Kikubali Cheo Kikuu Cha Kristo
“Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”—Mt. 28:18.
1. Mtu anayejidai kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo anaweza kujiuliza maswali gani? (Yohana 15:8-10)
JE! WEWE ni mwanafunzi wa Bwana Yesu Kristo? Je! wewe unakubali cheo chake kikuu katika mpango wa Mungu? Ikiwa ndivyo, je! maisha yako ya kila siku yanaonyesha kwamba unathamini (unamshukuru) Mwana wa Mungu na yale ambayo amefanya kwa ajili yako?
Ndiye aliye mkuu wa viumbe vya Mungu vyenye akili
2, 3. (a) Yesu Kristo ni “mfano wa Mungu asiyeonekana” katika maana gani? (Ebr. 1:3) (b) Yehova Mungu alimtumiaje Mwanawe mzaliwa wa kwanza, na kwa hiyo yeye ana cheo gani kati ya viumbe wote wenye akili? (Yohana 1:1-3)
2 Mtume Paulo anatusaidia tuone namna cheo cha Yesu Kristo kilivyo cha maana sana. Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo aliandika hivi: “Naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni viti vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake. Naye amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu vyote hushikana katika yeye.”—Kol. 1:15-17.
3 Kulingana na maneno haya yaliyoongozwa na Mungu, Mwana mzaliwa wa kwanza, mwanzo wa kuumba kwa Mungu, Ndiye aliye mkuu kati ya viumbe vyote vyenye akili. Yeye ni mfano wa Baba yake wa kimbinguni kwa sababu yeye ni mtu wa kiroho ambaye anaonyesha sifa zenye kupendeza za kimungu kama vile upendo, hekima, haki ya hukumu, rehema, fadhili na ustahimilivu. (Kut. 34:6, 7; Zab. 33:5; Rum. 16:27; 1 Yohana 4:8) Kupitia kwake, Yehova Mungu aliumba wana wa kimalaika milioni nyingi, ulimwengu wote ulio mkubwa sana pamoja na mamilioni milioni ya galaksi (vikundi vya nyota) vilivyomo, pamoja na dunia na namna nyingi mbalimbali za mimea na wanyama wenye uhai. Kuongezea hayo, “viti vya enzi,” “usultani,” “enzi” au “mamlaka” viliumbwa kupitia kwa Mwana huyu. Hivi ni vitu gani?
4. Ni kwa sababu gani “viti vya enzi,” “usultani,” “serikali” au “mamlaka” vilivyoumbwa kujiitia Mwana havingekuwa vyeo vya serikali za ulimwengu na kwa hiyo ni lazima vitie nini ndani?
4 Hivi havingeweza kuwa vyeo vya serikali za kilimwengu, kwa kuwa hivi vinatajwa na Maandiko kuwa ni vya kibinadamu wala si viumbe vya kimungu. (1 Pet. 2:13, 14) Kwa hiyo, “viti vya enzi,” “usultani,” “enzi” au “mamlaka” lazima vitie ndani namna ya utawala ambao unatokezwa na Yehova Mungu kupitia kwa Mwanawe, kutia na ufalme wa Melkizedeki na ule wa Daudi katika Yerusalemu.
5. (a) Kulingana na Wakolosai 1:18, uhusiano wa Yesu Kristo na kundi ni gani? (b) Uhusiano huu unapaswa uwe na matokeo gani juu ya washiriki kundi? (Mt. 23:8-10)
5 Kwa habari ya cheo cha Yesu Kristo kuhusiana na kundi, mtume Paulo anasema hivi: “Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, kanisa [kundi].” (Kol. 1:18) Kwa hiyo, kwa kufaa kundi linamwona yeye kuwa ndiye aliye mkuu, kichwa, wala si mwanadamu ye yote.
6. Ni jambo gani linaloweza kutokea Wakristo wakianza kuheshimu wanadamu kupita kiasi? (Marko 9:33, 34) (b) Hili linaonekanaje katika yale yaliyotokea katika kundi la Korintho?
6 Kukosa kukubali uhakika huu kunatokeza kutokupatana. Hii inaonyeshwa vizuri na vile kulivyotukia katika Korintho wa kale. Mtume Paulo alilazimika kuwaandikia ndugu huko hivi: “Ndugu zangu, nimearifiwa habari zenu na wale walio wa nyumbani mwa Kloe, ya kwamba iko fitina kwenu. Basi, maana yangu ni hii, ya kwamba kila mtu wa kwenu husema, Mimi ni wa Paulo, na, Mimi ni wa Apolo, na Mimi ni wa Kefa, na Mimi ni wa Kristo. Je! Kristo amegawanyika? ” (1 Kor. 1:11-13) Kwa sababu ya kuwaangalia sana wanadamu isivyofaa, washiriki wa kundi la Korintho waligawanyika vikundi vikundi. Walishindwa kufahamu kwamba wanaume waliochukua uongozi miongoni mwa (kati ya) Wakristo walikuwa watumishi tu wa Mungu na Kristo, wakiwatumikia ndugu zao.—1 Kor. 3:5-9.
7. (a) Je! maoni mabaya yaliyokuwako katika Korintho yalisababishwa na Paulo, Apolo au Petro? (b) Wazee wanawezaje kuwa kama mtume Paulo, na kwa hiyo ni jambo gani wanalopaswa kujilinda nalo?
7 Kwa furaha, Paulo, Apolo na Kefa, au Petro, hawakuwa na daraka lo lote juu ya hali iliyotokea katika kundi la Korintho. Wao bi nafsi waliweka mfano katika kumtazama Yesu Kristo kama kichwa. Kwa mfano, mtume Paulo, aliweza kusema: “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo.” (1 Kor. 11:1) Bila shaka wazee leo wanapaswa watake kuwa kama Paulo. Hii inahitaji waseme kwa kupatana. (1 Kor. 1:10) Wazee wanapoanza kutangaza hadharani maoni ya kibinafsi yaliyotofautiana sana, washiriki wa kundi watakuwa na maelekeo ya kuwaunga mkono wale ambao maoni yao yanaelekea kukubaliana na kufikiri kwao. Sana sana hali inakuwa yenye uzito zaidi wakati mzee mmoja anapoanza kuwavunjia heshima wazee wenzake, pengine akionyesha kwamba yeye ni mwenye bidii na mwaminifu zaidi yao au labda yeye ana ufahamu au ni mwenye huruma kuliko wao. (Linganisha 2 Samweli 15:2-6.) Hii inaweza kuwafanya wengine wa kundi wamfuate yeye na vilevile iharibu jitihada za baraza ya wazee katika kuangalia faida za kiroho za kundi.
8. Wazee wanapoweka mfano mzuri katika kutii ukichwa wa Kristo kundi linafaidikaje? (Efe. 4:11-16)
8 Kwa upande mwingine, wakati wazee wanapojitahidi kusema na kutenda kwa umoja, wakijiacha waongozwe kabisa na Maandiko katika kufanya maamuzi yao, kutakuwa na umoja katika kundi. Kundi zima litatiwa moyo limwone Yesu Kristo kama kichwa cha kundi, wala si mwanadamu ye yote.
9. Zaidi ya Yesu kuwa kichwa cha kundi, Wakolosai 1:18 linatoa sababu nyingine gani ya ukuu wa Mwana wa Mungu, na hii inapaswa kuwa na maana gani kwetu?
9 Akiendelea kuzungumza juu ya cheo kikuu cha Yesu Kristo, mtume Paulo anatoa sababu nyingine ya Mwana wa Mungu kuwa ndiye aliye mkuu. Tunasoma hivi: “Naye ni mwanzo, mzaliwa kwa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote.” (Kol. 1:18) Hakuna mtu aliyefufuliwa apate uzima usioweza kufa tena mbinguni kabla (mbele) ya Yesu Kristo. Kwa sababu yeye ndiye aliyekuwa wa kwanza kufufuliwa katika uzima mkamilifu (usio na upungufu), yeye ndiye “mzaliwa wa kwanza katika wafu.” Alitayarisha njia ili warithi pamoja naye waweze kushiriki naye katika urithi wa kimbinguni kwa kufufuliwa katika uzima usiyoweza kufa kama alivyo yeye. (Ebr. 6:19, 20; Ufu. 20:6) Ili mtu ashiriki katika ufufuo huo, ni lazima akubali ukichwa wa Yesu Kristo juu ya kundi. Kwa kweli, ye yote ambaye angepokea baraka za kimungu ni lazima afanye hivyo.—Flp. 2:9-11.
‘Utimilifu wote wakaa katika yeye’
10. Ni kwa namna gani ‘Mungu alipendezwa utimilifu wote ukae katika Mwana’?
10 Walakini, kukubali ukichwa wa Kristo si kufahamu tu cheo chake kikuu katika kundi. Angalia kwamba mtume Paulo anaendelea kusema: “Kwa kuwa katika yeye ilipendeza [Mungu] utimilifu wote ukae.” (Kol. 1:19) Kulingana na mapenzi yake Mungu, Yesu Kristo anacho cheo kilicho kikuu zaidi katika kundi, wala si katika cheo na mamlaka tu, bali pia katika kuwa na “utimilifu” wa kila kitu kinachohitajiwa na Wakristo. Mwana wa Mungu ndiye aliye na utimilifu wote wa sifa za kimungu, kutia na hekima. Kwa hiyo, yeye, wala si mwanadamu ye yote duniani, ndiye Wakristo wote wa kweli wanayetazama kama kielelezo chao na kama chanzo chao cha uongozi na mafundisho.
11. Kwa kuwa “utimilifu” wote unakaa katika Kristo, ni nini linaloweza kusemwa juu ya kuhitajiwa kwa filosofia na mapokeo ya wanadamu?
11 Mfano mkamilifu wa Yesu Kristo na mafundisho yake hayahitaji kuongezwa filosofia na mapokeo ya kibinadamu ili yakamilike. Katika barua yake kwa Wakolosai, mtume Paulo alieleza jambo hili zaidi alipoandika hivi: “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo. Maana katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili. Nanyi mmetimilika katika yeye aliye kichwa cha enzi yote na mamlaka.”—Kol. 2:8-10.
12. (a) “[Mambo] ya awali ya ulimwengu” ni yapi? (b) Ni kwa sababu gani mtume Paulo angeweza kuyaita mawazo na mafundisho yenye kuharibu imani “madanganyo matupu”?
12 Huko nyuma katika karne ya kwanza, Wakristo walikuwa katika hatari ya kupotezwa na “[mambo] ya awali ya ulimwengu,” yaani, kanuni za msingi za ulimwengu ulio na uadui na Mungu. Mambo haya ya bure yalitia ndani mawazo yasiyo ya maandiko ya Wagiriki pamoja na watu wengine wasio Wayahudi pamoja na mafundisho yasiyo ya Biblia ya mapokeo ya Kiyahudi Juujuu tu, nyingine za filosofia na mafundisho haya huenda yalionekana yakiwa yenye kupendeza. Huenda yaliambatana na sababu na hoja (maneno) zilizovutia fikira za kibinadamu. Lakini hazikuwa na msingi imara. Mafundisho haya yasiyo na msingi—yawe ni juu ya mafundisho ya kidini, juu ya mwenendo wa kibinadamu, au ni juu ya namna mambo yanapaswa kufanywa katika kundi—kwa kweli yalikuwa “madanganyo matupu.” Kwa hiyo, kulikuwa na sababu nzuri Wakristo wajiangalie wasipotezwe na waalimu wa uongo waondoshwe katika njia ya kweli.—Linganisha 1 Yohana 2:26, 27.
13. Kulingana na Wakolosai 2:16-19, ni mafundisho gani ya uongo yaliyokuwa yakiendelezwa na wengine, na ni kwa sababu gani mafundisho hayo yalikuwa yenye hatari?
13 Akizungumza juu ya maoni mengine yenye makosa yaliyokuwa yameenea sana, Paulo anaendelea kusema: “Mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo. Mtu asiwanyang’anye thawabu yenu, kwa kunyenyekea kwa mapenzi yake mwenyewe tu, na kuabudu malaika, akijitia katika maono yake na kujivuna bure, kwa akili zake za kimwili; wala hakishiki Kichwa, ambacho kwa yeye mwili wote ukiruzukiwa na kuungamanishwa kwa viungo na mishipa, hukua kwa maongeo yatokayo kwa Mungu.”—Kol. 2:16-19.
14. (a) Mkristo anawezaje kujiachilia ahukumiwe isivyofaa kuhusu kula na kunywa au kuadhimisha siku fulani? (b) Ni kwa sababu gani wale waliokuwa wakihukumu hivyo walikuwa na makosa?
14 Hivyo Wakristo walikuwa wakihimizwa wasiwaruhusu wengine wawe mahakimu wa kuhukumu imani na haki yao, wakidai kwamba hawawezi kuokolewa bila ya wao kutahiriwa waanze kufuata torati ya Musa. Watu mmoja mmoja waliokuwa wakihukumu katika njia hii walikuwa wakirudia “mafundisho ya awali,” mafundisho ya msingi ya ibada ya kweli, wakikataa maelezo zaidi ya Mungu ya mambo kwamba “utimilivu wote” sasa unakaa katika Kristo. Kwa hiyo, watu kama hao hawakuwa wakishikamana na Kichwa, Kristo, nao walikuwa wakiwaondoa watu mmoja mmoja wasifuate mafundisho yenye uzima yaliyokuwa ya lazima ili wakue kiroho.
15. Wakristo wa Kolosai wangepoteza nini kwa kukubali mambo ya waalimu wa uongo?
15 Kama Wakristo katika Kolosai wangejiachilia washawishwe na mwenye kuendeleza mafundisho ya uongo, matokeo yangekuwa kunyang’anywa “thawabu” iliyowekwa mbele yao. Thawabu hii ilikuwa nini? Ilikuwa thawabu yenye utukufu ya uzima usioweza kufa mbinguni.—1 Kor. 9:24-27; Flp. 3:14; 2 Tim. 4:7, 8; Ufu. 2:7.
16. Kulingana na maneno ya Paulo katika Wakolosai 2:18, mwalimu wa uongo angeonekanaje?
16 Kama alivyoonyesha mtume Paulo, mtu ambaye angenyang’anya Mkristo zawadi yenye thamani (bei) kuu ya uzima huenda akaonekana kuwa hana hatia yo yote. Mtume Paulo anamweleza kama mtu ‘anayenyenyekea kwa mapenzi yake mwenyewe.’ (Kol. 2:18) Kwa hiyo, kwa kuonekana tu, yeye alikuwa mtu mnyenyekevu sana. Walakini, unyenyekevu huu ulikuwa wa uongo tu.
17. (a) Mtume Paulo alikuwa na maana gani alipokuwa akimweleza mwalimu wa uongo kama mtu aliyekuwa ‘amechukua msimamo wake katika mambo aliyoyaona’? (b) Ni kwa namna gani mwalimu kama huyo wa uongo alikuwa “akijivuna bila sababu nzuri kwa akili zake za kimwili”?
17 Alivyokuwa kweli kweli ni wazi kutokana na uhakika wa kwamba mtume Paulo anamtaja mtu wa namna hiyo kama ‘ “akichukua msimamo wake katika’ mambo aliyoyaona, akijivuna bila sababu nzuri kwa akili zake za kimwili.” (Kol. 2:18, NW) Mtume Paulo alikuwa na maana gani aliposema hivyo juu ya mwalimu anayefundisha uongo? Usemi huu ‘kuchukua msimamo katika’ ulikuwa usemi uliotumiwa nyakati za kale kuhusiana na kutia jandoni mwa mambo ya siri ya kipagani. Bila kutosheka na kweli kamili na yenye kufahamika wazi iliyofunuliwa kupitia kwa Yesu Kristo, yeye alijivuna akiamini kwamba alikuwa amepata hekima na utakatifu wa juu zaidi ya ule walioushiriki ndugu zake Wakristo kwa kawaida. Kwa kujaribu kuongezea ukweli wa Kikristo mawazo ya uongo, yeye kwa kweli aliondoka katika kweli. Kulingana na maoni yake, maarifa na hekima havikuwa vimewekwa katika Mwana wa Mungu peke yake. Mtu kama huyu hakuamini maneno haya yaliyoongozwa na Mungu: “Ndani yake yeye [Kristo] hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika.” (Kol. 2:3) Yeye alisisitiza kwamba maarifa na hekima vilikuwa vimewekwa kwingineko ambako kundi lingetazamia kwa uongozi wala si katika Mwana wa Mungu tu.
Hali ya Mkristo leo
18. Kwa habari ya filosofia na maoni yasiyo ya maandiko, Wakristo wote, na zaidi wazee wanapaswa kujilinda na jambo gani?
18 Leo watumishi wa Mungu hawakutani na hali kama zile zile zilizokuwa zimeenea katika karne ya kwanza. Hata hivyo, tunaweza kujifunza mambo ya maana kutokana na mambo ambayo Paulo aliwaandikia Wakolosai. Kwa mfano, Wakristo wote, sana sana wazee, ni lazima wajiangalie wasijiingize katika mambo ya kipekee ya wengine tena wasiweke maoni yao wenyewe yasiyo ya maandiko pamoja na filosofia zao zilingane na kweli iliyofunuliwa katika mafundisho na mfano wa Yesu Kristo.—Linganisha 1 Timotheo 1:3, 4; 2 Timotheo 4:1, 2.
19. (a) Mashauri yote ya kiroho yanapaswa yawe na msingi gani, na kwa sababu gani? (b) Mkristo akikosa kufuata Maandiko, awatolee wengine filosofia za kibinafsi kama uongozi, yeye angekuwa akikana nini?
19 Shauri lo lote la kiroho ambalo huenda Mkristo akawatolea wengine lapaswa msingi wake uwe, si mapendezi ya kibinafsi au kanuni za kilimwengu, bali mfano na mafundisho ya Yesu Kristo. Kwa kuwa mambo yote aliyoyafundisha Mwana wa Mungu yalipatana kabisa na Maandiko yaliyoongozwa na Mungu, Biblia yote inaweza na inapaswa kutumiwa kwa kufaa katika kutoa msaada wa kiroho. (2 Tim. 3:16, 17) Mtu anayekosa kufuata Maandiko anaonyesha kwamba yeye amemdharau Kichwa cha kundi. (Linganisha Mathayo 7:24-27; 15:3-9; Yohana 17:17.) Vilevile hiyo ingeonyesha kwamba “utimilifu” wote haukai katika Kristo lakini kwamba “ukosefu” wa Kristo lazima utimilizwe na maoni ya kibinafsi na filosofia za kibinadamu.
20. Kama inavyoonekana wazi kutokana na Waebrania 5:14, ni kwa sababu gani ni hatari kujiachilia tuongozwe na maoni ya wengine?
20 Namna gani juu ya Wakristo ambao wanakubali kuongozwa na filosofia za kibinafsi pamoja na maoni ya wengine katika kuamua juu ya haki ya mwendo fulani? Huenda wakaumiza dhamiri zao na kuzuia ukuzi wao wa kiroho. Kwa sababu gani? Kwa upande mmoja, Biblia inaonyesha kwamba ni lazima ‘akili zizoezwe kwa kuzitumia.’ Kwa hiyo, wakati wengine wanapoongoza isivyofaa maamuzi ya watu mmoja mmoja, mtu huyo hatakua kiroho lakini ataendelea kuwa mtoto kiroho, asiweze kupambanua mema na mabaya—Ebr. 5:14.
21. Kujitahidi kufuata maoni ya kibinafsi ya wengine yasiyo ya maandiko kunawezaje kutufanya tujione kuwa na hatia juu ya mambo ambayo yenyewe si mabaya?
21 Zaidi ya hayo, kwa sababu ya kujaribu kufuata maoni tu ya Mkristo mwingine yasiyo ya Maandiko, huenda watu wengine wakajiona kuwa na makosa isivyofaa juu ya kuangalia mambo ya kibinafsi, kujifurahisha na mambo yanayofaa, tafrija, na mengine kama hayo. Kwa mfano, mshiriki wa kundi anayeheshimiwa huenda akatoa maoni mbele ya wengine ya kwamba “siku za mwisho” si wakati wa watumishi wa Mungu kuwa wakifikiria juu ya kutengeneza sana sana nyumba zao. Ijapokuwa huenda wengine wakajua kwamba hayo ni maoni ya mtu bi nafsi wakae bila kusumbuliwa nayo, huenda wengine wakajiona kuwa na makosa juu ya mipango yao. Wale wanaojiachilia waongozwe na maoni ya wengine isivyofaa huenda baadaye wakapatwa na magumu au masumbufu ambayo huenda yangeepukwa kama wangeendelea na mipango yao waliyoipanga kwa akili. Vivyo hivyo, wakati uongozi wa maoni ya watu wasiokamilika unapotumiwa badala ya Neno la Mungu katika sehemu nyingine za maisha, magumu mazito huenda yakatokea. Walakini sikuzote tunakuwa salama wakati msingi wa maamuzi yetu unapokuwa mfano na mafundisho ya Mwana mkamilifu wa Mungu.
Mtii Kristo kama kichwa
22. (a) Kwa sababu ya cheo kilichotukuzwa cha Yesu, tunapaswa tuzioneje amri zake? (b) Ni maswali huenda tukajiuliza kuhusu amri za Yesu zinazopatikana katika Mathayo 28:19, 20; Luka 21:34-36; 22:19, 20 na Yohana 13:34, 35?
22 Kwa sababu Yesu Kristo anacho cheo kilichotukuzwa sana, bila shaka amri zake zinapaswa kuonwa kwa uzito na kufuatwa kwa moyo wote. Je! wewe unajitahidi kushiriki katika kutoa ushuhuda na katika kufanya wanafunzi? (Mt. 28:19, 20) Je! wewe unakesha kiroho, bila kujiachilia ulemewe na masumbufu ya maisha ya kila siku au ulafi na ulevi? (Luka 21:34-36) Je! kushughulika (kufanya kazi) kwako na wengine kunaonyesha kwamba kwa kweli wewe unataka kuonyesha upendo wa kujinyima unaowatambulisha (fahamisha) wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo? (Yohana 13:34, 35) Unapokusanyika na waamini wenzako kwa utiifu ili uadhimishe Chakula cha Bwana cha Jioni, je! wewe unafikiri kwa uzito juu ya faida ambazo umepata kupitia kwa dhabihu ya Yesu? (Luka 22:19, 20; 1 Kor. 11:23-32) Je! wewe unachochewa uuangalie mwenendo wako ili uuendeleze msimamo wako safi uliopatikana wakati ulipokubali kwa imani faida zenye kufunika dhambi za damu ya Yesu iliyomwagwa?—1 Pet. 1:14-19.
23. Tulipatanishwaje na Mungu, na kwa hiyo tunapaswa kuendelea kufanya nini?
23 Hatupaswi kusahau kamwe kwamba wakati dhambi zetu zilipokuwa hazijafunikwa, tulikuwa adui za Mungu. Lakini, kupitia kwa damu ya Yesu iliyomwagwa juu ya mti wa kufisha, tumepatanishwa na Aliye Juu Zaidi na sasa tuna amani naye. (Kol. 1:20) Hata hivyo, baada ya kutakaswa na dhambi mara ya kwanza kwa kukubali dhabihu ya Yesu Kristo iliyotolewa kwa ajili yetu, inatupasa tuzidi kufanya bidii ili tuendelee katika hali isiyo na mawaa mbele za Yehova Mungu. Kwa mfano, katika barua yake kwa Wakolosai, mtume Paulo anaonyesha waziwazi yanayotakiwa katika mwenendo wa Mkristo.
Zuia tamaa mbaya
24. (a) Kabla ya kuwa mwanafunzi aliyebatizwa wa Kristo huenda mtu akawa alitumiaje viungo vya mwili wake na uwezo wake wa kusema? (b) Anapaswa kufanya nini sasa?
24 “Vifisheni,” aandika Paulo, “viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu.” (Kol. 3:5) Kabla ya kuwa mwanafunzi aliyebatizwa wa Yesu Kristo, huenda mtu akawa alitumia viungo vya mwili wake katika njia iliyo kinyume cha kusudi la Mungu. Mtume hata anasema: “Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo. Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu. Msiambiane uongo.” (Kol. 3:7-9) Ndiyo, matumizi mabaya ya viungo vya mwili na uwezo wa kusema ni jambo lisilomfaa mtu aliye na msimamo safi mbele za Mungu. Anapaswa kufisha tamaa mbaya za mwili, bila kuziachilia zifanye viungo vya mwili wake vitende dhambi. Anapaswa kuiga mfano wa mtume Paulo aliyesema juu yake mwenyewe hivi: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.”—1 Kor. 9:27.
25. (a) Ni kwa sababu gani kutamani ni ibada ya sanamu? (b) Kufahamu uhakika huu kunawezaje kutusaidia tuzishinde tamaa mbaya za kimwili?
25 Jambo moja linaloweza kutusaidia tuzizuie tamaa mbaya za mwili ni kutambua uzito wa kutamani—kuwa na tamaa sana ya kitu ambacho mtu hana haki kuwa nacho. Kama alivyosema Paulo, kutamani ni ibada ya sanamu. Hii ni kweli kwa sababu kitu hicho kinachotamaniwa sana kinaanza kuwa cha maana sana maishani mwa mtu huyo. Kinakuwa sanamu au kitu cha kuabudiwa kwake na kwa hiyo kinamzuia asimtolee Yehova Mungu ibada ya pekee. Vilevile kinamzuia asimpende Mungu kwa moyo wote, kwa sababu kutamani kwake huko kwa kichoyo kunamsukuma asiijali sheria ya kimungu. Biblia inaonyesha kwamba njia moja ambayo katika hiyo tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova ni kwa kutii amri zake kwa’ ushikamanifu. (1 Yohana 5:2, 3) Kwa hiyo, Mkristo anapofahamu kwamba tamaa mbaya inakua ndani yake, atafanya vizuri akikumbuka namna uhusiano (urafiki) wake na Mungu ulivyo na thamani (bei) kuu na namna unavyoweza kuwa upumbavu kuupoteza kwa kujifanya mwabudu sanamu.
Tendo linalofaa kuelekea waamini wenzetu
26. Je! kuendelea kukaa bila mawaa mbele za Yehova Mungu kunahusu kutojiingiza katika mwenendo mbaya tu na hii inaonyeshwaje katika Wakolosai 3:12, 13?
26 Walakini, kuendelea kuwa na msimamo usio na mawaa mbele za Yehova Mungu kunahusu mengi zaidi ya kujizuia kuwa na mwenendo mbaya na usemi usiofaa. Tendo linalofaa linahitajiwa. Kwa hiyo mtume Paulo aliendelea kuwasihi ndugu Wakolosai hivi: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama [Yehova] alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi.”—Kol. 3:12, 13.
27. Ni kwa sababu gani tunapaswa kuwatendea Wakristo wenzetu kidugu na kuonyesha roho ya kusamehe?
27 Fikiria anavyosema Paulo hapa. Kama Wakristo, tumetakaswa kwa damu ya Yesu Kristo na sisi tu ndugu na dada za kiroho. Kwa hiyo tunapaswa kutendeana katika njia ya kidugu. Kwa sababu ya kutokamilika, mara nyingi sisi sote tunashindwa kuonyesha sifa njema za Baba yetu wa mbinguni na za Mwanawe. Kwa kufaa, basi, hatupaswi kuwatendea vikali waamini wenzetu. Haingefaa Mkristo ajifanye hakimu wa ndugu zake, akitumia kwa kiburi haki anayodai kuwa nayo ya kuwaadhibu kwa sababu ya makosa yao. Sivyo, yeye anapaswa kuchukuliana na makosa yao kwa nia asiache kuwaonyesha huruma, fadhili, unyenyekevu, upole na uvumilivu. Ni kweli, huenda mtu akawa na sababu nzuri ya kumnung’unikia ndugu. Lakini anafanya vizuri akijiuliza, Je! kweli kosa la ndugu yangu ni kubwa sana hivi kwamba siwezi kumsamehe? Ndipo, mwenye kunung’unika anapoona makosa yake mwenyewe, atakuwa na nia zaidi ya kusamehe, kama na Yehova alivyomsamehe.—Mt. 18:21-35.
28. (a) “Amani ya Kristo” ni nini? (b) Inapoongoza mioyo yetu matokeo yanakuwa nini katika uhusiano (ushirikiano) wetu na waamini wenzetu?
28 Lakini namna gani ikiwa makosa ya wengine yanafadhaisha moyo wetu? Tunawezaje kuutuliza? Mtume Paulo anatoa shauri hili lililoongozwa na Mungu: “Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu.” (Kol. 3:15) “Amani” hii ni ule utulivu tunaoupata tunapokuwa wanafunzi wa Mwana wa Mungu. Inatokana na kujua kwamba tunapendwa na kukubaliwa na Yehova Mungu na Mwanawe. Wakati amani hii inapotawala mioyo yetu, tutajitahidi kusema na kutenda katika njia ambayo inaihifadhi. Tutaulinda uhusiano wetu wenye thamani kuu na Yehova Mungu na Yesu Kristo kwa kutendea waamini wenzetu katika njia ya fadhili na upendo. Hii itaendeleza amani kundini na kutuzuia tusiudhike kiasi cha kuwatenda ndugu zetu dhambi.—Efe. 4:26, 27.
29. Kutii shauri hili lililoongozwa na Mungu, “iweni watu wa shukrani” kutakuwa na matokeo gani mema?
29 Halafu, Paulo anapendekeza hivi: “Iweni watu wa shukrani.” (Kol. 3:15) Ndiyo, roho ya kuwa watu wa shukrani inafanya mengi katika kuhifadhi amani tunayojifurahisha kama Wakristo. Kwa sababu wanathamini sana yale ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wamefanya ili kuwawezesha watakaswe na dhambi wakiwa na tumaini la kupata uzima wa milele, wao hawaudhiki upesi wakati wengine wanapokosa katika njia fulani, bali wanawasamehe kabisa kwa moyo. Lo! hii ni tofauti sana namna gani na watu wasio na shukrani! Mara nyingi wao wananung’unika, na hawatosheki na hawana furaha hata kidogo. Nia yao ya uchoyo, isiyo ya upendo inawavunja moyo wale wanaoshirikiana nao na inatokeza ugomvi na vita. Kwa hiyo tutafanya vizuri tukisitawisha roho ya kuwa wenye shukrani.
30. ‘Kuacha neno la Kristo likae ndani yetu katika hekima yote’ kuna maana gani?
30 Baada ya kuwatia moyo Wakristo wawe wenye shukrani, Paulo anaandika hivi: “Neno la Kristo na likae ndani yenu katika hekima yote.” (Kol. 3:16) Hii ina maana gani? “Neno la Kristo,” au ujumbe kutoka kwa Kristo, mafundisho yote ya Kikristo, yapaswa yawe kawaida ya maisha yetu. (The Bible in Living English; Good News Bible; Weymouth, pembeni) Inatupasa tutumie mafundisho yote ya Kristo katika kila sehemu ya maisha yetu. Ili iwe hivyo, tunapaswa tujishirikishe sana katika ujumbe wa kweli ya Kikristo, tukiitafakari, au kuifikiria. “Neno la Kristo” linapokuwa sehemu ya maisha yetu kweli kweli katika utimilifu wote, litatuongoza, likitusaidia tufanikishe njia zetu. Neno hilo litatuongoza tutende kwa hekima. Maisha yetu yote yanapoongozwa na “neno la Kristo,” tutakuwa wenye kutia moyo na wenye kuwajenga ndugu zetu.
Maisha yetu yote yanahusika
31. Kulingana na Wakolosai 3:17, tunapaswa kufanya nini juu ya sehemu zote za maisha yetu?
31 Mambo ambayo yanawezesha kuhifadhi amani kati ya waamini wenzetu vilevile ni ya maana katika kupata furaha na uradhi katika sehemu nyingine zote za maisha. Haitupasi kusahau hata kidogo kwamba sisi ni wanafunzi wa Yesu Kristo kila siku, ndiyo, wakati wote. Mtume Paulo aliandika hivi: “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.” (Kol. 3:17) Kwa hiyo, katika mambo yote ya maisha, yatupasa tusema na kutenda katika jina la Mwana wa Mungu, yaani, kama wajumbe wake, na inatupasa kumshukuru Yehova Mungu kwa sababu ya cheo alichotupa sisi katika kusema na kufanya kazi.
32. (a) Ikiwa wake, waume, baba na watoto wanamheshimu Yesu Kristo inavyofaa, watakuwa wakitii shauri gani? (b) Wakristo walioajiriwa kazi wataifanya katika njia gani, na kwa sababu gani? (c) Wakristo wenye kuajiri wengine kazi watawatendeaje waliowaajiri kazi, na kwa sababu gani?
32 Hivyo, basi, kumheshimu Yesu Kristo kama Bwana ndiko kunakopaswa kuwafanye Wakristo wawe waume na akina baba bora, wake na akina mama wema, wana na binti watiifu na wafanya kazi na mabwana wenye mfano mzuri. Shauri hili la Paulo linaonyesha kwamba maisha yetu ya jamaa na kazi yetu ya kimwili inapaswa kushuhudia kwamba sisi ni Wakristo: “Ninyi wake, watiini waume zetu, kama ipendezavyo katika Bwana. Ninyi waume, wapendeni wake zenu msiwe na uchungu nao. Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana. Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa. Ninyi watumwa [leo, wanaoajiriwa], watiini hao ambao kwa mwili ni bwana zenu [leo, wenye kuajiri], katika mambo yote, si kwa utumwa wa macho, kama wajipendekezao kwa wanadamu, bali kwa unyofu wa moyo, [mkimwogopa Yehova]. Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa [Yehova] ujira wa urithi. [Mtumikieni] Bwana Kristo. Maana adhulumuye atapata mapato ya udhalimu wake, wala hakupa upendeleo. Ninyi akina bwana [leo, wenye kuajiri], wapeni watumwa [leo, wenye kuajiriwa] wenu yaliyo haki na ya adili, mkijua ya kuwa ninyi nanyi mna Bwana mbinguni.”—Kol. 3:18–4:1.
33. (a) Ni kukubali cheo cha nani kunakoweza kuonekana katika maisha ya Wakristo, na kukubali huko kunaonyeshwaje? (b) Tukizishika amri za Yesu Kristo tunaweza kuwa na uhakika gani?
33 Kwa hiyo, ikiwa sisi tunajidai kuwa wanafunzi wa Kristo, maisha zetu zapaswa zionyeshe kwamba sisi tunakubali cheo chake kikuu katika mpango wa Mungu. Hii yamaanisha kwamba inatupasa tutii amri zake na kuongozwa na mafundisho yake na mfano wake. Tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatupenda na vilevile Baba yake atatupenda. Yesu mwenyewe alisema: “Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake.” (Yohana 15:10) Kama watu wanaopendwa na kukubaliwa na Yehova Mungu na Yesu Kristo, tunaweza kuwa na hakika ya kupata zawadi ya uzima wa milele.—1 Yohana 2:25.
—Kutoka The Watchtower April 1, 1978.