Kufaidika Kutokana na Yaliyompata Yona
NI NINI YALIYOMPATA YONA?
Nabii Mwisraeli Yona aagizwa na Yehova Mungu aende mji wa Ninawi akaonye wakaaji wake juu ya kuharibiwa kwao kwa sababu ya uovu wao. Badala ya kutii, Yona aelekea kwingine, apanda merikebu ya kuelekea Spania. Yehova aleta dhoruba kubwa, nao mabaharia wapiga kura za kutupa waone mwenye kusababisha dhoruba. Kura yamwangukia Yona. Akubali yu mwenye hatia na kuwaomba wamtupe kutoka merikebuni, na kuwahakikishia tufani itatulia wakifanya hivyo. Wanakubali kwa kusitasita nayo tufani yatulia kweli.
Lakini Yona hafi maji. Yehova ana kazi anayotaka aifanye na kwa hiyo amekwisha tayarisha samaki mkubwa sana, kisha ammeza. Baada ya siku tatu amtapika katika nchi kavu. Kwa mara nyingine Yona apokea agizo la kuonya Waninawi. Wakati huu atii, aenda Ninawi na kuonya wakaaji wake kwamba baada ya siku 40 wataharibiwa kwa sababu ya uovu wao. Lakini, maajabu hayo! wote watubu tangu wakuu mpaka wadogo! Kwa hiyo Mungu abadili nia yake. Yona akasirika sana na kutoka mjini na kuanza kununa na kungojea. Ajuapo kwamba Mungu kweli amebadili nia yake, audhika naye Yehova amkemea.
NI HABARI YA KWELI?
Tunapofikiria ubora wa yaliyompata Yona kwetu, kwanza tunakabiliwa na ulizo hili: Je! kweli Yona aliishi na kupatwa na mambo yanayotajwa katika kitabu cha Biblia chenye jina lake? Ikiwa sivyo, ujumbe wa kitabu cha Yona ungekuwa hauna maana sana kwetu.
Wanafunzi wengi wa kisasa wa kidini wanatia shaka kama kweli Yona alipatwa na mambo hayo. Hivyo mwanadini mmoja Mprotestanti auliza hivi: “Mambo hayo hutokea katika ulimwengu kama wetu?” Nacho kikundi cha wanafunzi wa Kikatoliki chasema kwamba kitabu cha Yona ni “tukio la kusisimua na la kuchekesha” linalohusu “mfululizo wa kufanyiana mzaha kati ya Mungu na nabii wake” na kwamba kitabu hicho “kimekusudiwa kuchekesha” na kufundisha pia. Maoni mawili hayo yatosha, nayo ni mfano tu wa mengine mengi.
Lakini kuwa na maoni ya kwamba kitabu cha Yona si cha kweli kwa sababu mambo hayo hayatukii siku zetu hakupatani na mambo ya hakika wala na sehemu nyinginezo za Biblia. Biblia yaanza kwa kusimulia juu ya uumbaji. Je! leo twauona uumbaji ukiendelea? Biblia yaeleza pia juu ya miujiza, kutoka Mwanzo mpaka Ufunuo. Kwa sababu hatuioni miujiza hiyo leo yamaanisha kwamba haikutukia wakati wo wote? Vitabu vya Biblia viliandikwa kwa uongozi wa Mungu, lakini je! siku zetu tunaona uongozi huo wa Mungu ukifanya kazi? Kwa hakika, ni juu ya Yehova Mungu kuchagua wakati na njia ya kutumia uwezo wake wa kimungu.
Kwa habari ya sababu za kufikiria kitabu cha Yona kuwa cha kweli, angalia yafuatayo: Kitabu cha Yona chaanza kulingana na mtindo ule ule wa vitabu vitano vile vya manabii “wadogo”: “Neno la [Yehova] lilimjia Yona.” (Yona 1:1) Wanafunzi wa kale Waebrania walikikubali kitabu cha Yona kuwa cha kweli. Wasingaliweza kufanya hivyo kwa sababu ya matukio mengi yacho ya ajabu kama wasingalikuwa wanasadiki ni cha kweli. Unyofu na uwazi wa kitabu hicho unakihakikisha kuwa cha kweli. Yona hakuficha udhaifu wake kabla wala baada ya kuwahubiri Waninawi. Inastahili kuangaliwa pia kwamba wakati wa utawala wa Yeroboamu wa Pili (karne ya 9 K.W.K.) Yona, mwana wa Amitai, alitoa unabii uliotimizwa. (2 Fal. 14:23-25) Katika Maandiko ya Kiebrania majina ya Yona na baba yake yanaonekana hapo tu na katika Yona 1:1, Kwa hiyo, inaonekana kwamba Yona anayetajwa katika Yona 1:1 ndiye yule yule anayetajwa katika 2 Wafalme 14:25, na hiyo inaongeza uhakika wa kwamba aliishi.
Uhakika ulio wa maana zaidi ni kwamba Yesu Kristo alitaja habari ya Yona naye akaifungamanisha mara nyingi na matukio ambayo ukweli wayo si wa kutiliwa mashaka. Hivyo wakati mmoja alisema hivi: “Kwani kama vile Yona alivyokuwa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi, hivyo ndivyo Mwana wa Adamu atakavyokuwa siku tatu mchana na usiku katika moyo wa nchi.” (Mt. 12:39, 40) Asingetoa hoja au ulinganifu huo kama Yona hakuishi, au kama hakukaa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi!
Tena, Yesu Kristo alisema kwamba watu wa Ninawi wangesimama na kuwahukumu Wayahudi wa siku zake kwa sababu Waninawi walimsikiliza Yona wakatubu ijapokuwa sasa Wayahudi walikuwa na nabii mkubwa zaidi katikati yao na hali hawakuwa wakimsikiliza. (Mt. 12:41) Mwendo wa Wayahudi wa siku za Yesu ungewezaje kulinganishwa kwa njia isiyofaa na ule wa watu ambao hawakuishi wakati wo wote? Hiyo haiji. Lakini si hayo tu! Katika habari iyo hiyo Yesu aliwalaumu Wayahudi wa siku zake kwa kutomsikiliza ijapokuwa malkia wa Sheba alisafiri mwendo mkubwa akamsikilize Mfalme Sulemani, ambaye hakuwa mkubwa kama Yesu. Hakuna shaka kwamba Yesu, mtu mwenye hekima na maarifa zaidi ya wote waliopata kuishi, aliyaona maandishi ya kitabu cha Yona kuwa ya kweli kama maandishi yaliyomhusu Mfalme Sulemani na malkia wa Sheba. Maandishi hayo yanasimulia juu ya watu walioishi kweli na matukio yaliyotukia kweli.—Mt. 12:42.
TABIA NA SIFA ZA YONA
Yona alikuwa mtu wa aina gani? Inaelekea sana alikuwa mwoga na asiyeamini angeweza kufanya jambo kwa uhakika. Wengine wamemwita mwenye haya. Inaelekea kuwa hivyo, kwa maana alikimbia “apate kujiepusha na uso wa [Yehova],” badala ya kutimiza agizo lake. Lakini acheni kwanza tuangalie vile agizo lake kutoka kwa Yehova lilivyokuwa. Yeye aliamriwa kwenda Ninawi. Huo ulikuwa umbali gani? Ilikuwa zaidi ya maili 600 (au kilomita 960). Kwa kuwa siku hizo hakukuwa na njia za moja kwa moja kutoka Israeli mpaka Ashuru, pengine alipaswa kusafiri karibu maili 700 au 800 hivi (kati ya kilomita 1120 na 1280). Kwa njia gani? Kwa miguu! Kwa kusafiri karibu maili 25 (kilomita 40) kwa siku, huenda ikawa ilimchukua mwezi mmoja kufika Ninawi. Ninawi ulikuwa mji wa aina gani? Ulikuwa ndio mji mkuu wa milki ya ulimwengu ya Ashuru, nao ulijawa na wapagani 120,000 wenye sifa ya kuwa waovu. Haishangazi kwamba wazo la kwenda huko kuuhubiri ujumbe wa Yehova wenye onyo lilionekana kuwa agizo kubwa mno!
Njia ya Yona ya kutenda wakati Yehova Mungu alipobadili nia kwa sababu Waninawi walitubu inaelekea kuleta maoni mabaya juu ya Yona. Lakini kweli alikuwa mbaya hivyo, akijifikiria mwenyewe tu? Sivyo. Inaelekea Yona alikuwa mwaminifu kabisa, tena kabisa. Katika masimulizi yake aliyoyaandika yeye mwenyewe, anaeleza udhaifu na makosa yake bila kuficha. Isitoshe, yeye alikuwa shahidi mwaminifu pia kwa Yehova Mungu, kwa maana mabaharia wasioamini walipomwuliza yeye alikuwa nani, kwa ujasiri alijibu: “Mimi ni Mwebrania; nami namcha [Yehova], Mungu wa mbingu, aliyeziumba bahari na nchi kavu.” Ilihitaji ushujaa kusema hivyo wakati wa jaribu, na pia kuwaambia waziwazi kwamba alikuwa akikimbia agizo alilopewa na Yehova.—Yona 1:9.
Isitoshe, wakati kura ilipomwangukia, aliiona kama imetoka kwa Yehova, kwa maana kwa wazi alifahamu vile Neno la Mungu linavyosema juu ya kura. (Mit. 16:33; 18:18) Kwa hiyo, kwa kutotaka kuona mabaharia waaminifu hao wakivunjikiwa na merikebu yao kwa sababu yake, Yona akawaambia: “Nikamateni, mnitupe baharini; basi bahari itawatulilia; kwa maana najua ya kuwa ni kwa ajili yangu tufani hii imewapata.” (Yona 1:12) Kama angalikuwa mwenye kufikiria faida yake tu bila shaka angalinyamaza, akitumaini kwamba kwa njia fulani yeye na wale wengine waliokuwa katika merikebu wangefaulu kushindana na tufani hiyo. Kwa ufupi, na iangaliwe kwamba kutoa kwake ushuhuda juu ya Mungu wa kweli Yehova kulizaa matunda, maana baada ya tufani kutulia mabaharia walimtolea Yehova dhabihu na kumwekea nadhiri.
Tunayo pia sababu ya kuamini kwamba Yona alikuwa mpole na mwenye kufundishika. Wapole wana hali ya kutokasirika upesi nao wana nia ya kufundishwa, kama tusomavyo: “Wenye upole [Yehova] atawafundisha njia yake.” (Zab. 25:9) Yona hakuona uchungu bali alitubu. Alionyesha angeweza kukubali adhabu kali hiyo aliyopewa na Mungu. Hii ni wazi kutokana na sala aliyotoa alipokuwa tumboni mwa nyangumi yule, ambayo inaonyesha Yona alifahamu sana kitabu cha Zaburi. Kwa ufupi alisali hivi: “[Nafsi] yangu ilipozimia ndani yangu, nalimkumbuka [Yehova]; maombi yangu yakakuwasilia, katika hekalu lako takatifu. . . . Lakini mimi nitakutolea sadaka kwa sauti ya shukrani; nitaziondoa nadhiri zangu. Wokovu hutoka kwa [Yehova].”—Yona 2:7, 9; Zab. 50:14; 3:8.
KUJIFUNZA KUTOKANA NA YALIYOMPATA YONA
Tunaweza kujifunza nini kutokana na yaliyompata Yona? Mengi sana! Maandishi yake yanatukuza uwezo wa Yehova wa kuogofya, kwa mfano yakionyesha vile anavyoweza kutokeza dhoruba kubwa itimize kusudi lake kisha kuituliza kulingana na mapenzi yake. Yanatukuza pia kupendezwa kwa Yehova na mji wenye kujawa na wapagani na rehema kuu anayoweza kuchagua kuonyesha watu kama hao. Twaona pia vile Yehova alivyomstahimili nabii Wake Yona, akamfundisha masomo yenye kuhitajiwa sana.—Ayubu 37:23; Matendo 10:34, 35; Kut. 34:6, 7; Rum. 2:4.
Twajifunza kutokana na yaliyompata Yona kwamba ni mwendo wa hekima kutii amri za Yehova. Pia, tunasaidiwa kufahamu zaidi kwamba ni mapenzi ya Yehova kwetu kuonyesha wengine rehema. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwafahamisha kusudi la Yehova juu ya dunia na mwanadamu, tukiwa na matumaini kwamba wengine wataitikia kama vile Waninawi wa kale walivyoitikia mahubiri ya Yona. Na nyakati nyingine vipingamizi visivyoshindika vikielekea kutuzuia, imetupasa tuonyeshe imani kama aliyoonyesha Yona katika tumbo la nyangumi, kwamba kwa msaada wa Yehova tunaweza kuvishinda na kuendelea mbele tukatimize agizo letu.—Yak. 3:17; Mt. 5:7; Luka 6:35, 36; 17:5, 6.
Tunaweza pia kujifunza kutokana na mwendo wa Yona juu ya vile inavyotupasa kutenda na vile isivyotupasa kutenda. Kwanza, haitupasi kuepa mgawo au pendeleo gumu la utumishi tukipewa. Kama Yona, huenda baadaye tukaona kwamba si gumu mno kutoweza kutimizwa. Wengine wamedhani kwamba Yona aliamua kwenda Tarshishi kwa shughuli ya kibiashara. Kwa hiyo twaweza kujiuliza hivi, Je! nyakati nyingine sisi hufuatia mapendezi yanayohusu kazi ya kimwili hali tungeweza kuwa tukifanya ‘kazi nyingi ya Bwana’? Pia, je! sisi hubagua aina ya watu tutakaohubiri au eneo tutakalohubiri, kama inavyoelekea Yona alifanya? Kama Yehova angalimwamuru Yona ahubiri ujumbe wenye onyo kwa wakaaji wa mmojawapo wa miji ya Yuda, bila shaka asingalikataa. Halafu tena, je! sisi tu kama Yona, tukikosa kufanya yanayotupasa kuwa tukifanya kwa sababu ya kuogopa mwanadamu?—Ebr. 12:25; Yak. 4:13-15; 1 Kor. 15:58; Zab. 118:6.
Na tusisahau kwamba Yona alikuwa na sifa fulani za kupendeza zinazotupasa tuziige. Je! sisi tu wenye kusema mambo wazi, tu waaminifu katika maisha zetu za kila siku kama Yona, kwa habari ya aliyosema na mabaharia na pia kuandika kwake yote yaliyotukia? Je! sikuzote sisi huwa tayari kujitambulisha kuwa mashahidi wa Yehova, kama Yona? Je! tu wenye nia ya kutanguliza hali ya wengine mbele ya yetu wenyewe kama Yona wakati alipochukua hatua ya kuokoa mabaharia kwa kuwaomba wamtupe kutoka merikebuni, huku Yona akiona hiyo ingemletea kifo cha ghafula katika kilindi cha maji?—Zab. 11:7; 1 Pet. 3:15; Flp. 2:3, 4.
Kwa kweli, yaliyompata Yona yana masomo mengi kwetu, nasi twaweza kufaidika kutokana nayo. Hapo twajifunza tunayopaswa na tusiyopaswa kufanya. Tunajifunza kuziiga sifa njema alizoonyesha Yona, na kuepuka makosa. Tunatiwa moyo tuziige sifa za kupendeza za Yehova Mungu, hasa rehema yake, ustahimilivu wake na upendo wake. Hadithi ya Yona yenye kuvutia sana inatutia nguvu sana kwa maana kwa kweli mambo hayo yalimpata Yona!—Rum. 15:4.