Wakolosai—Mashauri Yanayofaa Juu ya Imani na Mwenendo
YESU Kristo ana cheo gani katika mpango wa Mungu? Ili Wakristo wa kweli wamkaribie Yehova na kupata wokovu, je! ni lazima waadhimishe sherehe fulani za pekee au wazoee kujinyima sana mambo, kwa mfano kwa kufunga kula? Ni matakwa gani yanayopasa kutimizwa na waume wenye kumcha Mungu, wake zao, watoto na wengineo?
Maulizo kama hayo yalihitaji kujibiwa kwa ajili ya Wakristo wa karne ya kwanza waliokuwa wakiishi katika mji wa Kolosai, Asia Ndogo. Wao walikuwa wamezungukwa na watu wa Mataifa wenye kushikilia sana mawazo ya kipagani ya kujinyima sana vitu, na pia walizungukwa na Wayahudi waliojiepusha na vyakula fulani na kuadhimisha siku fulani za pekee. Kwa kweli, kwa kadiri fulani fundisho la uongo lilikuwa limepenya ndani ya kundi.
Wakati mtume Paulo alipokuwa amefungwa gerezani Roma, alipokea ripoti juu ya waamini wenzake wa huko. Labda yeye hakuwa ametembelea Kolosai hata siku moja. (Wakolosai 1:7, 8; 2:1) Katika njia fulani-fulani walikuwa wakiendelea vizuri. Lakini mafundisho fulani ya uongo yaliwatia katika hatari ya kiroho, naye mtume alihangaishwa sana na jambo hilo. Kwa hiyo Paulo aliongozwa na Mungu akaandika barua yenye kugusa moyo kwa Wakolosai karibu na mwaka wa 60 kufika 61 W.K.a Mashauri yanayofaa ya barua hiyo yanayohusu imani na mwenendo yaliwajibia maulizo ya maana, kama vile inavyowajibia Wakristo wa karne ya 20.
Cheo cha Mwana Kinachopita cha Wengine
Barua ya Paulo ilielekezwa kwa “ndugu watakatifu, waaminifu katika Kristo,” yaani, kwa wafuasi wa Yesu waliopakwa mafuta wa huko Kolosai. Mtume alimshukuru Mungu katika sala kwa sababu ya imani yao, tumaini na upendo wao. Zaidi ya hilo, Paulo na Timotheo ‘hawakuwa wameacha kufanya maombi na dua ili hao wajazwe maarifa sahihi, hekima na ufahamu wa rohoni.’ Kusudi lilikuwa nini? ‘Ili kumpendeza kabisa Yehova.’—Wakolosai 1:1-12.
Sehemu kubwa ya maana ya maarifa hayo inahusu Mwana wa Mungu. Kupitia kwake Wakristo wanafunguliwa kwa ukombozi, na wanapata msamaha wa dhambi zao. Yeye ndiye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” mwanzo wa kazi za kuumba za Yehova ambaye kupitia kwake mamilioni ya wana wa kimalaika walitokezwa. Pia Mwana huyo ndiye “mzaliwa wa kwanza katika wafu,” kwa maana yeye ndiye alitayarishia warithi wenzake njia ya kufufuliwa ili washiriki pamoja naye mbinguni uzima usioweza kufa. Na kati ya mambo mengine, Yesu Kristo “ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa.” Yeye ndiye mwenye cheo kikubwa zaidi kati ya wafuasi wake waliopakwa mafuta.—Wakolosai 1:13-18.
Zaidi ya hilo, ‘Mungu aliona inapendeza utimilifu wote ukae katika Mwanaye.’ Yeye ndiye amejawa kabisa na sifa zinazoonyesha namna Mungu alivyo, kutia na ile sifa ya hekima—ndiyo, ana kila jambo linalohitajiwa na Wakristo ili wapate mafundisho na mwongozo. Mafundisho yake, yanayopatana na sehemu ile nyingine yote ya Maandiko, hayana ukosefu wa jambo lo lote. Kupitia kwake vitu vile vingine vyote katika mbingu na juu ya dunia vitapatanishwa kwa Mungu, na kwa sababu ya dhabihu ya Kristo “siri” ile takatifu iliyofichwa tangu zamani, inayotia ndani kupata kwa Mataifa tumaini la kushiriki pamoja naye utukufu wa kimbingu, imefunuliwa. Lakini upatanisho huo utategemea kama Wakristo watabaki wakiwa thabiti na kutokuondolewa katika tumaini la zile habari njema. Paulo alikuwa akijibidiisha akiwa mhudumu (minista) wa hizo habari njema zenye kumtegemea Kristo hasa, yule aliye na cheo kinachopita cha wengine katika mpango wa Mungu.—Wakolosai 1:19-29.
Mafundisho ya Uongo Yanapingwa
Ili Wakristo Wakolosai wafurahie lile pendeleo tukufu la kushiriki pamoja na Yesu katika uzima wa kimbingu, walihitaji kukumbuka kwamba ‘katika Kristo hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika.’ Kwa hiyo, inawapasa wajihadhari na mtu ye yote anayeweza ‘kuwafanya mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, wala si kwa jinsi ya Kristo.’ Ilikuwa lazima wakatae mawazo yasiyo ya Kimaandiko ya Wagiriki, na mafundisho yasiyo ya Kibiblia ya Wayahudi. Kukataa mafundisho ya uongo kwa namna iyo hiyo na kuchukua msimamo imara kwa ajili ya kweli ni mambo yanayohitajiwa kabisa kwa Mashahidi wa Yehova leo.—Wakolosai 2:1-12.
Halafu, Paulo anawatia nguvu Wakolosai wajizuie na wenye kuendeleza imani za Kiyahudi. Yeye alionyesha kwamba Mungu alikuwa ameiondoa Torati ya Musa, akaipigilia misumari kwenye mti wa mateso wa Yesu. Kwa hiyo, haiwapasi waruhusu mtu ye yote ahukumu imani yao na uadilifu wao kwa kutegemea chakula, kinywaji wala maadhimisho fulani. Kwa sababu gani? Kwa sababu vitu hivyo vilikuwa kivuli tu cha mambo yaliyokuwa yakija, “bali mwili ni wa Kristo.”—Wakolosai 2:13-17.
Ili kupambana na maoni mengine yenye makosa, Paulo alitoa onyo juu ya wale waliokuwa wakifurahia unyenyekevu usio wa unyofu wa moyo, unyenyekevu wa kinafiki na “[namna fulani ya] kuabudu malaika.” Inaonekana kuwa wengine katika Kolosai ama waliwaza walikuwa wakiendesha namna ya ibada ambayo malaika walidhaniwa kuwa wanaifuata ama waliwaabudu malaika wenyewe kwa njia ya moja kwa moja. Lakini jambo hilo na mambo mengine kama “unyenyekevu wa mzaha tu” (NW) na kujinyima sana vitu, au “kuutawala mwili kwa ukali,” yalionyeshwa kuwa “hayafai kitu kwa kuzizuia tamaa za mwili.” Vivyo hivyo leo, mambo kama kujinyima sana vitu na kuwa na unyenyekevu wa kusingizia tu hayatatuongezea hali yetu ya kiroho.—Wakolosai 2:18-23.
Ili kuendeleza hali ya kiroho ya kweli na kupambana na tamaa za kimwili zisizofaa, wanafunzi wa Yesu waliopakwa mafuta ni lazima ‘waendelee kukaza akili zao kwenye mambo yaliyo juu, si kwenye mambo yaliyo duniani.’ Ni kwa kufanya hivyo tu wanapoweza kutumainia kudhihirishwa pamoja na Kristo katika utukufu wa kimbingu. Vivyo hivyo, Wakristo wenye matumaini ya kidunia wanahitaji kuweka shauku zao za upendo juu ya mambo ya kiroho.—Wakolosai 3:1-4, NW; Mathayo 6:19-21.
Mashauri Yanayofaa Juu ya Mwenendo
Ni nini hasa kitakachotusaidia tumkaribie Yehova zaidi na kuwa watu wa kiroho zaidi? ‘Ueni mwili wenu kwa habari ya uasherati, uchafu, tamaa mbaya [ya ngono], mawazo mabaya na kutamani,’ akasema Paulo. Matumizi mabaya ya uwezo wa kusema kupitia mambo kama ghadhabu, mazungumzo ya matusi na kusema uongo lazima pia yaepukwe. Kama vile mtume alivyowaambia Wakolosai, ni lazima ‘tuvue kabisa utu wa kale na kuvaa utu mpya.’ Ni lazima tujivike huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, ustahimilivu na upendo—kile ‘kifungo kikamilifu cha mwungano.’ Yote hayo hayatatuletea amani sisi wenyewe tu, bali pia kundi zima litapata amani.—Wakolosai 3:5-17.
Mashahidi wa kisasa wa Yehova wanaweza kufaidika kama Wakristo Wakolosai kutokana na mashauri ya Paulo juu ya wajibu mbalimbali wa kijamaa na madaraka mengine. Wake wanaonywa kwa upole wajiweke chini ya waume zao. Waume wanapaswa kuendelea kupenda wake zao na ‘wasiwe na uchungu nao.’ Watoto wanapaswa kutii wazazi wao, na akina baba hawapaswi kuchokoza-chokoza watoto wao “wasije wakakata tamaa.”—Wakolosai 3:18-21.
Watumwa Wakristo walipaswa kuwa watiifu na walipaswa kutendewa kwa uadilifu na kwa haki na mabwana zao wenye kuamini. Filemoni na mtumwa wake, Onesimo, waliishi katika Kolosai, na bila shaka wote wawili walilipokea shauri hilo kwa kulithamini sana. Kanuni izo hizo zinapasa kufuatwa na Wakristo wa kisasa katika uhusiano wa matajiri wa kazi na wafanya kazi wao. Kwa kweli, lo lote tunalofanya, tunapaswa kulifanya kwa nafsi yote kama kwamba tunamfanyia Yehova.—Wakolosai 3:18–4:1.
Paulo alihimiza waamini wenzake wadumu katika sala, pamoja na kushukuru. Pia, walipaswa kusali ili Mungu afungue mlango wa kupitiwa na Paulo na wenzake ili ‘wainene siri [takatifu] ya Kristo.’ Hakika jambo hilo linapasa kutuchochea sana tumshukuru Yehova na kusali ili aikuze kazi ya kuhubiri Ufalme! Na kama Paulo anavyoshauri, usemi wetu wenyewe na uwe sikuzote na neema, ‘ukolee munyu.’ Yale tunayoyasema yanapasa kuwa mambo ya kupendeza, ya kuvutia wenye kutusikia tukisema, na yanapasa yawe na maelekeo ya kuokoa maisha ya wale wanaotii maneno yetu.—Wakolosai 4:2-6.
Salamu za kibinafsi na onyo la upole zilitolewa zikaimalizia barua hii yenye msaada mkubwa. Tikiko na Onesimo (ambao ni wazi ndio walioipeleka barua hiyo) wangewapasha Wakolosai kwa urefu habari za Paulo. Epafra, ambaye labda alikuwa amesaidia kulianzisha kundi la huko Kolosai, alisemwa kuwa alikuwa ‘akifanya bidii kwa ajili yao katika maombi yake.’ Paulo mwenyewe alimalizia kwa salamu ya kibinafsi na akasali kwamba wao waweze kufurahia fadhili zisizostahilika (neema).—Wakolosai 4:7-18.
Mashauri ya Paulo kwa Wakristo Wakolosai yanatusaidia tufahamu cheo cha Yesu Kristo kinachopita cha wengine katika mpango wa Mungu. Barua hiyo inatuonyesha mambo ambayo ni lazima tuyafanye—na mambo ambayo ni lazima tuyaepuke—ikiwa kweli tutaweza kumkaribia Yehova na kupata wokovu. Barua hiyo inaonyesha wazi matakwa ya Mungu kwa waume, wake, watoto na wengine wanaotaka kupata upendeleo wa kimungu. Kwa kweli, barua ya Paulo kwa Wakolosai inatoa mashauri yanayofaa juu ya imani na mwenendo.
[Maelezo ya Chini]
a Ona pia Aid to Bible Understanding, kurasa 365, 366; “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial,” kurasa 224-227. Vitabu vyote viwili vimepigwa chapa na Sosaiti.