Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 5/15 kur. 223-229
  • Kupanda Mbegu za Habari Njema Katika Ulimwengu Wenye Vita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupanda Mbegu za Habari Njema Katika Ulimwengu Wenye Vita
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “KUONGEZEKA KATIKA ULIMWENOU WOTE”
  • IMANI NA UPENDO NDANI YA MOYO
  • Kusimuliwa kwa Habari Njema Kwazaa Matunda Ulimwenguni Pote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Manufaa za Kupenda Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • ‘Mungu Ndiye Anayeikuza’!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Ufalme wa Mungu—Je, Unapata Maana Yao?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 5/15 kur. 223-229

Kupanda Mbegu za Habari Njema Katika Ulimwengu Wenye Vita

“Tumaini hili mlilisikia kwanza kwa kusimuliwa kwa kweli ya zile habari njema zilizojitokeza kwenu, hata kama vile kunavyozaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote.”​—Kol. 1:5, 6, NW.

1. Ni namna gani mbili za mbegu zinazopandwa ulimwenguni pote, na n’nani wanaozipanda?

NAMNA mbili za mbegu zinapandwa ulimwenguni pote leo​—⁠mbegu ya habari njema za amani ya milele na mbegu ya maenezi ya vita. Mbegu hii ya pili inapandwa na walio wengi, mbegu iliyotajwa kwanza na walio wachache.

2. (a) Ni sheria gani inayotimilika kwa habari ya kinachopandwa, si katika mambo ya ukulima tu, lakini vile vile katika mambo ya mataifa yote? (b) Ni kanuni gani kama ilivyotajwa na Paulo inayodumu kuwa kweli kwa habari ya kupanda mbegu za habari njema?

2 Mataifa yenye silaha yamo katika shughuli ya kupanda mbegu ya utayarishaji wa vita. Katika mambo ya ukulima na katika mambo ya ukamatano wa mataifa yote vile vile sikuzote inatokea kwamba kile kinachopandwa kinazaa, kinatokeza namna yake chenyewe. Ndivyo ambavyo imekuwa wakati wote tangu mwanadamu wa kwanza alipoanza ukulima. (Mwa. 3:17-19; 4:1, 2; 1:11, 12; 9:20) Sheria hii vile vile inatenda pasipo huruma katika maisha za mataifa. Unabii wa kimungu umekuwa kweli juu ya mataifa mengi, wala si juu ya Israeli wa kale peke yake: “Kwa maana wao hupanda upepo, nao watavuna tufani.” (Hos. 8:7) Kwa kuwa wingi wa wanadamu wamejitia katika kupanda mbegu ya utayarishaji wa vita, namna gani juu ya mbegu ya habari njema za amani? Je! yaweza kusitawi na kuzaa matunda na ongezeko? Ndiyo, kwa maana imeonyeshwa mara nyingi kuwa kanuni iliyo hakika kwamba “cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” (Gal. 6:7) Muumba wa mwanadamu aliiimarisha hivyo.

3. (a) Ni wakati gani kazi hii ya kuipanda mbegu ya amani ya habari njema ilipoanza? (b) Ni uamuzi gani tupaswao kufanya juu ya kupanda katika karne hii ya 20 yenye vita?

3 Leo wale wanaopanda mbegu ya habari njema za amani ya milele kwa kweli wanaendesha kazi iliyoanza karne kumi na tisa zilizopita. Sasa wanaiendesha kazi hii kwa kadiri ambavyo kwa vyo vyote lazima itazamwe na ulimwengu wote. Yaliyoonwa na wapanzi wa mbegu huko nyuma katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida yanaonwa na wapanzi wa mbegu wa leo katika karne hii ya 20 yenye vita. Wapenda amani ya milele duniani yawapasa kupendezwa. Lakini lazima sisi sote tuamue juu ya kama tunapenda kuwa wapanzi wa maenezi ya vita au wapanzi wa habari njema za amani. Uamuzi wetu ndio utakaoamua matokeo juu yetu.

4, 5. (a) Huko nyuma kuanzia mwaka wa 60 wa karne ya kwanza C.E., ni msiba gani wenye kushtua kwa kidini uliokuwa ukikaribia? (b) Kwa sababu ya msiba huo, ni kitu gani kilichotajwa na Yesu ambacho kingeweza kuleta faraja kwa Myahudi aliyekikubali’

4 Katika muda wa kuanzia mwaka wa 60 wa karne ya kwanza C.E. hali ilikuwa ya kushtua sana ikiwako chuki juu ya Milki ya Kirumi. Zaidi hii ilikuwa hivyo katika Mashariki ya Kati katika jimbo la Kirumi la Uyahudi. Uasi ulikuwa ukipangwa juu ya ukaaji na utawala wa nchi hiyo wa majeshi ya Kirumi chini ya usimamizi wa kipagani wa Kirumi. Mwisho wenye jeuri wa mji mtakatifu wa Yerusalemu ulikuwa ukikaribia. Mji huo kama mahali pakuu pa ibada ya Kiyahudi ulikuwa katika wakati wake wa mwisho. Kizazi cha Wayahudi ambao Yesu Kristo mwenyewe alihutubia mnamo huduma yake ya waziwazi duniani ndicho alichosema kisingepita mpaka Yerusalemu na hekalu lake lenye fahari vimeharibiwa. (Mt. 24:34, 1-22) Historia yakumbusha kwamba uharibifu huu wenye kuogofya ulikuja katika mwaka wenye maombolezo wa 70 C.E. Je! kuna lo lote ambalo lingeweza kuwaepusha Wayahudi na kutokuhuzunishwa kabisa katika uharibifu huo wa kidini wenye kushtua? Ndiyo, lilikuwako! Kulikuwako jambo moja tu lililoweza kufariji moyo wa Kiyahudi, mradi moyo wa Kiyahudi ungelikubali. Hilo lilikuwa nini? Yesu Kristo alilitaja wakati alipokuwa akiutoa unabii wake ulio mzuri sana juu ya mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi huko katika Mashariki ya Kati. Jambo hili lenye kufurahisha, lenye kuchangamsha alilizungumza alipokwisha kusimulia mateso ambayo yangewapata wanafunzi wake waaminifu. Alisema:

5 “Lakini yeye atakayevumilia hata mwisho ndiye atakayeokolewa. Na HABARI NJEMA hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakuja.”​—Mt. 24:13, 14, NW.

6. Yesu alitangaza habari za namna gani, nazo zilisimulia ufalme gani?

6 Uharibifu wenye msiba wa Yerusalemu na hekalu lake ulikuwa habari zenye kuhuzunisha kwa Wayahudi kuuzunguka ulimwengu ambao wangali waliutazamia mji huo wa kidunia kama mahali pao pakuu pa kidini. Kwao zilikuwa habari mbaya kupita zote. Lakini habari ambazo Yesu Kristo alizitangaza wakati wote wa huduma yake ya kidunia zilikuwa HABARI NJEMA, injili! Lakini habari njema za ufalme gani? Haukuwa ufalme ambao Yesu Kristo alisema ungeinuka juu ya ufalme wakati ule ule ambapo taifa lingeinuka juu ya taifa, kufuatwa na njaa, magonjwa ya kipuku na matetemeko ya dunia katika mahali pamoja baada ya pengine. Ulikuwa ndio ufalme wa pekee aliouendeleza Yesu na kuutangaza. Ulikuwa ndio ule alioutaja katika unabii ule ule, akiuita “ufalme wa mbinguni.” (Mt. 24:7; 25:1) “Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”​—Luka 21:10, 31.

7. (a) Mbele ya uharibifu wa Yerusalemu, n’nini kilichopaswa kutimilizwa na wanafunzi wa Kristo? (b) Kwa sababu gani uharibifu wa Yerusalemu haukuwashtua Wakristo, ukiwaacha wakiwa hoi?

7 Kwa hiyo, basi, hata mbele ya uharibifu wa Yerusalemu wa kidunia katika mwaka wa 70 C.E., kwa sababu ya uasi wake juu ya Milki ya Kirumi, “habari njema hizi” za ufalme wa Mungu, za ufalme wa mbinguni, zilipaswa kuhubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote, mataifa yaliyomo na yasiyokuwamo ndani ya Milki ya Kirumi. Kwa matokeo gani? Basi, majeshi ya Kirumi yalipouvunja Yerusalemu na hekalu lake, hili halikuwashtua waamini Mungu wa Kikristo, hata Wayahudi waliofanywa Wakristo. Kwa kweli hawa walikuwa wakiutazamia uharibifu huo. Wayahudi waliofanywa Wakristo katika Yerusalemu na katika sehemu yote nyingine ya jimbo la Uyahudi walitenda kwa kulitii shauri lililotolewa katika unabii wa Yesu; walikimbia kutoka Uyahudi na Yerusalemu upesi kama walivyoweza nyuma ya mazingira ya muda juu ya Yerusalemu ya majeshi ya Kirumi katika mwaka wa uasi wa Kiyahudi, mwaka wa 66 C.E. (Mt. 24:15-22; Luka 21:20-24; Marko 13:14-20) Wao walijua kwamba kuharibiwa kwa Uyahudi na Yerusalemu hakukumaanisha kuharibiwa kwa “ufalme wa mbinguni,” “ufalme wa Mungu.” Kwao hakuna mji wa kidunia uliouwakilisha ufalme wa Mungu tena. Wao waliliweka tumaini lao katika ufalme wa Mungu wa kimbinguni ambao ungekuja, ambao katika huo wangeshiriki.

8. (a) Wakristo walijawa na matumaini zaidi katika serikali gani, nalo hili lilionyeshwaje mpaka mwisho wa karne ya kwanza? (b) Hivyo ni akina nani waliowekewa mfano wa utendaji?

8 Uharibifu wa Yerusalemu uliwajaza matumaini zaidi kuliko wakati mwingine wo wote katika ufalme wa kweli wa Mungu wa Kimasihi. Uhakika ni kwamba wao waliendelea kuzitangaza habari njema za ufalme huo mpaka mwisho wenyewe wa karne ya kwanza, yajapokuwa mateso makali ya Milki ya Kirumi. Mtume wa Kikristo Yohana, aliyekufa karibu mwaka wa 100 C.E., aliupokea Ufunuo (kitabu kilichopangwa mwishoni mwa Biblia Takatifu) muda mfupi tu mbele ya kifo chake. Katika sura ya kwanza anaandika: “Mimi Yohana, ndugu yenu na mwenye kushiriki pamoja nanyi katika mateso na ufalme na subira ya Yesu Kristo, nalikuwa katika kisiwa kiitwacho Patmo, kwa ajili ya Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu.” (Ufu. 1:9) Kufikia hapo ‘habari njema za ufalme’ zilikuwa zimekwisha kuhubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote kwa kadiri kubwa hata zaidi kuliko ambavyo habari njema hizi zilivyokuwa zimehubiriwa mbele ya mwisho wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 C.E. Hivyo unabii wa Yesu juu ya kuhubiriwa kwa habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi ulimwenguni pote haukuwa umeshindwa. Hii iliweka mfano kwa kuhubiriwa kwa namna ile ile kwa “habari njema hizi za ufalme” katika mwisho wa taratibu ya mambo wa wakati wetu, ambao kwao unabii wa Yesu unatumika kwa njia ya kufikia upeo.

“KUONGEZEKA KATIKA ULIMWENOU WOTE”

9, 10. (a) Kuhubiriwa kwa habari njema ulimwenguni pote mbele ya uharibifu wa Yerusalemu kulishuhudiwa na nani, na namna gani? (b) Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo alijitiaje ndani katika mazungumzo na kundi asilolijua?

9 Kwamba kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme kulikotabiriwa kulitimilizwa mbele ya uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 C.E. ilishuhudiwa hata miaka mingi mbele ya msiba huo wa Kiyahudi. Ilishuhudiwa na nani? Na mtume wa Kikristo Paulo. Karibu na mwaka wa 60 au 61 C.E., alijikuta katika kifungo cha Kirumi katika nyumba ya faragha Rumi na katika minyororo. Mnamo miaka yake miwili au zaidi ya kufungiwa katika nyumba katika Rumi aliyaandikia makundi ya Kikristo katika Ugiriki na Asia Ndogo barua zilizoongozwa na roho ya Mungu. Mojawapo ya barua hizi liliandikiwa kundi katika mji wa Kolosai wa Asia Ndogo, uliokuwa karibu na miji ya Laodikia na Hierapoli ambapo vile vile palikuwa na makundi ya Kikristo. Uturuki ya kisasa iko katika maeneo haya leo. Mtume Paulo anaipeleka barua yake kwa jina lake mwenyewe na la Timotheo, mmisionari mwenzake. Paulo hakulianzisha kundi lililokuwa Kolosai, nayo barua yake yaonyesha kwamba hakufika huko hata kidogo. Lakini kupitia kwa Mkristo mwenzake mwenye kutembelea, Paulo alipata habari juu ya kundi hili la Kolosai. Alivutwa sana na ripoti hii iliyokuja kupitia kwake Epafra, hata akapendezwa kuiandika barua hii kwa Wakristo asiowajua. Anaanza, kwa kusema:

10 “Twamshukuru Mungu, Baba yake Bwana wetu Yesu Kristo, sikuzote tukiwaombea; tangu tuliposikia habari za imani yenu katika Kristo Yesu, na upendo mlio nao kwa watakatifu wote; kwa sababu ya tumaini mlilowekewa akiba mbinguni; ambalo habari zake mlizisikia zamani kwa neno la kweli ya Injili; iliyofika kwenu, kama ilivyo katika ulimwengu wote, na kuzaa matunda na kukua, kama inavyokua kwenu pia, tangu siku mlipoisikia mkaifahamu sana neema ya Mungu katika kweli; kama mlivyofundishwa na Epafra, mjoli wetu mpenzi, aliye mhudumu mwaminifu wa Kristo kwa ajili yenu; naye alitueleza upendo wenu [kwa kiroho].”​—Kol. 1:3-8.

11. (a) Kwamba kulimaanishwa kuhubiri ulimwenguni pote yaonyeshwaje katika Wakolosai 1:23? (b) Ni kwa njia gani hii ilivyokuwa hivyo juu ya kuhubiri wakati huo?

11 Wakati wa kuiandika barua hii Paulo, kama mmisionari mwenye ujuzi aliyesafiri sana, alikushuhudia kuhubiriwa kwa habari njema za ufalme ulimwenguni pote kwa ambayo anayoyasema katika utangulizi ulioko juu wa barua yake. Yeye anaandika juu ya “kusimuliwa kwa kweli ya zile habari njema zilizojitokeza kwenu, hata kama vile kunavyozaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote.” (Kol. 1:5, 6, NW) Kwamba anamaanisha kuhubiri ulimwenguni pote Paulo anahakikisha nyuma ya maneno fulani, anapozungumza juu ya ‘kutogeuzwa kwao na kuliacha tumaini la Injili mliyosikia habari zake, iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu; ambayo mimi Paulo nalikuwa mhudumu wake.’ (Kol. 1:23) Bila shaka, hii haikumaanisha kwamba kila mtu duniani chini ya mbingu alikuwa akifikiwa kwa kipekee. Ilimaanisha kwamba kuhubiriwa kwa habari njema kulikuwa kukisukumwa kwenye makao yote ya dunia inayokaliwa na watu chini ya mbingu na kwamba viumbe vyote vya kibinadamu, bila ya kujali lugha, rangi, kabila au taifa, vilikuwa vikipewa nafasi ya kuusikia ujumbe wa Ufalme. Haikuwako mipaka. Katika barua yake ya mapema kwa kundi katika Rumi (karibu mwaka wa 56 C.E.), Paulo alilionyesha kusudi lake la kuzipeleka habari njema Spania. Bara mbili za Amerika zilizoko mbali kuelekea magharibi hakuzijua wakati huo.​—Rum. 15:24.

12. Je! huo ndio uliokuwa utimizo kamili wa unabii juu ya kuhubiri, au n’nini kilichobakia?

12 Kuhubiriwa huku kwa “habari njema hizi za ufalme” na kundi la wakati huo lililokuwa dogo la wanafunzi wa Kristo mnamo karne ya kwanza katika Asia, Ulaya na Afrika kulikuwa katika utimizo wa unabii wa Biblia. (Mt. 24:14; Marko 13:10; Matendo 1:8) Lakini hakukukamilisha utimizo wa unabii. Ulipaswa kuwa na kifani kwa njia yenye kufikia upeo katika dunia nzima bara mbili za Amerika zikiisha kuvumbuliwa na watoka Ulaya na mbele ya uharibifu wa Yerusalemu mwasi wa mfano, Kristendomu wa kisasa, katika huu wakati wa mwisho wake tangu mwaka wa 1914 C.E.

13. Kulingana na Paulo, n’nini yaliyokuwa matokeo ya kueneza tumaini la Ufalme, kama ilivyoonyeshwa kwa habari ya Kolosai?

13 Matokeo ya kiroho ya kuenezwa huku kwa tumaini la Ufalme sasa yamepaswa yawe kama yale ya siku za mitume wake Yesu Kristo mnamo karne ya kwanza C.E. Kwa hiyo ebu na tuangalie ambavyo mtume Paulo anavyosema juu ya matokeo yake kwa habari ya kundi huko katika Kolosai, Asia Ndogo. Yeye anasema kwamba kwa Wakolosai kulikuwa kumekuwa “kusimuliwa kwa kweli ya zile habari njema zilizojitokeza kwenu, hata kama vile kunavyozaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote sawa na kunavyofanya vile vile miongoni mwenu.” (Kol. 1:5, 6, NW) Kwa hiyo “kusimuliwa” kwa neno lililonenwa ‘la kweli ya zile habari njema’ kulikuwa ‘kunazaa matunda’ ulimwenguni pote, kutia na Kolosai.

14, 15. (a) Hivyo Paulo alizifananisha habari njema na nini kama zilivyosimuliwa kwa njia ya kweli? (b) Maelezo yanayoonyeshwa hapa yanalingana na mfano gani uliotolewa na Yesu?

14 Hapa mtume Paulo anazifananisha “habari njema” zilizosimuliwa kwao kwa kweli na mbegu iliyopandwa udongoni. Udongo wenyewe ni mzuri nao wafaa, nayo mbegu yatia mizizi na kuchipuka na kuzaa matunda, matunda ya namna yake yenyewe. Mfano huu unalingana na mfano ambao Yesu Kristo aliutoa juu ya uwezo mbalimbali wa kuzaa wa udongo wa namna nne. Hivi ndivyo alivyosema:

15 “Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda. Hata alipokuwa akipanda, mbegu nyingine zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila; nyingine zikaanguka penye miamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara zikaota, kwa udongo kukosa kina; na jua lilipozuka ziliungua; na kwa kuwa hazina mizizi zikanyauka. Nyingine zikaanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikazisonga; nyingine zikaanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini.

16. Yesu mwenyewe alitoa maelezo gani juu ya mfano huu?

16 “Basi ninyi sikilizeni mfano wa mpanzi. Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia. Naye aliyepandwa penye miamba, huyo ndiye alisikiaye lile neno, akalipokea mara kwa furaha; lakini hana mizizi ndani yake, bali hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya neno, mara huchukizwa. Naye aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na lile shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai. Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini.”​—Mt. 13:3-8, 18-23.

17. (a) Mioyo ya Wakolosai ilikuwa kama nini katika mfano wa Yesu, na n’nani aliyekuwa amepanda mbegu ndani yao moja kwa moja? (b) Kwa hakika, “mbegu” ni nini, na katika hali gani?

17 Kulingana na ambavyo mtume Paulo alivyosikia kwa mgeni wake, Epafra, washiriki wa kundi la Kikristo katika Kolosai walikuwa wana mioyo iliyokuwa kama “udongo mzuri” uliosimuliwa na Yesu. Kwa hiyo “neno la ufalme” lililopandwa mioyoni mwao lilizaa matunda ya kadiri mbalimbali, kama vile 100, 60, 30. Mtume Paulo hakuwa amepanda mbegu kati ya mioyo ya Wakolosai, bali yaelekea huyu Epafra wa Kolosai ndiye aliyekuwa amefanya hivyo, kwa maana Paulo anamzungumza yeye katika barua kwa Wakolosai kama “Epafra, aliye mtu wa kwenu, mtumwa wa Yesu Kristo.” Vile vile Paulo anawaambia: “Kama mlivyofundishwa na Epafra, mjoli wetu mpenzi, aliye mhudumu mwaminifu wa Kristo kwa ajili yenu; naye alitueleza upendo wenu [kwa kiroho].” (Kol. 4:12; 1:7, 8; Filemoni 23) Huyu ‘mhudumu wa Kristo’ alikuwa akitenda kama wakili tu wa Mpanzi Mkuu wa mbegu, Yesu Kristo. Alisema Yesu: “Mbegu ni neno la Mungu.” (Luka 8:11) Ni “neno la ufalme.” Lakini siyo mbegu katika ghala, bali ni mbegu ‘inayopandwa,’ yaani, “neno la ufalme” la Mungu linalohubiriwa, kutangazwa, kufundishwa.

18. (a) Paulo aliendeleaje kuipanda “mbegu” katika nyumba yake ya kifungo? (b) “Mbegu” hii ina nini ndani yake, na ni kitu gani kilicho cha muhimu kwayo kutia mizizi katika mioyo ya kibinadamu?

18 Wanafunzi wale wanaojiunga pamoja chini ya Mpanzi Mkuu, Yesu Kristo, katika kuipanda, kuihubiri, kuitangaza, kuifundisha mbegu ya “neno la ufalme” ni “watendaji wa kazi pamoja nami kwa ajili ya ufalme wa Mungu,” kama anavyowaita mtume Paulo. (Kol. 4:11) Hata wakati Paulo alipokuwa huko katika nyumba ya kifungo Rumi, alifanya mengi zaidi kuliko kuandika barua, kama vile ile ya Wakolosai. “Akawakaribisha watu wote waliokuwa [kama vile Epafra] wakimwendea, akihubiri habari za ufalme wa Mungu, na kuyafundisha mambo ya Bwana Yesu Kristo, kwa ujasiri mwingi, asikatazwe na mtu.” (Matendo 28:30, 31) Kwa kuwa “mbegu” hii ya kiroho ndilo “neno la Mungu,” “neno la ufalme,” ndani yake mna habari njema, ujumbe wa tumaini, ujumbe wa serikali iliyo kuu kupita zote ya kuwabariki wanadamu wote, ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Ujumbe huu uliomo katika “mbegu” ni jambo ambalo yampasa mpokeaji wa “mbegu” alifahamu na kuuona ubora wake. Yampasa aipate maana yake, aielewe, kwa moyo wake. Kwa njia hii “mbegu” itatia mizizi moyoni mwake.

IMANI NA UPENDO NDANI YA MOYO

19. (a) Kulingana na Paulo, kusimuliwa kwa habari njema kulikuwa na matokeo gani ndani ya mioyo ya Wakolosai? (b) Kwa sababu ya “mbegu” iliyopandwa, kwa nini lazima kuwepo usitawi wa imani na upendo moyoni?

19 “Habari njema” zilikuwa na matokeo gani mioyoni mwa washiriki waliolifanyiza kundi katika Kolosai kama zilivyosimuliwa kwao kwa njia ya kweli? Zilikuwa na matokeo yaliyomvuta Paulo kuwaandikia barua yake bora, alipopata habari juu yake. Matokeo mioyoni mwao yalikuwa anayoyataja Paulo: “imani yenu katika Kristo Yesu, na upendo mlio nao kwa watakatifu wote,” “upendo wenu [kwa kiroho].” (Kol. 1:4, 8) Imani hiyo na upendo vilipaswa kusitawishwa mioyoni mwao ili “mbegu” ya “neno la Mungu” itie mizizi kuelekea chini na kuchipuka kuelekea juu na kujitokeza juu, hivyo ikizaa mbegu mpya zilizo hai, mara 30, 60 au 100 za ile mbegu ya kwanza. Lazima kuwemo usitawi huu moyoni kwanza mbele ya kuchipuka kunakozaa tena kile kilichopandwa ndani.

20. (a) Kwa sababu gani iliwapasa zaidi Mataifa kutumia imani ili waikubali “mbegu”? (b) Bila ya kujali kama ni Wayahudi au Mataifa iliwapasa kukubali mambo gani ya hakika yaliyo muhimu juu ya Yesu?

20 Kwa habari ya Mataifa, wasio Wayahudi, kama vile wengi wa kundi la Kolosai walivyokuwa, ilikuwa imechukua imani kwa upande wao kuikubali “mbegu” ya neno la Mungu. Iliwapasa kuiacha miungu mingi ya Kigiriki na ya Kirumi ambayo kwayo walikuwa wakf na kukaza imani yao sana juu ya Mungu wa pekee aliye hai na wa kweli, Muumba wa mbingu na nchi na wa vyote vilivyomo, ambaye jina lake ni Yehova. Lakini hata kama walikuwa Mataifa wasiotahiriwa au Wayahudi wa asili, iliwapasa vile vile kumwamini Yesu Kristo, kwamba Yesu huyu mzao wa Mfalme Daudi wa Yerusalemu alikuwa ndiye Masihi aliyeahidiwa au Kristo. Iliwapasa kuamini kwamba huyu ndiye aliyekuwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” Iliwapasa kuamini kwamba alikuwa “mzaliwa wa kwanza katika wafu” vile vile, kwa maana Yehova Mungu amemfufua kwa wafu kumweka kwenye uzima usiokoma mbinguni. Zaidi ya hayo, iliwapasa kuamini kwamba Yesu Kristo ndiye “kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa,” ambalo walitamani kuwa mali yake. Vile vile, kwamba “hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika,” kusudi kwamba filosofia zao za kipagani au mapokeo yao ya kidini yaliyofanyizwa na mwanadamu yasishikamanwe nayo tena.​—Kol. 1:15-18; 2:3, 8; Matendo 14:11-18.

21. (a) Iliwapasa Wakolosai kufanya nini na lile “neno” lililokuwa limewekwa vinywani mwao, na kwa sababu gani? (b) Ni sifa gani waliyopaswa kutumia na moyo wao iwavute wanene waziwazi?

21 Hayo ni mengine ya mambo ya muhimu yaliyokuwamo katika “kweli ya zile habari njema,” na katika mambo haya iliwapasa kuwa na imani kwa mioyo yao. Ilikuwa kama vile mtume Paulo alivyokuwa ameandika miaka fulani mapema kwa Warumi: “‘Neno’ la imani, tunalolihubiri. Kwa maana ukitangaza waziwazi [au, ukikiri] lile ‘neno lililomo kinywani mwako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, na kutumia imani moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua yeye kwa wafu, utaokolewa. Kwa maana kwa moyo mtu hutumia imani kwa ajili ya haki, bali kwa kinywa mtu hufanya tangazo la waziwazi [au, mtu hukiri] kwa ajili ya wokovu.” (Rum. 10:8-10, NW) Kwa maana mioyo ya Wakolosai ilikuwa kama “udongo mzuri,” wao walitumia imani kwa mioyo yao na kuikubali “mbegu” ya “neno la ufalme,” “neno la Mungu,” nao waliiacha itie mizizi moyoni mwao na kujionyesha yenyewe.

22, 23. (a) Iliwabidi Wakolosai hao kuamini Yesu alikuwa na cheo gani rasmi, na kwa hiyo wao walikuwa chini ya kanuni gani? (b) Kwa hiyo, kama vile Paulo mwandikaji wa barua, ni cheo gani cha serikali hiyo walichoshika, na ni amri gani ya Yesu waliyoshiriki kuitimiliza?

22 Pamoja na imani yao kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi au Kristo, iliwapasa kuamini kwamba Yehova Mungu alikuwa amemketisha penye mkono Wake mwenyewe wa kulia kama Kuhani-Mfalme, aliyetangulia kufananishwa na Melkizedeki mfalme wa Salemu wa kale. Kwa sababu hii, iliwapasa kuja chini ya ufalme wa kiroho wa Kristo. Ndiyo, iliwapasa kuamini kwamba Mungu “alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake.” (Kol. 1:13) Hawakuwa tu chini ya ufalme uliopo wa Mwana wa upendo wa Mungu, bali vile vile walikuwa “mabalozi badala ya Kristo” katika mpango wa Mungu wa “kupatanisha ufalme na yeye mwenyewe” kwa njia ya Kristo. (2 Kor: 5:19, 20, NW) Alipokuwa gerezani ambako Paulo aliiandikia barua yake kwa Wakolosai yeye alizungumza juu ya “uhuru wa kusema kuijulisha siri takatifu ya habari njema, ambazo kwa ajili yake mimi natenda kama balozi katika minyororo.” (Efe. 6:19, 20, NW) Kwa hiyo, kama vile mtume Paulo, kundi la Kolosai lilikuwa baraza ya mabalozi kwa ajili ya “siri takatifu ya habari njema.” Iliwalazimu kushiriki katika utimizo wa unabii wa Yesu, katika Mathayo 24:14, NW:

23 “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.”

24. (a) Wakolosai hao walikuwa mali ya taifa gani sasa, nao walikuwa na wajibu wa kuzaa matunda gani? (b) Kwa hiyo ni tunda la namna gani lililokuwa likizaliwa na “mbegu” iliyopandwa moyoni mwao?

24 Kwa kujitia katika utendaji huu wa kibalozi kwa ajili ya ufalme wa Mungu wa Kimasihi, Wakolosai hao walikuwa wakiyazaa matunda ya Ufalme. Walijihakikisha wenyewe kuwa sehemu ya “taifa lenye kuzaa matunda yake.” “Ufalme” ambao ulikuwa umeondoshwa kwa taifa la asili, la Israeli waliotahiriwa sasa lilikuwa limekwisha kupewa huo taifa la Israeli wa kiroho, taifa ambalo Wakristo hao Wakolosai walikuwa mali yake. (Mt. 21:43, NW) “Mbegu” ya mfano ya “neno la ufalme,” “neno la Mungu,” ilikuwa imekwisha kupandwa mioyoni mwao, na kwa kuwa sasa mioyo yao ilionekana kuwa udongo mzuri walikuwa wakizaa mazao ya namna ile ile ya kitu kilichokuwa kimepandwa mioyoni mwao. Yaani, wao vile vile walikuwa wakizaa, kuhubiri, kufundisha, “neno la ufalme” kwa wengine, wale walioko nje ya kundi la Kolosai.​—Mt. 13:19; Luka 8:11, 15.

25. Kwa sababu ya mfano uliowekwa na Wakolosai, ni ulizo gani tunalouliza juu ya karne yetu yenye vita, nasi tutamshukuru Mungu kwa ajili ya nini?

25 Mfano bora unaostahili kuigwa uliwekwa huko nyuma katika karne ya kwanza C.E. kukamatana na kundi la Kikristo katika Kolosai, Asia Ndogo. Je! namna yake inaonekana leo katika karne hii ya 20 yenye vita? Ikiwa ndivyo, basi sisi, kama vile mtume Paulo, tutakuwa na sababu ya ‘kumshukuru Mungu Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo sikuzote’ tunaposali kwake Yeye juu ya hali ya kidini.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki