Yazuie “Maelekeo ya Kuona Wivu”
MNA maelekeo yenye nguvu ndani ya wanadamu wasiokamilika ya kuwaonea wivu wale walio na ukubwa, walio na kufanikiwa kwingi zaidi au walio na mali zaidi za kimwili. Maelekeo haya ni yenye nguvu sana kwamba Biblia inasema: “Ni kwa maelekeo ya kuona wivu kwamba roho ambayo imekaa ndani yetu yazidi kutamani.”—Yak. 4:5, NW.
Ingawa roho, maelekeo au nia ya kuona wivu “inakaa” ndani yetu sote tulio wanadamu wasiokamilika, hii haiufanyi wivu jambo la kuachiliwa machoni pa Mungu. Wivu unakatazwa pamoja na uasherati, mwenendo mpotovu na mifululizo ya kulewa kama mazoea ya ufisadi ya mwili ambayo yanaweza kumfanya mtu asiurithi ufalme wa Mungu. (Gal. 5:19-21) Lakini kwa sababu gani Yehova Mungu anakataza wivu kwa nguvu hivyo?
Kwa sababu wivu una shina lake katika choyo nao haupaswi kabisa kuwa katika utu, njia na matendo ya Muumba. Sifa kuu ya Yehova Mungu ni upendo, na ni wale wanaoonyesha upendo kama huo peke yao anaowakubali kama watumishi wake.
Mtu mwenye wivu, akiwa hana upendo, anakataa ‘kufurahi pamoja nao wafurahio.’ (Rum. 12:15) Huenda hata akakimbilia udanganyifu, unyang’anyi au mazoea mengineyo ya udanganyifu katika jitihada ya kuwapokonya wengine mambo waliyo nayo. Au, huenda akajaribu kumvunjia heshima mtu anayeonea wivu, akipunguza sifa ya mambo yaliyotimizwa na huyo kwa lawama ya kadiri isiyofaa au kwa kutilia mashaka uwezo wake mbalimbali na makusudi. Hivyo wivu unazaa ugomvi, mgawanyiko, mateto, chuki na hata mapigano makali, ukiharibu ambao huenda ungekuwa ujamaa mwema na wenzako. Hili linatajwa katika Yakobo 4:1, 2, ambapo twasoma: “Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi? Si humu, katika tamaa zenu zifanyazo vita katika viungo vyenu? Mwatamani, wala hamna kitu; mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata.”
Bila shaka, maelekeo ya kuona wivu hayakomei kwa wale wanaojaribu kufikia ukubwa na ufanisi kwa njia za udanganyifu. Kwa mfano, bidii na utendaji vinasifiwa. Lakini huenda mtu akatia mkazo juu ya hivi kwa sababu ya maelekeo ya kuona wivu. Namna gani hivyo? Kwa sababu huenda akawa anafanya kazi kwa bidii, siyo kwa sababu ya kutimiliza jambo fulani lifaalo, lakini akiwa na tamaa ya kuwashinda wengine katika kazi, ufundi au matokeo. Wivu unamsukuma ayafikie yale ambayo wengine wamefikia na, kwa kweli, kuwapita. Jambo hili linakubaliwa na mwandikaji mwenye ufahamu wa Mhubiri: “Nikafikiri amali zote, na kila kazi ya ustadi, ya kwamba inatoka katika mtu kupingana na mwenzake. Hayo nayo ni ubatili na kujilisha upepo.”—Mhu. 4:4.
Wakati kusudi la mtu katika kazi linapoharibiwa na kujitukuza mwenyewe, kupendezwa ko kote na huruma kwa upande wake kwa wengine mara nyingi vinapitiliwa mbali. Udhaifu wao wa kimwili na akili unafikiriwa kidogo au hata kutofikiriwa. Kushindana kunachukua mahali pa ushirikiano wa kirafiki. Kanuni isiyofaa ya maamuzi huenda itumiwe kusudi kwamba uwezo wenyewe unakuwa ndiyo kanuni ya kushindanisha, kufikiria ubora au jitihada ya unyofu, isiyo ya kichoyo iliyokuwamo katika kazi ya mwingine kukiachiliwa mbali. Zaidi ubora wa mtu huenda ukaamuliwa kwa anavyoweza kutokeza, kuliko kwa namna yeye mwenyewe alivyo.
Bila shaka jitihada za kuwashinda wengine ni zenye kudhuru, nao watiao jitihada za namna hiyo ‘wanajilisha upepo,’ wanaufuatia utupu tu. Mtu anayezitangaza kazi zake bora na kujilinganisha na wengine anachochea mashindano na wivu. Kwa kujaribu kuwatazamisha wengine kwa ukubwa wake mwenyewe, kwa wivu anakataa kuzikubali sifa njema ambazo huenda wengine wanazo. Anakilinda cheo chake kwa wivu, akiogopa kwamba wengine wanaweza kuwa sawa naye na, pengine, hata kumpita. Tendo lote hilo linatofautiana na amri ya Maandiko inayotolewa kwa Wakristo: “Tusijisifu bure, tukichokozana na [kuoneana wivu].”—Gal. 5:26.
Katika makundi ya watu wa Mungu leo, zaidi wazee yawapasa kuwa waangalifu kwamba hawaanzi kujifikiria zaidi kupita kadiri na mambo waliyoyatimiliza. Hii ingeweza kuwafanya wawazuie wengine wasishiriki katika mapendeleo fulani kwa sababu ati wao wenyewe wanataka kuendelea kujulikana sana. Imewapasa sikuzote wakumbuke kwamba Yehova Mungu ndiye Yeye anayetoa ongezeko. Kundi ni la, si mwanadamu ye yote, bali Mungu.—Matendo 20:28; 1 Kor. 3:7.
Kwa mwanadamu ye yote au kikundi cha wanadamu kuwa wasiotaka kuacha wengine washiriki katika kutunza madaraka kungekuwa ni kutenda tofauti na uongozi wa roho ya Mungu. Mtume Paulo alimwagiza Timotheo kama mwangalizi awapitishie mambo aliyokuwa amejifunza “watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.” (2 Tim. 2:2) Basi, roho ifaayo ni kwa wazee kujaribu kusaidia wanaume wengine katika kundi kuzifikia sifa zinazohitajiwa kusudi watumikie pamoja nao katika kuyatunza madaraka ya kundi. Kama wangeshindwa kufanya hivi kwa sababu ya kuogopa, ama wakijua ama wasipojua vizuri, kwamba ubora wao ungepunguzwa katika kundi, wangekuwa wakizuia, siyo faida zao wenyewe tu, lakini faida za kundi zima. Kwa wazi wanaume wengi wanaostahili wanaweza kutimiliza kazi nyingi zaidi sana kuliko mmoja tu au wachache. Vile vile, kadiri kundi lilivyo na wazee zaidi wanaostahili, ndivyo utakavyokuwa mkubwa zaidi utimizo wa sifa njema zinazoweza kuunganishwa kwa ajili ya kuendeleza faida za kiroho.
Nia ifaayo kuelekea kuacha wengine washiriki katika mapendeleo ilitajwa na Musa alipomwambia Yoshua: “Je! umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa [Yehova] wangekuwa manabii, na kama [Yehova] angewatia roho yake.”—Hes. 11:29.
Kukosa kuionyesha nia hii kwaweza kuelekeza kwenye matokeo mazito. Mnamo wakati wa huduma yake ya kidunia Yesu Kristo alilionyesha hili wazi sana kwa mitume wake. Mtu fulani, kwa wazi aliyepewa uwezo na roho ya Mungu, alipotoa mashetani juu ya msingi wa jina la Yesu, mtume Yohana na wengine walijaribu kumkomesha kwa maana hakuwa akifuatana nao. Kwa wazi waliona kwamba mtu huyo hakuwa sehemu ya kikundi chao cha pekee na kufanya kwake kazi zenye nguvu kungepunguza sifa ya utendaji wao kwa njia hiyo. Aliposikia hivi, Yesu aliwaonyesha kosa lao. Kisha akaongezea onyo kali: “Ye yote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini.” (Marko 9:38-42) Ndiyo, nia hiyo ya kujifikiria mwenyewe kama ilivyoonyeshwa na mitume ingaliweza kufanya wapya na walio wanyenyekevu wakwazwe. Mungu asingeuona mwendo huo wenye kudhuru kama jambo lisilo kubwa.
Ikiwa twatamani hali yenye kukubalika na Yehova Mungu, imetupasa basi tujue wivu ulivyo—dhambi juu ya Mungu na wenzetu, ndiyo, wonyesho wa roho isiyo na upendo. Kwa sababu ya tunda baya linalotokezwa na wivu, tunayo sababu nzuri ya kuuchukia. Chuki hii yaweza kutulinda tusiwe na wivu wenyewe na tusichochee mashindano na wivu katika wengine.