Saidia Wengine Watembee kwa Kumstahili Yehova
‘Sisi hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kutembea kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema.’—WAKOLOSAI 1:9, 10.
1, 2. Ni nini hasa kiwezacho kuwa chanzo cha shangwe na uradhi?
“TUNAISHI katika trela kwenye shamba fulani. Kwa kuishi maisha sahili, tuna wakati mwingi zaidi wa kuwahubiria watu habari njema. Tumebarikiwa sana kwa pendeleo la kuwasaidia wengi wajiweke wakfu kwa Yehova.”—Mume na mke ambao ni wahudumu wa wakati wote nchini Afrika Kusini.
2 Je, hukubali kwamba kusaidia wengine huleta shangwe? Wengine hujitahidi kwa ukawaida kuwasaidia wagonjwa, wenye uhitaji, au wapweke—wakipata uradhi kwa kufanya hivyo. Wakristo wa kweli wana hakika kwamba kushiriki na wengine ujuzi juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo ndio msaada mkubwa wawezao kutoa. Huo tu ndio uwezao kufanya wengine wakubali fidia ya Yesu, wasitawishe uhusiano mzuri pamoja na Mungu, kisha wastahili kupata uhai udumuo milele.—Matendo 3:19-21; 13:48.
3. Ni msaada wa aina gani ambao yafaa tuzingatie?
3 Hata hivyo, namna gani kuwasaidia watu ambao tayari wanamtumikia Mungu, wanaofuata “Ile Njia”? (Matendo 19:9) Hapana shaka kwamba unapendezwa nao sana, lakini huenda usijue jinsi unavyoweza kufanya mengi zaidi au kuzidisha msaada unaoendelea kuwapa. Au huenda hali yako ikakuzuia usiweze kuwasaidia, hivyo kupunguza uradhi uwezao kupata. (Matendo 20:35) Tunaweza kujifunza kuhusu hali hizo mbili katika kitabu cha Wakolosai.
4. (a) Paulo aliwaandikia Wakolosai akiwa chini ya hali gani? (b) Epafrasi alihusikaje?
4 Mtume Paulo alipowaandikia Wakristo wa Kolosai, alikuwa Roma ambako alikuwa amezuiliwa nyumbani, japo angeweza kutembelewa. Kama uwezavyo kutarajia, Paulo alitumia uhuru wake mdogo kuhubiri Ufalme wa Mungu. (Matendo 28:16-31) Paulo angeweza kutembelewa na Wakristo wenzake, labda mara nyingine hata baadhi yao wakiwa wamezuiliwa pamoja naye. (Wakolosai 1:7, 8; 4:10) Mmoja wao alikuwa Epafrasi, mweneza-evanjeli mwenye bidii kutoka jiji la Kolosai huko Frigia, katika nchi tambarare mashariki ya Efeso katika Asia Ndogo (ambayo sasa ni Uturuki). Epafrasi alihusika sana katika kufanyizwa kwa kutaniko huko Kolosai, naye alifanya kazi nyingi kwa ajili ya makutaniko katika maeneo ya karibu ya Laodikia na Hierapolisi. (Wakolosai 4:12, 13) Kwa nini Epafrasi alisafiri kumwona Paulo huko Roma, na twaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Paulo alivyoitikia?
Msaada Wenye Matokeo kwa Wakolosai
5. Kwa nini Paulo aliandika yale aliyowaandikia Wakolosai?
5 Ili kushauriana na Paulo kuhusu hali katika kutaniko la Kolosai, Epafrasi alifunga safari yenye kuchosha kwenda Roma. Aliripoti juu ya imani, upendo, na jitihada za Wakristo hao za kueneza evanjeli. (Wakolosai 1:4-8) Lakini ni lazima pia awe alizungumzia hangaiko lake kuhusu uvutano usiofaa uliotisha hali ya kiroho ya Wakolosai. Paulo aliitikia kwa barua iliyopuliziwa ambayo ilipinga baadhi ya maoni ambayo kwamba walimu wasio wa kweli walikuwa wanaeneza. Alikazia fikira hasa fungu muhimu ambalo Yesu Kristo apaswa kutimiza.a Je, alisaidia tu kwa kukazia kweli muhimu za Biblia? Angeweza kuwasaidia Wakolosai katika njia gani nyingine, nasi twaweza kujifunza nini kuhusu kuwasaidia wengine?
6. Paulo alikazia nini katika barua yake kwa Wakolosai?
6 Mwanzoni mwa barua yake, Paulo alitoa ufahamu wenye kina juu ya aina fulani ya msaada ambayo huenda tusiitilie maanani. Hiyo ilikuwa njia ya kutoa msaada wenye matokeo kutoka mbali, kwa kuwa Paulo na Epafrasi walikuwa mbali sana na Kolosai. Paulo alisema kwa hakika hivi: “Sikuzote twamshukuru Mungu Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo tusalipo [kielezi-chini, “tukisali sikuzote”] kwa ajili yenu.” Naam, hizo zilikuwa sala hususa kwa ajili ya Wakristo wa Kolosai. Paulo aliendelea kusema: “Hiyo ndiyo sababu pia sisi, tangu siku tuliposikia juu ya hilo, hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho.”—Wakolosai 1:3, 9.
7, 8. Mara nyingi sala zetu za kibinafsi na za kutaniko hutia ndani jambo gani?
7 Tunajua kwamba Yehova ni “Msikiaji wa sala,” kwa hiyo tunaweza kutumaini utayari wake wa kusikiliza sala zetu zinazotolewa kupatana na mapenzi yake. (Zaburi 65:2, NW; 86:6; Mithali 15:8, 29; 1 Yohana 5:14) Hata hivyo, sala zetu zinakuwaje tunaposali kwa ajili ya wengine?
8 Huenda mara nyingi tukafikiri na kusali kuhusu ‘ushirika mzima wa ndugu zetu katika ulimwengu.’ (1 Petro 5:9) Au huenda tukasali kwa Yehova kuhusu Wakristo na wengineo katika eneo lililokumbwa na maafa au msiba. Wakati Wakristo wa karne ya kwanza sehemu nyinginezo waliposikia juu ya njaa kuu iliyokuwa Yudea, hapana shaka walisali sana kwa ajili ya ndugu zao hata kabla ya kupeleka fedha za msaada. (Matendo 11:27-30) Leo, mara nyingi sala kuhusu udugu mzima au kuhusu kikundi kikubwa cha akina ndugu hutolewa katika mikutano ya Kikristo, ambapo wengi wanahitaji kuzielewa ili waweze kusema “Ameni.”—1 Wakorintho 14:16.
Taja Mambo Kihususa Katika Sala
9, 10. (a) Ni vielelezo gani vinavyoonyesha kwamba inafaa kusali kuhusu watu hususa? (b) Sala ilitolewaje kihususa kwa ajili ya Paulo?
9 Lakini Biblia inatoa vielelezo vya sala kwa ajili ya wengine ambazo zilikuwa hususa zaidi, zikitaja watu kibinafsi. Fikiria maelezo ya Yesu kwenye Luka 22:31, 32. Alikuwa amezungukwa na mitume 11 waaminifu. Wote wangehitaji utegemezo wa Mungu katika nyakati ngumu zilizokuwa mbele, na Yesu alisali kwa ajili yao. (Yohana 17:9-14) Hata hivyo, Yesu alimtaja Petro kibinafsi, akiomba dua hususa kwa ajili ya mwanafunzi huyo. Vielelezo vingine: Elisha alisali kwamba Mungu amsaidie mtu mmoja hususa, mhudumu wake. (2 Wafalme 6:15-17) Mtume Yohana alisali kwamba Gayo aendelee vizuri kimwili na kiroho. (3 Yohana 1, 2) Na sala nyingine zilikazia fikira vikundi fulani hususa.—Ayubu 42:7, 8; Luka 6:28; Matendo 7:60; 1 Timotheo 2:1, 2.
10 Barua za Paulo zakazia sala ambazo ni hususa sana. Aliomba kwamba sala itolewe kwa ajili yake au kwa ajili yake na wenzake. Andiko la Wakolosai 4:2, 3 lasema: “Iweni mkidumu katika sala, mkibaki macho katika hiyo pamoja na utoaji-shukrani, wakati huohuo mkisali pia kwa ajili yetu, ili Mungu apate kutufungulia mlango wa kutamka, kusema siri takatifu juu ya Kristo, ambayo kwa ajili yayo, kwa kweli, mimi nimo katika vifungo vya gereza.” Fikiria pia hivi vielelezo vingine: Waroma 15:30; 1 Wathesalonike 5:25; 2 Wathesalonike 3:1; Waebrania 13:18.
11. Epafrasi alikuwa anasali kwa ajili ya akina nani alipokuwa Roma?
11 Hali ilikuwa hivyo pia kuhusu mwenzi wa Paulo huko Roma. “Epafrasi, ambaye ni kutoka miongoni mwenu, . . . awapelekea nyinyi salamu zake, akijikakamua mwenyewe sikuzote kwa ajili yenu katika sala zake.” (Wakolosai 4:12) Neno linalotafsiriwa “kujikakamua” laweza kumaanisha “kujitahidi sana,” kama vile mwanasarakasi katika michezo ya kale. Je, Epafrasi alikuwa anasali kwa bidii kuhusu waamini wa ulimwenguni pote tu au kuhusu waabudu wa kweli katika Asia Ndogo yote? Paulo alionyesha kwamba Epafrasi alikuwa anasali kihususa kuhusu wale waliokuwa Kolosai. Epafrasi alijua hali yao. Hatuwajui wote kwa majina, wala hatujui matatizo waliyokabili, lakini hebu wazia matatizo ambayo yawezekana walikabili. Labda kijana Lino alikuwa anapambana na uvutano wa falsafa zilizoenea, na huenda Rufo alihitaji nguvu za kukinza uvutano wa mazoea yake ya zamani katika Dini ya Wayahudi. Kwa kuwa Persisi alikuwa na mume asiyeamini, je alihitaji uvumilivu na pia hekima ya kulea watoto wake katika Bwana, na je, Asinkrito, aliyekuwa na ugonjwa wa kufisha, alihitaji kufarijiwa zaidi? Naam, Epafrasi alijua wale waliokuwa katika kutaniko lake la nyumbani, naye alisali kwa bidii kuwahusu kwa sababu yeye na vilevile Paulo walitaka watu hao wenye kujitoa watembee kwa kumstahili Yehova.
12. Tunawezaje kutaja mambo kihususa zaidi katika sala zetu za faragha?
12 Je, unaona kiolezo tulichowekewa ili tuweze kuwasaidia wengine? Kama ilivyotajwa, sala kwa ajili ya watu wote kwenye mikutano ya Kikristo hutia ndani mambo mengi, kwa kuzingatia wasikilizaji mbalimbali. Lakini tunaweza kuwa hususa sana katika sala zetu za kibinafsi au za familia. Ingawa tunaweza kumwomba Mungu awaongoze na kuwabariki waangalizi wote wasafirio au wachungaji wa kiroho, je, wakati mwingine hatuwezi kutaja mambo kihususa? Kwa mfano, kwa nini usitaje katika sala yako jina la mwangalizi wa mzunguko anayezuru kutaniko lako au kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko? Andiko la Wafilipi 2:25-28 na 1 Timotheo 5:23 laonyesha kwamba Paulo alihangaikia afya ya Timotheo na Epafrodito wakiwa mtu mmoja-mmoja. Je, sisi vilevile tunaweza kuonyesha upendezi kama huo kwa wagonjwa tunaojua kwa majina?
13. Ni hali za aina gani ambazo yafaa tutaje katika sala zetu za kibinafsi?
13 Ni kweli kwamba yatupasa kuepuka kujiingiza katika mambo ya faragha ya wengine, lakini inafaa sala zetu zionyeshe upendezi wa kweli kwa wale tunaojua na kupenda. (1 Timotheo 5:13; 1 Petro 4:15) Huenda ndugu akawa amepoteza kazi, na hatuwezi kumpa kazi nyingine. Hata hivyo, tunaweza kumtaja kwa jina na kukazia fikira tatizo lake katika sala zetu za kibinafsi. (Zaburi 37:25; Mithali 10:3) Je, tunajua dada mseja ambaye umri wake umezidi kuongezeka bila kupata mume au watoto kwa sababu ameazimia kuolewa “katika Bwana tu”? (1 Wakorintho 7:39) Katika sala zako za faragha kwa nini usimwombe Yehova ambariki na kumsaidia aendelee kuwa mwaminifu-mshikamanifu katika utumishi wake? Ukiwa mfano mwingine, huenda wazee wawili wamemshauri ndugu aliyekosea. Kwa nini kila mmoja wao asimtaje ndugu huyo kwa jina mara kwa mara katika sala zake za faragha?
14. Sala zinazotaja mambo kihususa zinahusianaje na kuwasaidia wengine?
14 Una nafasi nyingi za kutaja katika sala zako za kibinafsi watu ambao unajua wanahitaji utegemezo wa Yehova, faraja, hekima, na roho takatifu, au yoyote ya matunda yatokanayo na roho hiyo. Kwa sababu ya umbali au hali nyinginezo, huenda ukahisi kwamba huwezi kusaidia kimwili au moja kwa moja. Lakini usisahau kusali kwa ajili ya ndugu na dada zako. Unajua kwamba wanataka kutembea kwa kumstahili Yehova, lakini huenda wakahitaji msaada wa kufanya hivyo kwa kudumu. Sala ni njia muhimu ya kuwasaidia.—Zaburi 18:2; 20:1, 2; 34:15; 46:1; 121:1-3.
Jitahidi Kuwaimarisha Wengine
15. Kwa nini tupendezwe na sehemu ya mwisho ya kitabu cha Wakolosai?
15 Bila shaka, sala ya bidii inayotaja mambo kihususa, siyo njia pekee ya kuwasaidia wengine, hasa walio karibu nawe na unaowapenda. Kitabu cha Wakolosai hudhihirisha jambo hilo. Wasomi wengi wanaamini kwamba Paulo aliongeza tu salamu za kibinafsi baada ya kutoa mwelekezo wa kimafundisho na ushauri wenye kutumika. (Wakolosai 4:7-18) Kinyume cha hilo, tumekwisha ona kwamba sehemu hii ya mwisho ya kitabu ina ushauri ufaao kuzingatiwa, na kuna mengi zaidi ya kujifunza kutoka sehemu hiyo.
16, 17. Tunaweza kusema nini kuhusu ndugu waliotajwa kwenye Wakolosai 4:10, 11?
16 Paulo aliandika: “Aristarko mateka mwenzangu awapelekea nyinyi salamu zake, na ndivyo pia Marko binamu ya Barnaba, (ambaye mlizipokea amri kuhusu yeye ili mmkaribishe iwapo aja kwenu,) na Yesu aitwaye Yustasi, hawa wakiwa ni kati ya wale waliotahiriwa. Ni hawa tu walio wafanyakazi wenzangu kwa ajili ya ufalme wa Mungu, na hawahawa wamekuwa kwangu msaada wenye kutia nguvu.”—Wakolosai 4:10, 11.
17 Katika andiko hilo Paulo alionyesha ndugu fulani ambao walistahili kukumbukwa kwa njia ya pekee. Alisema ndugu hao walikuwa miongoni mwa Wayahudi waliotahiriwa. Jijini Roma kulikuwa na Wayahudi wengi waliotahiriwa, na sasa baadhi yao walikuwa Wakristo. Hata hivyo, wale ambao Paulo alitaja walikuwa wamemsaidia. Yaelekea hawakusita kushirikiana na Wakristo wasio Wayahudi, na hapana shaka walishirikiana na Paulo kwa shangwe kuwahubiria wale Wasio Wayahudi.—Waroma 11:13; Wagalatia 1:16; 2:11-14.
18. Paulo aliwapongezaje wengine waliokuwa pamoja naye?
18 Ona maelezo ya Paulo: “Hawahawa wamekuwa kwangu msaada wenye kutia nguvu.” Alitumia neno la Kigiriki ambalo laonekana katika Biblia mara hiyo moja tu. Watafsiri wengi hulitafsiri “faraja.” Hata hivyo, kuna neno jingine la Kigiriki (pa·ra·ka·le’o) ambalo sanasana hutafsiriwa “faraja.” Paulo alitumia neno hilo mahali pengine katika barua hiihii lakini si katika Wakolosai 4:11.—Mathayo 5:4; Matendo 4:36; 9:31; 2 Wakorintho 1:4; Wakolosai 2:2; 4:8.
19, 20. (a) Usemi ambao Paulo alitumia kwa ndugu waliomsaidia huko Roma wamaanisha nini? (b) Huenda ndugu hao wakawa walimsaidia Paulo katika njia zipi?
19 Hapana shaka kwamba wale ambao Paulo alitaja walikuwa wamefanya mengi kuliko kutoa faraja kwa mdomo tu. Wakati mwingine neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “msaada wenye kutia nguvu” kwenye Wakolosai 4:11 lilitumiwa katika maandishi yasiyo ya kidini kurejezea dawa ya kutuliza majonzi. Biblia New Life Version yasema: “Wamekuwa msaada ulioje kwangu!” Biblia Habari Njema hutumia maneno haya: “Wamekuwa msaada mkubwa kwangu.” Huenda ndugu hao Wakristo waliokuwa karibu na Paulo wakawa walifanya nini kumsaidia?
20 Paulo angeweza kutembelewa, lakini kulikuwa na mambo mengi ambayo hangeweza kufanya, kama vile kununua vitu vya lazima alivyohitaji—chakula na nguo kwa ajili ya majira ya baridi kali. Angewezaje kununua hatikunjo kwa ajili ya kujifunza au kununua vifaa vya kuandikia? (2 Timotheo 4:13) Je, huwezi kuwazia ndugu hao wakimsaidia Paulo kuhusiana na mahitaji yake, wakifanya mambo ya kawaida kama kumnunulia vitu au kutumwa naye kwenda hapa na pale? Huenda alihitaji kuchunguza hali ya kutaniko fulani na kulitia moyo. Kwa kuwa alikuwa amezuiliwa, hangeweza kufanya hivyo, kwa hiyo huenda ndugu hao walifanya ziara kwa niaba ya Paulo, wakipeleka ujumbe mbalimbali na kurudisha ripoti. Alitiwa nguvu kama nini!
21, 22. (a) Kwa nini tupendezwe na maneno ya Wakolosai 4:11? (b) Ni katika njia zipi tunaweza kutumia kielelezo cha wale waliokuwa pamoja na Paulo?
21 Aliyoandika Paulo kuhusu kuwa “msaada wenye kutia nguvu” yatoa ufahamu wenye kina juu ya jinsi tuwezavyo kuwasaidia wengine. Huenda wakawa wanatembea kwa kumstahili Yehova kwa kupatana na viwango vyake vya maadili, wakihudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Yafaa tuwashukuru kwa mambo hayo. Hata hivyo, je, tunaweza kufanya mengi zaidi tukiwa ‘misaada yenye kutia nguvu’ kama wale waliokuwa pamoja na Paulo?
22 Ikiwa unajua dada ambaye kwa hekima alitii andiko la 1 Wakorintho 7:37 lakini ambaye sasa hana familia karibu, je, unaweza kumhusisha katika shughuli fulani za familia, labda kumwalika kula naye mlo fulani, au kuhudhuria kikusanyiko cha marafiki au watu wa jamaa? Namna gani kumwalika asafiri pamoja na familia yako kwenda kwenye mkusanyiko au likizo? Au kumwomba ajiunge nanyi wakati ufaao mnaponunua chakula. Tunaweza kuwafanyia vivyo hivyo wajane wanawake au wajane wanaume, au labda wale ambao sasa hawawezi kuendesha gari. Linaweza kuwa jambo lenye kuthawabisha kwako kusikia mambo waliyoona au kupata ujuzi kutoka kwao juu ya mambo ya kawaida kama vile kuchagua matunda au kuchagua nguo za watoto. (Mambo ya Walawi 19:32; Mithali 16:31) Matokeo yatakuwa kwamba urafiki wenu utakua. Hivyo huenda wakahisi huru zaidi kukuomba uwasaidie ikiwa wanataka dawa fulani kutoka kwa duka la dawa, au vitu vya namna hiyo. Hapana shaka ndugu waliokuwa pamoja na Paulo huko Roma walimpa msaada wenye kutumika na wenye kutia nguvu, kama vile msaada wako uwezavyo kuwa. Wakati huo na sasa kuna baraka zaidi kwa kuwa vifungo vya upendo vinaimarishwa, nasi tumeazimia kwa uthabiti kutumikia Yehova pamoja kwa uaminifu-mshikamanifu.
23. Ingefaa kila mmoja wetu atumie wakati kufanya nini?
23 Kila mmoja wetu anaweza kufikiria hali ambazo zimetajwa katika makala haya. Ni vielelezo tu, lakini vinaweza kutukumbusha hali halisi ambazo tunaweza kuzidi kuwa “msaada wenye kutia nguvu” kwa ndugu na dada zetu. Hoja si kwamba tuige mtazamo wa wafadhili. Ndugu ambao wametajwa kwenye Wakolosai 4:10, 11 hawakuwa na lengo kama hilo. Walikuwa ‘wafanyakazi wenzi kwa ajili ya ufalme wa Mungu.’ Matokeo yenye kutia nguvu yalihusiana moja kwa moja na jambo hilo. Na tufanye vivyo hivyo.
24. Ni nini maana hasa ya kusali kwa ajili ya wengine na kujitahidi kuwatia nguvu?
24 Tunataja wengine kwa majina katika sala zetu za faragha na kujitahidi kuwatia nguvu kwa sababu hii: Twaamini kwamba ndugu na dada zetu wanataka ‘kutembea kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili.’ (Wakolosai 1:10) Jambo hilo lahusiana na jingine ambalo Paulo alitaja alipoandika juu ya sala za Epafrasi kuhusu Wakolosai, kwamba wapate ‘kusimama wakiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu.’ (Wakolosai 4:12) Tunaweza kutimizaje jambo hilo sisi binafsi? Hebu tuone.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Insight on the Scriptures, Buku la Kwanza, ukurasa wa 490-491, na “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” ukurasa wa 226-228, vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Je, Ulifahamu?
• Tunawezaje kuwa wenye kusaidia zaidi katika sala zetu za faragha?
• Ni katika maana gani Wakristo fulani walikuwa ‘misaada yenye kutia nguvu’ kwa Paulo?
• Tunaweza kuwa ‘misaada yenye kutia nguvu’ katika hali zipi?
• Lengo letu ni nini tunaposali kwa ajili ya ndugu na dada zetu na kujitahidi kuwatia nguvu?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Je, unaweza kumhusisha Mkristo mwingine katika matembezi ya familia yako?
[Hisani]
Courtesy of Green Chimney’s Farm