Kuitambua Roho Takatifu
JE! WEWE ulijua kwamba roho takatifu inaathiri maisha ya kila mmoja wetu? Na je! ulijua kwamba inaweza kufanya maendeleo makubwa sana katika maisha yako? Huenda hilo likakushangaza. Kwa uhakika, huenda ukauliza hivi: ‘Roho takatifu ni nani au ni nini?’
Ikiwa wewe ni wa moja la makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, labda umesikia kasisi fulani akibatiza mtoto awe Mkristo “katika jina la Baba na Mwana na Roho Mtakatifu.” (Mathayo 28:19, The New English Bible) Wanapoombwa waitambulishe roho takatifu, makasisi walio wengi wanajibu haraka hivi: ‘Roho takatifu ndiye mtu wa tatu wa Utatu, ambaye katika njia zote yuko sawa na Mungu yule Baba na sawa na Bwana Yesu Kristo.’
Hata hivyo, maoni haya hayakushikiliwa katika karne chache za kwanza za Wakati wa Kawaida wetu. Kutoa kielezi: Katika 381 W.K.—karibu karne tatu baada ya kifo cha mitume wa Yesu Kristo—Gregori wa Nazianzo aliandika hivi: “Watu fulani wanachukua kwamba [roho takatifu] ni nguvu (energeia), kiumbe fulani, wengine wanachukua kwamba ni Mungu, wengine hawawezi kuamua ni jambo jipi kati ya haya.”
Leo, makanisa yaliyo mengi katika Jumuiya ya Wakristo yanakubali maoni ya Kiutatu juu ya roho takatifu. Lakini je! hivyo ndivyo Biblia inavyounga mkono? Au ni maoni tu yenye msingi wa mapokeo? Kwa kweli, Biblia haisemi kamwe juu ya roho takatifu kwa njia ile ile inavyosema juu ya Mungu au Yesu. Kwa mfano, katika Biblia, roho takatifu haina jina la kibinafsi.
Je! hilo ni jambo dogo tu lisilo na maana? Sivyo, majina ni ya maana katika Biblia. Mungu alikazia umaana wa jina lake mwenyewe aliposema hivi: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW]; ndilo jina langu; na utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu.” (Isaya 42:8) Umaana wa jina la Yesu Kristo ulikaziwa kabla ya kuzaliwa kwake wakati malaika alipomwambia Mariamu hivi: “Jina lake utamwita Yesu.” (Luka 1:31) Ikiwa majina ya Baba na Mwana ni ya maana sana, kwa nini roho takatifu haina jina la kibinafsi? Kwa uhakika, jambo hili pekee linapasa kufanya mtu ashangae akitaka kujua kama kweli roho iko sawa na Baba na Mwana.
Maandiko na Roho Takatifu
Katika Maandiko ya Kiebrania, au “Agano la Kale,” kuna marejezo kwa “roho takatifu” na kwa “roho yangu [ya Mungu].” (Zaburi 51:11; Yoeli 2:28, 29, NW) Tunasoma kwamba roho takatifu inaweza kujaa mtu, kuja juu yake, na kumfunika kabisa. (Kutoka 31:3; Waamuzi 3:10; 6:34) Kiasi fulani cha roho takatifu kinaweza kuchukuliwa kutoka kwa mtu mmoja na kupewa kwa mwingine. (Hesabu 11:17, 25) Roho takatifu inaweza kuwa yenye utendaji juu ya mtu fulani, ikimwezesha afanye ajabu zinazozidi uwezo wa kibinadamu.—Waamuzi 14:6; 1 Samweli 10:6.
Ni shauri gani linaloweza kukatwa kiakili kutokana na taarifa hizo? Kwa uhakika si kwamba roho takatifu ni mtu. Sehemu fulani ya mtu inawezaje kuchukuliwa kutoka kwa mtu mmoja na kupewa kwa mwingine? Zaidi ya hilo, hakuna ushuhuda kwamba Yesu alipokuwa duniani, Wayahudi waaminifu waliiona roho takatifu kuwa mtu aliye sawa na yule Baba. Kwa uhakika wao hawakuiabudu roho takatifu. Bali, ibada yao ilielekezwa kwa Yehova tu, yule Mmoja ambaye Yesu mwenyewe alimwita “Baba yangu” na “Mungu wangu.”—Yohana 20:17.
Kama lile linaloitwa eti Agano la Kale, sehemu ya Biblia inayoitwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya,” inasema kwamba roho takatifu inaweza ‘kujaa’ mtu au kuwa ‘juu’ yake. (Matendo 2:4; Luka 2:25-27, NW) Roho takatifu ‘ilipewa,’ ‘ikamiminwa juu ya,’ na ‘kugawanywa.’ (Luka 11:13; Matendo 10:45; Waebrania 2:4, NW) Kwenye Pentekoste 33 W.K., wanafunzi walipokea “kiasi fulani cha” roho ya Mungu. (Matendo 2:17, NW) Pia Maandiko yanasema juu ya ubatizo kwa roho takatifu na juu ya kupakwa mafuta kwa kutumia hiyo.—Mathayo 3:11; Matendo 1:5; 10:38, NW.
Taarifa hizo za Kibiblia zinathibitisha kwamba roho takatifu si mtu. Kukata shauri hivi kunahakikishwa kunafaa wakati tunapoona kwamba roho takatifu imeorodheshwa pamoja na vitu vingine visivyo na utu. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba Stefano ‘alijaa imani na roho takatifu. (Matendo 6:5) Na mtume Paulo alijipendekeza kuwa mhudumu wa Mungu “kwa utakato, kwa maarifa, kwa ustahimilivu, kwa fadhili, kwa roho takatifu, kwa upendo usio na unafiki.”—2 Wakorintho 6:4-6, NW.
Ni kweli, nyakati fulani Biblia inaitaja roho takatifu kama mtu. Kwa mfano, Isaya alisema kwamba waasi fulani ‘walifanya roho takatifu ya Mungu ihisi imeumizwa.’ (Isaya 63:10, NW) Paulo alisema ingeweza ‘kuhuzunishwa.’ (Waefeso 4:30) Na hesabu fulani ya maandiko inasema kwamba roho takatifu inafundisha, inaongoza, inasema, na kutoa ushahidi. (Yohana 14:26; 16:13, 14; 1 Yohana 5:7, 8) Lakini pia Biblia inataja vitu vingine visivyo hai kuwa mtu, kama vile hekima, kifo, na dhambi. (Mithali 1:20; Warumi 5:17, 21) Kwa kweli hii ni njia ya kupambanua wazi sana ambayo nyakati fulani Maandiko huwa yanaeleza mambo.
Leo, sisi huwa tunataja Biblia jinsi hiyo tunaposema kwamba inasema jambo fulani au kufundisha fundisho fulani. Kwa kutumia semi hizo, hatumaanishi kwamba Biblia ni mtu, sivyo? Wala Biblia haimaanishi kwamba roho takatifu ni mtu inapotumia maneno yanayolinganika na hayo.
Basi, roho takatifu ni nini? Si mtu. Bali, ni kani ya utendaji ya Mungu mwenyewe, inayotumiwa naye kutimiza mapenzi yake. (Mwanzo 1:2) Lakini ni jinsi gani maisha zetu zinavyoathiriwa na roho takatifu? Na ni jinsi gani tunaweza kunufaika zaidi kibinafsi kutokana na utendaji wayo?