Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 8/1 kur. 348-351
  • “Nanyi Nyote Ni Ndugu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Nanyi Nyote Ni Ndugu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUMTAMBUA KRISTO KAMA KICHWA CHA KUNDI
  • KUBALI DARAKA
  • KUSITAWISHA ROHO YA UDUGU
  • Iweni na Juhudi Nyingi Katika Kupendana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Je! Wewe Unathamini “Zawadi Katika Wanaume”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Kikubali Cheo Kikuu Cha Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Elekeza Wapya Kwenye Tengenezo la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 8/1 kur. 348-351

“Nanyi Nyote Ni Ndugu”

“Maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu.”​—⁠Mt. 23:8.

1. Upendo unatia nini ndani, na ni nini kinachoweza kupatikana kwa kuuonyesha?

UPENDO si sifa inayopaswa kuonyeshwa na tengenezo lote tu. Bali, ni roho ya udugu inayopaswa kusitawishwa ndani ya kila mmoja wetu, bila kufikiri wengine tu ndio watakaoisitawisha. Ni sifa ambayo hutuwezesha kupendana katika udugu wa imani, inapoonyeshwa. Tumepaswa kusitawisha upendo huo wa agápe unaoongozwa na kanuni “kwa tendo na kweli,” kama watu walio ndugu.​—⁠-1 Yohana 3:18; Yohana 21:15-17.

2, 3. (a) Ni nani wanaotiwa katika neno “ndugu”? (b) Imewapasa ndugu waonaneje?

2 Kati ya Wakristo wa kwanza, neno lililokubalika kutumiwa kusalimu wanaume na wanawake wakiwa pamoja lilikuwa “ndugu” wala halikuhusu wanaume peke yao. (Matendo 1:14-16; Rum. 1:13) Neno hilo linatumiwa kutia ndani Wakristo wote, wanaume na wanawake, katika barua zote isipokuwa barua nne za Kikristo zilizoongozwa na Mungu, yaani, Tito, Filemoni, 2 Yohana na Yuda. Mtume Paulo pia aandika hivi: “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu.” (Rum. 12:10) Neno “ndugu” laonyeshwa kuwa lahusu wote katika 1 Wakorintho 15:6, ambapo Paulo autaja ufufuo wa Yesu, na kusema: “Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja.” Wakati Petro alipoonya Wakristo kwa upole wampinge adui kwa imara, aliendelea kusema hivi: “Mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.” (1 Pet. 5:9) Kwa wazi hii inatia ndani Wakristo wanaume na wanawake.

3 Yatupasa kweli tuwapende walio ndugu zetu katika Kristo. Upendo huo utatia ndani kumtegemea Kristo Yesu, na vilevile kuuthamini uhusiano wetu naye.​—⁠Yohana 15;5.

4. Twajifunza nini kutokana na maneno ya Yesu katika Mathayo 23:5-12?

4 Yesu alikazia sana kwamba ukichwa wake wa Kimasihi ulio chini ya ubaba wa Yehova ndio msingi wa udugu huo. Kwa mfano, alipokuwa akisema na makundi ya watu na wanafunzi wake, alionyesha unafiki wa waandishi na Mafarisayo, akawaambia hivi: “Matendo yao huyatenda ili kutazamwa na watu . . . Hupenda viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi, na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi.” Walitaka kusifiwa na kutukuzwa mno. Lakini Yesu aliendelea kuonyesha kwamba hali hiyo haipaswi kamwe kuwamo kati ya udugu wa Wakristo. Akanena hivi: “Ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.” Akaendelea kushauri kwamba “aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu. Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa.”​—⁠Mt. 23:5-12.

5. Yawapasa Wakristo wajiangalie wasifanye nini?

5 Ndipo Yesu alipowalaumu Mafarisayo kuwa “wanafiki.” Alionyesha hasa namna mawazo yao ya kujifikiria wenyewe tu na kujitukuza yalivyomchukiza Mungu, na hilo ni jambo lisilopaswa kuruhusiwa kati ya ndugu na dada wa Kikristo. Lakini nia mbaya zitalipenya kundi ikiwa washiriki wake hawapendani. Vilevile, lazima ndugu wa Kikristo sikuzote wajiangalie wasishushe daraka ambalo Kristo anatimiza kwa bidii sasa katika kundi, wakimtambua kabisa Yehova.

KUMTAMBUA KRISTO KAMA KICHWA CHA KUNDI

6. (a) Twawezaje kuonyesha tunamtambua Kristo kama kichwa? (b) Paulo atoa onyo gani la upole kutulinda?

6 Ili kumtambua Kristo kama kichwa, yampasa kila mmoja awe kama Kristo kwa kuonyesha wote upole na huruma, na hasa kupenda sana kila mtu aliyemo kundini. (Flp. 2:1, 2) Ili tukue kufikia kimo kamili cha Kristo ni lazima tusitawishe hali hiyo ya kupendana sana, kwa maana ni ulinzi. Tunaelezwa jambo hilo na mtume Paulo, anayesema kwamba imetupasa tuwe hivyo “ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.” Halafu sasa angalia maneno yake tofauti: “Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo. Katika yeye mwili wote ukiungamanishwa na kushikanishwa kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadiri ya utendaji wa kila sehemu moja moja, huukuza mwili upate kujijenga wenyewe katika upendo.”​—⁠Efe. 4:11-16.

7. Lazima tutambue nini juu ya Kristo?

7 Kwa hiyo lazima ikubaliwe kwamba Kristo Yesu huongoza na kuangalia kundi lake katika karne hii ya 20 sawa na alivyofanya wakati wa siku za kwanza za kundi. Lazima wote wafahamu kwamba Kristo Yesu ndiye Wakili aliyetoa ukombozi na vilevile ndiye Mfalme wa mileani wa wakati ujao.​—⁠Ebr. 2:10; Ufu. 20:6.

8. Yawapasa wote waonyesheje utii unaofaa?

8 Kushikamana sana na Kristo kama kichwa kunazuia watu mmoja mmoja wasiwe na maoni mabaya ya kujitukuza au kuwaona Wakristo wenzao kwa njia isiyofaa, kama maneno ya-mtume Paulo yanavyoonyesha: “Wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa, naye ni mwokozi wa mwili.” Upendo na umoja wapaswa kuendelea kuwako katika uhusiano huo, kama Paulo anavyoonyesha: “Waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake . . . Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Efe. 5:21-28) Kwa hiyo ndugu na dada pia kundini wanapangwa katika vyeo vyao mbalimbali wakiwa chini ya ukichwa wa Kristo. Wazee na watumishi wa huduma hawapaswi kujiona kuwa wakubwa zaidi katika kundi, bali imewapasa kutumikia kwa unyenyekevu waliomo kundini, kwa maana wamekabidhiwa kazi hiyo na Kristo. Hiyo inasaidia kulijenga kundi kwa upendo.​—⁠Rum. 14:19; 15:1, 2.

9. (a) Yawapasa Wakristo wote wajichukueje? (b) Ni kwa njia gani wale ambao wamekaa katika kweli kwa muda mrefu wanaweza kutia wengine moyo?

9 Kwa kuwa Yesu ana mamlaka ya ulimwengu wote, hakuna tena msingi wa kudai tuwe wakubwa wala mashuhuri kwa sababu ya uwezo wetu mbalimbali. Wakristo wanatambua kwamba Huyo ndiye Mwalimu wao. Kwa hiyo, habari njema zo zote tunazoweza kufundisha zimetoka kwa Kristo kupitia kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wala hazikutokana na uwezo wa mtu fulani. (Mt. 24:45-47) Hiyo yaendelea kuonyesha kwamba ‘kiongozi wetu ni mmoja’ na kwamba kundi wala njia ya kuliongoza haitegemei mwanadamu mmoja, hata awe ana uwezo wa namna gani. Kwa hiyo, mengi yanategemea vile Wakristo wanavyojichukua. Ndiyo kusema, je! wao wanaona sauti au usemi wao ndio unaopaswa kutawala, pengine kwa sababu ya miaka ambayo wamekuwa katika kweli, au kwa sababu walikuwa wakubwa wakati uliopita au kwa sababu ya cheo cha sasa? Au, kwa upande mwingine, wao wanafurahi kweli wakati wengine wanapokuwa na uwezo wa kueleza au kutumia Maandiko na kuonyesha busara ya kupanga mambo na kuyafanya? Je! wanawatia moyo kwa sababu hiyo? Hicho ni kipimo cha kweli cha kuona kama wanaupenda udugu na kutambua kwamba Kristo ndiye mwenye mamlaka, aliyetukuzwa na Yehova Mungu.​—⁠Mt. 28:18.

10. (a) Unyenyekevu wa akili waweza kuonyeshwaje? (b) Mambo ya uchokozi katika kundi yaweza kuepukwaje?

10 Unyenyekevu ni wa lazima kwa Mkristo. Unamzuia asijione mkubwa kuliko ndugu zake. Alipokuwa akiwaandikia Wafilipi, Paulo alishauri kwamba haitupasi ‘kutenda neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.’ Vilevile, yatupasa ‘kutenda mambo yote pasipo manung’uniko wala mashindano.’ (Flp. 2:3, 4, 14) Maneno hayo yaonyesha tena ubora wa kupenda ndugu zetu kwa unyenyekevu. Tukifuata shauri hilo hatutaelekea kufanya matata kwa sababu ya mambo tunayopendelea sisi wenyewe. Tena, wazee wenye kuonyesha unyenyekevu wa akili wataweza kufanya kazi na kukutana bila mashindano wala mabishano makali.

11. Imewapasa wote kundini wawe na nia na uhusiano gani?

11 Yawapasa Wakristo waonyesheje unyenyekevu huo pamoja na kujitoa wanapotumikia wengine? Je! hawaonyeshi hivyo kwa kuhurumia na kupendezwa na wote, kutia na wenye hali ya chini? Pia, hawaonyeshi hivyo kwa kuheshimu wote na kuwaona kuwa wanafaa? Paulo ajibu hivi: “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu . . . Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao. Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili.” (Rum. 12:10, 15, 16) Kutokana na maneno hayo tunaweza kuona namna inavyotupasa kusaidia wengine kwa bidii, na namna inavyotupasa kuwa na nia ya kufanya kazi kwa ajili ya ndugu zetu wa Kikristo na kufanya kazi pamoja nao pia. Sikuzote ni jambo jema sana kuonyesha tunapendezwa nao hivyo bila ya kungoja tuombwe tufanye hivyo.​—1 Kor. 10:24, 33; 13:4, 5.

12. Dada wanawezaje kutiwa moyo na mfano wa Tabitha?

12 Dada, pia, wanaweza kuwekea wengine mfano mwema. Tabitha (au, Dorkasi) alikuwa mfano bora, naye aliishi Yafa muda mfupi baada ya kuanzishwa kundi la Kikristo. “Mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. Ikawa siku zile akaugua, akafa.” Wanafunzi walipopata habari kwamba Petro alikuwa karibu katika Lida, walipeleka ujumbe aje Yafa. Ikawaje alipofika? “Petro akawatoa nje wote, akapiga magoti, akaomba, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua; hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai.” (Matendo 9:36-41) Tabitha alithawabishwa kweli kweli kwa sababu ya matendo mema yake! Hilo ni jambo la kutia akina dada moyo wafuate njia yake ya maisha, katika siku zetu pia. Kwa ufupi, maandishi yaonyesha huo ndio ufufuo wa kwanza uliofanywa na mtume.

KUBALI DARAKA

13. Imewapasa akina ndugu waonyeshe nia gani wanapokubali madaraka?

13 Hasa akina ndugu wamepaswa kukubali madaraka kwa kupenda katika kundi. Imewapasa kujitoa kwa hiari watumikie vema kundi walilogawiwa. Ziko nafasi nyingi sana zilizo wazi kwetu. Imetupasa tujichunguze kwa uaminifu, tukikumbuka kwamba tunataka kusitawisha hasa ushikamano wenye nguvu pamoja na Wakristo wenzetu na kuwasaidia katika kila njia inayowezekana. Ni jambo la kupendeza sana kwa akina ndugu kujaribu kustahili kuwa wazee au watumishi wa huduma kundini.​—1 Tim. 3:1.

14. Ndugu hao wanawezaje kusaidia wengine kundini?

14 Cho chote cha vyeo hivyo vilivyotajwa kisitafutwe kwa kusudi la kuwa na jina la ukubwa. Yampasa kila mmoja atake sana moyoni mwake kusaidia wengine, kufanya kazi akipendezwa sana na waliomo kundini, na kuendelea kusitawisha sifa za kiroho. Kwa wazi imekupasa utake sana kwa moyo kusaidia wengine kundini. Hasa imekupasa ujaribu kuwasaidia wapya au walio dhaifu. Utafanya hivyo mnapojifunza Biblia kama kikundi au katika utumishi wa kuhubiri mnapokwenda nyumba kwa nyumba, na hiyo ndiyo kazi ya maana zaidi. Unaweza kuwatia moyo kwa kuwasaidia kutayarisha migawo yao ya Shule ya Kitheokrasi. Unapopendezwa nao unawajenga, nako kufanya hivyo kwaonyesha unawapenda ndugu zako wa Kikristo.​—1 The. 2:7, 8; 1 Kor. 12:12, 25.

KUSITAWISHA ROHO YA UDUGU

15. (a) Twawezaje kujichunguza kwa uaminifu? (b) Kwa sababu gani haitupasi kujilinganisha na wengine kwa kujifikiria wenyewe tu?

15 Yatupasa sote tujichunguze kwa uaminifu kwa kusudi la kusitawisha ushikamano wenye nguvu zaidi pamoja na wengine kundini. Hatua ya kwanza ni kujichunguza kila mtu mwenyewe, badala ya kujilinganisha na wengine. Tunapojilinganisha na ndugu zetu isivyofaa, tunachochea roho ya mashindano, nayo yaweza kuleta “uadui.” (Gal. 5:20) Hiyo yatujulisha ubora wa kuonyesha unyenyekevu kwa kutotaka makuu​—⁠sifa ambayo ni ya kupendeza sana katika kusitawisha roho ya udugu. (1 Pet. 5:5, 6) Yatupasa tujichunguze kwa uaminifu tuone ni upande upi tunapoweza kusitawisha ushikamano wenye nguvu zaidi pamoja na ndugu zetu wa Kikristo.​—2 Kor. 13:5.

16. (a) Kwa sababu gani imetupasa tukuze roho ya udugu kundini: (b) Kutakuwa na matokeo gani tukitii maneno ya Paulo katika Wakolosai 3:15-17?

16 Kwa hakika, sote twapaswa kukuza roho ya udugu! Hiyo yaweza kuletea kila mmoja wetu furaha halisi, na vilevile kufanya ndugu zetu wa kiroho watupende kwa njia ya kufurahisha sana. (Efe. 6:23) Tukiwa na roho inayofaa, tunaweza kufikiria kadiri tunavyoweza kuukuza udugu kundini. (Luka 22:26) Tutataka kujitahidi mmoja mmoja tujipatanishe zaidi na wote waliomo kundini, tukitoa ushuhuda pamoja nao katika utumishi wa shambani, kwa njia hiyo tuimarishe kifungo cha upendo na shauku ya udugu halisi. (Matendo 20:18-21) Wakolosai 3:15-17 yaonyesha vizuri kwamba mtume Paulo alifikiria jambo hili: “Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani. . . . mkifundishana na kuonyana kwa zaburi, na nyimbo, na tenzi za rohoni [“nyimbo za kiroho,” NW]; huku mkimwimbia Mungu kwa neema mioyoni mwenu. Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.” Acheni pia tutie mioyo yetu nguvu iwe na kifungo kikamilifu cha upendo hata tutambue kwamba sote ni ndugu za kweli wa Kikristo, yote yakiisha kusemwa na kufanywa.​—⁠Yohana 13:35; Kol. 3:14.​—⁠Kutoka The Watchtower, Feb. 1, 1976.

[Maswali ya Funzo]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki