“Mungu Hana Upendeleo”
“(YEHOVA), Mungu wenu, yeye ndiye Mungu wa miungu, na Bwana na mabwana, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, asiyependelea nyuso za watu.” (Kum. 10:17) Maneno hayo yenye kutufariji, yaliyosemwa na nabii Musa, yamehakikishwa kuwa ya kweli mara nyingi na maandishi yanayoonyesha jinsi Mungu ameshughulika na wanadamu.
Watu wengi wamepata nafasi ya kuwa watumishi wanaokubaliwa na Mungu, kwa sababu yeye hana upendeleo. Mungu “hutaka watu wote ukombozi kwa ajili ya wote.” (1 Tim. 2:4-6) Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.” (1 Tim. 2:4-6) Kwa kuwa wanadamu wote wamekuwa mali ya Mungu na Kristo kupitia kwa dhabihu ya ukombozi, hakuna mtu anayenyimwa nafasi ya kupata wokovu. Mtu hapati wokovu kwa kutegemea kabila lake, cheo chake, ujuzi wake wala sura yake.
Fikiria kisa cha taifa la Israeli. Ni kweli kwamba Yehova Mungu alishughulika na Waisraeli peke yao, nao ndio waliokuwa na jina lake wakati huo. Lakini Mungu hakuwachagua wawe watu wake anaowatambua kwa sababu ya ukuu au wingi wao. Musa aliwaambia hivi: “[Yehova] hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote.” (Kum. 7:7) “Kwa sababu aliwapenda baba zenu, kwa sababu hiyo aliwachagua wazao wao baada yao, akakutoa katika Misri.”—Kum. 4:37.
Kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba Waisraeli hawakupendelewa walipochaguliwa hivyo? Kwa sababu wao ndio waliokuwa katika wajibu mkubwa kuliko mataifa mengine wasiomjua Yehova Mungu, wa kumtolea hesabu ya mambo waliyofanya. Kwa hiyo, walipokosa kutii sheria yake, walipata laana kubwa zaidi. Jambo hilo linaonekana katika Kumbukumbu la Torati 27:26: “Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya.”
Mataifa yale mengine yaliruhusiwa yaendelee kufuata njia zao, lakini wakaruhusiwa kupata faida kutokana na mipango mingi ya Mungu. Ingawa Yehova ana uwezo wa kunyima watu mwanga wa jua na mvua, aliutumia uwezo huo nyakati chache tu ili kutimiza kusudi fulani la pekee. (Kut. 10:23; Amosi 4:7) Kwa ujumla ameyatendea mataifa kama vile mtume Paulo anavyoeleza watu wa Listra walitendewa: “Zamani zilizopita [Mungu] aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe. Lakini hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.” (Matendo 14:16, 17) Wakati uo huo, Yehova Mungu amekuwa akitayarisha mambo yatakayowapa wanadamu wote baraka Yake kupitia kwa Masihi na wenzake, yaani, kupitia kwa ‘uzao wa Ibrahimu.’—Mwa. 22:18.
Wakati ambao Yehova Mungu alikuwa akiwatumia Waisraeli, watu mmoja mmoja katika mataifa mengine waliweza kuangaliwa naye vizuri. Jambo hilo linaonyeshwa na sala ambayo Mfalme Sulemani alitoa wakati wa kuwekwa wakf kwa hekalu juu ya Mlima Moria. Alimwomba Yehova akasema: “Hata na mgeni naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana kwa ajili ya jina lako; (maana watasikia habari za jina lako kuu, na za mkono wako ulio hodari, na za mkono wako ulionyoshwa;) atakapokuja na kuomba kuielekea nyumba hii; basi, usikie huko mbinguni, makao yako, ukatende kwa kadiri ya yote atakayokuomba mgeni huyo; ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukucha wewe kama watu wako Israeli.”—1 Fal. 8:41-43.
WATU WASIO WAISRAELI WALIBARIKIWA
Biblia inaeleza visa vingi kuonyesha kwamba hata watu wenye imani wasiokuwa Waisraeli walipewa na Yehova Mungu baraka za pekee.
Mfano mmoja ni mjane wa Sarepta aliyemwonyesha Eliya, nabii wa Yehova, ukarimu. Kwa sababu hiyo, mwujiza ulifanywa ukazuia unga na mafuta madogo ya mwanamke huyo yasimalizike wakati wa njaa nyingi. Mwujiza mkubwa zaidi ulifanywa mwanawe pekee alipofufuliwa.—1 Fal. 17:8-24; Luka 4:25, 26.
Rahabu, kahaba wa Yeriko, aliacha kazi yake yenye aibu akamwamini Yehova na kuchukua hatua ya kufuatana na Waisraeli, maana ndio waliokuwa wakitumiwa na Yehova. Basi, yeye na watu wa ukoo wake hawakuangamia pamoja na wakaaji wengine wa Yeriko. Tena, alipata pendeleo bila kujua, akaingizwa katika ukoo wa Masihi alipoolewa kwa njia ya heshima na Salmoni.—Ruthu 4:20-22; Mt. 1:5, 6; Ebr. 11:30, 31; Yak. 2:25.
Vivyo hivyo, Ruthu Mmoabu alipata kibali ya Mungu. Alimchagua Yehova awe Mungu wake, akaiacha nchi ya kwao kwa moyo wa kupenda ili kuishi kati ya Waisraeli, watu waliomtambua Yehova kuwa Mungu wa kweli. Naye Aliye Juu Zaidi alimruhusu aingie katika ukoo wa maana zaidi, uliomtokeza Masihi.—Mt. 1:5.
Masihi Yesu alipokuja, Waisraeli ndio waliopewa nafasi ya kwanza wawe wanafunzi wake washikamanifu kwa sababu ya agano ambalo Mungu alifanya na Ibrahimu babu yao. Halafu mwaka 36 W.K., kikundi cha kwanza cha watu wasiotahiriwa, wasiokuwa Wayahudi, kilipewa pendeleo ilo hilo. Mtume Petro aliwahutubia akawaambia hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.
FUATA MFANO WA MUNGU WA KUTOPENDELEA WATU
Kwa kuwa Mungu hapendelei watu fulani, wote wanaotaka kukubaliwa naye wanapaswa wawe kama yeye. Inawapasa waepuke kupendelea watu fulani kwa sababu ya elimu yao nyingi, pesa zao, cheo chao au mambo kama hayo. Haitupasi kuhukumu mwanadamu ye yote kwa kutegemea kanuni za kimwili zisizokamilika, au za kibinadamu. Jambo la maana si jinsi sura ya mtu ilivyo, bali jinsi alivyo moyoni.
Kwa sababu Mungu hana upendeleo, watumishi wake wana wajibu wa kusaidia wanadamu wenzao wapate maarifa sahihi ya kweli. Hakuna anayepaswa kudhani kwamba mtu fulani hastahili kusaidiwa hivyo. Watu wanaweza kusaidiwa wabadili njia zao ikiwa kweli wanataka kuzibadili. Mtume Paulo aliandikia Wakorintho akawaambia hivi: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi. Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa.” (1 Kor. 6:9-11) Basi, watu wakipatanisha maisha yao na mapenzi ya Mungu, wanaweza kukubaliwa wawe watumishi wake walio safi.
Tukithamini kwamba Mungu hapendelei watu, tutaweza kuwa na maoni ya kiasi juu ya vile wengine wanavyotufikiria. Hatutahangaikia kupendeza wanadamu hasa, wanaoweza kupendezwa nasi tujionyeshapo kijuujuu, bali tutahangaikia kumpendeza Yehova Mungu, auonaye moyo ulivyo. Tutafuata onyo la upole la Maandiko linalosema: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa Bwana ujira wa urithi. Mnamtumikia Bwana Kristo. Maana adhulumuye atapata mapato ya udhalimu wake, wala hakuna upendeleo.”—Kol. 3:23-25.
Hali ya Mungu ya kutopendelea watu imeletea wanadamu baraka nyingi kweli kweli. Wanadamu wote, si wachache tu, wamewekewa msingi wa kuingia katika msimamo unaokubaliwa naye, wakiwa na taraja la kuishi milele. Kwa kujua hivyo, imetupasa tusaidie watu wengi iwezekanavyo wapate maarifa sahihi ya kweli. Imetupasa tuepuke kupendelea watu fulani na kuacha kuhangaika mno juu ya jinsi wanadamu wanavyoweza kutufikiria. Tukifanya mambo yote kama kwamba tunamfanyia Yehova, na kufuata mfano wake wa kutopendelea watu, tunaweza kuwa na uhakika wa kupokea thawabu nyingi.