Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 8/1 kur. 352-356
  • Paradiso ya Kiroho Juu ya Dunia Chafu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Paradiso ya Kiroho Juu ya Dunia Chafu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • KUGEUZWA KWA WALIOLEMAZWA KIDINI
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 8/1 kur. 352-356

Paradiso ya Kiroho Juu ya Dunia Chafu

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1. Jitihada za wanadamu kupunguza uchafu wa dunia zimekuwa na matokeo kadiri gani?

BADO kuna maeneo madogo katika dunia hii yaliyo kama paradiso ya kidunia ya mfano. Walakini, kuendelea kuwako kwayo kunaharibiwa. Kwa muda wa miaka 20 iliyopita uchunguzi wa kisayansi wa kuchafuliwa kwa mazingira ya asili ya wanadamu wote kumefikiriwa sana. Kumekuwako na jitihada za kupunguza kuchafuliwa kwa dunia, maji na hewa, lakini mwendo wa uchafuzi ungali waendelea na kuongezeka.

2. Ijapo kuchafuliwa kwa mazingira ya asili, ni paradiso gani inayoenea, na tangu mwaka gani?

2 Bila kupatwa na uchafuzi huo wenye kuharibu wenye kuenea duniani pote, paradiso ya kiroho yasitawi na kujieneza zaidi na zaidi. Wakati inapopanuka, watu zaidi na zaidi wenye fikira za kiroho wanaifurahia na kuishi maisha zenye furaha zaidi. Hata wanapokea matumaini ya kuishi milele katika paradiso ya kidunia isiyochafuliwa. Bila shaka, paradiso ya asili ya kidunia ingali wakati ujao, bila hivyo kuchafuliwa kwa sasa kwa mazingira ya asili ya wanadamu kusingeruhusiwa kuendelee. Wanadamu hawana uwezo na hekima ya kurudisha makao ya kwanza ya kiparadiso kwenye dunia hii. Lakini tangu mwaka wa kwanza wa amani baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, paradiso ya kiroho imepandwa hapa duniani. Bila shaka hii ndiyo ile paradiso ambayo mtume wa Kikristo Paulo anaandika juu yake katika barua yake ya pili kwa kundi la karne ya kwanza katika Korintho, Ugiriki.

3. Mtume Paulo alisema nini katika barua yake ya pili kwa Wakristo Wakorintho juu ya paradiso hii?

3 Akiandika karibu na katikati ya karne ya kwanza, kama mwaka wa 55 W.K., aliliambia kundi hili la waamini wenzake hivi: “Kweli, si faida kwangu kuyisifu, lakini nitasema yulu ya maono na mafunulo ya Bwana. Ninayua mutu katika Kristo tangu miaka kumi na mine (kama katika mwili, siyui; kama inje ya mwili, siyui, Mungu anayua), mutu huyu alichukuliwa yulu hata mbingu ya tatu. Nami ninayua mutu huyu (kama katika mwili, kama inje ya mwili, siyui: Mungu anayua,) ya kama alichukuliwa yulu hata Paradiso, akasikia maneno yasiyoweza kusemwa na yasiyofaya mutu kuyasema. Kwa maneno ya mutu huyu nitayisifu, lakini kwa ajili yangu, mimi sitayisifu.”​—⁠ 2 Kor. 12:1-5, CSB.

4. (a) Ni nani yule “mutu katika Kristo” ambaye Paulo anataja? (b) Kwa habari ya hilo, alimaanisha nini aliposema, “Kwa maneno ya mutu huyu nitayisifu, lakini kwa ajili yangu, mimi sitayisifu”? (c) Juu ya hali yake alipokuwa anaona maono haya, ni kwa sababu gani alisema, “kama katika mwili, siyui; kama inje ya mwili, siyui”?

4 Hapa mtume Paulo hakuwa akisema juu ya mtu fulani mwingine, bali juu yake mwenyewe. Walakini, kama mtu aliyependelewa sana na Mungu, anasema juu yake mwenyewe alipokuwa na maono hayo yaliyosimuliwa juu yasiyo na mfano; na aweza kujisifu kwa kufaa juu ya jinsi alivyokuwa kama mtu alipokuwa katika hali hiyo yenye kupendelewa sana. Lakini yeye hawezi kujisifu kwa kufaa kama mtu wa kawaida bila mapendeleo hayo yenye maana sana kutoka kwa Mungu. Maono yake yalikuwa ya kweli sana hata ilikuwa kana kwamba alikuwako uko huko katika mwili wake wenye kuonekana, lakini kwa busara mwili wake wenye kuonekana ulibaki duniani na maono yake yalikuwa kama ya hali ya usingizi na aliyosikia yalikuwa wakati alipokuwa katika hali hii kama ya usingizi. Ikiwa maono haya yalitukia miaka kumi na minne kabla ya kuandika barua yake ya pili kwa kundi la Korintho, basi yalitukia kama mwaka wa 41 W.K., kabla ya safari yake ya kwanza ya umisionari pamoja na Barnaba, iliyokuwa kama mwaka wa 47/48 W.K. Kwamba aliyosikia yalikuwa katika lugha ya Kiebrania au Kigiriki, zilizojulikana kwake, ama katika lugha fulani ya kigeni isiyoweza kutafsiriwa katika lugha za kibinadamu zinazojulikana, mtume Paulo haelezi waziwazi.

5. Mtajo wake wa “mbingu ya tatu” waonyesha nini?

5 Katika kuchukuliwa kwake hata mbingu ya tatu, Paulo hakuchukuliwa juu na kupelekwa kwenye mbingu ya tatu ya mifululizo ya mbingu zilizofuatana. Yeye alichukuliwa kiwimawima, na, kama vile hesabu hii tatu au ya tatu inavyotumiwa katika Biblia kuonyesha ukubwa au mkazo, “mbingu ya tatu” ingeonyesha upeo wa kuinuliwa kwake, hali yake ya kukwezwa. Hali hii haikumfahamisha mambo yaliyo katika mbingu za watu wa kiroho kwa jinsi ile Yesu Kristo aliyeshuka kutoka mbinguni akarudi kwenye mbingu za kiroho anavyoyafahamu mambo yasiyoonekana ya kimbinguni. Kwa jinsi ya mfano, Paulo alikuwa amekwisha kuketi na Wakristo wenzake duniani “katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu.” (Efe. 2:6) Basi kuchukuliwa kwake hata “mbingu ya tatu” kungeonyesha kukwezwa sana kwa kiroho kwa Paulo juu ya hali ya kiroho ya Wakristo wenzake. Bila shaka hali hiyo ya kukwezwa ilimpa maono ambayo hakupata kuwa nayo kabla ya hapo, na haya yangejionyesha kwa jinsi alivyosema na kuandika.

6, 7. (a) Sababu gani ile “Paradiso” ambayo Paulo anataja si ile ile inayotajwa katika Ufunuo 2:7, NW? (b) Sababu gani ile “Paradiso” alikochukuliwa Paulo haikuwa “bustani ya Edeni”?

6 Kwa habari ya kuchukuliwa kwake “hata Paradiso,” huku kunashirikishwa hapa na “mbingu ya tatu.” Huku kungeonyesha jambo fulani la kiroho. Lakini hili lisingeonyesha kwamba ile paradiso ambako Paulo alipelekwa ilikuwa ndiyo ile inayotajwa katika ujumbe uliotumwa na Yesu Kristo aliyetukuzwa upelekwe kwenye kundi katika Efeso, Asia Ndogo: “Yeye aliye na sikio na asikie ambayo roho inayaambia makundi: Yeye ashindaye nitamruhusu kula ya mti wa uzima, ulio katika paradiso ya Mungu.” (Ufu. 2:7, NW) Hii “paradiso ya Mungu” ni ya mfano katika mbingu za kiroho zisizoonekana, ambamo mwili na damu haziwezi kuingia na ambamo jicho la kimwili haliwezi kuona. (1 Kor. 15:50) Wala hakuna dokezo lo lote la kuonyesha kwamba mtume Paulo aliona mifano ya vitu vilivyo katika mbingu za kiroho zisizoonekana kama alivyoona mtume Yohana, ambayo anatusimulia katika Ufunuo, sura ya nne. Hivyo haielekei sana kwamba mtume Paulo alichukuliwa hata kwenye “paradiso ya Mungu” akaone “mti wa uzima” wake.

7 Kwa habari ya paradiso ya kwanza ya kidunia, “bustani ya Edeni,” hakuna lo lote lisilojulikana na viumbe vya kibinadamu juu ya paradiso hiyo. Si jambo asiloweza mwanadamu kujua, na kurudishwa kwayo kwenye dunia chini ya ufalme wa Kimasihi wa Mungu kumefahamika kulingana na unabii wa Biblia. (Mwa. 3:8-24) Kwa sababu hiyo, mtume Paulo hangekuwa na lazima ya kupokea “maono na mafunulo [yasiyo ya asili] ya Bwana” ili ajifunze na kujua hilo.​—2 Kor. 12:1, CSB.

8, 9. (a) Ile njozi aliyopewa mtume Paulo ilikuwa juu ya paradiso gani, ikiwako wakati gani? (b) “Maneno yasiyoweza kusemwa” ambayo Paulo alisikia yalitia ndani nini, na kusema maneno hayo kungalimaanisha nini?

8 Walakini, kuna paradiso nyingine ambayo kwa unabii Maandiko Matakatifu hufananisha, hata kutupatia mfano wa kihistoria wa hii, katika nchi ya Yuda baada ya uhamisho wa Kibabeli wa Wayahudi. Paradiso hii ni ya kiroho katika wakati wetu, karne kumi na tisa baada ya kuchukuliwa kwa mtume Paulo “hata mbingu ya tatu” na “hata Paradiso” katika njozi isiyo ya asili. “Maneno yasiyoweza kusemwa na yasiyofaya mutu kuyasema,” ambayo Paulo alisikia wakati wa maono hayo ya kweli, yalikuwa juu ya paradiso hii ya kiroho iliyokuwa bado inakuja wakati ujao. Hali hii yenye baraka ya wanafunzi wa kweli wa Kristo ingetokea wakati wa “kuwapo” au parousia yake katika “mwisho wa taratibu ya mambo.”​—⁠Mt. 24:3, NW.

9 Paulo aliongozwa na Mungu atabiri juu ya “ukafiri” ambao ungelipata kundi la Kikristo kabla ya “kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo,” lakini haikufaa (haikuwa halali) kwake kama mwanadamu kusema juu ya paradiso hii ya kiroho, ambayo juu yake alisikia katika “maneno yasiyoweza kusemwa.” Kufanya hivyo kungalimaanisha kwake kutafsiri unabii wa Biblia uliohusika na paradiso hii ya kiroho.​—2 The. 2:1-3, NW; 2 Kor. 12:1-4, CSB.

KUGEUZWA KWA WALIOLEMAZWA KIDINI

10. Nabii Isaya alitabiri matokeo gani ya tendo la Mungu kwa ajili ya watu wake?

10 Maneno yenye kutia moyo kutokana na unabii wa Isaya juu ya kuokolewa kwa mabaki ya Israeli wa kiroho katika utumwa wenye kuogofya katika Babeli Mkuu na kuletwa kwa kisasi cha kimungu juu ya milki hiyo ya ulimwengu ya dini ya uongo, husema hivi: “Tazama, Mungu wenu atakuja na kisasi, na malipo ya Mungu; atakuja na kuwaokoa ninyi.” (Isa. 35:4) Nabii Isaya alitabiri itikio gani kwa maneno hayo yenye kutia moyo ambayo alitumiwa awaambie waabudu wa Yehova ambao kwa muda hali yao ya kidini ilikuwa imekuwa kama “jangwa,” “inchi kavu” isiyo na maji na nyika? (Isa. 35:1, CSB) Wangeonaje kuja kwa Mungu na kuwaokoa, hali wakati ule ule angekuwa akileta kisasi na malipo kwa waonezi na waharabu wao? “Ndipo,” ajibu nabii, “macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba; maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji; katika makao ya mbweha, walipokuwa wamelala, patakuwa na majani, pamoja na mianzi na manyasi.”​—⁠Isa. 35:5-7.

11. Ni nini linalomaanishwa na kufumbuliwa kwa “macho ya vipofu,” na huku kulifanywaje katika mwaka wa 537 K.W.K.?

11 Kufunguliwa kwa macho ya vipofu kulimaanisha kufunguliwa kutoka katika gereza lenye giza! Kumulikwa huko kwa macho kunakotokana na ukombozi ndiyo iliyokuwa kazi ambayo kwa hiyo Yehova alimweka Mtumishi wa Kimasihi wake afanye katika wakati wake, akimwambia hivi: “Nitakuhifadhi, nitakutoa uwe agano [au, rehani] la watu hawa, ili kuiinua nchi hii, na kuwarithisha urithi uliokuwa ukiwa; kuwaambia waliofungwa, Haya, tokeni; na hao walio katika giza, Jionyesheni.” (Isa. 49:8, 9) Hivyo katika mwaka wa 537 K.W.K., Babeli wa zamani ulipokuwa umekwisha kuangushwa na mshindi wa Kiajemi Koreshi Mkuu, Mungu aliwatoa watu wake waliohamishwa watoke katika kifungo chao cha muda mrefu katika Babeli, ili wauone mwanga wa uhuru katika “urithi” wao, nchi yao yenye kupendwa.

12. Ni kufumbuliwa gani kwa “macho ya vipofu” kulikotukia katika mwaka wa 1919?

12 Vilevile, katika mwaka wa 1919 W.K., Yehova alitoa mabaki yake waliotiwa mafuta ambao macho yao yalikuwa yamepofushwa na kifungo katika Babeli Mkuu ili wauone mwanga wa kibali yake katika hali yao ya kiroho iliyorudishwa. Kwa kadiri wakati ulivyosonga, macho yao yaliendelea kuonyesha uzuri zaidi wa hali yao ya kiroho.

13. Ni katika njia gani masikio yao yalikuwa ya “viziwi,” lakini kuzibuliwa kwa masikio yao kumetokeza nini?

13 Kwa habari ya masikio yao ya kufahamu kwa kiroho, haya yalikuwa yamefanywa yasisikie unabii wa Biblia juu ya kurudishwa kwao na juu ya kazi yao ya kutoa ushuhuda ulimwenguni pote baada ya kufunguliwa kwao kutoka Babeli Mkuu. Hawakuwa wamesikia wakielezwa maana sahihi ya unabii huo. Sasa, walipokwisha kurudia hali yao ya kiroho iliyofanywa upya, walianza kusikia unabii huo kama unavyoelezwa kupitia kwa tengenezo la Mungu wakapata kufahamu unabii huo unaotimizwa sasa. Ahadi hii ya kimungu imetimizwa kwa uaminifu: “Na katika siku hiyo viziwi watasikia maneno ya hicho chuo, na macho ya vipofu yataona katika upofu na katika giza. Wanyenyekevu nao wataongeza furaha yao katika [Yehova], na maskini katika wanadamu watafurahi katika Mtakatifu wa Israeli.” (Isa. 29:18, 19) Mpaka leo hii masikio ya waabudu wa Kikristo wa Yehova yameendelea kuwa yaliyozibuliwa yapate kusikia ujumbe unaotokana na kufunuliwa kwa unabii. Wanaendelea kuzibua masikio yao wapate kusikia amri za kimungu zinazotokana na Neno lake lililoandikwa kwa habari ya kazi ya Ufalme inayofanywa sasa katika dunia yote.

14. Ni ulema wa namna gani ambao mabaki walikuwa wamepata? (b) Kama ilivyotabiriwa, ‘wanaruka-rukaje kama kulungu’?

14 Pia mwujiza wa kiroho umetukia kwa habari ya “mtu aliye kilema.” Mabaki ya Israeli wa kiroho walikuwa wamelemazwa na Babeli Mkuu kupitia kwa kutumia kwake mamlaka za nchi za kisiasa, kisheria na za kivita. Uhuru wao kamili wa kwenda hadharani na wa kidini ulikuwa umezuiwa sana. Lakini wakati maneno yenye kutia moyo ya Mungu kupitia kwa Isaya yaliposikiwa na kutiwa nguvu kwa mikono iliyo dhaifu na kuimarishwa kwa magoti yaliyolegea kulipotukia, Waisraeli wa kiroho wenye kuitikia walirudishiwa hali ya kutembea imara bila kuyumba-yumba. Kama ilivyokuwa imetabiriwa: “Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu.” Kazi ngumu katika utumishi wa Ufalme wa Yehova zilianza kufanywa kwa nguvu. Kulikuwako kuruka-ruka, kuzidi, katika kazi iliyotakiwa kufanywa katika kuhubiriwa kwa “habari njema ya ufalme . . . katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Kusema kwa jinsi ya mfano, kulikuwa ni kupanda juu ili kuwatengeneza Waisraeli wote wa kiroho wapate kuuhubiri ujumbe wa Ufalme nyumba kwa nyumba.

15. “Ulimi wake aliye bubu” ulianza ‘kuimba’ wakati gani, na hili lilisababishwa na nini?

15 “Na ulimi wake aliye bubu utaimba.” (Isa. 35:6) Hili, pia, lilitimizwa wakati wa kurudishwa kwa mabaki ya Israeli wa kiroho kwenye hali yao ya kiroho inayofaa katika muda wa baada ya vita. Walikuwa na mengi ya kumsifia Mungu wa wokovu wao walipouona mgeuzo wa hali yao duniani. Badala ya kuendelea kutamani sana makao yao ya kimbinguni, waliona maisha yanakuwa yenye kuishika zaidi katika hali yao ya kiroho duniani. “Maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani.” Maisha katika utumishi wa Ufalme wa Mungu hapa duniani yakawa yenye kuburudisha kwao kiroho. Maji ya uzima yalianza kutiririka katika Biblia Takatifu wakati roho ya Mungu ilipowezesha ifahamike zaidi, na maana ya unabii wake ikawa kamili zaidi na yenye kutia moyo kwa kusisimua. Hivyo, je! hii haikuwa sababu yenye kuamsha kwa waabudu wa Yehova waliorudishwa, ambao ulimi wao ulikuwa umekuwa kama wa “bubu” kwa sababu ya ukiwa wa kiroho uliokuwa umetangulia kuwapata, ‘waimbe’? Ndiyo!

16. Kama ilivyotabiriwa katika Isaya 35:7, ni nini mengine yaliyokuwa matokeo ya baraka ya Yehova juu ya watu wake?

16 Kwa sababu ya baraka nyingi ambazo Mungu alimiminiza juu ya mabaki yake waliorudishwa wa Israeli wa kiroho, mambo zaidi yenye kufurahisha ya unabii wa Isaya yalitokea mbele yao katika maana ya mfano: “Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji; katika makao ya mbweha, walipokuwa wamelala, patakuwa na majani, pamoja na mianzi na manyasi.”​—⁠Isa. 35:7.

17. (a) Ni nini linaloonyeshwa na mtajo wa “mbweha”? (b) Kuonekana kwa “majani, pamoja na mianzi na manyasi” kwaonyesha badiliko gani?

17 Mtajo wa mbweha wakumbusha hali zenye ukiwa. Mbweha ni mbwamwitu mwenye kula mizoga ya wanyama wengine anayependa kukaa mara nyingi katika sehemu za nchi zenye mwitu na za upweke, na hata katika maeneo yanayofanana na majangwa. Kuwapo kwao kungeonyesha sehemu za nchi zenye ukavu na zenye ukame. Yakiachwa katika hali hiyo, makao hayo na mahali wanapolala mbweha yasingekuwa mahali penye kutamanika kuishi wanadamu. Wangetamani na kuomba maji, chemchemi, mvua. Kama sehemu hizo zingemwagiwa maji, zingefanyiza mabwawa yenye mianzi. Hata manyasi au mafunjo yangemea huko. Na mpambo wa majani mabichi ungefunika nchi ambayo wakati mmoja ilikuwa kama jangwa. Wanadamu wangehamia humo, na mlio wa mbweha usingelifanya tena giza zito la usiku liogofye. Badiliko la ajabu la namna hiyo lilianza katika mwaka wa 537 K.W.K.

18, 19. (a) Sehemu hii ya unabii ilitimizwaje katika habari ya nchi ya Wayahudi waliohamishwa? (b) Kwa jinsi ile ile, jambo gani limetukia tangu mwaka wa 1919 W.K.?

18 Kabla ya Wababeli walioshuka kwa njia ya kaskazini kuiacha nchi ya ufalme wa Yuda ukiwa, nabii Yeremia alitabiri matokeo ya kuja kwao, akisema hivi: “Sauti imesikiwa, Tazama, inakuja; mshindo mkuu kutoka nchi ya kaskazini, ili kuifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa, makao ya mbweha.” Pia, kama mneni wa Yehova, yeye anasema hivi: “Nami nitafanya Yerusalemu kuwa magofu, makao ya mbweha; nami nitaifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa, isikaliwe na mtu awaye yote.”​—⁠ Yer. 10:22; 9:11.

19 Kwa hiyo, wakati Wayahudi waliohamishwa walipotoka Babeli wakarudi kwao nchi yao ilipokwisha kuwa ganjo lisilokaliwa kwa muda wa miaka 70, kulikuwako makao, mahali wanapolala mbweha yaliyohitaji kugeuzwa kuwa maeneo yenye majani, yenye maziwa matulivu ya maji na kando zake mianzi na mafunjo au manyasi yangeweza kumea. Hivyo Wayahudi waliorudishwa walishinda ganjo hilo, na mbweha wakaondoka. Kwa jinsi ile ile, kusema kwa mfano, kulianza badiliko katika kuonekana kwa hali ya kiroho ya mabaki waliorudishwa wa Israeli wa kiroho tangu mwaka wa 1919 W.K. na kuendelea. Tangu wakati huo, uchafu wo wote wa hali yao ya kiroho uliovumbuliwa ulisafishwa. Lakini kwa habari ya mataifa ya kilimwengu, waliendelea kuichafua dunia kuliko isivyokuwa zamani. Ijapokuwa uchafuzi huu wa ulimwengu, tazama! paradiso ya kiroho imelimwa na mashahidi wa Kikristo wa Yehova, kwa kubarikiwa na Yeye na kwa heshima ya jina Lake.​—⁠Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 8.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki