Watu Wenye Juhudi ya Kazi Njema
1. Ni sababu gani zimepaswa zitufanye wenye juhudi ya kazi njema?
MAISHA yenye kusudi ni ya maana. Wakati moyo na akili zinapoungana kutafuta mradi unaofaa, mambo ambayo mtu anafanya kila siku yanakuwa ya maana, yakimpa huyo sababu ya kuishi. Watu wa namna hiyo wamepaswa wahesabiwe kuwa kati ya walio na furaha zaidi ulimwenguni; wale wanaoishi bila kusudi lo lote, wamepaswa wahesabiwe kati ya wenye kukata tamaa zaidi. Tamaa ya asili ya kutaka kuwa wenye furaha ni sababu ya kutosha kujenga maisha zetu juu ya kazi zinazotuletea faida sisi wenyewe na wengine. Juhudi ya kufanya kazi hizo inaleta baraka nyingi.
2. (a) Tunaweza kufuata mfano wa nani? (b) Hiyo itatuongoza kufanya kazi gani njema?
2 Yehova ndiye Mungu wa kazi njema, naye ni mwenye juhudi ya kuzitimiza. Kila jambo analofanya ni la kuwafaidi wanaomtumikia. Yesu aliweka mfano mkamilifu, akamfuata Baba yake. Watu wenye kumcha Mungu wanaotaka kumpendeza Yehova wanaweza pia kutambuliwa kwa kazi njema. Wanafunzi wa Yesu wakijitahidi kufuata mfano wake Baba yake atapata “watu walio mali yake hasa, wenye juhudi ya kazi njema.” (Tito 2:14, NW) Kazi njema za Mkristo ni zile zinazofaidi wengine. Jambo la mafaa zaidi tuwezalo kufanyia mtu mwingine ni kumsaidia amjue na kumtumikia Yehova. Kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ya kundi la Kikristo ni kazi njema yenye kufaidi zaidi. Uhitaji wa kuifanya na haraka yake inaifanya istahili tuifanye kwa juhudi nyingi zaidi kama tuwezavyo.
3, 4. (a) Juhudi ni nini? (b) Imetupasa tujiulize maulizo gani?
3 Juhudi ni nini? Ni bidii. Ni shauku nyingi ya kufanya yaliyo haki na yanayofaa. Palipo na juhudi pana uchangamfu, shauku, msisimko. Kupendezwa na kutaka kujua matokeo yatakavyokuwa kunafanya mtu atake kupata matokeo. Nia yenyewe inakuwa ya kujitahidi, kutumia moyo wote. Pasipo bidii, mtu anafanya mambo kwa sababu ni lazima tu na bila moyo wa kupenda. Anafanya juujuu tu. Hali yake ni baridi baridi. Kwa hiyo, je! wewe unaweza kusemwa kuwa mtu mwenye juhudi?
4 Jiulize kama una juhudi katika kazi njema. Je! unaweza kusemekana kuwa mwenye kusaidia utendaji wa kuhubiri wa kundi lako kwa bidii, kwa nafsi yote? Je! umevutwa na shauku ya kufanya yote uwezayo usaidie wengine wajifunze makusudi ya Yehova? Au, umetosheka na kushiriki tu, bila kupendezwa wala kujitahidi sana?
5. Nia yetu inafunua nini juu ya juhudi yetu?
5 Nia yako ndiyo itakayoamua wingi wa juhudi yako. Mwanafunzi mwenye juhudi kweli kweli hatatanguliza mapendezi yake mwenyewe yasiyo ya lazima, hayaweki mbele ya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Unaposhiriki, je! kushiriki kwako sikuzote kunaamuliwa na saa? Je! unashiriki kwa mwili tu na huku akili inafikiria mambo mengine? Je! mawazo yako yanakuwa juu ya mambo ya kupendeza utakayofanya baadaye, kama vile kutazama kipindi cha televisheni unachopenda sana au kwenda mahali fulani pa kujiburudisha ulikokaribishwa? Huenda utumishi ukaonwa kama jambo la kufanywa haraka haraka ili uingilie mambo unayotaka hasa. Huenda ukauona kama “wajibu” tu wa kufanywa nawe kama mmoja wa mashahidi wa Yehova, ukiutimiza kama wajibu tu na bila ya kuwa na shauku.
6. Kwa sababu gani uhitaji wa kujiadibisha haumaanishi kwamba hatuna juhudi?
6 Pengine wewe si mtu wa kufikiria mambo ya nje. Huenda ikawa ni vigumu kwako kusema na wengine, hasa wageni. Mambo ambayo wengine wanaelekea kuyafanya kwa vyepesi huenda yakawa magumu kwako kuyafanya. Pengine itakupasa ujiadibishe, hata ujilazimishe kuyafanya nyakati nyingine, kuendelea kusema. Hiyo haimaanishi kwamba unakosa juhudi. Katika mambo mengine, huenda juhudi yako ikawa nyingi zaidi kuliko ya wengine kwa maana unayofanya huenda yakaonyesha una imani yenye nguvu na nyingi zaidi. Jambo la maana ni kwako kuwa na shauku moyoni. Unafahamu kwamba imani ya kweli inaambatana na kuonyesha upendo kwa Yehova na kwa mwanadamu mwenzako. Juhudi ya kuhakikisha imani yako inakusaidia umalize vizuizi vinavyokufanya usionyeshe uwezo wako. Upendo mwingi sana unaleta ujasiri unaokufanya usimwogope mwanadamu. Kwa sababu hiyo unafanya kazi njema inayoonyesha juhudi ya kweli ya kutangaza waziwazi imani yako.
JUHUDI HAIPIMWI NA VIPIMO
7. (a) Kwa sababu gani si jambo la hekima kuweka vipimo au miradi? (b) Kipimo cha kweli cha kupimia juhudi ni nini?
7 Nyakati nyingine kumefanywa majaribio ya kuweka kanuni ya jitihada zitakazofanywa na kila mtu kutimiza vipimo fulani. Kwa sababu hiyo juhudi ikawa ikipimwa na kufaulu kwa mtu kutimiza miradi hiyo. Sikuzote hii imetokeza maelekeo ya kujilinganisha na wengine, nako kufanya hivyo hakujapata wakati wo wote kuwa kipimo sahihi wala kinachokubaliwa cha kupimia upendo na juhudi. (2 Kor. 10:12) Hata tukitafuta namna gani, hatutaona vipimo vilivyowekwa katika Neno la Mungu ambavyo lazima vitimizwe katika kuhubiri. Yehova hahesabu juhudi yetu kulingana na kadiri ya kazi tunayofanya. Yeye anaangalia zaidi makusudi yetu, tamaa zilizomo mioyoni mwetu. Takwa walilowekewa wote ni kwamba ‘tulifanye kwa nafsi yote.’ (Kol. 3:23, NW) Mungu anatoa nafasi za namna mbalimbali kisha anaacha kila mtu afanye “kama alivyokusudia moyoni mwake.” Tusipolazimishwa,’ jitihada yetu inaonyesha kweli yaliyomo mioyoni mwetu. (2 Kor. 9:7) Mambo tunayovutwa na mioyo yetu tuyafanye ndiyo yanayokuwa kipimo cha kweli cha juhudi yetu.
8. (a) Kwa sababu gani yanayoweza kufanywa na kila mtu yanatofautiana? (b) Jambo la maana ni nini?
8 Kila mtu akitoa kwa moyo, Yehova anaweza kuhesabu jitihada zetu zote kuwa zenye kulingana, ingawa huenda kadiri inayofanywa na kila mtu ikatofautiana. Hali za kipekee zinatofautiana. Umri, afya, madaraka ya jamaa, kazi ya kimwili na kadhalika, ni mambo yanayoamua kadiri ya utendaji wetu. Mtu mwenye hali zinazofaa huenda akaweza kusema na watu wengi zaidi juu ya ufalme wa Mungu kuliko vile mwingine anavyoweza. Mtu mwenye madaraka zaidi huenda akaweza kusema na watu wachache zaidi. Kwa sababu ya hali kutofautiana, huenda hesabu fulani ya saa ikaonyesha mtu fulani amejitahidi sana lakini ikaonyesha mwingine amefanya kidogo tu. Kwa hiyo, uwezo na nafasi yetu ya kufanya mengi haitupi sababu ya kujivuna, wala utumishi wetu mdogo usiosababishwa na kosa letu wenyewe haupaswi kutuaibisha. Jambo la maana ni kwamba tuwe na juhudi yenye kutuongoza tutumie kwa faida nafasi zo zote tunazozipata.
9. Ni kwa njia gani tunavyoweza kuonyesha juhudi yetu kwa kazi ya kuhubiri?
9 Wingi wa juhudi yetu unaonekana tunapokuwa macho kutumia na kutafuta nafasi za kuzitangaza habari njema, tukitafuta njia za ‘kukomboa’ wakati tufanye mengi zaidi. (Efe. 5:15, 16) Wakati madaraka mengine yanapopungua kwa muda, tunapokuwa na nia ya kuutumia wakati wa ziada unaopatikana katika utumishi wa Yehova unakuwa ushuhuda mzuri kwamba tuna juhudi. Vile vile, tunapochukua hatua ya kurekebisha hali zetu tupate wakati zaidi wa utumishi inaonyesha tuna shauku ya kufanya yote tuwezayo. Mhubiri mwenye juhudi aweza kuangalia kazi yake ya kimwili ilivyo, akitafuta njia za kupunguza wajibu wa kazi hiyo. Badala ya kukubali vivi hivi tu mambo yenye kumwekea vizuizi ati ndiyo apate faida za kimwili, aweza kuomba afanyiwe mabadiliko yatakayompa uhuru zaidi wa kufanya kazi ya Ufalme. Wenye juhudi wanajaribu kutumia wakati, nguvu na mali zao kwa faida zaidi, sikuzote wakijaribu kutanguliza faida za Ufalme.
10. Ni katika njia gani mkulima mwenye bidii ni mfano mwema wa mtu mwenye juhudi?
10 Tunapothamini kwamba uhitaji wa kuifanya kazi kwa haraka unaongezeka inahakikisha tuna juhudi. Mkulima mwenye bidii anajua kwamba imempasa ajitahidi sana sana nyakati za kupanda na kuvuna. Kwa sababu yeye mwenyewe anaona ana daraka la kufanya kazi na anapendezwa sana na matokeo, hafanyi jitihada zake kulingana na kanuni yo yote ya “chama cha wafanya biashara” kinachohitaji mtu ajitahidi kidogo tu kisha alipie kazi nyingine yo yote ya ziada atakayofanya. Yeye anafurahia kufanya kazi saa nyingi na kujitahidi sana inapokuwa lazima. Ikiwa tu wenye shauku nyingi ya kusaidia wengine, tutatumia wakati na nguvu zetu kwa hiari bila ya kufikiria tutakayotazamiwa kufanya. Wakati mambo yanapohitaji kufanywa, nasi tunapewa nafasi tusaidie, kujitoa kwetu bila choyo ni ushuhuda wenye kusifika wa kwamba tuna juhudi.
KAZI NJEMA HAZIHUSU KUUHUBIRI UFALME NA KUFANYA WANAFUNZI TU
11. Je! kuhubiri na kufanya wanafunzi ndizo kazi za pekee zilizo njema kwa Mkristo, na ikiwa sivyo, lazima kazi zile nyingine zionweje?
11 Ingawa tunatia mkazo unaofaa juu ya kazi ya kuhubiri kwa sababu ni ya haraka, bila shaka huo sio utendaji wa pekee unaoweza kutiwa katika “kazi njema.” “Kazi” inaweza kufafanuliwa kuwa “daraka fulani la wazi, wajibu au mgawo ambao mara nyingi ni sehemu ya utendaji fulani mkubwa zaidi.” Kuhubiriwa kwa habari njema ni sehemu ya utendaji mkubwa zaidi unaotia ndani kazi nyingi njema zinazofanywa na Wakristo kwa sababu wanapenda wengine. Ni kosa kudhani kwamba kazi nyingine njema hazina maana sana. Ingawa huenda kazi fulani zikatiliwa mkazo mwingi zaidi nyakati nyingine, kwa ujumla zote zina ubora unaolingana. Kila kazi njema inasaidia kuongeza nguvu, umoja na mazao ya kundi la Kikristo.
12. Ni kazi njema gani zinazoelezwa na Paulo katika Tito 2:1-10?
12 Katika barua yake kwa Tito, Paulo anatufahamisha sehemu mbalimbali za kazi njema za Mkristo. Wanaume walitiwa moyo wawe “wenye kiasi, wastahivu, wenye busara, wazima katika imani na katika upendo na katika saburi.” Nao wanawake wamepaswa wawe wenye bidii “wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe.” Kukiwa na mwenendo huo nyumbani utasaidia moja kwa moja kueneza habari njema. Neno la Mungu ‘halitatukanwa,’ nao watu wa nje ‘hawatakuwa na neno baya la kunena juu yetu.’ Mwishowe hiyo itasaidia ‘kuyapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’ (Tito 2:1-10) Ni wazi basi kwamba hizo zote ni kazi njema ambazo kwazo Mkristo aweza kuonyesha juhudi kwa kufaa.
KUTOKEZA KAZI NJEMA KATIKA JAMAA
13. (a) Ni maulizo gani ambayo huenda yakasaidia wazazi wapime juhudi yao ya kuona watoto wao wana hali njema? (b) Ni faida gani zinazotokana na juhudi hiyo?
13 Nyie wazazi, je! m wenye juhudi mkipenda watoto wenu? Kutaka sana kuona wakiwa na hali njema kunahusu mambo mengi zaidi kuliko kuwapa mahitaji yao ya kimwili tu, kuwapeleka mikutanoni au kujifunza nao Biblia kila juma. Juhudi ya kutaka kuona wakiwa na hali njema inaonyeshwa mnapopendezwa kwa unyofu kuona mambo wanayohitaji na magumu yao. Jiulize hivi: Mimi kweli najua vile watoto wangu wanavyoyaona matakwa ya Mungu? Je! nimewatayarisha kupambana na magumu ambayo huenda yakawakabili wakati ujao? Je! mimi niko macho kuwasaidia waondoe udhaifu mbalimbali kama vile kiburi, choyo, uvivu, na kadhalika? Je! najua wanayofundishwa shuleni na ni kwa kadiri gani wanaongozwa na mawazo ya ulimwengu? Je! watoto wangu wanajiona huru kunifikia na magumu yao au inakuwa lazima niwaulize-ulize? Je! naweza kujua kwamba kuna kasoro fulani kutokana na wanavyoonekana au kutokana na sauti yao? Je! mimi ni mwenye subira ninapojaribu kujua jambo lenyewe? Je! ninawafikiria na kuwahurumia, nikiendelea kuwahakikishia kwamba nawapenda? Unapojaribu kweli kuwajua watoto wako sana, kufahamu magumu yao na kuwasaidia kiroho, unafanya kazi njema inayoletea jamaa yako baraka na kulishuhudia jina la Yehova mtaani.
14. Ni kwa njia gani mke anavyoweza kuwa mwenye juhudi ya kazi njema nyumbani?
14 Maelekeo ya wanawake kuwa wenye ugomvi na wenye kutaka kujitegemea yameleta mafarakano mengi nyumbani na kuongeza talaka. Ni jambo linalostahili kusifiwa sana kumwona mke wa Kikristo akionyesha juhudi ya kazi njema kwa kumtii mumewe kwa upendo. Yeye anafanya mengi zaidi kuliko yanayoweza kutazamiwa ulimwenguni, akionyesha shauku ya kuongeza furaha na hali njema ya mumewe. Wakati mapendezi yao yanapotofautiana, heshima kwa ukichwa wake inamzuia mke asijaribu kumlazimisha mumewe kufanya jambo ambalo amekwisha kataa. Mke anafanya kazi za nyumbani kwa furaha na kupata thawabu yake wakati jamaa inaposhukuru. Kupika vyakula si kazi ndogo ya kila siku isiyo na maana bali ni pendeleo la pekee kutimiza uhitaji unaoongeza afya ya wale ambao mke anawapenda. Anatosheka kuendeleza nyumba yake kuwa malidadi kwa sababu jamaa yake inafurahia mazingira ya kupendeza. Hizi ni kazi njema zinazothaminiwa na jamaa yake, naye kwa haki ‘anajipatia sifa’ kutokana nazo.—Mit. 31:30.
15. Ni kwa njia gani mume anavyoweza kuonyesha juhudi yake?
15 Mume mwenye juhudi anampenda mke wake. Katika njia nyingi ndogo ndogo anajaribu kumpendeza bila kuachilia ukichwa wake wala faida bora za jamaa ndiyo afanye hivyo. Yeye hasisitizi mambo yafanywe yeye mwenyewe anavyotaka sikuzote; anafikiria maoni ya mke. Anamheshimu mkewe sana, si kumwona kama chombo tu cha kutoshelezea nyege zake. Anamfanya ajisikie anahitajiwa, na hii inasaidia mke kuwa mwenye ufundi na msaada zaidi. Juhudi ya mume kuonyesha upendo inamletea yeye mwenyewe pia faida zinazomwongezea furaha.
16. (a) Mkristo awezaje kuonyesha juhudi kwa kazi yake ya kimwili? (b) Faida za kufanya hivyo ni nini?
16 Inafaa Mkristo awe mwenye juhudi katika kazi yake ya kimwili. Hii haimaanishi atafute kwa bidii mali za kimwili ahakikishe jamaa ina usalama wa pesa. Bali, anatimiza wajibu wake kwa tajiri wake kwa nafsi yote, ‘kama kwa Yehova.’ (Kol. 3:22, 23) Anakuwa na tamaa ya kufanya kazi malidadi kabisa. Anajaribu kuwa mfanya kazi mwenye kushirikiana na wengine, mwenye mafaa na mwaminifu. Anatumia saa za kazi kwa faida bora bila kupoteza wakati wala vifaa ovyo ovyo. Anajitahidi kujipatia sifa ya kutegemeka na kutimiza ahadi yake. Kwa sababu hizo, matajiri wamependelea mara nyingi kuandika ndugu zetu wa kiroho. Na jambo la maana hata zaidi ni kwamba, sifa hizo zinafanya habari njema wanazopeleka kwa wengine ziwe za kuvutia zaidi.
17. Kujichunguza kwaweza kuonyesha nini juu yetu?
17 Tukithamini zaidi kazi njema zinazoelezwa katika Neno la Mungu imetupasa tujichunguze vizuri. Huenda kazi zetu zikaonyesha kwa njia nyingi kwamba tuna bidii ya kutenda yaliyo mema. Huenda ikatupasa kukubali kwamba hatukuwa wenye juhudi sana katika mambo mengine. Ikiwa tunataka tuwe wafuasi wanaostahili wa Kielelezo chetu, Yesu, huenda ikatupasa kutumia wakati mwingi zaidi kusitawisha juhudi nyingi zaidi. Ili mtu aweze kufanya maendeleo itampasa kujitahidi sana, lakini faida kubwa zenye kutosheleza zinazopatikana zinafanya kujitahidi kustahili.
MIFANO YA KISASA YA JUHUDI
18. Kichwa kimoja cha jamaa alionyeshaje juhudi yake?
18 Inatia moyo kuona wengine wenye juhudi ya kufanya kazi njema. Tunapata ushujaa tunapoona ndugu zetu wakionyesha juhudi hata wanapokabiliwa na hali zenye kujaribu. Kwa mfano, ndugu mmoja katika nchi ya Amerika ya magharibi ya kusini anatumikia kama mzee aliyewekwa naye ana jamaa kubwa. Anatakiwa afanye mambo mengi kwa maana ana madaraka ya kundi, madaraka ya jamaa na kazi ya kimwili. Hata hivyo, yeye ameziona kazi za kimwili zisizo za kitheokrasi kuwa msaada wa kumsaidia yeye na jamaa yake waweze kushiriki kama iwezekanavyo katika kazi njema za kundi. Alikuwa akifanya kazi ya kimwili kutimiza mahitaji ya jamaa tu, na kumwachia wakati wa kutumikia kama painia wa muda mara nne mwaka jana. Alipoulizwa sababu alifanya hivyo, alijibu hivi kwa wepesi: “Inategemea jambo unalotanguliza maishani . . . jambo linalotangulia hasa moyoni mwako.” Matokeo mengi ya juhudi yake yanaweza kuonekana katika uhakika wa kwamba wahubiri 29 katika kundi hilo walishiriki pamoja naye katika utumishi wa upainia wa muda mwaka uo huo.
19. Dada aliyeolewa alionyeshaje juhudi yake, nayo jamaa yake ikapata baraka gani?
19 Dada aliyeolewa ameonyesha juhudi kama hiyo. Yeye ni mwenye watoto watatu na mumewe si mwamini, na aliweka maisha yake wakf kwa Yehova karibu miaka mitano iliyopita. Kwa kuwa mumewe hakupenda dini sana, alikuwa na mashaka mengi juu ya ubora wa imani ambayo mkewe alidai kuwa nayo. Zamani, mke alikuwa amekosa mara nyingi kuonyesha “roho ya upole na utulivu” katika uhusiano wa jamaa na alipokuwa akishirikiana na wengine. (1 Pet. 3:1-4) Karibuni alipobadili tabia na mwenendo wake mumewe akasadiki vingine. Akaona kwamba mkewe hasisitizi sana juu ya mali za kimwili bali anafikiria sana mwenendo unaofaa wa Kikristo. Ingawa mke alitumia wakati mwingi katika utendaji wa imani yake, mumewe aliona kwamba mkewe alikuwa amezidi kupendezwa naye. Kwa sababu ya mke kutaka kwa unyofu kutii ukichwa wake uhusiano wao ukawa mzuri zaidi. Mume akaona kwamba mke wake ameanza kuwa na shauku ya kutunza nyumba vizuri. Akawa anaangalia watoto zaidi kuliko alivyoangalia mahitaji yao ya kimwili au elimu ya kimwili; wakawa wanajifunza Biblia kila siku. Rafiki za jamaa hiyo wakaona amebadilika kwa vile alivyokuwa mwenye furaha zaidi katika jamaa, na pia kwa sababu ya kuwa na mwenendo tofauti akiwa huko nje, kutia na kuwatembelea katika nyumba zao awape ujumbe wa Ufalme. Juhudi yake katika kutumia kanuni za Biblia ilimfanya awe mke na mama bora, ikaimarisha vifungo vya jamaa yake na kufanya wengine waone nguvu za ibada safi.
20. Ndugu mmoja mzee alihakikishaje ana juhudi?
20 Uzee haukumaliza juhudi ya wengi wa ndugu zetu wazee. Ndugu mmoja mwaminifu aliyetiwa mafuta na anayeshirikiana na kundi la mji wa New York amekuwa akimtumikia Yehova kwa juhudi tangu alipoweka maisha yake wakf mwaka wa 1915. Miaka hiyo iliyopita amepata madaraka ya karibu kila cheo cha uangalizi katika kundi. Ijapokuwa alipatwa na hali zenye kujaribu, hakuruhusu cho chote kipunguze juhudi yake katika kazi njema. Leo, hata akiwa na umri wa miaka 78, anawekea wengine mfano mwema kwa juhudi yake. Wakati afya mbaya inapomzuia asihudhurie mikutano au asishiriki katika utumishi wa shambani, watu wanajua mara moja kwamba hayuko. Mazungumzo yake, maelezo yake mikutanoni, na vile vile sala zake zinaonyesha kila mara kwamba anathamini kweli, kwamba analipenda tengenezo na kwamba anataka kuona wengine wakiwa na hali njema. Kundi linabarikiwa na kuwako kwa huyo ambaye kazi zake njema zinamtambulisha wazi sana kwamba ni mmoja wa “ndugu” waliotiwa mafuta wa Mfalme wa Kimasihi.—Mt. 25:40.
HUU NDIO WAKATI WA KUWA WENYE JUHUDI KATIKA KAZI NJEMA
21. Imewapasa wengine waweze kuona nini ndani yetu?
21 Haraka ya nyakati inayoongezeka inatilia mkazo ubora wa kufanya kazi njema. Sisi kama mashahidi wa Yehova tumekuwa ‘nuru yenye kuangaza kwa ulimwengu.’ (Mt. 5:14-16) Kazi na sifa ambazo wengine wanaziona ndani yetu zimepaswa ziwaongoze wamheshimu Yehova. Yehova mwenyewe amepaswa aweze kuona sisi tukionyesha juhudi ile ile aliyo nayo Yeye ya kufanya kazi njema. Wakristo wa uongo wanaonyesha kazi hiyo pindi kwa pindi tu na kwa sababu zisizofaa. Ikiwa sisi tu Wakristo wa kweli, kila jambo tunalofanya kila siku litaonyesha kwamba tunayo juhudi ya kufanya yaliyo mema, yanayofaa. Matunda ya roho ya Yehova yataonekana waziwazi katika mambo yote tunayofanya na kusema.—Gal. 5:22, 23.
22. Ikiwa tu wenye juhudi kweli kweli, tutafurahia kufanya nini?
22 Hatutatangaza tumaini letu waziwazi saa moja au mbili tu halafu tuache. Tunapokutana na mtu mwingine tutaiona hiyo kama nafasi inayowezekana kwetu kuzungumza naye juu ya imani yetu. Kuhangaikia wenye mfano wa kondoo kutatufurahisha tutakapoweza kutumia wakati na uwezo wetu mbalimbali kuwafundisha. Kwa kuwa tunasadiki habari njema ni bora sana, tutaendelea kuzitoa kwa upole hata kwa wale wanaozikataa kwanza. Ndiyo, “katika mambo yote” tutajitahidi kujihakikisha kuwa “kielelezo cha matendo mema.”—Tito 2:7.
23. Ni kitu gani kinachotuongoza tuendelee kufanya kazi njema, nacho kinatupa tumaini gani la wakati ujao?
23 Kutaka kwetu kuzoea kazi njema kunatokana na shauku nyingi ya kuonyesha upendo wetu kwa Yehova na kuhakikisha kwamba tunafikiria wanadamu wenzetu kama tunavyojifikiria wenyewe. (Mt. 22:37-39) “Dhiki kubwa” inapokaribia, tunajaribu hata zaidi ‘kuwatendea watu wote mema.’ (Gal. 6:10; Ufu. 7:14, 15) Tuna hakika kwamba tukiendelea kufanya kazi njema tutathawabishwa sana. Tunaitazamia kwa furaha siku inayokuja ambapo wanadamu wote duniani pote watazoea kazi njema kwa juhudi kwa kuunga mkono utawala wa Ufalme wa Kristo.
—Kutoka The Watchtower, May 15, 1975.