Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● “Wakati wa taabu” unaotajwa katika Danieli 12:1 ni nini?—U.S.A.
Andiko hili hasa linataja “wakati wa taabu” huu kwa habari ya ‘kusimama’ kwa Mikaeli.a Taabu hiyo inaelezwa wazi kuwa ambayo watu wa Mungu wataokoka. Danieli 12:1 inasema hivi: “Wakati huo [yaani, kipindi cha kushindana kati ya ‘mfalme wa kaskazini’ na ‘mfalme wa kusini’ kunakoongoza kwenye ‘wakati wa mwisho’ unaotajwa katika sura hii] Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa.”
Kitabu cha Biblia cha Ufunuo chamwonyesha Mikaeli huyu pamoja na malaika zake kama wakipiga vita yenye matokeo mazuri juu ya Shetani Ibilisi na mashetani wake. (Ufu. 12:7-9) Wanaposhindwa, tangazo linafanywa: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake.” (Ufu. 12:10) Kwa hiyo kushindwa kwa Shetani na mashetani wake kungekuwa ushuhuda wenye nguvu kwamba Mikaeli alikuwa amesimama na kutetea faida za ufalme wa Mungu uliozaliwa karibuni.
Kwa kuwa kusimama kwa Mikaeli kunatajwa kabla ya taabu, yeye na majeshi yake ya kimalaika ndio wanaoileta juu ya watu wasiomwogopa Mungu. Taabu ya pekee inayoelezwa kwa maneno yanayofanana na hayo katika Biblia ndiyo ‘dhiki kubwa’ ambayo “mkutano mkubwa” wa watumishi waaminifu wa Yehova Mungu wataokoka. (Ufu. 7:14) Bila shaka dhiki hiyo inaletwa juu ya watu wasimwogopa Mungu na majeshi ya kimalaika. Tunasoma maneno ya mtume Yohana juu ya yaliyofunuliwa kwake: “Nikaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, upepo usivume juu ya nchi, wala juu ya bahari, wala juu ya mti wo wote. Nikaona malaika mwingine, akipanda kutoka maawio ya jua, mwenye muhuri ya Mungu aliye hai; akawapigia kelele kwa sauti kuu wale malaika wanne waliopewa kuidhuru nchi na bahari, akisema, Msiidhuru nchi, wala bahari, wala miti, hata tutakapokwisha kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao.”—Ufu. 7:l-3.
Kwa hiyo wakati wa “taabu” unaozungumzwa katika unabii wa Danieli bila shaka ni sawa na ‘dhiki kubwa’ itakayoileta taratibu nzima ya mambo iliyo mbovu kwenye mwisho wake. Lakini watu waaminifu wa Mungu, ‘watiwa muhuri,’ na pia “mkutano mkubwa” wa wenzi wao, wataokoka dhiki hiyo yenye kuharibu inayokuja juu ya taratibu hii ya kidunia wakati ujao ulio karibu.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa ushuhuda unaohakikisha kwamba Mikaeli ni Yesu Kristo, tazama Aid to Bible Understanding, uk. 1152.