Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 1/1 kur. 9-15
  • Jipatanishe kwa Unyenyekevu na Njia ya Yehova ya Wokovu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jipatanishe kwa Unyenyekevu na Njia ya Yehova ya Wokovu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUPATA UNYENYEKEVU
  • UNYENYEKEVU WAHITAJIWA LEO
  • MIFANO YA KISASA YA UNYENYEKEVU
  • MWENDO UFAAO KUFUATA
  • Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kwa Nini Kujivika Unyenyekevu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Unyenyekevu
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • ‘Jivikeni Unyenyekevu wa Akili’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 1/1 kur. 9-15

Jipatanishe kwa Unyenyekevu na Njia ya Yehova ya Wokovu

”Watu wanyenyekevu utawaokoa; lakini macho yako yawapinga wenye kiburi.”​—2 Sam. 22:28, NW.

1. Ni nini liliotukia katika makundi ya mashahidi wa Yehova mwaka wa 1972?

KATIKA Septemba wa mwaka wa 1972 badiliko kubwa lilitokea kati ya makundi ya mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Tangu mwaka wa 1932 mpaka mwaka wa 1972, katika kila kundi mwanamume mmoja alikuwa ameonwa kama “mwangalizi wa kundi,” na mara nyingi alikuwa ametumikia miaka mingi katika cheo hicho. Lakini katika mwaka wa 1971 ilikumbukwa kutokana na Maandiko kwamba makundi ya Kikristo katika karne ya kwanza yalikuwa na baraza ya wazee au waangalizi badala ya mmoja tu. (1 Tim. 4:14; Flp. 1:1, NW) Kwa sababu hii mpango wa Maandiko ulifuatwa tena kuruhusu iwepo baraza ya wazee kufanya kazi katika kila kundi na kusudi uenyekiti wa baraza hiyo upokezanwe kwa zamu kila mwaka katika makundi. Hivyo, katika mengi ya makundi 28,407 ya mashahidi wa Yehova yaliyokuwako Septemba wa mwaka wa 1972, mtu mpya aliingia kama mwangalizi-msimamizi.

2. Badiliko katika mpango wa tengenezo lilisaidiaje zaidi kuwatambulisha watu wa Mungu duniani leo?

2 “Waangalizi wa makundi” au “watumishi wa makundi” wa zamani waliitikiaje? Karibu kila mmoja wao alilikubali badiliko kwa unyenyekevu na kushukuru kwamba Yehova alikuwa ameliongoza tengenezo lake Yeye kujipatanisha zaidi na Ukristo wa kwanza. Watu hawa walishuka kwa kupenda katika maana ya kuwa sehemu ya baraza ya wazee, yenye usawa wa vyeo, badala ya kuwa mtu mmoja anayetegemewa kama mwangalizi wa kundi. Je! badiliko kama hilo laweza kufanywa katika tengenezo la kilimwengu, yaani, kuwachukua wale wenye vyeo vikubwa na kuwaweka katika vyeo vingine kwa zamu, bila machafuko? Ni vigumu. Lakini hili liliwezekana kati ya mashahidi wa Yehova, kwa maana ni watu wasiofanya ‘lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu akimhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.’​—Flp. 2:3.

3. Mashahidi wa Yehova wanapataje kuwa na unyenyekevu wa akili?

3 Lakini mashahidi wa Yehova wanapataje kuwa na sifa hizo? Wao wanazaliwa wenye dhambi, wakiwa na ugonjwa wenye kufisha wa dhambi, kama Mfalme Daudi na wanadamu wengine wote. (Zab. 51:5) Hata hivyo, wamejifunza kwamba kujipatanisha na njia ya Yehova kwa unyenyekevu kwaweza kuongoza kwenye wokovu wa hali hiyo, kama vile kulivyoongoza kwenye wokovu wa Naamani au kuponywa na ukoma. Kwa habari ya Naamani, njia ya Yehova ndiyo iliyokuwa njia ya pekee. Mungu alikuwa na mpango kupitia kwa nabii wake Elisha, na Yeye asingebadilika. Mara Naamani alipojinyenyekeza akafuatana na mpango huo alibarikiwa kwa kuponywa na kuijua kweli. Kwa hiyo unyenyekevu ni jambo lipasalo sisi pia tujifunze.

4. Ni maana gani inayokamatanishwa na maneno yanayohusiana na unyenyekevu katika Kiebrania, Kigiriki na Kiingereza?

4 Neno lililotafsiriwa hapa “unyenyekevu” katika Maandiko ya Kiebrania lina asili yenye maana ya ‘kuwa umeinama.’ Unyenyekevu, upole, na adabu vyote vinahusiana na maana ya neno hilo. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo neno lililotumiwa kwanza linakamatanisha kutotaka makuu na unyenyekevu wa akili. Katika Kiingereza (humility), linatokana na neno la Kirumi humus, linalohusu nchi, dunia, nalo lamaanisha kutokuwa na kiburi au majivuno.

KUPATA UNYENYEKEVU

5. Ni nini kinachotusaidia tuione haja ya kusitawisha unyenyekevu?

5 Unyenyekevu ni sifa iwezayo kusitawishwa. Kwanza, lazima mtu awe na tamaa ya kuwa mnyenyekevu. Bila shaka nia hii inasitawishwa kwa kusoma Biblia. Ndani yake twajifunza kwamba “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.” (Yak. 4:6) Tunapata kufahamu kwamba Yehova anataka ‘tuwe wanyenyekevu katika kutembea’ na yeye. (Mik. 6:8, NW, chapa ya mwaka wa 1960) Kwa hiyo tamaa yetu ya kumpendeza Mungu inatufanya tutake kuisitawisha sifa ya unyenyekevu.

6. Kwa sababu gani kuuthamini uhusiano wetu na Yehova kunatusaidia tuwe wanyenyekevu?

6 Linalohusiana na hili ni shauri la kuthamini kwema kwa uhusiano wetu na Yehova. Inatupasa tumwogope ifaavyo, yaani, tuwe na heshima nyingi sana, woga wa kumchukiza, tukijua kwamba anayoyahitaji kwetu yanafaa. (Zab. 111:10; Mit. 8:13) Naye Sulemani alifungamanisha kumwogopa Yehova na unyenyekevu aliposema hivi: “Thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha [Yehova] ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.”​—Mit. 22:4.

7. Mfano wa Yehova katika habari hii unatusaidiaje?

7 Mfano wa Yehova wa unyenyekevu pia ni msaada kwetu. (2 Sam. 22:36; Zab. 18:35) Anawaonyesha wenye dhambi rehema na huruma; ndiyo, hata alifikia hatua ya kumtoa Mwanawe kama dhabihu kwa ajili ya dhambi za wanadamu. (1 Yohana 4:10) Ikiwa Yehova, mtu aliye mkuu kupita wote katika ulimwengu wote ni mnyenyekevu, je! sisi kama viumbe hafifu tusiwe hivyo?

8. Matendo na maneno ya Yesu yanatusaidiaje katika kusitawisha unyenyekevu?

8 Kielelezo alichokiweka Yesu imetupasa pia tukiige ikiwa tu Wakristo, wafuasi wa Kristo. (1 Pet. 2:21) Je! haikutabiriwa kwamba angekuwa “mnyenyekevu” alipokuwa akiingia Yerusalemu ajitokeze kama mfalme? (Zek. 9:9; Mt. 21:5) Kama Neno, Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu mbinguni, yeye aliyepata kuwa Yesu bila shaka alikuwa na cheo kitukufu, lakini “alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti.” Naye Paulo alilishauri kundi la Filipi ‘liwe na nia iyo hiyo ndani yao ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu,’ nia hiyo ikitia ndani na sifa ya unyenyekevu. (Flp. 2:5-8) Alipokuwa duniani kama mwanadamu, Yesu alizungumza juu ya thamani ya sifa ya unyenyekevu, akiwatia moyo wanafunzi wake wawe wanyenyekevu kama mtoto mdogo, na kuwakumbusha kwamba “ye yote atakayejidhili, atakwezwa.”​—Mt. 23:12; 18:4.

9. Sala inasaidiaje katika kuwa wanyenvekevu wa akili?

9 Msaada mwingine wa kujinyenyekeza ni sala. Inasaidia kutukumbusha sisi juu ya ukuu wa Mungu na uhafifu wetu, uhakika wa kwamba wako wengine wanaotamani kuingia katika uhusiano mwema na “Baba yetu” au kuuendeleza; na lo! namna ulivyo mpango mzuri ajabu uliofanywa na Yehova kupitia kwa Mwanawe tupate kusamehewa dhambi zetu! Sala inatusaidia tukumbuke kwamba sisi wenyewe hatuna cha kujivunia.​—Mt. 6:9-12.

10. Upendo unayafaaje mazungumzo juu ya unyenyekevu?

10 Sifa ya upendo, mojawapo la matunda ya roho ya Mungu, ni ya lazima katika kusitawisha unyenyekevu wa akili. (Gal. 5:22) “Upendo . . . haujivuni.” (1 Kor. 13:4) Twajifunza kuthamini kwamba upendo ulio wa maana zaidi ni upendo wetu kwa Yehova, halafu, yatupasa ‘tupende jirani zetu kama nafsi zetu wenyewe,’ yaani, yatupasa tujione kuwa sote tunalingana, si kujifikiria wenyewe zaidi ya tunavyowafikiria. (Mt. 22:37-39) Mashahidi wa Yehova wanataka wawe wanyenyekevu. Wao wanajua kutokana na funzo lao la Biblia kwamba Yehova analitaka jambo hili kwao. Wametafakari juu ya mifano ya Yehova na Kristo Yesu katika habari hii. Wanautumia kwa faida mpango wa sala, nao wanaendelea kujitahidi wadhihirishe upendo, ambao Yesu alisema ungewatambulisha wafuasi wake na unaowasaidia kusitawisha unyenyekevu wa akili.​—Yohana 13:34, 35.

UNYENYEKEVU WAHITAJIWA LEO

11, 12. Unyenyekevu unatusaidiaje katika huu ulimwengu uliojawa na chuki?

11 Kusitawisha sifa ya unyenyekevu kunatusaidia tupambane na magumu yanayopatikana katika ulimwengu huu wa kisasa, wenye choyo na uliojawa na chuki. Mungu alimwongoza mtume Paulo kwa roho yake atabiri kwamba “siku za mwisho” watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, . . . wenye kiburi.” (2 Tim. 3:1, 2) Nia hii imewashika sana watu wa namna zote za maisha, nasi bila shaka hatutaki itupate.

12 Watu wanakubali kwa vyepesi kwamba mapigano yaliyoko kati ya mataifa au makabila mbalimbali yanasababishwa na “kiburi” cha kitaifa au kikabila. Lakini kiburi ni kinyume cha unyenyekevu, nacho “kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.” (Mit. 16:18) Je! tunataka tugongane dafurao na Mungu kwa sababu ya kiburi cha kitaifa au kikabila? Hiyo ingemaanisha uharibifu wetu.

13. Unyenyekevu unawasaidiaje wanawake katika hii taratibu mbovu ya mambo?

13 Mpango wa kuwapa wanawake uhuru wao wenyewe ni jambo ambalo watu ulimwenguni pote wamejulishwa. Wanawake wengine wanaohusiana nao na wenye kuiona Biblia kama kitabu kilichobuniwa na wanadamu, wanadai kwa kiburi kwamba andiko lisemalo mwanamume ‘ni mfano wa utukufu wa Mungu; lakini mwanamke ni utukufu wa mwanamume,’ ni maoni ya kujitakia makuu tu ya wanaume. (1 Kor. 11:7) Kiburi cha wanawake hao kimewafanya wapingane moja kwa moja na Yehova, aliyekuongoza kuandikwa kwa Biblia kwa roho yake. Je! ninyi wanawake mtakao kupata kibali ya Mungu mnakuepuka kukosa huko kwa unyenyekevu? Mtume aliwaambia wanaume hivi katika kundi la Kikristo, “Nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari.” Je! ninyi wanawake hamwoni kwamba kutii kwenu pia amri hii ya Maandiko kunafanya unyenyekevu uwe mwepesi zaidi na kufanya maisha yenye kufurahisha zaidi?​—1 Pet. 5:6.

14. ‘Kichwa cha nyumba’ chawezaje kuwa kinyenyekevu?

14 Bila shaka, wazo la ukichwa wa mwanamume huenda likatumiwa kupita kiasi. Ili kutimiza daraka lake kama baba na mume, yampasa mume katika nyumba awe mnyenyekevu, aone makosa yake mwenyewe na kujitahidi ayaondoe, na kukubali makosa anapoyafanya. Unyenyekevu ungemfanya awe mwenye huruma, akiwafikiria wengine katika jamaa kabla ya kufanya maamuzi makubwa. Ungemsaidia pia awe mwenye kusamehe wengine katika jamaa wala si kutazamia wawe wakamilifu kwa maana Yehova hamtazamii yeye awe mkamilifu. Kwa kweli unyenyekevu unasaidia wote katika jamaa washinde magumu yanayotokana na kutofautiana kwa wanaume na wanawake, vijana na wazee. Unyenyekevu wa akili unatusaidia tuendelee ‘kuchukuliana katika upendo.’​—Efe. 4:2.

15. Unyenyekevu unatusaidiaje katika habari ya kuhubiri na kuvumilia mateso?

15 Unyenyekevu unatusaidia tujitie katika kazi aliyosema Yesu ingefanywa kabla ya mwisho wa hii taratibu mbovu ya mambo kuja. Alitabiri kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote, kazi ya kueleza wengine juu ya Ufalme, serikali ya Mungu ambayo kwayo anakusudia kuitawala dunia. (Marko 13:10) Unyenyekevu wa akili unatusaidia tuyafikirie maoni ya wale tunaowahubiri; unatusaidia tuifahamu hali yao tunapozungumza nao. Yesu alitabiri pia kwamba wafuasi wake wangechukiwa, wangeteswa kwa sababu ya kumfuata yeye. (Mt. 24:9) Unyenyekevu unatusaidia tupambane na upinzani huo kwa maana twajua Yehova ni mkuu kupita wote, na kwa hiyo hatumwasi yeye kwa kuruhusu hili litukie. Tunautegemea mfano aliouweka Yesu wa kupambana na mateso, kwa kuendelea kuwa mnyenyekevu mbele ya wale wenye kumtukana na kwa kuendelea kuwa mwaminifu kwa Baba yake.​—1 Pet. 2:23.

16. Kwa sababu gani unyenyekevu unasaidia katika shauri la adhabu?

16 Mtu mnyenyekevu ni yule anayekubali maonyo na adhabu. “Maonyo ya kumwadilisha mtu ni njia ya uzima.” (Mit. 6:23) Wenye kiburi wanachukia kuonywa; wao wanajiona hawafanyi kosa lo lote. Lakini wenye unyenyekevu wa akili wanajua wanafanya makosa nao wanashukuru kwa kuonyeshwa makosa. “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Ebr. 12:11) Kwa hiyo wale wanaokubali maonyo na adhabu wanasaidiwa wafanye maendeleo mema ya kiroho.

MIFANO YA KISASA YA UNYENYEKEVU

17. Kukubali alikuwa asiyejua kusoma wala kuandika kwa unyenyekevu kulimsaidiaje kijana mmoja?

17 Ikiwa wewe huwezi kusoma, je! ungekuwa mnyenyekevu vya kutosha kuweza kukubali hivyo na kuomba msaada? Kijana mmoja katika Afrika Magharibi alisimulia maono haya: “Niliona vibaya kwa sababu nikiwa mwenye umri wa miaka kumi na tisa sikujua kusoma wala kuandika. Lakini siku moja nilipata habari juu ya masomo ya ngumbaru yaliyoongozwa na mashahidi wa Yehova penye Jumba la Ufalme lao. Ijapokuwa sikuwa Shahidi, waliniruhusu nijiandikishe. Masomo ya ngumbaru yalikuwa sehemu ya mikutano yao ya kundi, nami nilikuwa nikiketi nisikilize sehemu iliyobaki ya kipindi cha jioni kuonyesha shukrani. Niliifurahia mikutano hiyo sana nami nikataka nitoe hotuba kama walivyokuwa wakifanya vijana wengine. Mmojawapo wa vijana hawa alianza kujifunza nami Biblia nyumbani. Kwa muda unaopungua miaka miwili si kwamba tu nilijifunza kusoma na kuandika, bali niliweza kustahili kushiriki katika utumishi wa shambani, kuonyesha wakf wangu kwa kubatizwa na kulifurahia pendeleo la kuwa painia.” Unyenyekevu wa mtu huyu ulimwezesha ajifunze kusoma na kuandika, apate maarifa ya kweli na kuwa mhudumu wa wakati wote, akiishiriki kweli na wengine.

18. Mtu mmoja mwenye majivuno alibadilikaje? Matokeo yakawa nini?

18 Katika sehemu ile ile ya dunia alikuwako mtu asiyekuwa mnyenyekevu. Kwa kweli, alimwambia mhudumu wa mashahidi wa Yehova aliyeonana naye kwa kujivuna kwamba hakuhitaji ye yote amfundishe, yeye akiwa msimamizi wa kampuni kubwa, kwa maana angeweza kujifunza Biblia mwenyewe. Walakini, alikubali mwaliko wa kuhudhuria mmojawapo wa mikutano ya kundi. Alivutwa sana na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi akaanza kuhudhuria kwa kawaida. Karibuni alijiandikisha katika shule, nayo nia yake yote ilibadilika alipoanza kuyakubali na kuyatumia mashauri aliyoyapokea shuleni. Aliomba awe na funzo la Biblia nyumbani naye akafanya maendeleo mema. Ndiyo, alijinyenyekeza naye sasa ana pendeleo la kutumikia kama mtumishi aliye wakf na kubatizwa wa Yehova Mungu.

19. Kiogozi mmoja wa kidini aliye kipofu alionyeshaje unyenyekevu?

19 Katika kisiwa kisicho mbali na Australia Shahidi kijana alimfikia mzee mmoja, na baada ya ziara nyingi akaanzisha funzo na kikundi cha watu watano au kumi hivi, akitumia saa mbili au tatu kila ziara. Sikuzote alikuwapo mzee mmoja kipofu naye alionyesha upendo mwingi sana juu ya Biblia. Karibuni alianza kuzungumza na kila mtu aliyekutana naye juu ya kweli aliyokuwa akijifunza. Baadaye iligunduliwa kwamba kipofu huyu alikuwa ndiye mchungaji wa mahali hapo wa Kilutheri. Baada ya miezi michache kikundi hiki kilianza kuhudhuria mingine ya mikutano ya mashahidi wa Yehova ijapokuwa iliwapasa watembee saa mbili na nusu au tatu. Karibuni, yule mchungaji mzee aliwaambia washiriki wengine wa kanisa kwamba alikuwa akiondoka kwa maana alijua kwamba aliyokuwa amefundisha zamani hayakuwa kweli. Ndiyo, alikuwa mnyenyekevu vya kutosha kuweza kulikubali kosa la mwendo wake wa zamani maishani na kuchukua hatua za kujipatanisha na njia ya Yehova ya wokovu.

20. Kwa sababu gani kiongozi mwingine wa kidini aliliacha kanisa lake?

20 Kiongozi mwingine wa kidini aliye mnyenyekevu alifikiwa katika kijiji kimoja katika kisiwa fulani cha South Pacific, naye alikubali pia awe na funzo la nyumbani la Biblia. Karibuni aliiona tofauti kati ya mafundisho ya kanisa lake na Biblia, na baada ya kujifunza mara mbili tu akaliacha kanisa lake. Washirika wenzake wa zamani walifadhaishwa na kuondoka kwake na kujaribu kumsihi aendelee kuwa mhudumu wao. Yeye aliwajulisha kwamba sasa angeushindania Ukristo wa kweli tu. Alizidi kufanya maendeleo ya kiroho naye sasa ni mmoja wa watumishi waliobatizwa wa Yehova, akiwasaidia wengine wajifunze kweli.

21. (a) “Utu mpya” unahusu nini? (b) Ni sifa gani njema iliyotolewa juu ya “utu mpa” wa mashahidi wa Yehova?

21 Mtume Paulo anatia moyo hivi: “Uvueni utu wa kale pamoja na mazoea yake, mjivike utu mpya, . . . jivikeni shauku nyingi ya huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na uvumilivu.” (Kol. 3:9-12, NW) Kwa hiyo sehemu ya utu mpya wa Kikristo ni unyenyekevu wa akili. Sifa hizi zinadhihirishwa na watu wa Yehova, nayo hii yafanya wengine wavutwe. Barua ifuatayo iliyopokewa na afisi ya tawi ya Philippine ya Watch Tower Society kutoka kwa msimamizi wa kampuni moja walipoajiriwa Mashahidi wawili yaonyesha hivyo: “Tunakaribia kurekebisha Kiwanda chetu nasi tungependa kujua kama mtataka kwa hisani yenu kutusaidia kutafuta wafanya kazi wenye ujuzi. Sababu kubwa zaidi iliyotuongoza tuiulize Sosaiti yenu ni kwa maana uchunguzi wetu hasa na tuliyoyaona yamehakikisha kwamba watu wa tengenezo lenu wangeweza kutegemewa sana wafanye kazi yo yote kwa bidii na uaminifu, nasi twastaajabu pia kwa sababu ya uwezo wao wa kufahamu na kujipatanisha na magumu yaliyopo ya fedha na kazi.”

22. Shahidi mmoja alionyeshaje kuithamini mikutano ya kundi, nayo matokeo yakawa nini?

22 Ijapokuwa wanaendelea vema katika kazi zao za kilimwengu, mashahidi wa Yehova hawasahau kwamba Yehova ndiye apaswaye kusifiwa, nao wanaendelea kulithamini pendeleo la kuhudhuria mikutano ya kundi la Kikristo wapate kuendelea kuusitawisha “utu mpya.” Jamaa moja ya Shahidi kijana wa kike ilipatwa na shida ikampasa yeye atafute kazi ya kilimwengu awasaidie kwa fedha. Alipohojiwa juu ya kazi hiyo, aliona kwamba angehitajiwa afanye kazi nyakati za mikutano fulani ya kundi, naye tajiri akakataa kufanya mabadiliko. Shahidi huyu wa kike alimwambia, “Naitaka kazi hii, bwana, lakini siwezi kubadilishana imani yangu na kazi,” na kwa hiyo akaikataa. Walakini, siku mbili baadaye msimamizi alituma mjumbe kwenye Jumba la Ufalme akamtafute na kumpa kazi ile pamoja na wakati wa kuwa huru kuhudhuria mikutano yote. Yehova alimbariki kwa jitihada zake za unyenyekevu za kumpendeza yeye.

23. (a) Mwangalizi mmoja mwenye kusafiri alionyeshaje nia ya unyenyekevu? (b) Waangalizi kati ya mashahidi wa Yehova wanapendezwa na nini?

23 Wajumbe wenye kusafiri wa mashahidi wa Yehova wanapewa mgawo wa kutembelea makundi kwa kawaida wayajenge kwa kiroho kwa hotuba na kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri pamoja nao. Muda fulani uliopita ziara hizi zilibadilishwa kutoka miezi minne kuwa kila miezi sita, na kwa hiyo wengine wa wanaofanya kazi hii, wajulikanao kama waangalizi wa mizunguko, hawakuhitajiwa tena kwa utumishi huu. Mtu mmoja kama huyo aliyekuwa akitumikia katika mji wa New York alisema hivi kwa unyenyekevu: “Niliposikia kwamba hesabu fulani wangeondolewa katika kazi ya mzunguko nilisali kwa Yehova kwamba, ikiwa ziara zangu zilikuwa zikizuia au hazikuwa zikisaidia makundi kama nyingine, mimi ningekuwa mmoja wa wale watakaoondolewa katika kazi ya kusafiri.” Lo! hiyo ni nia njema namna gani, inayoonyesha ile ya wazee au waangalizi kati ya mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote! Wao hawapendezwi kwa kiburi na cheo chao bali, na kuwaangalia wafuasi wenye mfano wa kondoo wa Yesu, wakijua kwamba “kondoo” ni wake yeye.​—⁠Yohana 10:14.

MWENDO UFAAO KUFUATA

24, 25. Lazima tufanye nini ikiwa twaamini wokovu ni wa wanyenyekevu?

24 Je! wewe wayaamini kweli maneno ya mwandikaji wa Biblia Daudi yaliyomo katika sala yake kwa Yehova: “Watu wanyenyekevu utawaokoa; bali macho yako yawapinga wenye kiburi”? (2 Sam. 22:28, NW) Ikiwa wayaamini, basi utataka uondoe dalili zo zote za kiburi maishani mwako, za kujidhania wewe u bora kuliko wengine kama ni kwa sababu ya kabila lako, taifa lako, elimu yako au hali yako katika maisha. Sisi sote twatokana na Adamu mwenye dhambi, kwa hiyo kwa kweli wenyewe hatuna cho chote kile cha kujivunia.​—Matendo 17:26.

25 Tuna tumaini la wokovu tukijipatanisha kwa unyenyekevu na njia ya Yehova. Lazima tufahamu kwamba “kila kitu kilichomo katika ulimwengu​—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake​—hakitokani na Baba, bali chatokana na ulimwengu. Tena, ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:16, 17, NW) Njia ya Yehova yamaanisha kwamba hatuwezi kujiingiza katika utafutaji wa vitu vya kimwili vya ulimwengu. Vyaweza kutufanya tupatwe na msiba, kama ilivyokuwa katika habari ya Gehazi mwenye pupa.

26. Sisi kama watu mmoja mmoja twataka kufuata mwendo gani wa tendo?

26 Kwa hiyo, mwendo wa kufuata ni kujifunza Maandiko, kupatanisha maisha yako na mapenzi ya Yehova na kuwa mmoja wa watumishi wake walio wakf na kubatizwa, ukiwasaidia wengine wajipatanishe na njia ya Yehova ya wokovu. Kwa wale waliokwisha chukua hatua hii, ni lazima kuendelea kuifuata njia ifaayo. “Hapo tulipofika na tuenende katika lilo hilo.” (Flp. 3:16) Hatutaki kamwe tuchukizwe na maneno ya Paulo, “Kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake,” katika uhusiano wetu na ndugu zetu wa Kikristo. (Flp. 2:3) Twataka tuithamini kabisa roho ya unyenyekevu katikati ya watu wa Mungu na kujitahidi tuiongeze roho hiyo. Twataka tuone furaha, uradhi kutokana nayo. Inatokeza na kuendeleza hali ya kupendeza na kuthawabisha, hii ikionyesha kwa unyenyekevu upendo kwa ushirika mzima wa akina ndugu. Kumbuka, pia, kwamba tengenezo la Yehova haliwezi kubadilika ati kwa sababu tu ya kupendeza watu mmoja mmoja.

27. Kwa sababu gani kulaumu-laumu kazi ya baraza ya wazee katika kundi kungekuwa kosa?

27 Ikiwa twakataa jambo fulani linalofanywa na baraza ya wazee au kulaumu-laumu namna jambo fulani linavyoshughulikiwa, tunakuwa wasioaminika kwa tengenezo la Yehova. Na tukumbuke kwamba wazee si wanaume walioongolewa karibuni; wao wamekuwa wakimtumikia Yehova miaka mingi. (1 Tim. 3:6) Nacho ni nini kinacholeta kutafuta-tafuta makosa au kulalamika? Je! mara nyingi si tamaa ya kujikuza machoni pa wengine? Ndiyo kusema, kiburi ndilo shina la ugumu wenyewe. Kwa kweli mwendo huu wa tendo huenda ukahusu kuipinga roho takatifu, kwa maana roho takatifu ndiyo yenye daraka la kuwekwa kwa wazee kundini. (Matendo 20:28) Sababu gani, basi, tumlaumu-laumu mmojawapo wa akina ndugu kwa sababu ya kushughulikia faida za Ufalme namna ambavyo roho takatifu yaelekea kumwongoza? Na ikiwa ndugu amekosea kwa namna alivyoshughulikia jambo fulani, imetupasa tuwe na imani ya kwamba roho takatifu itamwonyesha makosa.

28. Lazima sote tujue nini, kwa ajili ya hali njema yetu ya milele?

28 Katika ulimwengu wenye mashindano makali yenye chuki, kila jamii yenye ugomvi ikipigania faida zake yenyewe, ni tengenezo moja linalotokeza kama lililo tofauti, wafuasi wa kweli wa Yesu, mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Wengine wao wamedhihirisha imani yenye ushujaa kama yule msichana mdogo Mwisraeli aliyeishi wakati wa Naamani, wakiisema wanayoijua kuwa kweli kwa kutumaini kwamba wengine watafaidika. Huenda wakaonwa kama watu wasiojulikana, walio hafifu, lakini wao wanayo kibali ya Yehova. Wengine wametumikia katika vyeo vikubwa zaidi, kama vile Elisha, lakini wao pia wanapendezwa kwanza na kuwa na kibali ya Yehova; tamaa yao si kujipatia faida. Sisi sote na tufanye kazi pamoja nao, tukijua kwamba hakuna wokovu bila ya unyenyekevu na nia ya kujipatanisha na njia ya Yehova.

​—Kutoka The Watchtower, July 1, 1974.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki