Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 11/15 kur. 25-27
  • Je, Unamwiga Mungu Wetu Asiyebagua?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Unamwiga Mungu Wetu Asiyebagua?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Rekodi ya Yehova ya Kutobagua
  • Kujifunza Kutokana na Kutobagua kwa Yehova
  • Thamini Kikamili Sifa za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • “Mungu Hana Upendeleo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Mwige Yehova kwa Kutokuwa na Ubaguzi
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2021
  • Mwigeni Yehova, Mungu Wetu Asiye na Ubaguzi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 11/15 kur. 25-27

Je, Unamwiga Mungu Wetu Asiyebagua?

KUTOBAGUA—kwaweza kupatikana wapi? Kuna Mmoja asiye na ubaguzi, upendeleo, na uonevu hata kidogo. Ni Yehova Mungu, Muumba wa wanadamu. Hata hivyo, kuhusu wanadamu, mwandikaji Mwingereza wa karne ya 19 Charles Lamb aliandika kwa unyoofu hivi: “Kwa ufupi, mimi nimejawa na ubaguzi—wa mapendezi na machukio.”

Kuhusu kutobagua, mahusiano ya kibinadamu yamepungukiwa sana. Karne nyingi zilizopita Mfalme Sulemani wa Israeli mwenye hekima, alionelea kwamba “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9, Union Version ya Kiswahili chapa ya 1952) Chuki ya kijamii, mahitilafiano ya kitaifa, na uadui wa kifamilia waendelea kuongezeka. Kwa hiyo, je, kuamini kwamba wanadamu wenyewe waweza kukuza jamii isiyobagua ni jambo halisi?

Jitihada zenye uangalifu zinahitajiwa ili kudhibiti mitazamo yetu na kujiondolea ubaguzi wowote wenye mizizi ya ndani sana. (Waefeso 4:22-24) Bila kutambua twaweza kuelekea kuwa na mitazamo iliyofanyizwa na mazingira yetu ya kirafiki na ya kielimu na ambayo ilitia mizizi katika familia yetu, jamii yetu, na malezi yetu ya kitaifa. Mibetuko hiyo ionekanayo kuwa midogo mara nyingi huwa yenye kina sana na huendeleza mitazamo inayoongoza kwenye ubaguzi. Hata mwanasheria na mhariri wa Scotland Lord Francis Jeffrey alikiri hivi: “Hakuna lolote liponyokalo ufahamu wa mtu kwa muda mrefu kuliko kina chenye mizizi ya ndani sana cha ubaguzi wake.”

Lenaa ni mtu mmoja anayekiri kwamba jitihada zenye uangalifu zinahitajiwa ili kupigana na mbetuko wa kubagua. Kukomesha hisia za ubaguzi ndani yako mwenyewe, yeye asema huhitaji jitihada nyingi kwa sababu malezi ni uvutano wenye nguvu sana.” Lena atambua pia kwamba vikumbusha vya daima vinahitajiwa.

Rekodi ya Yehova ya Kutobagua

Yehova ni kielelezo kikamilifu cha kutobagua. Tangu kurasa za ufunguzi za Biblia, twasoma jinsi alivyodhihirisha kutobagua kwake katika mahusiano yake pamoja na wanadamu. Twaweza kujifunza mengi kutokana na vielelezo na vikumbusha hivyo bora.

Yehova alionyesha kutobagua katika kuongoza mambo hivi kwamba mtume Myahudi Petro alipiga mbiu ya habari njema kwa Kornelio na Wasio Wayahudi wengine katika 36 W.K. Wakati huo Petro alisema hivi: “Mungu hana upendeleo [“ubaguzi,” NW]; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.

Katika shughuli zake zote pamoja na familia ya kibinadamu, Yehova ameonyesha kwa udumifu kutobagua kwake. Kristo Yesu alisema hivi juu ya Baba yake: “Huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mathayo 5:45) Petro akimkweza zaidi Yehova kuwa Mungu asiyebagua, alishuhudia hivi: “Huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.”—2 Petro 3:9.

Katika siku ya Noa, wakati ‘maovu ya mwanadamu yalipokuwa makubwa duniani na kwamba kila kusudi alilowaza moyoni mwake lilikuwa baya tu sikuzote,’ Yehova aliamua uharibifu wa ulimwengu huo wa wanadamu. (Mwanzo 6:5-7, 11, 12) Hata hivyo, kwa amri ya Mungu na kwa kuonekana kwa urahisi na watu wa siku yake, Noa alijenga safina. Alipokuwa akijenga safina na wanawe, Noa alikuwa pia “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5, NW) Licha ya kujua mbetuko mwovu wa mioyo ya kizazi hicho, Yehova aliwatumia kwa kutobagua ujumbe ulio wazi. Aliwasihi mioyoni na akilini mwao kwa kumwamuru Noa ajenge na kuhubiri. Walikuwa na kila fursa ya kuitikia, lakini badala ya hivyo ‘hawakutambua, hata Gharika ikaja.’—Mathayo 24:39.

Hicho ni kielelezo bora kama nini cha kutobagua kwa Yehova! Katika siku hizi za mwisho zenye hatari, kielelezo hicho huwasukuma watumishi wa Mungu wapige mbiu ya habari njema ya Ufalme kwa kutobagua kwa njia iyo hiyo. Zaidi, hawajizuii kutangaza siku ya kisasi ya Yehova. Hadharani, wao huwatolea bila ubaguzi watu wote ujumbe wa Yehova ili wausikie.—Isaya 61:1, 2.

Ahadi za Yehova kwa wazee wa ukoo Abrahamu, Isaka, na Yakobo zilionyesha waziwazi kwamba yeye ni Mungu asiyebagua. Kupitia nasaba ya familia yao hususa kungekuja Yule aliyewekwa rasmi ambaye kupitia kwake ‘mataifa yote ya dunia yangejibarikia.’ (Mwanzo 22:18; 26:4; 28:14) Kristo Yesu alithibitika kuwa Yule aliyewekwa rasmi. Kupitia kifo cha Yesu na ufufuo wake, Yehova aliandaa njia ya wokovu kwa ajili ya wanadamu wote watiifu. Ndiyo, manufaa za dhabihu ya fidia ya Kristo zinapatikana bila ubaguzi.

Katika siku za Musa, kutobagua kwa Yehova kulidhihirika kuhusiana na binti za Selofehadi katika njia yenye kupendeza zaidi. Hao wanawake watano walikabili mashaka kuhusu urithi wa baba yao katika Bara Lililoahidiwa. Ilikuwa hivyo kwa sababu ilikuwa desturi katika Israeli kwa urithi wa nchi kupitishwa kupitia wana wa mtu. Hata hivyo, Selofehadi alikufa bila mwana wa kupokea urithi. Kwa hiyo, hao binti watano wa Selofehadi wakaleta ombi lao mbele ya Musa la kutaka watendewe bila ubaguzi, wakisema hivi: “Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu.” Yehova aliyasikiliza maombi yao akamwagiza Musa hivi: “Mtu akifa, naye hana mwana wa kiume, ndipo utampa binti yake urithi wake.”—Hesabu 27:1-11.

Ni kielelezo kilichoje cha upendo usio na ubaguzi! Ili kuhakikisha kwamba urithi wa kikabila usipitishwe na kupewa kabila jingine binti walipoolewa, walipasa kuolewa tu “katika jamaa ya kabila ya baba zao.”—Hesabu 36:5-12.

Ufahamu zaidi wenye kina katika kutobagua kwa Yehova waonekana katika siku za mwamuzi na nabii Samweli. Yehova alimpa utume wa kumtia mafuta mfalme mpya wa kabila la Yuda katika familia ya Yese Mbethlehemu. Lakini Yese alikuwa na wana wanane. Ni nani ambaye angetiwa mafuta awe mfalme? Samweli alivutiwa na kimo cha kimwili cha Eliabu. Hata hivyo, Yehova hakushawishwa na sura ya nje. Alimwambia Samweli hivi: “Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; . . . BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” Daudi, mwana mchanga zaidi wa Yese, alichaguliwa.—1 Samweli 16:1, 6-13.

Kujifunza Kutokana na Kutobagua kwa Yehova

Wazee Wakristo hufanya vema kumwiga Yehova kwa kuangalia sifa za kiroho za mwamini mwenzao. Ni rahisi kuhukumu mtu kulingana na viwango vyetu wenyewe, tukiruhusu hisia zetu wenyewe zizuie uamuzi wetu. Kama vile mzee mmoja alivyosema, “mimi hujaribu kushughulika na wengine katika njia impendezayo Yehova, wala si kwa kutegemea mawazo yangu yaliyofikiriwa kimbele.” Jinsi inavyonufaisha kwa watumishi wote wa Yehova kutumia Neno lake kuwa kiwango chao!

Vielelezo vya Kibiblia vilivyotangulia hutusaidia kupigana na hisia ambazo bado tuko nazo za ubaguzi wa kijamii au kitaifa. Kwa kuiga kutobagua kwa Yehova, twalinda kutaniko la Kikristo dhidi ya ubaguzi na upendeleo.

Mtume Petro alijifunza kuwa “Mungu hana upendeleo [“ubaguzi,” NW].” (Matendo 10:34) Upendeleo ni adui wa kutobagua, nao huvunja kanuni za upendo na muungano. Yesu alivutia maskini, wanyonge, na watu wa hali ya chini, akafanya mzigo wao uwe mwepesi. (Mathayo 11:28-30) Yeye alitokeza kwa kutofautiana sana na viongozi wa kidini Wayahudi, waliopiga ubwana juu ya watu, wakiwalemeza kwa mzigo mzito wa kanuni. (Luka 11:45, 46) Kufanya hivyo na kupendelea matajiri na walio maarufu bila shaka hakukupatana na mafundisho ya Kristo.—Yakobo 2:1-4, 9.

Leo, wazee Wakristo hunyenyekea ukichwa wa Kristo nao huonyesha kutobagua kuelekea watu wote wa Yehova waliojiweka wakfu. ‘Wanapolichunga kundi la Mungu lililo kwao,’ wanaepuka kuonyesha upendeleo kwa sababu ya matabaka ya kiuchumi, tofauti za kinyutu, au vifungo vya familia. (1 Petro 5:2) Kwa kumwiga Mungu asiye na ubaguzi na kutii onyo lake dhidi ya matendo ya upendeleo, wazee Wakristo huendeleza roho ya kutobagua katika kutaniko.

Kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova ni udugu wa kimataifa. Ni uthibitisho halisi wa kwamba jamii isiyo na upendeleo, wala ubaguzi yaweza kuwa uhalisi chini ya mwelekezo wa Yesu Kristo. Hao Mashahidi ‘wamevaa utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.’ (Waefeso 4:24) Ndiyo, wanajifunza kutokana na kielelezo kikamilifu cha Mungu asiye na ubaguzi, Yehova, nao wana taraja la uhai wa milele katika ulimwengu mpya usio na ubaguzi wowote.—2 Petro 3:13.

[Maelezo ya Chini]

a Jina la badala.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mtume Petro alijifunza kwamba Mungu hana ubaguzi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki