Sababu Hatukuambiwa “Siku Ile na Saa Ile”
“Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.”—Mt. 24:42.
1. (a) “Dhiki kubwa” inayokuja itamaanisha nini kwa wakaaji wote wa dunia? (b) Kama ilivyosemwa kwa unabii katika Mathayo 24:30, ni wakati gani ‘Mwana wa Adamu atakapokuja na mawingu ya mbinguni’?
WAKATI unakuja ambapo wakaaji wote wa dunia wataelekeana na tukio ambalo litamaanisha ama uzima ama kifo kwao. Yesu Kristo alilitaja kwa unabii aliposema hivi: “Wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” Kwa sababu ya kuuona uwezo wake wa kuharibu, huo ndio wakati “mataifa yote ya ulimwengu . . . watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi,” nao watajipiga-piga wakijisikitikia kwa sababu ya jambo litakalowapata.—Mt. 24:21, 22, 30.
2. Tunajuaje kwamba kutakuwa na waokokaji wa “dhiki kubwa” hiyo?
2 Lakini, ingawa ndivyo itakavyokuwa kwa “mataifa yote” kwa ujumla, sivyo itakavyokuwa kwa kila mtu, na si lazima iwe hivyo kwako mwenyewe. Kwa sababu gani? Kwa sababu Yesu alisema katika unabii uu huu kwamba ‘watu’ fulani wangeokolewa. Akitoa tumaini zuri ajabu, akajulisha kwamba wengine wangeachiliwa wawe na tumaini la “uzima wa milele.” (Mt. 24:22; 25:46) Na zaidi ya miaka 60 baada ya kutoa unabii huo alimfunulia mtume Yohana kwamba, wangekuwako watu ambao ‘wangetoka katika dhiki ile iliyo kuu’ wakiwa waokokaji “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” (Ufu. 7:9-14) Kwa kuchukua hatua inayofaa sasa, huenda wewe ukawa mmoja wa waokokaji hao.—Sef. 2:2, 3.
ITAKUWA WAKATI GANI?
3, 4. Mitume wa Yesu Kristo walikuwa wakifikiria nini walipouliza ulizo lililoandikwa katika Mathayo 24:3?
3 Kwa sababu sisi wenyewe pamoja na wapendwa wetu tunataka usalama, ni kawaida kuuliza hivi, “dhiki kubwa” hii itakuja wakati gani? Je! Biblia inatuambia?
4 Mitume wa Yesu Kristo waliuliza ulizo linalofanana na hilo: “Mambo haya yatakuwa lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” (Mt. 24:3, NW; Marko 13:3, 4) Walikuwa wakifikiria nini walipouliza ulizo hilo? Walikuwa wakiuliza juu ya wakati tuishio? Mistari inayotangulia katika Biblia inaeleza. Inaonyesha kwamba wakati uo huo tu ndipo mitume walipokuwa wametoka katika eneo la hekalu katika Yerusalemu pamoja na Yesu naye akayaambia makutano hivi: “Hamtaniona kamwe tangu sasa, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la [Yehova].” Nao walipokuwa wakiondoka katika eneo la hekalu, akawa amewaambia wanafunzi wake hivi akiyataja majengo ya hekalu: “Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa.” Hii kwa wazi ingemaanisha mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi. (Mt. 23:38-24:2) Mitume walikuwa wakiyafikiria mambo haya walipouliza ulizo lao.
5. (a) Je! jibu la Yesu lilizungumza juu ya mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi? (b) Tunajuaje kwamba jibu lake lilitia ndani mambo mengi zaidi ya hilo?
5 Yesu alijibu ulizo lao, lakini jibu lake likahusu mambo mengine zaidi ya yale yangeipata taratibu ya mambo ya Kiyahudi tu. Usemi unaotumiwa katika Mathayo 24:21, 22 waonyesha kwamba alikuwa akifikiria “dhiki kubwa” ambayo isingekuwa na kifani cho chote katika historia ya kibinadamu. Tena, katika mstari wa 30 (katika New World Translation) alionyesha kwamba “makabila yote ya dunia” yangehusika, si Wayahudi peke yao. Na katika sura ya 25, mstari wa 32, akatia ndani “mataifa yote.”
6. (a) Ni sehemu gani ya Mathayo sura ya 24 yenye utimizo zaidi ya mmoja? (b) Ni katika sehemu gani ya ulimwengu hasa utimizo wa kisasa umetukia?
6 Yote yaliyoandikwa katika Mathayo sura ya 24, mstari wa 4 mpaka wa 22 yalitimizwa huko nyuma katika karne ya kwanza, kati ya mwaka wa 33 na wa 70 C.E. Lakini yanahusu siku zetu pia, tangu mwaka wa 1914 C.E. ambao Biblia na historia ya kilimwengu pia inauonyesha kuwa mwaka wa maana katika historia ya ulimwengu. Matukio yenye kutimiza unabii wa Yesu yameonekana hasa katika nchi zinazofanyiza kilichofananishwa na Yerusalemu wa kale usioaminika, yaani, katika Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) ambayo inajidai kuwa katika uhusiano wa agano na Mungu wa Biblia.
7. Tangu mwaka wa 1914, ni kwa njia gani wadanganyifu wamekuja wakisema, ‘Mimi ndiye Kristo’?
7 Kama vile Yesu alivyosema kwa unabii, tangu mwaka wa 1914 C.E. wamekuwako wadanganyifu ambao wamejitokeza kama wenye kutimiza daraka la Masihi, wakisema, ‘Mimi ndiye Kristo.’ (Mt. 24:4, 5; Marko 13:5, 6) Wengine wa hawa wamekuwa viongozi wa kidini, kama vile mtu aliyejiita “Baba Mtukufu” na kuitwa “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” kuanzia mwaka wa 1930 na kuendelea. Wengine wamekuwa wanasiasa—kwa mfano, Nkrumah, aliyekuwa mtawala wa Ghana aliyepanga vingine maneno ya Yesu Kristo akaomba watu wake hivi: “Utafuteni kwanza ufalme wa kisiasa.” Hata Ukomunisti wa Kirusi umejidai kwamba utaleta baraka za Kimasihi za “Paradiso” kwa watu wake.
8. (a) Je! “vita na matetesi ya vita” yaliyosemwa kwa unabii na Yesu ni tofauti na ‘kuinuka kwa taifa juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme’ alikosema? (b) Je! ‘kuinuka kwa taifa juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme’ kunamaanisha vita vya ulimwengu tu?
8 Wakati uo huo kumekuwa na “vita na matetesi ya vita” kwa sababu ‘taifa limeinuka, juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme.’ (Mt. 24:6-8; Marko 13:7, 8) Inafaa kuangaliwa kwamba kumekuwa na vita vya ulimwengu viwili visivyo na kifani katika historia ya kibinadamu. Walakini, kumbuka kwamba usemi wa Yesu ‘taifa juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme’ ulihusu karne ya kwanza pia, kwa hiyo hauhusu vita vya ulimwengu tu. Vita vimeleta upungufu mbaya sana wa chakula na magonjwa, kama ilivyosemwa kwa unabii. Matetemeko ya dunia ya kuogofya “mahali mahali” yametokea pia katika siku zetu. Wewe unayafahamu mambo haya, kwa sababu ndizo habari zinazosikika kila siku katika kizazi chetu.
9. (a) ‘Habari njema za ufalme’ zimehubiriwa kwa kadiri gani katika siku zetu? (b) “Jina” ambalo kwa ajili yake wafuasi wa Yesu wamekuwa vyombo vya kuchukiwa na mataifa yote ni nini?
9 Ingawa hali zenye magumu zimetokea, kutia na kuzuka kwa uasi, mashahidi wa Yehova wa Kikristo wamehubiri ‘habari njema za ufalme’ katika “dunia yote inayokaliwa na watu,” ndiyo, katika zaidi ya nchi 200. Mamilioni ya watu wamewasikia kwa furaha, lakini wao wamekuwa pia “vyombo vya kuchukiwa na mataifa yote” kwa ajili ya jina la Bwana yao. Mambo haya pia yalikuwa yamekwisha semwa kwa unabii. (Mt. 24:9-14, NW; Marko 13:9-13) Kutumia tu jina “Yesu” siko kumeleta chuki hiyo juu yao; wengi wanaojidai kumwamini Yesu hawateswi kwa kufanya hivyo. Lakini mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanaonyesha kwamba Yesu Ndiye aliyetiwa mafuta na Mungu awe Mfalme mpya wa dunia naye ndiye mtu wa pekee ambaye kupitia kwake wanadamu wanaweza kumfikia Mungu kwa njia yenye kukubaliwa. (Luka 19:11-23; Yohana 14:6; Matendo 4:12) Hilo ndilo “jina,” au kinachomaanishwa nalo, ambalo linakasirisha watu wanaojaribu kwa choyo kufuatia mipango yao wenyewe.
10. (a) Katika karne ya kwanza, ni nini kilichokuwa kionyo kwa wafuasi wa Yesu waukimbie Yerusalemu? (b) “Chukizo” lilikuwa nini, napo “patakatifu” liliposimama palikuwa nini?
10 Katika karne ya kwanza, miaka 33 baada ya Yesu kutoa unabii wake, kulitokea jambo ambalo lilikuwa kionyo kwa wafuasi wake watoke kabisa nje ya Yerusalemu na ujirani wake. Yerusalemu wenyewe ‘ulizingirwa na majeshi yenye kupiga kambi,’ majeshi ya taifa lile lile ambalo mfalme wake ndiye aliyechaguliwa na Wayahudi badala ya Yesu Kristo. (Yohana 19:12-15) “Chukizo la uharibifu” lililosemwa kwa unabii, yaani majeshi ya Kirumi yakiwa chini ya Cestius Gallus, lilikuwa “limesimama katika patakatifu” huko Yerusalemu, “mji mtakatifu” wa Wayahudi. Hiyo ilionyesha kwamba wakati ulikuwa umefika kwa wale walioamini maneno ya Yesu Kristo wakimbie, wasijaribu kuokoa mali za kimwili. “Dhiki kubwa” ilikuwa karibu sana, nayo ilikuwa jambo lisilo na kifani katika historia ya Yerusalemu. Kwa ulinzi wa Mungu njia ikawa wazi ya kukimbia wakati majeshi ya Kirumi yalipoondoka kwa muda.—Mt. 24:15-22; Luka 21:20-22; Marko 13:14-20.
11. (a) Katika karne ya 20, “chukizo” limekuwa nini, napo “patakatifu” ni nini? (b) Itakuwaje kwa Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) kwa sababu ya kutumainia utawala wa kibinadamu badala ya ufalme wa Mwana wa Mungu?
11 Sehemu hii ya “ishara” imetimizwa pia kama zile nyingine zilivyotimizwa katika karne ya 20. Mwaka wa 1918 ndipo Federal Council of Churches (Baraza ya Mwungano wa Makanisa) ilipoushangilia Ushirika wa Mataifa kama “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani,” ikionyesha kwamba wao kweli walipendelea utawala wa kibinadamu badala ya kunyenyekea mamlaka ambayo Mwana wa Mungu Yesu Kristo alikuwa amepewa juu ya mataifa huko mbinguni. (Ufu. 11:15; 12:10) Lo! hili lilikuwa “chukizo” kama nini kwa Yehova Mungu! “Heshima” kama hizo zimelundikwa juu ya mrithi wa Ushirika, Umoja wa Mataifa, kwa njia hiyo ukawekwa mahali panapoonwa na Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) kama “patakatifu.” Lakini Biblia inasema kwa unabii kwamba “chukizo” hili, yaani Umoja wa Mataifa, ndilo litakaloleta uharibifu kwa wale wanaolitumaini, kwanza kwa Jumuiya ya Wakristo (ambayo inakaziwa fikira zaidi katika unabii wa Yesu ulio mkuu) kisha kwa sehemu nyingine yote ya Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. (Ufu. 17:1-5, 16-18) Hili halitakuwa jambo dogo. Alipokuwa akilisimulia, Yesu alisema kwamba “wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.”
12. Ili kuepuka uharibifu katika “dhiki kubwa” hiyo, lazima sisi mmoja mmoja tuchukue hatua gani?
12 Ili kuepuka kukatiliwa mbali katika dhiki hiyo, ni jambo la haraka kukimbia sasa, kutoka katika Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu), kujitenga kabisa na makanisa yake. Ni lazima kuonyesha kwa matendo wala si kwa maneno matupu kwamba mtu hapatani na unafiki wa Jumuiya ya Wakristo, ambayo imejidai kumwamini Kristo lakini ikashindwa kutumia mafundisho yake na badala yake ikajitia katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu. Ili awe kati ya waokokaji, lazima mtu ‘asiupende ulimwengu wala vilivyomo ulimwenguni’—hata sehemu yo yote yake—bali lazima awe mfuasi wa Mwana wa Mungu.—1 Yohana 2:15-17.
13. Utimizo wa kwanza wa Mathayo 24:4-22 umehusuje kwa kufaa matazamio ya Wakristo wa kweli?
13 Kumbuka kwamba sehemu yote hiyo ya unabii wa Yesu ulioandikwa katika Mathayo sura ya 24, mstari wa 4 mpaka wa 22, ina matumizi mawili kama ilivyoonyeshwa na matukio yaliyokwisha onekana. Utimizo wake wa kwanza ulitia nguvu kusadiki kwa Wakristo wa kweli kwamba mambo yaliyobaki nayo yatatimia pia.
BAADA YA DHIKI YA YERUSALEMU
14. (a) Mambo yaliyosemwa kwa unabii katika Mathayo 24:23-28 yanatukia wakati gani wa historia? (b) Kwa hiyo kuna tofauti gani kati ya onyo lililotolewa juu ya “Makristo wa uongo” lililoandikwa katika Mathayo 24:24 na onyo linalopatikana katika mistari ya 4 na 5?
14 Yaliyoandikwa katika Mathayo sura ya 24, mstari wa 23 mpaka wa 28, yanagusa matukio yaliyoanza kuonekana mwaka wa 70 C.E. na kuendelea mpaka siku za kuwapo kusikoonekana kwa Kristo (parousia). Onyo juu ya “Makristo wa uongo” halirudii tu yanayosemwa katika mstari wa 4 na wa 5. Mistari hiyo ya baadaye inasimulia kipindi kirefu zaidi—wakati ambapo watu kama vile Bar Kokhba Myahudi aliongoza uasi juu ya waonezi wa Kirusi miaka ya 131-135 C.E., au wakati wa baadaye ambapo kiongozi wa dini ya Bahai alijidai kuwa ndiye Kristo aliyerudi, na wakati ambapo kiongozi wa Wadoukhobor katika Canada alijidai kuwa ndiye Kristo Mwokozi. Lakini, hapa katika unabii wake, Yesu alikuwa ameonya wafuasi wake wasidanganywe na madai ya wanadamu wenye kujifanya.
15. Kufahamu kwamba kuwapo kwa Yesu kusingeonekana kungelindaje wanafunzi wake wasidanganywe?
15 Aliwaambia wanafunzi wake kwamba kuwapo kwake kusingekuwa katika nchi yao tu, bali kungekuwa kama umeme “utokavyo mashariki ukaonekana hata magharibi,” kwa maana angekuwa Mfalme asiyeonekana mwenye kuelekeza fikira zake duniani kutoka mbinguni. Kwa hiyo, akawaomba wawe wenye busara kama tai, na wafahamu kwamba chakula cha kweli cha kiroho kingepatikana kwa Yesu Kristo peke yake, yeye ambaye imewapasa wamkusanyikie kama Masihi wa kweli katika kuwapo kwake kusikoonekana, ambako kungeanza mwaka wa 1914 na kuendelea.—Mt. 24:23-28; Marko 13:21-23; tazama God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached, kurasa 320-323.
TANGU MWAKA WA 1914 C.E. NA KUENDELEA
16. Matukio yanayosimuliwa katika Mathayo 24:29–25:46 yanatimia katika kipindi gani?
16 Kama vile kulinganisha Maandiko na matukio ya historia kunavyoonyesha, kutoka mstari wa 29 katika sura ya 24 ya masimulizi ya Mathayo mpaka mwisho wa sura ya 25, matukio yanayosimuliwa yanafikia upeo katika kipindi kilichofuata mwaka wa 1914 C.E. Bila shaka, mengine ya matukio haya yalianza kutukia katika karne ya kwanza, lakini utimizo wa mwisho yanaoelekeza kwake ni katika karne ya 20. Ndivyo ilivyo kwa yale yanayosemwa juu ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” pia mifano ya wanawali kumi na talanta.—Mt. 24:45-47; 25:1-30.
17. (a) “Dhiki” inayotajwa katika Mathayo 24:29 ni nini? (b) Inawezaje kusemwa kwamba matukio yaliyoanza kutukia mwaka wa 1914 C.E. yanatukia “mara, baada ya” lililotukia mwaka wa 70 C.E.?
17 Wakati Mathayo 24:29 inapotaja jambo litakalotukia “baada ya dhiki ya siku zile,” inazungumza matukio yaliyoanza kutukia tangu mwaka wa 1914 C.E., na hiyo ilikuwa baada ya “dhiki kubwa” iliyoupata Yerusalemu mwaka wa 70 C.E. Ni kweli kwamba, kulingana na maoni ya mwanadamu mwenye maisha mafupi, huenda matukio ya siku zetu yasionekane kuwa yanakuja “mara, baada ya” yale yaliyotukia mwaka wa 70 C.E. Lakini Mungu, ambaye kwake miaka elfu ni “kama siku ya jana ikiisha kupita,” ana maoni tofauti juu ya mambo.—Zab. 90:4; linganisha “upesi” katika Ufunuo 1:1.
18. Eleza utimizo wa Mathayo 24:29.
18 Tangu mwaka wa 1914 C.E. imetukia sawa na ilivyosemwa kwa unabii: “Jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa mwanga wake, na nyota zitaanguka mbinguni, na nguvu za mbinguni zitatikisika.” Kuanzia mwanzo wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, wanadamu waliingia katika kipindi cha giza kweli kweli. Hakukuwa na mwanga juu ya wakati ujao kutokana na vyanzo ambavyo mwanadamu alizoea kutegemea. Kulingana na historia, mbingu halisi pia zilionwa kuwa makao ya ndege. Lakini mapema katika karne ya 20 mwanadamu alifaulu kurusha ndege-ulaya, ambayo karibuni ilitumiwa kwa makusudi ya vita. Hii ikafanya maroketi yenye kuua yatengenezwa, hata vyombo vilivyopeleka wanadamu mwezini, mpaka anga ikaonekana inaweza kuwa kituo cha kijeshi cha kuongozea dunia. Wakati uo huo, woga wa mwanadamu uliongezeka ilipokuwa ikichunguzwa na kuonekana kwamba dunia ilikuwa ikipigwa na miale ya jua na nyota kutoka anga za juu. Mbingu halisi zimeanza kuonekana na watu wengi katika kizazi hiki kuwa zenye dalili ya taabu inayokuja, si kwa sababu mbingu zenyewe zimebadilika, bali kwa sababu ya mambo ambayo mwanadamu mwenyewe anafanya na kwa sababu ya ujuzi wake ulioongezeka unaohusu nguvu za anga za juu ambazo hawezi kuziongoza.—Mt. 24:29; Marko 13:24, 25.
19. Haya yote yanaelekeza kwenye tukio gani linalosimuliwa katika Mathayo 24:30?
19 Haya yote yanaelekeza kwenye mwisho wa taratibu hii ya mambo, kwenye wakati ambapo, kama Mathayo 24:30 inavyosema, ‘itaonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza.’ Wakati huo sasa u karibu sana!—Marko 13:26.
20. Kwa sababu gani si kila mtu ‘atakayeomboleza,’ nao mstari unaofuata unaonyeshaje hivyo?
20 Walakini, si kila mtu atakayehuzunika wakati ‘Mwana wa Adamu atakapokuja na uwezo’ kuharibu taratibu hii mbovu ya mambo. Kufikia wakati huo, “wateule” wote, wafuasi 144,000 wa Yesu Kristo waliotiwa mafuta kwa roho watakuwa wamekwisha kusanywa, kama vile Yesu alivyosema kwa unabii. (Mt. 24:31; Marko 13:27) Wengine pia wanajiunga na watiwa mafuta hao kwa wingi, wakishiriki pamoja nao kutoa ushuhuda kwa mataifa yote juu ya ufalme wa Mungu wa Kimasihi.—Zek. 8:23.
21. Tunawezaje kuwa na hakika kwamba wakati wa “kuja” kwa Mwana wa Adamu u karibu sana?
21 Wao hawana shaka juu ya utimizo wa mambo aliyoyasema Yesu kwa unabii. Yesu alisema hivi: “Basi kwa mtini jifunzeni mfano; tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno u karibu; nanyi kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa [Mwana wa Adamu] yu karibu, milangoni.” “Hayo yote” aliyotaja kwa unabii yanaweza kuonekana sasa waziwazi kabisa.—Mt. 24:32-34; Marko 13:28, 29.
KUHAKIKISHA WAKATI
22. Ni “kizazi” kipi ambacho Yesu alimaanisha kingeona “kuja” kwake akiwa na uwezo wa kuharibu?
22 Ni wakati gani basi Mwana wa Adamu atakapokuja na uwezo wa kuharibu awaondoe wote katika dunia hii wanaopenda uovu? Yesu mwenyewe anajibu hivi: “Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” (Mt. 24:34; Marko 13:30) “Kizazi” hicho ni kipi? Ni kile ambacho kimeshuhudia matukio yenye kutimiza unabii tangu mwaka wa 1914 C.E. Hakuna shaka juu ya ukweli wa aliyoyasema Yesu. Kwa kutia mkazo akaendelea kusema hivi: “Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita.”—Mt. 24:35; Marko 13:31; linganisha Mathayo 5:18.
23. Yesu alisema nini juu ya kama kulikuwa na mtu mwenye kujua “siku ile na saa ile” ya tukio hilo?
23 Je! Yesu alitoa maelezo zaidi ya haya, akawaambia wanafunzi wake wakati barabara wa kutukia kwa jambo hili? Sivyo, yeye aliwaambia kwamba “siku ile na saa ile” haikujulikana na kiumbe cho chote, naye akatilia jambo hilo mkazo kwa kulirudia-rudia mara tano. Alisema, “Habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.”—Mt. 24:36–25:13.
24. Katika utimizo wa karne ya kwanza wa unabii juu ya “dhiki kubwa,” je! wanafunzi wa Yesu waliambiwa mapema wakati barabara ambapo dhiki kubwa ingetokea?
24 Kumbuka kwamba katika utimizo wa karne ya kwanza wa unabii wa Yesu juu ya “dhiki kubwa,” hawakupewa tarehe ya mapema juu ya wakati ambapo walipaswa waukimbie Yerusalemu. Bali, walipaswa wakeshe waone ishara fulani—‘chukizo, kama lilivyonenwa na nabii Danieli, limesimama katika patakatifu.’ (Mt. 24:15, 16) Ilionekana mwaka wa 66 C.E. Kwa kutii wafuasi wa Yesu walitoka mjini, na kulingana na vile maandishi ya historia yanavyosema, wakakaa upande mwingine wa Mto Yordani katika jimbo la Pella lenye milima. Walakini, baada ya hapo miaka kadha ilipita kabla ya “dhiki kubwa” kuupata Yerusalemu mwaka wa 70 C.E. Hakuna kinachoonyesha kwamba wafuasi wa Yesu waliambiwa mapema wakati dhiki hiyo ingetokea. Walikuwa wamekwisha ingia katika mahali pa usalama; hakukuwa na sababu yao kutaka kujua.
25, 26. Kwa sababu gani uhakika wa kwamba Nuhu alipashwa habari mapema juu ya siku ambapo gharika ingekuja hautuwekei msingi wa kutazamia tupashwe habari za mapema juu ya “siku” ile na “saa ile” ya kuja kwa “dhiki kubwa”?
25 Lakini je! Yesu mwenyewe hakuzilinganisha siku za Nuhu na wakati wa kuwapo kwake? (Mt. 24:37-39) Na je! Nuhu hakuambiwa mapema siku barabara ambapo gharika ingeanza? Ndiyo, lakini sababu ya Nuhu kuambiwa “siku ile” hailingani na hali yetu. Nuhu na jamaa yake walipaswa waujue wakati ambapo gharika ingeanza ili waweze kuingiza aina zote za msingi za wanyama wawe salama safinani kisha wao wenyewe waingie kabla maji ya gharika hayajaanza kuporomoka. Hili ni jambo ambalo wasingaliweza kulifanya miezi mingi mapema, kwa maana kama wangalifanya hivyo akiba ya chakula ingalikwisha mapema isivyofaa. Kwa hiyo Mungu alimwambia Nuhu katika wakati barabara hivi: “Baada ya siku saba nitainyeshea dunia mvua, siku arobaini mchana na usiku; na kila kilicho hai nilichokifanya juu ya uso wa nchi nitakifutilia mbali.”—Mwa. 7:4.
26 Walakini, sisi hatuna haja ya kujua “siku ile na saa ile” ambapo hatua ya Mungu ya kuharibu itaanza. Sisi hatukupewa wanyama tuwalinde waokoke wala kuhifadhiwa kwa watu wenye kumcha Mungu, wanaopatikana sasa katika zaidi ya nchi 200 kuzunguka dunia, hakutegemei kuingia kwao wote ndani ya mjengo halisi katika mahali pamoja. Kutimizwa kwa kusudi la Mungu, kutia na kuhifadhiwa kwa watu wake, hakuhitaji wajulishwe mapema “siku ile na saa ile.”
MATUMAINI KWA WAOKOKAJI
27. Ili kuwa kati ya waokokaji wa “dhiki kubwa,” lazima matakwa gani yatimizwe?
27 Biblia inaonyesha wazi kwamba watakuwako waokokaji wa “dhiki kubwa” inayokuja, nayo inaonyesha mambo yanayotakiwa kwa kuwa kati ya waokokaji hao. Ufunuo 7:14 wausimulia “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa dhiki, ukisema: “Wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Hii maana yake ni kwamba “dhiki kubwa” itakapotokea kwa ghafula wao wataonekana safi na wenye kukubalika mbele za Yehova Mungu. Watakuwa walitakiwa wafanye nini? Kuonyesha imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa kama msingi wa kusamehewa dhambi zao, vile vile kuendelea kujitahidi kufanya mapenzi ya Mungu.—Yohana 3:36; Yak. 2:26.
28. Kuna matumaini gani huko mbele kwa wale watakaoiokoka “dhiki kubwa” hiyo?
28 Matumaini yatakayokuwa mbele ya “mkutano mkubwa” wa waokokaji yatakuwa mazuri ajabu. Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, “atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai.” (Ufu. 7:17) Wakiwa wameachwa huru na taratibu zote za uonezi ambazo zimeshiriki kufanya maisha duniani yawe yenye kuchukiza, “mkutano mkubwa” wakati huo watakuwa katika hali nzuri kabisa ya kuondolewa udhaifu na kutokamilika kwa kibinadamu. Yesu Kristo atatumia kwao faida kamili za dhabihu yake yenye kulipia dhambi. Watakapokuwa wakiuitikia msaada wake kwa utii, watafanya maendeleo mpaka wakamilike. Kwa njia hii magonjwa, uzee na kifo kinachosababishwa na dhambi na kutokamilika kulikorithiwa zitaharibiwa milele mwishowe. (Ufu. 21:3-5) Hata madhara yaliyosababishwa na kifo yataondolewa kabisa mamilioni mamilioni yatakapokuwa yakifufuliwa kwa wafu. (Yohana 5:28, 29) Watakaofufuliwa watakuwa pia na nafasi ya kupata uzima usiokoma.
29. Jambo la hekima kwetu mmoja mmoja kufanya sasa ni nini?
29 Kwa kweli “siku ile na saa ile” ya kutokea ghafula kwa dhiki yaweza kumaanisha kwako ama uzima ama mauti. Basi, je! usingekuwa mwendo wa hekima kwako kuhakikisha kwamba unaishi sasa kana kwamba “siku ile na saa ile” itakuja kesho? Sisi hatujui “siku ile na saa ile” ambapo “dhiki kubwa” itatokea. Lakini hiyo haibadili uhakika wa kwamba inakaribia mbio mbio. Kipindi chote kinaonyeshwa waziwazi katika Neno la Mungu. “Kizazi” ambacho Yesu alisema kwa unabii kingeona matukio ya mwaka wa 1914 na “dhiki kubwa” pia sasa kimezeeka. Hiyo inaendelea kuonyesha hali ni yenye haraka nayo imepaswa itufanye tufikirie kwa uangalifu kama sisi wenyewe tunaishi kwa kutambua kabisa kwamba “siku ile na saa ile” ya hukumu ya Mungu imekaribia sana.
[Picha katika ukurasa wa 484]
Yesu Kristo alisimulia kwa wafuasi wake matukio ambayo yangeelekeza kwenye mwisho wa taratibu ya mambo
[Picha katika ukurasa wa 487]
Walipokwisha kukimbilia usalama, hakukuwa na haja ya Wakristo kujua wakati barabara ambapo “dhiki kubwa” ingetokea kwa ghafula juu ya Yerusalemu