Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 12/1 kur. 531-534
  • Sababu Kwa Nini Yesu Alitoa Mfano Wa “Wanawali Kumi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sababu Kwa Nini Yesu Alitoa Mfano Wa “Wanawali Kumi”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSUDI LA MFANO
  • ARUSI KATIKA NYAKATI ZA BIBLIA
  • SABABU KWA NINI NENO LA MFANO “WANAWALI” (BIKIRA) LINATUMIWA
  • WAKATI WA KUWA MACHO KULIKO ILIVYO KAWAIDA
  • Nuru ya Elimu Wakati wa “Umalizio wa Mfumo wa Mambo”
    Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
  • Wale Wanawali Wenye Hekima na Wapumbavu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Je, ‘Utaendelea Kukesha’?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Somo Kuhusu Kuwa Macho​—Mabikira
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 12/1 kur. 531-534

Sababu Kwa Nini Yesu Alitoa Mfano Wa “Wanawali Kumi”

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1. Yesu alijionyeshaje kuwa mwalimu mkuu?

MWALIMU bora ni yeye anayeweza kutoa mifano kwa njia ya kueleweka na nyepesi, anapofundisha uhakika au kanuni fulani ya maisha. Yesu Kristo alikiweka kielelezo bora kama mwalimu. Kwa hiyo, twamwona akifundisha kwa kutumia mifano hasa, mifano ya unabii yenye mambo au kanuni zenye kutumika za maisha. (Mt. 13:34, 35) Mna maana nyingi sana ndani yayo.

2. Mifano ina ubora gani?

2 Kwa kweli, mifano kama ile Yesu aliyoitumia, kwa kawaida ni yenye manufaa katika kuelewesha jambo fulani, kwa maana (1) inavuta kupendezwa na fikira, (2) inaamsha uwezo wa kuwaza, (3) inaamsha mawazo ya ndani na kuufikia moyo, (4) inalisaidia kumbukumbu, na (5) inaihifadhi kweli, kwa maana msingi wayo ni maisha na mambo ya asili, hali maneno matupu yanaweza kubadili maana.

3. Kwa sababu gani mafundisho ya Yesu si makuukuu au magumu kueleweka leo?

3 Kwa hiyo, mafundisho ya Yesu si makuukuu, nasi twaweza kuyaelewa na kufaidika sana nayo kana kwamba yalifundishwa wakati wetu, ijapokuwa alifundisha duniani zaidi ya miaka 1,900 iliyopita. Kwa kweli, mengi yayo yanatumika hasa katika siku zetu.

KUSUDI LA MFANO

4, 5. Ni nini kusudi la mfano wa “wanawali kumi”?

4 Mmojawapo wa mifano yenye kupendeza zaidi ya Yesu ni ule wa “wanawali kumi.” Huu pia ni wenye maana nyingi sana kwetu, hasa wakati huu. Kusudi lake lilikuwa nini? Ulitolewa uwasaidie Wakristo, hasa Wakristo wanaoishi leo, wafahamu kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme.

5 Mitume wa Yesu walikuwa wamemwuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” (Mt. 24:3, NW) Kwa kujibu, alitaja matukio mengi, kutia na mifano kadha, iliyomo katika Mathayo sura za 24 na 25. Mambo hayo yote aliyoyataja ni sehemu zinazoifanyiza ishara kubwa ya kuwapo kwake kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme.

6. Zaidi ya kuwasaidia tu wanafunzi wa Yesu wafahamu kuwapo kwake kusikoonekana, ni mambo gani mengine unayowafanyia?

6 Mfano wa Yesu wa “wanawali kumi,” ulioandikwa katika Mathayo 25:1-12, haukutolewa kusudi tu wanafunzi wake wanaoishi duniani wakati wa kuja kwake mara ya pili wakufahamu kuwapo kwake. Zaidi ya hayo, Yesu aliukusudia mfano kuwaonyesha haja ya kuwa macho wasije wakakosa kufahamu, kama vile Mafarisayo wakati wa kuja mara ya kwanza kwa Yesu. Pia, mfano huu unaonyesha madaraka na wajibu ambao wanafunzi wa Kristo wangekuwa nao wakati wa kuwapo kwake kama Mfalme. (Zab. 110:3) Yesu aliwataka wote ambao Mungu alikuwa amewapa “mwito wa mbinguni” waendelee kuwa waaminifu na kuupata ule mradi mzuri ajabu wa kuwa warithi wenzake katika Ufalme.​—Ebr. 3:1; Rum. 8:17; Ufu. 20:4, 6.

ARUSI KATIKA NYAKATI ZA BIBLIA

7, 8. Simulia kujitayarisha kwa bibi-arusi wa Kiisraeli siku ya arusi yake.

7 Kwa kuwa mfano wa “wanawali kumi” unatia na karamu ya arusi, itasaidia kuangalia masimulizi mafupi ya desturi zilizofuatwa arusini wakati ambao Yesu aliutoa mfano.

8 Ijapokuwa ni wazi kwamba arusi yenyewe haikuwa na sherehe za upuzi, hata hivyo ulikuwako mwadhimisho wenye shangwe nyingi wa arusi katika Israeli. Siku ya arusi, bibi-arusi kwa kawaida alijitayarisha sana nyumbani kwao. Alijitayarisha kwa ndoa kwa kujipamba mavazi yake yaliyo bora, na vito vya thamani. Katika nyakati hizo za kale alivaa pia utaji wa namna fulani uliofunika kichwa na, nyakati nyingine, ukafika miguuni. (Yer. 2:32; Isa. 3:19, 23; 49:18) Kifuniko hiki cha kichwani kilifananisha unyenyekevu wa bibi-arusi kwa bwana-arusi wake.​—Mwa. 24:65; 1 Kor. 11:5-10.

9, 10. (a) Bwana-arusi alijitayarishaje? (b) Simulia maandamano ya arusi, na uonyeshe sababu gani kulikuwa na haja ya kuwa macho kwa upande wa wale wenye kungojea njiani.

9 Akiwa vile vile amevaa mavazi yake bora, bwana-arusi alikuwa akiondoka nyumbani kwao jioni kuelekea kwenye nyumba ya wazazi wa bibi-arusi, akisindikizwa na rafiki zake. Kutoka hapo maandamano yaliendelea kutoka nyumbani kwa bwana-arusi au nyumba ya baba yake, yakifuatana na wapiga muziki au waimbaji na kwa kawaida na watu wenye taa.

10 Watu waliokuwa wakielekea njia hiyo walikuwa wakipendezwa sana na maandamano. Wengine walikuwa wakijiunga na maandamano, hasa wanawali wenye taa, wakiimulika njia na kuongeza uzuri wa mwadhimisho. (Yer. 7:34; 16:9; Isa. 62:5) Kwa kuwa hakukuwa na haja ya haraka, iliwezekana bwana-arusi akae sana nyumbani kwao na, halafu tena, iliwezekana maandamano yakae kidogo kabla ya kuondoka nyumbani kwa bibi-arusi, hata, kukawa usiku sana, na watu wengine waliokuwa wakingojea njiani waliweza kusinzia na kulala. Kuimba na kushangilia kungeweza kusikiwa kwa mbali, huku wale waliokusikia wakiwa hawajalala wakipaza sauti: ‘Haya, bwana arusi.’ Watumishi walikuwa tayari kumlaki bwana-arusi, nao wale walioalikwa kwenye chakula cha jioni walikuwa wakiingia nyumbani pamoja naye. Baada ya bwana-arusi na wafuasi wake kuingia nyumbani mwake na kufunga mlango, kulikuwa kuchelewa mno kwa wageni wazembe kuingia.​—Mwa. 29:22; Mt. 22:1-3, 8.

11, 12. Usimulie mfano wa “wanawali kumi” kwa maneno yako mwenyewe, ukieleza mambo makuu.

11 Tunapouangalia mfano huu, twauona namna ulivyoifaa njia ya maisha ya wakati huo. Unasema hivi, kama ulivyoandikwa katika Mathayo 25:1-12:

12 “Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara. Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaa taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi. Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, ‘Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki.’ Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, ‘Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika.’ Lakini wale wenye busara wakawajibu, wakisema, ‘Sivyo, hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kwa wauzao, mkajinunulie.’ Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa. Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie. Akajibu akasema, Amin, nawaambia, siwajui ninyi.”

SABABU KWA NINI NENO LA MFANO “WANAWALI” (BIKIRA) LINATUMIWA

13. Kwa sababu gani Yesu hakumtaja bibi-arusi katika mfano huu?

13 Alipokuwa akiusimulia mfano huu, Yesu hakumtaja bibi-arusi. Kwa sababu gani? Kwa sababu alitaka kukazia hali fulani za madaraka ya “ndugu” zake waliotiwa mafuta na kuzaliwa kwa roho walipokuwa wangali duniani na kabla ya kuunganishwa naye kwa ufufuo kuingia mbinguni. Hakutaka kuvuruga ufahamu wa matumizi ya mfano huo. Kwa hiyo aliufupiza mfano huu uwafananishe wao, si kama “bibi-arusi,” bali kama “wanawali kumi.”

14. Toa sababu kwa nini ililifaa kusudi la Yesu, katika mfano huu, kuwataja “ndugu” zake kama “wanawali” badala ya “bibi-arusi.”

14 Wanapokuwa duniani watiwa mafuta hao wanahesabiwa kama ‘walioposewa’ Kristo, kama wanawali safi. (2 Kor. 11:2, 3) Wachache waliobaki wa jamii hii ya watu duniani sasa ‘wanaalikwa karamu ya arusi ya Mwana-Kondoo.’ (Ufu. 19:9) Ndoa yenyewe inatokea mbinguni. Wao wangali hawajaupata urithi wa kimbinguni. Jamii ya “bibi-arusi” inachaguliwa kati ya “wanawali kumi.” Kama vile mfano unavyoonyesha, si wote wanaojihakikisha kuwa wenye busara. Wengine ni wapumbavu. Neno “bibi-arusi” linatumiwa kwa warithi wenzi wa Kristo kama kundi na kama jamii ya kimbinguni ya watu wenye kufikia hesabu ya 144,000 mwishowe. Kama watu mmoja mmoja, wawe ni wanaume au wanawake, wanaitwa kwa njia mbalimbali “watoto wa Mungu,” “ndugu” za Kristo na “bikira.”​—1 Yohana 3:2; Mt. 25:40; Ufu. 14:1, 4; Gal. 3:28.

15. Ni kwa njia gani waliotiwa mafuta walivyo “bikira” (“wanawali”)?

15 Ni kwa njia gani walivyo “bikira”? Biblia inaeleza. Kwa habari ya wale 144,000, wanaoonekana wamesimama pamoja na Mwana-Kondoo wa Mungu juu ya Mlima Sayuni wa kiroho, inasema hivi: “Hawa ndio wasiotiwa unajisi pamoja na wanawake [kama vile kahaba wa kidini Babeli Mkuu, na binti zake], kwa maana ni bikira. Hawa ndio wamfuatao Mwana-Kondoo kila aendako.” (Ufu. 14:4; 17:3-5) Baada ya kuwa waliozaliwa kwa roho, wenye tumaini la kutawala pamoja na Kristo mbinguni, hawafanyi “uzinzi” wa kiroho na ulimwengu huu. Kwa hiyo, Wakristo hawa hawajitii unajisi na taratibu ya kidini wala ya kisiasa ya ulimwengu huu. Hawajitii kwa njia yo yote katika siasa wala shughuli za serikali za kibinadamu.​—2 Tim. 2:3, 4.

16. Kwa sababu gani hawa Wakristo waliotiwa mafuta hawajaribu kuwa rafiki za ulimwengu?

16 Cheo cha Wakristo hawa “bikira” kilionyeshwa waziwazi na mtume Paulo alipoandika hivi: “Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo; atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake.” (Flp. 3:20, 21) Wakristo hawa ni rafiki za watu, wanaowatembelea katika nyumba zao wakiwa na habari njema za Ufalme. Lakini wao si rafiki za ulimwengu, yaani, za taratibu ya mambo ya ulimwengu huu. Biblia inawakemea vikali wale Wakristo wa kujidai wanaojifanya rafiki za ulimwengu, ikisema: “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”​—Yak. 4:4; 1:27.

17. Wakristo hawa ni kama msichana aliyeposwa katika Israeli ya kale kwa njia gani?

17 Kwa hiyo wale wanaopokea “mwito wa mbinguni” kutoka kwa Mungu lazima ‘wafanye imara kuitwa kwao na uteule wao.’ (2 Pet. 1:10, 11) Wanatamani kupokea muhuri ya Mungu ya kukubaliwa kabisa kabla Mungu hajaziamuru “pepo nne” ziiharibu hii taratibu ya mambo. (Ufu. 7:1-8) Hii inahitaji kujitoa kwa uaminifu kwa upande wao, “wafananishwe na mfano wa Mwana wake [Mungu].” (Rum. 8:29) Hivyo, wako kama vile bikira aliyeposwa katika Israeli, anayetaka kuendelea kuwa safi na bila ya kutiwa unajisi. Wanapokuwa duniani sasa wanaunyenyekea ukichwa wa Yeye ambaye amewaposa, wakitazamia kutukuzwa kama “bibi-arusi” wao mbinguni. (Kol. 1:18) Katika Israeli ya kale bikira aliyeposwa aliyefanya uasherati na mwanamume mwingine alihesabiwa kuwa mzinzi na kuuawa. (Kum. 22:23, 24) Vivyo hivyo, wasioaminika watapoteza tumaini la uzima wa kimbinguni wa hawa “bikira” waliochumbiwa.​—Ufu. 21:7, 8.

WAKATI WA KUWA MACHO KULIKO ILIVYO KAWAIDA

18. Mtume Paulo anaionyeshaje haja ya kuwa macho, hasa wakati huu?

18 Kwa hiyo, katika wakati huu wa kujitahidi, kuna haja ya kuwa macho namna isivyo kawaida. Mtume Paulo anawaambia hao hivi: “Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie. Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. Wakati wasemapo, ‘Kuna amani na salama,’ ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa. Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi. Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa nuru, na wana wa mchana; sisi si wa usiku, wala wa giza. Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe.”​—1 The. 5:1-6.

19. Mkristo mzembe anaweza kujikuta katika hali gani?

19 Kwa hiyo ungekuwa msiba, hasa wakati huu, kwa ye yote wa hawa kulala kwa kiroho, kuwa baridi au mzembe. Wakifuata mazoea ya kilimwengu, au walegee katika kuuhubiri Ufalme, wanaweza kujikuta katika hali ya ‘mtumwa mbaya.’ Yesu alisema kwamba, huyo akianza kuwaza kwamba, “Bwana wangu anakawia; akaanza kuwapiga wajoli wake, na kula na kunywa pamoja na walevi; bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani. . . atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wanafiki.” (Mt. 24:48-51) Huu sio wakati wa kushirikiana na “walevi” wa kiroho. Ye yote wa “bikira” hawa waliochumbiwa na Kristo akiishi sasa au kusema kwa njia ya wale wanaoziunga mkono taratibu za kidini za “Babeli mkuu,” milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, anajionyesha kuwa mlevi pamoja na hii taratibu yenye mfano wa kahaba naye ‘atapokea mapigo yake.’​—Ufu. 17:1, 2, 6; 18:4.

20. Ni habari gani zaidi juu ya mfano wa “wanawali kumi” tuwezazo kutazamia?

20 Kwa hiyo twaona kwamba mfano wa Yesu wa “wanawali kumi” unatoa onyo kali. Lakini mna maana zaidi katika mfano huu. Mfano huu unatoaje uongozi imara kwa watu wa Mungu leo? Nini maana ya “taa,” “mafuta,” na vitu vingine vya mfano? Mambo haya yatazungumzwa katika sehemu ya pili ya makala hizi katika toleo hili.

​—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki