Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 8/15 kur. 13-18
  • Wema Mwingi wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wema Mwingi wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wema wa Mungu
  • Wema Waonyeshwa Katika Uumbaji
  • Udhambi na Kuopolewa kwa Ainabinadamu
  • Wema wa Mungu Leo
  • Mweneo Mkubwa Ajabu wa Wema wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Yehova Ni Mfano Bora Sana wa Wema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • “Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”
    Mkaribie Yehova
  • Wema—Unaweza Kuusitawishaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 8/15 kur. 13-18

Wema Mwingi wa Yehova

“Ni mwingi kama nini wema wako, ambao umeweka kama hazina kwa ajili ya wale wanaokuhofu wewe!”—ZABURI 31:19, NW.

1, 2. (a) Ni kazi gani kubwa sana ambayo Yehova alianza wakati fulani zamani za kale? (b) Yehova alisimuliaje tokeo la utendaji wake mbalimbali wa kuumba?

KULIKUWAKO wakati Mungu alipoanza kuumba ‘mbingu kuwa kiti chake cha enzi, na dunia kuwa mahali pa kuweka miguu yake.’ (Isaya 66:1) Rekodi ya kimungu haifunui wakati hilo lilitukia. Inataarifu tu hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.” (Mwanzo 1:1) Wakati wa kipindi cha uumbaji, mamilioni mengi ya vikundi vya nyota yaliumbwa, mengi yakiwa na maelfu ya mamilioni ya nyota. Kuelekea ukingo wa nje wa mojawapo vikundi hivyo vya nyota kulikuwa nyota nyangavu iliyozungukwa na sayari nyingi ndogo kwa kulinganishwa, matufe meusi. Moja yazo ilikuja kuitwa dunia. Ikilinganishwa na nyota nyangavu kubwa, dunia ilikuwa duni (si kitu). Hata hivyo, hiyo ndiyo ambayo Yehova alikusudia iwe mahali pa kuweka miguu yake.

2 Hivyo Yehova aligeuza uwezo wake mwingi wa kuumba kuelekea Dunia-sayari. “Mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” alikuwa kwenye upande wake akiwa Stadi wa Kazi wakati tungamo hilo dogo, lisilo na mwangaza lilipobadilishwa wakati wa kipindi cha “siku” sita ndefu za kuumba. Ikawa, kwa ufananisho, mahali pa kupumzika palipofaa miguu ya Mungu. (1 Wakolosai 1:15; Kutoka 20:11; Mithali 8:30) Hapo ndipo mahali ambapo Mungu alikusudia kuweka aina mpya ya uhai wenye akili: ainabinadamu. Wanadamu wa kwanza wawili, walioumbwa kutoka viasili vilivyopatikana ardhini, waliwekwa katika mazingira yenye kupendeza, ya kiparadiso. (Mwanzo 1:26, 27; 2:7, 8) Tokeo la mwisho la kitendo hicho chenye kutokeza cha uumbaji kilikuwa kikamilifu sana, na chenye kupendeza sana, hivi kwamba Biblia inafunua hivi maoni ya Mungu juu yacho asubuhi—sehemu ya mwisho—ya siku ya sita ya kuumba: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.”—Mwanzo 1:31.

Wema wa Mungu

3. Ni sifa gani yenye kutokeza inayofunuliwa katika uumbaji?

3 Maelfu ya miaka baadaye, mzao wa wale wanadamu wawili wa kwanza aliufikiria wakati wa uumbaji akaandika hivi: “Mambo yake [sifa zake, NW] yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.” (Warumi 1:20) Naam, ubora wa hali ya juu sana wa dunia na wa viumbe walio juu yayo kwa kweli ulikuwa wonyesho wa ajabu wa sifa za Mungu zisizoonekana—mojawapo isiyo ndogo ni wema mwingi wa Mungu. Inafaa kama nini basi, kwamba Mungu alitamka kwamba kila kitu ambacho alikuwa ameumba kilikuwa chema!—Zaburi 31:19.

4, 5. Wema ni nini?

4 Wema ni sifa ya sita ya matunda ya roho ya Mungu yanayoelezwa na mtume Paulo kwenye Wagalatia 5:22. Mafunzo yaliyotangulia katika gazeti la Mnara wa Mlinzi yamezungumzia matunda matano ya kwanza ya roho, yakionyesha umaana wa hizo katika ukuzi wa utu wa Kikristo uliokomaa.a Lakini, ni muhimu kama nini, tusisahau wema! Kwa kufaa, sasa tunatoa uangalifu wetu kwa sifa hiyo.

5 Wema ni nini? Ni sifa au hali ya kuwa mwema. Ni ubora wa kiadili, usafi. Hivyo, hiyo ni sifa chanya (nzuri) inayojionyesha katika kufanya vitendo vyema na vyenye manufaa kuelekea wengine. Tunaweza kuonyeshaje sifa hiyo ya kupendezeka? Kimsingi, ni kwa kumwiga Yehova. Hivyo, kabla ya kuzungumza zaidi jinsi sisi tukiwa Wakristo mmoja mmoja twaweza kuonyesha wema, acheni tuchunguze wema ambao Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, ameonyesha katika kuiandalia familia ya kibinadamu na kwa kushughulika nayo.

Wema Waonyeshwa Katika Uumbaji

6. Ni nini kilichohimiza Yehova aumbe aina nyingine za uhai zenye akili?

6 Ni nini kilichomhimiza Baba yetu wa kimbingu mwanzoni ashiriki kuuonea shangwe uhai pamoja na viumbe wenye akili walio hai? Mtume Yohana ajibu swali hilo asemapo: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Naam, upendo usio na ubinafsi ulisukuma Chanzo kikubwa cha uhai kuumba aina nyingine zenye uhai, akiwaandalia baadhi yazo makao ya kimbingu na nyingine makao ya kidunia. Bila shaka, hatujui mengi jinsi mbingu ilivyo au juu ya jinsi viumbe wa mbinguni walivyo. Wao ni roho—wasioonekana na macho ya kibinadamu—na maskani yao yamo katika milki ya kiroho. Lakini tazama maskani ya kidunia yanayokuzunguka ambayo Yehova aliwaandalia watoto wake wa kibinadamu. Na ebu fikiria ainabinadamu yenyewe. Halafu utaanza kuona kwa macho yako mwenyewe ushuhuda wenye nguvu wa wema wa Mungu.

7-9. Wema wa Mungu unaonekanaje katika njia ambayo aliiumba dunia na mwanadamu juu yayo?

7 Yehova aliwapa wazazi wetu wa kwanza uhai. Isitoshe, alifanya maisha yawezekane kuwa yenye kupendeza, kuonewa shangwe sana sana. Kwanza, aliumba maskani yao, dunia, ikiwa na mzunguko, eneo la hali-joto, na hewa zote zikiwa sawasawa kabisa. Alianzisha kawaida zinazofuatwa na maji, naitrojeni, na oksijeni zilizofanya kazi kwa ukamilifu kwa faida na burudisho la wanadamu. Alifunika uso wa dunia kana kwamba kwa zulia la maelfu ya aina za mimea, nyingine ziwe chakula cha mwanadamu na nyingine zinazopendeza jicho hasa. Aliijaza mbingu ndege wanaopendeza sana kwa rangi zao na nyimbo zao. Alijaza bahari makundi ya samaki na nchi aina nyingi za wanyama, wengine wa mwitu na wengine wawezao kufugwa. Huo ni ukarimu mwingi kama nini! Na ni ushuhuda ulioje wa wema wa Mungu wa kutoka moyoni!—Zaburi 104:24.

8 Tazama, sasa, jinsi Mungu alivyomuumba mwanadamu. Mikono, miguu ndivyo vinavyohitajiwa hasa kumwezesha adumishe usawaziko wake na kwenda huko na huko kwa urahisi. Hivyo, aweza kupata chakula na mahitaji mengineo kwa ajili yake mwenyewe, kutokana na vifaa vipatikanavyo kwa wingi sana kumzunguka duniani. Yehova aliandaa ladha hivi kwamba kula na kunywa hakukuwa vitendo vya kufanywa kwa mradi tu ili kupata nishati—kama vile inavyofanywa leo kwa kuunganisha mashine kwenye tundu la umeme. La, kula na kunywa kulibuniwa kutoe shangwe, kwa kuwa hakujazi tumbo tu bali pia kunaamsha hisia ya ladha. Yehova alimpa mwanadamu masikio pia kisha akamzingira kwa sauti nyingi ili kupendeza masikio hayo. Ni raha kama nini kusikiliza mvumo wenye kuburudisha wa kijito kinachotiririka mbio, na uvumi wa hua, au kicheko cha kitoto! Naam, kwa sababu ya wema wa Mungu, yajapokuwa mambo yote mabaya ambayo yametukia tangu uumbaji, bado ni shangwe kuwa hai.

9 Tazama pia, hisi zetu nyingine. Kuna rangi nyingi mbalimbali zenye kupendeza kama nini ili kuvutia macho yetu! Na kunaridhisha kama nini kunusa manukato mororo ya ua! Si ajabu kwamba mtunga zaburi alimwambia hivi Yehova kwa mkazo: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kuti-sha, matendo yako ni ya ajabu”!—Zaburi 139:14.

Udhambi na Kuopolewa kwa Ainabinadamu

10. Wanadamu walio wengi wameitikiaje wema wa Mungu, hata hivyo wanaendeleaje kunufaika nao?

10 Kwa kuhuzunisha, wakati ulipopita wazazi wetu wa kwanza walionyesha ukosefu wa uthamini kwa wema wote wa Mungu kuwaelekea. Walionyesha hilo walipokosa kutii amri za Yehova wakahalifu amri ile moja tu ambayo Mungu alikuwa amewapa. Matokeo yakawa, wao na wazao wao wakaja kujua huzuni, kuteseka, na kifo. (Mwanzo 2:16, 17; 3:16-19; Warumi 5:12) Katika mamileani (maelfu ya miaka) ambayo yamepita tangu kitendo hicho cha kutotii, ainabinadamu walio wengi wameonyesha ubaridi au ukosefu wa uthamini kuelekea wema wa Mungu. Lakini, ijapokuwa hivyo, watu wasio na shukrani na wasiothamini, bado hunufaika na wema wa Mungu. Kwa njia gani? Mtume Paulo aliwaelezea wenyeji wa Listra katika Esia Ndogo hivi: “[Mungu] hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.”—Matendo 14:17.

11. Ni kwa njia gani wema wa Mungu unafanya zaidi ya kuandaa maskani yenye kupendeza kwa ainabinadamu?

11 Lakini wema wa Mungu haukuishia katika kuendelea kutoa tu maandalizi yenye kupendeza ya kudumisha uhai ambayo yamejaa duniani. La, alifanya zaidi. Yehova alijionyesha mwenyewe kuwa tayari kusamehe dhambi za wazao wa Adamu na kuendelea kusitawisha mahusiano pamoja na walio waaminifu miongoni mwa ainabinadamu. Sehemu hiyo ya wema wa Mungu ilitokezwa kwa Musa wakati Yehova alipoahidi ‘kupitisha wema wake wote mbele ya [Musa].’ Kisha Musa akasikia tangazo rasmi hili: “BWANA [Yehova, NW], BWANA [Yehova, NW], Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi.”—Kutoka 33:19; 34:6, 7.

12. Ni maandalizi gani ya Sheria ya Musa yaliyoonyesha wema wa Yehova?

12 Katika siku ya Musa, Yehova alisimami-sha mfumo wa kisheria kwa ajili ya taifa jipya la Israeli ambao kwa huo watenda dhambi wasiokusudia wangeweza kupata msamaha wa dhambi wa muda tu, au wa ufananisho. Kupitia agano la Sheria ambalo Musa alipatanisha, Waisraeli walikuwa taifa la pekee la Mungu nao walifunzwa kumtolea Yehova dhabihu mbalimbali za wanyama ambazo zingefunika dhambi zao na vitendo vyao visivyo safi. Hivyo, zijapokuwa nyutu zao zisizokamilifu, Waisraeli wenye kutubu wangeweza kuendelea kumfikia Yehova kwa kukubalika na kujua kwamba ibada yao ilikuwa yenye kupendeza kwake. Mfalme Daudi, mshiriki wa taifa hilo chini ya Sheria, alionyesha kutambua kwake wema wa Mungu katika jambo hilo: “Usiyakumbuke makosa ya ujana wangu, wala maasi yangu. Unikumbuke kwa kadiri ya fadhili zako, Ee BWANA [Yehova, NW], kwa ajili ya wema wako.”—Zaburi 25:7.

13. Yehova aliandaaje njia yenye kufaa zaidi ya dhabihu za wanyama kwa ajili ya kusamehewa dhambi?

13 Wakati ulipopita wema wa Yehova ulimsukuma aandae njia ya kusamehe dhambi iliyofaa zaidi na yenye kudumu. Hiyo ilikuwa kupitia dhabihu ya Yesu, aliyekuwa mzao wa Mfalme Daudi. (Mathayo 1:6-16; Luka 3:23-31) Yesu hakutenda dhambi. Hivyo, alipokufa, uhai wake uliotolewa katika dhabihu ulikuwa na thamani kubwa sana, na Mungu alikubali dhabihu hiyo kuwa fidia ambayo ingetumiwa kuhusu wazao wote wa Adamu wenye dhambi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu; wanahesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu [kupitia achilio kwa njia ya fidia iliyolipwa na Kristo Yesu, NW] ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho kwa njia ya imani katika damu yake.—Warumi 3:23-26.

14. Ni matumaini gani ya ajabu yanayofanywa yawezekane kwa wanadamu kupitia dhabihu yenye kufidia?

14 Imani katika dhabihu ya Yesu yenye kufidia inatimiza mengi kwa ajili ya Wakristo, mengi sana kuliko yale ambayo dhabihu za wanyama chini ya agano la Sheria zilitimiza kwa ajili ya Waisraeli. Iliongoza kwenye kutangazwa rasmi kwa hesabu ndogo ya Wakristo kuwa waadilifu na kufanywa kwao kwa njia ya roho ya Mungu kuwa wana wake. Kwa njia hiyo wakawa ndugu za Yesu, wakapata tumaini la kufufuliwa wakiwa viumbe wa roho ili washiriki pamoja naye katika Ufalme wake wa kimbingu. (Luka 22:29, 30; Warumi 8:14-17) Ebu wazia kwamba Mungu angefungulia viumbe walio hai matumaini ya kimbingu kama hayo kwenye sayari hii ndogo, dunia! Kikundi kidogo chenye kuthamini tumaini hilo chabaki bado. Lakini kwa Wakristo wengine mamilioni, kuzoea imani katika fidia kwafungua njia ya kuonea shangwe kile ambacho Adamu na Hawa walipoteza—uhai wa milele kwenye dunia-paradiso yenye mfano wa bustani. Agano la Sheria pekee halikuwa limeweza kutoa matumaini ya wakati ujao wala ya kimbingu wala ya kidunia kwa wenye kuambatana nalo.

15. Ni nini kinachotiwa ndani katika habari njema?

15 Inafaa kama nini kwamba ujumbe juu ya mipango mipya ambayo Mungu alikuwa ameanzisha kupitia Yesu Kristo unaitwa “Habari Njema,” kwa kuwa unaonyesha wema wa Mungu. (2 Timotheo 1:9, 10, HNWW) Nyakati nyingine katika Biblia, habari njema huitwa “habari njema ya ufalme.” Leo habari hiyo inakazia ukweli wa kwamba Ufalme umesimamishwa chini ya utawala wa Yesu aliyefufuliwa. (Mathayo 24:14; Ufunuo 11:15; 14:6, 7) Hata hivyo, habari njema inahusisha zaidi. Kama inavyoonyeshwa na maneno ya Paulo kwa Timotheo ambayo yametoka tu kunukuliwa, inatia ndani maarifa ya kwamba Yesu alitoa dhabihu yenye kufidia kwa ajili yetu. Bila dhabihu hiyo, uhusiano wetu na Mungu, wokovu wetu wenyewe—bila kutaja Ufalme wa Yesu na makuhani na wafalme 144,000 waliotwaliwa kutoka dunia—haungewezekana. Fidia ni wonyesho wa ajabu kama nini wa wema wa Mungu!

Wema wa Mungu Leo

16, 17. Unabii wa Hosea 3:5 ulitimizwaje (a) katika 537 K.W.K.? (b) katika 1919 W.K.?

16 Alipokuwa akitazama mbele kwenye “siku za mwisho,” mtume Paulo alionya hivi: “Watu watakuwa . . . wasiopenda mema.” (2 Timotheo 3:1-3) Hata maonyesho ya wema ya kawaida, kama vile ukarimu na ujirani, hayangethaminiwa. Basi, unabii wenye kuchangamsha moyo wa Hosea 3:5 ni wenye kutia moyo kama nini: “Wana wa Israeli watarejea, na kumtafuta BWANA [Yehova, NW], Mungu wao, na Daudi, mfalme wao; nao watamwendea BWANA [Yehova, NW] na wema wake kwa kicho siku za mwisho.”

17 Unabii huo ulitimizwa kwanza katika 537 K.W.K. wakati Wayahudi waliporudi kwenda kwenye Bara Lililoahidiwa kutoka uhamishoni katika Babuloni. Katika nyakati za kisasa, ulianza utimizo wao katika mwaka 1919 wakati mabaki wa Israeli wa kiroho walipotoka nje ya tengenezo la Shetani wakaanza kutafuta Yehova na wema wake kwa juhudi. Walipata kwamba Yesu Kristo alikuwa akitawala katika mamlaka ya kimbingu tangu 1914, akiwa ndiyo yule “Daudi, mfalme wao.” Chini ya usimamizi wake wa kimbingu, walikubali kwa idili daraka la kutangaza habari njema hiyo kwa mataifa. Kwa njia hiyo wakaanza kutimiza agizo lililorekodiwa kwenye Mathayo 24:14: Habari njema ya ufalme [uliosimamishwa] itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.”

18. Ni nani wameungana na mabaki wa Israeli wa kiroho katika kutangaza rasmi habari njema?

18 Leo, “mkutano mkubwa” ambao hupokea kwa shangwe wema wa Yehova wameungana na mabaki wa wapakwa-mafuta. (Ufunuo 7:9) Sasa, zaidi ya milioni nne wanarudia kusema maneno yaliyosemwa na malaika aliyeonwa na mtume Yohana katika njozi wanapoyatangazia mataifa yote hivi: “Mcheni Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja. Msujudieni yeye aliyezifanya mbingu na nchi na bahari na chemchemi za maji.”—Ufunuo 14:7.

19. Taja ushuhuda mmoja wa wema wa Mungu ulio mkubwa zaidi?

19 Ushuhuda mmoja wa wema wa Mungu ulio mkubwa zaidi ni kwamba anaturuhusu kuwa wafanyikazi wenzake katika kazi hiyo yenye kufikia upeo mkubwa. Ni pendeleo kama nini kwetu kukabidhiwa “Habari Njema ya utukufu wa Mungu ahimidiwaye [mwenye furaha, NW]”! (1 Timotheo 1:11) Kwa kuhubiri na kufundisha kwetu wengine habari hiyo, tunaonyesha kwa kadiri ya juu sana, tunda hilo lenye umaana la roho ya Mungu, wema. Hivyo, tuna mwelekeo wa Daudi mtumishi wa Mungu wa kale, aliyesema hivi: “Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu. Wataiimba haki yako.”—Zaburi 145:7.

20. Ni habari gani zaidi kuhusu wema itakayozungumzwa katika makala inayofuata?

20 Hata hivyo, je, kushiriki katika kuhubiri habari njema ni njia pekee ya kuonyesha wema maishani mwetu? Hasha! Tunatiwa moyo kuwa “waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1, NW) Wema wa Mungu unaonyeshwa katika njia mbalimbali. Hivyo, wema wetu wapasa kuathiri sehemu nyingi za maisha zetu. Baadhi ya hizo zitazungumzwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Tunda moja moja la roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujidhibiti.

Je! Waweza Kujibu?

◻ Ni katika njia gani uumbaji unaonyesha wema wa Mungu?

◻ Yehova alifanya mipango gani ili kusamehe dhambi za wanadamu wenye kutubu?

◻ Kwa utimizo wa Hosea 3:5, ni lini mabaki wa wapakwa-mafuta walipomjia Yehova na wema wake, na hilo liliongoza kwenye nini?

◻ Ni upi ushuhuda mmoja wa wema wa Mungu ulio mkubwa zaidi leo?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Uumbaji unatoa ushuhuda wa wema mwingi wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kuruhusiwa kwetu kushirikikatika kazi ya kuhubirini uthibitisho wenye kutokezawa wema wa Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki