Je! Roho Takatifu Ni Nafsi Kweli?
ROHO takatifu inaweza kuhuzunishwa na inaweza kusema, kufundisha, kutoa ushuhuda, kuwa mkumbushaji na msaidizi. Je!’ usingetazamia mambo hayo yasemwe juu ya nafsi, naam, juu ya “nafsi ya tatu” ya Utatu? Na hali mambo mengine yanayotajwa juu ya roho ya Mungu hayatumiwi kamwe kuhusu nafsi. Kwa mfano, roho hiyo inaweza ‘kumiminwa’ juu ya wanadamu na ‘kuwajaa.’ Tueleweje hilo? Roho takatifu ya Mungu ni nani au ni nini hasa?
NI NAFSI AU NI NGUVU YA UTENDAJI?
Maneno ya Kiebrania na Kigiriki ya “roho” hayamaanishi utu. Yanamaanisha pumzi, upepo. (Linganisha Zekaria 2:6; Ayubu 41:16; Yohana 3:8.) Kwa hiyo maneno hayo yanamaanisha jambo lisiloonekana, nguvu ya utendaji. Nguvu ya utendaji hiyo inaweza ‘kumiminwa’ au kutiwa ndani ya watu wengi sana wakati ule ule na inaweza ‘kuwajaa,’ kama inavyotajwa juu ya roho takatifu.—Matendo 2:4, 33.
Bila shaka, Biblia yatumia neno “roho” kuhusu watu. Twasoma: “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) “Naye hufanya malaika zake kuwa roho.” (Ebr. 1:7, NW) Mungu na wana wake wa kimalaika wenye kushikamana naye ni watakatifu na kwa hiyo wote ni ‘roho takatifu.’ Huenda basi roho takatifu ya Mungu ikawa nafsi pia (au mtu)? Namna gani juu ya kazi inazofanya kama kusema, kuongoza watu, kufundisha, kutoa ushuhuda na kadha wa kadha? Je! kazi hizo hazionyeshi roho ya Mungu ina utu? Sivyo. Angalia maelezo ya kitabu cha wenye kuamini Utatu, New Catholic Encyclopedia (Vol. 13, uk. 575):
“Mengi ya maandiko ya A[gano] J[ipya] yanaonyesha roho ya Mungu kuwa kitu, si mtu; hiyo inaonekana hasa katika ulinganifu wa roho na uwezo wa Mungu. Wakati roho ya Mungu inapotajwa kama kwamba inasema, inazuia, inatamani, inakaa (Matendo 8.29; 16.7; Rum. 8.9) na kufanya mambo mengine kama hayo, mtu hana haki ya kukata maneno mara moja kwamba vifungu hivyo vinaonyesha roho ya Mungu ni Mtu; maneno ayo hayo yanatumiwa pia kuhusu mambo au mawazo yanayopewa sifa za mtu kwa kusudi la kusihi au kutia mkazo (tazama Rum. 8.6; 7.17). Hivyo, habari zinazozunguka kifungu cha maneno ‘kukufuru roho’ (Mt. 12.31; linganisha Mt. 12.28; Lk. 11.20), zaonyesha kwamba uwezo wa Mungu ndio unaotajwa.”
Naam, kitu kinaposemwa kama kwamba kina sifa za mtu, hiyo haihakikishi kina utu. Kwa mfano, Biblia yasema dhambi ‘ilitawala,’ ‘ikapata nafasi,’ ‘ikafanya kutamani,’ ‘ilidanganya,’ ‘ikaua.’ (Rum. 5:21; 7:8-11) Vivyo hivyo hekima inatajwa kama mtu na kama kwamba ina “watoto” na “kazi.” (Mt. 11:19; Luka 7:35) Hata hivyo hakuna anayeweza kudai kwamba hiyo yamaanisha “dhambi” na “hekima” ni watu. Vivyo hivyo roho ya Mungu inapopewa sifa za mtu, hiyo haipingani na ushuhuda wa wazi wa Biblia unaoonyesha ni “kitu, si mtu.”
Kwa kuwa roho takatifu inashirikishwa sana na Chanzo chake, yaani Mungu, mtu anayetenda kinyume cha mapenzi ya Mungu ‘ahuzunisha roho yake.’ (Efe. 4:30) Roho takatifu itahuzunishwaje ikiwa si mtu (au nafsi)? Maneno ya mtume Paulo juu ya roho yake mwenyewe au nia kuu yake yaonyesha hivyo. Katika 1 Wakorintho 5:3-5 twasoma hivi: “Kwa maana kweli, nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo. Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu; kumtolea Shetani mtu huyo.”
Katika habari hii, Wakristo wa Korintho walijulishwa na barua ya Paulo roho yake au nia yake ilikuwa nini kuhusu kuachiliwa kwa maongozi mapotovu kundini. Kwa hiyo walipokutana wazungumze hilo, roho au nia yenye nguvu ya Paulo ilikuwa papo hapo kati yao, kama kwamba ilikuwa mtu. Baada ya uamuzi kufanywa ukipatana na roho aliyoonyesha Paulo, Wakristo Korintho wangeweza kusema, ‘Sisi wenyewe na roho ya Paulo tumeamua kumfukuza mtu huyo asiyetubu.’ Kwa upande mwingine, kama wangalitenda kinyume cha roho ifaayo iliyoonyeshwa na mtume, ‘wangaliihuzunisha.’
Huenda mtu akapinga akisema, ‘Lakini hayo yote hayabadili uhakika wa kwamba Biblia yataja Baba, Mwana na Roho Mtakatifu kwa pamoja. Bila shaka hiyo yahakikisha kwamba Roho ni mtu (au nafsi).’
Kwa hiyo, twaweza kuangalia maandiko mawili yanayoonyeshwa kama mifano ya kuhakikisha hivyo: “Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu, na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote.” “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu.”—2 Kor. 13:14; Mt. 28:19, Union Version.
Je! maandiko haya, 2 Wakorintho 13:14 na Mathayo 28:19, yanahakikisha kwamba “Roho Mtakatifu” ni “nafsi ya tatu” ya Utatu? Je! yanasema kwamba Baba, Mwana na Roho Mtakatifu ni Mungu mmoja? Sivyo, nao wanapotajwa kuwa Baba, Mwana na Roho Mtakatifu bila maelezo zaidi, hatuoni uhusiano wao ni nini. Tena, uhakika wa kwamba ubatizo utafanywa kwa “jina” la roho takatifu hauhakikishi kwamba roho ni mtu (au nafsi). Hata wenye kuamini Utatu wanakubali kwamba neno “jina” katika Mathayo 28:19 halimaanishi jina la mtu. Mwanafunzi Mgiriki A. T. Robertson (Word Pictures in the New Testament, Vol. I, uk. 245) asema hivi: “Matumizi ya jina ([Kigiriki] onoma) hapa ni ya kawaida katika Septuagint na yanaonyesha uwezo au mamlaka.” Kwamba neno “jina” likitumiwa hivyo si lazima liwe la mtu, inaweza kuonyeshwa kwa mfano wa usemi wa Kiingereza “kwa jina la sheria.” Hakuna mtu anayefahamu Kiingereza atakayekata maneno kutokana na usemi huo kwamba sheria ni mtu. Usemi huo wamaanisha ‘kwa kutambua yanayowakilishwa na sheria,’ mamlaka yake. Vivyo hivyo, kubatizwa ‘kwa jina la roho’ kwamaanisha kutambua roho hiyo na chanzo chake na kazi zake.
NI “MSAIDIZI” SI MTU
Namna gani Biblia inapotaja roho kama “msaidizi,” “mfariji” au “mteteaji”? Je! huo si uhakikisho kamili kwamba roho ni mtu? Angalia:
Katika Yohana 16:7, 8, 13, Authorized Version yamtaja Yesu akisema: “Nisipoenda zangu, Mfariji [pa·raʹkle·tos] hatawajieni; lakini nikiondoka, nitampeleka kwenu. Naye ajapo, ataukaripia ulimwengu . . . wakati yeye, Roho wa kweli, ajapo, atawaongozeni mwingie katika kweli yote.”
Kuhusu kifungu hicho, New Catholic Encyclopedia (Vol. 13, kur. 575, 576) chasema: “Mt. Yohana aona wazi sana kwamba Roho ni mtu achukuaye mahali pa Kristo katika Kanisa, hata anatumia kijina cha kiume (masculine pronoun) [e·keiʹnos] anapotaja Roho ingawa [pneuʹma, roho] si neno la kike wala la kiume (16.8, 13-16). Kwa hiyo, ni wazi kwamba Mt. Yohana aliwaza Roho Mtakatifu ni Mtu, ambaye ni tofauti na Baba na Mwana, na ambaye yupo pamoja na waaminifu akifanya kazi ndani yao pamoja na Mwana aliyetukuzwa na pamoja na Baba (14. 16; 15.26; 16.7).”
Lakini je! Yohana alitumia kijina cha kiume bila kujali kwamba neno “roho” si la namna ya kiume wala ya kike? Je! kusudi lake lilikuwa kuonyesha kwamba roho ni mtu kweli? Sababu gani usirudie kusoma mtajo uliotangulia, uliotolewa katika Yohana sura ya 16? Anatumia neno “yeye” kuhusu nini? Je! halitumii kuhusu neno “Mfariji”? Naam, nalo neno la Kigiriki lililotafsiriwa hivyo ni pa·raʹkle·tos na limo katika hali ya kiume. Kwa haki basi, Yohana alitumia vijina vya hali ya kiume katika kifungu hicho kwa sababu alipaswa kufuata sarufi (grammar).
Walakini, Yohana hakutumia vijina vya kiume wakati neno pneuʹma (roho), lisilo katika hali ya kiume wala ya kike, lilipotangulia kutajwa. Hiyo yaweza kuonekana wazi kwa kusoma tafsiri zilizotafsiriwa neno kwa neno, kama ile ya Rotherham. Katika Yohana 14:16, 17, Rotherham atafsiri maneno ya Yesu ifuatavyo: “Mimi nitamwomba Baba, na Mteteaji Mwingine [pa·raʹkle·tos] yeye atawapa ninyi, ili yeye [wa kiume] apate kuwa pamoja nanyi kwa vizazi vyote,—Roho [pneuʹma] ya kweli,—ambayo ulimwengu hauwezi kuipokea, kwa sababu hauioni wala haupati kuijua. Lakini ninyi mnapata kuijua; kwa sababu pamoja nanyi inakaa, na ndani yenu imo.” Angalia kwamba anatumia neno “yeye” anapotaja jina pa·raʹkle·tos ambalo liko katika hali ya kiume, kisha anatumia neno “ambayo” (si ‘ambaye’) anapotaja jina pneuʹma lililotangulia.
Uchunguzi wa uangalifu wa vifungu vinavyotumiwa na wenye kuamini utatu hauungi mkono dai lao kwamba roho ni mtu (au nafsi), “nafsi ya tatu” ya Utatu wa Miungu.
Maandiko yote, yanaonyesha roho ya Mungu “si mtu,” bali na “kitu.”a
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate maelezo zaidi, tazama kijitabu “The Word”—Who Is He? According to John na Aid to Bible Understanding, kurasa 1541-1548.