Daraka Bora Mno la Kristo Yesu Katika Makusudi ya Mungu
KWA Wakristo wa karne ya kwanza katika Korintho, Ugiriki, mtume Paulo aliyeongozwa na roho ya Mungu aliandika: “Kwa maana bila ya kujali ahadi za Mungu ni ngapi, zimekuwa Ndiye katika yeye [Kristo Yesu]. Kwa hiyo pia kupitia kwake yeye ‘Amina’ yasemwa kwa Mungu.”—2 Kor. 1:20, NW.
Ni kwa njia gani ahadi zote za Mungu zinakuwa “Ndiyo” katika Kristo Yesu na kwamba “kupitia kwake yeye ‘Amina’ yasemwa kwa Mungu”? Jibu kwa maulizo haya latusaidia kukifahamu cheo bora ambacho Kristo Yesu anajaza katika matumizi ya Mungu ya enzi yake.
Yehova Mungu aliona yafaa kufanya Mwanawe mzaliwa wa kwanza awe aliye mkuu katika kutimilizwa kwa makusudi Yake yote. Ahadi zote za Mungu zilizoandikwa katika Maandiko Matakatifu zinakuwa “Ndiyo” kupitia kwa Kristo Yesu kwa maana ni kupitia kwake yeye—kwa namna alivyokuwa kama mtu na kwa aliyoyafanya—kwamba ahadi zote hizi zinatimia. Warumi 15:8 yatuambia kwamba, kwa taifa la Israeli, “Kristo amefanyika mhudumu . . . kwa ajili ya kweli ya Mungu, kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu [na Mungu].” Kwa njia ya Mwanawe, Mungu ameondoa sababu yo yote ya kutia mashaka akilini mwa wale wanaomtumikia Yeye na kuzitumainia ahadi Zake.
“AMINA” INAYOSEMWA KWA MUNGU
Hii ilikuwa hivyo si juu ya ahadi na unabii peke yake ambao Yesu aliutimiza wakati wa maisha yake kama mwanadamu. Vile vile alihakikisha utimizo wa ahadi za Mungu za baraka zote za wakati ujao vile vile. Kwa sababu gani Yesu aliweza kuchukua daraka hilo kubwa katika mambo? Kwa nini aliyoyafanya mnamo wakati wake wa maisha ya kidunia yalikuwa ya muhimu sana? Ni kwa sababu hii ilitokeza msingi halali kwa Yehova Mungu azitimilize ahadi hizo na kuzileta baraka zilizoahidiwa. Yehova Mungu, akiwa ni Mungu wa utakatifu, uadilifu na haki, alipanga Mwanawe atokeze msingi halali kwa kuumwaga uhai wake wa kibinadamu kama ukombozi kwa wanadamu wenye dhambi. Hii ilitokeza jambo lililohitajiwa ili Mungu ashughulike na wanadamu wasiokamilika na afute dhambi zao kwa msingi wa haki. (Linganisha Warumi 3:23-26.) Hii yamaanisha kwamba kurudishwa kwa hali za haki duniani katika taratibu mpya, ufufuo wa wafu, kuondolewa kwa dhambi na kutokukamilika na kuletwa kwa ukamilifu wa kibinadamu, afya na uzima wa milele vyote vyawezekana kwa sababu ya aliyoyafanya Yesu alipokuwa duniani.
Vile vile ni kwa sababu ya haya kwamba “kupitia kwake yeye [Kristo Yesu] ‘Amina’ yasemwa kwa Mungu.” Neno “amina” lamaanisha “kwa hakika,” “kwa kweli,” “kweli.” Mtu anayelitumia neno hili kwa njia hiyo anautangaza uhakika wa yaliyosemwa (au yatakayosemwa) naye aonyesha kwamba anaukubali na kuutegemeza moyo wote ukweli wake. Yesu Kristo wenyewe anaitwa “Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli.” (Ufu. 3:14) Ni kupitia kwake kwamba Mungu ametupa sisi thibitisho na uhakika wa kwamba ahadi Zake zote ni za kweli na lazima zitatimia. Hivyo, kwa sababu ya utu wa Yesu na kazi mna nguvu nyingi katika “Amina” tunayoisema kwa Mungu mwishoni mwa sala zetu—sala zinazofanywa ‘katika jina la Yesu.’—1 Kor. 14:16; Yohana 14:13, 14.
Ndiyo, ni vema tujiulize: Namna gani kama Mwana wa Mungu asingekuja duniani azaliwe kama mwanadamu mkamilifu, kama asingetumikia kama “Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli” kwa habari ya makusudi ya Mungu, na kama angeshindwa kuushika ukamilifu wake kwa Mungu alipokutana na mashambulio ya Shetani, asife kifo cha dhabihu juu mti wa mateso? Bila ya yeye “Amina” yetu mwishoni mwa sala zetu ingekuwa na maana gani? Ni matumaini ya kadiri gani ambayo tungekuwa nayo katika ujamaa wetu na msimamo wetu na Mungu katika kumfikia Yeye kama isingalikuwa ni kwa sababu ya dhabihu ya ukombozi aliyoitoa Kristo Yesu, ambayo kwayo dhambi zetu zinasamehewa? Tumaini letu la uzima wa milele katika taratibu mpya ya haki lingekuwa kubwa kadiri gani kama isingalikuwa ni kwa sababu Mungu “amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua [Kristo Yesu] katika wafu”?—Matendo 17:31.
UTIMILIFU WOTE WAKAA KATIKA YEYE—KWA NJIA GANI?
Lo! namna ambavyo uchaguzi alioufanya Mungu wa huyu Mwanawe mzaliwa wa kwanza ulivyokuwa kamili! Wakati uhai wa Mwana huyo ulipohamishwa kuja duniani kusudi kwamba achukuliwe mimba na kuzaliwa kama mwanadamu mkamilifu, tayari alikuwa amekwisha kuwa na kumbukumbu lisilolinganika la utumishi kwa Mungu kwa wazi likirudia nyuma kwenye mamilioni ya miaka. Kwa maana alikuwa amekuwa na Baba yake tangu mwanzo wa kuumba, yeye mwenyewe akiwa ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Kol. 1:15; Yohana 1:1, 2) Kupitia kwake kila uumbaji mwingine—viumbe vya kimalaika, mbingu zenye nyota, jua, mwezi, Dunia ya sayari, bahari, nchi, miti, mimea, maua, viumbe vya baharini, ndege, wanyama wa nchi na mtu mwenyewe—ulifanywa. Kama vile Paulo anavyoandika: “Naye amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu vyote [vilifanywa vitokee kupitia kwake] . . . Naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote. Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake, akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni.” (Kol. 1:16-20) Ni kwa njia gani kwamba ‘Mungu alipendezwa utimilifu wote ukae’ katika Kristo Yesu? “Utimilifu” huu unaopatikana katika Mwana wa Mungu ni nini?
Mtume mwenyewe analionyesha shauri hili wazi kwa kusema hivi nyumaye, “katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili.” (Kol. 2:9) Vile vile mtume Yohana anatusaidia tufahamu anapoandika kwamba “Neno [Yesu kabla hajawa mwanadamu] alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli. Kwa kuwa katika utimilifu wake sisi sote tulipokea, na neema juu ya neema. Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo.”—Yohana 1:14, 16, 17.
Ndiyo, Yesu alikuwa amejawa sana na ujuzi na sifa za kimungu za Baba yake, na vile vile tunda la roho ya Mungu, hata angeweza kusema kwamba “aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9) Lakini si hayo tu. Kwa kumfanya Yesu njia ambayo kwayo makusudi Yake yote yanatimia, yeye ambaye katika yeye unabii wote wapata maana ya kweli, Mungu amefanya ‘ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zisitirike.’ (Kol. 2:2, 3) Bila ya kujua yote ambayo Neno la Mungu laeleza juu ya Mwana huyu, hatuwezi tukapata ufahamu kamili wa Maandiko na unabii wake mbalimbali, wa mapenzi ya Mungu na makusudi.
Ni kupitia kwa Yesu ahadi za Mungu zilivyokuja kudhihirika; kwa mwendo wa maisha yake Yesu Kristo alitumiwa kufanya ahadi hizi ziwe, si maneno tu, bali uhakika. Kwa hiyo kwa kweli “katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili.” Yeye alikuwa zaidi ya mfano wenye kufananisha kitu ambacho mwishowe kitakuja. Yeye hakuwa Masihi wa mfano lakini kitu chenyewe. Yeye hakuwa kuhani mkuu wa mfano. Yeye ndiye aliyekuwa yule wa kweli aliyefananishwa, katika maana na uhakika. Kama vile mtume anavyosema juu ya mipango ya agano la Torati lililotolewa kupitia kwa Musa, “mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.” (Kol. 2:16, 17) Ndiyo, ‘katika yeye utimilifu wote unakaa’ vile vile kwa sababu Mungu amempa uwezo kamili alitimilize kusudi la kimungu. Kwa hiyo Kristo Yesu aliyefufuliwa angeweza kuwaambia wanafunzi wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mt. 28:18) Amefanywa “kichwa cha enzi yote na mamlaka” atawale kama Mfalme katika taratibu mpya ya Mungu ya haki. (Kol. 2:10) Yeye ni “Wakili Mkuu wa uzima” wa Mungu, ambaye usimamizi wake wa faida za uzima za dhabihu yake ya ukombozi ndiyo njia ya pekee iliyotolewa na Mungu kwetu tupate uzima wa milele.—Matendo 3:15, NW.
Kwa sababu ya daraka hili lililo bora ambalo Kristo Yesu analo katika kusudi la Mungu, lo! namna maneno yake yalivyokuwa kweli na yasivyotiwa chumvi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi”! (Yohana 14:6) Je! wewe umejifunza yote uwezayo juu ya Mwana wa Mungu? Je! sasa wajaribu kujipatia faida ambazo daraka lake bora laweza kukuletea? Je! wewe unampa yeye heshima inayomstahili yeye kwa kunyenyekea kabisa na kwa hiari kwa ukichwa wake katika maisha yako ya kila siku? Je! wewe unayaweka matumaini yako yote ya wakati ujao juu ya mpango wa Mungu kupitia kwake kama Wakili Mkuu wa uzima? Ufanye hivyo sasa na upokee “kutokana na utimilifu wake, hata fadhili zisizostahili juu ya fadhili zisizostahili” kutoka kwa Yehova Mungu, Baba yake Kristo Yesu.—Yohana 1:16, NW.