Kumaliza Haya
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
JE! WEWE waona ni vigumu kuanza mazungumzo, hasa na wageni? Je! wewe unakawia kufahamiana na watu wapya? Je! unajisikia mwenye kusitasita kujiunga na utendaji wa kikundi cha watu? Basi kwa wazi wewe una haya.
Haya zinaweza kuvutia. Ndivyo zilivyo katika watoto—vitoto vya miaka michache vinavyokutazama vikikukodolea macho au vyenye kuficha nyuso zao ukiviangalia kidogo tu. Hata hivyo, je! hatufurahii kuona hawa pia wakimaliza woga na kuanza kututumaini sisi, hata wakionyesha usitawi wa kitoto?
Wewe si kitoto tena. Nasi tunapozidi kukua, watu kwa haki wanatazamia mengi zaidi kwetu. Kama vile mtume Paulo alivyosema: “Nilipokuwa mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapa nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto.” (1 Kor. 13:11) Ni kweli, nyakati nyingine kadiri fulani ya haya inaweza kuvutia hata katika watu wazima. Inafanana na adabu, hali ya kujinyenyekeza, na adabu inavutia sikuzote, si kitu umri wa mtu ni mkubwa namna gani.
Lakini kujizuia kwa sababu ya haya kunazidi kujizuia kwa adabu. Nako kukiendelea kupita kiasi kunaweza kukuzuia vibaya sana usipate vitu vyote ambavyo ungeweza kupata maishani. Kwaweza kuwa kama kamba au mnyororo unaokufunga, ukikuzuia usitembee. Kwaweza kupunguza maendeleo yako ya kuwa mwanamume au mwanamke mzima, kwa njia hiyo kukufanya upoteze wakati wenye thamani katika miaka ya ukuzi. Kwaweza kufanya jambo dogo, kama vile kula chakula ukiwa mbele ya wengine kuwe jambo la kuchukiza.
Lakini kwa sababu gani watu wengine ni wenye haya au woga hali wengine hawana? Haya zinaweza kumalizwaje au hata kuzuiwa ili zisikatize furaha yako ya kuishi?
Kwanza, ujue kwamba kuwa mtu wa kawaida hakuna maana ya kwamba utakuwa mwenye ulimi, mtu mwenye kukaa katika makundi ya watu saa zote. Sote tunaweza kushukuru kwamba watu wengine kwa asili ni wanyamavu kuliko wengine na kwamba wengine hawaogopi kukaa peke yao kwa vipindi fulani, wakifanya uchunguzi mwingi, wakifikiri au wakitafakari tu. Watu hao huenda wasisaidie kufanya mazungumzo yawe mazuri kama wengine. Lakini wanayosema huenda yakawa ya maana na yanayostahili. (Linganisha Mithali 17:27, 28.) Hata hivyo, kuna tofauti ya kuwa mnyamavu kwa asili au mtulivu na kuwa mwenye haya, mwenye soni au mwenye kusitasita. Ni nini kinachosababisha tabia hizi za mwisho?
SABABU ZA KUWA NA HAYA
Sababu ni hali ya akili, ambayo yenyewe yaweza kusababishwa na mambo mbalimbali. Malezi ya mtu yaweza kufanya hivyo. Huenda mtu aliyelelewa mjini akajiona huru akiwa karibu na watu kuliko mtu aliyelelewa mashambani au katika eneo lisilokaliwa na watu wengi. Pengine sura ya kimwili inahusika. Tunapokua mara nyingi tunapitia katika hatua za ukuzi zenye kutatiza. Huenda sura yetu isiwe nzuri sana, au sehemu za mwili wetu huenda zikawa hazilingani na nyingine katika mwili au zikawa hazilingani na uso. Huenda tukachokozwa-chokozwa juu yake, au tukachokozwa juu ya ufupi au urefu au unene au kukonda kwetu. Au pengine tuna tatizo la usemi, kusema kitembe au kusitasita wakati wa kusema.
Huenda hata wazazi wetu wakahusika bila kukusudia. Ingawa wanatupenda, huenda wakatutazamia tupate maksi ya juu kuliko tunavyoweza shuleni, tuwe wenye uwezo mwingi wa kufanya mashindano ya michezo, na kadhalika. Kukosa kwetu kufanya kama wanavyotazamia huenda kukatufanya tuwe wenye haya. Wakilaumu-laumu makosa yetu ya sarufi (grammar) au adabu zetu mbele ya wengine, huenda hii ikatuhusu kwa njia wasiyodhani. Au ikiwa maulizo yetu yanasukumiwa mbali kama ‘ya kipumbavu’ huenda tukavunjika moyo juu ya thamani ya mazungumzo.—Kol. 3:21.
KUUMALIZA UGUMU
Lakini kuwa na wasiwasi juu ya mambo ya zamani hakutabadili lo lote, sivyo? Jambo la maana ni yale unayoweza kufanya sasa uumalize ugumu wenyewe. Kwa kweli, jambo la maana hasa ni kuwa na maoni yaliyosawazika juu ya watu na kutokuhangaikia sana wanavyodhani juu yako. Ni kweli, watu wengine ni wakali na wenye kulaumu-laumu nao wanadharau wengine. Lakini si kila mtu aliye hivyo. Sababu gani uache watu wakali wakumalizie furaha inayoweza kutokana na kushirikiana na wengine? Tukiacha mambo fulani mabaya yaliyotupata yatubadili tunaweza kuwa kama wale Waisraeli waliopoteza ushujaa wao hata ‘sauti ya jani lililopeperushwa ikawa inawakimbiza.’ (Law. 26:36) Furaha haiwezi kuja bila kutatua magumu fulani.
Pengine huna uso au umbo zuri kama ambavyo ungalitaka liwe. Lakini watu wengi wenye nyuso na miili ya kuvutia wanakuwa wasiofanikiwa maishani. (2 Sam. 14:25; 15:5, 6; 18:9, 14; Mit. 31:30) Jambo la maana hasa ni vile ulivyo kwa ndani, katika “utu wa moyoni usioonekana.” Hicho ndicho Mungu anachopendezwa nacho, si kuona “sura ya nje, bali . . . moyo.” (1 Pet. 3:4; 1 Sam. 16:7; Zab. 51:6) Watu wanaostahili kuwa rafiki zako watakuthamini wewe kwa njia iyo hiyo, kulingana na kanuni unazoishi kwazo, mambo yaliyomo moyoni na akilini mwako. Zakayo alikuwa mfupi sana, kwa wazi Paulo alikuwa na macho yasiyoona vizuri, Elisha alikuwa na kipara, lakini wote hawa waliheshimiwa na Mungu na watu wenye haki kwa sababu ya mambo waliyofanya na yaliyokuwa moyoni mwao.—Luka 19:1-10; Gal. 4:15; 6:11; 2 Fal. 2:23, 24.
Musa alikuwa na ugumu wa kusema uliomfanya asitesite kusema mbele ya watu wote. Lakini, wakati ulipopita, kwa wazi alishinda ugumu huu. (Kut. 4:10; linganisha Kumbukumbu la Torati 31:30; 32:1, 2) Kusema kitembe na kubabaika kunaweza kumalizwa au kuondolewa sana ukitia bidii. Kubabaika hakusababishwi na mwili; kunasababishwa na kizuizi cha akili kinacholeta wasiwasi au kuvuruga akili. Dawa yenye msaada ni kusoma kwa sauti kwa mwendo wa taratibu. Kisha sema kwa njia iyo hiyo. Kama vile unavyoelekea zaidi kuanguka unapopiga mbio kuliko unapotembea, ndivyo ilivyo na katika kusema. Sema kwa utaratibu mpaka uache kidogo kidogo kubabaika. Ndipo unapoweza kuongeza mwendo kidogo kidogo. Unaposema mbele ya watu wengi, kumbuka kwamba si watu wengi wanaofurahia wasiwasi wako. Wanakutaka ufaulu. Ingawaje, ukifaulu wao ndio watakaofaidika. Kwa hiyo badala ya kukudharau, watu wengi watakuwa wakikutazamia ufanikiwe.
Kusema kitembe huenda kukasababishwa au kusisababishwe na mwili. Lakini kumbuka kwamba katika utoto (au unapojifunza lugha mpya) viungo vya kusema—ulimi, midomo, koo—vyote lazima vijifunze kutamka kila mlio. Vinajifunza kwa mazoezi, vikirudia-rudia miendo ile ile. Ili kuondoa au kupunguza kusema kitembe, fanya mazoezi ya kutamka, ukitumia viungo vya kusema (hasa ulimi) kwa miendo iliyo ya lazima ili kutoa milio sawa. Katika mazungumzo, maneno yanapokuja yenye matamshi magumu, punguza mwendo. Bidii yenye subira italeta maendeleo.
Jifunze kutojichukua kwa uzito sana ukijifanya usiyeweza hata kujicheka mwenyewe pindi kwa pindi. Kijana mmoja aliyekuwa mwenye masikio makubwa alikuwa akiambia wengine kwamba alipozaliwa wazazi wake hawakujua kama atatembea au kuruka kama ndege. Ucheshi wako waweza kukuburudisha wewe. Kumbuka, pia, kwamba si kila mara unapochokozwa-chokozwa kwa njia mbaya; huenda ikawa ni dalili ya kupendwa. Hivyo mithali ya Kijeremani, “Was sich liebt, das neckt sich,” ya maanisha, “Anayependwa anachokozwa.”
KUANZA KUJARIBU
Jambo la maana ni kuanza kujaribu. Huwezi kujifunza kuogelea hata kidogo usipotaka kulowana. Wala huwezi kumaliza haya usipokuwa na nia ya kutia bidii ya kuanza mazungumzo, kufahamiana na watu wapya, kushiriki na wengine kufanya mambo. Ujue kwamba kila mtu nyakati nyingine atajisikia kutokuwa huru sana au kuwa mwenye wasiwasi anapokuwa na watu fulani. Lakini usifanye mambo madogo yawe makubwa na magumu kufanywa. Kuanza mazungumzo kwaweza kuwa kwepesi kama kusema, “Sijapata kukuona hapo kwanza; unaitwa nani?” Kisha unaweza kuuliza mtu huyo atoka wapi, anafanya nini sasa, mambo yakoje kazini au shuleni, pengine umwulize juu ya mipango yake ya wakati ujao. Ukionyesha unapendezwa na wengine, wao wataonyesha wanapendezwa nawe. Na hasa ukionyesha shukrani kwa mema unayoona katika wengine utakuwa na rafiki wengi.—Luka 6:38.
Hiyo ndiyo njia ya kufaulu katika kumaliza ugumu huo. Fikiria wengine, namna ya kuwafaidi, nawe hutakuwa mwenye kujifikiria mwenyewe. Kama vile Paulo alivyoshauri Wakristo katika Korintho, mara nyingi inatupasa ‘kukunjuka’ katika upendano wetu na kuhangaikia wengine. (2 Kor. 6:11-13) Upendo umepaswa utuvute kufanya hivyo, kutia bidii badala ya kuacha haya zituongoze. Fikiria vile Yesu Kristo alivyofanyiwa mzaha na kudhihakiwa bila sababu. Hata hivyo yeye alionyesha upendo wa kweli na akapendezwa na watu wa namna zote.—1 Pet. 2:21-24.
Mtume Paulo alikwenda Korintho “katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi,” kwa wazi akifikiria kama ataweza kutumikia Wakorintho vema na kumaliza maoni mabaya yaliyokuwa kati yao. Ingawa wapinzani fulani walidharau sura na usemi wake, yeye hakuacha maoni yao yaliyopotoka yamzuie asitumikie faida za Mungu na za mwanadamu mwenzake. (1 Kor. 2:3; 2 Kor. 10:10) Mfanya kazi mwenzake aliye kijana Timotheo pengine alikuwa kimya-kimya kwa asili. (2 Tim. 1:6, 7) Lakini hii haikumzuia asikubali migawo migumu.—1 Tim. 1:3, 4; 4:12, 13.
Haya nyingi sana zitatufanya “wakaa-peke-yao.” Mithali 18:1 inatuonya hivi: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.” Ili tuwe na uamuzi maishani imetupasa tuone mambo yalivyo hasa kwa kushirikiana na kuzungumza. Akili na mioyo yetu inahitaji msisimko na burudisho ambalo linaweza kuletwa na ushirika huo. (Rum. 14:7) Ama sivyo akili na mioyo yetu inaweza kuwa kama vyumba ambavyo madirisha yake na mapazia yamefungwa, vinavyoanza kuwa na harufu mbaya. Ni kweli, kusoma kunaweza kuongezea mawazo lakini hakuwezi kuwa bora kuliko ushirika na watu walio hai.
Acha upendo ukuongoze uanze kujaribu, leo, kumaliza haya. Kisha kila siku utaona yako maisha yakiwa na mambo mengi ya kupendeza zaidi, ya kuthawabisha zaidi—kwako mwenyewe na kwa wale unaoonyesha unapendezwa nao.