Maswali Kutoka kwa Wasomaji
●Nyakati nyingine mume wangu ananipiga. Je! nitengane naye au nimtaliki kisheria?
Ni wazi kwamba mume au mke anapotenda mwenzake vibaya anafanya kosa; Neno la Mungu linakataza watu wasifanye hivyo. Lakini Biblia inahimiza wenzi wa ndoa wakae pamoja pia. Wewe peke yako ndiwe unayeweza kuamua kama hali yako ya nyumbani imezidi kiasi hata mtengano uhitajiwe.
Yehova alianza ndoa iwe njia ya kuzaa na kuwa na ushirika wenye kufurahisha. (Mwa. 2:18-24) Wakati mume na mke wa kwanza walipokataa uongozi wa Muumba wao na kuchagua kufuata njia yao wenyewe, ugomvi na huzuni uliingia katika ndoa yao. Akitangulia kuona kwamba wanawake wasio wakamilifu wangepinga ukichwa wa waume, na kwamba katika ndoa nyingi waume wasiokamilika wangetumia ukichwa wao vibaya, Mungu alimwambia mwanamke hivi: “Tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala.” (Mwa. 3:16) Ni jambo la kusikitisha kwa sababu utawala huo umekuwa wenye ukatili na jeuri mara nyingi.
Kwa sababu ya ndoa kuwa na matendo ya jeuri mara nyingi, wakuu wametunga sheria kuhusu tatizo hilo. Kwa mfano, kitabu Corpus Juris (Vol. 19, kur. 47, 48) kinasema: “Kuendelea kutendwa matendo ya jeuri yenye kuumiza mwili au kuujeruhi, na vilevile kuogopa kwamba huenda wakati ujao mambo yakawa hatari, kunakubaliwa kama sababu ya kutosha ya talaka karibu katika mahakma zote. Si wakati kila jeuri ndogo tu inapofanywa . . . Jeuri halisi inayoweza kuleta talaka lazima iwe imekuwa ya kuhatirisha uhai, mkono au mguu, au afya ya mtu.”
Walakini, jambo hilo ni gumu kufahamika kwa maana mume na mke pia wanaweza kuwa na kosa, na huenda wote wawili wakawa wameshiriki kufanya kuwe na tatizo hilo. Nyakati nyingine mke asemapo kwamba mumewe anampiga, mume anadai kwamba yeye anampiga mkewe ili kujitetea tu au kujaribu kumpa adhabu. Kitabu American Jurisprudence (Vol. 26, uku. 641) kinasema: ‘Kulingana na kanuni, kutumia nguvu kwa njia yo yote ni kumtenda mke jeuri, isipokuwa wakati ambao kusudi la kufanya hivyo ni kumlazimisha atii usimamizi ambao jamaa inapewa, kwa mfano kwa kumzuia asiwe mwenye hasira-hasira na kumfanya awe na adabu njema.’
Kama mume wako angekuwa ni Mkristo, hapo ungeweza kuomba halmashauri ya hukumu ya wazee wa kundi lako ikusaidie. Kwa kuzungumza naye juu ya sheria ya Mungu huenda wakamsaidia aone uhitaji wa kubadili njia zake. Biblia inasema kwamba ugomvi, hamaki (hasira ya ghafula) na ubishi ni “matendo ya mwili” yanayoweza kumwondoa mtu katika Ufalme wa Mungu. (Gal. 5:19-21; Mt. 5:22) Kwa hiyo, mtu ye yote anayejiita Mkristo, anayehamaki-hamaki bila kutubu, anaweza kutengwa na ushirika.
Lakini inaonekana kwamba mume wako haamini, kwa hiyo huenda akawa hajali sana maoni ya Mungu. Hata hivyo, unaweza kuwaomba wazee wakusaidie. Bila shaka, wao hawatajaribu kujiingiza katika ndoa yenu. Lakini ikiwa mume wako anaweza kukubali kuzungumza nao ili hali nyumbani ziwe na maendeleo au yeye mwenyewe afurahie maisha kwa njia nzuri zaidi, wazee wanaweza kuwasaidia nyote wawili.
Wanaweza kutumia busara na Maandiko ili kuonyesha ubora mwingi wa utulivu na subira na sababu inayofanya hasira nyingi iletee wote wanaohusika huzuni nyingi. (Mit. 14:17, 29; 22:24, 25) Wanaweza kueleza habari za kielelezo ambacho Kristo aliwekea waume; yeye alionyesha upendo, kwa hiyo ni wazi kwamba upendo hauruhusu mume atende mkewe vibaya. (Efe. 5:25-33) Mume anayefuata kielelezo hicho atafanya maisha yampendeze zaidi yeye mwenyewe pamoja na mkewe. Vilevile, huenda wazee wakaweza kuwasaidia nyote wawili mjichunguze mwone upande mnaoweza kufanya maendeleo. Je! labda mume wako anakupiga kwa sababu ya kunywa kileo? (Mit. 23:29, 30) Inawezekana kwamba analeta matata nyumbani mwake kwa sababu huko kazini kunatokea mambo ya kumvuruga moyo? Ewe mke, je! ndiwe unayefanya akupige? Je wewe unamnung’unikia-nung’unikia au kumwudhi? “Kutona-tona daima . . . na mwanamke mgomvi ni sawasawa.” (Mit. 27:15; 19:13; 21:9 25:24) Je! wewe ndiwe unayeongeza makaa katika moto wakati kunapokuwa na ubishi, badala ya kutulia? “Upendo . . . hauudhiki.”—Zab. 139:23, 24; 1 Kor. 13:4, 5, NW; linganisha Waefeso 4:26.
Lakini namna gani mume wako akiendelea kuwa mwenye jeuri ajaposaidiwa hivyo? Je! Biblia inasema kwamba lazima mke aendelee kukaa na mumewe hata anapompiga-piga na kuhatirisha afya na uhai wake? Tunasoma hivi: “Mwanamke, ambaye ana mume asiyeamini, na mume huyo anakubali kukaa naye, asimwache mumewe.” (1 Kor. 7:13) Nyakati nyingine huenda mke Mkristo akaamua mwishowe kwamba mumewe mwenye kumtenda jeuri ‘hakubali kukaa naye.’ Hapo huenda mke akaona kwamba jambo la mwisho ambalo lazima afanye ni kutengana au kutalikiana naye kisheria ili ajipatie ulinzi. Kwa habari hiyo, Biblia inashauri hivi: “Mke asiachane na mumewe; lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe.” —1 Kor. 7:10, 11.
Kwa kuwa mke mwenye tatizo hilo la ndoa ndiye anayepaswa kujifanyia uamuzi wa mwisho, unapaswa ufikirie sana mambo haya: Ukiendelea kukaa naye, huenda ukaweza kumsaidia awe Mkristo baadaye? (1 Pet. 3:1, 2) Je! utashindwa kushirikiana sana na watoto wako au kuwafundisha habari za Mungu kwa sababu ya kutalikiana au kutengana na mumeo? Namna gani kutoshelezwa nyege zako? Talaka ambayo msingi wake si uasherati haitakupa uhuru wa kuolewa tena, basi je! nyege zitakusumbua? (Mt. 19:9) Je! utalazimika kutafuta kazi ya kimwili, halafu kwa njia hiyo ujiletee mikazo na matatizo ya namna nyingine? Je! kazi hiyo itakumalizia wakati unaotumia sasa katika utendaji wa kiroho? Naam, kutengana kunaweza kutatua matatizo fulani, lakini kwa kawaida kunaleta mengine.
Baadhi ya mambo hayo yalihusika katika kisa cha mwanamke mmoja wa Wisconsin. Miaka kadha baada ya kuoana, mumewe alianza kunywa sana mwishoni mwa juma wakati ambao hakuwa akifanya kazi yake ya kukata miti. Kwa sababu ya kunywa vileo, alikuwa akikasirika mara nyingi na kufanya jeuri. Karibu na wakati huo mkewe akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kujaribu kuwa mke mwema sana, asiyeleta ubishi wala kudai mambo yafanywe. Hata hivyo, siku nyingi za Ijumaa wakati mke huyo pamoja na watoto wake waliporudi kutoka mikutano ya Kikristo mumewe alimchapa makofi, akampiga mateke na kumpiga ngumi mikononi. Nyakati mambo hayo yalipokuwa yakitokea mke alikuwa akilazimika kukimbia na kuondoka nyumbani. Yeye pamoja na watoto wake walikaa katika ghala ya majani makavu nyakati nyingi za usiku, na kuziba milango ya ghala hiyo kwa mabunda ya majani mpaka mumewe aliporudiwa tena na fahamu.
“Mbona unaendelea kukaa naye?” watoto walimwuliza mama yao. Yeye aliwaambia alifanya hivyo kwa sababu aliwapenda na hakutaka kuwaacha, na vilevile kwa sababu baba yao alikuwa akiiruzuku jamaa, naye asingeweza kufanya hivyo. Hakuwaambia kamwe kwamba hakumpenda baba yao, bali aliwaeleza kwamba kuijua kweli ya Biblia kulimwezesha kuvumilia na kuwa Mkristo mwenye furaha. Aliendelea kuchapwa zaidi ya miaka ishirini. Sasa anafurahi kwa sababu kumi kati ya watoto wake kumi na mmoja wanamtumikia Yehova, naye mumewe ameacha kunywa, akafanya maendeleo ya kujizuia asikasirike na hata anakwenda na mkewe kwenye mikutano ya Kikristo. Ni kweli kwamba huenda kusiwe na matokeo hayo nyakati zote. Lakini masimulizi hayo yanakuonyesha mambo unayoweza kufikiria kuhusu hali yako.
Basi, kusudi la mashauri yanayotolewa na Biblia ni kwamba wenzi wa ndoa waendelee kujitahidi kukaa pamoja wajapokuwa na matatizo kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu. Lakini, hali zako zikielekea kuwa hatari sana au mbaya sana hata zihitaji kuchukuliwa hatua fulani, hapo lazima uamue kama utatafuta ulinzi kwa kuchukua hatua ya kisheria.
● Katika Yohana 16:5, kwa sababu gani Yesu alisema hivi: “Hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi?” na hali Petro na Tomaso walikuwa wamemwuliza hivyo muda mfupi tu kabla ya hapo?
Maneno hayo yote yalisemwa usiku wa mwisho ambao Yesu alikuwa pamoja na wanafunzi wake. Jioni hiyo Petro aliuliza hivi: “Bwana, unakwendapi?” (Yohana 13:36) Muda mfupi baadaye Tomaso naye alisema: “Bwana, sisi hatujui uendako; nasi twaijuaje njia?” (Yohana 14:5) Kwa hiyo huenda ikaonekana kama kwamba maandiko yanapingana tusomapo maneno ya Yesu katika Yohana 16:5, anaposema: “Hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi?”
Lakini, inaonekana kwamba Yesu alikuwa akifikiria jambo fulani. Hali zilizokuwako kabla Petro hajauliza ulizo lake zinaelekea kuonyesha kwamba alikuwa akijifikiria sana kwa kumwuliza Yesu ulizo alilomwuliza, na labda maneno ya Tomaso yalionyesha alikuwa na wasiwasi akidhani kwamba wanafunzi wasingekuwa na uongozi wa kutosha. Lakini, baada ya wao kuuliza maulizo yao, masimulizi yanaonyesha pia onyo ambalo Yesu alitoa kuhusu mateso ambayo yangekuja. Kama inavyoonyesha Yohana 16:6, maelezo aliyotoa yalisumbua mioyo ya wanafunzi na kuwafanya wahuzunike kuhusu mateso hayo na vile Yesu angeondoka asiwe kati yao. Kwa hiyo wakati Yesu aliposema: “Hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi?” hakuwa akieleza habari ambazo Petro na Tomaso walikuwa wamemwuliza hapo kwanza. Kwa kutumia neno “aniulizaye,” alikuwa na maana ya kwamba wakati uo huo alipokuwa akieleza habari alizokuwa akifikiria, hakuna aliyemwuliza aendako. Basi maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba wanafunzi waliingiwa sana na huzuni wasiendelee kumwuliza Yesu maulizo, zaidi juu ya utukufu ambao angekwenda kupata, juu ya faida ambazo waabudu wa kweli wangepata akipokea utukufu huo na jinsi jambo hilo lingetimiza kusudi la Mungu.