Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 12/15 kur. 563-569
  • ‘Kuishi Si Tena Kwa AJili Yetu Wenyewe’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Kuishi Si Tena Kwa AJili Yetu Wenyewe’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! TU HURU KWELI, WENYE KUJITEGEMEA?
  • TOFAUTI KATI YA MABWANA
  • MTUMWA ANAFANYA MAPENZI YA NANI KWANZA?
  • KUTUMIA WAKATI WAKO “USIPOKUWA NA SHUGHULI”
  • “Mlinunuliwa Kwa Bei”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • “Mtumikieni Yehova”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Fidia
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 12/15 kur. 563-569

‘Kuishi Si Tena Kwa AJili Yetu Wenyewe’

“Maana, upendo wa Kristo watubidisha; maana . . . alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe.”​—2 Kor. 5:14, 15.

1. Watu wengi wanatendaje kwa habari ya maoni ya uhuru na utumwa?

LO! UHURU unathaminiwaje! Pande zote leo watu wanasifu uhuru na usawa. Maoni ya uhuru na kujitegemea yanaonekana sana hata wengi wanaasi kwa kutotaka waongozwe na mtu mwingine, au waishi kwa ajili ya mtu mwingine. Huenda umepata kuwasikia wakisema, ‘Nataka niishi mimi nitakavyo.’ Hawataki wawe watumwa wa mtu ye yote. Kwa watu walio wengi, neno lenyewe “mtumwa” linawakumbusha visa vya karne zilizopita wakati watu wasio na tumaini walipojitahidi wakipiga makasia katika jahazi, wakafanya kazi ngumu wakichimbua mawe au wakatumikia mapenzi ya bwana fulani mkatili.

2. Je! utumwa ni jambo lililowahusu watu wa vizazi vilivyopita tu?

2 Matokeo mabaya ya utumwa​—ya wanadamu kuwako kama mali tu ya mtu mwingine​—yanaonekana hata wakati wetu. Habari za Umoja wa Mataifa za mwaka wa 1972 zilisema kwamba ‘chanzo cha ugomvi wa kijamii katika nchi nyingi leo kinasababishwa moja kwa moja na namna mbalimbali za utumwa. Karibuni mauaji makubwa ya wanaume, wanawake na watoto yamefanywa na watu waliokuwa watumwa zamani, juu ya wale waliokuwa mabwana zao wakati mmoja.’

3. Kwa sababu gani yaweza kusemwa kwamba utumwa umeenea zaidi leo kuliko idhaniwavyo kuwa kwa kawaida?

3 Huenda ukadhani, ‘Hayo hayanihusu mimi; mimi si mtumwa.’ Walakini, mwandikaji mashuhuri aliyeuona mwenyewe utumwa wa Milki ya Kirumi alihakikisha kwamba kila mtu katika milki nzima alikuwa mtumwa kwa njia fulani. Kulingana na wazo lile lile, wanadamu wote leo ni watumwa. Mwandikaji huyo mashuhuri, mtume Paulo, hakujifikiria kama asiyehusika bali alisema hivi akiwaandikia Wakristo Rumi: “Mimi ni mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi. . . . Naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.”​—Rum. 7:14, 23.

JE! TU HURU KWELI, WENYE KUJITEGEMEA?

4, 5. Kuna ushuhuda gani kwamba sote tumetumikishwa?

4 Mtume Paulo hakumaanisha kwamba wazazi wake mwenyewe walikuwa wamemwuza katika utumwa wa dhambi kwa makusudi; wala wazazi wetu wenyewe hawakutufanyia hivyo. Lakini Paulo alifahamu kwamba, kwa kuchagua kutenda dhambi kwa makusudi, babu yetu sote, Adamu, alijiuza mwenyewe na wazao wake wote wa wakati ujao​—wanadamu wote​—katika utumwa wa kutokamilika, dhambi na mauti. (Rum. 5:12) Bila shaka hii inafikia wakati wetu na kututia sisi sote, kwa maana twaona kutuzunguka, na katika maisha zetu wenyewe, ushuhuda wa utumwa huu​—ushuhuda wa namna ya makosa, dhambi na magonjwa yenye kudhuru.

5 Na hali wako wengine leo wanaojidai kwa uhodari kuwa wana uhuru. Wengine wanatangaza uhuru wao wa kufanya ngono. Lakini je! njia yao ya maisha yaonyesha kwamba wao wako huru kweli? Ni kweli, huenda wakawa wanaishi kwa ajili yao wenyewe, wakitosheleza tamaa zao wenyewe. Lakini, hiyo inautilia mkazo uhakika wa kwamba wao ni watumwa wa kutokamilika na dhambi. Namna gani juu ya mtu ambaye pupa yake inamvuta apate pesa, mali au heshima? Yeye pia, anakua mzee zaidi na dhaifu zaidi, anapatwa na ugonjwa fulani na mwishowe anakufa. Ndivyo ilivyo hata kwa viongozi wa vyama vya “haki” za raia, za wanawake na za walio wachache. Mwisho wao ni mmoja​—kifo​—ikihakikisha kwamba wao ni watumwa kweli wa Wafalme Dhambi na Mauti.​—Rum. 5:21.

6. Kutumikishwa huku kumepaswa kuelekeze kwenye maulizo gani kwa upande wetu?

6 Je! hii maana yake ni kwamba hali ya wanadamu haina tumaini? Je! hakuna ukombozi kutoka dhambi na mauti? Na ikiwa kuna mpango wa ukombozi, je! ungali waweza kuishi kama utakavyo, au jambo fulani lahitajiwa kwako uweze kufaidika kutokana na mpango huu?

7. Mpango umefanywaje wa ukombozi kutoka utumwa huu?

7 Fundisho la msingi la Biblia ni kwamba Mungu alifanya mpango kwa rehema yake wanadamu wapate kukombolewa kutoka utumwa wa dhambi na mauti. Hii ilikuwa kwa njia ya Mwanawe wa pekee, ambaye akawa mwanadamu mkamilifu Yesu. Kupatana na kusudi la Mungu kwake, Yesu aliutoa uhai wake kama dhabihu kama “ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.” (1 Tim. 2:5, 6, NW) Ijapokuwa ukombozi au bei yake ililipwa kwa njia hiyo “kwa ajili ya wote,” si wote watakaozipata faida zake zote. Kwa sababu gani sivyo?

8. Kwa sababu gani si wanadamu wote wanaozipokea faida za ukombozi?

8 Wale wenye hali ya kukubalika mbele za Muumba peke yao ndio watakaozipata faida zote za mpango wa ukombozi​—kukombolewa milele kutoka kwa dhambi, magonjwa, uzee na mauti. Ijapokuwa wote wanakaribishwa wawe na hali yenye kukubalika, si wote wanaotaka kuukubali kwa sababu ya daraka linalohusika. Wengi hawataki watende kupatana na uhakika wa kwamba ukombozi au bei yake imelipwa kwa ajili yao. Hawataki kukubali kwamba wamenunuliwa na kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo ndio Wenyewe wao au Mabwana wao, wanaostahili utii kamili. Wote wanaoendelea kutotii au ambao baadaye wanamkana Yehova Mungu na Yesu Kristo mwishowe kama Wenyewe wao wanazikosa faida za mpango wa ukombozi.​—Mt. 10:33; Yohana 3:36; Ebr. 10:26, 27; 2 Pet. 2:1-3.

9. Wanadamu wote wamewekewa uchaguzi gani?

9 Kwa hiyo ulizo lililoko mbele ya wanadamu wote ni, Mimi nataka nimtumikie nani kwa hiari​—dhambi nikitazamia kufa, au Mungu na Kristo nikitazamia uzima? (Rum. 6:16) Huenda wengine wakasema, ‘Huo si uchaguzi wenye kufaa. Afadhali nife kuliko kuwa mtumwa milele.’ Lakini je! huko ni kuwaza kwenye busara linapokuwa shauri la kumtumikia Mungu na Kristo? Je! Yesu hakusema kwamba “kweli itawaweka huru”? (Yohana 8:32) Kwa hiyo, je! tusitazamie kwamba kumtumikia Mungu na Kristo kutaleta uhuru wa namna inayotakiwa na kila mtu mwenye moyo mnyofu? Ebu fikiri:

TOFAUTI KATI YA MABWANA

10. Wakristo wana “mabwana” wa namna gani mbinguni?

10 Kuna sababu nzuri kwa wanadamu kutaka wawe watumwa wa Mungu na Kristo. Wao si kama mabwana wakatili wa karne zilizopita waliokuwa wakali sana kwa watumwa wao wakawatumia kwa faida yao wenyewe bila kuijali hali yao njema na furaha. Yehova Mungu na Mwanawe walivyowafanyia wanadamu yashuhudia kupendezwa kwingi na upendo usio na mipaka.

11, 12. Ni kwa njia gani tulivyo na deni ya Mungu?

11 Yehova Mungu Ndiye ambaye tuna deni yake kwa ajili ya uzima. ‘Yeye aliviumba vyote, na kwa sababu ya mapenzi yake vilikuwako, navyo vikaumbwa.’ (Ufu. 4:11) Angeweza kufikiliza adhabu ya kifo juu ya Adamu na Hawa wasiotii kabla hawajaweza kuwa wazazi. Ingalikuwa hivyo hakuna mmoja kati yetu angezaliwa. Lakini, akivutwa na rehema kwa wazao wao wasiozaliwa, Yehova Mungu aliwaruhusu wanadamu wawili wa kwanza waendelee kuishi na kuzaa. Bila ya kujali hali isiyo na shukrani ya wazao wao, yeye hakuwanyima wanadamu mipango yake ya ukarimu ya kuendelezea uhai. (Mt. 5:45) Hata “wapagani” wasingeweza kupingana na maneno ya mtume Paulo kwamba Mungu “alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.”​—Matendo 14:17; Zab. 104:13-15, 24.

12 Lakini wonyesho wa Mungu wa upendo na fadhili zisizostahili haukukomea hapo. Ili wanadamu wenye dhambi na wasiostahili waweze kuchagua kuingia katika uhusiano wenye kukubaliwa naye na kukombolewa na dhambi na mauti, Mungu ‘hakumzuia’ Mwanawe mpendwa zaidi asipatwe na kifo cha aibu. (Rum. 8:32, NW) Wengi wa wanadamu wataipata nafasi ya uzima bila kifo watakapofufuliwa kutoka kwa wafu kwa sababu hiyo. (Matendo 24:15) Ebu fikiri, Yehova Mungu aliwafanyia hivi wanadamu ambao hata hawakuikubali mamlaka yake maishani mwao. Ni kama vile mtume Paulo alivyowaandikia Wakristo katika Rumi: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.”​—Rum. 5:8.

13. Kwa sababu gani tuna deni ya Yesu Kristo?

13 Kununuliwa kwa wanadamu wenye dhambi kwa “damu ya thamani” ulikuwa ushuhuda mkubwa pia wa upendo mwingi sana wa Yesu mwenyewe. (1 Pet. 1:19, 20) Kama vile Yesu mwenyewe alivyosema: “Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo. . . . Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe.” (Yohana 10:15-18) “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Kwa kweli Yesu alifanya mengi zaidi. Hakufia rafiki zake tu, bali ulimwengu wa wanadamu kwa ujumla wasiokubali kuwa na deni yo yote kwa Baba yake. (1 Yohana 2:2) Sasa, ni mtu gani ambaye angalikuwa na nia ya kufanya hivyo kwa ajili ya watu wasiomheshimu baba yake? Sisi tuna deni kweli kweli kwa Yesu Kristo kwa sababu ya kutununua akipoteza uhai wake, akituwekea wazi nafasi ya kupata uhuru wa dhambi na mauti.

14. Tutendeje kwa sababu ya deni hii?

14 Kwa sababu ya upendo mkuu wa Mungu na Kristo, je! moyo wako waamshwa utake kuwa katika utumishi wao? Je! wewe unajisikia kama watu fulani wa nyakati za kale ambao walichagua kwa hiari waendelee kuwa watumwa wa mabwana zao Waebrania wenye ukarimu, ingawa walipewa uchaguzi wa kuwa huru? (Kut. 21:2-6) Hilo ndilo itikio la moyoni la wale wanaothamini yale ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wamewafanyia. Kama vile Paulo alivyoandika, “upendo wa Kristo watubidisha.” (2 Kor. 5:14) Angalia kwamba yeye hakusema Mungu anatulazimisha au kwamba Kristo analazimisha wanadamu wawatolee utumishi wa uaminifu. Bali, nguvu yenye kulazimisha ni “upendo wa Kristo.” Na, kwa kuwa Yehova Mungu anatupenda sisi kama vile Mwanawe atupendavyo, upendo wa Mungu una nguvu ile ile yenye kulazimisha.

15. Uhusiano wa Mkristo na Yehova na Yesu Kristo ni wa namna gani?

15 Uhusiano uwezao kuingia katika huo na Mungu na Kristo, ikiwa hujafanya hivyo bado, si wa vivi hivi tu, bali ni wenye uchangamfu na wa karibu. Usiku wake wa mwisho kama mwanadamu akiwa pamoja na wanafunzi wake, Yesu aliwahakikishia hivi kwa uchangamfu: “Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 15:15) Kwa kusema hivi Yesu hakuwa akimaanisha kwamba hali yao hasa haikuwa ile ya watumwa tena, kwa maana wangali waliwiwa maisha zao na Mungu, na karibuni Kristo alipaswa awalipie “bei ya ukombozi.” Alikuwa na maana ya kwamba hakuwa akiwatendea kama watumwa tu, wale wanaopewa migawo lakini wasipewe habari zote. Sivyo, walipaswa watendewe kama “rafiki,” kama wasiri wenye kutumainika na kuheshimika.

16. Kwa sababu gani utumishi kwa Mungu na Kristo si mzigo?

16 Kwa hiyo twaona kwamba hakuna mzigo wa utumwa kwa Mungu na Kristo. Msingi wa amri zao ni upendo nazo ni za kuwalinda watiifu na madhara na kuwahakikishia furaha na hali njema ya milele. (1 Yohana 5:3) Hakuna nira ya uonezi inayowangoja wale ambao wanachagua kujikana wakivutwa na upendo ili wawe watumwa wa Mungu na Kristo. Yesu Kristo alisema, “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Akiwa na mabwana wenye upendo kama hao, ni mwanamume au mwanamke gani mwenye nia ifaayo ambaye angetaka afuate mwendo wa kujitegemea kwa kujitakia mwenyewe?

MTUMWA ANAFANYA MAPENZI YA NANI KWANZA?

17. Upendo wa Mungu na Kristo umepaswa uwe na matokeo gani juu ya namna tuishivyo?

17 Ikiwa upendo wa Mungu na Kristo unakulazimisha wewe uwatumikie, hii itaonyeshwa kwa namna unavyoishi maisha yako. Hutakuwa ukiishi kwa ajili yako mwenyewe. Kama vile mtume Paulo alivyoandika: “[Kristo] alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa . . . kwa ajili yao.” (2 Kor. 5:15) Hii hasa inatia nini ndani?

18-20. (a) Kama ilivyoonyeshwa na Yesu, ni nini kinachotangulia ikiwa mtu haishi tena kwa ajili yake mwenyewe? (b) Je! Yesu alimaanisha kwamba hatufai kitu?

18 Ufikirie uhusiano wa halisi wa mtumwa na bwana wake. Je! mtumwa mwaminifu na mwenye kuaminika aweza kuacha kumtumikia bwana wake au kuuchukua utumishi huo kama usio na maana sana? Je! aweza kufikiria raha zake mwenyewe kwanza au mapendezi ya kipekee maishani? Hasha! Basi namna gani juu ya watumwa wa Mungu na Kristo?

19 Mfano uliotumiwa na Yesu Kristo unatoa jibu lenye nguvu kwa ulizo hili. Aliuonyesha uhakika wa kwamba siku hizo watumwa waliofanya kazi mashambani waliwatayarishia pia mabwana zao chakula cha jioni. Hili lilionekana kama jambo alilolistahili bwana. Yesu alisema: “Je! [bwana] hatamwambia [mtumwa], Nifanyie tayari chakula, nile; jifunge unitumikie, hata niishe kula na kunywa, ndipo nawe utakapokula na kunywa? Je! atampa asante yule mtumwa, kwa sababu ameyafanya aliyoagizwa?” Kisha, kwa habari ya utimizo wa migawo yao, Yesu aliwashauri wanafunzi wake waseme: “Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya.”​—Luka 17:7-10.

20 Hapa Yesu hakuwa akipendekeza kwamba Wakristo wawe wakijidharau sikuzote, wakijirahisisha, wakijifikiria kama wasiofaa kitu. Sivyo, bali alikuwa akiwashauri waukumbuke sana uhusiano wao kwa Mungu na Mwanawe. Kama Wakristo, mapenzi yao na raha zao wenyewe hazitangulii, kwa maana Kristo alikufa ili “wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe.”

21. Kwa sababu gani ‘kuishi si tena kwa ajili yetu wenyewe’ ni kugumu nyakati nyingine?

21 Bila shaka, kumtumikia Mungu na Kristo si kwepesi sikuzote, lakini utumishi huo si sababu ya magumu kamwe. Wenyewe ni chanzo cha furaha na burudisho. Walakini, wanadamu wasio na imani na majeshi ya viumbe vibaya vya kiroho ndio wanaowatatiza Wakristo. (Efe. 6:11, 12; 2 The. 3:1-3) Haya ndiyo yamekuwa maono ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo nyakati za kisasa, hasa katika nchi zinazotawaliwa na watawala wenye kutumia nguvu. Mara nyingi wameteswa kwa sababu ya kuitii amri ya Yesu kulihubiri na kulifundisha Neno la Mungu. (Mt. 28:19, 20) Nyakati nyingine wamepatwa na mateso kwa sababu wanakataa kujitia katika mambo ya kisiasa na ya kijeshi ya mataifa kwa uaminifu. (Yohana 6:15; 17:16) Njia nyepesi zaidi ya kufanya mambo ingekuwa kushindwa, kuishi ‘maisha mema, ya adili,’ huku wakikubali kufanya kulingana na madai ya serikali zenye chama kimoja. Lakini Wakristo hawa hawaishi kwa ajili yao wenyewe. Wao ni watumishi wa Mungu na Kristo. Wakishukuru kwa ajili ya upendo usio na kifani walioonyeshwa, wao ni wenye nia ya kutaabika, ndiyo, hata kufa, katika utumishi wa uaminifu.

22, 23. (a) Mashahidi vijana wa Czechoslovakia walivumilia nini? (b) Ni nini kilichowawezesha waendelee kuwa waaminifu?

22 Hivyo, katika kitabu Even Under the Sky There Is Hell (1971, ukurasa 117) mwandishi wa habari wa Czechoslovakia aliyasimulia mateso ya ukatili ya mashahidi wa Yehova katika kambi ya kazi ngumu ya Wakomunisti wakati wa mwaka wa 1951: “Sikuzote mimi nitawakumbuka wafuasi wa Yehova [mashahidi wa Yehova] kwa kuwasifu na kwa utambuzi, hasa vivulana, waliokataa kutumikia jeshini wakahukumiwa kwa sababu hiyo. Hata hivyo walidumu katika imani yao . . . nao walikataa kufanya kazi katika mashimo ya madini ya uranium (madini nyeupe na nzito inayotumiwa kutengeneza silaha za atomiki). Majemadari wa kambi walitumia kila kitu walichokuwa nacho kuwalazimisha wafanye kazi, lakini lo lote walilojaribu lilikuwa kazi bure; wengi wao waliona ni afadhali kufa kuliko kufanya kazi wakiongezea tisho la Urusi la silaha za atomiki. Mkuu wa kambi Palacek aliwasimamisha mbele ya makao makuu siku nyingi wakiwa katika theluji nyingi sana wakati wa majira ya baridi na kuwamwagia maji mpaka wakakauka. Lo! kilikuwa kisa cha kuogofya, nitakachokumbuka mpaka kufa kwangu.”

23 Ni nini kilichowawezesha vijana hawa kuendeleza uaminifu? Wao walifahamu kwamba walikuwa wamenunuliwa kwa “damu ya thamani” nao hawakutaka wawe wasioaminika kwa Wenyewe wao, Yehova Mungu na Yesu Kristo. Walisadiki kabisa kwamba, hata wakiuawa na wanadamu, Mungu na Kristo wasingewasahau nao wangewafufua. Waliuamini uhakikisho ulioongozwa kwa roho ya Mungu: “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.” (Ebr. 6:10) “Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi [uhai] yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya.”​—Luka 17:33.

24. Ni katika hali gani zinazolingana na hizo twaweza kuonyesha kwamba ‘hatuishi kwa ajili yetu wenyewe’?

24 Ingawa huenda wewe mwenyewe usipatwe na jaribu kali kama hilo la uaminifu wako kwa Mungu, hata hivyo, je! hata sasa unamweka yeye mbele? Pengine jaribu la uaminifu wako linahusu washiriki wa jamaa​—pengine wanakutukana, wakisema wewe ‘unaiheshimu mno dini yako.’ Au, yawezekana wanashule wenzako au wafanya kazi wenzako wanakukaza uziache kanuni zako za Kikristo. Je! wewe unafanya nini sasa nawe utafanyaje ukipatwa na magumu hayo? Huenda kushindwa na mateso au mikazo kukaelekea kufanya maisha yawe mepesi zaidi, yenye kuvumilika zaidi; hali kuwa mwaminifu kwa Mungu kwaweza kumaanisha kutukanwa zaidi kwa kitambo. Ukiikumbuka deni yako kwa Mungu na Kristo, utafanya uamuzi ufaao. Utaendelea ‘kumtukuza Mungu.’​—1 Kor. 6:20.

KUTUMIA WAKATI WAKO “USIPOKUWA NA SHUGHULI”

25. Ni nini zaidi kuliko uvumilivu wa uaminifu kinachotiwa ndani katika ‘kuishi si tena kwa ajili yetu wenyewe’ wakati tunapoteswa?

25 Hata hivyo, kuishi si tena kwa ajili yetu wenyewe kwatia mengi zaidi kuliko uvumilivu wa uaminifu tunapoteswa. Wakristo wanasihiwa hivi: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa [Yehova] ujira na urithi. Mnamtumikia Bwana Kristo.” (Kol. 3:23, 24) Kwa hiyo, kuishi si tena kwa ajili yetu wenyewe kwatia ndani kila upande wa maisha​—adili, namna mtu anavyofikiri, anavyotenda, anavyosema na anavyofanya kazi, utii wa mke, matumizi ya mume ya ukichwa na kutii wazazi.​—Kol. 3:5-22.

26. Ni kwa njia gani Wakristo wa jina tu wanavyotenda vingine kwa mwenendo wao?

26 Walakini, pengine umeona kwamba Wakristo wengi wa kujidai wanafanya vingine. Inajulikana sana kwamba hata kati ya Wakristo wa jina tu wanaoona haja ya adabu, kutojizuia​—ulevi, ufisadi na kuharibu mali​—mara nyingi kunakuwa katika sherehe zinazohusiana na sikukuu za makanisa. Likizo, jioni na Jumamosi na Jumapili ndizo nyakati ambazo watu zaidi na zaidi wanaona wako huru ‘kuishi’ kama wapendavyo.

27, 28. (a) Ingawa kuna wakati wa kuburudika, Wakristo wa kweli hawatafanya nini au kuwaza nini? (b) Ni kwa njia gani njema wanavyoutumia wakati wao ‘wasipokuwa na shughuli’?

27 Bila shaka, kuburudika na kufurahi kunafaa ili kuwa na maisha na utu uliosawazika. Naye Mkristo wa kweli anatumia kwa kufaa kadiri fulani ya wakati wake katika mambo yenye kuburudisha na kufurahisha. Lakini yeye haishi kwa ajili ya anasa tu. Yeye haweki kando sehemu fulani ya maisha yake kama “wakati wangu,” wakati ambao aweza kusahau kwamba anamtumikia Mungu.

28 Kwamba ndivyo ilivyo yaonekana kutokana na njia njema ambavyo watumishi wa Kikristo wa Yehova wanautumia wakati wao ‘wasipokuwa na shughuli.’ Zaidi ya kufanya mambo yenye kufurahisha wao wanafanya mambo yanayohusiana na ibada yao. Wanapendezwa na kuzungumza juu ya Muumba wao na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kila juma. Ushirika mzuri na maagizo yanayopokewa yanaifanya mikutano hii yenye kufurahisha zaidi. Hata wakati jamaa zinaposafiri, wanaweza kutia mikutano ya Kikristo katika mipango yao. Hivyo wanafurahia jambo jingine​—nafasi ya kukutana na rafiki wapya, ndugu na dada za kiroho, katika mji au nchi nyingine. Wanapokaa mbali na Jumba la Ufalme, pengine wakipiga kambi msituni, wanafurahia kutafakari juu ya Muumba wao na mazungumzo ya Maandiko kama vikundi vya jamaa. Halafu, tena, wengi wa mashahidi wa Yehova wanapanga likizo yao itie na kufaidika kabisa kutokana na makusanyiko makubwa ya Kikristo yanayopangwa kila mwaka.

29. Tunapofikiria kuutumia wakati wetu ‘tusipokuwa na shughuli,’ twaweza kufikiria nini kwa kufaa?

29 Kwa hiyo wakati wewe mwenyewe unapofikiria jioni, Jumamosi na Jumapili au likizo, ifikirie hali yako mbele za Mungu na Kristo. Jaribu kufanya yatakayokuburudisha kwa kimwili, akili au kwa kiroho. Mradi wako na uwe kupata nguvu utakazozitumia kwa faida katika utumishi wenye kuendelea kwa Mungu baada ya kipindi “usipokuwa na shughuli” kimekwisha. Ingawa huenda ulimwengu ukasema, ‘Safiri kidogo uisahau kawaida yako,’ onyesha unathamini yale ambayo Mungu na Kristo wamekufanyia. Epuka mambo yawezayo kuisumbua dhamiri yako na kukufanya utazame yaliyopita kwa masikitiko hali ungaliweza kuwa na wakati wenye kuthawabisha na kuburudisha.

30. Ni maulizo gani yanayotokea juu ya wale wanaojidai kumwamini Mungu lakini waishio kwa ajili ya anasa?

30 Kwa kweli, imempasa mtumishi wa Mungu akumbuke kufanya mambo yote kwa utukufu wa Muumba wake. (1 Kor. 10:31) Ajapokuwa asiyekamilika, imempasa ajitahidi kuzuia maelekeo yenye dhambi na ‘kutojitoa kama mtumishi wa dhambi.’ (Rum. 6:16) Walakini, pengine umeona kwamba watu wengine wasemao wanamwamini Muumba na Mwanawe wanaishi maisha ya kila siku yenye msingi wa kupata anasa zote wawezazo kuzipata wakati uu huu. Kinachokosekana ni nini? Yawezekana kwamba hawaoni tumaini la wakati ujao? Maisha yako ya kila siku yanaongozwaje hasa na maoni yako juu ya wakati ujao? Tutaiachia makala ifuatayo shauri hili.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki