Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 2/1 kur. 51-55
  • “Endeleeni Kufanya Hivi Kwa Kunikumbuka Mimi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Endeleeni Kufanya Hivi Kwa Kunikumbuka Mimi”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Fanyeni Hivi kwa Kunikumbuka Mimi’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • “Kondoo Wengine” na Chakula cha Jioni cha Bwana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kwa Nini Tunaadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanaadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana kwa Njia Tofauti na Dini Nyingine?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 2/1 kur. 51-55

“Endeleeni Kufanya Hivi Kwa Kunikumbuka Mimi”

MARA moja kwa mwaka katika tarehe ya Biblia ya Nisani 14, usiku wa Kupitwa, watu wa Yehova walio wakf wanakusanyika pamoja katika sehemu zote za dunia kupatana na amri ya Yesu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19, NW; Kut. 12:2-6) Inafaa Chakula cha Bwana cha Jioni kiadhimishwe usiku huo wa kweli wa Kupitwa (au Passover, Kiingereza), kila mwaka baada ya machweo ya jua, katika mtaa wa mtu.

Ni nani wanaokaribishwa wahudhurie? Bila shaka yale mabaki machache ya waliotiwa mafuta kwa roho ya Yehova watahudhuria, lakini pia wote wale wa “mkutano mkubwa” unaoongezeka, wenye matumaini ya kidunia, wanakaribishwa kwa uchangamfu wawepo, na vilevile wote wanaopata kufahamu mipango ya Yehova. (Ufu. 12:17; 7:4, 9) Je! huu ni wakati wa desturi za kidini au mafumbo ya kiroho? Hata kidogo. Bali, wakati huu wa kila mwaka, unaohusu mifano ya mkate na divai, unakumbusha wahudhuriaji mambo ambayo Yesu Kristo aliwafanyia miaka mia kumi na tisa iliyopita na kuwakumbusha hayo yote yana maana gani kwao leo na kwa wakati ujao usio na kikomo.​—1 Kor. 11:23-26.

Tarehe hii ya maana inaamuliwaje? Katika karne ya kwanza Yesu na Wakristo wa kwanza walikubali uamuzi wa tarehe ya Nisani 14 (ambayo ilianza wakati wa machweo ya jua) kama ilivyowekwa na makuhani wa Kiyahudi hekaluni katika Yerusalemu. Inastahili kuangaliwa kwamba Yesu aliadhimisha chakula cha Kupitwa Nisani 14, kama ilivyoamriwa katika torati ya Musa. (Kut. 12:6-8; Law. 23:5; Mt. 26:18-20) Yeye hakula chakula cha Kupitwa Nisani 15, kama wafanyavyo Wayahudi wengi leo. Baada ya hekalu kuharibiwa mwaka wa 70 W.K., iliwapasa Wakristo kujiamulia tarehe ya Kupitwa ya Nisani 14 ingekuwa lini.

Wakati Mfalme wa Kirumi Konstantino alipofanya Ukristo wa uasi wa imani uwe ndiyo dini ya serikali (325 W.K.), Baraza ya Nikaea iliamuru mwadhimisho wa Pasaka ufanywe sikuzote Jumapili inayofuata mara baada ya mwezi mpevu (mzima) unaotokea siku ambayo kwa kawaida ni Machi 21 wakati wa masika, wakati ambapo mchana na usiku zina urefu ule ule mmoja. [Kiingereza ni spring (vernal) equinox]. Siku ya kumi na nne tangu mwezi mpya ulipoonekana, ambayo waliichukua kama siku ya mwezi mpevu, ilipofika Jumapili, mwadhimisho wa Pasaka uliahirishwa mpaka Jumapili iliyofuata. Kusudi lake lilikuwa kuepuka kuadhimisha wakati ule ule pamoja na Wayahudi na Wakristo wachache walioitwa Wakuarto-desima, ambao bado waliadhimisha siku ya kumi na nne ya Nisani. Kwa njia hiyo Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) imefanya “Alhamisi kuu” yao Alhamisi sikuzote ili kuadhimisha Kijio cha Mwisho cha Yesu, na “Ijumaa kuu” yao Ijumaa sikuzote kuadhimisha kifo chake.

Hasa kufikia mwaka wa 1880 waabudu wa Yehova waliotiwa mafuta walikuwa wamejitenga na mazoea ya Jumuiya ya Wakristo ya kuadhimisha Chakula cha Bwana cha Jioni mara nyingi kwa mwaka nao wakakiadhimisha Nisani 14 tu baada ya machweo ya jua. Tangu wakati huo na kufika karibu mwaka wa 1919 Wakristo waliotiwa mafuta walikubali tarehe za kuamulia Nisani 14 zilizowekwa na kalenda ya Kiyahudi. Walitambua kwamba kalenda ya Kiyahudi ilipanga “Kupitwa” (“Passover”) iwe Nisani 15, baada ya machweo ya jua. Hata hivyo, Wakristo hao waliotiwa mafuta walipanga kuadhimisha Chakula cha Bwana cha Jioni usiku wa Nisani 14, kama Yesu alivyofanya. Ingawa hivyo Wakristo hao walitumia kalenda ya Kiyahudi kukubali uamuzi wa mwezi wa Nisani kwa kila mwaka.

Kalenda ya kisasa ya Kiyahudi inaamua mwanzo wa mwezi wao wa Nisani kulingana na uchunguzi wa kisayansi wa mwezi mpya. Walakini, kwa kawaida robo ya kwanza ya mwezi mpya inaonekana Yerusalemu saa kumi na nane au zaidi baadaye. Katika nyakati za karibuni, kila mwaka baraza inayoongoza ya mashahidi wa Yehova imeamua mwezi mpya halisi unaoonekana Yerusalemu, na hivyo ndivyo tarehe ya kwanza ya Nisani ilivyoamuliwa katika nyakati za Biblia. Kwa sababu hiyo mara nyingi kumekuwa na tofauti ya siku moja au mbili kati ya tarehe ya Ukumbusho ya mashahidi wa Yehova na Nisani 14 inayofuatwa na kalenda ya kisasa ya Kiyahudi.a

Kulingana na njia yetu ya kisasa ya kuhesabu, tarehe ya Ukumbusho inapangwa kulingana na mwezi mpevu ulio karibu zaidi baada ya masika yenye urefu ule ule wa mchana na usiku. Kwa mfano, mwaka wa 1975 tarehe ya Ukumbusho ilikuwa Alhamisi, Machi 27, baada ya machweo ya jua, nayo iliheshabiwa siku kumi na nne tangu mwezi mpya ulipoonekana Yerusalemu (karibu zaidi na masika hayo yenye mchana na usiku wenye kulingana urefu). Kwa kufaa, kulikuwako pia mwezi mpevu Alhamisi, Machi 27, 1975. Tarehe ya Ukumbusho mwaka wa 1976, iliyohesabiwa kulingana na njia yetu ya sasa, ni Jumatano, Aprili 14, baada ya machweo ya jua. Mwezi mpevu pia unatokea tarehe ii hii. Kwa hiyo wakati ujao ikitokea watu wo wote wa Yehova wasiweze kupashana habari na baraza inayoongoza, wanaweza kuamua tarehe ya Ukumbusho kwa usahihi kutokana na kalenda za mahali pao zenye kuonyesha mwezi mpevu wa kwanza baada ya masika yenye urefu ule ule wa mchana na usiku. Kwa hiyo mwadhimisho ungefanyika baada ya machweo ya jua ya siku ambayo mwezi mpevu unatokea.b

Kufanywe nini kukiwa na tukio lisilotazamiwa usiku wa Chakula cha Bwana cha Jioni? Namna gani kukiwa na dhoruba kali au kitu kingine kikubwa kufanya isiwezekane kundi la mahali likutane wote wakiwa pamoja katika wakati uliowekwa? Ikiwa hivyo, inaweza kufaa akina ndugu wakutane vikundi vikundi vya ujirani au katika vikundi vya jamaa, ikiwa lazima. Kwa njia hiyo wanakusanyika pamoja wakumbushwe maana ya mifano ya Ukumbusho ya mkate na divai. Nyakati za matukio hayo yasiyotazamiwa, mmoja wa ndugu walio wakf (au dada aliye wakf, ikiwa hakuna ndugu) angeweza kuzungumza masimulizi ya Biblia katika Mathayo 26:17-30; Luka 22:7-23, 28-30; na 1 Wakorintho 11:20-31 kwa ufupi. Ikiwa lazima kundi likutane vikundi vikundi, hesabu ya jumla ya waliohudhuria katika vikundi hivyo ingeweza kutumwa kama ripoti ya hudhurio la kundi lote.

Kwa habari ya mifano (mkate na divai), bila shaka jitihada nyingi zifanywe kuhakikisha kwamba wale walio wa mabaki yaliyotiwa mafuta wamepewa mkate na divai, hata ikiwa mmoja ni mgonjwa sana nyumbani au hospitalini. Ikiwa tu kuna ugumu wa pekee sana hata mmoja wa mabaki yaliyotiwa mafuta asiweze kula mifano Nisani 14, ndipo anapoweza kuadhimisha Ukumbusho siku ya kumi na nne ya mwezi mfupi unaofuata (siku ya mwezi mpevu unaofuata), kupatana na kanuni inayopatikana katika Hesabu 9:10, 11, na 2 Mambo ya Nyakati 30:1-3, 15, inayohusu maadhimisho ya Kupitwa. Mwadhimisho huo uliochelewa uripotiwe mara baada ya kuadhimishwa.

Namna gani ikiwa zaidi ya kundi moja watatumia Jumba la Ufalme lile lile? Ingefaa kupanga vipindi vyenyewe kwa kufikiriana kwa kulipa kundi moja wakati wa kutosha kutoka jumbani na lile jingine wakati wa kutosha kuanza kipindi chao. Kwa kusudi hili, nyakati nyingine majumba ya ziada yamekodiwa kwa mwadhimisho wa Ukumbusho. Mambo yakiwa hivyo, huenda makundi kadha yakaona inafaa kujiunga pamoja wawe na mkutano mmoja. Ndipo ripoti ya jumla ingeweza kutumwa, ikitaja majina ya makundi yenye kuhusika.

Utaratibu wa matukio ulikuwaje siku za Yesu? Katika mwadhimisho wa kwanza wa Chakula cha Bwana cha Jioni, Mathayo mwenyewe alikuwako. Anaeleza hasa utaratibu wa mambo yaliyotokea. Yesu na wanafunzi wake kumi na wawili waliadhimisha chakula cha Kupitwa kwa kutumia mwana-kondoo wa kuokwa na mkate usiotiwa chachu, kukumbusha wenye kula yaliyotukia Waisraeli walipokombolewa Misri mwaka wa 1513 K.W.K. Hakukuwa na mafumbo yo yote ya kiroho juu ya matumizi ya mwana-kondoo huyo wa kuokwa na mkate usiotiwa chachu wa kukumbushia Waisraeli mambo hayo. (Mt. 26:17-19; Zab. 119:2, 14) Baada ya chakula cha Kupitwa, Yesu alimfunua msaliti wake, Yuda, halafu huyo akafukuzwa. (Mt. 26:20-25; Yohana 13:29, 30) Sasa Yesu alibaki na mitume kumi na mmoja waaminifu ambao alianzisha nao chakula kipya cha jioni kilichohusu kula mkate usiotiwa chachu na kunywa kikombe cha divai nyekundu kabisa. Nyakati zote hizo Yesu alitoa sala ya shukrani, kwanza kwa ajili ya mkate kisha kwa ajili ya divai. (1 Kor. 11:24, 25) Baada ya Yesu kutoa maelezo marefu na sala, walimaliza kwa kuimba sifa, kisha wakaondoka kwenda uliko Mlima wa Mizeituni. Basi, hiyo inaonyesha utaratibu wa kawaida unaopaswa kufuatwa hata leo yetu.​—Mt. 26:26-30; Yohana 13:31–18:1.

Mifano ya mkate na divai inatukumbusha nini? Mkate usiotiwa chachu unatukumbusha juu ya mwili wa Yesu wa nyama, namna “aliteswa katika mwili” (1 Pet. 4:1); namna alivyotoa mwili wake wa nyama “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu” (Yohana 6:51); namna alivyo “Mwana-Kondoo aliyechinjwa” (Ufu. 5:12); na namna agano la Torati lilivyoondolewa ‘kwa kuligongomea kwenye mti wa mateso.’ (Kol. 2:14) Mfano wa divai nyekundu unatukumbusha namna Yesu amekuwa Mkombozi wetu kwa sababu tumekombolewa na “damu ya thamani” ya Yesu (1 Pet. 1:19); na namna damu yake yenye uhai ilivyotumiwa kuhalalisha agano jipya ambamo warithi wenzake wanaingizwa (1 Kor. 11:25). Ingawa wale wa “mkutano mkubwa” hawali mifano, wanakumbushwa faida za hatua ya Yesu na za agano jipya ambalo kupitia kwalo wanapata faida nyingi. (Ufu. 7:9, 10, 14) Kweli, Yehova amepanga tukombolewe kupitia kwa uwezo wa dhabihu ya Kristo yenye kulipia dhambi, si kufaidi watiwa mafuta tu bali pia na wale wote watakaopata uzima wa milele hapa duniani.​—Law. 16:11; 1 Yohana 2:2.

Mkutano unaongozwaje? Katika kusanyiko la Ukumbusho ndugu anayetumikia kama mwenyekiti anakaribisha kwa ufupi na kufungua mkutano kwa wimbo na sala. Hii inafuatwa na hotuba ya Ukumbusho, inayotolewa na msemaji mwenye uwezo (mmoja wa watiwa mafuta akipatikana) aliyechaguliwa na waangalizi waliowekwa. Isingefaa ndugu kadha wazungumze juu ya sehemu sehemu za hotuba ya Ukumbusho kama inavyofanywa katika hotuba moja yenye wasemaji wengi. Inapendekezwa msemaji atoe sala mbili fupi juu ya mifano. (Mt. 26:26, 27) Baada ya mifano kupitishwa kwa wasikilizaji na baada ya maelezo ya ziada ya msemaji, maelezo ya mwisho yanaweza kutolewa na mwangalizi-msimamizi isipokuwa kama yeye ndiye anayeongoza kipindi cha Ukumbusho. Mkutano utakwisha na wimbo wa mwisho na sala.

Ni wale walio mabaki yaliyotiwa mafuta peke yao wanaokula mifano inayopitishwa hapa na pale kwa wasikilizaji. Baada ya sala fupi, mkate unapitishwa kwanza. Kisha, baada ya sala nyingine, divai inapitishwa. Mkate na divai hazipitishwi pamoja. Wale wanaokula na kunywa ‘inavyostahili’ wamepaswa wale na kunywa mifano yote miwili.​—1 Kor. 11:27, 28.

Biblia inasema kwamba Yesu aliumega mkate, kwa wazi aupitishe kwa mitume waliokuwa pande zote mbili za meza. (Mt. 26:26) Hilo si jambo la lazima katika hali yetu leo, kwa maana Yesu hakuwa akiweka utaratibu wa desturi ya kidini. Hivyo hakuna maana ya mfano katika umegaji wa mkate usiotiwa chachu. Kumbuka kwamba hakuna mfupa wa mwili wa Yesu usio na dhambi uliovunjwa alipokufa. (Kut. 12:46; Zab. 34:20; Yohana 19:33, 36) Hesabu ya vikombe na hesabu ya sahani zinazotumiwa inategemea hesabu ya watu wa kupitisha wanaotakiwa. Sehemu ya mkate usiotiwa chachu inaweza kuwekwa juu ya kila sahani inayotumiwa nayo divai inaweza kumiminwa katika vikombe kabla ya mkutano kuanza.

Ni mkate na divai ya aina gani itakayotumiwa? Kwa kuwa Yesu alichukua mkate usiotiwa chachu uliotumiwa kwa kawaida kwa Kupitwa, sisi leo tunatumia mkate usiotiwa chachu. Mikate mingine ya Kiyahudi isiyotiwa chachu inayoitwa “matzos” inatengenezwa na unga wa ngano na maji tu, nayo inaweza kutumiwa na Wakristo katika mwadhimisho wa Ukumbusho. Lakini tusingetumia “matzos” inayotengenezwa kwa kuongeza vikolezo, kama vile chumvi, sukari, vimea vya kuchachisha, mayai, vitunguu, na kadhalika.

Huenda Mashahidi wengine wakapendelea kutengeneza mkate mdogo usiotiwa chachu kwa unga (wa ngano, mchele au nafaka nyingine) na maji. Hiyo inaweza kufanywa ifuatavyo: Changanya kikombe kimoja na nusu cha unga na kikombe kimoja cha maji, uukande unga uwe na unyevunyevu (umajimaji mdogo). Katika mahali tambarare (au juu ya mbao ya kutandazia chapati), palipo na unga-unga wa kutosha, utandaze ule unga uliokanda uwe mwembamba iwezekanavyo. Uweke juu ya kikaangio chenye moto mwingi, uchome-chome matundu matundu katika mkando huo, na kuufanya mkate uliotandazika. Uwe mkavu na unaoweza kuvunjika kwa vyepesi.

Divai ya kutumiwa kwa Ukumbusho iwe divai nyekundu kabisa kama iliyotumiwa na Wayahudi katika maadhimisho ya Kupitwa. Tunaona kwamba katika Mathayo 26:29 Yesu anataja “uzao wa mzabibu,” na wakati huo wa mwaka ungeweza kuwa ni divai iliyotiwa chachu peke yake. Divai ya mizabibu isiyochanganywa na kitu kingine ndiyo inayofaa tu kuwa ukumbusho wa damu ya Yesu iliyomwagika. Damu ya Kristo ilitosha bila kuongezwa vitu vingine, kwa hiyo divai inayotumiwa isitiwe vitu vitamu-vitamu au vinginevyo, bali iwe divai nyekundu. Kukiwa na ugumu wa kupata mifano (mkate na divai), basi mipango ingeweza kufanywa mapema kutosha kuweza kuipata. Kwa kuwa mifano yenyewe si mitakatifu, baada ya mwadhimisho na kufungwa kwa mkutano, mkate na divai inaweza kupelekwa nyumbani na kuchukuliwa kama vitu vya kawaida, vya kutumiwa wakati mwingine kama vitu vya kawaida.​—1 Sam. 21:4.

Ni nani wanaopaswa kula mifano? Ni wale wa “kundi dogo” peke yao wanaoingizwa katika agano jipya na kwa hiyo ndio wanaotakiwa kula mifano. (Luka 12:32) Mitume kumi na mmoja waaminifu, wakiwa kikundi cha waliotazamiwa kutiwa mafuta, ndio waliokuwa kiini cha wale ambao baadaye wangeingizwa katika agano jipya siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. (Luka 22:20) Kwa kuwa “mkutano mkubwa” si ‘viumbe vipya’ walio katika agano jipya, wao hawali mkate wala kunywa divai wakati huo wa kila mwaka.​—2 Kor. 5:17.

Kila mmoja wa watiwa mafuta anayehudhuria Ukumbusho anajichunguza mapema aone kama anastahili kula na kama kweli anao ushuhuda wa roho. (Rum. 8:16, 24; 1 Kor. 11:27-29) Mara kwa mara wako wengine waliokuwa wakila na kunywa zamani ambao wamepata kujua kwamba uhusiano wao na Mungu si ule wa mwana aliyetiwa mafuta. Imewapasa kwa kufaa waache kula na kunywa, lakini hiyo isingeonyesha kwamba wamekuwa wasioaminika. Ni kwamba tu uhusiano wao na Yehova umeonyeshwa wazi kuwa wenye tumaini la kidunia.

Wale wanaohesabiwa kuwa wenye kula na kunywa ni wale wanaojulikana kuwa watumishi waaminifu waliobatizwa, wa Mungu. Hatukaribishi watu waliotengwa na ushirika wahudhurie. Lakini mtu wa namna hiyo akiwapo, hakuna sababu ya kuhangaika ikiwa ameketi katika mstari mmoja na wengine wala hakuna sababu ya kuhangaika akila na kunywa mifano. Mtu wa namna hiyo hahesabiwi kuwa amekula, hata iweje.

Sikuzote inafurahisha kuona wapya wengi sana wakihudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho. Baada ya programu, kunakuwa na furaha ya kushirikiana na wapya na sisi kwa sisi. Ushirika huo wenye furaha unajenga na kutia kila mtu moyo kweli kweli. Programu ya jioni sikuzote inatoa chakula kingi cha kufikiriwa kwa kumshukuru sana Yehova, ikitukumbusha yote ambayo Yeye amefanya kupitia kwa Mkombozi wetu, Yesu Kristo Bwana wetu, kwa sababu ya kutupenda. (Mt. 20:28; 1 Pet. 3:15) Baada ya kufika nyumbani programu ikiwa imekwisha, jamaa ya mashahidi wa Yehova inaweza kutumia wakati ikizungumza maana ya wakati huo. Hiyo inasaidia kuunganisha jamaa zaidi na kuwatajirisha kiroho.

Wazee wanafanya mipango ya uangalifu kuona kwamba mwadhimisho wa Chakula cha Bwana cha Jioni wa kundi la kwao unafaa. Usiku huu mmoja, mioyo na akili za watu wa Yehova walio wakf, watiwa mafuta na wale wa “mkutano mkubwa,” zinamsifu Mungu wetu Mwenye Enzi Kuu, Yehova, wote wakiwa wamekusanyika kwa umoja. Wanamshukuru Yesu Kristo tena Mkombozi wetu ambaye alionyesha anatupenda sana kwa kutoa uhai wake wa kibinadamu tupate kuponywa. Kila mwaka mabaki yaliyotiwa mafuta na “mkutano mkubwa” wanapendezwa kumkumbuka yeye kama mshindi wa Kimasihi wa ulimwengu.​—Yohana 16:33.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa sababu izo hizo, mara kwa mara Wayahudi wa kisasa wanaona ni lazima waongeze mwezi wao wa kumi na tatu wa mwaka katika wakati ulio tofauti na ule ambao mashahidi wa Yehova wanaongeza. Basi, nyakati hizo tarehe yao ya Kupitwa inakuwa mwezi mmoja baada ya tarehe ya Ukumbusho ya mashahidi wa Yehova.

b Tarehe za Kupitwa na Ukumbusho kwa kawaida zinatokea kulingana na utaratibu wa baada ya kila miaka kumi na tisa. Kwa maelezo zaidi tazama Aid to Bible Understanding, ukurasa 1677, chini ya kichwa kidogo “The Metonic Cycle.” Tazama pia kurasa 1076-11»» upate habari za Chakula cha Bwana cha Jioni.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki