Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w20 Februari kur. 14-19
  • Fuatilia Amani kwa Kuushinda Wivu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fuatilia Amani kwa Kuushinda Wivu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WIVU UNAWEZA KUSABABISHWA NA NINI?
  • SITAWISHA UNYENYEKEVU NA HALI YA KURIDHIKA
  • ‘FUATILIA MAMBO YANAYOLETA AMANI’
  • Wivu Sifa Mbaya Inayoweza Kutia Sumu Akili Zetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Yazuie “Maelekeo ya Kuona Wivu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Jinsi ya Kuishi Maisha Yenye Furaha
    Amkeni!—2014
  • Je, Wewe Hujilinganisha na Wengine?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
w20 Februari kur. 14-19

MAKALA YA 8

Fuatilia Amani kwa Kuushinda Wivu

“Na tufuatilie mambo yanayoleta amani na mambo ya kujengana.”—ROM. 14:19.

WIMBO 113 Amani Tuliyo Nayo

MUHTASARIa

1. Wivu uliathirije familia ya Yosefu?

YAKOBO aliwapenda wanawe wote, lakini alimpenda sana Yosefu mwana wake ambaye alikuwa na umri wa miaka 17. Ndugu za Yosefu walitendaje? Walianza kumwonea wivu, na wivu huo ukawafanya waanze kumchukia. Yosefu hakuwa amefanya jambo lolote ambalo lingewafanya ndugu zake waanze kumchukia. Ingawa hivyo, walimuuza Yosefu utumwani na kumdanganya baba yao kwamba mwanawe mpendwa alikuwa ameuawa na mnyama wa mwituni. Wivu ulisababisha wavuruge amani ya familia na kuufanya moyo wa baba yao uhuzunike sana.—Mwa. 37:3, 4, 27-34.

2. Kulingana na Wagalatia 5:19-21, kwa nini wivu ni hatari sana?

2 Katika Maandiko, husuda au wivub unaorodheshwa miongoni mwa ‘matendo hatari ya mwili’ ambayo yanaweza kumfanya mtu asistahili kurithi Ufalme wa Mungu. (Soma Wagalatia 5:19-21.) Kwa kawaida, husuda au wivu ndiyo chanzo cha tabia nyingine zenye kudhuru kama vile chuki, mizozo, na milipuko ya hasira.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Kisa cha ndugu za Yosefu kinaonyesha jinsi kuwa na wivu kunavyoweza kuharibu uhusiano mzuri uliopo na kuvuruga amani katika familia. Ingawa hatuwezi kufanya kama ndugu za Yosefu walivyofanya, sisi sote tuna moyo wenye hila na usio mkamilifu. (Yer. 17:9) Hivyo, haishangazi kwamba nyakati nyingine tunahitaji kupambana na hisia za wivu. Acheni tuchunguze baadhi ya mifano ya kuonya katika Biblia ambayo inaweza kutusaidia kutambua sababu zinazoweza kufanya hisia za wivu zitie mizizi moyoni mwetu. Kisha tutachunguza njia hususa za kushinda wivu na kuendeleza amani.

WIVU UNAWEZA KUSABABISHWA NA NINI?

4. Kwa nini Wafilisti walimwonea wivu Isaka?

4 Ufanisi wa kimwili. Isaka alikuwa tajiri, na Wafilisti walimwonea wivu kwa sababu ya ufanisi wake. (Mwa. 26:12-14) Hata walifukia visima ambavyo alitegemea ili kunywesha mifugo yake. (Mwa. 26:15, 16, 27) Kama Wafilisti hao, baadhi ya watu leo huwaonea wivu wale walio na vitu vingi zaidi vya kimwili kuliko wao. Hawatamani tu kuwa na vitu ambavyo wengine wanavyo, bali pia wanatamani watu hao wavipoteze vitu hivyo.

5. Kwa nini viongozi wa kidini walimwonea Yesu wivu?

5 Wengine wanapopendwa zaidi. Viongozi wa dini ya Kiyahudi walimwonea Yesu wivu kwa sababu alipendwa sana na watu wa kawaida. (Mt. 7:28, 29) Yesu alikuwa mwakilishi wa Mungu, na alikuwa akifundisha kweli. Ingawa hivyo, viongozi hao wa kidini walieneza uwongo mbaya sana na maneno ya uchongezi ili kumchafulia Yesu jina. (Marko 15:10; Yoh. 11:47, 48; 12:12, 13, 19) Tunapata onyo gani kutokana na simulizi hilo? Ni lazima tupinge mwelekeo wowote wa kuwaonea wivu ndugu na dada walio na sifa zinazowafanya wapendwe sana kutanikoni. Badala ya kuwaonea wivu, tunapaswa kujitahidi kuiga matendo yao ya upendo.—1 Kor. 11:1; 3 Yoh. 11.

6. Diotrefe alionyeshaje kwamba ana wivu?

6 Mapendeleo ya kitheokrasi. Katika karne ya kwanza, Diotrefe aliwaonea wivu wale waliokuwa wakiongoza katika kutaniko la Kikristo. Alitaka “kuwa wa kwanza” miongoni mwa ndugu na dada kutanikoni, hivyo alieneza maneno mabaya ili kumharibia sifa mtume Yohana na ndugu wengine waliokuwa na madaraka. (3 Yoh. 9, 10) Ingawa huenda tusifikie hatua ya Diotrefe, inawezekana sisi pia tukaanza kumwonea wivu Mkristo mwenzetu aliyepata pendeleo fulani tulilotamani—hasa ikiwa tunahisi kwamba sisi pia tunastahili kupata pendeleo hilo, na kwamba tunaweza kulishughulikia vizuri zaidi kuliko yeye.

Mkusanyo wa picha: 1. Ua la mwituni lililositawi likiwa limetia mizizi kwenye udongo mzuri. 2. Ua hilohilo likiwa limesongwa na magugu. 3. Dada watatu wakizungumza pamoja kwa shangwe kwenye Jumba la Ufalme huku dada mwingine akisimama peke yake akiwa amekasirika.

Moyo wetu ni kama udongo, na sifa zetu nzuri ni kama maua maridadi. Lakini wivu ni kama magugu yenye sumu. Wivu unaweza kusonga sifa nzuri kama vile upendo, huruma, na fadhili na kufanya zisisitawi (Tazama fungu la 7)

7. Wivu unaweza kutuathirije?

7 Wivu ni kama magugu yenye sumu. Mbegu ya wivu inapotia mizizi moyoni mwetu, inaweza kuwa vigumu kuing’oa. Wivu hurutubishwa na hisia nyingine zisizofaa, kama vile kiburi, ubinafsi, na roho ya mashindano. Wivu unaweza kusonga sifa nzuri kama vile upendo, huruma, na fadhili na kufanya zisisitawi. Mara tu tunapoona wivu ukichipuka, tunahitaji kuung’oa kutoka moyoni mwetu. Tunaweza kuushindaje wivu?

SITAWISHA UNYENYEKEVU NA HALI YA KURIDHIKA

Mkusanyo wa picha: 1. Ua la mwituni lililositawi likiwa limetia mizizi kwenye udongo mzuri. 2. Mtu aking’oa magugu kuzunguka ua hilo la mwituni. 3. Dada wanne wakizungumza pamoja kwa shangwe kwenye Jumba la Ufalme.

Tunaweza kufanya nini ili tushinde wivu ulio kama magugu? Kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, tunaweza kung’oa wivu na kupanda unyenyekevu na hali ya kuridhika (Tazama fungu la 8 na 9)

8. Ni sifa gani zinazoweza kutusaidia kushinda wivu?

8 Tunaweza kushinda wivu kwa kusitawisha unyenyekevu na hali ya kuridhika. Moyo wetu unapofurika sifa hizo nzuri, wivu hautapata nafasi ya kusitawi. Unyenyekevu utatusaidia tusijifikirie kupita kiasi. Mtu mnyenyekevu hahisi kwamba anastahili kupata mengi zaidi kuliko wengine. (Gal. 6:3, 4) Mtu aliyeridhika anatosheka na kile alicho nacho na hajilinganishi na wengine. (1 Tim. 6:7, 8) Mtu mnyenyekevu na aliyeridhika anapoona mwingine akipata kitu kizuri, anafurahi pamoja naye.

9. Kulingana na Wagalatia 5:16 na Wafilipi 2:3, 4, roho takatifu itatusaidia kufanya nini?

9 Tunahitaji msaada wa roho takatifu ya Mungu ili tuepuke wivu na kusitawisha unyenyekevu na hali ya kuridhika. (Soma Wagalatia 5:16; Wafilipi 2:3, 4.) Roho takatifu ya Yehova inaweza kutusaidia tuchunguze mawazo yetu ya ndani kabisa na pia nia yetu. Kwa msaada wa Mungu, tunaweza kung’oa mawazo na hisia zenye kudhuru na kupanda mawazo na hisia zinazojenga. (Zab. 26:2; 51:10) Fikiria mfano wa Musa na Paulo, wanaume ambao walifanikiwa kushinda mwelekeo wa kuwa na wivu.

Musa, Yoshua, na Waisraeli fulani wamesimama karibu na hema la mkutano. Yoshua anamwomba Musa awakataze wanaume wawili wanaotenda kama manabii.

Mwisraeli mwenye umri mdogo anakimbia kwa Musa na Yoshua ili kuwajulisha kwamba wanaume wawili kambini wanatenda kama manabii. Yoshua anamwambia Musa awazuie wanaume hao, lakini Musa anakataa. Badala yake, anamwambia Yoshua kwamba anafurahi kuwa Yehova amewapa wanaume hao wawili roho Yake. (Tazama fungu la 10)

10. Musa alijaribiwa na hali gani? (Tazama picha kwenye jalada.)

10 Musa alikuwa na mamlaka kubwa juu ya watu wa Mungu, lakini hakuruhusu wivu umfanye ang’ang’anie pendeleo hilo. Kwa mfano, katika pindi moja, Yehova alichukua sehemu ya roho yake takatifu kutoka kwa Musa na kuwapatia wazee fulani wa Israeli waliokuwa wamesimama karibu na hema la mkutano. Muda mfupi baada ya hapo, Musa alisikia kwamba wazee wawili ambao hawakuwepo kwenye hema la mkutano walikuwa pia wamepokea roho takatifu na kuanza kutenda kama manabii. Musa alitendaje Yoshua alipomwambia awakataze wazee hao wawili? Uangalifu ambao Yehova aliwaonyesha wanaume hao wawili haukumfanya Musa awaonee wivu. Badala yake, alitenda kwa unyenyekevu na kushangilia pamoja nao kwa sababu ya pendeleo walilopata. (Hes. 11:24-29) Tunajifunza nini kutoka kwa Musa?

Mkusanyo wa picha: 1. Kwenye mkutano wa baraza la wazee, ndugu mwenye umri mkubwa anaombwa amzoeze mzee wa kutaniko mwenye umri mdogo zaidi ili aweze kuongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi. 2. Mzee mwenye umri mdogo zaidi akiongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi huku ndugu mwenye umri mkubwa akiwa ameketi na kusikiliza. 3. Ndugu mwenye umri mkubwa akimpa mkono mzee mwenye umri mdogo zaidi na kumpongeza.

Wazee Wakristo wanaweza kuigaje unyenyekevu wa Musa? (Tazama fungu la 11 na 12)c

11. Wazee wanaweza kumwigaje Musa?

11 Ikiwa wewe ni mzee wa kutaniko, je, umewahi kuombwa umzoeze ndugu mwingine ili ashughulikie pendeleo ambalo unalipenda sana? Kwa mfano, huenda unapenda mgawo wa kuongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi kila juma. Lakini ikiwa wewe ni mnyenyekevu kama Musa, hutakuwa na hofu ukiombwa umzoeze ndugu mwingine, ili baada ya muda, aweze kushughulikia pendeleo hilo. Badala yake, utafurahia kumpa msaada ndugu yako.

12. Wakristo wengi leo wanaonyeshaje unyenyekevu na hali ya kuridhika?

12 Fikiria hali nyingine ambayo ndugu wengi wenye umri mkubwa wanakabili. Kwa miaka mingi, wametumikia wakiwa waratibu wa baraza la wazee. Lakini wanapofikisha umri wa miaka 80, wanaacha mgawo wao kwa hiari. Waangalizi wa mzunguko wanaofikisha umri wa miaka 70 wanaacha mgawo wao kwa unyenyekevu na kukubali mgawo tofauti wa utumishi. Na katika miaka ya hivi karibuni, Wanabetheli wengi kote duniani wamepata migawo mipya ya kwenda shambani. Ndugu na dada hao waaminifu hawana hisia za uchungu kuelekea wale wanaoshughulikia migawo ambayo walikuwa wakiifurahia.

13. Kwa nini Paulo angeweza kushawishika kuwaonea wivu wale mitume 12?

13 Mtume Paulo ni mfano mwingine wa mtu aliyesitawisha unyenyekevu na hali ya kuridhika. Paulo hakuruhusu wivu usitawi moyoni mwake. Alitimiza huduma yake kwa bidii, lakini alisema hivi kwa unyenyekevu: “Mimi ni mdogo zaidi kati ya mitume, nami sistahili kuitwa mtume.” (1 Kor. 15:9, 10) Wale mitume 12 walimfuata Yesu wakati wa huduma yake duniani, lakini Paulo alikuja kuwa Mkristo baada ya kifo na ufufuo wa Yesu. Ingawa mwishowe, Paulo aliwekwa rasmi kuwa “mtume kwa mataifa,” hakupata pendeleo la kuwa mmoja wa wale mitume 12. (Rom. 11:13; Mdo. 1:21-26) Badala ya kuwaonea wivu wale mitume 12 ambao walikuwa wameshirikiana kwa ukaribu pamoja na Yesu, Paulo aliendelea kuridhika na pendeleo alilokuwa nalo.

14. Tutafanya nini ikiwa tumeridhika na tuna sifa ya unyenyekevu?

14 Tukiridhika na kuwa wanyenyekevu, tutakuwa kama Paulo na tutawaheshimu wale ambao Yehova amewapa mamlaka. (Mdo. 21:20-26) Ameweka mpango kwamba wanaume waliowekwa rasmi waongoze katika kutaniko la Kikristo. Licha ya kwamba wao si wakamilifu, Yehova anawaona ‘wanaume hao kuwa zawadi.’ (Efe. 4:8, 11) Tunapowaheshimu wanaume hao waliowekwa rasmi na kufuata mwongozo wao kwa unyenyekevu, tunaendelea kukaa karibu na Yehova na kufurahia amani pamoja na Wakristo wenzetu.

‘FUATILIA MAMBO YANAYOLETA AMANI’

15. Tunahitaji kufanya nini?

15 Hatuwezi kuwa na amani kati yetu ikiwa tutaruhusu wivu usitawi. Tunahitaji kung’oa kabisa wivu kutoka katika moyo wetu na kuepuka kupanda hisia za wivu katika mioyo ya wengine. Ni lazima tuchukue hatua hizo muhimu ili tutii amri ya Yehova ya ‘kufuatilia mambo yanayoleta amani na mambo ya kujengana.’ (Rom. 14:19) Ni mambo gani hususa tunayoweza kufanya ili kuwasaidia wengine washinde wivu, na tunaweza kufanya nini ili kuendeleza amani?

16. Tunaweza kuwasaidiaje wengine washinde wivu?

16 Mtazamo na matendo yetu yanaweza kuwaathiri sana wengine. Ulimwengu unataka mtu ‘ajionyeshe’ vitu alivyo navyo. (1 Yoh. 2:16) Lakini mtazamo huo huchochea wivu. Tunaweza kuepuka kuwachochea wengine kuwa na wivu kwa kutozungumza mara kwa mara kuhusu vitu tunavyomiliki au tunavyopanga kununua. Pia, tunaweza kuepuka kuchochea hisia za wivu kwa kuwa na kiasi inapohusu mapendeleo tuliyo nayo kutanikoni. Ikiwa tutazungumza sana kuhusu mapendeleo tuliyo nayo, tutakuwa tukitengeneza mazingira ya wivu kusitawi. Kinyume cha hilo, tunapowaonyesha wengine upendezi wa kibinafsi na kutambua mambo mazuri wanayotimiza, tunawasaidia waridhike na tutaendeleza umoja na amani kutanikoni.

17. Ndugu za Yosefu walifanikiwa kufanya nini, na kwa nini?

17 Tunaweza kushinda pambano dhidi ya wivu! Fikiria tena mfano wa ndugu za Yosefu. Miaka mingi baada ya kumtendea vibaya Yosefu, walikutana naye tena nchini Misri. Kabla ya Yosefu kujitambulisha kwa ndugu zake, aliwajaribu ili kujua ikiwa walikuwa wamebadilika. Aliwaandalia mlo na akampa chakula kingi zaidi Benjamini, ndugu yao mdogo. (Mwa. 43:33, 34) Lakini hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba ndugu hao walimwonea wivu Benjamini. Badala yake, walimjali kikweli ndugu yao na pia Yakobo, baba yao. (Mwa. 44:30-34) Kwa kuwa ndugu za Yosefu walikuwa wameacha kuwa na wivu, walifanikiwa kurudisha amani katika familia yao. (Mwa. 45:4, 15) Vivyo hivyo, ikiwa tutang’oa hisia zozote tulizo nazo za wivu, tutafanya familia yetu na kutaniko letu liwe na amani.

18. Kulingana na Yakobo 3:17, 18, ni nini kitakachotokea ikiwa tutasitawisha hali zenye amani?

18 Yehova anataka tushinde wivu na tufuatilie amani. Ni lazima tujitahidi sana ili kufanya mambo hayo mawili. Kama tulivyoona katika makala hii, tuna mwelekeo wa kuwaonea wengine wivu. (Yak. 4:5) Na tumezungukwa na ulimwengu unaochochea wivu. Lakini ikiwa tutasitawisha unyenyekevu, hali ya kuridhika, na uthamini, hatutakuwa na wivu. Badala yake, tutasitawisha hali zenye amani zitakazosaidia kufanya tunda la uadilifu lisitawi.—Soma Yakobo 3:17, 18.

UNGEJIBUJE?

  • Roho takatifu inaweza kutusaidiaje kushinda wivu?

  • Unyenyekevu na hali ya kuridhika inaweza kutusaidiaje kushinda wivu?

  • Mtazamo wetu mzuri unaweza kuwasaidiaje wengine kushinda wivu?

WIMBO 130 Uwe Mwenye Kusamehe

a Tengenezo la Yehova lina amani. Lakini amani hiyo inaweza kuvurugika ikiwa tutaruhusu hisia za wivu zisitawi. Katika makala hii, tutazungumzia mambo yanayosababisha wivu. Pia, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kushinda tabia hiyo yenye kudhuru na jinsi ya kuendeleza amani.

b UFAFANUZI WA MANENO: Kama inavyoonyeshwa katika Biblia, husuda au wivu haumfanyi tu mtu atamani kuwa na vitu ambavyo wengine wanavyo bali pia humfanya atamani wavipoteze vitu hivyo.

c MAELEZO YA PICHA: Wakati wa mkutano wa baraza la wazee, ndugu mwenye umri mkubwa ambaye ni kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi anaombwa amzoeze mzee mwenye umri mdogo zaidi jinsi ya kushughulikia jukumu hilo. Ingawa ndugu mwenye umri mkubwa anapenda mgawo wake, anaunga mkono kwa moyo wote uamuzi wa wazee kwa kumpa ndugu huyo mapendekezo hususa na kumpongeza kutoka moyoni.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki