamoja na fundisho kwamba nafsi za wanadamu haziwezi kufa kiasili (ambalo lilikuwa limetumiwa na watu waliovutiwa kupita kiasi na falsafa ya Plato na ambalo liliwafanya wakubali mawazo kama vile mateso ya milele ya nafsi katika moto wa helo). Wasomi wengi pia wa Jumuiya ya Wakristo, wanajua kwamba mafundisho hayo hayafundishwi katika Biblia,b lakini kwa kawaida wahubiri hawasemi hivyo wakiwa kwenye mimbari. Kwa kutofautisha, Ndugu Russell alianza kampeni kubwa ya kushiriki na kila mtu aliyependa kusikia yale ambayo Biblia husema hasa.
Yenye kutokeza pia ni yale ambayo Ndugu Russell alifanya na kweli nyinginezo zenye umaana mkubwa ambazo alijifunza kutoka kwa Neno la Mungu. Alitambua kwamba Kristo angerudi akiwa mtu wa roho aliye mtukufu, asiyeonekana kwa macho ya kibinadamu. Mapema kama 1876, alitambua kwamba mwaka 1914 ungetia alama mwisho wa Nyakati za Mataifa. (Luka 21:24, KJ) Vivyo hivyo, wasomi wengine wa Biblia walikuwa wameng’amua baadhi ya mambo hayo na walikuwa wameyatetea. Lakini Ndugu Russell alitumia mali zake zote ili kuyatangaza kimataifa kwa kiwango kisichopata kufanywa na mtu au kikundi kinginecho wakati huo.
Aliwahimiza wengine walinganishe kwa uangalifu maandishi yake na yale ya Neno lililopuliziwa la Mungu ili kwamba waridhike kwamba yale waliyokuwa wakijifunza yalipatana kikamili nalo. Akimjibu mmoja aliyeandika barua ya kuulizia, Ndugu Russell alijibu: “Ikiwa ilifaa kwa Wakristo wa mapema kuthibitisha yale waliyopokea kutoka kwa mitume, ambao walikuwa wamepuliziwa na walidai hivyo, ni kwa maana kadiri kubwa jinsi gani kwamba wewe ujiridhishe mwenyewe kikamili kwamba mafundisho hayo yanakamatana kwa ukaribu na maagizo ya mitume yaliyoonyeshwa na yale ya Bwana wetu;—kwa kuwa mtungaji wayo hadai kuwa amepuliziwa, bali adai tu kuhusu mwongozo wa Bwana, kuwa anaongozwa naye katika kulisha kundi lake.”
Ndugu Russell hakudai kuwa na uwezo usio wa kawaida, wala mafunuo ya kimungu. Yeye hakudai sifa kwa yale aliyofundisha. Alikuwa mwanafunzi wa Biblia mwenye kutokeza. Lakini alieleza kwamba uelewevu wake wenye kutokeza wa Maandiko ulikuwa kwa sababu ‘ya uhakika tu wa kwamba wakati wa Mungu uliowekwa ulikuwa umefika.’ Yeye alisema: “Kama mimi nisingesema, na hakukupatikana wakili mwingine, mawe yenyewe yangepiga kelele.” Alijirejezea kuwa kama kidole cha shahada tu, akielekeza kwa yale yaliyoandikwa katika Neno la Mungu.
Charles Taze Russell hakutaka utukufu kutoka kwa wanadamu. Ili kurekebisha kufikiri kwa wowote ambao walielekea kumpa heshima kupita kiasi, Ndugu Russell aliandika, katika 1896: “Kwa vile kwa kadiri fulani, tumetumiwa katika huduma ya gospeli kwa neema ya Mungu, inafaa kusema hapa yale ambayo tumeyasema mara nyingi faraghani, na katika safu hizi hapo awali,—yaani, kwamba ingawa tunathamini upendo, huruma, tumaini na ushirikiano wa watumishi wenzetu na wa nyumba yote ya imani, hatutaki heshima kuu, na kicho, kuelekea sisi au maandishi yetu; wala hatutaki kuitwa Muadhama au Rabi. Wala hatutaki kwamba kikundi chochote cha kidini kiitwe kwa jina letu.”
Kifo chake kilipokaribia, yeye hakuwa na maoni kwamba hakukuwa na mambo mengine ya kujifunza, kwamba hakukuwa na kazi zaidi ya kufanywa. Alikuwa amesema mara nyingi juu ya kutayarisha buku la saba la Studies in the Scriptures. Alipoulizwa kulihusu kabla ya kifo chake, alimwambia Menta Sturgeon mwandamani wake: “Mtu mwingine aweza kuliandika.” Katika wasia wake alionyesha tamaa kwamba The Watch Tower liendelee kutangazwa chini ya mwelekezo wa halmashauri ya wanaume waliojitoa kabisa kwa Bwana. Alisema kwamba wale ambao wangetumikia hivyo wangekuwa wanaume “waaminifu-washikamanifu kabisa kwa mafundisho ya Maandiko—hasa kuhusiana na fundisho la Fidia—kwamba hakuna kukubaliwa na Mungu na hakuna wokovu kwenye uhai wa milele isipokuwa kupitia imani katika Kristo na utii kwa Neno Lake na roho yalo.”
Ndugu Russell aling’amua kwamba bado kulikuwa na kazi nyingi ya kufanywa katika kuhubiri habari njema. Kwenye kipindi cha maswali na majibu katika Vancouver, B.C., Kanada, katika 1915, aliulizwa ni lini wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta kwa roho walioishi wakati huo wangetarajia kupokea zawadi yao ya kimbingu. Yeye alijibu: “Mimi sijui, lakini kuna kazi kubwa ya kufanywa. Itahitaji maelfu ya akina ndugu na mamilioni ya fedha ili kuifanya. Mahali ambapo hayo yatatoka mimi sijui—Bwana ajua yale yanayomhusu.” Kisha, katika 1916, muda mfupi kabla ya kuanza safari ya kutoa hotuba ambapo alikufa, alimwita A. H. Macmillan, msimamizi-msaidizi, kwenye ofisi yake. Katika pindi hiyo alisema: “Mimi siwezi kuendelea zaidi na kazi, na bado kuna kazi kubwa ya kufanywa.” Kwa muda wa saa tatu alimwelezea Ndugu Macmillan juu ya kazi kubwa ya kuhubiri ambayo aliona mbele, kwa msingi wa Maandiko. Ndugu Macmillan alipopinga, yeye alijibu: “Hii si kazi ya mwanadamu.”
Badiliko Katika Usimamizi Latahini Sana
Washiriki wengi wa Ndugu Russell walisadiki sana kwamba Bwana alisimamia mambo. Kwenye maziko ya Ndugu Russell, W. E. Van Amburgh alisema: “Mungu ametumia watumishi wengi katika wakati uliopita na Yeye bila shaka atatumia wengi wakati ujao. Kujitakasa kwetu si kwa mtu fulani, au kwa kazi ya mtu, bali kwa kufanya mapenzi ya Mungu, kama vile Yeye atakavyoyafunua kwetu kupitia Neno Lake na miongozo yake ya kimungu. Mungu angali aelekeza mambo.” Ndugu Van Amburgh hakutikisika kamwe katika usadikisho huo hadi kufikia kifo chake.
Hata hivyo, kwa kusikitisha, kulikuwa na wengine waliodai kumheshimu Russell lakini waliodhihirisha roho tofauti. Kama tokeo, hali zilizobadilika baada ya kifo cha Russell zilitokeza kutahini na kupepeta. Vikundi vya waasi-imani vilitokea si katika Marekani tu bali pia katika Belfast, Ireland; katika Copenhagen, Denmark; katika Vancouver na Viktoria, British Columbia, Kanada; na katika sehemu nyinginezo. Katika Helsinki, Finland, wengine walikuwa na maoni kwamba baada ya kifo cha Russell hakukuwa tena na mfereji wa nuru ya kiroho. Baada ya kuhimizwa na watu fulani mashuhuri, 164 waliacha tengenezo huko. Je, hilo lilikuwa na baraka ya Mungu? Kwa muda fulani walichapa gazeti lao wenyewe na kufanya mikutano yao wenyewe. Hata hivyo, baadaye kikundi hicho kiligawanyika, kikafifia, na kikaacha kuwako; na wengi wao walifurahi kurudi kwenye mikutano ya Wanafunzi wa Biblia. Hata hivyo, si wote waliorudi.
Kifo cha Ndugu Russell, pamoja na matukio yaliyofuata, pia kilikuwa mtihani kwa R. E. B. Nicholson, mwandishi wa ofisi ya tawi ya Australia, na kulimfanya adhihirishe yale yaliyokuwa moyoni mwake. Baada ya kifo cha Russell, Nicholson aliandika: “Kwa zaidi ya robo karne nimempenda, si kwa ajili ya kazi yake tu, bali pia kwa ajili ya tabia yake njema, nimeshangilia katika kweli ambazo amepeleka zikiwa kama ‘nyama kwa wakati unaofaa,’ na katika shauri lake, nikiheshimu utu wa huruma, fadhili, na upendo uliochanganywa vizuri na uhodari na jitihada za bidii kufanya kitu chochote na kuwa na ujasiri ili kutimiza yale aliyoamini kuwa mapenzi ya Kimungu au kufunguka kwa Neno Lake. . . . Kuna hisi ya upweke mtu anapong’amua kwamba utegemezo huo wenye nguvu hauko hai tena.”
Joseph F. Rutherford, msimamizi mpya wa Watch Tower Society, hakuwa aina ya mtu ambaye Nicholson alifikiri alipaswa kuwa na daraka la usimamizi ambalo Ndugu Russell alikuwa nalo. Nicholson akawa mchambuzi wa waziwazi kuhusu njia ya moja kwa moja ambayo habari mpya ya funzo la Biblia ilishutumu dini bandia. Kabla ya muda mrefu kupita aliacha tengenezo, na akaondoka na mali nyingi ya Sosaiti (ambayo alikuwa amesajilisha kwa jina lake mwenyewe) na wale walioko Melbourne ambao, hao nao walikuwa na mwelekeo wa kumtegemea. Kwa nini ilitukia hivyo? Inaonekana kwamba Nicholson alikuwa amejiruhusu kuwa mfuasi wa mtu; hivyo, mtu huyo alipokufa, unyoofu wa Nicholson na bidii katika kumtumikia Bwana vikapoa. Hakuna yeyote kati ya wale waliokengeuka wakati huo aliyesitawi. Hata hivyo, inafaa kuangalia kwamba, Jane Nicholson, ingawa ana umbo mdogo, hakujiunga na mume wake katika kukengeuka kwake. Ujitoaji wake ulikuwa kwanza kwa Yehova Mungu, naye aliendelea kumtumikia wakati wote hadi kufikia kifo chake katika 1951.
Wengi walitambua kwamba yale yaliyokuwa yakitukia katika miaka iliyofuata kifo cha Ndugu Russell yalikuwa yakitimiza mapenzi ya Bwana. Mmoja wa watumishi wa Yehova katika Kanada aliandika kuhusu hilo kwa Ndugu Rutherford akisema:
“Ndugu Mpendwa, usinielewe vibaya sasa ninapokuandikia yale ninayokuandikia. Tabia yako na ile ya mpendwa Ndugu Russell zinatofautiana sana kama vile mchana na usiku. Wengi, ole wao, wengi sana, walimpenda Ndugu Russell kwa sababu ya utu wake, tabia, n.k.; na watu wachache sana walimpinga yeye. Wengi walikubali kweli kwa sababu tu Ndugu Russell alisema hivyo. Kisha, wengi wakaanza kumwabudu mtu huyo . . . Unakumbuka wakati ambapo Ndugu Russell alizungumza waziwazi kwenye mkusanyiko kuhusu kosa hilo la ndugu wengi wenye makusudi mazuri, akitegemeza hotuba yake kwenye Yohana na malaika. (Ufunuo 22:8, 9) Alipokufa tunajua sote kile kilichotukia.
“Lakini wewe Ndugu Rutherford, una tabia ambayo haiwezi kulinganishwa na ile ya Ndugu Russell. Hata sura yako ni tofauti. Si kosa lako. Ilikuwa zawadi yako ya siku uliyozaliwa, na hungeweza kuikataa. . . . Tangu ulipowekwa uongoze mambo ya SOSAITI, umepata uchambuzi usio wa haki na masingizio mabaya zaidi, yote hayo yakifanywa na akina ndugu. Na bado yajapokuwa hayo yote umekuwa mwaminifu-mshikamanifu na mwenye kujitoa kwa Bwana mpendwa na kwenye agizo lake lililorekodiwa katika Isaya 61:1-3. Je, Bwana alijua yale aliyokuwa akifanya alipokuweka uongoze mambo? Bila shaka alijua. Wakati uliopita sote tulielekea kuabudu kiumbe zaidi ya Muumba. Bwana alijua hilo. Kwa hiyo aliweka kiumbe chenye tabia tofauti ili kiongoze mambo, au ninapaswa kusema kisimamie kazi, ile kazi ya mavuno. Wewe hutaki mtu yeyote akuabudu. Mimi ninajua hilo, lakini kwa kweli unataka kwamba wote wenye imani ileile yenye thamani waonee shangwe nuru ambayo inaangaza sasa kwenye kijia cha wenye haki, kama vile Bwana aonavyo kuwa yafaa kwayo kuangaza. Na hilo ndilo Bwana ataka lifanywe.”
Kuelewesha Wazi Utambulisho wa “Mtumishi Mwaminifu na Mwenye Hekima”
Wengi waliopepetwa nje wakati huo walishikilia maoni ya kwamba mtu mmoja, Charles Taze Russell, alikuwa “mtumishi mwaminifu na mwenye hekima” aliyetabiriwa na Yesu kwenye Mathayo 24:45-47 (KJ), ambaye angegawanya chakula cha kiroho kwa nyumba ya imani. Hasa kufuatia kifo chake, The Watch Tower lenyewe lilijulisha maoni hayo kwa miaka kadhaa. Kwa kufikiria daraka kubwa ambalo Ndugu Russell alikuwa nalo, ilionekana kwa Wanafunzi wa Biblia wa wakati huo kwamba mambo yalikuwa hivyo. Yeye binafsi hakuendeleza wazo hilo, lakini alikubali yale yaliyoonekana kuwa mambo ya akili ya hoja hizo za wale waliozipendelea.c Hata hivyo, yeye alikazia pia kwamba, mtu yeyote ambaye Bwana angetumia katika daraka hilo lazima awe mnyenyekevu na mwenye bidii ili amletee Bwana Mkubwa utukufu, na kwamba ikiwa yule aliyechaguliwa na Bwana angeshindwa, mahali pake pangechukuliwa na mwingine.
Hata hivyo, kadiri nuru ya kweli ilivyong’aa kwa kuendelea kwa uangavu mkubwa zaidi baada ya kifo cha Ndugu Russell, na kuhubiri ambako Yesu alikuwa ametabiri kulipoenea kwa kadiri kubwa zaidi, ikawa wazi kwamba “mtumishi mwaminifu na mwenye hekima” (KJ), au “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” (NW), hakuwa ametoweka Ndugu Russell alipokufa. Katika 1881, Ndugu Russell mwenyewe alikuwa ametoa maoni kwamba “mtumishi” huyo alifanyizwa na baraza lote la Wakristo watiwa-mafuta kwa roho walio waaminifu. Alikuwa na maoni kwamba alikuwa mtumishi anayetia ndani watu wengi, jamii ya watu walioungana kufanya mapenzi ya Mungu. (Linganisha Isaya 43:10.) Uelewevu huo ulihakikishwa tena na Wanafunzi wa Biblia katika 1927. Mashahidi wa Yehova leo wanatambua gazeti The Watch Tower na vichapo vingine vinavyohusiana kuwa vile vinavyotumiwa na mtumwa mwaminifu na mwenye busara katika kutoa chakula cha kiroho. Hawadai kwamba jamii hiyo ya mtumwa haiwezi kukosea, bali wao huiona kuwa mfereji mmoja ambao Bwana anatumia wakati wa siku za mwisho za mfumo huu wa mambo.
Wakati Kiburi Kilipokuwa Kizuizi
Hata hivyo, kulikuwa na nyakati ambapo, watu mmoja-mmoja wenye madaraka walipokuja kujiona kuwa mfereji wa nuru ya kiroho, hivi kwamba wakapinga yale yaliyoandaliwa na tengenezo. Wengine walishindwa na tamaa ya kuwa na uvutano mkubwa zaidi wa kibinafsi. Walitaka wengine wawafuate, au, kama vile mtume Paulo alivyosema, ‘wawavute wanafunzi wawafuate wao wenyewe.’ (Mdo. 20:29, 30, NW) Bila shaka, hilo lilitahini makusudi na msimamo wa kiroho wa wale ambao walijaribu kuwashawishi. Fikiria mifano fulani:
Barua za pekee kwa Wanafunzi wa Biblia katika Allegheny, Pennsylvania, ziliwaalika kwenye mkutano katika Aprili 5, 1894. Ndugu na Dada Russell hawakualikwa na hawakuhudhuria, lakini wengine karibu 40 walihudhuria. Barua hiyo, iliyotiwa sahihi na E. Bryan, S. D. Rogers, J. B. Adamson, na O. von Zech, ilisema kwamba mkutano ungetia ndani mambo yanayohusu “hali njema [yao] iliyo bora sana.” Zilithibitika kuwa jitihada zenye kudhuru za watu hao wenye hila ili kutia sumu akili za wengine kwa kufunua yale waliyoona kuwa mabaya katika shughuli za kibiashara za Ndugu Russell (ingawa mambo ya hakika yalionyesha mambo tofauti), kwa kutoa hoja kwamba Ndugu Russell alikuwa na mamlaka makubwa zaidi (ambayo walitaka wao wenyewe wawe nayo), na kwa kulalamika kwa sababu alipendelea kutumia fasihi ili kueneza gospeli na mikutano ya madarasa ya Biblia badala ya kutoa hotuba tu (ambapo wangeweza kutoa maoni ya kibinafsi kwa urahisi zaidi). Kutaniko liliathiriwa sana na yale yaliyotukia, na wengi walikwazwa. Lakini wale waliokengeuka hawakuja kuwa watu wa kiroho zaidi au wenye bidii zaidi katika kazi ya Bwana.
Zaidi ya miaka 20 baadaye, kabla ya kifo chake, Ndugu Russell alieleza kusudi lake la kumtuma Paul S. L. Johnson, msemaji mwenye uwezo sana, hadi Uingereza ili aimarishe Wanafunzi wa Biblia huko. Kwa sababu ya kuheshimu takwa la Ndugu Russell, Sosaiti ilimtuma Johnson hadi Uingereza katika Novemba 1916. Hata hivyo, mara tu alipofika Uingereza, alifukuza wasimamizi wawili wa Sosaiti. Huku akijiona mwenyewe kuwa mtu wa maana, alitoa hoja katika hotuba na barua kwamba yale aliyokuwa akifanya yalitangulia kuwekewa kivuli na Maandiko ya Ezra, Nehemia, na Mordekai. Alijidai kuwa ndiye yule mtumishi (au, mwanamume msimamizi) aliyerejezewa na Yesu katika kielezi chake kwenye Mathayo 20:8. Alijaribu kusimamia fedha za Sosaiti, na akapeleka mashtaka katika Mahakama Kuu ya London ili atimize malengo yake.
Aliposhindwa katika jitihada zake, alirudi New York. Huko alitafuta kuungwa mkono na watu fulani waliokuwa wakitumikia kwenye baraza la waelekezi la Sosaiti. Wale waliosadikishwa kukubaliana naye walijitahidi kutimiza malengo yao kwa kujaribu kupitisha azimio ili kukinza sheria za Sosaiti zilizompa msimamizi mamlaka ya kuongoza mambo yayo. Walitaka wawe na uwezo wa kufanya maamuzi yote. Hatua ya kisheria ilichukuliwa na Ndugu Rutherford ili kulinda salama masilahi ya Sosaiti, na wale waliokuwa wakitafuta kuharibu kazi yayo waliombwa waondoke kwenye Kao la Betheli. Kwenye mkutano wa kila mwaka wa wenye hisa wa Sosaiti mapema mwaka uliofuata, wakati baraza la waelekezi na maofisa walo walipochaguliwa kwa mwaka ambao ungefuata, wale waliokuwa wachochezi walikataliwa kabisa. Labda baadhi yao walifikiri kwamba hawakukosea, lakini wengi wa ndugu zao wa kiroho walidhihirisha kwamba hawakukubali. Je, wangekubali karipio hilo?
Baada ya hapo, P. S. L. Johnson alitokea kwenye mikutano ya Wanafunzi wa Biblia akifanya ionekane kwamba alikubaliana na itikadi na utendaji wao. Lakini baada ya kuungwa mkono na wengine, angepanda mbegu za shaka. Ikiwa yeyote angedokeza kujitenga na Sosaiti, alikataza hilo kinafiki—hadi uaminifu-mshikamanifu wa kikundi ulipofifia kabisa. Alijitahidi kuwavuta akina ndugu kwa kutumia barua na hata kwa safari za kibinafsi, si katika Marekani tu, bali pia katika Kanada, Jamaika, Ulaya, na Australia. Je, hilo lilifanikiwa?
Labda ilionekana hivyo wakati walio wengi katika kutaniko moja walipoamua kukatisha uhusiano na Sosaiti. Lakini walikuwa kama tawi lililokatwa kutoka kwa mti—kijani kibichi kwa muda, kisha lililofifia na lisilo na uhai. Wapinzani walipofanya mkusanyiko katika 1918, tofauti zilitokea, na kukawa na mgawanyiko. Mgawanyiko zaidi ulifuata. Wengine waliendelea kwa muda wakiwa mafarakano madogo yenye viongozi waliowaheshimu. Hakuna yoyote kati ya hayo yaliyojitoa kwa kazi ya kutoa ushahidi hadharani katika dunia yote inayokaliwa kuhusu Ufalme wa Mungu, ambayo ni kazi ambayo Yesu aliwagawia wafuasi wake.
Mambo hayo yalipotokea, ndugu walijikumbusha yale yaliyorekodiwa kwenye 1 Petro 4:12 (NW): “Wapendwa, msitatanishwe juu ya kuwaka miongoni mwenu, ambako kunatukia kwenu kuwa jaribu, kama kwamba jambo geni linawapata.”
Wale waliotajwa juu si ndio pekee walioruhusu kiburi kidhoofishe imani yao. Wengine walifanya hivyo pia, kutia na Alexandre Freytag, meneja wa ofisi ya tawi ya Sosaiti ya Geneva, Uswisi. Alipenda kuvuta uangalifu kwake mwenyewe, angeongeza mawazo yake mwenyewe alipotafsiri vichapo vya Sosaiti kwa Kifaransa, na hata akatumia vifaa vya Sosaiti ili kuchapa habari yake mwenyewe. Katika Kanada, kulikuwa na W. F. Salter, meneja wa tawi la Sosaiti ambaye alianza kupinga fasihi za Sosaiti, alijulisha kwamba alitazamia kuwa msimamizi atakayefuata wa Watch Tower Society, na, baada ya kufukuzwa, akatumia barua za Sosaiti isivyo haki kuagiza makutaniko katika Kanada na nchi za kigeni yajifunze habari ambayo yeye mwenyewe alikuwa ameandika. Katika Nigeria, kulikuwa na G. M. Ukoli miongoni mwa wengine ambaye, mwanzoni alionyesha bidii kwa ajili ya kweli lakini akaanza kuiona kuwa njia ya kupata faida za kimwili na cheo cha kibinafsi. Baadaye, malengo yake yaliposhindwa, alianza kuwachambua ndugu waaminifu katika magazeti ya habari. Na kulikuwa na wengine.
Hata katika miaka ya karibuni, watu mmoja-mmoja waliokuwa na madaraka makubwa ya usimamizi walionyesha roho iyo hiyo.
Bila shaka, watu hao kwa kweli walikuwa na uhuru wa kuamini yale waliyochagua. Lakini mtu yeyote anayetetea maoni yaliyo tofauti na yale yaliyo katika vichapo vya tengenezo fulani hadharani au faraghani na ambaye anafanya hivyo hali akidai kuwakilisha tengenezo hilo, husababisha mgawanyiko. Mashahidi wa Yehova walishughulikiaje hali hizo?
Hawakuanzisha kampeni ya mnyanyaso dhidi ya watu hao (ingawa mara nyingi wale waliojitenga waliwatenda vibaya wale waliokuwa ndugu zao wa kiroho), wala hawakutaka kuwaumiza kimwili (kama ilivyofanywa na Kanisa Katoliki kupitia Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini). Badala yake, walifuata shauri lililopuliziwa la mtume Paulo, aliyeandika: “Mfulize kuangalia wale wasababishao migawanyiko na sababu za kukwaza kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, na mwaepuke. Kwa maana watu wa namna hiyo ni watumwa, si wa Bwana wetu Kristo . . . Kwa maongezi laini na usemi wa kusifu-sifu wao hushawishi mioyo ya wasio na hila.”—Rum. 16:17, 18, NW.
Wengine walipotazama yale yaliyokuwa yakitukia, wao pia walipewa fursa ya kudhihirisha yale yaliyokuwa mioyoni mwao.
Maoni ya Mafundisho Yaliyohitaji Kurekebishwa
Mashahidi wa Yehova hukubali waziwazi kwamba uelewevu wao wa kusudi la Mungu umepata marekebisho mengi kwa muda wa miaka. Jambo la kwamba ujuzi wa kusudi la Mungu ni wenye kuendelea lamaanisha kwamba ni lazima kuwe na badiliko. Si kwamba kusudi la Mungu hubadilika, lakini nuru ya elimu anayowapa watumishi wake kila wakati hutaka kuwe na marekebisho katika maoni yao.
Kutoka kwa Biblia Mashahidi huonyesha kwamba hilo lilikuwa kweli pia kuhusu watumishi waaminifu wa Mungu wakati uliopita. Abrahamu alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova; lakini alipoondoka Uru, mwanamume huyo wa imani hakujua nchi ambayo Mungu alikuwa akimwelekeza, na kwa miaka mingi hakuwa na uhakika kabisa jinsi Mungu angetimiza ahadi yake ya kufanyiza taifa kubwa kutoka kwake. (Mwa. 12:1-3; 15:3; 17:15-21; Ebr. 11:8) Mungu alifunua kweli nyingi kwa manabii, lakini kulikuwa na mambo mengine ambayo hawakuelewa wakati huo. (Dan. 12:8, 9; 1 Pet. 1:10-12) Vivyo hivyo, Yesu aliwaeleza mitume wake mambo mengi, lakini hata mwishoni mwa maisha yake ya kidunia aliwaambia kwamba bado kulikuwa na mambo mengi ya wao kujifunza. (Yn. 16:12) Baadhi ya mambo hayo, kama vile kusudi la Mungu kuwaleta Watu wa Mataifa katika kutaniko, hayakueleweka hadi mitume walipoona yale yaliyokuwa yakitukia hasa katika kutimiza unabii.—Mdo. 11:1-18.
Kama vile inavyoweza kutazamiwa, wakati mabadiliko yametaka kutupilia mbali maoni yaliyopendelewa hapo kwanza, hilo limetahini wengine. Isitoshe, si marekebisho yote katika uelewevu yamekuja mara moja tu. Kwa sababu ya kutokamilika, nyakati nyingine kuna mwelekeo wa kupita kiasi kabla ya msimamo sahihi kujulikana. Hilo laweza kuchukua wakati. Wengine walio na mbetuko wa kuwa wachambuzi wamejikwaa juu ya hilo. Fikiria kielelezo kimoja:
Mapema kama 1880, vichapo vya Watch Tower vilizungumzia mambo mbalimbali yanayohusiana na agano la Kiabrahamu, agano la Sheria, na agano jipya. Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imesahau ahadi ya Mungu kwamba kupitia mbegu ya Abrahamu familia zote za dunia kwa kweli zingejibarikia zenyewe. (Mwa. 22:18) Lakini Ndugu Russell alipendezwa sana na kujua jinsi Mungu angelitimiza hilo. Alidhani aliona katika maelezo ya Biblia ya Siku ya Ufuniko ya Wayahudi juu ya jinsi hilo lingetimizwa kuhusiana na agano jipya. Katika 1907, wakati maagano hayohayo yalipozungumzwa tena, mkazo wa pekee ukiwekwa kwenye jukumu la warithi-washirika wa Kristo katika kuletea wanadamu baraka zilizotabiriwa katika agano la Kiabrahamu, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia waliteta vikali.
Wakati huo kulikuwa na vipingamizi fulani kuhusiana na uelewevu mzuri wa mambo. Wanafunzi wa Biblia bado hawakuona kwa usahihi msimamo ambao Israeli wa asili alikuwa nao kuhusiana na kusudi la Mungu. Kizuizi hicho hakikuondolewa hadi ilipodhihirika waziwazi kwamba Wayahudi wakiwa watu hawakupendezwa kutumiwa na Mungu katika kutimiza neno lake la unabii. Kizuizi kingine kilikuwa kule kutoweza kwa Wanafunzi wa Biblia kutambulisha kwa usahihi “umati mkubwa” wa Ufunuo 7:9, 10. (NW) Utambulisho huo haukuwa wazi hadi umati mkubwa ulipoanza hasa kujidhihirisha wenyewe katika kutimiza unabii. Wale waliomchambua sana Ndugu Russell hawakuelewa mambo hayo pia.
Hata hivyo, kwa uwongo, wale waliodai kuwa ndugu Wakristo walishtaki kwamba The Watch Tower lilikuwa limekana kwamba Yesu siye Mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu, kwamba lilikuwa limeikataa katakata fidia na kukana uhitaji na uhakika wa kulipia (kufunika) dhambi. Hakuna lolote la mambo hayo lililokuwa la kweli. Lakini baadhi ya wale walioyasema walikuwa watu mashuhuri, na wakawavuta wengine baada yao kuwa wanafunzi. Huenda hawakukosea katika baadhi ya mambo waliyofundisha kuhusiana na agano jipya, lakini je, Bwana alibariki yale waliyokuwa wakifanya? Kwa wakati fulani, baadhi yao walifanya mikutano, lakini vikundi vyao vikatokomea mbali.
Kwa kutofautisha, Wanafunzi wa Biblia waliendelea kushiriki katika kuhubiri habari njema, kama vile Yesu alivyowaamuru wanafunzi wake. Wakati huohuo, waliendelea kujifunza Neno la Mungu na kutazama kuona matukio ambayo yangetia nuru juu ya maana yalo. Hatimaye, wakati wa miaka ya 1930, vizuizi vikuu vya uelewevu mzuri wa maagano viliondolewa, na taarifa zilizosahihishwa juu ya jambo hilo zilitokea kwenye Mnara wa Mlinzi na vichapo vilivyohusiana.d Hiyo ilileta shangwe iliyoje kwa wale waliokuwa wamengoja kwa subira!
Je, Matarajio Yao Yalikuwa Sahihi?
Nyakati nyingine Wanafunzi wa Biblia walikuwa na matumaini na matarajio ambayo yamedhihakiwa na wachambuzi. Na bado, shina la matumaini na matarajio hayo yote lilikuwa tamaa kubwa ya kuona kutimizwa kwa yale ambayo Wakristo hao wenye bidii walitambua kuwa ahadi zisizoshindwa za Mungu.
Kutokana na funzo lao la Maandiko yaliyopuliziwa, walijua kwamba Yehova alikuwa ameahidi baraka nyingi kwa mataifa yote ya dunia kupitia mbegu ya Abrahamu. (Mwa. 12:1-3; 22:15-18) Waliona ahadi katika Neno la Mungu kwamba Mwana wa binadamu angetawala akiwa Mfalme wa kimbingu juu ya dunia yote, kwamba kundi dogo la wale waaminifu lingechukuliwa kutoka duniani ili kushiriki naye katika Ufalme wake, na kwamba hao wangetawala wakiwa wafalme kwa miaka elfu. (Dan. 7:13, 14; Luka 12:32; Ufu. 5:9, 10; 14:1-5; 20:6) Walijua ahadi ya Yesu kwamba angerudi na kuwachukua wale ambao alikuwa amewatayarishia mahali mbinguni. (Yn. 14:1-3) Walijua ile ahadi kwamba Mesiya angechagua pia baadhi ya mababu walio waaminifu wawe wakuu duniani pote. (Zab. 45:16) Walitambua kwamba Maandiko yalitabiri juu ya mwisho wa mfumo wa mambo wa kale ulio mwovu na wakang’amua kwamba hilo lilishirikishwa na vita ya siku ile kuu ya Mungu Mweza Yote kwenye Har–Magedoni. (Mt. 24:3; Ufu. 16:14, 16) Walivutiwa sana na maandiko yaliyoonyesha kwamba dunia iliumbwa ili ikaliwe milele, kwamba wale walioishi juu yayo wangekuwa na amani ya kweli, na kwamba wote ambao wangedhihirisha imani katika dhabihu ya kibinadamu ya Yesu iliyo kamilifu wangefurahia uhai wa milele katika Paradiso.—Isa. 2:4; 45:18; Luka 23:42, 43; Yn. 3:16.
Ingetazamiwa kwamba wangejiuliza ni lini na jinsi gani mambo hayo yangetukia. Je, Maandiko yaliyopuliziwa yaliandaa dalili zozote?
Kwa kutumia kronolojia ya Biblia ambayo ilikuwa imeelezwa kwanza na Christopher Bowen wa Uingereza, walifikiri kwamba miaka 6,000 ya historia ya kibinadamu ilikwisha katika 1873, kwamba baada ya hapo walikuwa katika kipindi cha saba cha miaka elfu ya historia ya kibinadamu, na kwamba kwa hakika walikuwa wamekaribia mpambazuko wa ile Mileani iliyotabiriwa. Mfululizo wa vitabu uitwao Millennial Dawn (na baadaye uliitwa Studies in the Scriptures), ulioandikwa na C. T. Russell, ulivuta fikira kwenye maana ya hayo kulingana na yale ambayo Wanafunzi wa Biblia walielewa kutoka kwa Maandiko.
Jambo jingine lililoonwa kuwa laweza kuwa ishara nyingine ya wakati lilihusu mpango ambao Mungu alianzisha katika Israeli wa kale kwa ajili ya Yubile, mwaka wa kuachiliwa huru, kila mwaka wa 50. Huo ulikuja baada ya mfululizo wa vipindi saba vya miaka 7, kila kimoja chavyo kikiishia na mwaka wa sabato. Wakati wa mwaka wa Yubile, watumwa Waebrania waliwekwa huru na mashamba ya urithi yaliyokuwa yameuzwa yalirudishwa. (Law. 25:8-10) Hesabu zilizotegemea kipindi hiki cha miaka ziliongoza kwenye mkataa wa kwamba labda Yubile kubwa zaidi kwa dunia yote ilikuwa imeanza katika vuli ya 1874, kwamba ilionekana Bwana alikuwa amerudi katika mwaka huo na alikuwapo bila kuonekana, na kwamba “wakati wa urudisho wa vitu vyote” ulikuwa umefika.—Mdo. 3:19-21, KJ.
Wakitegemea wazo la kwamba labda matukio ya karne ya kwanza yangepata ufanani katika matukio mengine baadaye, walifanya mkataa pia kwamba ikiwa kubatizwa na kutiwa mafuta kwa Yesu katika vuli ya 29 W.K. kulifanana na mwanzo wa kuwapo kwake kusikoonekana katika 1874, basi kupanda kwake punda kuingia Yerusalemu akiwa Mfalme katika masika ya 33 W.K. kungeelekeza kwenye masika ya 1878 kuwa wakati ambao angepata uwezo wake akiwa Mfalme wa kimbingu.e Wao walifikiri pia kwamba wangepewa zawadi yao ya kimbingu wakati huo. Hilo lilipokosa kutukia, walifanya mkataa kwamba kwa kuwa wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta wangeshiriki naye katika Ufalme, ufufuo kwenye uhai wa roho wa wale ambao tayari wanalala katika kifo ulianza wakati huo. Pia sababu zilitolewa kwamba mwisho wa upendeleo wa pekee wa Mungu kuelekea Israeli wa asili hadi kufikia 36 W.K. labda ulielekeza kwenye 1881 ukiwa wakati ambapo fursa ya pekee ya kuwa sehemu ya Israeli wa kiroho ingekoma.f
Katika hotuba “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” iliyotolewa na J. F. Rutherford mnamo Machi 21, 1920, katika jumba la Hippodrome katika New York City, fikira zilielekezwa kwenye mwaka 1925. Mwaka huo ulifikiriwa kuwa wa maana kwa msingi gani? Katika kijitabu kilichotangazwa mwaka huohuo, 1920, ilionyeshwa kwamba ikiwa Yubile kamili 70 zingehesabiwa kuanzia tarehe iliyofikiriwa kuwa ndiyo Waisraeli waliingia Bara Lililoahidiwa (badala ya kuanzia baada ya Yubile halisi ya mwisho kabla ya kuhamishiwa Babiloni na kisha kuhesabu hadi mwanzo wa mwaka wa Yubile mwishoni mwa kipindi cha miaka 50), hicho kingeweza kuelekeza kwenye mwaka 1925. Kwa msingi wa yale yaliyosemwa huko, wengi walitumaini kwamba labda waliobaki wa kundi dogo wangepokea zawadi yao ya kimbingu kufikia 1925. Mwaka huo pia ulihusishwa na matarajio ya ufufuo wa watumishi wa Mungu waaminifu wa kabla ya Ukristo kwa kusudi la kutumikia duniani wakiwa wawakilishi wakiwa na cheo cha wakuu wa Ufalme wa kimbingu. Ikiwa hilo lingetukia kikweli, lingemaanisha kwamba wanadamu walikuwa wameingia katika muhula ambao kifo kingekoma kuwa bwana mkubwa, na mamilioni wanaoishi wakati huo wangekuwa na tumaini la kutokufa kamwe duniani. Ni taraja la kupendeza kama nini! Ingawa walikosea, walishiriki taraja lao na wengine.
Baadaye, wakati wa miaka ya kuanzia 1935 hadi 1944, pitio la muundo wote wa kronolojia ya Biblia lilifunua kwamba kutafsiriwa vibaya kwa Matendo 13:19, 20 katika King James Version,g pamoja na mambo fulani mengineyo, kulikuwa kumesababisha kosa la kronolojia kwa zaidi ya karne moja.h Hilo liliongoza baadaye kwenye wazo—nyakati nyingine likisemwa kwa shaka, nyakati nyingine kwa uhakika—la kwamba mileani ya saba ya historia ya kibinadamu ingeanza katika 1975, matukio yanayoshirikishwa na kuanza kwa Utawala wa Mileani wa Kristo labda yangeanza kutukia wakati huo.
Je, imani za Mashahidi wa Yehova katika mambo hayo zilithibitika kuwa sahihi? Kwa kweli hawakukosea katika kuamini kwamba Mungu bila shaka angefanya yale aliyoahidi. Lakini baadhi ya hesabu zao za wakati na matarajio waliyoshirikisha pamoja nayo yalisababisha kuvunjika moyo sana.
Kufuatia 1925, hudhurio la mikutano lilishuka kwa kutazamisha katika makutaniko mengine katika Ufaransa na Uswisi. Tena, katika 1975, ilivunja moyo wakati matarajio yaliyohusu kuanza kwa Mileani yalipokosa kutokea. Kama tokeo, wengine waliacha tengenezo. Wengine walitengwa, kwa sababu walitaka kupotosha imani ya washiriki. Bila shaka, kuvunjika moyo kwa sababu ya tarehe kulisababisha hayo, lakini katika pindi nyingine kulikuwa na sababu za ndani zaidi. Baadhi ya watu pia walibisha dhidi ya uhitaji wa kushiriki katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Wengine wao hawakuchagua tu kuacha tengenezo; walikuwa wagomvi katika kupinga tengenezo ambalo walikuwa wameshirikiana nalo, na walitumia magazeti ya habari na televisheni ili kujulisha maoni yao. Hata hivyo, idadi ya waliokengeuka ilikuwa ndogo kwa kulinganisha.
Ingawa mitihani hiyo ilifanya wengine wakapepetwa na kupeperushwa mbali kama makapi wakati ngano inapopurwa, wengine walibaki imara. Kwa nini? Kuhusu ono lake mwenyewe na maono ya wengine katika 1925, Jules Feller alieleza: “Wale walioweka tumaini lao katika Yehova walibaki imara na wakaendelea na utendaji wao wa kuhubiri.” Walitambua kwamba kosa lilikuwa limefanywa lakini kwamba Neno la Mungu halikuwa limeshindwa hata kidogo, na kwa hiyo hakukuwa na sababu ya ama kuacha tumaini lao wenyewe lididimie ama kupunguza mwendo wa kazi ya kuelekeza watu kwenye Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu.
Baadhi ya matarajio hayakutimizwa, lakini hilo halikumaanisha kwamba kronolojia ya Biblia haikuwa na thamani yoyote. Unabii uliorekodiwa na Danieli kuhusu kutokea kwa Mesiya majuma 69 ya miaka baada ya “kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu” ulitimizwa kwa wakati barabara, katika 29 W.K.i (Dan. 9:24-27) Mwaka 1914 pia ulitiwa alama na unabii wa Biblia.
1914—Matarajio na Uhalisi
Katika 1876, C. T. Russell aliandika makala ya kwanza kati ya nyingine ambamo alionyesha mwaka 1914 kuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa zilizorejezewa na Yesu Kristo. (Luka 21:24, KJ) Katika buku la pili la Millennial Dawn, lililotangazwa katika 1889, Ndugu Russell alionyesha mambo mengi ya kutoa sababu ambayo yangewezesha wasomaji kuona msingi wa Kimaandiko wa yale yaliyosemwa na kujichunguzia wenyewe. Katika kipindi cha karibu karne nne kilichoongoza hadi 1914, Wanafunzi wa Biblia waligawanya mamilioni ya nakala za vichapo vilivyokazia fikira kwenye mwisho wa Nyakati za Mataifa. Vichapo vingine vichache vya kidini vilitambua kronolojia ya Biblia iliyoelekeza kwenye mwaka 1914, lakini ni kikundi gani isipokuwa kile cha Wanafunzi wa Biblia kilichoendelea kuitangaza kimataifa na kuishi katika njia iliyoonyesha kwamba waliamini kwamba Nyakati za Mataifa zingeisha mwaka huo?
Mwaka 1914 ulipokaribia, matarajio yalipanda. Ungeleta nini? Katika The Bible Students Monthly (Buku 6, Na. 1, lililotangazwa mapema katika 1914), Ndugu Russell aliandika: “Ikiwa tuna tarehe na kronolojia sahihi, Nyakati za Mataifa zitakwisha mwaka huu—1914. Maana yake nini? Hatujui kwa uhakika. Tarajio letu ni kwamba utawala wenye utendaji wa Mesiya utaanza karibu na wakati wa mwisho wa kipindi cha utawala cha Mataifa. Tarajio letu, liwe kweli au si kweli, ni kwamba kutakuwako madhihirisho ya ajabu ya hukumu ya Kimungu dhidi ya ukosefu wote wa haki, na kwamba hilo litamaanisha kuvunjwa kwa mifumo mingi ya wakati huu, ikiwa si yote.” Alikazia kwamba hakutazamia “mwisho wa ulimwengu” katika 1914 na kwamba dunia yadumu milele, lakini kwamba utaratibu wa mambo wa sasa, ambao Shetani ndiye mtawala, utapitilia mbali.
Katika toleo lalo la Oktoba 15, 1913, The Watch Tower lilikuwa limesema: “Kulingana na ufahamu bora zaidi wa kronolojia tuwezao, ni karibu wakati huo—iwe ni Oktoba 1914, au baadaye. Bila kushikilia kauli, tunatazamia matukio fulani: (1) Mwisho wa Nyakati za Mataifa—utawala wa Mataifa ulimwenguni—na (2) Kuanzishwa kwa Ufalme wa Mesiya ulimwenguni.”
Hilo lingetukiaje? Ilionekana kuwa yafaa kwa Wanafunzi wa Biblia wakati huo kwamba huko kungetia ndani utukuzo wa wowote walio duniani bado ambao walikuwa wamechaguliwa na Mungu kushiriki katika Ufalme wa kimbingu pamoja na Kristo. Lakini walihisije wakati hilo lilipokosa kutukia katika 1914? The Watch Tower la Aprili 15, 1916, lilisema: “Tunaamini kwamba tarehe zimethibitika kuwa sahihi kikweli. Tunaamini kwamba Nyakati za Mataifa zimekwisha.” Hata hivyo, uliongezea hivi waziwazi: “Bwana hakusema kwamba Kanisa lote lingetukuzwa kufikia 1914. Tulifanya mkataa huo tu na, bila shaka tukakosea.”
Katika jambo hilo walikuwa kama mitume wa Yesu. Mitume walijua na walifikiri waliamini unabii mbalimbali kuhusu Ufalme wa Mungu. Lakini katika nyakati mbalimbali walikuwa na matarajio yenye makosa kuhusu ni jinsi gani na lini hayo yangetimizwa. Hilo lilifanya wengine wakate tamaa.—Luka 19:11; 24:19-24; Mdo. 1:6.
Wakati Oktoba 1914 ulipopita bila badiliko lililotazamiwa la uhai wa kimbingu, Ndugu Russell alijua kwamba kungekuwako kujipekuapekua sana moyo. Katika The Watch Tower la Novemba 1, 1914, aliandika: “Acheni tukumbuke kwamba sisi tumo katika majira ya kutahini. Mitume walikuwa na majira kama hayo wakati wa muda wa kati ya kifo cha Bwana na Pentekoste. Baada ya kufufuliwa kwa Bwana, Yeye alitokea wanafunzi Wake mara chache, na hawakumwona Yeye kwa siku nyingi. Kisha wakakata tamaa na kusema, ‘Hakuna haja ya kungoja’; ‘Ninaenda kuvua samaki,’ mmoja akasema. Wengine wawili wakasema, ‘Tutaenda nawe.’ Walitaka kwenda kwenye biashara ya uvuvi na kuacha kazi ya kuvua watu. Huo ulikuwa wakati wenye kutahini kwa wanafunzi. Vivyo hivyo wakati huo upo sasa. Ikiwa kuna sababu yoyote ambayo ingeongoza yeyote kuacha Bwana na Kweli Yake na kuacha kutoa dhabihu kwa ajili ya Kusudi la Bwana, basi si upendo wa Mungu tu ndani ya moyo ambao umesukuma kupendezwa katika Bwana, bali jambo jingine; labda kutumaini kwamba wakati ulikuwa mfupi; kujitakasa kulikuwa kwa wakati fulani tu.”
Mambo yalionekana kuwa hivyo kwa watu fulani. Fikira na tamaa zao zilikuwa zimekazwa hasa juu ya taraja la kuweza kubadilishwa kwenye uhai wa kimbingu. Hilo lilipokosa kutukia katika wakati uliotarajiwa, walikosa kuona maana ya mambo yenye kushangaza yaliyotukia katika 1914. Walikosa kutambua kweli zote zenye thamani ambazo walikuwa wamejifunza kutoka kwa Neno la Mungu, na wakaanza kuwadhihaki watu ambao walikuwa wamewasaidia kujifunza hizo.
Kwa unyenyekevu, Wanafunzi wa Biblia walichunguza Maandiko tena, ili waache Neno la Mungu libadilishe mtazamo wao. Usadikisho wao kwamba Nyakati za Mataifa zilikuwa zimekwisha mwaka 1914 haukubadilika. Hatua kwa hatua walikuja kuona waziwazi zaidi jinsi Ufalme wa Kimesiya ulivyokuwa umeanza—kwamba ulisimamishwa mbinguni wakati Yehova alipokabidhi mamlaka kwa Yesu Kristo, Mwanae; pia, kwamba hilo halikuhitaji kungojea hadi warithi-washiriki wa Yesu wainuliwe kwenye uhai wa kimbingu bali kwamba wangetukuzwa naye baadaye. Kwa kuongezea, walikuja kuona kwamba kuenezwa kwa uvutano wa Ufalme hakukuhitaji kwanza manabii waaminifu wa zamani wafufuliwe, bali Mfalme angetumia Wakristo waaminifu-washikamanifu wanaoishi sasa kuwa wawakilishi wake kuwatolea watu wa mataifa yote fursa ya kuishi milele wakiwa raia wa kidunia wa Ufalme.
Mwono huo mtukufu ulipofunuka machoni pao, walitahiniwa na kupepetwa zaidi. Lakini wale waliompenda Yehova kikweli na wakafurahi kumtumikia walikuwa wenye shukrani kwa mapendeleo ya utumishi yaliyofunguka kwa ajili yao.—Ufu. 3:7, 8.
Mmoja wao alikuwa A. H. Macmillan. Baadaye aliandika: “Ingawa mataraja yetu kuhusu kuchukuliwa hadi mbinguni hayakutimizwa katika 1914, mwaka huo ndio uliokuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa . . . Hatukusikitika sana hasa kwamba kila kitu hakikutukia kama vile tulivyokuwa tumetazamia, kwa sababu tulikuwa wenye shughuli mno na kazi ya Photo-Drama na matatizo yaliyoletwa na vita.” Yeye aliendelea kuwa mwenye shughuli katika utumishi wa Yehova na alisisimuliwa kuona idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme ikiongezeka kufikia zaidi ya milioni moja wakati wa maisha yake.
Akitazama nyuma kwenye mambo aliyoona wakati wa miaka 66 katika tengenezo, yeye alisema: “Nimeona majaribu mengi makali yakikumba tengenezo na kutahiniwa kwa imani ya wale waliomo. Kwa msaada wa roho ya Mungu tengenezo liliokoka na likaendelea kusitawi.” Kuhusu marekebisho ya uelewevu kadiri wakati ulivyopita, yeye aliongeza: “Kweli za msingi tulizojifunza kutoka kwa Maandiko zilibaki vilevile. Kwa hiyo nilijifunza kwamba tunapaswa kukubali makosa yetu na kuendelea kutafuta katika Neno la Mungu ili kupata nuru zaidi. Hata iwe ni mabadiliko gani ambayo tungelazimika kufanya wakati mmoja au mwingine katika maoni yetu, hilo halingebadili uandalizi wa fadhili wa fidia na ahadi ya Mungu ya uhai wa milele.”
Wakati wa maisha yake, Ndugu Macmillan aliona kwamba, miongoni mwa masuala yaliyosababisha kutahiniwa kwa imani, kulikuwa na mawili yaliyofunua yale yaliyokuwa hasa mioyoni mwa watu mmoja-mmoja, utayari wa kutoa ushahidi na uthamini kwa tengenezo la kitheokrasi. Jinsi gani hivyo?
Utumishi wa Shambani na Tengenezo Yawa Masuala
Kuanzia toleo lalo la kwanza, na kwa mkazo wenye kuongezeka baada ya hapo, Zion’s Watch Tower lilihimiza kila Mkristo wa kweli ashiriki kweli na wengine. Baada ya hapo, wasomaji wa Watch Tower walitiwa moyo mara kwa mara kuthamini pendeleo na daraka lao la kupiga mbiu ya habari njema kwa wengine. Wengi walishiriki katika njia ndogo, lakini wachache kwa kadiri fulani walikuwa katika mstari wa mbele katika kazi, wakihubiri nyumba hadi nyumba ili kumpa kila mtu fursa ya kusikia ujumbe wa Ufalme.
Hata hivyo, kuanzia mwaka 1919, ushiriki katika utumishi wa shambani ulikaziwa kwa nguvu zaidi. Ndugu Rutherford alikazia jambo hilo kwa dhati katika hotuba jijini Cedar Point, Ohio, mwaka huo. Katika kila kutaniko lililoomba Sosaiti kulipanga kitengenezo kwa ajili ya utumishi, mipango ilifanywa ili mwelekezi wa utumishi, aliyeteuliwa na Sosaiti, ashughulikie kazi hiyo. Alipaswa achukue uongozi yeye mwenyewe na kuona kwamba kutaniko lilikuwa na ugavi uliohitajiwa.
Katika 1922, The Watch Tower lilitangaza makala yenye kichwa “Utumishi Ni wa Lazima.” Ilielekeza kwenye uhitaji mkubwa wa watu kusikia habari njema za Ufalme, ikaelekeza fikira kwenye amri ya kiunabii ya Yesu kwenye Mathayo 24:14, na kuwaambia wazee makutanikoni: “Mtu yeyote asifikiri kwamba kwa sababu yeye ni mzee darasani utumishi wake wapaswa uwe wa kuhubiri tu kwa mdomo. Ikiwa fursa zamruhusu kwenda miongoni mwa watu na kuwakabidhi ujumbe uliochapwa, hilo ni pendeleo kubwa na ni kuhubiri gospeli, mara nyingi kwa matokeo zaidi ya njia nyingineyo ya kuihubiri.” Kisha makala hiyo ikauliza: “Je, yeyote ambaye amejitakasa kabisakabisa kwa Bwana aweza kujitetea mwenyewe kwa kuwa mzembe wakati huu?”
Wengine walijizuia. Walizusha visababu vya aina zote. Hawakufikiri kuwa yafaa “kuuza vitabu,” ingawa kazi hiyo haikuwa inafanywa ili kufaidika kifedha na ingawa ni kupitia vichapo hivyohivyo kwamba walikuwa wamejifunza kweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Wakati kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba kwa kutumia vitabu siku ya Jumapili kulipotiwa moyo, kuanzia mwaka 1926, wengine walipinga hilo, ingawa Jumapili ilikuwa siku ambayo watu wengi waliweka kando kidesturi kwa ajili ya ibada. Tatizo la msingi ni kwamba walijiona wenyewe kuwa wa maana zaidi kuweza kuhubiri nyumba hadi nyumba. Na bado, Biblia husema wazi kwamba Yesu alituma wanafunzi wake kwenye nyumba za watu ili kuhubiri, na mtume Paulo alihubiri ‘hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.’—Mdo. 20:20; Mt. 10:5-14, NW.
Mkazo juu ya utumishi wa shambani uliongezeka, na wale ambao mioyo yao haikuwasukuma kumwiga Yesu na mitume wake wakiwa mashahidi waliacha tengenezo hatua kwa hatua. Kutaniko la Skive katika Denmark, pamoja na wengine, lilipungua kufikia nusu hivi. Kati ya watu mia hivi walioshirikiana na Kutaniko la Dublin katika Ireland, ni wanne tu waliobaki. Kulikuwa na kutahiniwa na kupepetwa kwa aina hiyohiyo katika Marekani, Kanada, Norway, na nchi nyinginezo. Hilo lilitakasa makutaniko.
Wale ambao kwa kweli walitaka kumwiga Mwana wa Mungu waliitikia ifaavyo kitia-moyo kutoka kwa Maandiko. Hata hivyo, utayari wao haukufanya iwe rahisi kwao kuanza kwenda nyumba hadi nyumba. Wengine walikuwa na wakati mgumu kuanza. Lakini mipango ya kutoa ushahidi wa kikundi na makusanyiko ya utumishi wa pekee yalikuwa kitia-moyo. Dada wawili kutoka Jutland kaskazini, katika Denmark, walikumbuka kwa muda mrefu siku yao ya kwanza ya utumishi wa shambani. Walikutana na kikundi, wakasikia maagizo, wakaanza kwenda kwenye eneo lao, lakini kisha wakaanza kulia. Ndugu wawili waliona yale yaliyokuwa yakitukia na wakawaalika dada wafanye kazi pamoja nao. Upesi wakaanza kuchangamka tena. Baada ya kuonja utumishi wa shambani, wengi walijawa na shangwe na walikuwa na msisimko wa kufanya zaidi.
Kisha, katika 1932, The Watch Tower likawa na makala yenye sehemu mbili yenye kichwa “Tengenezo la Yehova.” (Matoleo ya Agosti 15 na Septemba 1) Hiyo ilionyesha kwamba uchaguzi wa uzee katika makutaniko haukuwa wa kimaandiko. Makutaniko yalihimizwa kutumia katika vyeo vya madaraka wanaume wale tu waliokuwa watendaji katika utumishi wa shambani, wanaume walioishi kulingana na madaraka yaliyomaanishwa na jina Mashahidi wa Yehova. Hao wangefanya kazi wakiwa halmashauri ya utumishi. Mmoja wao, akiteuliwa na kutaniko, angewekwa rasmi na Sosaiti kuwa mwelekezi wa utumishi. Katika Belfast, Ireland, hilo lilipepeta nje wengine zaidi ambao tamaa yao ilikuwa ni umashuhuri wa kibinafsi badala ya utumishi wa unyenyekevu.
Kufikia miaka ya mapema ya 1930, wengi wa wale waliokuwa Ujerumani waliokuwa wakijaribu kupinga utumishi wa shambani walikuwa wameacha kushirikiana na makutaniko. Wengine wao waliacha kwa woga kazi ilipopigwa marufuku katika 1933 katika majimbo mengi ya Ujerumani. Lakini maelfu walivumilia kutahiniwa huko kwa imani na wakawa na hiari ya kuhubiri kujapokuwa na hatari zilizohusika.
Kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme iliongeza mwendo duniani pote. Utumishi wa shambani ukawa sehemu ya maana ya maisha ya Mashahidi wa Yehova wote. Kwa kielelezo, kutaniko katika Oslo, Norway, lilikodisha mabasi kwenye miisho-juma ili kusafirisha wahubiri hadi majiji ya karibu. Walikutana mapema asubuhi, wakawa katika eneo lao kufikia saa tatu au nne, wakafanya kazi kwa bidii katika utumishi wa shambani kwa muda wa saa saba au nane, na kisha wakajiunga na kikundi cha basi kwa ajili ya safari ya kurudi nyumbani. Wengine walisafiri kwenye maeneo ya mashambani kwa baiskeli, mikoba ya vitabu na katoni zikiwa zimepakiwa ugavi wa ziada. Mashahidi wa Yehova walikuwa wenye furaha, bidii, na umoja katika kufanya mapenzi ya Mungu.
Katika 1938, wakati fikira zilipoelekezwa tena kwenye kuwekwa rasmi kwa wanaume wenye madaraka makutanikoni,j kuondolewa kwa uchaguzi wote wa watumishi wa mahali kulikaribishwa kwa ujumla. Makutaniko yalipitisha maazimio kwa furaha yakionyesha uthamini kwa tengenezo la kitheokrasi na kuomba “Sosaiti” (waliyoelewa kuwa yamaanisha mabaki watiwa-mafuta, au mtumwa mwaminifu na mwenye busara) kupanga kutaniko kitengenezo kwa ajili ya utumishi na kuweka watumishi wote. Baadaye, Baraza Linaloongoza linaloonekana liliweka rasmi wale waliohitajiwa na kupanga makutaniko kitheokrasi kwa ajili ya utendaji wenye umoja na matokeo. Ni vikundi vichache tu vilivyojizuia na kuacha tengenezo wakati huo.
Kujitoa kwa Ajili ya Kueneza tu Ujumbe wa Ufalme
Ili tengenezo liendelee kuwa na kibali cha Yehova, ni lazima lijitoe kwa kazi tu ambayo Neno lake linaamuru kwa ajili ya siku yetu. Kazi hiyo ni kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Hata hivyo, kumekuwa na visa vichache ambavyo watu mmoja-mmoja waliofanya kazi kwa bidii kwa kushirikiana na tengenezo pia walijaribu kulitumia ili kuendeleza miradi iliyoelekea kukengeusha washiriki wao kwenye utendaji mwingineo. Walipokaripiwa, hilo liliwatahini, hasa walipohisi kwamba makusudi yao yalikuwa yanayofaa.
Hilo lilitukia nchini Finland katika mwaka 1915, wakati ndugu fulani walianzisha shirika liitwalo Ararat na kutumia safu za chapa ya Kifinland ya The Watch Tower ili kuhimiza wasomaji walo wajiunge na shirika hilo la kibiashara. Yule aliyeanzisha utendaji huo katika Finland aliitikia kwa unyenyekevu wakati Ndugu Russell alipoonyesha kwamba yeye na washiriki wake walikuwa wanajiacha “wavutwe mbali kutoka kwa kazi ya maana ya Gospeli.” Hata hivyo, kiburi kilimzuia ndugu mwingine ambaye alikuwa amekuwa mwenye utendaji katika utumishi wa Yehova kwa zaidi ya mwongo mmoja katika Norway asikubali shauri hilohilo.
Wakati wa miaka ya 1930, katika Marekani, tatizo kama hilo lilitokea. Hesabu fulani ya makutaniko yalikuwa yakitangaza karatasi zao wenyewe za kila mwezi za maagizo ya utumishi, zilizotia ndani vikumbusho kutoka kwa Bulletin ya Sosaiti pamoja na mambo yaliyoonwa na ratiba ya mahali ya mipango ya utumishi. Mojawapo kikaratasi hicho, kilichotangazwa katika Baltimore, Maryland, kiliunga mkono kwa dhati utendaji wa kuhubiri lakini pia kikatumiwa kuendeleza shughuli fulani za kibiashara. Mwanzoni Ndugu Rutherford alitoa kibali kwa ukimya kwa baadhi ya shughuli hizi. Lakini ilipong’amuliwa ni nini kingetokana na kujihusisha na shughuli kama hizo, Mnara wa Mlinzi likasema kwamba Sosaiti haikuziidhinisha. Hilo lilimtahini sana Anton Koerber, kwa kuwa alikuwa amekusudia kuwasaidia kifedha ndugu zake kwa njia hiyo. Hata hivyo, baadaye, alitumia tena uwezo wake kikamili ili kuendeleza kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova.
Tatizo kama hilo lilitokea katika Australia kuanzia 1938 na likazidi wakati wa marufuku juu ya Sosaiti (Januari 1941 hadi Juni 1943). Ili kushughulikia yale ambayo yalionekana wakati huo kuwa mahitaji yanayofaa, ofisi ya tawi ya Sosaiti ilianza kuwa na shughuli katika utendaji mbalimbali wa kibiashara. Hivyo, kosa kubwa lilifanywa. Walikuwa na vinu (mashine) vya kupasua mbao, “mashamba ya Ufalme” zaidi ya 20, kampuni ya uhandisi, jiko la kuokea mikate, na biashara nyinginezo. Mashirika mawili ya uchapaji yalisitiri utoaji wenye kuendelea wa vichapo vya Sosaiti wakati wa marufuku. Lakini baadhi ya shughuli zao za biashara ziliwahusisha katika kukiuka kutokuwamo kwa Kikristo, kazi hiyo ikifanywa kwa kisingizio cha kuandaa fedha na kuwategemeza mapainia wakati wa marufuku. Hata hivyo, dhamiri za wengine zilisumbuliwa sana. Ingawa walio wengi waliendelea katika tengenezo, kukoma kwa ujumla kwa kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme kulianza. Ni nini kilichokuwa kikizuia baraka za Yehova?
Wakati marufuku juu ya kazi ilipoondolewa katika Juni 1943, ndugu waliokuwa katika ofisi ya tawi walitambua kwamba biashara hizo zapaswa kukomeshwa, ili kukazia fikira kwenye kuhubiri juu ya Ufalme ambako ni kwenye maana zaidi. Katika muda wa miaka mitatu, hilo lilitimizwa, na familia ya Betheli ilipunguzwa kufikia kiasi cha kawaida. Lakini bado ilikuwa lazima kuelewesha mambo na hivyo kurudisha tumaini kamili katika tengenezo.
Nathan H. Knorr, msimamizi wa Sosaiti, na katibu wake M. G. Henschel alizuru Australia ili kushughulika kihususa na hali hiyo katika 1947. Katika kuripoti juu ya jambo hilo, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Juni 1, 1947, lilisema hivi kuhusu utendaji wa kibiashara uliokuwa umeendeshwa: “Haikuwa kazi ya kimwili ya kila siku ya akina ndugu katika kupata riziki iliyohusika, bali lilikuwa jambo la kwamba ofisi ya Tawi ya Sosaiti ilikuwa imepata aina mbalimbali za viwanda na kuwaita wahubiri kutoka sehemu zote za nchi, hasa mapainia, ili kufanya kazi katika viwanda hivyo badala ya kuhubiri gospeli.” Hilo lilikuwa hata limeongoza kwenye kuhusika katika vita katika njia isiyo ya moja kwa moja. Kwenye mikusanyiko katika kila mojawapo majiji makuu ya mikoa, Ndugu Knorr alisema waziwazi kwa akina ndugu kuhusu hali hiyo. Kwenye kila kusanyiko azimio lilipitishwa ambalo kwalo akina ndugu wa Australia walikubali kosa lao na kuomba rehema na msamaha wa Yehova kupitia Yesu Kristo. Hivyo, uangalifu umetakiwa na mitihani imekabiliwa ili kwamba tengenezo liendelee kujitoa kwa kueneza tu ujumbe wa Ufalme wa Mungu.
Mashahidi wa Yehova wanapopitia historia yao ya kisasa, wanaona uthibitisho kwamba Yehova kwa kweli amekuwa akiwasafisha watu wake. (Mal. 3:1-3) Mitazamo, imani, na mazoea yasiyofaa yameondolewa mbali hatua kwa hatua, na watu wowote ambao wamechagua kushikamana nayo wameondolewa pia. Wale wanaobaki si watu wanaotaka kuridhiana kweli ya Biblia ili kuunga mkono falsafa za kibinadamu. Wao si wafuasi wa mwanadamu bali ni watumishi walio wakfu wa Yehova Mungu. Wao huitikia kwa furaha mwelekezo wa tengenezo kwa sababu wao huona ithibati madhubuti kwamba tengenezo ni la Yehova. Wanashangilia katika nuru ya kweli inayozidi kung’aa. (Mit. 4:18) Kila mmoja wao hulihesabu kuwa pendeleo tukufu kuwa Mashahidi wa Yehova walio watendaji, wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu.
[Maelezo ya Chini]
a Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, Chapa ya Ziada, Aprili 25, 1894, kur. 102-104.
b Kuhusu Utatu, ona New Catholic Encyclopedia, Buku 14, 1967, ukurasa 299; Dictionary of the Bible, ya J. L. McKenzie, S. J., 1965, ukurasa 899; The New International Dictionary of New Testament Theology, Buku 2, 1976, ukurasa 84. Kuhusu nafsi, ona New Catholic Encyclopedia, Buku 13, 1967, kurasa 449-450, 452, 454; The New Westminster Dictionary of the Bible, iliyohaririwa na H.S. Gehman, 1970, ukurasa 901; The Interpreter’s Bible, Buku 1, 1952, ukurasa 230; Peake’s Commentary on the Bible, iliyohaririwa na M. Black na H. H. Rowley, 1962, ukurasa 416.
c Kulingana na Ndugu Russell, mke wake, ambaye baadaye alimwacha, alikuwa wa kwanza kutumia Mathayo 24:45-47 kumwelekea. Ona matoleo ya Watch Tower ya Julai 15, 1906, ukurasa 215; Machi 1, 1896, ukurasa 47; na Juni 15, 1896, kurasa 139-140.
d Vindication, Kitabu cha Pili, kur. 258-259, 268-269; Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) Aprili 1, 1934, kur. 99-106; Aprili 15, 1934, kur. 115-122; Agosti 1, 1935, kur. 227-237.
e Jambo la kwamba 1878 ulikuwa mwaka wa maana lilionekana kuwa likitegemezwa na rejezo kwenye Yeremia 16:18 (‘kifani cha Yakobo,’ KJ) pamoja na hesabu zilizoonyesha kwamba miaka 1,845 ilikuwa imepita tangu kifo cha Yakobo hadi kufikia 33 W.K., wakati Israeli wa asili walipotupiliwa mbali, na kwamba ufanani, au mithili, ya hayo ingeenea kuanzia 33 W.K. hadi kufikia 1878.
f Kwa kueneza ufanani zaidi, ilisemwa kwamba kuachwa ukiwa kwa Yerusalemu katika 70 W.K. (miaka 37 baada ya Yesu kukaribishwa akiwa mfalme na wanafunzi wake alipopanda punda kuingia Yerusalemu) kungeweza kuelekezea mwaka 1915 (miaka 37 baada ya 1878) kukiwa tokeo la msukosuko wa kuasi sheria ambao walifikiri Mungu angeruhusu kuwa njia ya kuleta mwisho wa mifumo iliyoko ya ulimwengu. Tarehe hiyo ilitokea katika chapa nyinginezo za baadaye za Studies in the Scriptures. (Ona Buku 2, kurasa 99-101, 171, 221, 232, 246-247; linganisha ile iliyochapwa tena ya 1914 na chapa za mapema, kama vile chapa ya 1902 ya Millennial Dawn.) Ilionekana kwao kwamba hayo yalifaa vema na yale yaliyokuwa yametangazwa kuhusu mwaka 1914 kuwa ukitia alama mwisho wa Nyakati za Mataifa.
g Linganisha fasili katika The Emphasised Bible, iliyotafsiriwa na J. B. Rotherham; ona pia kielezi-chini kwenye Matendo 13:20 katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References.
h Ona “The Truth Shall Make You Free,” sura ya 11; “The Kingdom Is at Hand,” kurasa 171-175; pia The Golden Age, Machi 27, 1935, kurasa 391, 412. Kwa kutumia majedwali hayo ya kronolojia ya Biblia yaliyosahihishwa, ingeweza kuonwa kwamba utumizi wa hapo awali wa tarehe 1873 na 1878, pamoja na tarehe zinazohusiana zinazotokana na hizo kwa msingi wa ufanani mbalimbali wa matukio ya karne ya kwanza, ulitegemea kutokuelewa.
i Ona Insight on the Scriptures, Buku 2, kurasa 899-904.
j Ona Sura ya 15, “Usitawi wa Muundo wa Tengenezo.”
[Blabu katika ukurasa wa 619]
Kutahiniwa na kupepetwa hakushangazi
[Blabu katika ukurasa wa 621]
“Wanakataa kuvutwa kutoka kwenye Neno la Bwana”
[Blabu katika ukurasa wa 623]
“Hatutaki heshima kuu, na kicho, kuelekea sisi au maandishi yetu”
[Blabu katika ukurasa wa 624]
“Mungu angali aelekeza mambo”
[Blabu katika ukurasa wa 626]
“Mtumishi mwaminifu na mwenye hekima” hakuwa ametoweka Ndugu Russell alipokufa
[Blabu katika ukurasa wa 627]
Jitihada zenye kudhuru ili kutia sumu akili za wengine
[Blabu katika ukurasa wa 628]
Wengine waliruhusu kiburi kidhoofishe imani yao
[Blabu katika ukurasa wa 629]
“Mfulize kuangalia wale wasababishao migawanyiko . . . na mwaepuke”
[Blabu katika ukurasa wa 630]
Wengine walishtaki kwa uwongo kwamba “The Watch Tower” lilikuwa limeikataa katakata fidia
[Blabu katika ukurasa wa 635]
“Tulifanya mkataa huo tu na, bila shaka tukakosea”
[Blabu katika ukurasa wa 636]
Wale waliompenda Yehova kikweli walikuwa wenye shukrani kwa mapendeleo ya utumishi yaliyofunguka kwa ajili yao
[Blabu katika ukurasa wa 638]
“Je, yeyote ambaye amejitakasa kabisakabisa kwa Bwana aweza kujitetea mwenyewe kwa kuwa mzembe wakati huu?”
[Blabu katika ukurasa wa 641]
Mitazamo, imani, na mazoea yasiyofaa yameondolewa mbali hatua kwa hatua
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 622]
W. E. Van Amburgh
Katika 1916, W. E. Van Amburgh alijulisha hivi: “Kazi hii kubwa ya ulimwenguni pote si kazi ya mtu mmoja. . . . Ni kazi ya Mungu.” Ingawa aliona wengine wakikengeuka, yeye alibaki imara katika usadikisho huo hadi kufikia kifo chake katika 1947, akiwa na umri wa miaka 83.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 633]
Jules Feller
Alipokuwa kijana, Jules Feller aliona mitihani mikali ya imani. Baadhi ya makutaniko katika Uswisi yalipungua kufikia nusu ya ukubwa wayo au hata chini zaidi. Lakini baadaye aliandika: “Wale walioweka tumaini lao katika Yehova walibaki imara na kuendelea na utendaji wao wa kuhubiri.” Ndugu Feller aliazimia kufanya hivyo pia, na kama tokeo, hadi kufikia 1992 ameonea shangwe miaka 68 ya utumishi wa Betheli.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 634]
C. J. Woodworth
Akiandikia mmoja aliyeacha utumishi wa Yehova kwa sababu wafuasi wa Yesu Kristo watiwa-mafuta hawakuchukuliwa hadi mbinguni katika 1914, C. J. Woodworth alisema:
“Miaka 20 iliyopita wewe na mimi tuliamini katika ubatizo wa vitoto; katika haki ya Kimungu ya makasisi kutoa ubatizo huo; kwamba ubatizo ulikuwa wa lazima ili kuepuka mateso ya milele; kwamba Mungu ni upendo; kwamba Mungu aliumba na aendelea kuumba mabilioni ya viumbe katika mfano Wake ambao kwa mihula ya umilele watakuwa kwenye mioto yenye kusonga ya kiberiti chenye kuwaka, wakiomba tone moja la maji lipunguze uchungu wao bila kufanikiwa . . .
“Tuliamini kwamba baada ya mtu kufa, yeye yuko hai; tuliamini kwamba Yesu Kristo hakufa kamwe; kwamba Yeye hangeweza kufa; kwamba hakuna Fidia iliyopata kulipwa au itapata kulipwa; kwamba Yehova Mungu na Kristo Yesu Mwana Wake ni mtu yuleyule mmoja; kwamba Kristo alikuwa ndiye Baba Yake mwenyewe; kwamba Yesu alikuwa ndiye Mwana Wake mwenyewe; kwamba Roho Takatifu ni mtu; kwamba moja kuongeza moja, kuongeza moja, tokeo ni moja; kwamba wakati Yesu alipotundikwa kwenye msalaba na kusema, ‘Mungu Wangu, Mungu Wangu, mbona Umeniacha,’ Yeye alikuwa tu akijisemeza; . . . kwamba falme za sasa ni sehemu ya Ufalme wa Kristo; kwamba Ibilisi amekuwa mbali mahali fulani katika Helo isiyojulikana mahali ipo, badala ya kuwa na umiliki juu ya falme za dunia hii . . .
“Ninamsifu Mungu kwa siku ambayo alileta Kweli ya Sasa mlangoni pangu. Ilikuwa yenye kufaa sana, yenye kuburudisha akili na moyo sana, hivi kwamba niliacha upesi uwongo na mambo ya upuuzi ya zamani na nikatumiwa na Mungu kufungua pia macho yako yaliyopofushwa. Tulishangilia pamoja katika Kweli, tukifanya kazi pamoja kwa miaka kumi na mitano. Bwana alikustahi sana ukiwa msemaji; Sikupata kamwe kumjua mtu ambaye angeweza kufunua uwongo wa Babiloni kama wewe. Katika barua yako unauliza, ‘Ni nini kinachofuata?’ Lo! sasa ndiyo sehemu yenye kuhuzunisha! Kitu kinachofuata ni kwamba unaruhusu moyo wako umchukie yule ambaye kazi zake za upendo na baraka zake kutoka Juu zilileta Kweli kwa mioyo yetu sote wawili. Uliacha tengenezo, na kuchukua kondoo kadhaa pamoja nawe. . . .
“Labda ninaonekana kuwa mpuuzi kwako kwa sababu sikuenda Mbinguni, Oktoba 1, 1914, lakini wewe huonekani kuwa mpuuzi kwangu—la hasha!
“Wakati huu ambapo mataifa kumi makubwa kati ya mataifa ya dunia yanafurukuta katika uchungu mkali wa kifo chayo, kwangu inaonekana kuwa wakati usiofaa hasa kumdhihaki mtu huyo, na mtu pekee, ambaye kwa miaka arobaini amefundisha kwamba Nyakati za Mataifa zingekoma katika 1914.”
Imani ya Ndugu Woodworth haikutikisika wakati matukio ya 1914 yalipokosa kutimiza yale yaliyotarajiwa. Yeye aling’amua tu kwamba kulikuwa na mengi zaidi ya kujifunza. Kwa sababu ya tumaini lake katika kusudi la Mungu, alifungwa miezi tisa gerezani katika 1918-1919. Baadaye alitumikia akiwa mhariri wa magazeti “The Golden Age” na “Consolation.” Alibaki imara katika imani na mwaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo la Yehova hadi kufikia kifo chake katika 1951, akiwa mwenye umri wa miaka 81.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 637]
A. H. Macmillan
“Nimeona hekima ya kumngoja Yehova kwa subira ili atueleweshe vizuri zaidi mambo ya Kimaandiko badala ya kukasirika kwa ajili ya wazo jipya. Nyakati nyingine matarajio yetu ya tarehe fulani yalikuwa zaidi ya yale ambayo Maandiko yaliruhusu. Wakati matarajio hayo yalipokosa kutimizwa, hilo halikubadili makusudi ya Mungu.”
[Picha katika ukurasa wa 620]
Mtihani mkuu wa imani ulihusu kutambua thamani yenye kulipia dhambi ya dhabihu ya Yesu
[Picha katika ukurasa wa 625]
Wengine waliomheshimu Russell walipata kwamba itikio lao kwa tabia ya Rutherford lilifunua yule waliomtumikia hasa
[Picha katika ukurasa wa 639]
Mkazo ulipoongezwa juu ya utumishi wa shambani, wengi waliacha kushiriki; wengine walionyesha bidii zaidi
“Watch Tower,” Aprili 1, 1928
“Watch Tower,” Juni 15, 1927
“Watch Tower,” Agosti 15, 1922
[Picha katika ukurasa wa 640]
Tengenezo la kitheokrasi lilipotangulizwa, wale waliotafuta umashuhuri wa kibinafsi walipepetwa nje