Usiache Utajiri Wala Umaskini Uwe Uangamivu Wako
UTAJIRI unaweza kudhuru matajiri, kama vile umaskini unavyoweza kudhuru maskini. Mithali ya kale iliyoongozwa na Mungu, ambayo ni ya kweli leo kama ilivyokuwa kweli ilipoandikwa, inauonyesha uhakika huu vizuri: “Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; uangamivu wa maskini ni umaskini wao.”—Mit. 10:15.
Lakini ikiwa mali za tajiri ni mji wa nguvu, zinamdhuruje? Ni wazi kwamba matajiri wanaelekea kuona utajiri wao kama ulinzi, kama ukuta unaozunguka mji. Kwa maana kwa kawaida utajiri unawawezesha kupata chakula kizuri, nyumba nzuri nzuri na faida nyingine za kimwili. Bila shaka pesa zina thamani fulani, kama vile Biblia inavyosema: “Kama vile fedha ilivyo ulinzi.”—Mhu. 7:12.
Lakini je! utajiri unafanya mtu asiweze kupatwa na cancer (donda baya sana), ugonjwa wa moyo na misiba mingine? Je! utajiri unaweza kununua furaha—ndoa yenye usalama, au watoto wenye adabu njema na heshima? Badala yake, huenda mtu akapoteza afya yake na kuharibu uhusiano wa jamaa yake kwa sababu ya kujaribu mno kuwa mmoja wa matajiri wakubwa. Ni kama vile mithali nyingine iliyoongozwa na Mungu inavyoeleza: “Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; ni kama ukuta mrefu katika mawazo yake.”—Mit. 18:11.
NAMNA UTAJIRI UNAVYOWEZA KULETA UANGAMIVU
Naam, tajiri anapoona utajiri wake wa kimwili kuwa wa maana sana anakuwa akiota tu. Kwa kweli, utajiri unaweza kuletea mtu uangamivu. Kwa mfano, umepata kuona kwamba matajiri ndio wanaoshambuliwa mara kwa mara na wavunja sheria? Mara nyingi habari zinaonyesha wametoroshwa na kufichwa mpaka bei ya ukombozi itolewe, na nyakati nyingine wanauawa. Au jambo hilo linawapata wapendwa wao, na kuharibu jamaa.
Utajiri unaleta msiba pia kwa njia nyingine. Limekuwa jambo la kawaida kwa watoto wa matajiri kukataa njia ya maisha ya wazazi wao wenye kufuatia mali za kimwili. Huenda hata wakawakataa wazazi wao, na kuleta huzuni kuu katika jamaa.
Lakini lililo baya zaidi ni matokeo ambayo utajiri unaweza kuwa nayo juu ya uhusiano wa mtu na Mungu. Ingawa huenda wasiwe wanakataa kuamini Mungu, watu wanaelekea kumweka Yeye nyuma katika maisha zao. Kwa kweli, wanajitumainia wenyewe kuliko vile wanavyomtumainia Mungu. Nia hiyo baadaye inaleta uangamivu, kama vile Yesu Kristo alivyoonyesha katika mfano wake juu ya tajiri aliyejishughulisha kupita kiasi na kutosheleza tamaa zake mwenyewe.—Luka 12:16-21; Mit. 11:28.
Lakini si lazima utajiri ufanye mtu awe mwenye kiburi na kujitumainia mwenyewe tu. Tajiri anaweza kufikiri juu ya Mungu kwa uzito na uhitaji wa mapenzi ya Mungu kutendeka juu ya dunia hii. Pengine wewe unafanya hivyo. Pengine mashahidi wa Yehova wanapokutembelea kuzungumza nawe juu ya ufalme wa Mungu unasikiliza. Pengine unachukua vitabu vya kusaidia kujifunza Biblia na kujitolea kwa ukarimu usaidie kwa mchango. Lakini je! hayo ndiyo yanayotakiwa ili kumpendeza Mungu?
Jambo lililotukia kabisa linatusaidia tufahamu. Tajiri mmoja alimfikia Yesu akamwuliza alitakiwa kufanya nini ndiyo ‘apate uzima wa milele.’ Mtu huyo tayari alikuwa anatii sheria za Mungu za msingi, lakini Yesu alipomweleza kwamba lazima aache kuhangaikia mali za kimwili hasa ili ampendeze Mungu na kupata uzima wa milele, na badala yake awe mwanafunzi wa Yesu na kuiga mfano wake wa kueleza wengine mambo ya kiroho, tajiri huyo alikwenda zake kwa huzuni. Kwa sababu gani?—Mt. 19:16-22.
Tatizo linajulishwa katika mfano ambao Yesu alitumia juu ya wale wanaosikia “neno la ufalme.” Yesu alieleza hivi juu ya mtu wa namna fulani anayetajwa katika mfano huo: “Shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno.” (Mt. 13:22) Mara nyingi wingi wa mali unakuwa na matokeo hayo. Kwa kawaida matajiri wanahangaikia faida zao wenyewe za kimwili hata hawaangalii “neno la ufalme” linavyostahili kuangaliwa. Je! ndivyo wewe ulivyo?
Ikiwa unataka kweli kumpendeza Mungu, huu ndio wakati wa kufanya badiliko. Usiache shughuli za faida za kijamii na za kibiashara zikusonge kiroho. Ikihitajiwa, fanya mabadiliko kabisa ili uweze kujifunza Neno la Mungu kwa kawaida. Mashahidi wa Yehova watakusaidia kwa furaha, bila malipo. Na uwe mmoja wa wanafunzi wa Kristo, ufuate mfano wake kweli kweli, na hivyo uishike zawadi ya Mungu ya “uzima wa milele.”
USIACHE UMASKINI UWE UANGAMIVU WAKO
Kwa upande mwingine, lazima maskini nao wajihadhari, kwa maana umaskini nao unaweza kuwaletea uangamivu. Huenda wakawa wanajidai kumwamini Mungu, na kufuata dini ya kweli, lakini umaskini unaweza kusonga roho yao na kupotoa kuwaza kwao. Mtu mwenye hekima wa zamani za kale alitambua kwamba hilo lingeweza kutokea, na kwa hiyo akasali hivi: “Nisiwe maskini sana nikaiba, na kulitaja bure jina la Mungu wangu.”—Mit. 30:9.
Akiwa katika shida nyingi, mtu aweza kushawishwa aibe. Mara nyingi leo maskini anaona wengi wanaomzunguka wakiwa na wingi wa vitu na huenda akaona uchungu juu ya hali hiyo isiyo haki. Lakini hali hizo hazimpi mtu haki ya kuiba, chini ya sheria za Mungu wala zile za mwanadamu.
Mtu akishindwa na kushawishika na kuiba au kufanya jambo jingine kama hilo la udanganyifu, matokeo yanakuwa nini? Huenda akajikuta gerezani, nalo jambo hilo linaweza kumwaibisha yeye na jamaa yake pia. Tena, huenda dhamiri yake ikamtesa, au huenda hata ikaungua naye akawa mkosaji wa sikuzote. Asipochukua hatua za kusahihisha mwendo wake, atakataliwa na Mungu na kupoteza tumaini la kupata uzima wa milele katika taratibu mpya ya Mungu yenye haki, inayokaribia sasa.
Imempasa mtu afahamu kwamba mali alizo nazo sizo zinazomfanikisha kwa kweli. Bali, ni uhusiano wake unaofaa na Yehova Mungu. Kwa sababu gani? Kwa sababu Mungu peke yake ndiye anayeweza kuanzisha na ataanzisha serikali yenye haki ambayo haitakuwa na udhalimu, wengine wakipendelewa zaidi ya wengine. Ahadi ya Neno la Mungu Biblia iliyo hakika ni kwamba wote wanaotimiza matakwa ya Mungu ya kuishi wakati huo watafurahia wingi wa mazao mazuri ya dunia.—Isa. 25:6-9; Ufu. 21:3, 4.
Kwa sasa, wakati udhalimu wa taratibu hii umeruhusiwa kuwapo, mtu awe ni tajiri au maskini hiyo haihusu uhusiano wake na Mungu. Ni kama vile mithali iliyoongozwa na Mungu inavyosema: “Tajiri na maskini hukutana pamoja; [Yehova] ndiye aliyewaumba wote wawili.” (Mit. 22:2) Naam, wote wanasimama mbele za Mungu wa kweli, Yehova, juu ya msingi wa namna walivyo, si mali walizo nazo.
Ndivyo wale wanaomwabudu Yehova Mungu kwa kweli wanavyoonana pia. Wao hawahukumu wengine kulingana na hali yao ya uchumi au ya kijamii, bali wanawakubali kwa vile walivyo kama watu. Je! wewe ungependa kushirikiana na watu wanaotendeana hivyo? Unaweza kuwapata katika Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova.