Kwa Sababu Gani Watu Hawawezi Kusamehewa Dhambi Nyingine?
WAKATI mtunga mashairi Mjeremani Heinrich Heine, alipokuwa akifa na kufikiria maisha ya ufisadi aliyoishi, alijifariji na wazo hili: “Mungu atanisamehe. Hiyo ni kazi yake.” Kwa kusema hivyo, Heine alikuwa akirudia aliyosema mtunga mashairi Mwingereza, Pope, karne moja iliyotangulia: “Kukosa ni kwa kibinadamu; kusamehe ni kwa kimungu,”
Ni kweli kwamba Yehova Mungu hufurahia kusamehe. Ndivyo alivyoandika nabii Mika: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema.” Musa na Daudi pia walitoa ushuhuda kwamba Mungu ana nia ya kusamehe.—Mik. 7:18; Kut. 34:6, 7; Zab. 103:2, 3.
Lakini hatupaswi kukata maneno kutokana na maandiko hayo kwamba Mungu hufurahia rehema sana hata yuko tayari kusamehe watu dhambi zote, hata ziwe za namna gani. Kwa sababu gani? Kwa sababu Yehova ni Mungu mwenye hekima na haki ya hukumu, si mwenye upendo tu. Kama angesamehe watu dhambi zote asingekuwa mwenye hekima wala mwenye haki ya hukumu, nazo sheria zake ni za haki kabisa, kwa kusudi la kuleta amani na utaratibu katika ulimwengu wake wote.
Kama Mungu angesamehe watu dhambi zote angekuwa akiwatia moyo watende dhambi. Kufanya hivyo kungebatilisha sheria zake. Jinsi gani? Kwa mfano, kama watu wote wenye kuvunja sheria za bara-barani wangesamehewa, kungekuwa na faida gani kutunga sheria hizo?
Yehova Mungu alimfanya mwanadamu awe kiumbe chenye uhuru wa hiari; yaani, alimfanya akiwa na uwezo wa kutofautisha kati ya kufanya yaliyo haki kwa kutii sheria ya Mungu na kufanya makosa kwa kutoitii, naye angefanya lo lote la mambo hayo akiwa na uhuru wa kuchagua. Walakini, alipaswa pia kutoa jibu kwa matendo yake. Ndiyo sababu, wakati Yehova Mungu aliponena na Musa juu ya fadhili Zake kuu za upendo na nia Yake ya kusamehe, aliendelea kusema, “lakini hatakosa kamwe kutoa adhabu.” Lakini Yehova hakuwa akimaanisha adhabu ya uharibifu wa milele hapa.—Kut. 34:7, NW.
Lakini, mtume Yohana ataja kwamba ziko dhambi ‘zilizo za mauti,’ yaani, zinazostahilisha mtu uharibifu wa milele, na kwamba ingekuwa kazi bure wengine wakiombea mtu asamehewe dhambi hizo. (1 Yohana 5:16, 17) Ni jambo gani linaloamua kama mtu aweza kusamehewa dhambi fulani au kama hawezi? Ni namna ya dhambi yenyewe na hali. Bila shaka Yehova hakusamehe Adamu na Hawa dhambi zao. Mungu aliwapa amri nyepesi aone kama walithamini mambo; hawakupaswa kula tunda la mti fulani; naye aliwaonya matokeo yangekuwa nini wakilila. Waliumbwa wakiwa wakamilifu katika akili na mwili. Wao walikosa kutii kwa makusudi. Wasingeweza kusema hawakujua, kama mtume Paulo alivyoweza baadaye, wala wasingeweza kudai walikuwa wamerithi kutokamilika na maelekeo ya kutenda dhambi, kama Mfalme Daudi. Kwa hiyo kulikuwa na msingi gani wa kusamehe Adamu na Hawa dhambi zao? Hakukuwa na wo wote!
Bila shaka dhambi aliyotenda Yuda Iskariote ni mmoja wa mifano mibaya sana ya dhambi asiyoweza kusamehewa mtu. Yuda alikuwa ameshirikiana na Yesu miaka miwili au zaidi, akasikia mafundisho ya Yesu, akamwona akifanya miujiza, na alijua Yesu alikuwa Mwana wa Mungu. Bila shaka aliona pia kwamba kikundi chote cha waeneza Injili kilikuwa cha watu wanyofu, waaminifu, na wasio wachoyo. Hata hivyo Yuda alikuwa mnafiki, mwibaji wa makusudi. Naye hakumsaliti Yesu kwa sababu ya pupa tu bali kwa sababu alikuwa na kinyongo na Yesu, kwa kuwa Yesu alikubali kupakwa mafuta ya bei. Alichukizwa kwa sababu alikosa nafasi ya kuiba tena pesa zilizotumiwa kununua mafuta, kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa mweka hazina wa wanafunzi wa Yesu. Kwa kuwa alikuwa amefanya moyo wake ukawa mgumu, alipita kiasi cha kumtubia Mungu, asiweze kumwomba msamaha. Kwa sababu hizo Yesu alimwita “mwana wa upotevu.”—Mt. 26:6-16; Yohana 12:1-8; 17:12.
Waandishi na Mafarisayo wasingeweza kusamehewa dhambi za kumtesa Yesu na kumfisha. Waliweza kuona kwamba Yesu alikuwa ametumwa na Mungu, kutokana na mambo aliyofundisha na miujiza aliyofanya. (Yohana 3:2; 14:11) Lakini kwa sababu alifunua wazi unafiki wao na kuwaambia walitumia watu wa kawaida kwa faida zao, walisema kwa uovu kwamba alifanya kazi hizo kwa uwezo wa Shetani Ibilisi. Yesu alisema hivi juu ya dhambi yao: “Yeye atakayenena neno juu ya [roho takatifu] hatasamehewa katika ulimwengu wa sasa, wala katika ule ujao.”—Mt. 12:31, 32.
Naam, wakati watu hao walipoona roho takatifu ya Mungu ikifanya kazi ndani ya Yesu, akitoa mashetani ndani ya watu, akiponya wagonjwa na kufufua wafu, kisha wakamdhihaki wakisema alikuwa akifanya hayo kwa uwezo wa Ibilisi mwenyewe, walikuwa wakiikufuru roho takatifu ya Mungu. Yesu alifanya vizuri kuwalaumu vikali akiwaambia hivi: “Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje hukumu ya jehanum?”—Mt. 23:33.
Maneno ya mtume Paulo yanaonyesha wazi kwamba yawapasa Wakristo wa kweli wajiangalie wasitende dhambi wasizoweza kusamehewa: “Kwa maana hao waliokwisha kupewa nuru, . . . na kufanywa washirika wa [roho takatifu], . . . wakaanguka baada ya hayo, haiwezekani kuwafanya upya tena hata wakatubu; kwa kuwa wamsulibisha Mwana wa Mungu mara ya pili kwa nafsi zao, na kumfedhehi kwa dhahiri.” Tena anasema hivi: “Kwa maana tukizoea dhambi kwa makusudi tukiwa tumekwisha pokea maarifa sahihi ya kweli, hakuna tena dhabihu yo yote ya dhambi iliyobaki, bali . . . kuna wivu mkali sana utakaowala wale wanaopinga.”—Ebr. 6:4-6; 10:26, 27, NW.
Kwa kuwa Mkristo aweza kutenda dhambi ambazo Mungu hasamehei mtu, hilo lapaswa kuwa onyo kwa Wakristo wote walinde mioyo yao wasije wakawa na hatia ya dhambi hizo. Lakini angalia kwamba, isipokuwa katika kisa cha Adamu na Hawa, dhambi ambazo mtu hawezi kusamehewa ni zile za kuzoea, si dhambi moja tu. Hivyo Wakristo fulani walioacha haki walipokazwa katika Ujeremani ya Nazi na katika Liberia, walitubu baadaye na ikaonekana wazi kwamba Yehova Mungu aliwasamehe. Mfalme Daudi na mtume Petro walisamehewa ingawa walitenda dhambi mbaya sana, lakini hawakuzizoea.
Maadamu tunahuzunika kwamba tumetenda dhambi na kutubu kwa unyofu na kujitahidi kufanya maendeleo ya kushikamana na kanuni ya Mungu, tunaweza kufarijiwa na maneno haya: “Tukienenda nuruni, kama yeye alivyo katika nuru, . . . damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.” Dhambi yote? Naam, yatusafisha dhambi zote ambazo huenda tukatenda tunapotembea nuruni, kwa maana tufanyapo hivyo, hatuwezi kuwa na hatia ya kuzoea kwa makusudi dhambi tusiyoweza kusamehewa. (1 Yohana 1:7) Na twaweza pia kupata faraja kwa sababu Yehova ni mwenye ufahamu na hufurahia kuonyesha rehema kupitia kwa Kristo.—Zab. 103:8-14; Mik. 7:18, 19.