Je! Wewe Unaambilika Kweli?
YEHOVA Mungu anathamini sana kuambilika kwa upande wa wale wanaomtumikia yeye. Imetupasa tutazamie hili. Kwa maana Mungu mwenyewe ameweka mfano bora sana wa kuambilika, akiwa mwenye kufikika kwa sala ya watu wa namna zote, nyakati zote, chini ya namna zote za hali.—Zab. 65:2.
Ushuhuda wa kwamba Mungu anathamini sana kuambilika waonekana kwa kumtuma Mwanawe duniani na kumfanya aishi chini ya hali za vivi hivi. Kwa kusudi gani? Kati ya mambo mengine, ili Mwanawe, Yesu Kristo, “apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu,” si “asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote.” Kwa sababu yake, Wakristo wanaweza ‘kukikaribia kiti [cha Mungu] cha neema kwa ujasiri,’ na kwa hakika. (Ebr. 2:17, 18; 4:15, 16; 10:19, 21, 22) Yehova Mungu ataka iwe hivyo.
Leo, watu kwa ujumla wanatengana kidogo kidogo; mawasiliano—kati ya washiriki wa jamaa, kati ya wale wenye mamlaka na wale wanaopaswa kutii mamlaka—yanaharibika kidogo kidogo. Hii imepaswa itufanye tuuthamini zaidi sana uhitaji wa lazima wa kuwa wenye kuambilika. Hatuwezi kuacha hali hizo zisizofaa za kilimwengu ziingie kidogo kidogo katika kundi la Kikristo na kuidhoofisha roho ya uchangamfu na upendo wa kweli uliomo. Ni nani hasa wanaopaswa kuwa macho, nao wanawezaje kujilinda na hatari hiyo?
Waume wa Kikristo, wanaopaswa ‘kupenda wake zao kama nafsi zao wenyewe,’ wamepaswa wailinde sifa hii. Wazazi pia wanapaswa wadumishe kuambilika na watoto wao ikiwa hawataki ‘wakate tamaa.’ Na, katika kila kundi la Kikristo, wazee (waangalizi) wamepaswa wajihakikishe kuwa wenye kuambilika kweli kweli katika shughuli zao na ndugu na dada zao wote.—Efe. 5:28, 33; Kol. 3:19, 21; 1 Pet. 5:1, 3.
KUJIHAKIKISHA WENYEWE KUWA WENYE KUAMBILIKA
Jawabu la kuwa wenye kuambilika ni kupendezwa na wengine kwa unyofu na kweli. Haitoshi kusema kwamba tunaambilika, kwamba tuna mpango wa ukaribishaji mwema. Kama vile isemavyo mithali: “Wanadamu hutangaza kila mtu hisani yake mwenyewe.” Lakini maneno hayatoshi. Lazima tuonyeshe kwamba tunaambilika kweli kwa namna ambavyo twashughulika na wengine. (Mit. 20:6; 1 Yohana 3:18) Ikiwa kweli tunajali watu na tuna nia ya kuwatumikia, wao wataona hivyo.
Mzee katika kundi ana mgawo wa roho takatifu kutumikia kama mchungaji chini ya Kristo Yesu. Lakini mgawo huu usimfanye ajione ni mkuu zaidi kuliko wengine, kwa maana yeye mwenyewe ni sehemu ya kundi kama mmoja wa “kondoo.” (Matendo 20:28; 1 Pet. 5:2, 4) Badala yake, imempasa ashukuru kwamba Kichwa cha kundi, Kristo Yesu, kilimhesabu kustahili kutumikia washiriki wenzake wa kundi na kwamba Mungu alimstahilisha kwa kumpa kadiri fulani ya maarifa, ufahamu na hekima. (1 Tim. 1:12; 2 Kor. 3:5) Mali hizo za kiroho ni kama hazina kutoka kwa Mungu. Badala ya kujiona bora, atakuwa mwenye furaha kwamba, kwa fadhili za Mungu zisizostahili, ana jambo la kutoa kwa faida ya ndugu zake, mashauri mema na maarifa, yote yakiwa msingi wake ni Neno la Mungu mwenyewe na yakiwa yametolewa humo. Badala ya kujiona mkubwa machoni pake mwenyewe, atajaribu kwa unyenyekevu kutumia hazina hiyo ya maarifa kumletea Yehova na Mwanawe sifa, Kichwa cha kundi.—1 Kor. 4:7; 1 Pet. 4:10, 11.
JE! UNAJIFANYA KUPATIKANA?
Kwa wazi, huwezi kuwa mwenye kuambilika ikiwa hupatikani uweze kuambiwa. Juu ya Yehova Mungu, mtume Paulo angeweza kusema, “hawi mbali na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Mtumishi wa Mungu Musa alikuwa na nia ya kuvumilia daraka lenye kuchosha la kusaidia watu na matatizo yao “tangu asubuhi hata jioni.”—Kut. 18:13-16.
Bila shaka, huenda wazee wa Kikristo wakawa na madaraka mengi ya kuangalia—huenda wakawa na jamaa zao wenyewe zinazohitaji kuangaliwa nao. Nao pia wanapendezwa na kushiriki kuzitangaza habari njema kwa waliomo katika ulimwengu wa wanadamu, kufanya wanafunzi wengi kama wawezavyo. Lakini ikiwa wanataka wawe wachungaji wema wa kundi lazima wasawazishe haya na mengine ili wajifanye kupatikana na ndugu na dada zao katika kundi wanaotafuta habari au msaada kwa maulizo ya kipekee na matatizo.
Katika mahali pa mikutano ya Kikristo mara nyingi ni shauri tu la kuacha wengine waone kwamba upo, unapatikana na una nia ya kusema. Ikiwa mtu anaonekana “mwenye shughuli nyingi” sikuzote, huenda wengi wakasita-sita kumfikia. Maandishi ya kundi yana thamani kadiri fulani, lakini haya siyo yanayoonyesha mtu ni mchungaji wa kweli wa “kondoo.” Ingekuwa afadhali kushughulika nayo baada ya “kondoo” wenyewe walio hai kuangaliwa ifaavyo.—Linganisha Mithali 27:23; Yohana 10:2-4.
Bila shaka, ni jambo jema kuchukua hatua ya kwanza katika kuonyesha kupendezwa na wengine, kuwafikia. Hii inapatana na mfano wa Mungu, kwa maana yeye hakuwangoja wanadamu wamfikie kwanza, bali alichukua hatua za kwanza mwenyewe. (Yer. 7:13, 25; 2 Kor. 5:20; 1 Yohana 4:10, 19) Walakini, hata katika hili ni lazima kuonyesha kwamba hatufuati utaratibu tu wa kuwa (au kuonekana) wenye urafiki. Kupendezwa kwetu lazima kuwe kunyofu na kwa kweli.—1 Pet. 1:22.
Je! tunasikiliza kweli mtu fulani anapotoa ulizo au tatizo? Huenda jambo hili likaonekana dogo, hata lisilo na maana, kwetu. Lakini kwa mtu anayelitoa, huenda likawa kubwa. Wazazi wengine wana hatia ya ‘kuchokoza’ watoto wao na kuwahuzunisha kwa kuwapuza au hata kuwafanyia mzaha kwa sababu ya kuleta matatizo fulani yanayoelekea kuwa madogo madogo. Imewapasa wazee wajihadhari wasifanye lili hili kwa wale wanaowatumikia kundini. Kwa maana ni wazi Yehova Mungu sivyo alivyo. Kama vile Yakobo 1:5 atuambiavyo, Yehova Mungu si “mnyiminyimi” juu ya kutupa msaada wa matatizo yetu—matatizo ambayo bila shaka yangeonekana madogo sana kulingana na maoni yake yaliyo juu sana—bali yeye atusikia na kusaidia kwa ukarimu, bila kuudhika au kutulaumu kwa kumjia tukiwa na mambo hayo.
Wakati mmoja wazazi fulani walimletea Mwana wa Mungu watoto wadogo. Wanafunzi wa Yesu walijaribu kuzuia hili, kwa wazi wakiona kwamba ‘Bwana wao alikuwa na mambo ya maana zaidi ya kuchukua wakati wake na fikira.’ Lakini Yesu aliona uchungu alipoona hivi, akawakaripia wanafunzi wake, na kuwakumbatia watoto hao na kuwapa uangalizi uliotakiwa.—Mt. 19:13, 14; Marko 10:13-16.
Kwa kweli mfano mwema ambao yeye na Baba yake walituwekea umepaswa utuvute sote tuhakikishe kwamba sisi, pia, ni wenye kuambilika kweli kweli. Tukifanya hivyo, tutaongeza roho njema katika kundi la Mungu, roho ya Kikristo kweli ya uchangamfu na matumaini, upendo na upendano wa kidugu. Tutakuwa baraka kwa wengine nasi pia tutabarikiwa sana.