Elekeza Wapya Kwenye Tengenezo la Mungu
“Muupende ushirika mzima wa Ndugu.”—1 PETRO 2:17, NW.
1, 2. Licha ya mafundisho, ni mambo gani ambayo walimu Wakristo wanawapa wengine?
KAZI ya mwalimu ni kuwapa wengine mambo ya hakika. Lakini mwalimu bora anafanya zaidi ya hilo. Anapokeza wengine adili, anamsaidia mwanafunzi aone umaana wa anayojifunza na kumwonyesha jinsi anavyoweza kuyatumia kwa faida kubwa zaidi. Hasa iko hivyo kwa mwalimu Mkristo. Ni kweli kwamba ni lazima awape wengine “kweli ya Mungu.” (Warumi 1:25) Lakini hiyo inatia zaidi ya maarifa ya fundisho. Biblia inatia moyo kufundisha kumwogopa Yehova na pia sifa za wema na kutenda mambo ya akili.—Zaburi 34:11; 119:66.
2 Yesu alitaja mambo mengine yanayopaswa kufundishwa: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20, NW ) ‘Mambo yote yaliyoamriwa’ ni kutia kushiriki kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo ilitabiriwa ingefanywa siku zetu. (Mathayo 24:14) Na kuna jambo jingine tunalopaswa kuwapokeza wanafunzi wa Biblia wetu. Ni jambo gani? Ili kupata jibu la hilo, fikiria huduma ya mtume Paulo na uone jambo lililokuwa maarufu katika kufundisha kwake.
Paulo Akiwa Mfanyaji wa Tengenezo
3. Paulo alichukua hatua gani alipokuwa akifundisha watu waliokuwa wamependezwa karibuni katika Korintho?
3 Wakati wa ziara yake ya kwanza katika Korintho, mtume alikuta wengi wenye kusikiliza, ujapokuwa upinzani uliotoka kwa jumuiya ya Wayahudi. Hata hivyo, Paulo hakuwafundisha watu hao waliopendezwa karibuni wakiwa mmoja mmoja tu. Tunasoma hivi: “Akaondoka huko [kwenye sinagogi la Wayahudi] akaingia katika nyumba ya mtu mmoja jina lake Tito Yusto, mcha Mungu, ambaye nyumba yake ilikuwa mpaka mmoja na sinagogi.” (Matendo 18:7) Nyumba hiyo ikawa mahali pa wanafunzi wapya kukutania na kuabudu pamoja. Muda si muda Paulo akawafanya kuwa tengenezo la kundi.—1 Wakorintho 1:2.
4. Ni nini kilichotokea baada ya muda mfupi wa Paulo kuanza kufundisha huko?
4 Baadaye Paulo alisafiri akaenda mpaka Efeso ambako jambo kama ilo hilo lilitokea. Alifundisha watu wenye kupendezwa wakiwa mmoja mmoja “nyumba kwa nyumba.” (Matendo 20:20) Lakini pia alifanya mipango haraka ili wanafunzi wapya waweze kushirikiana pamoja. “Akawatenga wanafunzi [kutoka kwa Wayahudi, akatolea hotuba] watu kila siku katika [jumba la shule la] Tirano.” (Matendo 19:9) Muda si muda kikundi hicho cha Wakristo, pia, kikafanywa tengenezo la kundi lenye wazee waliowekwa.—Matendo 20:17, 18.
5. Walimu Wakristo wa kwanza walifanya nini na wapya upesi ilivyowezekana?
5 Basi, kwa wazi wapya walipoukubali ukweli katika karne ya kwanza, hawakuachwa wakiwa peke yao. Walikusanywa katika makundi. Makundi hayo yalifurahia kupokea kitia-moyo kutoka kwa baraza linaloongoza la wakati huo. Ndugu waliokomaa, kama Paulo na Barnaba, walitumia wakati mwingi kufundisha katika makundi hayo yaliyofanywa karibuni na “kulihubiri neno la [Yehova], pamoja na watu wengine wengi.” (Matendo 15:30-35) Kwa sababu gani ilikuwa hivyo? Ni kwa sababu gani wapya hawakuachwa wakiwa peke yao wategemee dhamiri zao zilizotoka kuzoezwa ili ziwaongoze kufanya yaliyo haki?
Kwa Sababu Gani Kukawa Makundi?
6. Ni kwa sababu gani Wakristo wa kwanza walikuwa wamefanywa tengenezo la makundi?
6 Kuna sababu nyingi. Baadhi ya sababu hizo tutataja humu. Kwanza, mtu alipokuwa Mkristo, aliacha kukubaliana na ulimwengu uliomzunguka katika mambo mengi. (Yohana 17:14, 15) Kama angeachwa akiwa peke yake, jambo hilo lingefanya awe katika hali ya upweke sana. Hata hivyo, kama alishirikiana na Wakristo wenzake katika kundi la kwao, angetiwa nguvu nao ili aendelee kujitenga. Kuongezea hilo, Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangekuwa na “umoja.” (Yohana 17:11) Umoja huo ulionwa hasa kwenye makundi. Pia Yesu alisema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Ili Wakristo waonyeshe upendo huo kwa njia ambayo ingetumika kuwa ishara kwa watu wa nje, walipaswa wawe katika jumuiya mbalimbali. Jumuiya hizo zilikuwa makundi ya Kikristo ya mahali, ambamo Wakristo waliangalia hali njema ya kiroho na kimwili ya mmoja na mwenzake. (Wafilipi 2:4) Kwa mfano, kusaidia wajane ambako Paulo alizungumza na Timotheo kwa wazi kulifanywa kitengenezo kupitia makundi.—1 Timotheo 5:3-10
7. (a) Ni nini maana ya maneno ya Paulo katika Waebrania 10:24, 25? (b) Makundi ya Kikristo ya karne ya kwanza yalitimiza sehemu gani katika kazi ya kuhubiri?
7 Kwa hiyo, maneno ya Paulo yalikuwa kitia-moyo cha moja kwa moja cha kuunga mkono kundi la mahali hapo aliposema: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Kuongezea hayo, kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme kulikotimizwa kwa njia yenye kutokeza sana katika karne ya kwanza kwa wazi kulifanywa kwa njia ya kitengenezo kupitia makundi. (Warumi 10:11-15) Kwa hiyo, roho takatifu iliongoza wazee katika kundi la Antiokia wapeleke Paulo na Barnaba wawe wamisionari katika maeneo yasiyogawiwa mtu, na Paulo alikubali mamlaka ya wazee katika kundi la Yerusalemu ya kuweza kumpa miongozo juu ya mahali alipopaswa kuhubiri.—Matendo 13:1-3; Wagalatia 2:8-10.
Makundi ya Mahali-Mahali Leo
8, 9. Ni nyingine gani kati ya sababu zinazopasa kutufanya sisi pia, tuelekeze wenye kupendezwa wetu kwenye kundi la kwetu?
8 Sisi leo tunaweza kujifunza nini kutokana na msingi huo wa mambo yaliyokuwako? Kwamba sisi, pia, twapaswa kuelekeza waliopendezwa karibuni kwenye kundi la Kikristo la mahali petu. Leo, kama ilivyokuwa katika siku za Paulo, Ukristo si dini ya watu wenye kukaa peke yao. “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe,” ndivyo kinavyoonya kitabu cha Mithali. (Mithali 18:1) Kwa upande mwingine, ‘anayeenenda na wenye hekima, atakuwa na hekima.’ (Mithali 13:20) Wapya wanahitaji utegemezo wa kiroho, kiadili na kimoyoni unaotolewa na kundi la Kikristo. Wanahitaji kupata upendo wa Wakristo wenzao, huduma ya wazee na umoja wenye kupendeza unaofanya kuwa Mkristo kuwe jambo lenye kufurahisha na la kipekee sana.—Zaburi 133:1.
9 Leo, pia, kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme ulimwenguni pote kunaongozwa kwa njia ya kitengenezo kwa sehemu kubwa kupitia makundi ya Kikristo ya mahali. (Mathayo 24:14) Kwa hiyo, tunapofundisha wapya takwa lao la kushiriki kazi hiyo, ni lazima tuwaelekeze kwenye kundi la mahali petu na kuwaonyesha jinsi ya kushirikiana nalo.
Udugu wa Mataifa Yote
10. Taja maandiko fulani yanayosema juu ya umoja wa mataifa yote wa Wakristo wa karne ya kwanza.
10 Hata hivyo, mtume Paulo alielekeza wapya katika makundi mengi zaidi ya kundi la mahali pao tu. Aliwaambia Waefeso: ‘Kuna mwili mmoja, roho moja, kama na mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu.’ (Waefeso 4:4) Kulikuwako “mwili” mmoja tu ulimwenguni pote, wala si makundi kadha yaliyotawanyika yenye kujitegemea. Pia Yesu alikuwa akizungumza juu ya washiriki walio hai duniani wa “mwili” huo aliposema juu ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” aliyepewa mamlaka ya ‘kulisha watu wa nyumba yake.’ (Mathayo 24:45-47) Watu mmoja mmoja ulimwenguni pote wangepaswa kukubali mamlaka ya “mtumwa” huyo iwapo ‘wangelishwa’ naye. Matokeo ya hilo yangekuwa ni ushirika wa Wakristo wa mataifa yote.
11. (a) Petro aliitaje hilo tengenezo la Wakristo wa mataifa yote? (b) Ni mpango gani uliodumisha umoja wa mafundisho wa Wakristo wa karne ya kwanza? Paulo alionyeshaje alitambua mpango huo?
11 Kwa hiyo, mtume Petro alitaja Wakristo wote wa siku zake kuwa “ushirika mzima wa ndugu.” (1 Petro 2:17, NW ) Walikuwa “ushirika” wa mataifa yote (Kigiriki, adelphotes’, “udugu”). Wapya walikuwa si sehemu ya kundi la mahali pao tu bali pia sehemu ya udugu wote wa mataifa yote. Makundi yalikuwa yakipashana habari. (Wakolosai 4:15, 16) Kulipokuwa masuala ya mafundisho ya kidini, Wakristo hawakujifanyia maamuzi yao wenyewe. Ili kupata jibu lenye mamlaka, walitumainia wazee wa kundi la Yerusalemu waliotumika kama baraza linaloongoza la ulimwengu katika siku hizo. (Matendo 15:2, 6-22) Paulo mwenyewe alitambua mamlaka ya kimafundisho ya baraza hilo. Ingawa alikuwa ameupokea ukweli kupitia ufunuo wa pekee kutoka kwa Yesu Kristo, bado yeye alisafiri mpaka Yerusalemu akawaeleza habari njema alizohubiriwa, ‘isije ikawa labda alikuwa akipiga mbio bure, au amepiga mbio bure.’—Wagalatia 1:11, 12; 2:1, 2, 7-10.
12. Ni mazoea gani mengine yaliyounganisha “ushirika mzima wa ndugu” karibu karibu?
12 Ili kudumisha umoja wa kufikiri na kutenda wa “ushirika mzima” wa ndugu, wahudumu wasafirio, kama Timotheo, Tito na Epafrodito walitumwa wawatembelee na kuwajenga, na barua kama vile za Paulo, Petro, Yakobo, Yohana na Yuda zilitawanywa kati yao. Kwa sababu udugu huo ulikuwako, Wakristo walio tajiri zaidi katika nchi nyinginezo walisikia juu ya uhitaji wa ndugu zao katika Yudea wakati wa taabu huko, na Paulo aliweza—kupitia makundi —kufanya msaada upelekwe kitengenezo kwa waliokuwa wahitaji. (1 Wakorintho 16:1-4) Wakristo mmoja mmoja walitiwa moyo pia waliposikia ripoti za uvumilivu na imani ya ‘ushirika mzima wa ndugu zao ulimwenguni.’—1 Petro 5:9, NW.
Wajulishe Wapya kwa “Ushirika Mzima”
13. Kuna mifanano gani mingine kati ya “ushirika mzima wa ndugu” ulimwenguni pote katika karne ya kwanza na leo?
13 Je! kuna “ushirika mzima wa ndugu” kama huo leo? Hakika ndiyo. “Mtumwa mwaminifu mwenye akili” angali yupo na angali na daraka la ‘kulisha watu wa nyumba yake.’ (Mathayo 24:45-47) Kama ilivyokuwa katika siku za Paulo, Baraza Linaloongoza linawakilisha “mtumwa” huyo na kuongoza kazi ya kuhubiri “habari njema” ulimwenguni pote. Pia, umoja wa mataifa yote unatiwa nguvu leo kwa barua na vitabu vilivyochapwa kutoka kwa Baraza Linaloongoza hilo, na pia kwa walimu waliokomaa wanaohudumu katika makundi. Kwa hiyo, mtu anapojifunza ukweli, anajifunza kuwa sehemu ya kundi la kwao na pia kuhisi kwamba yeye ni sehemu ya ‘ushirika wote wa ndugu’ ulimwenguni pote. Ni daraka la mwalimu Mkristo kusaidia mwanafunzi wa Biblia wake afanye hivyo. Tunaweza kufanyaje hivyo?
Kuwasaidia Wengine Wapende “Ushirika Mzima”
14. Ni njia gani ambazo umeona zinafanikiwa kuambia wanafunzi wa Biblia juu ya kundi la kwenu na pia tengenezo la watu wa Mungu la mataifa yote?
14 Mwalimu Mkristo anaweza kumwambia mwanafunzi wake juu ya kundi na udugu wa mataifa yote, halafu anaweza kumwonyesha. Anaweza kuwaambiaje? Hizi ni baadhi ya njia ambazo walimu wenye ujuzi wameona kuwa ni zenye matokeo: Tumia wakati kabla au baada ya funzo la Biblia kuzungumza juu ya kundi na umaana walo wa Kimaandiko, na pia “mtumwa mwaminifu mwenye akili” na jinsi linavyotutumikia leo. Eleza lilivyo Jumba la Ufalme na mikutano. Sema juu ya mambo yenye kupendeza ambayo umejifunza wakati wa mikutano. Wakati wa sala zako kabla na baada ya funzo, taja kundi la kwenu na pia udugu wa mataifa yote.
15. Ni nyingine zipi kati ya njia bora sana za kuonyesha wenye kupendezwa kundi la kwenu na tengenezo la mataifa yote?
15 Lakini tunaweza kuonyeshaje mambo hayo? Hizi ni njia ambazo zimethibitika kuwa zenye mafanikio: Upesi iwezekanavyo, waalike washiriki wenzi wa kundi waende pamoja nawe kwenye funzo ili mwanafunzi huyo aanze kufanya urafiki mpya na wengine upesi iwezekanavyo. Ni jambo la maana atambue kwamba iwapo anapoteza marafiki wo wote katika mfumo wa mambo ya kale, atapata marafiki wapya wengi hata zaidi katika ‘ushirika wote wa ndugu katika ulimwengu.’ (1 Petro 5:9, NW; Mathayo 19:27-29) Tumia kwa ukamili broshua Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20. Broshua hiyo inasimulia juu ya tengenezo la mataifa yote la kisasa la Mashahidi wa Yehova na ina picha nzuri za kusanyiko kubwa, Jumba la Ufalme, mkutano ukiendelea, kazi ya kuhubiri, na kadhalika. Itampa mwanafunzi wazo lenye kuonekana la ukubwa wa “ushirika mzima wa ndugu.” Vivyo hivyo, sura ya 23 ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, inaeleza kwa picha zenye rangi juu ya tengenezo la Mungu duniani.
16. (a) Tunapaswa kufanya nini na wanafunzi wa Biblia wetu upesi iwezekanavyo? Kwa sababu gani ya Kimaandiko? (b) Tunaweza kufaidikaje na ziara ya mwangalizi wa mzunguko au wa wilaya ili kuwasaidia wanafunzi wa Biblia wetu wawe sehemu ya watu wa Mungu?
16 Kumbuka, pia, kwamba Paulo alifanya mikutano kitengenezo katika Efeso. Alifanya hivyo karibu mara moja alipopata wenye kupendezwa. (Matendo 19:9, 10) Aliambia kundi la Korintho kwamba ‘mtu ye yote asiye mwamini au mtu wa kawaida’ akiingia kwenye mkutano wa Kikristo uliopangwa vizuri, ‘siri za moyo wake zinakuwa wazi, hata kwamba aanguke kifudifudi na kumwabudu Mungu, akitangaza: “Kweli kweli Mungu yuko katikati yenu.’ ” (1 Wakorintho 14:24, 25, NW ) Hali moja na hiyo leo, mwanafunzi anapoanza kushirikiana na kundi la mahali bila kukawia, ndivyo atakavyotambua mahali ulipo ukweli bila kukawia. Kwa sababu hiyo, walimu Wakristo wanawaalika wanafunzi wao wahudhurie mikutano ya kundi na makusanyiko makubwa upesi iwezekanavyo. Ikiwa lazima, wanajitolea ili wampitie mwenye kupendezwa na kuandamana pamoja kwenye mikutano. Kundi lao linapotembelewa na “Tito” au “Epafrodito” wa kisasa, yaani mwangalizi wa mzunguko au wa wilaya, wanahakikisha kwamba mwanafunzi wa Biblia wao anakutana naye na mkeye, labda hata kuwaalika wageni hao washiriki funzo la Biblia la kawaida.
17. Kwa hiyo, sehemu ya maana sana ya kazi yetu ya kufundisha na kufanya wanafunzi ni nini? (Mathayo 28:19, 20) Kufanya hivyo kunafaidije wanafunzi wetu?
17 Kundi la Yehova ulimwenguni pote la wapakwa mafuta ni “nguzo na msingi wa kweli.” (1 Timotheo 3:15) Ili walioanza kupendezwa karibuni wafaidike na “msingi” (“tegemezo,” NW ) huo, ni lazima wajiunge na mamia ya maelfu ya wapole wanaomiminika ili washirikiane na wapakwa mafuta hao. (Zekaria 8:23) Leo wapole hao wanafanyiza udugu wa mataifa yote. Walioanza kupendezwa karibuni wanapokuwa sehemu ya huo, wanafurahia tegemezo na ulinzi wote unaotolewa nao. Wanapendezwa na upendo wa kidugu wa Wakristo wenzao na wana nafasi ya kupeana upendo wao pia. (Waberania 13:1) Hilo linamaanisha kwamba pia wanakuwa sehemu ya umati wa mataifa yote usio na hesabu ambao utaokoka dhiki kubwa inayokuja na kuingia katika umilele wa ushirika wenye furaha pamoja. (Ufunuo 7:9-17) Kwa hiyo unapofundisha wanafunzi wa Biblia wako mafundisho ya kidini, usisahau kuwaelekeza kwenye “ushirika mzima wa ndugu” na kuwafundisha waupende.—1 Petro 2:17, NW.—Kutoka w11/1/84.
Je! Wewe Unakumbuka?
◻ Paulo alifanyaje kuhusu watu wenye kupendezwa aliokuwa amewapata karibuni katika Efeso na Korintho?
◻ Paulo aliwafaidije wapya kwa njia hiyo?
◻ Licha ya kufundisha mambo ya kidini, tunapaswa kuwa macho kuwajulisha wanafunzi wa Biblia wetu nini?
◻ Baadhi ya njia zinazofaa za kufanya hivyo ni njia gani?
[Picha katika ukurasa wa 10, 11]
Wapya wanakaribishwa kwa uchangamfu kwenye “ushirika mzima wa ndugu”