Yehova Aweza Kukufanya Uwe Mwenye Nguvu
“Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo.”—ISAYA 40:29.
1, 2. Ni yapi baadhi ya mathibitisho juu ya wingi wa nguvu ya Yehova?
YEHOVA ni Mungu “mwingi wa nguvu.” Twaweza kuona uthibitisho wa ‘uweza wa milele na Uungu’ wa Mungu katika fahari ya uumbaji wake uonekanao. Wale wanaokataa kukiri uthibitisho huo wa Uumbaji wake hawana udhuru.—Zaburi 147:5; Warumi 1:19, 20.
2 Nguvu ya Yehova huja kuonekana hata zaidi wanasayansi wachunguzapo kindani sana ulimwengu wote mzima, ukiwa na galaksi zao zisizoweza kuhesabika na zinazoenea kwa mamia ya mamilioni ya miaka-jua. Katika usiku wenye giza lakini uliotakata, tazama mbingu na uone kama hutahisi kama mtunga-zaburi: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?” (Zaburi 8:3, 4) Na Yehova ametutunza sisi wanadamu kwa njia nzuri kama nini! Yeye alimwandalia mwanamume na mwanamke wa kwanza makao mazuri ya dunia. Hata udongo wayo ulikuwa na nguvu—za kuotesha mimea, kutoa chakula kisichochafuliwa chenye lishe bora. Wanadamu na wanyama hupata nguvu zao za kimwili kutokana na wonyesho huo wa nguvu ya Mungu.—Mwanzo 1:12; 4:12; 1 Samweli 28:22.
3. Mbali na vitu vionekanavyo vya ulimwengu wote mzima, ni nini kingine kinachoonyesha nguvu ya Mungu?
3 Zaidi ya mbingu kustaajabisha na maisha ya mimea na wanyama kufurahisha, hizo zatuonyesha nguvu ya Mungu. Mtume Paulo aliandika: “Mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.” (Warumi 1:20) Lakini kuna uthibitisho mwingine wa nguvu yake unaofaa tuangalie na kuthamini. ‘Ni nini,’ huenda ukajiuliza, ‘kinachoonyesha nguvu ya Mungu kuliko ulimwengu wote mzima?’ Jibu ni Yesu Kristo. Hakika, akiwa amevuviwa mtume Paulo asema kwamba Kristo aliyetundikwa mtini ni “nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.” (1 Wakorintho 1:24) ‘Kwa nini?’ huenda ukauliza, ‘Na hilo lahusuje maisha yangu sasa hivi?’
Nguvu Kupitia Mwana Wake
4. Nguvu ya Mungu ilionyeshwaje kwa habari ya Mwana wake?
4 Nguvu ya Mungu ilionyeshwa kwa mara ya kwanza alipomwumba Mwana wake wa pekee, kwa sura yake. Mwana huyu wa roho alimtumikia Yehova akiwa “stadi wa kazi” akitumia nguvu nyingi sana za Mungu katika kuumba vitu vingine vyote. (Mithali 8:22, 30) Paulo aliwaandikia hivi ndugu zake Wakristo katika Kolosai: “Katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; . . . vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake.”—Wakolosai 1:15, 16.
5-7. (a) Katika wakati uliopita, wanadamu walihusikaje katika maonyesho ya nguvu ya Mungu? (b) Kuna sababu gani ya kuamini kwamba nguvu ya Mungu yaweza kuonyeshwa katika hali ya Wakristo leo?
5 Sisi ni sehemu ya ‘vitu vilivyoumbwa juu ya nchi.’ Kwa hiyo, je, ingewezekana sisi wanadamu tupewe nguvu ya Mungu? Naam, katika shughuli zote za Mungu pamoja na wanadamu wasiokamilika, nyakati nyingine Yehova amewapa watumishi wake nguvu ya ziada ili watimize makusudi yake. Musa alijua kwamba, kwa ujumla, wanadamu huishi kwa miaka 70 au 80. (Zaburi 90:10) Vipi juu ya Musa mwenyewe? Yeye aliishi akawa na umri wa miaka 120, na bado “jicho lake halikupofuka, wala nguvu za mwili wake hazikupunguka.” (Kumbukumbu la Torati 34:7) Ingawa hilo halimaanishi kwamba Mungu anawezesha kila mmoja wa watumishi wake kuishi muda mrefu hivyo au kudumisha nguvu kama hiyo, lathibitisha kwamba Yehova aweza kuwapa wanadamu nguvu.
6 Jambo lionyeshalo zaidi uwezo wa Mungu wa kuwapa wanaume na wanawake nguvu ni kile alichofanyia mke wa Abrahamu. “Sara mwenyewe alipokea uwezo [“nguvu,” NW] wa kuwa na mimba, alipokuwa amepita wakati wake; kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu.” Au fikiria jinsi Mungu alivyowapa nguvu waamuzi na wengine katika Israeli: ‘Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na manabii; ambao walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu.’—Waebrania 11:11, 32-34.
7 Nguvu hizo zaweza kutumiwa kwa sisi pia. Si kwamba sasa tutazamie kupata watoto kimwujiza, au kuonyesha nguvu kama Samsoni. Lakini twaweza kuwa wenye nguvu, kama Paulo alivyotajia wanadamu wa kawaida katika Kolosai. Ndiyo, Paulo aliandikia wanaume, wanawake, na watoto, kama wale waliomo makutanikoni leo, naye alisema kwamba wao walikuwa ‘wakifanywa wenye nguvu nyingi kwa nguvu zote.’—Wakolosai 1:11, NW.
8, 9. Katika karne ya kwanza, nguvu ya Yehova ilionyeshwaje wazi kwa wanadamu kama sisi?
8 Katika huduma ya Yesu ya duniani, Yehova alionyesha wazi kwamba uwezo wake ulikuwa ukifanya kazi kupitia Mwana wake. Kwa mfano, katika pindi ambapo umati ulipommiminikia Yesu katika Kapernaumu, “nguvu ya Yehova ilikuwa hapo ili afanye uponyaji.”—Luka 5:17, NW.
9 Baada ya ufufuo wake, Yesu alihakikishia wafuasi wake kwamba wao ‘wangepokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yao roho takatifu.’ (Matendo 1:8) Hilo ni kweli kama nini! Mwanahistoria fulani aripoti juu ya matukio ya siku chache baada ya Pentekoste ya 33 W.K.: “Mitume wakatoa ushuhuda wa kufufuka kwake Yesu kwa nguvu nyingi.” (Matendo 4:33) Paulo mwenyewe alipewa nguvu kwa ajili ya kazi ambayo Mungu alikuwa amemwagiza afanye. Baada ya kugeuzwa na kuona kwake tena, yeye ‘alifuliza kujipatia nguvu hata zaidi naye alikuwa akiwatatanisha Wayahudi waliokaa katika Damasko alipokuwa akithibitisha kwa mawazo yenye kufuatana vizuri kwamba huyu ndiye Kristo.’—Matendo 9:22, NW.
10. Nguvu kutoka kwa Mungu ilikuwaje yenye msaada kwa hali ya Paulo?
10 Hakika Paulo alihitaji nguvu ya ziada, tufikiriapo nguvu za kiroho na za kiakili zinazohitajika kutimiza safari tatu za umishonari za maelfu ya maili. Yeye alivumilia pia aina zote za magumu, akivumilia kufungwa gerezani mara kadha na kukabili ufia-imani. Yeye alifanyaje hivyo? Yeye alijibu: “Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu.”—2 Timotheo 4:6-8, 17; 2 Wakorintho 11:23-27.
11. Kuhusu nguvu ya Mungu, Paulo alirejezea tumaini gani kwa watumishi wenzake katika Kolosai?
11 Basi, haishangazi kwamba Paulo, alipokuwa akiandikia ‘ndugu zake katika muungano na Kristo’ walioko Kolosai, aliwahakikishia kwamba wao ‘wangefanywa wenye nguvu nyingi kwa nguvu zote kwa kadiri ya uweza wa Yehova wenye utukufu ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.’ (Wakolosai 1:2, 11, NW) Ingawa maneno hayo yalielekezwa hasa kwa Wakristo wapakwa-mafuta, wote wanaofuata hatua za miguu ya Kristo waweza kunufaika sana kwa yale aliyoyaandika Paulo.
Watiwa Nguvu Katika Kolosai
12, 13. Barua kwa Wakolosai iliandikwa katika mandhari-nyuma ya aina gani, na yaelekea ilipata itikio gani?
12 Labda kutaniko katika Kolosai, lililoko katika mkoa wa Roma wa Asia, lilifanyizwa kupitia mahubiri ya Mkristo mmoja mwaminifu aitwaye Epafra. Yaonekana kwamba aliposikia kwamba Paulo alifungwa gerezani katika Roma karibu na 58 W.K., Epafra aliamua kumzuru mtume huyo na kumtia moyo kwa ripoti nzuri ya upendo na uthabiti wa ndugu zake katika Kolosai. Yaelekea kwamba Epafra alipitisha ripoti fulani zenye uaminifu juu ya matatizo fulani katika kutaniko la Kolosai yaliyohitaji kurekebishwa. Paulo naye akahisi himizo la kuandikia kutaniko barua ya kitia-moyo na himizo. Wewe pia waweza kupata kitia moyo kingi kutoka kwa sura ya 1 ya barua hiyo, kwa sababu inaonyesha wazi jinsi Yehova aweza kufanya watumishi wake wawe na nguvu.
13 Unaweza kuwazia jinsi lazima ndugu na dada katika Kolosai walivyohisi Paulo alipowafafanua kuwa “ndugu waaminifu katika muungano na Kristo.” Wao walikuwa wapongezwe kwa ajili ya ‘upendo walio nao kwa watakatifu wote’ na kwa ‘kuzaa matunda ya habari njema’ tangu wakati walipokuwa Wakristo! Je! maelezo ayo hayo yaweza kusemwa juu ya kutaniko letu, na juu yetu sisi mmoja-mmoja?—Wakolosai 1:2-8, NW.
14. Paulo alikuwa na tamaa gani kuhusu Wakolosai?
14 Paulo aliguswa sana na ripoti aliyopokea hivi kwamba aliwaambia Wakolosai kwamba hajaacha kusali kwa niaba yao na kuomba kwamba ‘wajazwe maarifa ya mapenzi ya Mungu katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; wakienenda kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana.’ Yeye alisali kwamba wao ‘waendelee kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu, wakifanywa wenye nguvu nyingi kwa nguvu zote kwa kadiri ya uweza wake wenye utukufu ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.’—Wakolosai 1:9-11, NW.
Twatiwa Nguvu Leo Pia
15. Twaweza kuonyeshaje mtazamo uleule ulioonyeshwa katika mambo yale ambayo Paulo aliwaandikia Wakolosai?
15 Paulo alituwekea kielelezo chema kama nini! Ndugu zetu ulimwenguni pote wahitaji sala zetu ili wavumilie na kudumisha shangwe yao wajapoteseka. Kama Paulo, twapaswa kuwa dhahiri katika sala zetu tupatapo habari kwamba ndugu katika kutaniko jingine, au nchi nyingine, wanakabili nyakati zilizo ngumu sana. Yaweza kuwa kwamba kutaniko la karibu laathiriwa na msiba wa asili au magumu fulani ya kiroho. Au yaweza kuwa kwamba Wakristo wanavumilia katika nchi iliyokumbwa na vita za wenyewe kwa wenyewe au mauaji ya kikabila. Katika sala twapaswa kumwomba Mungu asaidie ndugu zetu ‘waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana,’ wakiendelea kuzaa matunda ya Ufalme wanapovumilia, na kuendelea katika kupata ujuzi sahihi. Kwa njia hiyo watumishi wa Mungu hupokea uwezo wa roho yake, ‘wakifanywa wenye nguvu nyingi kwa nguvu zote.’ Unaweza kuwa na hakika kwamba Baba yako atasikia na kuitikia.—1 Yohana 5:14, 15.
16, 17. (a) Kama Paulo alivyoandika, twapaswa kushukuru kwa ajili ya nini? (b) Watu wa Mungu wamefunguliwa na kusamehewa kwa njia gani?
16 Paulo aliandikia Wakolosai kwamba walipaswa ‘kumshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru.’ Sisi vilevile na tumshukuru Baba yetu wa kimbingu kwa ajili ya mahali petu pafaapo katika mpango wake, pawe ni pa kimbingu au pa kidunia pa Ufalme wake. Mungu alifanyaje wanadamu wasiokamilika wafae machoni pake? Paulo aliwaandikia ndugu zake watiwa-mafuta hivi: “Alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi.”—Wakolosai 1:12-14.
17 Hata tuwe na tumaini gani, la kimbingu au la kidunia, sisi humshukuru Mungu kila siku kwa kutukomboa kutoka katika mfumo huu mwovu wa giza, kunakotimizwa na imani yetu katika andalio lenye thamani sana la dhabihu ya fidia ya Mwana mpendwa wa Yehova. (Mathayo 20:28) Wakristo wapakwa-mafuta wamenufaika na fidia inayotumiwa kwao kwa njia ya pekee ili wao waweze ‘kuhamishwa na kuingizwa katika ufalme wa Mwana wa pendo la Mungu.’ (Luka 22:20, 29, 30) Lakini “kondoo wengine” pia hunufaika kutokana na fidia hata sasa. (Yohana 10:16) Wao waweza kupokea msamaha wa Mungu ili wawe na msimamo wenye uadilifu mbele yake wakiwa rafiki zake. Wao wana fungu kubwa katika kutangaza “habari njema ya ufalme” katika wakati huu wa mwisho. (Mathayo 24:14) Kwa kuongezea hayo, wao wana tumaini ajabu la kuwa waadilifu kabisa na wakamilifu kimwili, kufikia mwisho wa Utawala wa Kristo wa Mileani. Usomapo ufafanuzi ulioko katika Ufunuo 7:13-17, yaelekea sana utakubali kwamba ufafanuzi huo ni uthibitisho wa kukombolewa na kubarikiwa.
18. Ni upatanisho gani uliotajwa katika Wakolosai ambao Mungu angali anatimiza?
18 Barua ya Paulo yatusaidia kutambua jinsi tulivyo na deni kubwa kwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Mungu alikuwa akitimiza nini kupitia Kristo? “[Ili] apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu aliyoimwaga juu ya mti wa mateso, hata hivyo viwe ni vitu vilivyo juu ya dunia au vitu vilivyo mbinguni.” Kusudi la Mungu ni kurudisha uumbaji wote katika upatano kamili pamoja naye, kama ilivyokuwa kabla ya uasi katika Edeni. Yule aliyetumiwa kuumba vitu vyote ndiye Yule anayetumiwa sasa kutimiza upatanisho huo.—Wakolosai 1:20, NW.
Watiwa Nguvu kwa Kusudi Gani?
19, 20. Kuwa kwetu watakatifu na bila mawaa kwategemea nini?
19 Madaraka huja kwetu sisi ambao tunapatanishwa na Mungu. Pindi moja tulikuwa wenye dhambi na kutenganishwa na Mungu. Lakini sasa, baada ya kuweka imani katika dhabihu ya Yesu na akili zetu zikiwa zimeondolewa kwenye kazi zilizo mbovu, kwa msingi tumo katika hali ya ‘utakatifu isiyo na mawaa,’ ‘bila lawama mbele ya Mungu.’ (Wakolosai 1:21, 22) Ebu wazia, kama vile Mungu hakuwaonea haya wale mashahidi waaminifu wa kale, ndivyo haoni haya kwa ajili ya sisi, aitwe Mungu wetu. (Waebrania 11:16) Leo, hakuna mtu awezaye kutushtaki kwa kubeba jina lake tukufu kwa uongo, wala kwa kuwa waoga wa kutangaza jina hilo hadi miisho ya dunia!
20 Lakini, ebu ona tahadhari ambayo Paulo aongezea katika Wakolosai 1:23: “Mkidumu tu katika ile imani, hali mmewekwa juu ya msingi, mkawa imara; msipogeuzwa na kuliacha tumaini la Injili [“habari njema,” NW] mliyosikia habari zake, iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.” Mambo mengi sana yategemea kudumisha kwetu uaminifu kwa Yehova, tukifuata hatua za Mwana wake mpendwa. Yehova na Yesu wametufanyia mambo mengi sana! Na tuonyeshe upendo wetu kwao kwa kufuata shauri la Paulo.
21. Kwa nini tuna sababu kubwa ya kusisimuka leo?
21 Ni lazima Wakristo Wakolosai walisisimuka sana kusikia kwamba ‘habari njema waliyoisikia’ tayari ilikuwa ‘imehubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’ Leo inasisimua hata zaidi kusikia kadiri ambayo habari njema za Ufalme inavyotangazwa na Mashahidi wanaozidi sana milioni nne na nusu katika zaidi ya nchi 230. Kwani, kila mwaka karibu watu 300,000 kutoka kwa mataifa yote wanapatanishwa na Mungu!—Mathayo 24:14; 28:19, 20.
22. Hata tukipatwa na mateseko, Mungu aweza kutufanyia nini?
22 Ingawa kwa wazi Paulo alikuwa mfungwa gerezani alipoandika barua kwa Wakolosai, yeye hakusikitikia kamwe hali yake. Badala ya hivyo, yeye alisema: “Ninashangilia sasa katika mateso yangu kwa ajili yenu.” Paulo alijua jinsi ilivyokuwa “kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.” (Wakolosai 1:11, 24, NW) Lakini alijua kwamba yeye hakufanya hivyo kwa nguvu yake mwenyewe. Yehova alikuwa amemfanya kuwa mwenye nguvu! Ndivyo ilivyo leo. Maelfu ya Mashahidi ambao wamefungwa na kunyanyaswa hawajapoteza shangwe yao katika kutumikia Yehova. Badala ya hivyo, wao wamekuja kuthamini ukweli wa maneno ya Mungu kama yapatikanavyo katika Isaya 40:29-31: “Huwapa nguvu wazimiao . . . Wamngojeao BWANA watapata nguvu mpya.”
23, 24. Ni nini siri takatifu inayotajwa katika Wakolosai 1:26?
23 Huduma ya habari njema juu ya Kristo ilikuwa muhimu sana kwa Paulo. Alitaka wengine wathamini thamani ya fungu la Yesu katika kusudi la Mungu, kwa hiyo aliifafanua kuwa “ile siri takatifu iliyokuwa imefichwa tangu mifumo ya mambo iliyopita na tangu vizazi vilivyopita.” Lakini, si kwamba ingedumu ikiwa siri sikuzote. Paulo aliongezea: “Lakini sasa imefanywa dhahiri kwa watakatifu wake.” (Wakolosai 1:26, NW) Uasi ulipotokea katika Edeni, Yehova alitoa ahadi ya mambo bora zaidi yaliyokuwa yakija, akitabiri kwamba ‘uzao wa mwanamke ungeponda kichwa cha nyoka.’ (Mwanzo 3:15) Hili lilimaanisha nini? Kwa vizazi vingi, kwa karne nyingi, hilo lilibaki likiwa fumbo. Kisha Yesu akaja, naye ‘akaufunua uzima na kutokuharibika kupitia habari njema.’—2 Timotheo 1:10.
24 Ndiyo, “ile siri takatifu” yahusika sana na Kristo na Ufalme wa Kimesiya. Paulo alitaja “vitu vilivyo mbinguni,” akirejezea wale watakaoshiriki katika utawala wa Ufalme pamoja na Kristo. Wao watakuwa na fungu kubwa katika kuletea baraka nyingi mno “vitu vilivyo juu ya dunia,” wale watakaofurahia paradiso ya milele hapa. Basi, waweza kuona jinsi ilivyofaa kwa Paulo kurejezea “utajiri wa utukufu wa siri [“siri takatifu,” NW] hii.”—Wakolosai 1:20, 27.
25. Kama ionyeshwavyo katika Wakolosai 1:29, mtazamo wetu sasa wapasa kuwa nini?
25 Paulo alitazamia mahali pake katika Ufalme. Lakini alitambua kwamba hakikuwa kitu cha kuketi kitako tu na kutumaini. “Ninafanya kazi kwa bidii, nikijikakamua mwenyewe kwa kupatana na utendaji wake na ambao wafanya kazi katika mimi kwa nguvu.” (Wakolosai 1:29, NW) Ona kwamba Yehova, kupitia Kristo, alimfanya Paulo kuwa na nguvu ili aweze kutimiza huduma ya kuokoa uhai. Yehova aweza kufanya vivyo hivyo na sisi leo. Lakini twapaswa kujiuliza, ‘Je, nina roho ya kueneza evanjeli niliyokuwa nayo nilipojifunza kweli kwa mara ya kwanza?’ Jibu lako ni nini? Ni nini kiwezacho kutusaidia sisi mmoja-mmoja kuendelea ‘kufanya kazi kwa bidii na kujikakamua wenyewe kwa kupatana na utendaji wa nguvu ya Yehova’? Makala ifuatayo inazungumzia jambo hili.
Je, Uliyaona Mambo Haya?
◻ Kwa nini twaweza kuwa na hakika kwamba Yehova aweza kuonyesha nguvu yake kwa niaba ya wanadamu?
◻ Ni nini mandhari-nyuma ya maneno ya Paulo katika Wakolosai sura ya 1?
◻ Mungu anatimizaje upatanisho unaotajwa katika Wakolosai 1:20?
◻ Kwa nguvu yake, Yehova aweza kutimiza nini kupitia sisi?
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 8]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
KOLOSAI