Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 226-228
  • Kitabu cha Biblia Namba 51—Wakolosai

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Biblia Namba 51—Wakolosai
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA WAKOLOSAI
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Wakolosai—Mashauri Yanayofaa Juu ya Imani na Mwenendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Yehova Aweza Kukufanya Uwe Mwenye Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Saidia Wengine Watembee kwa Kumstahili Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Dumisha Imani Katika Mungu na Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 226-228

Kitabu cha Biblia Namba 51—Wakolosai

Mwandikaji: Paulo

Mahali Kilipoandikiwa: Rumi

Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 60-61 W.K.

1. Mji wa Kolosai ulikuwa wapi?

KWA kuacha Efeso nyuma yao, wanaume wawili walisafiri mashariki kupitia Asia Ndogo kandokando ya Mto Maeander (Menderesi). Walipofikia kitawi cha mto huo ambacho chaitwa Liko, katika nchi ya Frigia, walienda upande wa kusini-mashariki ili waufuate mto kwa kupitia katika bonde lenye kuzungukwa na mlima pande zote. Mbele yao ulikuwako mwono mzuri: malisho yaliyo mabichi yenye rutuba yakiwa na makundi makubwa ya kondoo. (Bidhaa za sufi zilikuwa chanzo kikuu cha pato kwa jimbo hilo.a) Wakisonga mbele kupanda bonde hilo, wasafiri hao walilipita lile jiji tajiri la Laodikia, upande wa kulia, likiwa ndilo kitovu cha usimamizi wa Kirumi kwa wilaya hiyo. Upande walo wa kushoto, ng’ambo ya mto, wangeweza kuona Hierapoli, yenye umaarufu kwa ajili ya mahekalu na chemchemi za maji moto. Katika majiji yote mawili mlikuwamo makundi ya Kikristo, na pia katika ule mji mdogo wa Kolosai, karibu kilometa kumi na sita juu zaidi kwenye bonde hilo.

2. (a) Wajumbe wawili waliotumwa na Paulo kwenda Kolosai walikuwa nani? (b) Ni jambo gani lajulikana kuhusu kundi la Kolosai?

2 Wasafiri hao walikuwa wakienda Kolosai. Wote wawili walikuwa Wakristo. Angalau, mmoja wao alilijua vizuri mkoa huo, kwa maana alikuwa wa kutoka Kolosai. Jina lake lilikuwa Onesimo, naye alikuwa mtumwa mwenye kurudia bwana wake, aliyekuwa mshiriki wa kundi huko. Mwandamani wa Onesimo alikuwa Tikiko, mwanamume huru, na wote wawili walikuwa wajumbe waliopelekwa kutoka kwa mtume Paulo, wakiwa wamechukua barua kutoka kwake waliyoandikiwa “ndugu wenye imani katika muungano pamoja na Kristo huko Kolosai.” Kwa kadiri tujuavyo, Paulo hakuzuru kamwe Kolosai. Lile kundi, ambalo sana-sana lilikuwa la Wasio Wayahudi, labda lilianzishwa na Epafra, aliyekuwa amefanya kazi-jasho miongoni mwao na sasa akawa yupo pamoja na Paulo katika Rumi.—Kol. 1:2, 7; 4:12, NW.

3. Barua ya Wakolosai yafunua nini juu ya mwandikaji, na pia wakati na mahali ilipoandikiwa?

3 Mtume Paulo ndiye aliyekuwa mwandikaji wa barua hii, kama vile yeye aeleza katika maneno yake ya kufungua na ya kufunga. (1:1; 4:18) Pia umalizio wake waeleza kwamba aliiandika akiwa gerezani. Huu ungekuwa ndio wakati wa kutiwa kwake gerezani mara ya kwanza katika Rumi, 59-61 W.K., ambapo aliandika barua kadhaa za kitia-moyo, huku ile barua kwa Wakolosai ikipelekwa pamoja na ile iliyopelekwa kwa Filemoni. (Kol. 4:7-9; Flm. 10, 23) Yaonekana iliandikwa karibu wakati mmoja na barua kwa Waefeso, kwa maana mawazo na vifungu vingi vyasema mamoja.

4. Ni kitu gani chashuhudia ukweli wa Wakolosai?

4 Hakuna sababu za kutia shaka juu ya kudumishwa kwa uasilia wa barua kwa Wakolosai. Kuwapo kwayo pamoja na nyaraka nyingine za Paulo katika ile funjo la Chester Beatty Papyrus No. 2 (P46) ya karibu 200 W.K. kwaonyesha kwamba ilikubaliwa na Wakristo wa mapema kuwa moja ya barua za Paulo. Ukweli wayo washuhudiwa na wenye mamlaka wale wale wa mapema ambao washuhudia uasilia wa barua nyinginezo za Paulo.

5. (a) Ni nini kilichomfanya Paulo kuwaandikia Wakolosai? (b) Barua hii yakazia nini?

5 Ni nini kilichomfanya Paulo kuandika barua kwa Wakolosai? Kwanza, Onesimo alikuwa akirudi Kolosai. Epafra alikuwa amejiunga na Paulo majuzi, na bila shaka ripoti yake kuhusu hali zilizokuwa Kolosai zilitoa sababu zaidi ya kuandika barua hiyo. (Kol. 1:7, 8; 4:12) Hatari fulani ilitisha kundi la Kikristo huko. Dini za siku hiyo zilikuwa katika hatua hatua za kufumuka, na dini mpya zilikuwa zikifanyizwa daima kwa kuzichanganya na sehemu za zile za zamani. Kulikuwako falsafa za wasiomcha Mungu zenye kutia ndani desturi za kidini za kujinyima mno, uwasiliani-roho na ushirikina wa kuabudu sanamu, na mambo haya, yakiwa pamoja na kujiepusha kwa Wayahudi na vyakula na mwadhimisho wa siku, huenda yalishawishi watu fulani katika kundi. Hata kama tatizo lilikuwa nini, yaonekana lilikuwa sababu ya kutosha kumfanya Epafra afunge ile safari ndefu ya kwenda Rumi akaone Paulo. Hata hivyo, jambo la kwamba kundi lote kwa ujumla halikuwa katika hatari ya mara ile ile laonyeshwa na ripoti ya Epafra yenye kutia moyo kuhusu upendo na uthabiti wao. Aliposikia ripoti hiyo, Paulo alitokeza utetezi thabiti kuhusu maarifa sahihi na ibada safi kwa kuandika barua hii kwa kundi la Kolosai. Ilikazia kwamba ukuu ambao Kristo amepewa na Mungu kwa kulinganishwa na falsafa ya wasiomcha Mungu, ibada ya malaika, na mapokeo ya Kiyahudi.

YALIYOMO KATIKA WAKOLOSAI

6. (a) Paulo atoa sala gani kwa ajili ya Wakolosai? (b) Paulo azungumza nini kuhusu cheo na huduma ya Yesu kuhusiana na kundi?

6 Uwe na imani katika Kristo, kichwa cha kundi (1:1–2:12). Baada ya salamu za kufungua zilizotoka kwa Timotheo na yeye mwenyewe, Paulo atoa shukrani kwa sababu ya imani ambayo Wakolosai wanayo katika Kristo na kwa sababu ya upendo wao. Wamejifunza juu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu kutokana na kuhubiri kwa Epafra habari njema miongoni mwao. Tangu asikie ripoti hiyo kuwahusu, Paulo hajakoma kusali kwamba wapate kujazwa “maarifa sahihi ya penzi lake katika hekima yote na ufahamu wa kiroho, ili kutembea kwa njia yenye kumstahiki Yehova” na ‘kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu wakiwa na shangwe.’ (1:9-11, NW) Baba amewakomboa akawaingiza katika “ufalme wa Mwana wa upendo wake,” aliye mfano wa Mungu asiyeonekana, na ambaye vitu vyote vimeumbwa kupitia yeye na kwa ajili yake. Yeye ndiye Kichwa cha kundi na mzaliwa wa kwanza kutoka kwa wafu. Kupitia damu ya Yesu, Mungu aliona ni vema kupatanisha tena vitu vyote kwake mwenyewe, ndiyo, kutia na Wakolosai waliokuwa wametengwa kando wakati mmoja, ‘mradi, bila shaka, wao waendelea katika imani.’—1:13, 23, NW.

7. Paulo ahubiri nini, na kwa kusudi gani?

7 Paulo ashangilia kujazia miteseko ya Kristo kwa ajili ya kundi, ambalo yeye alipata kuwa mhudumu walo. Hii ilikuwa ili kuhubiri kikamili kwa masilahi (faida) yao neno la Mungu kuhusu ‘ile siri takatifu, mali tukufu ambazo sasa Mungu amefurahia kujulisha watakatifu wake.’ ‘Ni Kristo ambaye sisi twafanya ajulikane peupe,’ asema Paulo, ‘tukishauri na kufundisha kwa hekima yote, kwamba tupate kutokeza kila mtu kamili katika muungano pamoja na Kristo.’—1:26-28, NW.

8. Kwa nini Paulo ajitahidi sana kwa ajili ya ndugu zake?

8 Jitihada za Paulo kwa ajili ya Wakolosai, Walaodikia, na wengine ni kwa kusudi la kwamba wapate kufarijiwa na kuungwa pamoja katika upendo kwa upatano, ili wapate “kujua kabisa siri [takatifu, NW] ya Mungu, yaani, Kristo; ambaye ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika.” Yeye hataki kuwaona wakidanganywa na hoja zenye kusihi sana, bali wapaswa kuendelea kutembea katika muungano pamoja na Kristo, wakiwa ‘wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; wamefanywa imara kwa imani.’ ‘Sasa Paulo atoa onyo. “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu.’—2:2, 3, 7, 8.

9. Paulo aonya juu ya ibada ya aina gani, na kwa nini Wakolosai hawapaswi kujitiisha kwenye ile Sheria?

9 Uwe mfu kwa kazi za mwili, lakini hai kwa Kristo (2:13–3:17). Ingawa wao walikuwa wafu katika makosa yao na katika kutotahiriwa, Mungu amewafanya hai pamoja na Kristo, akifutilia mbali ile hati iliyoandikwa ya Sheria, ambayo ilishtaki Wayahudi. ‘Kwa hiyo mtu yeyote asiwahukumu’ kwa habari ya Sheria au miadhimisho yayo, ambayo ni kivuli tu cha yule aliye uhalisi, Kristo. Pia, kama wao wamekufa pamoja na Kristo kuelekea mambo ya msingi ya ulimwengu, mbona wao wajitiisha kwenye yale maagizo: “Msishike, wala msionje, wala msiguse,” kulingana na amri na mafundisho ya wanadamu? Namna ya ibada ambayo mtu ajitwika mwenyewe kwa njia ya kujionyesha, kuwa na unyenyekevu wa kujifanya tu, kutenda mwili vikali sana—mambo haya hayana thamani yoyote katika kupambana na tamaa za mwili.—2:16, 21, NW.

10. Mtu aweza kuendeleaje kutafuta mambo yaliyo juu na kuvikwa ule “utu mpya”?

10 Badala ya hivyo, Paulo ashauri hivi: “Endeleeni kutafuta mambo yaliyo juu, ambako Kristo ameketi kwenye mkono wa kulia wa Mungu. Endelezeni akili zenu zikiwa zimekazwa juu ya mambo yaliyo juu, si juu ya mambo yaliyo duniani.” Hili laweza kufanywa kwa kuvulia mbali utu wa zamani na kuvaa utu mpya, ambao kupitia maarifa sahihi haufanyi tofauti yoyote ya kimwili kati ya Myahudi na Mgiriki, kwa kuwa “Kristo ni mambo yote na katika wote.” Yamaanisha kuvikwa nguo za shauku nyororo za huruma, fadhili, udhalili wa akili, upole, na ustahimilivu “kama wachaguliwa wa Mungu.” Mtume asema hivi: “Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, nyinyi pia fanyeni hivyo. Lakini, zaidi ya mambo yote haya, jivikeni wenyewe upendo, kwa maana ni kifungo kikamilifu cha muungano.” Katika neno au katika kazi, kila jambo lapasa kufanywa “katika jina la Bwana Yesu, kupitia yeye tukishukuru Mungu aliye Baba.”—3:1, 2, 11-14, 17, NW.

11. (a) Ni shauri gani ambalo latolewa kuhusu familia na mahusiano mengine? (b) Ni salamu gani ambazo zapelekwa kwa kumalizia?

11 Mahusiano na wengine (3:18–4:18). Kwa habari ya mahusiano ya kifamilia, acheni wake wawe wenye ujitiisho kwa waume na acheni waume wapende wake zao, acheni watoto watii wazazi na acheni akina baba wasichokoze watoto wao. Watumwa wapaswa kuwa watiifu kwa mabwana-wakubwa wao katika kuhofu Yehova, na mabwana-wakubwa wapaswa kushughulika na watumwa wao kwa uadilifu. Acheni wote wadumu katika sala na kuendelea kutembea kwa hekima kuelekea wale walioko nje. Tikiko na Onesimo watawasimulia kibinafsi mambo yanayohusu Paulo na wafanya kazi wenzake kwa ajili ya Ufalme wa Mungu. Wao wapeleka salamu Kolosai, na Paulo pia awasalimu akina ndugu kule Laodikia, akiomba kwamba wabadilishane barua anazowapelekea. Paulo aandika salamu ya kumalizia kwa mkono wake mwenyewe: “Endeleeni kuzingatia akilini vifungo vyangu gerezani. Fadhili zisizostahiliwa na ziwe pamoja nanyi.”—4:18, NW.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

12. Ni kweli gani zenye kuburudisha zilizotolewa na barua ya Paulo kwa Wakolosai, na kukiwa na mafaa gani kwa kundi?

12 Twaweza kuwazia jinsi habari za kuwasili kwa ndugu hao wawili kutoka Rumi zilivyosambaa miongoni mwa ndugu kule Kolosai. Kwa taraja lenye hamu nyingi wangekusanyika, yawezekana kwenye nyumba ya Filemoni, ili wasikie kusomwa kwa barua ya Paulo. (Flm. 2) Jinsi ilivyotoa kweli zenye kuburudisha juu ya cheo kamili cha Kristo na uhitaji wa maarifa sahihi! Jinsi falsafa za binadamu na mapokeo ya Kiyahudi yalivyorudishwa mahali payo kwa uwazi, na amani na neno la Kristo vikakwezwa! Hapa palikuwa chakula kwa akili na moyo kwa ajili ya wote kundini—waangalizi, waume, wake, akina baba, watoto, mabwana-wakubwa, watumwa. Hakika kulikuwako ushauri mzuri kwa ajili ya Filemoni na Onesimo walipoingia tena kwenye uhusiano wa bwana-mkubwa na mtumwa. Jinsi uongozi mzuri ulivyotolewa kwa waangalizi katika kurudisha kundi kwenye fundisho la haki! Jinsi maneno ya Paulo yalivyoongezea uthamini wa Wakolosai kwa ajili ya pendeleo la kufanya kazi kwa nafsi yote kama kwamba kwa Yehova! Na shauri lenye kujenga kwa Wakolosai juu ya kujiweka huru na mawazo na mazoea yenye kuingiza utumwani wa ulimwengu labaki likiwa ujumbe ulio hai kwa ajili ya kundi leo.—Kol. 1:9-11, 17, 18; 2:8; 3:15, 16, 18-25; 4:1.

13. Paulo atoa onyo gani la upole kwa habari ya maneno yenye neema, sala, na ushirika wa Kikristo?

13 Ushauri bora sana kwa ajili ya mhudumu Mkristo watolewa kwenye Wakolosai 4:6: “Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.” Maneno yenye neema ya ukweli yatathibitika kuwa yenye kutia hamu kwa watu wenye mioyo yenye utafutaji haki na yatawaletea mafaa ya kudumu. Pia, sala ya Mkristo aliye macho sana, yenye kusemwa kutoka kwa moyo wenye uthamini, italeta baraka tele kutoka kwa Yehova: “Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani.” Na lo! jinsi shangwe na burudisho lenye kujenga vinavyopatikana katika ushirika wa Kikristo! ‘[Endeleeni, NW] kufundishana na kuonyana,’ asema Paulo, ‘mkimwimbia Mungu Yehova mioyoni mwenu.’ (4:2; 3:16) Utapata mambo mengine yenye thamani ya maagizo timamu, yenye kutumika utafutapo kupitia barua kwa Wakolosai.

14. (a) Ni uhalisi gani unaokaziwa katika Wakolosai? (b) Tumaini la Ufalme lakaziwaje?

14 Kuhusu kufuata Sheria, barua hiyo yasema: “Mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.” (2:17) Uhalisi huo wa Kristo ndio unaokaziwa katika Wakolosai. Barua hiyo yarejezea mara nyingi kwenye tumaini tukufu lililohifadhiwa mbinguni kwa ajili ya wale walio katika umoja na Kristo. (1:5, 27; 3:4) Wao waweza kuwa wenye shukrani kabisa kwamba tayari Baba amekwisha wakomboa kutoka kwa mamlaka ya giza na kuwapanda katika “ufalme wa Mwana wa pendo lake.” Kwa hiyo, wamekuwa chini ya amri ya Huyo ambaye ni “mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni viti vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka.” Huyu hasa astahili kutawala katika uadilifu kwenye Ufalme wa Mungu. Kwa hiyo, ndiyo sababu Paulo ashauri kwa upole Wakristo wapakwa mafuta hivi: “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu.”—1:12-16; 3:1.

[Maelezo ya Chini]

a The New Westminster Dictionary of the Bible, 1970, ukurasa 181.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki