Wewe Utakuwa Hai Uone “Kuja” kwa Kristo?
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. Mara nyingi watu wanaonaje kuja kwa Kristo kuhukumu dunia kunapotajwa?
SISI sote tumesikia mara nyingi kwamba Kristo atakuja tena aihukumu dunia, awaharibu waovu na kuwapa thawabu wema.
2 Lakini jambo lenye hatari kubwa linapotajwa, ni kawaida ya kibinadamu kufikiri, ‘Haliwezi kunipata mimi.’ Kwa hiyo, wengi wajidaio kuamini kuja kwa Kristo wanakubali kwamba lazima kutukie wakati watu fulani watakapokuwa wakiishi. Lakini wanasema, ‘Hakutatukia katika wakati wangu.’
3. Watu hao wasioamini wanasahau nini?
3 Watu hawa wanausahau uhakika wa kwamba Yesu Kristo alisema kungekuwa na ushuhuda wa kutosha wakati huo ukaribiapo. Zaidi ya hilo, ingehitaji imani kukubali kukaribia kwa wakati huo—wakati wa kuja kwake kufanya hesabu na wakaaji wa dunia. Ingehitaji moyo mnyofu, pamoja na kuwa macho kuona unabii mbalimbali wa Biblia na matukio ya ulimwengu. Yesu alituamsha kwa ulizo lake: “Atakapokuja Mwana wa Adamu, je! ataiona imani duniani?”—Luka 18:8.
4. Je! watu walio hai leo watakuona “kuja” kwa Kristo?
4 Yajapokuwa mashaka ya watu wengi sana, yaweza kusemwa kutokana na aliyosema, Yesu juu ya kuja kwake kwamba watu wengi wanaosoma makala hii, na mamilioni ya wengine, watakuwa hai walione tukio hilo lenye kutikisa dunia. Kwa sababu gani hivyo?
NI WAZI KWA MUNGU LAKINI MWANADAMU HAWEZI KUHESABU
5. Ni mambo gani yaonyeshayo kwamba Mungu ameweka wakati barabara wa kuja kwa Kristo kufikiliza hukumu?
5 Ni wazi kwamba Mungu ana wakati barabara wa kuja kwa Kristo kufikiliza hukumu juu ya dunia. Mwanadamu ambaye alifanywa kwa mfano wa Mungu ana akili ya kuwekea mambo wakati. Kwa hiyo Mungu alitoa njia ili mwanadamu aweke hesabu ya miaka, miezi na siku. (Mwa. 1:14-16) Orodha sahihi ya tarehe tangu kuumbwa kwa mwanadamu na kuendelea imewekwa katika Biblia. Mfano mzuri sana wa orodha hiyo ya tarehe ni hesabu ya Biblia ya “nyakati saba” za utawala wa Mataifa juu ya wanadamu bila ya kukatizwa kwa kimungu, zilizoanza mwaka wa 607 B.C.E. kufika mwaka wa 1914 C.E. Hesabu hii ilikuwa hata na asili ya unabii. Ilikuwa orodha ya mapema ya tarehe.a
6. Kwa kuwa Mungu ametupa akili ya kuweka wakati na orodha nyingi za tarehe, twaweza kutazamia kuhesabu wakati wa “siku” ya “kuja” kwa Kristo?
6 Lakini ye yote asiwe na wazo la kwamba, aweza kuhesabu wakati wa “kuja” huko kwa Kristo kufikiliza hukumu kwa kutumia orodha ya tarehe tu. Kristo mwenyewe aliwaambia mitume wake hivi: “Habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.”—Mt. 24:36.
7. Twawezaje kuwa na hakika kwamba hakuna mwanadamu leo awezaye kujua wakati barabara wa hukumu juu ya ulimwengu huu?
7 Sasa, twajua kwamba Yesu Kristo alikuwa amekuwako mbinguni pamoja na Baba yake wakati wa kuumbwa kwa dunia. (Yohana 1:1-3; Kol. 1:13-17) Alijua wakati barabara wa kuumbwa kwa Adamu na Hawa pia. (Mwa. 1:26, 27) Alijua wakati hasa miaka 6,000 ya historia ya mwanadamu ingemalizika. Alijua barabara wakati siku ya saba ya Mungu, siku yake kuu ya pumziko, ingeanza na wakati ingemalizika. (Mwa. 2:1-3) Lakini, akiwa na maarifa yake yote kamili juu ya orodha ya tarehe, alipokuwa duniani yeye hakuijua siku wala saa ya kufikiliza kwake hukumu juu ya ulimwengu huu, kabla ya utawala wake wa miaka elfu kuanza. (Ufu. 20:4-6) Basi, ni kwa njia gani mwanadamu mwingine ye yote leo awezavyo kujua?
“KAMA ILIVYOKUWA SIKU ZA NUHU”
8. Ikiwa hakuna mwanadamu angeweza kuhesabu wakati wa tukio hili, kwa sababu gani Yesu akatoa habari zake?
8 Walakini, Yesu hakutaja kisa hicho cha wazi bure. Katika sehemu ya kwanza ya maelezo yake (katika Mathayo 24:4-35) alisema kwa unabii hali nyingi za ulimwengu zingetokea ambazo zingekuwa kama onyo kwamba alikuwa karibu kuchukua hatua, naye alishauri tuwe macho juu ya tukio hili, akisema hivi: “Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.”—Mt. 24:37-39.
9. Yesu alikuwa akimaanisha kipindi gani cha wakati alipozungumza juu ya “siku za Nuhu,” na je! wakati huo watu walipewa onyo?
9 Hapa Yesu, alipokuwa akitaja “siku za Nuhu,” kwa wazi alimaanisha kipindi cha wakati ambacho Nuhu alijenga safina. Safina ilikuwa kitu walichopaswa kutambua watu, lakini wao waliendelea kulipuza onyo lililotolewa kwa kimungu.
10. Imetupasa tutazamie nini leo, kulingana na maneno ya Yesu juu ya siku za Nuhu?
10 Kulingana na unabii wa Yesu, hali za kijamii kati ya wanaume na wanawake duniani, pamoja na mambo mengine aliyoyazungumza Yesu, ni onyo kwa watu wote leo. Usahihi wa unabii huu waonyeshwa wazi zaidi kwa kusoma masimulizi yanayolingana na haya katika Marko sura ya 13 na Luka sura ya 21, pamoja na njozi ya Yohana inayosimuliwa katika Ufunuo sura ya 6.b
11. (a) Je! kuna uwezekano wa kwamba watu walio hai leo wataiona “siku” hiyo? (b) Ni kipindi gani cha wakati kinachozungumzwa na Yesu kama “kuwapo” kwake, nacho chatofautianaje na “kuja” kwake katika maana ambayo alitumia neno hilo katika Mathayo sura ya 24?
11 Mambo haya yaonyesha nini juu ya uwezekano wa kwamba watu walio hai sasa wataona, ndiyo, hata waishi baada ya “siku ile na saa ile”? Hivi: Wengine, ingawa wachache tu, walitii onyo la Mungu, wakaiona Gharika na wakaokolewa nayo. Kwa hiyo leo, watu wanalisikia onyo na wengi wao, ingawa wachache wakilinganishwa na idadi ya watu wa dunia, watasikia na kuokoka. (Ufu. 7:9-17) Yesu alikitaja kipindi hiki (katika Mathayo 24:36-39 iliyotajwa juu) tangu mwisho wa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914 C.E. kama “kuwapo” (NW) kwake. Wakati huu angeikagua dunia kwa kutoonekana. Pia angeongoza kazi ya kuonya watu na kuwakusanya pamoja wasiodhihaki, watiio na kuonyesha imani. Ndipo ‘angekuja’ akiwa na uwezo wa kuharibu adui za Mungu. Sasa onyo hili linatolewa kweli kwa kinywa, kwa kuhubiriwa kwa habari njema hizi za Ufalme duniani pote.—Mt. 24:14.
12. Onyesha urefu wa kipindi ambacho watu walipata nafasi ya kupokea onyo juu ya Gharika ulikuwa karibu wakati gani.
12 Kwa habari ya “kuwapo” kwa Yesu kabla ‘hajaja’ kuiharibu taratibu hii ya mambo, ufikirie urefu wa kipindi ambacho Nuhu aliijenga safina. Alikuwa mwenye umri wa miaka 500 alipoanza kupata wana. (Mwa. 5:32) Wana hawa watatu wote walikua na kuoa, wakati huo Nuhu akiwa karibu na umri wa miaka 550. Wakati huo Mungu alimpa maagizo ajenge safina. (Mwa. 6:18) Gharika ilitokea Nuhu alipokuwa mwenye umri wa miaka 600. (Mwa. 7:6) Hii ingeruhusu iwepo miaka 50 hivi kama kipindi kilichotangulia Gharika, ambacho katika hicho watu wangeweza kuangalia na kufuata onyo. Lakini watu walishughulika mno na mambo ya kila siku ya maisha, wasionyeshe imani yo yote katika ujumbe wa Nuhu uliotoka kwa Mungu.
HAKUNA TAREHE YA MAPEMA ITAKAYOTOLEWA
13. Je! uhakika wa kwamba Mungu alimpasha Nuhu habari mapema kwamba Gharika ingekuja siku fulani unahakikisha kwamba tutapokea onyo la mapema juu ya wakati barabara wa kufikiliza kwa Kristo hukumu juu ya dunia?
13 Wakati wa Nuhu yeye aliambiwa juma moja kabla ya maji ya gharika kuanguka, aingize namna za wanyama mbalimbali zilizopaswa kuhifadhiwa. (Mwa. 7:1-16) Lakini hii haihakikishi kwamba kungekuwa na onyo la mapema katika wakati wetu juu ya siku barabara ya “kuja” kwa Kristo kuiharibu taratibu hii ya mambo. Huko nyuma kwa wazi Nuhu alipaswa ajue ni wakati gani angeanza kuingiza wanyama katika mahali pa usalama. Kama angewaingiza upesi mno, pengine wakati ambapo yeye alidhani mwisho ulikuwa karibu sana, hii ingeleta hasara isiyofaa juu ya akiba ya chakula alichokuwa ameweka safinani. Kwa upande mwingine, kama gharika ingekuja kwa ghafula bila ya kujulikana, Nuhu asingaliweza kuwakusanya wanyama safinani mapema. Onyo la mapema ambalo Mungu alimpa lilikuwa fupi sana, lakini la lazima, na lenye kutosha kutimiza kusudi la Mungu.
14. Yesu alionyeshaje kwamba Wakristo wa kweli wasingejua mapema wakati barabara wa “kuja” kwake?
14 Kwamba wanafunzi wa Yesu Kristo pia, Wakristo wa kweli duniani, watakuwa hawajui mapema wakati barabara wa “kuja” kwa Kristo katika maana ya kuua yaonyeshwa kwa aliyoyasema kama yalivyoandikwa katika Mathayo 24:42-44. Angalia kwamba maneno haya hayakuelekezwa kwa ulimwengu kwa ujumla. Yalielekezwa moja kwa moja kwa wanafunzi wa Kristo: “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu. Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa. Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.”
KUTOKUJUA SIKU ILE KWAFANYIZA JARIBU
15. Kwa sababu gani Mungu anaacha Wakristo leo bila kujua wakati barabara wa “kuja” kwa Kristo?
15 Ni nini kusudi la Mungu kwa kuwaacha Wakristo bila ya kujua wakati bara bara wa kuja kwa Bwana Yesu Kristo kufikiliza kisasi cha Yehova? Ni kuhitaji wote wajidaio kuwa wanafunzi wa Kristo wahakikishe kama wao ni Wakristo wa kweli wakati wote. Hawawezi kuwa wazembe na kujishughulisha na mambo na mazoea ya kilimwengu halafu, kabla tu ya dakika ya mwisho, wavae namna ya uchaji wa Mungu. Bila shaka, hawawezi kumdanganya Yesu Kristo kwa mwendo huo. Lakini Mungu ataka watu wote wafahamu wazi kwamba kuna tofauti ya wazi kabisa kati ya wale wamtumikiao Mungu kweli na wale wasiofanya hivyo. (Mal. 3:18) Wanahakikisha walivyo moyoni kwa matunda yao.—Mt. 7:17-20.
16. Eleza maneno ya Yesu: “Mmoja atwaliwa, mmoja aachwa.”
16 Kulingana na mambo haya yote ya hakika, pamoja na maneno ya unabii ya Yesu, mamilioni ya watu walio hai sasa wataiona “siku” ya kuja kwa Kristo kutoa hukumu juu ya taratibu hii ya mambo, ya kidini, ya kisiasa, ya kibiashara na ya kijamii. Lakini kuokoka kufikilizwa kwa hukumu hiyo ni jambo tofauti. Yesu alisema hivi: Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa; wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa.’ (Mt. 24:40, 41) Juma nyingi mapema Yesu alikuwa amesema maneno yanayofanana na hayo, yakiongoza wanafunzi waulize, “Wapi, Bwana?” Akajibu, “Ulipo mzoga, ndipo watakapokutanika tai.” (Luka 17:37) ‘Wanaotwaliwa’ ni wenye busara nyingi, kama tai, wakusanyikao kwa yeye wamfahamuye kuwa Masihi, wapate kula karamu ya kiroho atayarishayo Yehova ndani ya mahali pake pa usalama. Watakusanyika pamoja na makundi ya Mungu duniani, chini ya Masihi wake wa kweli. Wale ‘watakaoachwa’ watakuwa wale wasiokesha kiroho na ambao kwa njia hiyo wanatiwa ndani ya njia ya kichoyo ya maisha, kama vile watu wa siku za Nuhu. Hao ‘wanaachiwa’ uharibifu pamoja na taratibu ya mambo ya ulimwengu ambamo wamejitia.
17. Ni nini kinachohitajiwa ili kuokoka kufikilizwa kwa hukumu kunakoianzisha “siku” hiyo?
17 Ndiyo, ili kuiokoka kazi ya kuua itakayoanza “siku” hiyo imani yahitajiwa. Hii yaweza kupatikana kwa kujifunza Biblia tu. Lazima ‘tukeshe’ tuone kwamba matendo yetu yana msingi wa kanuni za haki za Biblia, tukijua kwamba kwa hakika siku hiyo ya kuanza kwa kazi ya kuua inakuja, kwa kweli, i karibu. (Hab. 2:3) Hatuwi wazembe kwa “kukumbuka kukaribia kwa kuwapo kwa siku ya Yehova,” wakati wa Mungu wa kutoa hukumu. Twaacha sehemu zote za maisha zetu ziongozwe kiroho ili tuweze ‘kupatikana naye mwishowe bila doa na lawama na katika amani.’—2 Pet. 3:12-14, NW.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama kitabu Is This Life All There Is?, kilichochapwa na Watchtower Bible and Tract Society, mwaka wa 1974.
b Kwa mazungumzo kamili ya sura nzima ya Mathayo 24, tazama kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.