Kulindwa na Imani na Tumaini
“[Kristo] alifunuliwa . . . hata imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu.”—1 Pet. 1:20, 21.
1. Ulizo la kama uzima ndio uu huu tu linahusuje watu?
JE! UZIMA ndio uu huu tu? Ulizo hilo linahusu kila mtu aliye hai leo. Ni ulizo linalofadhaisha watu wengi, na jibu ambalo mtu anakubali linaongoza sana maisha yake. Kila mwaka makumi ya maelfu ya watu wanaona kwamba jibu lifaalo linawaletea furaha ya kweli na kutoa uongozi wenye kusudi kwa maisha yao. Kwa upande mwingine, kwa sababu ya kukubali majibu mabaya, mamilioni na mamilioni ya watu wanatumiwa na wenzao kwa faida zao wenyewe nao wanaishi maisha zisizoleta uradhi mwingi.
2. Kwa sababu gani maoni ya mwenye kuamini mwanadamu alitokea kwa mageuzi hayaridhishi?
2 Mfikirie anayeamini mwanadamu alitokea kwa mageuzi. Kwake huyo, uzima ndio uu huu tu. Lakini hilo lamwacha akiwa na nini? Mageuzi hayawezi kueleza kwa sababu gani hali za ulimwengu zinazidi kuwa mbaya wala hayawezi kutoa ufumbuzi wa magumu ya maisha ambayo lazima ayakabili. Naye bana tumaini la wakati ujao. Mageuzi yanamtolea yeye kama mtu tumaini la mwishowe tu la kuwa mfu milele.
3, 4. Ni nini kinachoonyesha kwamba watu wengi wenye kujidai kuwa wanadini hawana imani na tumaini la kweli?
3 Namna gani juu ya washiriki wa matengenezo ya kidini wasiofundisha Neno la Mungu au wanaosingizia tu kufanya hivyo? Je! wao ni afadhali? Je! wana imani ya kweli na tumaini lenye msingi mzuri? Kama mjuavyo, watu wengi wanaojidai kuwa wanadini wanafuatia sana mali za kimwili kama wale wasiojidai kuwa na dini yo yote. Wao wanaishi kwa ajili ya leo tu, wakijitahidi kujipatia riziki, kupata vitu vya starehe na kukaa kwa starehe. Hi kufikia mradi wao, huenda wakakosa kufuata kanuni, wakakosa kujali hali njema ya wanadamu wenzao na, kama matokeo, kupatwa na maumivu makali ya dhamiri inayosumbuka. Kwa kweli washiriki wengi wa matengenezo haya hawaamini yanayofundishwa na dini yao. Lakini wanafuatana na mapokeo, wasitake kuwa tofauti na jirani zao. Hata wanalipa pesa zilizochumwa kwa jasho kwa ajili ya sherehe zilizo sehemu ya dini hiyo, lakini wasizoamini zina ubora wo wote.
4 Lakini namna gani ikiwa sivyo mtu alivyo? Namna gani ikiwa yeye anaiamini dini yake kweli naye anapatanisha matumaini yako nayo? Hata hivyo, kuna faida gani kama hakufundishwa kweli? Bila kujua, anajenga maisha yake yote juu ya uongo, na hii itamkatisha tamaa baadaye.
5. Ni nini hali ya wale ambao imani na tumaini lao lina msingi imara wa Biblia?
5 Ni kweli peke yake, kama ilivyowekwa katika Neno la Mungu, iwezayo kufaidi wanadamu milele. Neno hilo linatoa msingi wa imani ya kweli. (Linganisha Warumi 10:5-15.) Halitii moyo nia ya kuamini hata ushuhuda usipokuwapo. Bali, linatoa ushuhuda wa kutosha kama msingi wa imani ya mtu. Kama matokeo, Wakristo wa kweli wanajua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli, kwamba Biblia ndilo Neno lake, na kwamba tumaini lenye msingi wa ahadi zake halitakosa kutimizwa wakati wo wote. (Yos. 21:45) Wanasadikishwa kwamba, sawa na alivyoahidi, Mungu ataiharibu taratibu mbovu iliyopo karibuni na kuigeuza dunia hii iwe paradiso ya kupendeza. (Ufu. 11:18; 21:3, 4) Wanaamini sana kwamba ufalme wake kupitia kwa Mwanawe utawafufua wafu na kusaidia watiifu wafikie ukamilifu. (Yohana 5:26-29) Wanasadiki kwamba hata sasa Mungu anawaangalia watumishi wake. (1 Pet. 5:6, 7) Kusadiki huku, kwenye msingi wa Neno la Mungu, ndiko kunakolinda watumishi waaminifu wa Yehova na migogoro ya maisha yasiyo na imani na tumaini.
KULINDWA NA UTAFUTAJI WA MALI ZA KIMWILI
6. Kwa sababu gani imewapasa watumishi wa Yehova wasichukue imani na tumaini lao vivi hivi tu kama inavyoonyeshwa katika habari ya Asafu?
6 Lakini, ingawa Wakristo wa kweli wana imani hiyo na tumaini hilo, hawawezi kusahau uhakika wa kwamba, wakiwa wazembe, maoni ya ulimwengu ya kutafuta mali za kimwili yanaweza kuwaambukia. Imani yao inaweza kudhoofika na tumaini lao kufifia. Hili ndilo lililompata mtu aliyeitwa Asafu aliyeishi karne nyingi zilizopita. Aliona kwamba nia yake juu ya ufanisi wa waovu ilikuwa imemwondolea furaha. Kwa habari ya mawazo yake ya ndani, Asafu aliandika hivi:
“Nami miguu yangu ilikuwa karibu na kupotoka, hatua zangu zilikuwa karibu na kuteleza. Maana naliwaonea wivu wenye kujivuna, nilipoiona hali ya amani ya wasio haki. Maana hawana maumivu katika kufa kwao, na mwili wao una nguvu. Katika taabu ya watu hawamo, wala hawapati mapigo pamoja na wanadamu. Hivyo kiburi kimekuwa mkufu shingoni mwao, jeuri huwavika kama nguo. Macho yao hutokeza kwa kunenepa, wameipita kadiri ya mawazo ya mioyo yao. Hudhihaki, husimulia mabaya, husimulia udhalimu kana kwamba wako juu. Wameweka kinywa chao mbinguni, na ulimi wao hutanga-tanga duniani. Nao husema, Mungu ajuaje? Yako maarifa kwake aliye juu? Fahamu, ndivyo walivyo wasio haki, na kwa kustarehe sikuzote wamepata mali nyingi. Hakika nimejisafisha moyo wangu bure, nimenawa mikono yangu kwa kutokukosa.”—Zab. 73:2-9, 11-13.
7, 8. (a) Kulikuwa na ubaya gani kwa kuwaza kwa Asafu? (b) Ni nini chanzo halisi cha furaha?
7 Kuwaza kwa Asafu kulikuwa hatari. Alikuwa amesahau kwamba furaha ya kweli na uradhi hauji kupitia kwa ufanisi wa mali za kimwili tu. Yeye kwa kweli alikuwa akiwaza kama wale ambao hawakuwa wakimtumikia Yehova Mungu. Kama vile yeye mwenyewe alivyosema, “Ndivyo walivyo wasio haki.”—Zab. 73:12.
8 Ubaya wa kuwaza kwa Asafu watiliwa mkazo zaidi katika Zaburi 144. Katika zaburi hii Daudi aonyesha waovu wakiyataja mawazo yafuatayo: “Wana wetu na wawe kama miche waliokua ujanani. Binti zetu kama nguzo za pembeni zilizonakishwa kwa kupamba hekalu. Ghala zetu na zijae zenye akiba za jinsi zote. Kondoo zetu na wazae elfu na makumi elfu mashambani mwetu. Ng’ombe zetu na wachukue mizigo, kusiwe na kushambuliwa. Wala kusiwe na kuhamishwa, wala malalamiko katika njia zetu. Heri watu wenye hali hiyo.” Hivyo ndivyo ingeelekea kuwa. Lakini je! ufanisi wa mali za kimwili tu ndicho chanzo cha furaha? Sivyo; mali zenyewe peke yazo zaweza kuacha maisha yakiwa matupu na yasiyo na maana. Furaha ya kweli iko mahali pengine. Katika sehemu ya mwisho ya mstari wa 15 Daudi aonyesha msemaji mwingine akianza kusema; humo Daudi aonyesha kwa kufaa kinacholeta furaha ya kweli, akisema, “Heri watu wenye [Yehova] kuwa Mungu wao.” (Zab. 144:12-15) Je! hivyo ndivyo wewe unavyoyaona maisha? Bila shaka, uhusiano mwema na Muumba unaleta furaha ya kweli.
9. (a) Ni nini kilichomzuia Asafu asikwazwe kabisa na kuwaza kubaya? (b) Alipata kuwa na maoni gani juu ya uhusiano wake na Yehova?
9 Ingawa Asafu alikuwa amekuwa karibu kukwazwa kwa sababu ya kukosa kuutambua uhusiano huu ulio wa maana sana, alirudiwa na fahamu. Yeye, kama mtunga zaburi Daudi, alipata kufahamu kwamba uhusiano mwema na Yehova Mungu ulikuwa wa maana kupita jambo jingine lo lote. Badiliko hili katika maoni ya Asafu lilitokeaje? Alipotambua kwamba kuwaza kwake kulikuwa kubaya, Asafu alikwenda patakatifu. Huko, kati ya kundi la watu wa Yehova, alianza kufahamu kwamba ulioelekea kuwa ufanisi wa waovu ni wa muda tu, hali uhusiano mwema na Mungu unaongoza kwenye baraka za milele, kutia na mali za kimwili. (Zab. 73:15-22; 72:16) Akiwa na moyo wenye kujaa shukrani, ndipo Asafu alipomwambia Mungu maoni yake kwa maneno yapatikanayo katika Zaburi 73:23-28:
“Mimi ni pamoja nawe daima, umenishika mkono wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanikaribisha kwa utukufu. Ni nani niliye naye mbinguni, wala duniani sina cha kupendeza ila Wewe. Mwili wangu na moyo wangu hupunguka, bali Mungu ni mwamba wa moyo wangu na sehemu yangu milele. Maana wajitengao nawe watapotea; umewaangamiza wote waliokuacha Wewe. Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana [Yehova], niyahubiri matendo yako yote.”
10. Maoni ya Mkristo yamepaswa kuwa nini juu ya mali za kimwili, na maoni haya yanayofaa yatamzuiaje asipoteze upendeleo wa Mungu?
10 Ikiwa wewe ni Mkristo aliye, wakf, je! hivi ndivyo wewe unavyojisikia juu ya uhusiano wako na Yehova? Imetupasa sote tujisikie hivyo. Lakini yawezekana kwamba pengine wengine wameacha kuwaza kwa ulimwengu juu ya mali za kimwili kuongoze maoni yao? Huku wanapojidai kumtumikia Mungu, je! kwa kweli wao wanatanguliza kupata mali za kimwili katika maisha? Bila shaka mwendo huo ungekuwa wenye madhara kwa uhusiano wao na Yeye ambaye uzima wao wamtegemea. Yesu Kristo alisema hivi kwa kweli: “Uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” (Luka 12:15) Akiwa chini ya uongozi wa Mungu mtume Yohana aliandika hivi: “Dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.” (1 Yohana 2:17) Ni kweli, hali ya uchumi ya ulimwengu inatikisika; yaweza kuwa vigumu kuruzuku jamaa ya mtu. Lakini tukiwa na imani na tumaini zinazowekwa juu ya Yehova, tutalindwa na kishawishi cho chote cha kufanya utumishi wetu kwa Mungu usiwe na maana sana katika maisha. Bila ya kujali hali zitakazotokea, tutaweza kuukabili wakati ujao kwa matumaini kamili, tukijua kwamba Mungu anaangalia watumishi wake waaminifu. Yeye anaahidi hivi: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”—Ebr. 13:5; Mt. 6:25-34.
KULINDWA NA MAONGOZI YA MOJA KWA MOJA YA MASHETANI
11. Mfalme Sauli aligeukia nini katika jaribio la kujua yaliyoko wakati ujao?
11 Watu wa ulimwengu, wanatafuta uongozi kutoka vyanzo vinavyozidi tu kuharibu hali yao, kwa sababu ya kutokuwa na imani hiyo. Ndivyo Mfalme Sauli wa Israeli ya kale alivyofanya. Kwa sababu ya kumtenda Yehova dhambi, Sauli alikatiliwa mbali na mawasiliano yote ya kimungu. Kama yeye alivyosema, “Mungu ameniacha; hanijibu tena, wala kwa manabii, wala kwa ndoto.” Alipokuwa karibu kupambana na Wafilisti katika pigano, Sauli alitaka sana uongozi juu ya anavyompasa kufanya. (1 Sam. 28:15) Kwa hiyo, badala ya kumwomba Yehova Mungu msamaha kwa unyenyekevu, aligeukia uchawi apate msaada. Kinyume cha Torati ambayo alikuwa na wajibu wa kuitii kama Mwisraeli, yeye alimwendea mchawi.—Law. 19:31; 20:6; 1 Sam. 28:8.
12. Je! kwenda kwa Sauli kwa mchawi kulimletea faraja na uongozi alioutaka, na kwa sababu gani ikawa hivyo?
12 Lakini je! tendo la Sauli lilimpa faraja na uongozi alioutaka? Hata kidogo. Alipokea ujumbe wa majonzi. Kwa habari ya matokeo uliokuwa nayo juu yake, maandishi ya Biblia yatuambia hivi: “Mara Sauli akaangukia chini kifulifuli, akaingiwa na hofu kuu.” (1 Sam. 28:20) Bila shaka yeye hakuifanya hali yake iwe afadhali kwa alilolifanya. Ingawa alikuwa amemwambia mchawi kwamba alitaka aseme na Samweli nabii, Sauli alijua kwamba Samweli alikuwa amekwisha kufa, asiweze kusema. Uhakika wa kwamba sheria ya Mungu ilikataza kusema na wafu kama jambo la kuchukiza sana ungalipaswa kumfahamisha Sauli kwamba yaliyoelekea kuwa mazungumzo na wafu kupitia kwa wachawi yalikuwa madanganyo yenye hila yaliyotendwa na majeshi mabaya ya kiroho,—Kum. 18:10-12.
13. Kwa sababu gani kujua kwa mtu inayosema Biblia hakumzuii asitumbukie katika mtego alimotumbukia Mfalme Sauli?
13 Huenda mtu akajua isemayo Biblia juu ya mambo haya. Hata hivyo, uchapaji mwingi unaofanywa juu ya mafumbo huenda ukamfanya mtu mtafiti. Huenda akapata habari za mtu fulani anayesemekana kutabiri wakati ujao kwa usahihi. Au huenda akapata habari juu ya njia mbalimbali za uaguzi zinazotumiwa—mbao za kuagulia, ESP (yaani, uwezo wa kufahamu maajabu fulani bila msaada wa milango ya akili), unajimu, kukaza macho penye tufe ili kupata maarifa ya wakati ujao na vivyo hivyo. Huenda akavutwa sana hata akataka kuona mwenyewe kama kweli mambo hayo yanafanyika. Huenda akawa na nia ya ‘kujaribu lo lote mara moja.’
14. Ni nini kinachoweza kuwapata wale wanaojaribu kufumbua mafumbo?
14 Je! hilo ni jambo la hekima? Kwa wazi sivyo. Utafiti wake waweza kumfanya asumbuliwe na mashetani. Kusumbuliwa na mashetani kwaweza kumpotezea usingizi na hata kumtia woga mwingi saa za mchana. Huenda hata akaanza kusikia sauti ngeni, zikishauri kwamba ajiue mwenyewe au mtu mwingine. Hii si dhana tu. Visa vya kweli vyahakikisha haya yametokea kweli.
15, 16. Yehova anaonaje mazoea ya kufumbua mafumbo?
15 Ikiwa kweli twaliamini Neno la Mungu, hatutaacha utafiti wo wote usiofaa juu ya mafumbo usitawi akilini mwetu, nalo hili litakuwa ulinzi. Yehova Mungu halioni jambo hili vivi hivi tu. Ili kuwalinda Waisraeli wasidanganywe na kudhuriwa na viumbe vibaya vya kiroho, alifanya mazoea ya uaguzi yawe kosa linalostahili kifo. Neno la Mungu lilisema hivi: “Usimwache mwanamke mchawi kuishi.” (Kut. 22:18) “Tena mtu mume au mtu mke aliye na pepo, au aliye mchawi, hakika atauawa.”—Law. 20:27.
16 Je! maoni ya Yehova juu ya wachawi, walozi na waaguzi yamebadilika? Hata kidogo! Amri kutoka kwa Mungu ingali ipo juu ya wanaoshikilia mazoea ya uchawi. Ufunuo 21:8 unawapanga kati ya wale wanaostahili hukumu ya “mauti ya pili.” Hiyo maana yake ni mauti ya milele ambayo kwayo kupona hakuwezekani. Kwa hiyo, ikiwa watu wo wote ambao wamejitia katika jambo la namna hii wanataka kuyafanya mapenzi ya Mungu, huu ndio wakati wa kuyaondoa maishani mwao.
17. Wale wanaotafuta kibali ya Mungu wamepaswa wafanye nini na vitu vinayoshirikishwa na mafumbo?
17 Kwa habari ya vyombo vyo vyote vinavyoshirikishwa na mazoea ya uchawi, hakikisha hakuna cho chote cha vitu hivyo kimo nyumbani mwako. Ufuate mfano wa wale walioikubali ibada ya kweli katika Efeso, ambao juu yao Matendo 19:19 yasema hivi: “Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote.” Waefeso waaminifu hawakusita kuviharibu vitu hivi ijapokuwa vilikuwa vya gharama nyingi sana.
18. Hali iliyomo katika Jumuiya ya Wakristo kwa habari ya mafumbo inafunua nini juu ya wakati ujao wa viongozi wake wa kidini?
18 Kutokea kwa mapendezi ya mafumbo siku hizi katikati ya Jumuiya ya Wakristo bila shaka kwaonyesha kushindwa kwa viongozi wake wa kidini. Hata waitwao watu wenye elimu wanawaendea watabiri, wanaingia katika unajimu, wanachukua hirizi za bahati nasibu au kutafuta mapozo kutoka kwa waganga wanaoomba miungu ya uongo katika sehemu fulani za dunia. Ingewashangaza sana wengi wa watu hawa kujifunza kwamba Biblia inakataza wanayoyafanya. Wao hawakuambiwa Neno la Mungu linavyosema. Viongozi wao wa kidini wameshindwa kuwafundisha mambo haya na hivyo wamewaacha bila ulinzi na shambulio la mashetani.
KULINDWA TUSIJE TUKASHINDWA NA WOGA MWINGI WA MAUTI
19. Kulingana na Waebrania 2:14, 15, Shetani ametumia njia gani yenye nguvu kuongoza watu?
19 Zaidi ya kupagawa na mashetani, njia nyingine yenye nguvu ambayo Shetani ametumia kuongoza wanadamu ni woga mwingi wa mauti. Angalia vile Waebrania 2:14, 15 inavyosema juu ya hili. Hapa Yesu Kristo anatajwa kama yeye aliye katika cheo cha ‘kumharibu yeye aliye na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi.’ Twaambiwa pia kwamba Yesu aweza ‘kuwaacha huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa.’
20. Onyesha namna Shetani ametumia woga wa mauti yenye jeuri kushikilia watu utumwani.
20 Hakuna shaka kwamba wanadamu kwa ujumla wanaogopa maisha yao yasikatiliwe mbali mapema mno kwa njia yenye jeuri. Hii ndiyo namna ya mauti inayotajwa katika andiko hili, naye Shetani Ibilisi ametumia kabisa woga mwingi wa mauti hiyo. Yeye anatumia woga mwingi kuongoza wanadamu kwa werevu wafanye kama aombavyo. Matukio ya karne hii yaonyesha hili vizuri. Kwa mfano, katika Ujeremani ya Nazi watu wengi waliyaogopa matokeo ya kutofanya wakuu wao walivyoagiza. Watu hawa waliuogopa uwezekano wa kuuawa. Kwa hiyo walitenda kinyume cha matamko ya dhamiri yao na kufanya uvunjaji mbaya sana wa sheria juu ya wanadamu.
21, 22. Ni nini kinachokomboa watumishi waaminifu wa Yehova wasiogope sana kuuawa kwa Jeuri?
21 Walakini, imani yetu na tumaini tulilopewa na Mungu laweza kutulinda tusije tukawa wenye woga sana hata kuyaacha tunayojua kuwa haki, na hivyo kuharibu dhamiri yetu na kupoteza kibali ya kimungu. Haitupasi kuogopa bure, kwa maana twajua Yehova atupenda, kwamba maisha zetu ni zenye thamani sana kwake. Angalia maneno yafuatayo yenye kufariji ya Yesu Kristo: “Ninyi rafiki zangu, msiwaogope hao wauuao mwili, kisha baada ya hayo hawana wawezalo kutenda zaidi. Lakini nitawaonya mtakayemwogopa; mwogopeni yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni huyo. Je! mashomoro watano hawauzwi kwa senti mbili? wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”—Luka 12:4-7.
22 Kweli, wanadamu wanaweza kuuua mwili. Lakini hawawezi kuharibu nafsi milele. (Mt. 10:28) Nayo “nafsi” katika habari hii ni nini? Ni haki ya mtu aliyopewa na Mungu awe kiumbe hai: Wanadamu hawawezi kumfuta mtu katika mpango wa Mungu na kwa hiyo wafanye isiwezekane aishi tena. Kwa hiyo wo wote wanaokataa kushindwa na woga mwingi wa mauti na wanaoendeleza ukamilifu, hata wakati maisha zao zinapotolewa, wanaendelea kuishi kulingana na maoni ya Mungu. Yehova atailinda haki yao ya uzima. Yeye hatasahau hata jambo moja juu yao. Yeye akumbuka utu wao, ukuzi wao wa akili na maono katika maisha. Naye atazirudisha hizi katika ufufuo.—2 Kor. 1:8, 9.
23. Imani na tumaini zinawezaje kututia nguvu tunapotishwa na mauti?
23 Kuamini ahadi ya Mungu ya ufufuo kwaweza kututia nguvu tufanye yaliyo haki hata ikiwa hilo laweza kumaanisha mauti kwetu. Imani hiyo inatuwezesha tufahamu kwamba uzima wa milele utakaofurahiwa kwa kufufuliwa kwa wafu ni wenye thamani nyingi zaidi kuliko miaka michache ya maisha sasa. Inatulinda tusije tukahatirisha nafasi yetu ya kupata uzima wa milele. Hivyo ndivyo imani ilivyowafanyia watu wenye imani wa nyakati za kale; juu yao kitabu cha Biblia cha Waebrania chasema: “Waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi [kuridhiana na waliyotakiwa wafanye kwa kuacha yaliyo haki], ili wapate ufufuo ulio bora.”—Ebr. 11:35.
24. Imani ilimwezesha Yesu Kristo avumilie nini?
24 Imani isiyotikisika katika uwezo wa Yehova wa kufufua na kumthawabisha ndiyo iliyomwezesha Yesu Kristo pia kuendeleza ukamilifu wote. Ebu fikiria aliyoyavumilia. Alitukanwa, akachapwa makofi, akapigwa ngumi, akatemewa mate, akapigwa mijeledi na, mwishowe, akapigiliwa misumari katika mti, afe kama mvunja sheria aliye mbaya zaidi sana. Lakini Yesu Kristo hakuyumbayumba. Hakuisahau thawabu. Lo! ni mfano wenye kutia imani nguvu namna gani aliotuwekea! Kama vile Waebrania 12:2, 3 isemavyo: “Kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili [mti wa mateso] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni [“nafsini,” NW] mwenu.”
25. Ni faida gani zinazotokana na kuishi kupatana na kweli ya kwamba uzima sio uu huu tu?
25 Kwa kweli, uzima sio uu huu tu. Kuishi kupatana na uhakika huo kunatufanya tuepuke maisha ya bure na matupu ya watu wenye kufuatia mali za kimwili. Hata uwezekano wa kufa hauwezi kufifisha furaha yetu katika kuishi sasa wala kutufanya tukate tamaa na kuwa na wasiwasi juu ya wakati ujao. Shukrani kwa Mungu kwa kufanya iwezekane watafutaji wa kweli wenye unyofu wa moyo wawe na tumaini na imani imara!
[Picha katika ukurasa wa 320]
Wivu wa Asafu juu ya ufanisi wa waovu ulimwondolea furaha—mpaka alipotambua kwamba uhusiano mwema na Mungu peke yake ndio unaoongoza kwenye baraka za milele