Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 3/1 kur. 105-107
  • Sifa ya Kupendeza ya Wema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sifa ya Kupendeza ya Wema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • IGA WEMA WA MUNGU
  • Wema Mwingi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • “Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”
    Mkaribie Yehova
  • Mweneo Mkubwa Ajabu wa Wema wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Wema—Unaweza Kuusitawishaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 3/1 kur. 105-107

Sifa ya Kupendeza ya Wema

WEMA ni ubora wa adili, kufaa. Sifa hii inaweza kuchangamsha moyo kweli kweli. Ina nguvu nyingi sana za kuongoza watu wafanye yaliyo mema na yenye kufaidi wengine. Kulingana na Biblia, wema ni tunda la roho ya Mungu. (Gal. 5:22) Imefaa basi Mungu akawa ndiye mfano bora wa wema.

Kisa kimoja kilichotukia siku za huduma ya Yesu ya kidunia kinakazia jambo hilo la maana. Kijana mmoja tajiri alimwita “Mwalimu mwema,” kisha akamwuliza, “Nifanye nini nipate kuurithi uzima wa milele?” Yesu Kristo alimjibu kwa kuelekeza fikira za kijana huyo kwa Mungu, akimwambia: “Kwa nini kuniita mwema? hakuna aliye mwema ila mmoja, ndiye Mungu.”​—Marko 10:17, 18.

Kwa kuwa Yesu Kristo alikuwa Mwana mkamilifu wa Mungu, alikuwa na ubora wa adili au wema. Walakini, yeye hakukubali kupewa cheo ‘Mwema,’ kwa sababu yeye mwenyewe alikuwa akifuata tu mfano bora wa wema wa Baba yake. Yesu Kristo alipokataa kupewa cheo ‘Mwema,’ alimtukuza Baba yake akaonyesha ndiye mfano halisi wa wema.​—Linganisha Yohana 7:16-18.

IGA WEMA WA MUNGU

Yatupasa tuhangaikie kuiga wema wa Mungu, kama Yesu Kristo. Twaweza kufanya hivyo tukithamini tu jinsi Yehova Mungu ameonyesha wanadamu wema wake.

Kuwako tu kwa taifa la kibinadamu kunatosha kuhakikisha Mungu ni mwema. Dunia hii ina vitu vingi vizuri sana vya kuendeleza uhai. Hata watu wasio na shukrani hufaidika na mipango ya Mungu ya ukarimu.​—Mt. 5:45; Luka 6:32-35; Matendo 17:25.

Biblia yaonyesha kwamba Yehova Mungu aweza kuwanyima mwanga wa jua na mvua wale wasiomtumikia, akitaka. Lakini, kwa wema wake, ni mara chache sana ametumia uwezo huo, na alipoutumia aliutumia muda mfupi tu na kwa kusudi fulani. (Kut. 10:23; Amosi 4:7; Yak. 5:17, 18) Ni kama vile mtume Paulo alivyowaonyesha wakaaji wa Listra ya kale: “Lakini hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.” (Matendo 14:17) Taratibu zisizokamilika za kibinadamu ndizo zimezuia mamilioni ya watu leo wasifaidike kabisa na mipango mingi ya Mungu, wala si yeye aliyefanya hivyo.

Zaidi ya kuwezesha wanadamu wawe hai, Yehova Mungu alitutolea msingi wa kutuweka huru na dhambi na mauti. Alijipatia hasara kwa kufanya hivyo, akamtoa Mwanawe wa pekee kwa ajili yetu na kumwacha atoe uhai wake kama ukombozi. Bila shaka Yehova Mungu hakuwa na lazima ya kufanya hivyo. Hakuna mwanadamu aliyestahili ukombozi wala faida zake. Sababu ni kwamba, ijapokuwa tunajitahidi sana, tunashindwa kufikia mfano wa Mungu wa wema na haki.

Akikazia upendo mwingi na wema wa Mungu kwa kumtoa Mwanawe kama ukombozi, mtume Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Warumi (5:6-8): “Kwa maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu. Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.”

Kwa njia ambayo Yehova Mungu ameonyesha wema, twaweza kuona kwamba hiyo ni sifa yenye kuelekea upande ufaao. Inahusu kutendea hata watu wasio na shukrani mambo mema na yenye kuwafaidi.

Mtu anayeiga wema wa Mungu hafanyi yaliyo haki halafu anaachia hapo. Ingawa “mtu aliye mwema” ni mwenye haki, asiye na upendeleo, mwaminifu na mnyofu kwa adili, yeye ni mchangamfu, mwenye ufahamu na huruma pia. Yeye hujali watu kweli kweli. Yeye hutafuta nafasi za kuonyesha watu fadhili na huruma, akiwasaidia walio na shida sana kwa moyo wa kupenda na kwa shauku. Akifahamu kwamba Yehova Mungu alimtoa Mwanawe kwa ajili ya ulimwengu wa wanadamu, “mtu aliye mwema” ataka wengine wapokee faida za mpango wa ukombozi, kwa hiyo yeye hujitahidi sana kusaidia wengine waingie pamoja na Muumba katika uhusiano anaoukubali.

“Mtu aliye mwema” anatofautiana sana na mwenye kushikilia sana sheria na kanuni. Hiyo yaonyeshwa vizuri katika habari ya Yesu Kristo na viongozi wa dini ya Wayahudi katika karne ya kwanza W.K. Kwa mfano, siku ya sabato Yesu Kristo alipoona mwanamume mwenye mkono uliopooza, alimhurumia akamponya mkono wake. Walakini, viongozi wa kidini walikasirika sana, wakauchukua uponyi huo kama kuvunja mapokeo ya kushika sabato. Kushikilia maoni yao ya haki kuliwafanya wagumu wasiweze kuhurumia mtu aliyekuwa na shida. (Luka 6:8-11) Ni wazi kwamba nia ya viongozi wa kidini ya kujiona kuwa wenye haki ilikosa uchangamfu. Hata ilikuwa kinyume cha roho ya Neno la Mungu.

Lakini namna gani juu ya mtu afanyaye mambo kwa sababu ni wajibu tu? Kama inavyoonekana wazi katika Warumi 5:6-8, hata anapokuwa haki, wengine hawapendezwi naye. Huenda wakamheshimia kufuata haki, hata huenda wakastaajabia vile anavyofuata kanuni. Lakini wasingejisikia wakitaka kujinyima mambo ili wamsaidie, achia mbali kufa kwa ajili yake.

Sivyo alivyo “mtu aliye mwema.” Yeye anapendezwa sana na wengine na huwafanyia kazi bila kujifikiria mwenyewe, bila kutaka thawabu wala kujipatia mapendeleo ya pekee. Yeye huvuta mioyo ya wengine kwa kujitoa bila kufikiria yake tu. Kufanya hivyo huwafanya watake kumtendea mema. Ni kama vile Yesu Kristo alivyoonyesha: “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa [mapajani] mwenu.”​—Luka 6:38.

Bila shaka mtume Paulo alifanya kama maneno hayo yanavyosema. Alipokuwa akiwakumbusha wazee wa kundi la Efeso alivyowatendea, alisema hivi: “Kwa hiyo kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi. Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”​—Matendo 20:31, 33-35.

Wazee hao walikuwa wamependezwa na Paulo kwa sababu aliwawekea mfano wa kuonyesha wema. Walipoona kulikuwa na uwezekano wa kutomwona tena akiwa na mwili wa nyama, walilia sana “wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu.”​—Matendo 20:37, 38.

Tunapofikiria yale ambayo Yehova Mungu ametufanyia, inatupasa kuiga wema wake, kama mtume Paulo. Kwa kusudi hilo, na tutafute nafasi za kutendea wengine mema, tujitoe bila kufikiria yetu wenyewe, tusaidie walio na shida kimwili na kiroho. Tukifanya hivyo, sisi pia twaweza kupendwa na wengine.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki