Kiburi Ni Hatari
JE! Unavutwa kwa watu wanaojionyesha sikuzote kuwa wenye haki? Badala yake, je! huchukizwi na wale wanaojivuna-vuna juu ya uwezo wao, mambo waliyotimiza, utajiri au cheo? Je! inakuudhi kwamba watu wengine ni wenye haraka haraka kuonyesha makosa ya wengine lakini wanakataa kukubali yao wenyewe, hata wakiudhika wakati wanapoonyeshwa kosa fulani?
Ndiyo, wonyesho huo wa kiburi unachukiza na kukasirisha. Hakuwezi kuwa na shaka kwamba kiburi kina matokeo mabaya juu ya wengine, kikibomoa badala ya kujenga. Kinaweza kuchochea uchungu na huenda mwishowe kikaharibu uhusiano mwema na wanadamu wenzako.
Kiburi ni nini hasa? Ni kujiheshimu kupita kiasi; maoni yasiyofaa ya ukuu juu ya uwezo wa mtu, hekima, uzuri, utajiri na cheo. Kwa kawaida kinajionyesha wazi kwa mwenendo wa majivuno, wa kichwa kikubwa, wa mtu kujifikiria makuu.
Kwa kuwa kiburi ni kosa la kawaida kati ya wanadamu wasiokamilika, yafaa tukizuie na kwa njia hiyo tuyaepuke madhara yake. Hii yahitaji tukuze au tuendeleze utambuzi wa moyoni juu ya uhakika wa kwamba kiburi hakina msingi ufaao. Bila kujali kabila, taifa, elimu, uwezo, mambo yaliyotimizwa au hali za uchumi, wanadamu wote ni wenye dhambi nao ni wazao wa watenda dhambi. Hiyo si sababu ya kujivuna, sivyo?
Lakini huenda mtu akasema, ‘Nimejitahidi sana nipate cheo au ukubwa ninaoufurahia sasa.’ Lakini je! hiyo yampa msingi wo wote wa kuwa mwenye kiburi? Vema, yeye alijipa mwenyewe akili ya kukuza uwezo fulani? Kama angalizaliwa akiwa na kasoro kubwa za akili au za kimwili, jitihada zake zote zingalimwezesha hata kukaribia kuyatimiza aliyoyatimiza? Sababu iliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu inatoa usawa ufaao juu ya hili. Twasoma hivi: “Ni nani anayekupambanua na mwingine? nawe una nini usichokipokea? Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea?”—1 Kor. 4:7.
Zaidi ya kujifikiria kwa kadiri inayofaa, heshima kwa cheo cha wanadamu wenzako ni ya lazima katika kuzuia kiburi. Shauri la Biblia ni: “Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.”—Flp. 2:3.
Ni vema kwa Mkristo kujua kwamba huenda waamini wenzake wakawa na sifa fulani zilizo bora. kuliko zake mwenyewe. Huenda wakawa wenye mfano mwema sana katika kuonyesha upendo, fadhili, au huruma. Huenda ikawa miaka mingi ya kujifunza Maandiko imewapa wengine ufahamu bora wa kanuni za Biblia na matumizi yake kwa maisha ya kila siku. Ijapokuwa huenda wengine wasiwe na maarifa sana, huenda wakawa walipata ujuzi wenye thamani sana maishani. Waweza kujifunza jambo fulani kwao, pia, hata ikiwa nishauri tu la kupata kujua kwamba huenda zikawako zaidi ya njia moja za kufikiria mambo. Hii itamzuia mtu asifanye kosa la kujaribu kuweka kila mtu katika hali ile ile na kuwa mshupavu katika kufanya maamuzi au kudharau mawaidha.
Mtu akimfanya mwingine ajione mdogo au hafifu kwa sababu ya kujifikiria mkuu katika maarifa, uwezo au ujuzi ni hatari. Kwa mfano, katika kundi la Kikristo huenda mtumishi wa huduma akamfikia mzee akiwa na waidha. Sasa, kwaweza kutokea nini mzee akimpuza bila ya kufikiria waidha lake ifaavyo, akionyesha kwamba mtumishi wa huduma anasema kabla zamu yake haijafika? Je! mtumishi wa huduma asingeudhika na kuhuzunika kwa sababu ameeleweka vibaya? Wakati ule ule kuonyesha kiburi, ingawa kidogo, kwaweza kushusha heshima ya mtumishi wa huduma kwa mzee. Kwa sababu ya makusudi yake kutiliwa mashaka bila sababu inayofaa, huenda mtumishi wa huduma akaazimu kwa wazi au kwa njia isiyo wazi kwamba uamuzi wa mzee kwa ujumla si bora. Kwa kuchukizwa na lililotokea, huenda akamhadithia rafiki mkubwa yote yaliyomo moyoni mwake nayo maoni ya huyo rafiki pia yaweza kuharibiwa kwa kitambo.
Mfano wa Yesu Kristo bila shaka unastahili kuigwa. Yeye hakuacha ‘ujuzi umletee majivuno.’ (1 Kor. 8:1) Ijapokuwa yeye alikuwa na majibu sahihi yote, hakuwatenga wengine kwa kukaza fikira kwenye uwezo wake mkuu zaidi, maarifa, ujuzi wala hekima. Hakuwafanya wanafunzi wake wadhani kwamba baada ya kuwaacha wasingeweza kuifanya kazi kwa kadiri ambayo alikuwa ameifanya. Bali, alionyesha matumaini kwao akawaheshimu, akiwaambia wanafunzi wake hivi: “Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” (Yohana 14:12) Na kama baraza, wanafunzi wa Yesu Kristo walifanya kazi za kadiri kubwa kuliko alizokuwa amefanya nao walizifanya kwa kipindi kirefu zaidi.—Linganisha Mathayo 5:14.
Sasa, ikiwa Yesu kama mwanadamu mkamilifu angeweza kusema matumaini hayo juu ya waamini, sababu gani mwanadamu ye yote asiyekamilika aazimu kwamba wengine hawawezi kabisa kufanya awezavyo? Mtu anayeonyesha kuwaza huko kwenye kiburi anajitatanisha mwenyewe na wengine. Anavunja wengine moyo wasitake kufanya kazi naye kwa sababu wanafanywa wajione kuwa hafifu na wasiostahili kutumainiwa. Kama matokeo, wananyimwa kadiri fulani ya kupendezwa kwa kipekee.
Walakini, “roho” ya kiburi yenye nguvu ni hatari hata zaidi. Yawafanya wale walio nayo wachukie kuonyeshwa makosa ipasavyo, wakatae kusahihishwa au kutiwa adabu, kwa kweli, wayakatae mashauri ya Neno la Mungu. Hii inawafanya wafuate njia ya maisha ambayo bila shaka itawaletea uharibifu wenyewe. Mithali ya Biblia yasema vyema: “Aonywaye mara nyingi akishupaza shingo, atavunjika ghafula, wala hapati dawa.” (Mit. 29:1) Hivi ndivyo ilivyo kwa maana mtu mwenye kiburi chenye nguvu anajiweka katika hali ya kumpinga Mungu na yale ambayo Yeye anatazamia kwa wale ambao Yeye anawakubali kama watumishi Wake. Kama vile Biblia isemavyo: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.”—1 Pet. 5:5.
Kwa hiyo, ni lazima kwa Wakristo kujitahidi wazuie kiburi. Si kwamba tu mtu mwenye kiburi aweza kudhuru wengine, bali huenda yeye pia akapoteza kibali ya Mungu na uzima. Kwa kweli kiburi ni hatari.