Dumisha Imani Katika Mungu na Kristo
Mambo Makuu Kutokana na Wakolosai
IMANI katika Yehova Mungu na Yesu Kristo ni ya muhimu kwa wokovu. Lakini kudumisha imani kwataka jitihada. Ndivyo ilivyokuwa kwa Wakristo katika Kolosai, jiji moja la mashariki ya Efeso katika Esia Ndogo. Kwa nini? Kwa sababu walimu bandia huko walishikilia kimakosa kwamba wokovu ulitegemea tohara, chakula alichokula mtu, na kushika miadhimisho fulani.
Basi, yaeleweka ni kwa nini mtume Paulo alihangaikia hali njema ya kiroho ya Wakristo wa Kolosai, na kwa uhakika alitaka wadumishe imani yao katika Mungu na Kristo. Hivyo basi kuelekea mwisho wa kifungo-gereza cha kwanza cha mtume katika Roma (60-61 W.K. hivi), yeye aliwaandikia Wakolosai barua iliyokusudiwa kukinza maoni yenye makosa na kujenga imani yao. Acheni tuone jinsi sisi pia twaweza kunufaika na maneno yake yenye upendo.
Thamini Cheo cha Kristo
Mapema katika barua yake, Paulo alikazia uthamini kwa cheo cha Yesu. (1:1-2:12) Aliwapongeza Wakolosai kwa imani yao kuhusiana na Kristo na upendo wao kwa waamini wenzao. Paulo alitaja umaana mkubwa zaidi wa Kristo kuwa ndiye Mmoja ambaye vitu vingine vyote viliumbwa kupitia kwake, aliye Kichwa cha kundi, na mzaliwa wa kwanza kutoka kwa wafu. Upatanisho pamoja na Mungu hutekelezwa kupitia Kristo, ambaye ndani yake zimesitiriwa (zimefichwa) hazina zote za hekima na maarifa. Kwa sababu ya yote haya, Wakristo wapaswa kuendelea kutembea katika mwungano pamoja na Kristo na wasiache mtu yeyote awachukue kama windo kupitia falsafa ya kibinadamu.
Kupitia Kristo, Mungu aliiondoa Sheria. (2:13-23) Kwa njia ya kitamathali ilipigiliwa misumari kwenye mti ambao Yesu alikufa juu yayo. Matakwa ya Sheria yalikuwa “kivuli cha mambo yajayo; bali mwili (uhalisi, NW) ni wa Kristo.” Kwa kumshika sana Kristo, wao hawangeacha binadamu yeyote awakoseshe ile zawadi ya uhai usiokufa katika mbingu.
Thamini Mungu na Kristo
Halafu Paulo alihimiza Wakolosai wavae utu mpya na kujitiisha kwenye mamlaka ya Yesu Kristo. (3:1-17) Kwa kuweka akili zao juu ya mambo yaliyo juu, wangekuwa wakitanguliza masilahi ya kiroho maishani. Hii ilitaka kuondolea mbali mitazamo na usemi wenye makosa. Wangekuwa wabarikiwa kama nini kama wangejivika sifa kama huruma, udhalili wa akili, na upendo! Amani ya Kristo ingedhibiti ndani ya mioyo yao ikiwa wangefanya kila jambo kwa jina la Yesu, wakimshukuru Mungu kupitia yeye.
Uthamini kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo wapasa pia kuongoza mahusiano ya Mkristo na wengine. (3:18-4:18) Wake, waume, watoto, watumwa, na mabwana-wakubwa walipaswa kutimiza wajibu wao mbalimbali kwa kuhofu Mungu na kwa kumtambua Kristo. Na yahitajiwa kama nini kudumu katika sala na kutembea katika hekima!
Barua ya Paulo kwa Wakolosai yaweza kutusaidia tuepuke mafundisho bandia ambayo yangetunyima zawadi ya uhai. Mkazo wa mtume juu ya kutambua mamlaka ya Yehova na Mwana wake yaweza kuwa na uvutano mzuri juu ya mishughuliko yetu na wengine. Nasi twahakikishiwa baraka nyingi tukidumisha imani yetu katika Mungu na Kristo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]
Barua kwa Laodikia: “Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu,” Paulo akawaandikia Wakolosai, “fanyeni kwamba usomwe katika kanisa [kundi, NW] la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi.” (Wakolosai 4:16) Laodikia lilikuwa jiji tajiri katika magharibi mwa Esia Ndogo, lenye kuunganishwa kwa barabara na majiji kama Filadelfia na Efeso. Yaelekea kwamba kazi ya Paulo huko Efeso ilifika mbali hadi Laodikia, ingawa hakuhudumu huko. Yeye alipeleka barua kwa Wakristo Walaodikia, ingawa wanachuo fulani huamini kwamba hiyo ilikuwa nakala ya ile aliyowaandikia Waefeso. Barua kwa Walaodikia haipatikani katika Biblia, yawezekana kwa sababu haikuwa na habari ambazo twazihitaji leo, au labda ilirudia mambo yaliyozungumzwa kwa utoshelevu katika barua nyingine za kikanoni.
[Picha]
Mabomoko huko Laodikia