Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 5/15 kur. 229-236
  • Kusimuliwa kwa Habari Njema Kwazaa Matunda Ulimwenguni Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kusimuliwa kwa Habari Njema Kwazaa Matunda Ulimwenguni Pote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! KUNA TENDO LO LOTE KUU LA KISASA LINALOLINGANA NA HILO?
  • MATUNDA YA MFULIZO
  • Kupanda Mbegu za Habari Njema Katika Ulimwengu Wenye Vita
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Yehova Aweza Kukufanya Uwe Mwenye Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kitabu cha Biblia Namba 51—Wakolosai
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Manufaa za Kupenda Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 5/15 kur. 229-236

Kusimuliwa kwa Habari Njema Kwazaa Matunda Ulimwenguni Pote

1. N’nini lililokuwa tukio lenye kuogofya la karne ya kwanza C.E., na, mbele ya kujulikana kwake ulimwenguni pote, n’nini kilichokuwa kimehubiriwa ulimwenguni pote?

KATIKA karne ya kwanza iliyokuwa mwanzo wa Wakati wetu wa Kawaida tukio lenye kuogofya sana halikuwa kuteketezwa moto kwa mji wa Rumi katika mwaka wa 64 C.E., bali mazingiwa na uharibifu wa mji wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 C.E. Kwa sababu ya ushindi wake wa kutokeza juu ya mji huo wenye ngome imara, Jemadari wa Kirumi Tito alithawabishwa kwa kufanyiwa maandamano ya ushindi aliporudi Rumi katika mwaka wa 71 C.E., tao la ushindi likijengwa kwa heshima yake. Lakini, vita ya damu pamoja na Wayahudi waasi haikumalizika mpaka ngome yao ya mwisho ya Kiyahudi ilipotekwa, ngome ya Masada inayoelekeana na Bahari ya Chumvi, katika mwaka wa 73 C.E. Hii ilileta aibu nyingi, suto na mvunjo wa kidini kwa Wayahudi ulimwenguni pote, makumi ya maelfu yao wakiuzwa utumwani. Lakini, miaka mingi mbele ya habari mbaya hizi kwa wale Wayahudi waliotahiriwa kujulikana ulimwenguni pote, habari njema za furaha ya milele zilikuwa zimekwisha kuenezwa sehemu zote za ulimwengu uliojulikana wakati huo. Zilikuwa habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi, ufalme usiotegemea Yerusalemu wa kidunia.

2. (a) Ni akina nani waliozichukua habari njema hizo katika karne hiyo ya kwanza C.E.? (b) Ukristo ulikuwa una eneo kubwa namna gani kutoka mashariki mpaka magharibi, mbele ya kuteketezwa moto kwa Rumi?

2 Ni akina nani waliozichukua habari njema hizo katika karne hiyo ya kwanza C.E.? Si Wayahudi wa asili waliotahiriwa walioutazamia Yerusalemu kama mahali pao pakuu pa kidini. Bali, ni wale walioshtakiwa kwa uongo na Mfalme Nero juu ya kuteketezwa moto kwa Rumi, yaani, wafuasi wenye amani na wasiodhuru wa Yesu Kristo waliokuwa wameitwa “Wakristo” kwanza katika mji wa Kishamu wa Antiokia. (Matendo 11:26) Huko nyuma wanafunzi hao wa Kikristo walitia ndani na maelfu ya waamini wa Kiyahudi, kama vile mitume wa Kikristo Simoni Petro na Paulo. Mbele ya kuteketezwa moto kwa Rumi mtume Petro alijikuta Babeli, Mesopotamia, alikoandikia barua kwa Wakristo katika Asia Ndogo yote. Mtume Paulo alijikuta amefungiwa katika nyumba na kuandikiwa rufani yake kwa ajili ya Ukristo isikiwe mbele ya Mfalme Nero, mnamo miaka isiyopungua miwili ya kukaa kwake Rumi, Italia. (1 Pet. 5:13; Matendo 28:30, 31) Kutoka Babeli, karibu na mpaka wa mashariki wa Milki ya Kirumi, ulikuwa umbali wa karibu maili 2,000 kufika Rumi wenyewe. Lo! ni eneo kubwa hilo kwa Ukristo kufika!

3, 4. (a) Mbele ya barua yake kwa Wakolosai, kweli ilikuwa imepenyaje ndani ndani ya Afrika na vile vile kwingineko? (b) Kulingana na barua ya Paulo, ni kwa kadiri gani ambavyo “habari njema” zilivyokuwa zikizaa matunda?

3 Kwa kuongolewa kwa towashi wa Kiethiopia wa Malkia Kandake na mhubiri wa Injili Filipo, Ukristo ulikuwa umepenya mbali vile vile kuelekea kusini, kushuka hata Ethiopia kusini ya Misri. (Matendo 8:26-39) Hivyo habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi zilikuwa zikipenya ndani ndani ya Afrika na Asia na Ulaya. Kati ya Wakristo ambao mtume Petro aliandikia barua yake ya kwanza yenye mambo mengi, katika majimbo matano katika Asia Ndogo, walikuwamo Wakristo katika Kolosai, Laodikia na Hierapoli katika jimbo la Kirumi la Asia. (1 Pet. 1:1) Karibu na wakati wa barua ya Petro yenye mambo mengi, mtume Paulo aliliandikia kundi la Kikristo la Kolosai moja kwa moja na kuwatajia barua yake aliyoliandikia kundi katika Laodikia. (Kol. 4:16) Ni kwa Wakristo hawa wa Kolosai Paulo alizungumza juu ya “kusimuliwa kwa kweli ya zile habari njema” ulimwenguni pote, hii ikiwa miaka mingi mbele ya mwisho kuja juu ya Yerusalemu wa kidunia katika mwaka wa 70 C.E. Habari njema hizo ziliambatana na tumaini kwa wale waliozikubali habari njema, na kwa kutaja hili Paulo anaandika, akisema:

4 “Tumaini hili mlilisikia kwanza kwa kusimuliwa kwa kweli ya zile habari njema zilizojitokeza kwenu, hata kama vile kunavyozaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote sawa na kunavyofanya vile vile miongoni mwenu, tangu siku mliposikia na kuzijua kwa usahihi fadhili zisizostahili za Mungu katika kweli.”​—Kol. 1:4-6, NW.

5. Katika Wakolosai 1:23, Paulo alikaziaje kuhubiriwa kwa habari njema ulimwenguni pote?

5 Kwamba tumaini la ufalme wa Mungu wa kimbinguni lilikuwa limekwisha kuenezwa ulimwenguni pote yakaziwa na Paulo wakati barua yake inapoendelea kuwaambia Wakolosai: “Bila shaka, mradi mnaendelea katika imani, mkiwa imara juu ya msingi na thabiti bila ya kuondoshwa katika tumaini la zile habari njema mlizozisikia, na zilizohubiriwa katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu. Juu ya habari njema hizi mimi Paulo nilipata kuwa mhudumu.”​—Kol. 1:23, NW.

6. (a) N’nani waliokuwa wahudumu wa habari njema, mbali na Paulo? (b) Wahudumu hao walishirikije pamoja tumaini la habari njema na wengine?

6 Mtume Paulo hakuwa mhudumu wa pekee wa habari njema huko nyuma. Wakristo wote waaminifu wa karne hiyo ya kwanza walikuwa wahudumu, kutia na mwanafunzi Epafra wa Kolosai, aliyemtembelea Paulo mnamo kifungo chake katika nyumba katika Rumi. (Kol. 1:7, 8; 4:12, 13) Wahudumu hawa wote wa habari njema walijiunga katika kulishiriki tumaini lao na wengine, zaidi si kwa kuzinakili kwa mkono habari za injili za maisha yake Kristo wala barua zilizoandikwa na wanafunzi wake walioongozwa na roho ya Mungu, bali zaidi kwa neno la kinywa, kwa kuwahubiria wasikiaji wote na kwa kutoa mafundisho ya maneno kwa wote wenye kupendezwa. Twaweza tu kuuwazia wingi wa kazi iliyoungana na hili kwa wafanya kazi chini ya hali hizo za karne ya kwanza. Wahudumu hao wa Kikristo walikuwa nazo habari njema zilizo za pekee kuzieleza kwa ulimwengu wa karne ya kwanza. Hawakuwa kimya juu ya Ufalme, bali walisema sana juu yake.

7. (a) Kwa sababu “mbegu” ya habari njema haikupandwa katika udongo usiozaa, ni nini kilichotukia katika kundi la Wakolosai na wengine? (b) Kwa sababu “habari njema,” kama zilivyosimuliwa kwa njia ya kweli, zilikuwa ‘zikizaa matunda,’ ni nini kilichotimilizwa wakati wa miaka 30 tangu Yesu alipoanza kuhubiri?

7 “Mbegu” ya “neno la ufalme” lililozungumzwa kwao haikuanguka kwenye udongo usiozaa. Lakini kutoka katika udongo mzuri wa mioyo mizuri na ya uaminifu kulitokea ukuzi wenye kuzaa mbegu kama ile iliyopandwa. Kulitokea kuongezeka kwa mbegu ya habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi kwa njia ya kusimuliwa kwake kwa wengine wote waliokuwa karibu au walioweza kufikiwa. Hivyo, sawa na alivyosema mtume Paulo kwa Wakristo Wakolosai, ‘kusimuliwa kwa kweli ya zile habari njema . . . kunazaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote sawa na kunavyofanya vile vile miongoni mwenu.’ (Kol. 1:5, 6, NW) “Kusimuliwa kwa kweli ya zile habari njema” kulikuwa kukizaa matunda na kuongezeka si kati ya kundi la Kolosai peke yake lakini vile vile katika makundi mengine yote katika Ulaya, Asia na Afrika. “Mbegu” waliyoizaa ilitumiwa katika kuupanda ujumbe wa Ufalme mioyoni mwa wengine. Basi, ni ajabu kama nini kwamba kwa muda wa miaka 30 tangu Yesu Kristo alipoanza kuipanda mbegu kwa kuhubiri kwake ufalme wa Mungu ushuhuda huo wa Ufalme uliletwa katika “dunia yote inayokaliwa na watu”!​—Mt. 4:12-17; 24:14, NW.

JE! KUNA TENDO LO LOTE KUU LA KISASA LINALOLINGANA NA HILO?

8. Uwezo wa ukuzi wa mbegu iliyopandwa sawasawa ni mkuu namna gani, na je! mbegu ya “neno la Mungu” imepoteza uwezo huo wa ukuzi katika karne hii ya 20?

8 Uwezo wa ukuzi katika mbegu inayopandwa katika udongo wenye rutuba ni mwingi sana sana. “Mbegu” ya “neno la ufalme” iliustaajabisha ulimwengu kwa uwezo wake huko nyuma miaka 1,900 iliyopita. Je! mbegu hiyo ya “neno la Mungu” imeupoteza uwezo wake katika hii karne ya 20? Sivyo inavyopaswa kuwa, wala sivyo ilivyo! Yaliyoandikwa kwa Waebrania waliofanywa Wakristo karne kumi na tisa zilizopita yangali kweli leo: “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili.”​—⁠Ebr. 4:12.

9. (a) Je! uzee umeupunguza uwezo wa ukuzi wa “mbegu” ya Neno la Mungu? (b) Kwa sababu gani hapa tunauangalia ukuzi wa ushirika wa Kristendomu?

9 Uzee haukuupunguza uwezo wake wa ukuzi. Inatupasa tuonyeshe nini kwa uhakika huu? Je! tuseme kwamba ndiyo makao ya kidini yajulikanayo kama Kristendomu? Kulingana na makadirio yaliyochapwa ya ushirika wa makanisa ya Kristendomu, alipofikia kilele kuanzia mwaka wa 1960 alipatwa na anguko la muda katika ushirika kwa makumi ya mamilioni. Lakini sasa makadirio ya karibuni zaidi yanampa Kristendomu kilele kipya cha washiriki 985,363,400.​—Tazama The 1973 World Almanac and Book of Facts, ukurasa wa 343, chini ya kichwa “Idadi ya Kidini ya Ulimwengu.”

10, 11. (a) Ni ulizo gani juu ya ukuzi linalotokea juu ya Kristendomu, na je! ukuzi wa idadi wahakikisha yeye hayumo katika ‘wakati wake wa mwisho’? (b) Ni hali gani zilizotabiriwa na Paulo kwa “siku za mwisho” ambazo huenda zikawa ndiyo sababu ya magumu ya kidini ya Kristendomu?

10 Na ikubaliwe kwamba Kristendomu hapunguki katika ushirika wake unaodaiwa. Lakini, je! yawezekana vile vile kwamba ubora wa washiriki wake unaongezeka kwa kiroho, ili kuzaa Wakristo wa kweli zaidi? Ebu na tuwalinganishe wao na namna ya Wakristo katika Kolosai, ambao kwao Paulo alivutwa sana kuandika kwa hiari. Wakristo hao Wakolosai walikuwa tofauti sana na ambavyo watu walio wengi waliojidai kumtumikia Mungu wangekuwa nyumaye, “katika siku za mwisho.” Uhakika wa kwamba Kristendomu, nyuma ya zaidi ya karne kumi na sita za kuwako, anaongezeka haukani kwamba yeye hayumo katika “siku za mwisho” zake. Kwamba yeye yumo katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kupambana nazo” (NW) haiwezi kutiliwa shaka. Je! mtume Paulo alitabiri ni nini ingekuwa sababu ya hili, na je! hii ndiyo sababu ya magumu ya kidini ya Kristendomu? Paulo alisema:

11 “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. [Kwa sababu gani?] Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake.”​—2 Tim. 3:1-5.

12, 13. (a) Basi je!, Kristendomu analinganaje na kundi la kale la Kolosai kwa kiroho? (b) Kristendomu anaeleza Sala ya Bwana itatimizwa namna gani kwa habari ya ufalme wa Baba wa kimbinguni?

12 Nani awezaye kukana kwamba masimulizi haya ya unabii hayaelezi sababu ya magumu ya Kristendomu leo, nyuma ya karne kumi na sita za ukuzi wa idadi. Unabii huu ulioongozwa na roho ya Mungu unapotimizwa juu yake, Kristendomu anajihakikisha mwenyewe kuwa tofauti kabisa na namna ambavyo kundi la Kolosai lilivyokuwa. Kwa karne hizi zote Kristendomu amesali kwa kawaida anayoiita Sala ya Bwana. Sala hii ya kielelezo kama ilivyotolewa na Bwana Yesu Kristo katika Mahubiri yake juu ya Mlima yaanza kwa kusema: “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe. Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatendeke duniani, kama yanavyotendeka mbinguni.” (Mt. 6:9, 10, Authorized Version) Kristendomu leo anakueleza kuja huku kwa ufalme wa kimbinguni kuwa ni kwa njia ya kusimamishwa kwa Ufalme katika mioyo ya waamini. Kama vile Daktari Adam Clarke alivyosema alipokuwa akieleza juu ya Mathayo 6:10:

13 “Wakati ufalme wa haki, amani, na furaha, katika Roho Mtakatifu, unaposimamishwa moyoni, ndipo kunapokuwapo msaada wa kutosha uliofanywa kwa ajili ya utimizo wa mapenzi ya Kimungu.”​—Commentary, Kit. cha 5, ukurasa wa 86, safu ya 1.

14. (a) Kwa kuwa ukuzi wa Kristendomu wavunja mwendo nyuma ya ule wa idadi ya watu ulimwenguni, viongozi wake wa kidini wanakuelezaje kuja kwa Ufalme? (b) Vita viwili vya ulimwengu ndani ya miaka 32 vinatokezaje ulizo juu ya kuja kwa Ufalme kwa habari ya Kristendomu?

14 Kwa muda mrefu ilidhaniwa kwamba ufalme wa Mungu ungekuja wanadamu wote wakigeuzwa kuwa washiriki wa makanisa ya Kristendomu. Lakini kwa kuwa sasa Kristendomu amevunja mwendo nyuma ya ukuzi wa idadi ya ulimwengu, viongozi wa kidini wanasema kuja kwa Ufalme ni ndani tu ya mioyo ya kadiri ya watu wanaoamini. Hawafundishi kwamba ufalme wa Mungu wa Kimasihi utakuja juu ya hii taratibu ya mambo ya kilimwengu na kuiharibu kisha kutawala kama serikali iliyo hakika juu ya wakaaji wote wa dunia na kuijaza dunia yote na haki na amani na furaha milele. (Dan. 2:44; 7:13, 14) Yesu Kristo alisema: “Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema.” Na: “Hazina yenu ilipo, ndipo itakapokuwapo na mioyo yenu.” (Luka 6:45; 12:34) Lakini je! uhakika uko wapi kwamba Ufalme wa Mungu umesimamishwa hata mioyoni mwa washiriki wa makanisa ya Kristendomu na kwamba mioyo yao iko pamoja na ufalme wa Mungu kama hazina yao? Je! vita viwili vya ulimwengu ndani ya miaka 32 ya hii karne ya 20 ndio ushuhuda wa kwamba ‘ufalme wa Mungu wa haki, amani, na furaha, katika Roho Mtakatifu’ ulisimamishwa mioyoni mwa mamia ya washiriki wa makanisa ya Kristendomu?

15. (a) Katikati ya vile vita viwili vya ulimwengu, ni tengenezo gani lililokuwa “hazina” ya Kristendomu? (b) Mrithi wa Ushirika anafanya nini juu ya mwendo wa kasi wa silaha?

15 Mnamo miaka 20 kati ya vita viwili vya ulimwengu Ushirika wa Mataifa kwa ajili ya amani ya ulimwengu na usalama ulikuwa ndiyo hazina ya Kristendomu, kwa maana makanisa yake yalisema: Ushirika wa Mataifa ndio “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Lakini je! uko wapi Ushirika wa Mataifa leo? Na je! Umoja wa Mataifa ulioufuata, unatimiliza nini katika kuukomesha mwendo wa kasi wa silaha za mataifa yote za kupigania ukuu wa kijeshi katika vita ya tatu ya ulimwengu inayokuogofisha kuwako kwa wanadamu wote? Kufanyizwa kwa silaha zenye hatari zaidi ndiko kunakojibu.

16. Je! ufalme wa Mungu kwa kweli unakuja ijapokuwa hali ya Kristendomu, nao wanadamu wote wanaambiwa nini juu yake leo?

16 Mambo haya yote yanahakikisha kwamba ufalme wa Mungu haukusimamishwa mioyoni mwa viongozi wa kidini wala washiriki wa makanisa ya Kristendomu na kwamba haukuingia mioyoni mwao. Ufalme wa Mungu hauwezi kutazamiwa uje kwa njia hiyo, nao hautakuja kwa njia hiyo. Lakini ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo unakuja kuijibu Sala ya Bwana, nayo serikali hiyo ya kitheokrasi kwa kweli ipo milangoni sasa. Hivi ndivyo wanadamu wote wanavyoambiwa leo katika ‘habari njema za ufalme’ ambazo Yesu Kristo alitabiri zingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote mbele ya mwisho kuja. (Mt. 24:14, NW) Habari njema hizi, “neno la ufalme,” zinapandwa kama mbegu katika dunia yote, katika nchi 208 na vikundi vya visiwa, nazo zinazaa matunda kama vile katika siku za mtume Paulo. Na kama alivyoliambia kundi la Kikristo katika Kolosai, ‘zinazaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote sawa na zinavyofanya vile vile miongoni mwenu.’ (Kol. 1:6, NW) Ndani na nje ya Kristendomu mbegu hii ya habari njema inapandwa.

17. (a) Ikiwa si Ufalme, n’nini kinachosimamishwa mioyoni mwa wanadamu, na namna gani? (b) Kwa hiyo, kama vile katika siku za Paulo, ‘kuzaa matunda na kuongezeka’ kwa habari njema kumetukiaje, ajapokuwapo Kristendomu?

17 Na kwa habari ya ukamatano kati ya ufalme wa Mungu na moyo wa kibinadamu, siyo Ufalme, bali mbegu ya habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi ndiyo inayoingia moyoni. “Mbegu” hii inasimamishwa humo kwa kutia mizizi na kuzaa matunda. Mbegu hii inapandwa kwa kuhubiriwa kwa habari njema kwa wale wote watakaozisikia na kuzipokea. Mbegu hii ya habari njema inazaa matunda kwa kukifanya kinywa kiseme, kutokana na wingi wa moyo wa wale ambao mioyoni mwao mbegu imekwisha kupandwa. Hivyo kupandwa kwa “mbegu” kunamfanya kila mtu ambaye mbegu imepandwa katika moyo wake ufaao awe mtangazaji mpya wa habari njema. Ndiyo sababu mbegu ya habari njema inaongezeka kwa kutangazwa kwa habari njema na wahubiri wa Ufalme zaidi na zaidi. Na ajapokuwa Kristendomu anajaribu kuzuia kupandwa kwa mbegu ya Ufalme katika mioyo ya kibinadamu, mashahidi wa Kikristo wa Yehova wanazidi kuitapanya mbegu ya habari njema ulimwenguni pote. Vivyo hivyo, kama vile katika siku za mtume Paulo, uzaaji wa matunda na kuongezeka vimetukia​—ulimwenguni pote, ajapokuwapo Kristendomu.

MATUNDA YA MFULIZO

18. Kupandwa kwa “mbegu” kumetokeza nini mbali na watangazaji wa Ufalme, na kwa hiyo ni sifa gani zinazowapambanua mashahidi wa Yehova wa Kikristo leo?

18 Kupandwa huku kwa mbegu ya habari njema za Ufalme kumezaa matunda kwa wingi nako kumeongezeka zaidi kuliko kutokeza tu watangazaji zaidi wa Ufalme. Kumekuwa na matunda ya mfulizo katika mioyo ya wale ambao ndani yao mbegu imepandwa na wanaoutangaza Ufalme. Kumetokeza tofauti ya yale ambayo mtume Paulo alitabiri juu ya Kristendomu katika 2 Timotheo 3:1-5. Kumetokeza mambo yale yale kulikoyatokeza katika mioyo na maisha za kundi la Kikristo katika Kolosai ambao Paulo aliandikia barua. Kumetokeza sifa za Kikristo anazozitaja Paulo katika barua yake, yaani, upendo, tumaini na amani. Uwezo mbalimbali wa mwujiza unaolipambanua kundi la kweli la Kikristo huenda ukatoweka kufuata kifo cha mitume wa Kikristo, lakini, Paulo alisema, “basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.” (1 Kor. 13:13) Haya ndiyo mambo yanayobaki, siyo pamoja na Kristendomu mwenye vita, bali pamoja na mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Imani, tumaini, upendo vinawapambanua.

19. (a) Paulo aliandika nini juu ya imani, upendo na tumaini la kundi la Kolosai? (b) Ni upendo wa namna gani uwavutao mashahidi wa Yehova wa Kikristo kufunua vinywa vyao na kuhubiri?

19 Akasema Paulo kwa Wakolosai: “Tuliposikia habari za imani yenu katika Kristo Yesu, na upendo mlio nao kwa watakatifu wote; kwa sababu ya tumaini mlilowekewa akiba mbinguni; ambalo habari zake mlizisikia zamani kwa neno la kweli ya Injili . . . Epafra, mjoli wetu mpenzi . . . naye alitueleza upendo wenu [kwa kiroho].” (Kol. 1:4, 5, 7, 8) Sio upendo wa kimwili, wenye nyege ulioupambanua ulimwengu wa kipagani wenye kuzungumza Kigiriki katika siku za mtume Paulo, bali ‘upendo kwa kiroho’​—⁠huu ndio uliotokezwa na kupandwa kwa habari njema katika mioyo ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo leo. Upendo huu wa kweli wa Kikristo ni sehemu ya tunda la roho ya Mungu, kulingana na maneno ya Paulo katika Wagalatia 5:22. Ni upendo huu wa kiroho katika moyo unaowavuta kuvifungua vinywa vyao katika kuhubiri.

20. N’nini kinachotukia kwa sifa ya upendo katika Kristendomu leo kama ilivyotabiriwa, na kwa hiyo ni sala gani ya Paulo ambayo lazima washirikiane naye kuitimiza, na namna gani?

20 Unabii wa Yesu juu ya mwisho wa hii taratibu ya mambo ya kilimwengu unatimizwa katika Kristendomu leo, yaani, “Kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa.” (Mt. 24:12) Lakini sala ambayo mtume Paulo aliisema alipokuwa akiwaandikia Wakolosai inatimizwa kwa mashahidi wa Yehova wa Kikristo leo: “ili wafarijiwe mioyo yao, wakiunganishwa katika upendo.” (Kol. 2:1, 2) Lakini lazima washirikiane na sala ya mtume kwao kwa kuyafanya yale ambayo mtume aliwaandikia Wakolosai: “Jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”​—Kol. 3:14.

21. Upendo huo wawapasaje mashahidi wa Yehova walio na vyanzo mbalimbali katika ujamaa wao kwa mtu na mwenzake?

21 Kwa hiyo, si ajabu kwamba, wajapokuwa mashahidi wa Yehova wa Kikristo leo wanatoka katika “kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” wao hawavikubali vizuizi vyo vyote vya kikabila, kitaifa wala vya rangi ya ngozi kati yao wenyewe. Si kwamba tu wao hawapigani kati yao wenyewe katika makundi yao na makusanyiko makubwa, lakini wao wanakataa kujitia katika vita vyo vyote vya mataifa yote visivyo vya kitheokrasi. Vita hivyo vingewalazimisha mashahidi wa Kikristo wa nchi moja kuwaua Wakristo wenzao wa nchi nyingine.​—Ufu. 7:9.

22. Ili waufuate mwendo huo katika ulimwengu huu inahitaji imani katika mambo gani ya hakika, na lazima wawe kama Wakolosai namna gani kwa habari ya imani yao?

22 Inahitaji imani kuu kuufuata mwendo huu katika ulimwengu wenye vita. Lakini, kama vile kundi lililokuwamo katika Kolosai, mashahidi wa Yehova wa karne yetu ya 20 wanayo imani kamili katika haki ya sheria na kanuni za mwenendo zilizowekwa katika Biblia Takatifu. Wao wanayo imani kwamba Mungu ndiye Mbuni wa Biblia na kwamba ni Kitabu cha kitheokrasi, ambacho lazima washikamane nacho bila ya kutia shaka. Wao wanayo imani kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu naye ndiye Bwana wao ambaye maneno yake na mifano lazima waifuate bila ya kugeuka. Ili wawe “wasio na mawaa wala lawama” mbele yake, wao wanafanya kama Wakolosai: ‘wakidumu tu katika ile imani, hali wamewekwa juu ya msingi, wakiwa imara.’ Mtume Paulo aliwaambia Wakristo Wakolosai kwamba yeye aliufurahia “uthabiti wa imani yenu katika Kristo.” (Kol. 1:22, 23; 2:5) Kwa sababu kama hiyo sisi twaweza kuwafurahia mashahidi wa Yehova wa leo.

23. (a) Mnamo wakati huu wa mabwana wa kisiasa, wao wanaweka imani yao katika nani kama Bwana wao? (b) N’nini kinachowatia nguvu kuvumilia hata kwenye kifo chenye jeuri wakiwa matesoni?

23 Wako mabwana wengi wa kisiasa duniani kwa sasa, lakini mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanajiepusha na siasa za kilimwengu. Kwa sababu gani? Kwa sababu wao ‘wamempokea Kristo Yesu, Bwana.’ Kwa kufaa sana, basi, wao wanalitii onyo la upole la mtume Paulo kwa Wakolosai: “Enendeni vivyo hivyo katika yeye [Kristo]; wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani.” (Kol. 2:6, 7; 1 Kor. 8:5, 6) Kuna maelfu ya mifano katika historia ya karne ya 20 kuhakikisha kwamba waabudu wa Kikristo wa Yehova kama Mungu watashikamana na imani hii katika Yesu Kristo kama Bwana wao hata kufa kwenyewe, hata kwenye kifo chenye jeuri mikononi mwa watesi. Imani yao katika ufufuo wa wafu inawatia moyo kufanya hivi. Wanayo imani ya Wakristo Wakolosai, ambayo, mtume Paulo alisema, ndiyo “imani katika utendaji wa Mungu, aliyemfufua yeye [Kristo] kwa wafu.”​—Kol. 2:12, NW.

24. (a) Ni jambo gani jingine lililowatia Wakolosai nguvu kuendelea kuwa wenye kukubalika kwa Mungu, nao iliwapasa kufanya nini juu yake? (b) Kwa sababu gani wao waliishi katika wakati mzuri sana wa kufanyiza imani, na kwa hiyo kwa sababu gani walijisikia wamependelewa sana?

24 Karne kumi na tisa zilizopita, wee! Wakolosai hao walikuwa na “tumaini” la namna gani! Lilikuwa jambo la muhimu katika kuwasaidia wazidi kukubalika kwa Mungu kupitia kwa Kristo; na kwa sababu hiyo yenye nguvu mtume Paulo aliwakumbusha Wakristo hao Wakolosai juu ya ‘kutogeuzwa na kuliacha tumaini la Injili mliyosikia habari zake, iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.’ (Kol. 1:22, 23) Wakristo Wakolosai, wengi wao ambao bila shaka waligeuzwa kutoka mataifa ya kipagani, waliishi katika wakati mzuri zaidi sana wakati ambapo sehemu za siri za makusudi ya Mungu zilifunuliwa wazi kwanza, hii ikiwawezesha waamini wenye kumcha Mungu wajifaidi na kufunuliwa huko. Bila shaka waamini hao Wakolosai lazima wawe walijisikia wamependelewa sana sana katika habari hii mtume Paulo alipowaandikia na kusema kwamba alifanywa mhudumu ‘alitimize neno la Mungu; siri ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake; ambao Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa utukufu wa siri hii katika Mataifa, nao ni Kristo ndani yenu, tumaini la utukufu.’​—Kol. 1:25-27.

25. Maneno ya Paulo yalimaanisha nini kwa habari ya waamini huko nyuma, na ni sifa gani za Kikristo zilizoendelezwa na tumaini hilo katika Wakolosai?

25 Hii ilimaanisha kwamba kwa mara ya kwanza mpango huo mtakatifu ulitokea kama “Kristo ndani” ya waamini kutoka mataifa ya kipagani yasiyo ya Kiyahudi wala si ndani ya waamini wa Kiyahudi peke yao. Sasa Kristo akiwa katika umoja na hawa wote msingi wa tumaini la ajabu ulitokea, “tumaini la utukufu” wake. Tumaini hili basi lilikuwa lile la kushiriki kwao pamoja na Kristo Masihi katika ufalme wake wa kimbinguni kwa ajili ya baraka ya milele ya wanadamu wote. Ah, kumbe, ni sifa bora kama nini za Kikristo zinazotokezwa na tumaini hilo! Mtume Paulo alisema kwamba upendo na imani ya Wakolosai vilikuwapo “kwa sababu ya tumaini mlilowekewa akiba mbinguni.” (Kol. 1:4, 5) Tumaini la ajabu kama hilo lipo leo!

26. Wakati huu, n’nini tumaini la mashahidi wa Yehova wa Kikristo kwa habari ya utawala, na kwa kusudi gani?

26 Basi je!, nini tumaini la mashahidi wa Yehova wa Kikristo la wakati huu wa mageuzi na mvurugo wa kisiasa? Je! ndilo tumaini la kuwa mfalme au malkia wa Uingereza? Je! ni kuwa rais wa Jamhuri ya Ufaransa? Je! ni kuwa waziri mkuu wa Ujeremani ya Magharibi? Je! ni kuwa mwenyekiti wa Chama cha Kikomunisti cha Urusi? Je! ni kuwa gavana wa Nchi ya New York au nchi nyingine yo yote katika United States ya Amerika? Hata kidogo! Tumaini la mashahidi wa Kikristo siyo kujaza vyeo hivyo vya kisiasa katika serikali zo zote za ulimwengu za hii taratibu ya mambo iliyohukumiwa. Waache wanasiasa wenye kujitafutia vyeo wa Kristendomu na upagani wavijaze vyeo hivyo vya kilimwengu duniani hata mwisho. Wale wa mashahidi wa Yehova walio na mwito wa juu kama ule wa Wakolosai wa karne ya kwanza wanatumainia cheo cha kiserikali walichowekewa akiba mbinguni, katika umoja na Yesu Kristo “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana.” Katika ufalme huo wa kimbinguni watamtumikia Mungu na kusaidia kuwabariki wanadamu wote.

27. Kwa habari ya wale Mashahidi wanaotamani kuishi katika dunia ya paradiso, matumaini yao n’nini juu ya utawala, nao watakuwaje kati ya wale ambao Mungu atahifadhi kuingia katika taratibu yake mpya?

27 Kwa habari ya wale mashahidi wa Kikristo wa Yehova wanaotamani kuishi katika dunia ya Paradiso yenye amani na isiyochafuliwa, tumaini lao si kuishi milele chini ya alama ya bendera ya kitaifa ya United States, wala chini ya alama ya bendera ya kitaifa ya Urusi kwa muda wote utakaokuja, wala chini ya alama ya taifa jingine lo lote la hii taratibu ya mambo iliyopo. Tumaini lao ni kuishi milele duniani chini ya ufalme wa kimbinguni wa Yehova Mungu Mwenye Enzi Yote wa ulimwengu wote. Katika serikali hiyo ya kitheokrasi Yesu Kristo na kundi lake lililotukuzwa watatawala kama wafalme na makuhani kwa ajili ya hali njema isiyokoma ya wanadamu wote, walio hai na waliokufa. Hawa wanaoitumainia Paradiso ya kidunia wanaitazamia Serikali hii peke yake kwa ukombozi kutoka utawala wote mbaya juu ya wanadamu wa Shetani Ibilisi na mawakili wake wote, wa kishetani na wa kibinadamu. Kwa sababu ya tumaini hilo la ajabu lililo zuri kupita yote wao hawana tamaa wala nia ya kujitakia makuu kwa ajili ya vyeo vyo vyote vya kisiasa vya mataifa ya kidunia. Wao hawataki ushirika wo wote katika lawama ya umati wa watu kwa sababu ya dhambi na upotovu wa siasa. Wao wanajua kwamba wale wanaojiepusha na uchafu huo wa kilimwengu ndio atakaowahifadhi Mungu kuingia katika taratibu Yake mpya.

28. Shukrani zamwendea nani kwa ajili ya hizo “habari njema,” nazo zimetokeza sifa gani za Kikristo kuwavuta wahubiri wasonge mbele hata mwisho?

28 Shukrani zote ni kwa Yehova Mungu kupitia kwa Yesu Kristo kwa ajili ya “habari njema” hizo zisizo na kifani. Hizi ndizo habari njema zinazohubiriwa leo kwa kuumba kote kuliko chini ya mbingu. Masimulizi ya habari njema hizi yanazaa matunda na kuongezeka, kupitia kwa uwezo wenye ushindi wa Mungu Mwenye Nguvu Zote. Wale wanaoipokea mbegu ya habari njema hizi wanasitawisha ndani yao wenyewe imani, tumaini na upendo kama matokeo, wajapokuwa wamo katika ulimwengu wenye vita. Ni “habari njema” za kweli peke yake ziwezazo kutokeza sifa hizo zilizo kama za Kristo. Wakivutwa na sifa hizi, mashahidi wa Kikristo wa Yehova wataendelea kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu, hata mwisho wa majira haya ya kupanda yenye kuzaa matunda.

​—Kutoka The Watchtower, Nov. 15, 1973.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki