Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 10/15 kur. 459-465
  • “Yehova Ni Nani” Hata Wote Wamwabudu Yeye?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Yehova Ni Nani” Hata Wote Wamwabudu Yeye?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • IBADA YA SERIKALI KAMA MUNGU
  • VITU VYA KIMWILI VYAABUDIWA KAMA MUNGU
  • Kupambana na Hayawani Wawili Wakali Sana
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • N’nini Kinachozuia Amani ya Ulimwengu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kitabu cha Ufunuo Kinamaanisha Nini kwa Maadui wa Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Roho Takatifu Yafanya Kazi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 10/15 kur. 459-465

“Yehova Ni Nani” Hata Wote Wamwabudu Yeye?

1. Ni ulizo gani juu ya ibada lililo halisi na lenye kuhusu leo, na kwa sababu gani?

TANGU wakati wa kale mpaka karne hii ya 20, wakuu wa serikali za kisiasa wameabudiwa kama miungu. Watu wanaojua sana historia ya kibinadamu wanajua hilo. Mafarao wa kifalme wa Misri ya kale walitazamwa kama miungu, kila Farao anayetawala akionwa kama mwana wa Mungu-jua. Kaisari Augusto, mtawala wa kwanza wa Milki ya Kirumi, aliabudiwa baada ya kufa; ndivyo na waliomfuata. Hata wakati walipokuwa hai, watawala hao walikuwa wakitajwa kama “Mungu.” Yapata miaka elfu mbili baadaye, ilipokwisha kumalizika Vita ya Ulimwengu ya Pili katika mwaka wa 1945, Mtawala Hirohito wa Japan alikataa waziwazi kuwa mungu, mwana wa mungu-jua wa kike Amaterasu. Lakini washupavu fulani wachache wangali wakishikamana na ibada ya watawala katika Nchi ya Mashariki. Usoni mwa miungu yote ya kiume na ya kike ya mataifa ya kale na ya kisasa, ulizo hili ni halisi na lenye kuhusu hata kwa leo, Ni mungu gani anayestahili kuabudiwa?

2. Tangu mwanzo wa serikali ya kisiasa ya kufanywa na wanadamu, watu walio wengi wamekuwa na hatia ya ibada ya namna gani?

2 Mungu mmoja wa taifa baada ya mungu mwingine amefunuliwa kuwa si wa kweli kwa kadiri wakati umesonga. Kisa tusichoweza kusahau ni kile cha karibuni cha Nikita Khrushchev wa Chama cha Kikomunisti aliyemfunua wazi marehemu Joseph Stalin mwenye kujinyakalia utawala kama mungu wa Urusi. Njia yenye kufunua uongo karibu inakuwa yenye kuchekesha. Lakini kuabudiwa kwa wakuu wa serikali za kisiasa kumekuwa na matokeo mazito kwa ulimwengu wa wanadamu. Idadi zisizohesabika za watu huenda wakafikiri kwamba sasa ni wenye akili mno, ni watu wa kisasa mno, wasiweze kuabudu miungu ya kisiasa. Na hata hivyo, namna gani juu ya kuabudiwa kwa Serikali yenyewe? Au juu ya taratibu ya ulimwengu pote ya kisiasa ya utawala? Tangu mwanzo wa serikali za kisiasa zilizofanywa na wanadamu maelfu ya miaka iliyopita, umati mkubwa wa wanadamu wamekuwa wenye hatia ya ibada hiyo ya Serikali. Kusema hivi si kutia chumvi.

3, 4. (a) Serikali ya kisiasa ilianzaje duniani, na kwa sababu gani hakuna sababu nyingi za kuupinga uhakika huo? (b) Katika Ufunuo 13:1-8, Yohana anafananishaje kuanza kwa serikali hiyo?

3 Karne kumi na tisa zilizopita, mwanadamu ambaye ameandikwa katika historia na ambaye maandishi yake yamesomwa na mamia ya mamilioni mpaka sasa, alitumia mifano ya waziwazi aonyeshe namna ibada ya ulimwenguni pote ya taratibu ya siasa ya kibinadamu ilivyoanzishwa. Ilianzishwa na mtu fulani ambaye mwanadamu huyu, Yohana mwana wa Zebedayo, alimfananisha na joka jekundu. Yohana hampi joka huyu maana ambayo taifa la China linampa joka wake anayependwa sana mwenye kichwa kimoja. Yohana anamtumia joka huyo kama mfano unaomfaa mtu mwenye uwezo unaozidi wa kibinadamu, ambaye Yohana anatambulisha kwa usemi wa “joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani.” (Ufu. 20:2; 12:3, 9) Je! ni kuwazia tu, je! ni upumbavu kusadiki kwamba taratibu ya kibinadamu ya siasa ilitokana na huyu? Tufikiriapo namna taratibu za kisiasa zilizofanywa na wanadamu zimetawala na kutenda tangu nyakati za kale, hakuna sababu nyingi za kupinga uhakika wa kwamba taratibu ya kisiasa ilianzishwa na Shetani Ibilisi. Na tuangalie sasa namna Yohana anavyofananisha hili:

4 Akifananisha wanadamu wote wenye kusumbuka, wasioridhika, wenye choyo na bahari isiyotulia, Yohana anaendelea kusema hivi: “Naye [yaani, joka jekundu] akasimama juu ya mchanga wa bahari. Kisha nikaona mnyama akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba, na juu ya pembe zake ana vilemba kumi,na juu ya vichwa vyake majina ya makufuru. Na yule mnyama niliyemwona alikuwa mfano wa chui, na miguu yake alikuwa kama miguu ya dubu, na kinywa chake kama kinywa cha simba; yule joka akampa nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi. Nikaona kimoja cha vichwa vyake kana kwamba kimetiwa jeraha la mauti, na pigo lake la mauti likapona.Dunia yote ikamstaajabia mnyama yule. Wakamsujudu yule joka kwa sababu alimpa huyo mnyama uwezo wake; nao wakamsujudu yule mnyama, wakisema, Ni nani afananaye na mnyama huyu? Tena ni nani awezaye kufanya vita naye? . . . akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa. Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu.”​—Ufu. 12:17–13:1-8.

5, 6. Mnyama huyo mwenye umbo baya sana anafananisha nini, kulingana na ndoto ya Danieli ya wanyama waliotoka baharini?

5 Watu waliuliza hivi: “Ni nani afananaye na mnyama huyu?” Hivyo sisi tunauliza: Ni mfano wa nini? Kutokana na masimulizi ya Yohana juu ya mnyama huyu wa mfano na yanayompata, hakuwezi kuwako shaka juu ya anachofananisha.

6 Sehemu aliyo nayo mnyama yule katika kitabu cha Ufunuo yaonyesha anachofananisha, taratibu ya ulimwenguni pote ya utawala wa kisiasa juu ya wanadamu wote. Uhakika wa kwamba yule mnyama alionekana kama chui lakini alikuwa na miguu ya dubu na kinywa cha simba unapatana sana na uhakika wa kwamba taratibu ya ulimwengu ya siasa imejionyesha yenyewe katika namna mbalimbali za serikali katika nyakati na mahali mbalimbali. Bila shaka Yohana aliongozwa afikirie aliyoona nabii wa kale Danieli katika ndoto ya unabii: ya kwamba kwanza ni mnyama aliye kama simba aliyetoka katika bahari yenye msukosuko, kisha mnyama aliye kama dubu, na baada yake mnyama aliye kama chui. Tena, Danieli aliambiwa waziwazi kwamba wanyama hao walifananisha tawala za kisiasa ambazo zingetokea na kuitawala dunia kama mataifa yenye nguvu mno. (Dan. 7:1-18) Hivyo yule mnyama mwenye sura mbaya ambaye Yohana aliona alifananisha taratibu ya ulimwenguni pote ya kisiasa ambayo imejionyesha yenyewe katika namna nyingi za serikali.

IBADA YA SERIKALI KAMA MUNGU

7, 8. (a) Kuabudu mnyama wa mfano wakati uo huo kulikuwa kuabudu nani? (b) Kwa sababu gani kuabudu Serikali ni jambo la kufikiriwa na watu hao wanaokataa kwamba wao hawaabudu cho chote?

7 Si lazima kuzungumza hapa mambo yote juu ya alichoona Yohana katika njozi yake iliyoongozwa na Mungu. Jambo kubwa hapa tunalotaka tukazie fikira zetu ni kwamba “mnyama” huyu kutoka baharini aliabudiwa na ulimwengu mzima wa watu; alitendewa kama mungu asiyeshindika. Kuabudiwa kwa Serikali ya kisiasa kama mungu, kulikofananishwa hivyo katika njozi ya Yohana, wakati uo huo kulikuwa ndiko kuabudiwa kwa mtu fulani aliye mkuu zaidi kuliko na Serikali ya kisiasa. Huyo alikuwa nani? Huyo alikuwa Shetani Ibilisi aliye kama joka, kwa maana anafananishwa kama akiipa Serikali ya kisiasa mamlaka, uwezo, kiti cha enzi au kiti cha serikali.

8 Kwa hiyo, si ajabu kwamba Bwana ambaye Yohana alikuwa mwanafunzi wake alinena juu ya Shetani Ibilisi kama “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 14:30; 16:11, NW) Na Paulo, mwanafunzi mwenzi wa Yohana, alimwita Shetani Ibilisi “mungu wa taratibu hii ya mambo.” (2 Kor. 4:4, NW) Hili ni jambo la kufikiriwa na watu wengi hao leo wanaojisifu kwamba hawaabudu cho chote hata kidogo, Je! wao, kama Wakomunisti wasioamini kuwako kwa Mungu, wanaiabudu Serikali ya kisiasa? Huenda wakakana kufanya hivyo, lakini ulizo zito la kitaifa linapotokea, vita ya kati ya mataifa inapotokea au utawala wa kitaifa unapohatirishwa, hapo wanafanya nini? Ndiyo, ni nini wanachoabudu kama mungu wakati huo? Mwendo wao wa tendo ndipo unapoifunua kweli na kuonyesha wazi kabisa kwamba wanayosema kwa vinywa vyao si kweli.

9. Imempasa kila mmoja wetu ajiulize ulizo gani juu ya ibada, na huenda wanasiasa wenye ukaidi wakauliza ulizo gani wakati wa kufanya uamuzi?

9 Leo utukuzo wa taifa unaenea duniani pote. Bila kujali kama mtu anajidai kuwa mwanadini au sivyo, hakuna mtu anayeweza kuliepa ulizo la kipekee, Mimi naabudu nani au nini? Nguvu isiyoonekana inayoongoza taratibu ya mambo ya ulimwenguni pote ya siasa, yaani, Shetani Ibilisi aliye kama joka, ataka, kwa siri, amlazimishe kila mkaaji wa dunia amwabudu kupitia kwa Serikali ya kisiasa. Walakini, haifai kumwabudu yeye, kwa maana, karibuni siku fulani, yeye mwenyewe atafunuliwa kama mungu wa uongo. Lakini haitawezekana kumfunua Mungu wa kweli wa ulimwengu wote kama mwongo. Je! kwa unyofu wa moyo twataka kumwabudu Huyo? Wakati wa kuamua kwetu juu ya hili hauwezi kukawizwa zaidi. Hasa itawapasa wanasiasa wa ulimwengu huu wafanye uamuzi wenye kukata maneno juu ya wanalotaka kweli kufanya katika habari hii. Utakuwa ole kwao ikiwa wakati huo, kwa kukaidi, watauliza ulizo hili, ‘Ni nani Huyo (Yeye tuliyetajiwa kwa jina), hata wote, kutia na sisi wanasiasa, wamwabudu Yeye?’

10, 11. Ni wakati gani ulizo kama hilo lilipoulizwa na Farao wa kale wa Misri, na kwa sababu gani?

10 Tunayo historia ya kutusaidia tuamue vizuri. Sasa itawafaa watawala wa kisiasa na wanaowaunga mkono wakifikirie kisa cha kweli cha mkuu wa serikali ya kale ya kisiasa aliyetokeza ulizo lilo hilo. Mtu huyo alikuwa Farao mfalme wa karne ya kumi na sita kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Kisa kilikuwa wakati alipokabiliwa na ndugu wawili Musa na Harumi, na wazee wengine wa watu wa Israeli waliotumikishwa. Ndipo ulizo juu ya aliyekuwa Mungu wa kweli lilipojaribiwa. Akimtumia Haruni kama mneni wake, Musa alimwambia Farao hivi: “[Yehova], Mungu wa Israeli, asema hivi, Wape watu wangu ruhusa waende, ili kunifanyia sikukuu jangwani.” Ikiwa Farao anayeambiwa hapa alijiona kama Mafarao wengine kuwa mungu, yeye hakutaka akane uungu wake mwenyewe kwa kumtii Mungu wa watu wale ambao Farao wakati huo alikuwa akiwatumia vibaya kama watumwa wa Misri. Basi, likarudi ulizo la Farao lenye kukaidi na jibu lake mwenyewe:

11 “[Yehova] ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusu waende zao? Mimi simjui [Yehova], wala sitawapa ruhusu waende zao.”​—Kut. 5:1, 2; 3:18, 19.

12, 13. (a) Hapa palikuwa na mpambano kati ya nani na nani, na ni nani aliyeshinda? (b) Mkombozi wa Israeli alikuwa na haki ya kutoa amri gani iliyohusu ibada mwanzoni mwa Amri Kumi?

12 Kwa vyo vyote, hali hiyo ilimaanisha mpambano kati ya Mungu wa Waisraeli watumwa na Farao wa Misri, ambaye yaelekea sanamu yake kama mungu iliwekwa kati ya sanamu za miungu mingi mingine yote ya Misri, ambalo wakati huo lilikuwa ndilo taifa lenye nguvu mno la dunia inayokaliwa na watu. Historia yenye kutegemeka inaonyesha aliyekuwa mshindi katika mpambano huu mkubwa. Miungu yote ya Misri ya kale ilifunuliwa kuwa ya uongo, na Mungu mshindi wa Waisraeli akawatoa katika nyumba ya utumwa, kuvuka Bahari ya Shamu mpaka kwenye Mlima Sinai Uarabuni, alikowapa Amri Kumi na mamia ya sheria nyingine za kuwaongoza kama taifa. Mwanzoni mwa hizo Amri Kumi Mkombozi wa kimungu wa Waisraeli alikuwa na haki kamili ya kuamuru watu wake waliokombolewa, akisema hivi:

13 “Mimi ni Yehova Mungu wako, ambaye amekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya watumwa. Haikupasi uwe na miungu mingine yo yote mbele ya uso wangu. Haikupasi ujifanyie wewe mwenyewe sanamu ya kuchonga wala umbo mfano wa cho chote kilicho katika mbingu juu wala kilicho duniani chinichini wala kilicho katika maji chini ya dunia. Haikupasi uvipigie magoti wala kushawishwa kuvitumikia, kwa sababu mimi Yehova Mungu wako ni Mungu mwenye kutaka ibada ya pekee, niletaye adhabu juu ya wana kwa sababu ya kosa la akina baba, juu ya kizazi cha tatu na juu ya kizazi cha nne, kwa habari ya wale wanaonichukia mimi; lakini nikitumia fadhili za upendo kuelekea kizazi cha elfu kwa habari ya wale wanaonipenda mimi na kushika amri zangu.”​—Kut. 20:1-6, NW.

14. Yehova Mungu anatofautianaje na “mungu wa taratibu hii ya mambo” kwa habari ya sanamu, na kwa sababu gani?

14 Hizo za kwanza mbili za Amri Kumi zatambulisha kwa jina Mungu asiye na kifani, Mungu ambaye sifa yake hailinganishwi na ile ya ye yote aitwaye “mungu,” hata Shetani Ibilisi mwenyewe, “mungu wa taratibu hii ya mambo.” Shetani Ibilisi anaruhusu sanamu za kuabudu zifanywe hata zake mwenyewe na zile za “miungu” inayoshirikiana naye. Lakini Mungu ambaye jina lake ni Yehova anakataza kabisa kufanyizwa kwa sanamu yo yote ya kuwa badala yake na anakataza sanamu nyingine zo zote za kuabudu zisishirikishwe na ibada Yake. Yeye hawezi kulinganishwa na kitu cho chote kilichoumbwa, sanamu yo yote iliyofanywa na wanadamu. Kupitia kwa nabii mwingine aliyekuja baada ya Musa, alisema hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu; sitampa mwingineo utukufu wangu mwenyewe, wala sifa yangu sanamu za kuchonga.”​—Isa. 42:8, NW.

15. Kwa sababu gani Yehova aweza kusemwa kuwa “Mungu mwenye wivu,” na kwa hiyo ni ulizo gani ambalo huenda wakuu wa kisiasa wakauliza juu ya jambo hili?

15 Tangazo hili la kimungu lataka ibada ya pekee imwelekee Yehova kama Mungu na linazuia matumizi ya sanamu zote zinazofanywa na wanadamu na zinazopewa ibada ya kadiri fulani. Kwa sababu ya kutoonekana kwake huenda wanadamu wakadhani kwamba Yeye anahitaji sanamu zifanywe zisaidie waabudu kuelekeza uangalifu wao kwake Yeye. Lakini sanamu hizo zingekuwa uongo mtupu, zisiweze kumfananisha Yeye namna alivyo kweli. Kwa kweli zingekuwa zikipotoa fikira za mwabudu na kupunguza sifa ya Mungu katika kukadiri kwa mwabudu huyo. Mungu mmoja aliye hai na wa kweli hawezi hata kufananishwa na sanamu iliyofanywa isiyo na uhai. Yeye hajishirikishi mwenyewe na yo yote inayojifanya yenyewe iwe miungu, na haiwapasi waabudu wake wa kweli ‘wawe na miungu mingine yo yote mbele ya uso wake,’ kama washiriki pamoja naye katika uungu wa kweli. Yeye anadai ibada ya pekee kutoka kwa waabudu wake, na kwa sababu hii anaweza kusemwa kuwa “Mungu mwenye wivu.” Wapende wasipende, viumbe vyake vyote vyenye akili vitatakiwa vimtolee yeye ibada ya pekee ikiwa vyataka kuishi kwa furaha milele. Kwa sababu hii, wale wenye mamlaka ya kisiasa leo huenda wakatumia usemi wa Farao na kuuliza, “‘Yehova ni nani,’ hata wote wamwabudu yeye?”

VITU VYA KIMWILI VYAABUDIWA KAMA MUNGU

16, 17. (a) Zaidi ya Serikali, watu wanaabudu vitu gani vingine leo? (b) Watu wengi wanafanyaje kupenda mno vitu vya kimwili kuwa mungu kwao wenyewe?

16 Bila kufahamu unalofanya kweli, umati ulio mkubwa wa wanadamu unamwabudu yule “mnyama” wa mfano, Serikali ya kisiasa ambayo, katika namna moja au namna nyingine, inatawala “kila kabila na jamaa na lugha na taifa.” (Ufu. 13:7) Lakini kuna mambo mengine ambayo wanadamu wenye choyo na wasiokamilika wanaweza kutukuza kama miungu katika maisha zao. Sayansi ya kisasa imefanywa kuwa “ng’ombe mtakatifu” wa kuabudiwa katika maisha za wengi wanaodhani kwamba wanasayansi wa kibinadamu wanaweza kufanya cho chote, kutatua magumu yote. Vile vile, katika wakati huu wenye michezo na tafrija za namna nyingi sana, kuna kusifu mno kwa “mabingwa” wa michezo na waimbaji maarufu, mabingwa wa sinemani na wachezaji maarufu wenye kupigiwa vifijo vya sifa wa redio na televisheni. Uasherati sikuzote unaendelea kupata waabudu zaidi na zaidi wakati kanuni za zamani za adili na adabu zinapopungua.

17 Vile vile, katika wakati huu ambapo ulimwengu wa wanadamu umekuwa na vifaa vingi sana vya starehe, vifaa vya kufanya kazi iwe nyepesi, vitu vya kusafiria kwa haraka kufika mbali, na vyakula vya namna nyingi, huenda mtu akashawishwa atafute wingi wa vitu hivi. Au, kupanda kwa bei za ulimwengu na ongezeko lake la magumu ya kiuchumi huenda kukamlazimisha mtu asumbukie zaidi kupata vitu vya kimwili. Vyo vyote iwavyo, huenda akawa mpenda vitu vya kimwili mno, hata asiwe na wakati au asipendezwe na mambo ya kiroho. Ijapokuwa huenda asipende kukubali hivyo, kupenda mno vitu vya kimwili kumekuwa mungu kwake.

18. Je! kuabudu Vitu vya Kimwili ni hekima, na kwa sababu gani Aguri bin Yake hakutaka kupewa utajiri wa vitu vya kimwili mpaka atosheke?

18 Ibada ya Kupenda Mno Vitu vya Kimwili si ya hekima. Bila shaka itaharibu hali ya mtu ya kiroho. Aguri bin Yake, mtu wa nyakati za kale aliyetaka kuepuka ibada yenye hatari ya miungu ya uongo, alizitambua hatari za kupenda mno vitu vya kimwili. Akisema na Muumba wa dunia, upepo na mvua, Aguri alisema hivi: “Nimekuomba mambo mawili. Usininyime kabla sijafa. Uniondolee mbali ubatili na uongo. Usinipe umaskini wala utajiri. Acha nile chakula kilicho kadiri yangu, nisije nikashiba nikakukana na kusema: [Yehova] ni nani? wala nisiwe maskini sana nikaiba, na kulitaja bure jina la Mungu wangu.”​—Mit. 30:1, 7-9.

19. Ni nia gani juu ya Mungu ambayo kupenda mno vitu vya kimwili kunafanyiza katika mtu mwenye pupa kama Ile ya wanasiasa, na kwa sababu gani mwenye kupenda mno vitu vya kimwili hatapata uzima kutoka kwa Mungu?

19 Katika ulimwengu ambamo mna utajiri mwingi mno na pia umaskini mbaya sana, ni lazima tuwe kama Aguri bin Yake na kufuata mwendo huo ulio salama. Inatupasa tuepuke mambo hayo mawili yawezayo kutuzuia tusimwabudu Mungu wa kweli. Wingi wa vitu vya kimwili kwa kusudi la kutosheleza pupa waweza kututia katika hali ile ile kama watawala wa serikali ambao ni wenye pupa ya uwezo wa kisiasa, hata wanatumia maneno yenye kukaidi ya Farao wa kale na kusema: “[Yehova] ni nani?” Ikiwa hiyo ndiyo nia inayofanyizwa, si na uwezo wa kisiasa tu bali pia na pupa ya mali za kimwili, basi mtafutaji wa mali nyingi mno za kidunia anafanya Vitu vya Kimwili, si Yehova, viwe Mungu wake? Kwa kuwa Yehova ni Mungu mwenye wivu, yaani, Mungu anayetaka ibada ya pekee ya waabudu wake, mtu hawezi kutumikia vyote viwili wakati ule ule apate zawadi ya uzima wa milele mikononi mwa Mungu wa kweli.

20. Mtu mmoja mwenye hekima zaidi kuliko Aguri alisema nini juu ya kujaribu kutumikia Mungu na Mali wakati ule ule mmoja?

20 Mtu mwenye hekima zaidi kuliko Aguri bin Yake alisema hivi: “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali [Mammon].”​—Mt. 6:24, Authorized Version ya King James.

21. Wale wanaojidai kutokuamini mungu ye yote hata hivyo ni wenye hatia ya ibada ya namna gani?

21 Leo wanadamu wote wananaswa katikati ya majeshi ya utukuzo wa taifa na kupenda mno vitu vya kimwili. Wengi wanaabudu vyote viwili, taifa na kupenda mno vitu vya kimwili. Wengine, ijapokuwa hawapendezwi sana na siasa za kitaifa, wanaikubali ibada ya kupenda mno vitu vya kimwili. Ni mtu gani duniani leo awezaye kusema kwamba yeye haabudu cho chote? Huenda akafikiri kwamba, kwa sababu yeye anajivunia kutosadiki katika Mungu ye yote mwenye akili, yeye haabudu mungu wala miungu. Lakini akijichunguza kwa unyofu, ataona kwamba anafanya utukuzo wa taifa, kupenda mno vitu vya kimwili, michezo, mambo ya wanaume na wanawake, tumbo lake mwenyewe, na mambo mengine ya kichoyo, kuwa miungu yake na kuitumikia. Zaidi ya hayo, katika kuabudu mambo haya ya ulimwengu, pasipo kujua anamwabudu mwenye choyo, Shetani Ibilisi, “mungu wa taratibu hii ya mambo.” Hakuna faida ya mtu kujipumbaza mwenyewe. Sote na tuwe wanyofu kwetu wenyewe na kuyakubali mambo ya hakika.

22. Kwa sababu ya mambo ambayo ibada ya miungu hiyo imeletea watu, inawapasa watu wawe wakifikiri namna gani juu ya ibada?

22 Kuabudiwa kwa miungu yote hii ya uongo kumeuleta ulimwengu katika hali yenye taabu ulimo leo. Kuabudiwa kwa miungu yote hiyo hakukuleta amani, furaha na hali njema ya jamii yote ya kibinadamu. Mtu ye yote mwenye akili angefikiri kwamba sasa ni wakati kwa watu walio katika taabu watilie shaka kama inafaa tena kuitumikia miungu ambayo imewaletea fadhaa na matatizo hayo. Inawapasa wafahamu kwamba lazima aweko Mungu wa kweli, Mungu mwenye faida ya kweli na yenye kudumu kwa waabudu wake. Huyo angeweza kuwa nani?

23, 24. Ni Mungu gani anayepinga miungu yote hiyo ya uongo, Naye ni Mungu wa Biblia kwa njia gani?

23 Kuna Mungu mmoja tu aliye tofauti na miungu mingine ile yote ya uongo na yenye hatari. Yeye si Mungu asiyejulikana kwa jina. Jina lake limetangazwa kote kote katika nchi hasa tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka wa 1918. Jina lake ndilo mashuhuri kuliko yote katika kile kitabu ambacho kimepata kuenezwa zaidi kati ya wanadamu kuliko kitabu cho chote kilichopata kuchapwa, na katika kitabu hicho jina lake laonekana karibu mara elfu saba. Kitabu hicho ndicho kitabu kimoja kilichoongozwa na Mwenye jina hilo lenye kutajwa mara nyingi. Kwa sababu hiyo kitabu hicho ndicho chenye kushambuliwa kuliko vitabu vyote katika ulimwengu wote, hata ikawa kwamba ndicho kitabu kati ya vyote ambacho watu hawakiamini. Kitabu hicho chaitwa Biblia Takatifu, Maandiko Matakatifu. Jina la Yeye ambaye Biblia inaandika tangu mwanzo mpaka mwisho kama Mungu ni Yehova. Hivyo yeye ndiye Mungu wa Biblia. Hakuna faida kupinga uhakika huu, kwa maana katika Zaburi 83:18 Biblia yasema hivi:

24 “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”

25. Ni akina nani hasa ambao wamekabilishwa na ulizo la ukaidi juu ya kuabudu Yehova, nasi sasa twaiendea Biblia tukiwa na maulizo gani juu Yake?

25 Hasa tangu mwaka wa 1919 C.E., waabudu wake, wanaojulikana ulimwenguni pote kama mashahidi wa Yehova wa Kikristo, ndio wamekuwa wenye kulitangaza na kulitukuza jina lake mpaka sasa katika dunia yote katika nchi na visiwa vya bahari zisizopungua 207. Kwa kufaa sana, wao ndio wamekabilishwa na ulizo hili la ukaidi, “‘Yehova ni nani,’ hata wote wamwabudu yeye?” Hilo ni ulizo la maana. Lastahili jibu lenye mamlaka. Jibu lenye mamlaka liwezalo kutoa mkazo unaofaa wenye kusadikisha linatokana na Biblia peke yake, Kitabu cha Yehova. Ndani yake, anasema nini juu yake mwenyewe? Ndani yake, ameandikisha nini juu ya kazi zake na matendo yake na wanadamu? Yeye yu bora namna gani kuipita miungu mingine yote ambayo wanadamu wameabudu katika vizazi vyote? Atafanya nini juu ya hali ya mambo ya sasa ya ulimwengu? Atathibitishaje kwamba yeye peke yake ndiye anayestahili sisi tumwabudu kama Mungu? Hivyo, basi, na tuiendee Biblia Takatifu tupate majibu!

[Picha katika ukurasa wa 460]

Mkuu mwenye mamlaka wa serikali alisema hivi wakati mmoja kwa njia ya ukaidi: ‘Yehova ni nani, hata nisikilize sauti yake?’

[Picha katika ukurasa wa 461]

. . . Yeye alijua​—akiwa amechelewa mno​—wakati ukaidi wake kwa Mungu wa kweli ulipomwongoza yeye na wale waliomfuata kwenye msiba

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki