Je! Wewe Unathamini “Zawadi Katika Wanaume”?
USIKU uliotangulia kifo cha Yesu, yeye aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Sitawaacha ninyi yatima.” Kisha akawaahidi kuwapelekea msaidizi, roho takatifu ya Mungu, ambayo ingetenda juu ya akili na mioyo yao kama mkumbushaji na mwalimu na pia ingekuwa mshuhudiaji juu ya Kristo. (Yohana 14:18, 26; 15:26) Kristo, akiwa mbinguni, angekuwa Kichwa chao naye angewaongoza. Mungu hakumpa mwanadamu ye yote wala baraza ya wanadamu ukichwa huo, bali alimwekea Mwanawe ukichwa huo.—Kol. 1:18.
Zaidi ya roho takatifu, Kristo alitumia malaika pia kutumikia kundi lake duniani. (Ebr. 1:13, 14) Lakini alifanya jambo jingine tunaloweza kushukuru. Mmoja wa mitume wake aliandika hivi: “Alipopanda juu alichukua watumwa; alitoa zawadi katika wanaume.” (Efe. 4:8, NW) Mwandikaji hapa alifafanua Zaburi 68:18 akaitumia kwa Yesu Kristo kama Wakili Mkuu wa Yehova. Yesu alipanda mbinguni akiwa ‘ameushinda ulimwengu’ kwa mwendo wake wa kushika ukamilifu. Alishinda mauti pia na Shetani Ibilisi kwa sababu Mungu alimfufua kwa wafu. (Yohana 16:33; Ebr. 2:10, 14; Matendo 2:24) Kama mshindi Yesu alichukua “watumwa” kutoka kwa adui. “Watumwa” hao ni wanadamu waliokuwa wamekuwa watumwa kwa dhambi na mauti. Sasa walikuwa wanaweza kutumiwa na Mungu. Sasa Kristo angeweza kutoa “watumwa” hawa wake watumikie Yehova Mungu na kundi lake la Kikristo.
Ni kwa njia gani “watumwa” hawa, waliotolewa na Kristo kama Kichwa, ni “zawadi katika wanaume”? Wao ni wanaume wenye uwezo mbalimbali unaohitajiwa ili kundi liwe na hali njema. Wanaume hao wamekuwa watumishi wa Mungu, ambaye roho yake inawaongoza wamtumikie Yehova kwa jitihada nyingi na kwa moyo wote. Wanaume wote wa Kikristo wanayo nafasi hii, lakini wengine huonyesha imani na juhudi kubwa zaidi. Yesu Kristo huona mwendo wao wa kujaribu “kufikia” utumishi mkubwa zaidi. (1 Tim. 3:1, NW) Yeye ataka wanaume wenye imani kama hiyo awatumie kundini. Kupitia kwa roho takatifu ya Mungu yeye huzidisha uwezo mbalimbali walio nao wafundishe, walichunge kundi la Mungu, wasaidie, watie moyo na kuongoza, kwa kusudi la kutengeneza upya wale waliomo kundini wajipatanishe zaidi na mapenzi ya Mungu. Kristo huwatayarisha kufanya huduma ya pekee, kuangalia kazi fulani za kundi. Kusudi lao ni kusaidia ndugu na dada wa Kikristo wakuze hali ya kiroho, ili roho ya Mungu ifanye kazi kundini kwa uhuru zaidi. “Zawadi katika wanaume” zinasaidia kuleta umoja wa kundi, mpaka “wote waufikie umoja katika imani . . . kufikia kimo cha ukamili wa Kristo.”—Efe. 4:11-13, NW.
Leo twaziona ‘zawadi hizi katika wanaume’ wakitumikia kama wazee na watumishi wa huduma. Wanaume hawa wanajua kwamba wao si ‘watawala’ wala “mabwana” wa kundi, wala wao si mababa, bali ni ndugu, “wenzi wafanya kazi.” (1 Kor. 4:8; 2 Kor. 1:24, NW) Imewapasa ‘kuongoza’ katika kufanya yaliyo haki, kulihubiri neno la Mungu, kukaripia, kutia moyo na kufundisha, lakini si kuamuru wala kutwika wengine dhamiri zao. (Ebr. 13:7; 2 Tim. 4:2) Kazi yao ni kutumikia ndugu zao, “ili [sisi tuliomo kundini] tusiwe . . . tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.”—Efe. 4:14; Gal. 5:13.
MAPATANO KAMA KUNDI
Kwa hiyo wazee katika makundi ya mashahidi wa Yehova wanajua kwamba wao, pamoja na kila mshiriki mwingine wa kundi, ni kama ‘viungo’ vya mwili, kama vile mtume asemavyo: “Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua [katika mambo yote] hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo. Katika yeye mwili wote ukiungamanishwa na kushikanishwa kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadiri ya utendaji wa kila sehemu moja moja, huukuza mwili upate kujijenga wenyewe katika upendo.”—Efe. 4:15, 16.
Kiungo cha mwili hutegemea viungo vingine pia kilindwe na kufaidiwa. Hivyo, washiriki wote wa kundi, kutia na wazee na watumishi wa huduma, wanategemeana. Wanajua kwamba roho ya Mungu ndiyo inayotimiza mapenzi ya Mungu, si uwezo wao wenyewe, kupitia kwa roho ya moyo wote ya ndugu. Kazi ya wazee ni kutia ndugu moyo wawe na roho hiyo ya moyo wote. Pia, wanaona kwamba ukuzi wa kiroho, utendaji laini na ongezeko haliji kwa sababu hasa ya uwezo wa tengenezo, bali ‘kwa kuwa wenye kuungamana’ katika kifungo chenye kuunganisha cha upendo kupitia kwa utendaji wa roho ya Yehova.—Kol. 3:14.
Ndugu na dada wote, kama sehemu ya kundi, wana shirika la wazi katika utendaji wa kundi wenye mapatano. Wanatambua kwamba hizo “zawadi katika wanaume” zilizo nzuri zinastahili kuheshimiwa, kwa faida ya kundi lote. (Ebr. 13:17) Kila mmoja hushiriki kutenda kulingana na imani yake, hali zake na uwezo wake, akishirikiana na “kila kiungo” kitoacho kinachohitajiwa. Hivyo kundi lote ni lenye furaha, bila sehemu zo zote zenye ‘kuwasha’ wala zenye kukwaruzana.
Je! si hekima ya ajabu kwa upande wa Kristo kama Kichwa cha kundi kutoa hizi “zawadi katika wanaume”? Je! haifariji kuwa na wanaume wa kutusaidia, ndugu zetu, wanaofanya kazi pamoja nasi na wenye kupatwa na magumu na mambo yale yale yanayotupata? Je! hatuwaonei shauku na kuthamini kwamba wamejitoa waongozwe na roho ya Mungu hata uwezo mbalimbali waliozaliwa nao umeongezwa wakaanza kumtumikia Mungu na sisi sote?
Zawadi hutolewa kutimiza uhitaji fulani, au kufurahisha mtu. Bila shaka Kristo alikuwa akifikiria mambo hayo alipotoa “zawadi katika wanaume.” Kwa hiyo imewapasa wazee na watumishi wa huduma wajitahidi kuona kwamba washiriki wote wa kundi wana furaha. Waepuke kufanya waogopwe na akina ndugu. Wala wasijione kuwa “Wenye fadhili” ambao ndugu wana deni kwao, kwa maana haiwapasi kuwa kama watawala wa taratibu ya mambo ya ulimwengu huu. (Luka 22:25, 26) Kristo ndiye Mwenye fadhili ambaye wote wana deni yake. Yeye husimamia mambo ya kundi ili atuletee furaha. ‘Nira yake ni laini na mzigo wake ni mwepesi.’—Mt. 11:30; 1 Tim. 6:15.
Kwa hiyo imewapasa wote kundini wamshukuru Yehova Mungu kupitia kwa Kristo kwa ajili ya mpango wake unaotofautiana sana na ule wa ulimwengu huu. Kuthamini kunakofaa kunaweza kutusaidia tupate “kumfahamu sana Mwana wa Mungu,” na kumtambua kabisa kama Kichwa cha kundi. Hiyo itatuendeleza katika uhusiano unaofaa na Yehova Mungu—ambaye kwa kweli ndio mradi mkubwa wa Wakristo wote wa kweli!—Efe. 4:13; Yer. 9:23, 24.