Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 9/1 kur. 399-406
  • Faida Zenye Kudumu Kutokana na Kuifuata Biblia Kama Jamaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Faida Zenye Kudumu Kutokana na Kuifuata Biblia Kama Jamaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KANUNI YA BIBLIA KWA NDOA
  • SEHEMU YA MUME
  • SEHEMU YA MKE
  • KUZOEZA WATOTO
  • Kutimiza Fungu Letu la Kuendeleza Maisha Yenye Furaha ya Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Kufanikisha Maisha ya Jamaa
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Mume Anayejipatia Heshima Nyingi
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 9/1 kur. 399-406

Faida Zenye Kudumu Kutokana na Kuifuata Biblia Kama Jamaa

1. Kuna ushuhuda gani kwamba mamilioni ya jamaa wanapata matatizo mazito?

LEO tunaweza kuona ushuhuda pande zetu zote kwamba mamilioni ya wanaume, wanawake na watoto wanapata matatizo mazito katika kuishi pamoja kama vikundi vya jamaa. Katika nchi nyingi, matengano, talaka na jamaa zenye kufarakana yanaongezeka kwa kadiri kubwa sana. Wajapokuwa wanaishi katika nyumba moja, idadi kubwa ya watu waliooana hawafanyi zaidi kuliko kuvumilia wenzi wao. Waume, wake na watoto mara nyingi hawashirikiani sana, kila mshiriki wa jamaa anakwenda njia yake mwenyewe. Kwa hiyo, si wazi kwamba watu kila mahali wako katika uhitaji mkubwa wa uongozi wenye kutegemeka?

2. Ni nini mojawapo la malengo (makusudi) makuu ya Biblia?

2 Lengo kubwa la Biblia ni kutoa maongozi ya maisha yatakayofaidi daima wote wanaoyafuata. Hakuna sehemu ya maisha ambayo katika hiyo shauri la Biblia haliwezi kutumiwa kwa faida ya kweli. “Kila andiko . . . linafaya kwa mafundisho, na kwa kuonya watu yulu ya makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa mafundisho katika haki; ili mutu wa Mungu awe mukamilifu, ametengenezwa kabisa kwa kila tendo jema.”​—2 Tim. 3:16, 17, Swahili Congo Bible.

3. Sababu gani twaweza kusema kwamba yale ambayo Biblia inatoa kuwa uongozi wetu ni ya kweli?

3 Yale ambayo Biblia inatoa kwa uongozi wetu ni ya kweli sana. Haituachi katika hali ya kudhani kwamba wale wanaojaribu kufuata shauri lake hawatakuwa na matatizo. Sivyo, Biblia inakubali waziwazi kwamba kutakuwako matatizo. Lakini haifiki hapo tu, kushauri kwamba tukubali mambo kama yalivyo na tusiudhike nayo tu. Biblia inaonyesha tuwezalo kufanya katika njia ya uhakika ili tushindane kwa matokeo mema na matatizo na kujifurahisha uhusiano mzuri pamoja na wanadamu wenzetu, kutia na jamaa zetu wenyewe.

KANUNI YA BIBLIA KWA NDOA

4. Ni nani aliyeanzisha ndoa, na kusudi lake lilikuwa nini juu ya mpango huo?

4 Tangu kitabu chenyewe cha kwanza cha Biblia tunajifunza kwamba Yehova Mungu ndiye Mwanzishi wa ndoa. (Mwa. 2:22-24) Akiwa Mungu wa upendo, alikusudia kwamba ndoa imletee mume na mke pia furaha na vile vile kutoa mpango imara wa kuzaa watoto. Ndoa ilikusudiwa iwe mwungano wa daima, kama inavyoonyeshwa na ambayo Yesu Kristo aliwaambia Mafarisayo fulani waliomwuliza juu ya shauri la talaka: “Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” (Mt. 19:4-6) Kwa wazi, kuheshimu kanuni hii ya kwanza kungaliweza kuzuia nyingi za huzuni na maumizo yanayotokana na talaka na jamaa zilizofarakana.

5. Sababu gani sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilivumilia ndoa ya kuwa na wake zaidi ya mmoja, vile vile talaka kwa sababu nyingine kuliko kukosa uaminifu kwa mpango wa ndoa?

5 Uhakika wa kwamba Yehova Mungu alivumilia ndoa ya kuwa na wake zaidi ya mmoja na talaka kwa sababu nyingine kuliko kukosa uaminifu kwa mpango wa ndoa katikati ya Waisraeli haukumaanisha kwamba alikuwa ameacha kanuni yake ya ndoa. Wakati sheria ilipopewa kupitia kwa Musa, ndoa ya kuwa na wake zaidi ya mmoja na talaka ilikuwa imekuwa mazoea yaliyoimarishwa. Akijua maelekeo ya Waisraeli, Yehova Mungu kwa hekima alitoa amri hizo zitumike kama kizuizi cha mazoea mabaya chini ya hali zilizokuwako wakati huo. Yesu Kristo alieleza hili wakati aliposema hivi: “Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi.”​—Mt. 19:8.

6. Wanafunzi wa Yesu walionaje juu ya kuwekwa upya kwa kanuni ya kwanza ya ndoa, na kwa sababu gani?

6 Walakini, maneno ya Yesu Kristo yalionyesha kwamba kanuni ya kwanza ya Mungu ya ndoa ingetumika kwa wafuasi wa Kikristo. Wanafunzi wake walionaje? Je! walifahamu sana kwamba huu ulikuwa ndio mpango bora? Waliyosema yanaonyesha kwamba hawakuwa na maoni yaliyosawazika kweli kweli juu ya shauri hili. Waliwaza hivi: “Mambo ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa.” (Mt. 19:10) Wanafunzi walijua matatizo yaliyomo katika ndoa ambayo yangeweza kutokea kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu. Basi wakaona kwamba ingekuwa afadhali kukaa bila kuoa kuliko kuhatirisha uwezekano wa kuungana daima katika ndoa na mtu fulani ambaye ingekuwa vigumu sana kupatana naye. Walakini, Yesu Kristo hakulaumu ndoa wakati alipokuwa akipendekeza kukaa bila kuoa.​—Mt. 19:11, 12.

7. Sababu gani inafaa kuiona ndoa kwa uzito sana?

7 Ndiyo, wanafunzi wa Yesu hawakuwa wenye makosa katika kuiona ile kanuni ya kwanza ya ndoa kwa uzito. Ndoa katikati ya wanadamu wasiokamilika ina mambo yasiyofaa yasiyoweza kuachwa bila kuangaliwa. Biblia inawaambia waziwazi wale wanaoamua kuoa kwamba “watakuwa na dhiki katika mwili.” (1 Kor. 7:28) Ndoa inaleta madaraka mazito, masumbufu na shida. (1 Kor. 7:32-35) Kwa mfano, misiba na ugonjwa yaweza kulemea na kuleta mikazo sana juu ya jamaa.

8. Maoni yanayopatana na Maandiko juu ya uzito wa ndoa yamepaswa yamwezeshe anayetazamiwa kuwa mume au mke afanye nini, na ni matokeo gani yenye kuhuzunisha yanayoweza kuepukwa kwa njia hiyo?

8 Kwa hiyo, yeye anayeongozwa na Biblia atafahamu kwamba ndoa ni jambo fulani ambalo mwanamume au mwanamke amepaswa ajitayarishie kiakilini na kimoyoni. Wale wanaofikiria kuoa na kuolewa imewapasa wafikirie sana uwezo wao wa kuwa waume na akina baba wema, na wake na mama watoto wema. Imewapasa watangulie kuamua kwa kujua udhaifu mkubwa alio nao mtu wanayetaka kuona naye na kama wanaweza kupambana na udhaifu huu katika njia ya upendo na yenye ufahamu kwa muda wa maisha. Imewapasa wajiulize wenyewe kama kweli wana nia ya kujinyima mambo fulani na kufanya kila jambo wawezalo ili wamletee furaha yeye anayetazamiwa kuwa mwenzi wao wa ndoa. Wanaume na wanawake wengi wangaliweza kujiepusha wenyewe na kuepusha wenzi wao wasipatwe na maumivu na huzuni nyingi ikiwa wangalifikiria sana yale ambayo Biblia inasema watu waliooana wamepaswa watazamie. Badala ya kufanya jambo fulani haraka haraka ambalo hawakuwa wamejitayarishia, wangaliweza kungoja mpaka wakati ambapo wangekuwa tayari kutwaa madaraka ya ndoa na ambapo wangekuwa na ufahamu unaohitajiwa kuchagua mwenzi wa kuishi naye muda mrefu. Mwendo huo ungaliwaletea faida yenye kudumu kweli kweli.

9. Biblia inasema nini juu ya uwezekano wa wanadamu wasiokamilika kuona furaha katika ndoa?

9 Walakini, Biblia inapofikiria mambo haya yasiyofaa haimaanishi kwamba ndoa zenye furaha haziwezi kuwamo katikati ya wanadamu wasiokamilika. Kwa kinyume, Maandiko yanafunua kwamba mke mwema, kwa mfano, ni hazina ya kweli na baraka kuu kwa mume wake. Tunasoma hivi: “Apataye mke apata kitu chema; naye ajipatia kibali kwa [Yehova].” (Mit. 18:22) “Mke mwema, ni nani awezaye kumwona? Maana kima chake chapita kima cha marijani.” (Mit. 31:10) Pia Biblia inatia moyo mume hivi: “Umfurahie mke wa ujana wako.” (Mit. 5:18) Ijapokuwa kutokamilika, watu waliooana, hasa wanapojitahidi kufuata kanuni za Biblia, wanaweza kuona uradhi na furaha katika uhusiano wao.

SEHEMU YA MUME

10. Ni mambo gani yanayotiwa katika kutumia kwa mume ukichwa kwa kufuata mfano wa Yesu Kristo?

10 Maandiko yawatia moyo waume wafuate mfano mkamilifu wa Yesu Kristo katika kutumia kwao ukichwa. Ukichwa wa mume haumstahilishi amtawale mke wake, akimshusha cheo. Badala yake, unaweka juu yake daraka la kutokunyima upendo wake, kutanguliza hali njema ya mke wake na faida kuliko tamaa zake mwenyewe. “Enyi waume,” akaandika mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu, “wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake.” (Efe. 5:25) Matumizi ya Kristo Yesu ukichwa juu ya kundi si ya ukatili au yenye kuonea kamwe. Upendo wake wa kujitoa, pamoja na uhakika na tumaini lake katika washiriki wa kundi, kweli, ‘unawabidisha’ waitikie kwa upendo ule ule, wakijitahidi kumpendeza.​—2 Kor. 14, 15; linganisha 1 Yohana 5:2, 3.

11. Waume wanawezaje kuonyesha kwamba wanawapenda wake zao kama miili yao wenyewe?

11 Akionyesha mfano wa namna ya upendo ambao imewapasa waume wawaonyeshe wake zao, mtume Paulo aliendelea kusema hivi: “Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa.” (Efe. 5:28, 29) Kwa kawaida waume hawadharau matendo yao wenyewe, wakijifanya wenyewe kuonekana wasiofaa kitu, wakitesa miili yao kwa ukatili, na kutoangalia uhitaji wao wa kupumzika na kuburudika. Hawataki wawe na sifa ya kuwa “vinyangarika” (watu wasiofaa kitu), bali wanatamani waheshimike machoni pa wengine. Kwa hiyo kufuata shauri la Biblia kungekuwa na maana ya kuwapa wake zao heshima ya namna ile ile na kufikiria wanakojitakia wenyewe.

12. Ili mume ‘amgawie mke wake heshima kama chombo dhaifu,’ ni lazima afanye nini?

12 Ikiwa mume atampenda mke wake kama ajipendavyo mwenyewe, yampasa amjue kweli kweli. Hivi ndivyo Biblia inavyowaamuru waume: “Endeleeni kukaa . . . pamoja na [wake zenu] kulingana na maarifa, mkiwagawia heshima kama chombo dhaifu, ndiye mwanamke.” (1 Pet. 3:7, NW) Mume anapojua maoni ya mke wake na udhaifu wake​—wa kimwili, wa moyoni na vinginevyo​—aweza kumtendea kwa huruma, kama chombo chenye bei. Inampasa mume awe na nia ya kuzungumza mambo ya jamaa pamoja na mke wake katika njia yenye utulivu na akili, akipata maoni na mawazo yake ikiwa mke atajiona kwamba ana cheo chenye kuheshimika nyumbani. Imempasa mke ajione huru kusema na kuhakikisha kwamba analosema katika kuzungumza mambo mazito halitadharauliwa bali litafikiriwa kwa kufaa. Zaidi ya hayo, inampasa mume awe macho kuangalia maneno zaidi kuliko neno moja tu linalosemwa. Yaliyomo ndani ya moyo yaweza kufunuliwa kwa namna ya sauti, ishara za uso au kwa ukosefu wa shauku au nia. Mume anayemjua mke wake hatakosa kuangalia mambo hayo na kuendelea bila akili na jambo fulani ambalo huenda likatokeza kuudhika kwa lazima.

13. Ni wakati gani ambapo imempasa mume awe imara ijapokuwa maoni yanayoonyeshwa na mke wake, na hili lawezaje kuwa lenye faida?

13 Bila shaka, kama kichwa cha jamaa, mume asingeshindwa na mke wake anapojua waziwazi kwamba faida za jamaa nzima zingeharibiwa kwa njia hiyo. Anafahamu kwamba ana wajibu wa Maandiko kutegemeza yaliyo mema bila kuangalia maoni ambayo mke wake anaonyesha. Ikiwa mume angefuata matakwa ya mke kinyume cha uamuzi wake bora, angekuwa akikosa kumheshimu Mungu, ambaye amemwaminisha cheo cha kuwa kichwa cha jamaa. (1 Kor. 11:3) Na ikiwa baada ya hapo mambo yanaletea jamaa shida, hili lingemfanya amwonee mke wake uchungu. Kwa upande mwingine, kusimama kwake imara kwa ajili ya anaoamini sana kuwa ndio mwendo unaofaa kutakuwa kwa faida ya jamaa. Baadaye mke wake atakapoona hekima ya uamuzi uliofanywa, atafurahi kwa vile mume wake alisimama imara. Hili litasaidia kuongeza heshima yake kwa mume wake na kumfanya asitumie sana uvutano wake wa kike ili amgeuze mume wake afanye mambo kulingana na njia yake.

SEHEMU YA MKE

14. Ni sehemu gani ya Maandiko ya mke?

14 Kwa habari ya sehemu ya wake, Biblia inasema hivi: “Watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno; wakiutazama mwenendo wenu safi, na wa hofu. Kujipamba kwenu . . . kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; yaani, roho ya upole na utulivu.”​—1 Pet. 3:1-4.

15. Mke awezaje kuonyesha utii wake, na kwa kufanya hivyo anaweza kupata faida gani?

15 Mke anayetaka kufuata shauri hili la Maandiko atamwuliza mume wake juu ya mambo ya maana​—⁠vitu vikubwa vinavyotakiwa kununuliwa, ahadi za kuajiriwa kazi na mambo kama hayo​—kabla ya kuyafanya. Mke atajitahidi kujua nia ya mume wake juu ya mambo na kufanya mambo ya jamaa katika njia anayojua itakubaliwa na mume wake. Kwa kufanya hivi, atapata faida nyingi. Mume wake hataona lazima ya kumwekea sheria kwa kujaribu kuzuia matendo yake yasiyo ya hekima. Atakuwa na hakika na kutumaini kwamba mume wake atamruhusu atumie sana uwezo na nia yake katika kuangalia jamaa.​—Mit. 31:11-31.

16. Ni faida gani zinazoweza kumjia mke anayetii shauri la Biblia ijapokuwa mume wake asiliangalie?

16 Utii wa mke hauwezi kuwa rahisi sikuzote, hasa ikiwa mume ni mtu asiyefikiria, asiyetumia akili na hata anaepuka kutimiza daraka. Walakini, jambo moja ni hakika; hali haitakuwa bora ikiwa mke anajaribu kujitwalia ukichwa, sikuzote ni mwenye chokochoko au anamlaumu mume wake na kumtazamia afanye mambo kupita awezavyo. (Mit. 21:9, 19; 27:15, 16) Badala ya “kufoka” (kukasirika ghafula) kwa sababu mume anakosa kuangalia jambo fulani, mke atakuwa na matokeo bora sana kwa kujaribu kumtia moyo mume wake na kudumisha utulivu na hali ya moyo iliyo sawa katika hali zenye taabu. “Roho ya upole na utulivu” yake labda ndiyo inayohitajiwa ili kumfanya mume afikirie sana njia ile anayotendea mwenyewe na kuanza kufanya mabadiliko katika maisha yake. Hata ijapokuwa maendeleo yawe ya polepole sana, mke anayefuata shauri la Biblia anapata faida. Anaepuka masikitiko makubwa, uchungu na mabaya ambayo yangetokea kwa sababu ya kupingana wazi na mume wake.​—Mit. 14:29, 30; 1 Pet. 3:10, 11.

17. Sababu gani ni jambo la hekima mke asifanye ugomvi juu ya makosa ya mume wake asiliangalie?

17 Vile vile, mume anapofanya maamuzi mabaya, mke anayefanya ugomvi kwa sababu ya hili hapati sana faida. Wanadamu wana maelekeo ya kujitetea wenyewe hata wanapokuwa wamekosa. Hivyo ikiwa mke anafanya ugomvi kwa sababu mume wake ametumia uamuzi mbaya, huenda akapata matokeo mabaya sana kuliko na anavyotaka. Huenda mume akaazimu zaidi asijali ambayo mke anasema ili kumhakikishia kwamba hana haja ya shauri lake. Kwa upande mwingine, ikiwa maoni ya mke yanaonyesha ufahamu wa kwamba sisi wanadamu hatuwezi kuepuka kabisa makosa katika uamuzi, labda mume ataelekea zaidi sana kufikiria maoni yake wakati mwingine. (Yak. 3:2) Wakati huo fahari yake isingehusika sana na jambo hilo.

KUZOEZA WATOTO

18. Watoto wanaongozwa vyema au vibaya namna gani kwa kadiri wazazi wanavyofuata au hawafuati shauri la Biblia?

18 Watoto wanaongozwa vyema au vibaya kwa kadiri wazazi wanavyofuata au hawafuati shauri la Biblia katika kutimiza sehemu zao mmoja mmoja. Ikiwa mke anadharau mamlaka ya mume wake iliyopewa na Mungu, huenda wakati mwingine watoto wakaonyesha heshima kidogo kwa wazazi. Huenda wakamtumia mzazi mmoja juu ya mwingine katika kujaribu kupata wanachotaka. Walakini, mke anaposaidia watoto kwa neno na kwa mfano wathamini uamuzi wa mume wake, wanaona faida ya kumkaribia baba yao wapate shauri. (Mit. 12:4) Kukubali kwa mume makosa waziwazi na nia yake ya kufikiria mashauri na maoni ya jamaa kwaweza kufanyiza sana roho changamfu ya jamaa. Kunapokuwako na ishara za waziwazi kwamba anathamini uamuzi wa mke, watoto pia wataheshimu na kuthamini shauri la mama yao. (Mit. 6:20-23; 31:28, 29) Ndiyo, uhusiano mchangamfu, wa upendo na wenye kuheshimu kati ya mume na watoto ambao Biblia inatia moyo uwepo unaivuta jamaa pamoja na kuwafanya watoto waitikie agizo la wazazi wao.

19. Sababu gani mazoezi yanayofaa ya watoto si kazi rahisi?

19 Mazoezi yanayofaa ya watoto si kazi rahisi bila shaka. Watoto wanaonyesha tabia mbaya kama utundu, uasi na choyo tangu mwanzo wenyewe wa maisha. Inawapasa wazazi wawe macho waangalie maelekeo mabaya kisha wachukue hatua zinazofaa za kutoa adhabu na kuwarudi watoto wao, wakifanya hivyo kwa uvumilivu. (Mit. 22:15; 29:15) Inawapasa pia waweze kufahamu matatizo ambayo yangeweza kutokana na mambo ambayo huenda yakaonekana kuwa si mabaya yenyewe. Mara nyingi ni shauri la wazazi kuweza kuhakikisha wakati mwendo fulani si mzuri tena.

20. Sababu gani kujitenga na watu ni hatari ya kuepukwa?

20 Kwa mfano, kuna tofauti kati ya faragha na kujitenga na watu. Kadiri fulani ya faragha ni yenye faida ili kufikiri sana, kufikiri kwenye kujenga na kufanya mpango. Lakini kujitenga na watu ni kwa hatari, kwa vile kunamzuia mtu asipate yaliyosawazika ya fikira za wengine, maono na uamuzi wao. Huenda kukamfanya mtu awe mwenye kujifikiria mwenyewe na asione haja na maoni ya wengine. Kwa kujiona mwenyewe, huenda mwenye kujitenga na watu akajisikitikia mwenyewe au akawa mwenye kufuata shauri lake mwenyewe, mkatili na mkali. “Ajitengaye na wenzake,” yasema mithali ya Biblia, “hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.”​—Mit. 18:1.

21. Wazazi labda wanaweza kufanya nini ili kusaidia watoto wao waepuke kujitenga na watu?

21 Watoto walio na maelekeo ya kujitenga na watu wapaswa waonyeshwe kwamba wanatakiwa na kufurahiwa na washiriki wa jamaa, kwamba mawazo yao, tabia za moyoni na maono yao ni ya maana kwa wazazi wao. Katika mfano unaowekwa na wazazi wao ni lazima waone uthibitisho wa kweli kwamba furaha ya kweli inatokana na kujitolea kusaidia wengine. (Matendo 20:35) Wazazi wanaweza kutoa uthibitisho huo, si kwa kufikiria na kusikitikia sana watu walio na shida tu, bali pia kwa kufanya kadiri wawezavyo wawe msaada. Labda linalotakiwa tu ni kufanyia watu wa makamu, walio dhaifu au wenye vizuizi kazi kama kwenda dukani kununua wanavyotaka, kusafisha nyumba au kazi nyingine za nyumbani. Mtoto aweza kufundishwa kushiriki utendaji huo wakati wa umri wenyewe wa uchanga. Hili laweza kumsaidia sana mtoto afahamu maana ya kufikiria hali njema ya watu wengine.

22. Watoto wanawezaje kujitenga na watu wazima, na huku kwaweza kuwa na matokeo gani juu yao?

22 Inawapasa pia wazazi waangalie kwamba hawawatii moyo au kuruhusu wanao na binti zao wajitenge wenyewe wakiwa na michezo, rafiki na mawazo yao wenyewe. Ni lazima jamaa ifanye mambo pamoja ili kudumisha kupashana habari kuzuri. Ni lazima wazazi waangalie kwamba hawafanyi mambo ivi hivi tu kama jamaa. Labda wageni wanapokuja nyumbani au jamaa inatembelea mahali kwingine, watoto kama kawaida wanajitenga wenyewe na ushirika wa watu wazima na kuwa mbali wakati wa matembezi yote. Huenda hata wakaambiwa kufanya hivyo. Ikiwa watoto wanashinda hivyo wakishirikiana na wale wenye umri wao peke yake, wanawezaje kusitawisha thamani ya hekima inayotokana na umri na ujuzi? (Mit. 1:20, 21; 8:1-11) Wanawezaje kujifunza kuwa na maongezi yenye maana pamoja na watu wazima na kufahamu ambayo watu wazee wanatamani, kuhangaikia, kuona na kuhitaji? (Law. 19:32) Je! maoni yao hayatakuwa ya kipumbavu, wakitazama mambo kwa maoni ya kitoto yasiyo na akili tu? Wakati uo huo, je! wazazi vile vile hawatakuwa na maoni ya kipumbavu, wasifahamu fikira za watoto wao? Je! hawatakuwa na mtengano kati yao na watoto katika nyumba yao?

23. Wazazi wanawezaje kushindwa kujua fikira na maoni hasa ya watoto wao?

23 Huenda pia wazazi wakashindwa katika njia nyingine kujua maoni na fikira hasa za watoto wao na kwa njia hiyo wakose kupashana habari nao. Hili lawezaje kutukia? Kwa kujitia katika shughuli za kipekee, huenda wazazi wasiwe na wakati wa kuwasikiliza watoto wao na kufahamu maitikio yao. (Linganisha Mithali 27:23.) Huenda wakawauliza watoto wao juu ya mambo yanayotendeka shuleni na namna wanavyokuona kuvuta tumbako, kutumia dawa za kulevya ili kupata raha, mwenendo kati ya wanaume na wanawake, na vivyo hivyo. Labda ijapokuwa wanaona kwamba hawana uhakika wote juu ya shauri hilo, huenda wazazi wakaridhika na maelezo mafupi ya watoto wao. Kwa sababu ya kutoangalia mara nyingi ushuhuda juu ya maoni ya ndani ya watoto wao kama yanavyoonyeshwa na namna ya sauti yao, ishara za uso na kadiri ya shauku au nia yao, huenda wakati mwingine wazazi hao hata wasione nia na matendo yanayoonyesha kwamba wanao na binti zao hawana kweli ya yale wanayosema. Huenda wazazi wakadhani kwamba mambo yanaendelea sawasawa na watoto wao kwa vile wanapatiwa vitu vya kimwili. Walakini, huenda kweli watoto hao hawaridhiki na wanasadiki kwamba wazazi wao hawapendezwi na hali njema yao. Kwa wazi, kutoangalia huku kwa wazazi kunatokeza uharibifu wa kupashana habari kwa maana kwa jamaa.

24. Ni shauri gani ambalo Waefeso 6:4 linawapa akina baba, na ni jambo gani liwezalo kutukia ikiwa halifuatwi?

24 Zaidi ya kujitahidi kusiwe kukosa kujua fikira na maoni ya watoto wao, ni lazima wazazi wajue namna ya kuwatia adabu. Biblia yawaagiza akina baba hivi: “Nanyi baba, musichokoze watoto wenu; lakini muwalee katika azabu na maonyo ya [Yehova].” (Efe. 6:4, Swahili Congo Bible) Azabu ya baba yawezaje kuchokoza watoto wake? Huenda akapita kiasi katika amri zake, akiwa mkali pasipo lazima au pengine ni mwenye kugeuka-geuka. Azabu haiwezi kutolewa kwa hasira kali. Kwa kuwa hasira inatokeza hasira, huenda watoto wakajaa hasira na kumwonea baba uchungu. Pengine watanyenyekea azabu yake kwa sababu wanalazimishwa watii nguvu yake kuu tu. Wakati wo wote hili linapotukia, azabu hiyo haitawaongoza kweli watende yaliyo mema. Inaweza kutokeza ndani yao yaliyo mabaya zaidi kupita​—chuki, uchungu na uasi.

25. Imempasa baba afanye nini ili azabu yake iwe na matokeo mema kwa watoto wake?

25 Baba anayejaribu kufanya watoto wao wajue kwamba anawapenda sana na anakaza juu yao ubora na kufaa kwa njia ya uzima inayopatana na Biblia atakuwa na matokeo yaliyo tofauti kabisa. Kweli, huenda kwanza watoto wasifahamu sikuzote kufaa kwa azabu ya baba yao. Lakini wanapoifikiria baadaye, wanaweza kuithamini kama wonyesho wa baba mwenye upendo anayewaangalia kweli kweli.​—⁠Ebr. 12:5-11.

26. Sababu gani kutumia kwa baba wakati unaofaa akiwa pamoja na watoto wake ni kwa maana sana?

26 Kutia azabu ni sehemu ndogo tu ya daraka la Maandiko la baba kwa watoto wake. Ana wajibu pia kutumia wakati unaofaa akiwa pamoja nao ili mfano na kufundisha kwake kuweze kuondoa mavutano mabaya wanayopata shuleni na kwingineko. Baba anayelifikiria hili sana hatadhani kwamba ametimiza wajibu wake wote ikiwa labda anaongoza funzo la Biblia la kila juma pamoja na jamaa yake. Anafahamu kwamba kulea watoto katika “maonyo ya [Yehova]” ni daraka la kutimiza kila siku ikiwa inawezekana.​—Kum. 6:6, 7.

27. Ni mambo gani yaliyomo katika kutoa kwa baba agizo la kila siku kwa watoto wake?

27 Agizo la kila siku halimaanishi kwamba kila wakati baba yampasa awe akiwatajia watoto wake Maandiko. Lakini ni lazima ajue ambayo Biblia inasema na kupeleka ile roho ya ujumbe wake kwa watoto wake. Nia yake mwenyewe, maneno na matendo yake yamepaswa yapatane na Maandiko. Wakati wo wote watoto wanapohitaji uongozi, imempasa aweze kuwasaidia waone mambo kutokana na maoni ya Maandiko. Katika njia hii, Neno la Mungu litakuwa waziwazi mbele ya watoto. Mke aweza kuwa mwenye msaada mkubwa kwa mume wake katika kutoa malezi hayo ya maana.​—Mit. 1:8; 6:20; 31:26.

28. Ikiwa mume hafuati shauri la Neno la Mungu, inampasa mke afanye nini?

28 Namna gani ikiwa mume halithamini Neno la Mungu? Namna gani ikiwa mke peke yake ndiye anayethamini shauri lake? Ikiwa ni hivyo daraka la kulea watoto katika “maonyo ya [Yehova]” linamkalia mke. (Linganisha Mithali 31:1) Hii si hali inayofaa sana, lakini si isiyo na tumaini. Wanawake wengi wamekuwa na matokeo mazuri katika kusaidia watoto wao wawe watumishi wa Yehova wenye mfano mzuri.

29. Habari ya Timotheo yaonyeshaje kwamba mama aweza kutoa malezi mazuri ya Maandiko ijapokuwa mumewe haamini?

29 Chukua mfano wa Timotheo katika karne ya kwanza C.E. Aliona ubora wa Maandiko kwa sababu ya jitihada za mama yake Eunike na labda pia bibi yake (nyanya) Loisi. Mama yake alianza kumfundisha mwana wake Maandiko wakati wa utoto wake, ijapokuwa inaonekana kama ilikuwa vigumu kwa mama kwa sababu mume wake alikuwa asiyeamini. Ndiyo sababu mtume Paulo aliweza kumwambia Timotheo hivi: “Tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.” (2 Tim. 3:15) Ndiyo, kutokana na kumbukumbu lake la mambo ya zamani, hakuna wakati ambapo Timotheo alijua kuwa hakuwa amefahamishwa Maandiko Matakatifu. Malezi hayo bora yalisaidia sana kumfanya awe mfano mzuri katika ujana. Alisifiwa sana na wote waliomjua sana. (Matendo 16:1, 2) Mtume Paulo alisema kwa habari ya Timotheo wakati wa kuliandikia kundi katika Filipi: “Sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli. . . . mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya Injili, kama mwana na baba yake.”​—Flp. 2:20-22.

30. Imewapasa wazazi waoneje juu ya kulea watoto hata kama ni juzijuzi tu ndipo wameona ubora wa Biblia?

30 Hakuwezi kukawako shaka kwamba kulea watoto katika njia ambayo Biblia inaonyesha kunataka wakati mwingi na jitahada. Lakini je! wakati unaotumiwa na jitihada haufai? Je! haileti thawabu wakati watoto wanapojithibitisha kuwa sifa kwa wazazi wao? Hata ikiwa zamani wazazi wameshindwa kwa sababu hawakuona ubora wa Biblia, bado wanaweza kuondoa uharibifu unaotokana na kukosa uongozi na adabu inayofaa. Matumizi ya kanuni za Biblia yaweza hata kuifikia mioyo ya watoto wenye umri mkubwa zaidi kidogo wanapoona kwamba wazazi wao kweli wanapendezwa na hali yao njema.

31. Ni nini linalotakiwa kwa mtu anayetaka kuifuata Biblia, naye anafaidikaje?

31 Kufuata Biblia kunaleta faida yenye kudumu kweli kweli. Ili tufanye hivyo, inatupasa tujue hasa inayosema na kutafuta kuongozwa na roho ya mafundisho yake katika yote tufanyayo. Hili ni jambo lisiloweza kufanywa usiku mmoja. Lataka kujifunza Neno la Mungu kwa kuendelea na shauku ya kufuata shauri lake lenye hekima. Halafu, huku nako kunaongoza kwenye furaha, usalama, uradhi na amani ya kweli. Kama kitabu cha Biblia cha Mithali kinavyosema: “Heri mtu yule aonaye hekima, na mtu yule apataye ufahamu. Maana biashara yake ni bora kuliko biashara ya fedha, na faida yake ni nyingi kuliko dhahabu safi. Yeye ana thamani kuliko marijani, wala vyote uvitamanivyo havilingani naye. Ana wingi wa siku katika mkono wake wa kuume, utajiri na heshima katika mkono wake wa kushoto. Njia zake ni njia za kupendeza sana, na mapito yake yote ni amani. Yeye ni mti wa uzima kwao wamshikao sana; ana heri kila mtu ashikamanaye naye.”​—Mit 3:13-18.

​—Kutoka The Watchtower, Mar. 1, 1975

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki