Je! Wewe Ni Mgeni Mwenye Busara?
JE! WEWE ni mgeni wa namna gani? Ni nini kusudi lako la kutembelea watu? Je! watamani kuwa mgeni wa wale wawezao kuandalia chakula kilicho bora zaidi? Je! wautafuta mwaliko wa wale walio wakuu, matajiri au wenye uwezo?
Ulimwengu unayatafuta mambo hayo. Wengi wamekufanya ‘kujulikana sana na jamii’ shughuli yao ya maisha. Orodha ya “Nani ni Nani” ndicho kiongozi chao. Lakini kitabu cha Biblia cha Mithali chaonyesha wazi uongo wa shughuli hii nacho kinatoa onyo litakalomsaidia mtu kuepuka mtego uliomo humo. Mwandikaji mwenye hekima anasema:
“[Wewe] utakapoketi kula chakula pamoja na mtawala, mwangalie sana yeye aliye mbele yako. Tena ujitie kisu kooni, kama ukiwa mlafi. Usivitamani vyakula vyake vya anasa; kwa maana ni vyakula vya hila.”—Mit. 23:1-3.
Mithali inakuonya ‘wewe’ msomaji juu ya mwenendo wako mbele ya wale walio na mamlaka, ikionya juu ya hatari ya kujaribu kuwa na ushirika wa siri mno na watu wenye uwezo. Si watu wengi wapatao kuketi mezani pa mfalme wa kweli, lakini nyakati nyingine wanakula mezani pa mtu mwenye mamlaka. Kwa kawaida kuna vyakula vya namna nyingi, divai nzuri, na vinginevyo, vikimshawishi mtu kutokujizuia. Mgeni katika meza kama hiyo amepaswa awe mwangalifu mara mbili asije akajipendekeza kupita kadiri. Imempasa aizuie hamu yake—kwa usemi wa mfano, ‘ajitie kisu kooni’—zaidi ikiwa yeye ni “mlafi,” anayeelekezwa kwa vyepesi katika kula au kunywa mno. Ikiwa ni mwenye hekima, bila shaka mgeni atauangalia mwenendo wake wote katika hali hii, kwa maana hataki asemekane kuwa asiye na kiasi au mwenye pupa na mtu huyo mwenye mamlaka.
“Usivitamani vyakula vyake vya anasa; kwa maana ni vyakula vya hila,” yaonya mithali. Mgeni hapaswi kudanganyika afikiri kwamba mwaliko huu wa kula kwa kawaida unamaanisha kwamba yeye ni mtu aliyependelewa, wala haimpasi kujaribu kufanya urafiki mwingi mno kwa kiburi na mtu huyo. Hii ingeweza kuelekeza kwenye aibu yake na hata maanguko. Kifikirie kisa cha Hamani, aliyehasirika wakati ule ule alipofikiri yeye alikuwa ndiye rafiki mkubwa sana wa Mfalme Ahasuero wa Uajemi.—Esta 5:8-11; 7:1-10.
UFAHAMU WAHITAJIWA
Kwa upande mwingine, huenda wewe ukawa mtu aliyemo katika hali ya kumtendea mtu fulani wema. Au huenda ukawa unayo mamlaka kama mzee katika kundi la Kikristo. Uhitaji wa kutumia ufahamu unapokuwa mgeni katika nyumba ya mtu mwingine unakaziwa baada ya mistari michache: “Usile mkate wa mtu mwenye husuda”; asema Mfalme Sulemani wa kale, “wala usivitamani vyakula vyake vya anasa; maana aonavyo nafsini mwake, ndivyo alivyo. Akuambia, Haya, kula, kunywa; lakini moyo wake hauwi pamoja nawe. Tonge lile ulilokula utalitapika, na maneno yako matamu yatakupotea.”—Mit. 23:6-8.
Onyo hili linatumika kwa watu wote. Huenda ukakubali mwaliko wa mtu na kuona kwamba kwa nje anaonekana mkarimu sana na mchangamfu, akikuambia ule na kunywa bila wasiwasi. Lakini kwa kweli analichungulia na kulionea kijicho kila tonge unalolila. Kwa kuwa yeye si wa namna ya watoao kitu kwa moyo wa ukunjufu, yeye anatazamia kitu fulani kwa ajili ya anachokitoa. Kwa hiyo yeye amekwisha kutumainia kitu fulani cha siri, akifanya hivi “nafsini mwake”—ndiyo njia yake ya maisha, namna atendavyo. Kama ukivitamani vitu vyake vizuri, huenda ukawa mgeni wa mara kwa mara nyumbani mwake. Hii ingekuwa kucheza mikononi mwake. Kwa maana matembezi yako ya mara kwa mara yaweza kuja kukufanya ujisikie una masharti, yakikuweka kidogo chini ya uwezo wake. Ndivyo yeye alivyoona.
Usipotumia ufahamu na kuchukua hatua ya kuukomesha ushirika huo wa ndani mapema utanaswa bila ya kujua, kama vile katika mtego, nawe utaona ni vigumu sana kutoka. Kwa mfano, ikiwa wewe ni mzee wa Kikristo na mtu yule mwingine anakuja kuhitaji kuonyeshwa makosa au kukaripiwa, huenda ukasita-sita kufanya hivyo. Kwa maana unajisikia kidogo una deni yake, kunakuwako haya fulani, labda woga. Huenda ukajipa mwenyewe udhuru usiufanye wajibu wako kama mwangalizi kwa sababu huenda ukaonekana kuwa asiye na shukrani ukiisha kuukubali “ukaribishaji” wake—ijapokuwa kwa kweli, kama ulijua au sivyo, ‘moyo wake haukuwa pamoja nawe’ wakati huo wote. Au huenda ukaogopa kwamba atakukasirikia na kukukumbusha, hata mbele ya wengine, kwamba ulikuwa na nia sana ya kula chakula chake kizuri.
Ndiyo, kupendezwa kwako na vitu vyake vizuri huenda kukakufanya uwe mwenye kusita-sita usije ukauhatirisha uhusiano wako ‘mtamu’ naye. Huenda hata ukafikia hatua ya kupendelea, ukimpendelea mtu huyu akiwamo katika ugomvi na mwingine, kwa njia hiyo ukifanya udhalimu, ukimdhuru mtu mwingine na kuleta madhara juu ya kundi na shutumu juu yako mwenyewe.—Mit. 17:23.
Kisha, “tonge lile ulilokula utalitapika, na maneno yako matamu yatakupotea.” Unapougundua mtego uliomo ndani yake, kama ilivyo, inakuchukiza kukifikiria chakula chake. Waona kwamba urafiki mwema, ufaao ambao ulifikiri ulikuwa unakuza haukusitawi. Maneno matamu ya urafiki na shukrani, mambo yaliyozungumzwa ili yajenge kiroho na kutia moyo, yamepotezwa bure, na vilevile wakati wako. Unajisikia kutaka ‘kutapika’ kweli kweli.
Kanuni inayosemwa katika mithali vile-vile ingetumika kwa mambo mengine yasiyo chakula. Twaweza kuingia katika hali kama hiyo kwa kuipenda nyumba iliyo nzuri na ya starehe ya mkaribishaji wetu, kidimbwi chake cha kuogelea, mashua yake au vitu vingine vyenye kustarehesha au kitu cha kujifurahishia awezacho kutoa.
WAKATI MWINGINE WA UANGALIFU
Ukosefu wa uangalifu ufaao na busara waweza kumwelekeza mtu kwenye namna nyingine ya hali isiyotamanika. Mithali 25:17 yasema: “Mguu wako usiingie katika nyumba ya jirani yako ila kwa kiasi; asije akakukinai na kukuchukia.” Hata rafiki mwema ana uhitaji fulani wa kuwa peke yake, nayo matembezi yako marefu mno, ya mara nyingi mno au ya kipumbavu yaweza kumfanya afikie hatua ambapo kwa hakika anaona uchungu kwa ajili ya kuja kwako.
Tena, onyo hili lingetumika kwa waangalizi wa Kikristo vilevile katika kutembelea akina ndugu wakatoe msaada wa kiroho. Imewapasa wawe na busara, wakijaribu kutokutembelea nyakati zisizofaa. Ikiwa kunao ugumu ulio hakika wa kuzungumza, mara nyingi ni hekima kupanga mipango mapema. Haiwapasi waangalizi watembelee mara nyingi sana hata kuichukiza jamaa, nao imewapasa wajiepushe na kuchukua muda mrefu sana kwa ujinga katika matembezi yao.
Kwa kweli, inahitaji ufahamu, heshima na kupendezwa kwa kweli na hali njema ya mtu yule mwingine ili kuwa mgeni mwema.