Kuendeleza Maoni Yenye Kusawazika Juu ya Wakati
“Utujulishe kuzihesabu siku zetu, tujipatie moyo wa hekima.”—Zab. 90:12.
1, 2. Sote tunapatwa na nini wakati upitapo?
UHAI ni mali yenye thamani nyingi sana. Bila huo vitu vingine vyote havina maana. (Mt. 6:25-27; 16:26) Lakini hata katika ulimwengu wetu wa kisasa muda wa maisha wa wanadamu bado ni mfupi nao humalizika upesi mno. Ni kama vile mwandikaji wa zaburi ya 90 alivyoandika zamani: “Miaka sabini ndio muda wa maisha yetu, themanini nguvu zetu zikivumilia; miaka yenye kufanya haraka ni kazi ngumu na huzuni, hivyo inapita haraka na kusahauliwa.”—Zab. 90:10, New English Bible.
2 Katika nchi nyingi, mtu akifikia umri wa miaka 30 anakuwa katika ujana. Lakini, ufupi wa muda wa maisha ya kibinadamu wamaanisha kwamba wakati huo amekwisha anza kuzidi kudhoofika kimwili, uwezo mbalimbali na utendaji wa mwili umeanza kupungua. Naam, miaka yapita upesi kweli kweli.
3. Ni kwa sababu gani watu hawangojei kutimizwa kwa tamaa zao?
3 Kwa hiyo basi, si ajabu wanadamu kwa ujumla hujali sana wakati. Si ajabu, pia, kwamba wanadamu peke yao kati ya viumbe vyote vya dunia vilivyo hai ndio wanaohangaikia wakati ujao kwa kutumia akili, wakipanga mambo watakayofanya wakati huo kwa bidii, wakitaka sana kujua mambo yatakayotendeka wakati ujao. (Mhu. 3:11) Kwa sababu watu huwa na wakati mwingi sana kabla hawajafa, wao huelekea kuwa wenye haraka wasitake kungoja kuona wakitimiza matakwa yao.
4, 5. (a) Yehova Mungu yu tofauti namna gani kwa jinsi aonavyo wakati? (b) Kwa sababu gani kuchagua kwa Mungu wakati wa kufanya jambo fulani kwatamanika zaidi kuliko kwa wanadamu?
4 Hali ya mwanadamu asiyekamilika basi yatofautiana sana na ya Muumba wake, ambaye ni wa milele, asiyekuwa na wakati wa kuwako Kwake. Mwandikaji yule yule wa zaburi ya 90 aliandika juu Yake hivi: “Kabla milima haijazaliwa, au dunia na ulimwengu havijazaliwa katika utungu wa kuzaa, kutoka kizazi mpaka kizazi wa milele ndiwe Mungu. . . . kwa maana katika kuona kwako miaka elfu ni kama jana.”—Zab. 90:2-4, NE.
5 Lakini je! hii inafanya Yehova Mungu awe baridi juu ya wakati? Sivyo; wala haimzuii asipendezwe sana sana na wakati ujao pamoja na matukio yake. Walakini, kwa sababu yeye aweza kuona mambo, si kulingana na maoni ya wanadamu wasiokamilika, wanaoishi muda mfupi, bali kulingana na maoni ya umilele, Yehova Mungu hakazwi kamwe na wasiwasi atimize jambo kabla hajaishiwa na wakati. (Zab. 90:2; 2 Pet. 2:8) Yeye aweza kuchunguza wakati wote na kuamua ni wakati gani hasa atakapochukua hatua na kutimiza makusudi yake yasiyoshindwa katika wakati ufaao kabisa, wakati ulio bora kwa wote wanaohusika, si kwa haraka mno wala si kwa kuchelewa mno.
6. Ijapokuwa Mungu ana wakati wa milele, je! hili lamzuia asifanye jambo fulani kulingana na wakati uliopangwa?
6 Akiwa na ujuzi huo juu ya wakati ujao na akiwa na uwezo wote, Mungu aweza kujiwekea wajibu na kufanya jambo wakati fulani ujao aliopanga, na nyakati nyingine amejulisha wanadamu hilo. Kwa mfano, alimwambia Abramu (Ibrahimu): “Ujue hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake, watawatumikia watu wale, nao watateswa muda wa miaka mia nne.” (Mwa. 15:13; Matendo 7:6, 7) Kulingana na unabii wake, mwishoni mwa ile miaka mia nne Yehova Mungu aliweka huru wazao wa Ibrahimu, Waisraeli, kutoka utumwani, wakaanza kutoka Misri.
7. (a) Wakati wa Mungu uliopangwa kufunguliwa Wayahudi waliohamishwa Babeli ulitimizwaje barabara? (b) Kwa habari ya kutokea kwa Masihi?
7 Baadaye, Mungu alitabiri kungekuwa na kipindi cha miaka 70 cha ukiwa wa Yuda, na wakati kipindi hicho kilipokwisha Wayahudi walikombolewa katika wakati barabara. (Yer. 25:8-11; Dan. 9:2) Vivyo hivyo, kutokea kwa Masihi kulitabiriwa kwamba kungetukia miaka 483 (“juma” 69 za miaka) kutoka wakati wa kutoa agizo la kujenga upya kuta za Yerusalemu na, katika wakati barabara, mwishoni mwa kipindi hicho mwaka wa 29 W.K., Yesu Kristo alibatizwa akatiwa mafuta awe Masihi aliyeahidiwa.—Dan. 9:24-27.
8. Je! yawezekana kwetu kujua wakati sehemu fulani ya kusudi la Mungu itakapotukia ikiwa hakutangaza wakati barabara?
8 Kwa hiyo, wakati Yehova Mungu ajulishapo wakati fulani wa kutimizwa kwa sehemu fulani ya kusudi lake la kimungu, watumishi wake waaminifu wanaweza kutegemea kabisa usahihi kamili wa orodha iliyotangazwa. Lakini wakati hakufanya tangazo hilo, hawawezi kuamua wakati wa kutimizwa kwa kusudi hilo. Ndivyo ilivyo juu ya kuweka wakati wa kutokea kwa “dhiki kubwa” ambayo Mwana wa Mungu alitabiri, wakati wa hukumu ya kimungu itakayofungulia njia mwanzo wa utawala wa Ufalme wa miaka elfu moja, utakaoletea dunia hii na wakaaji wake baraka zisizoeleweka.—Mt. 24:21, 22; Ufu. 7:14-17.
MAMBO YALIYOFICHWA NA MAMBO YALIYOFUNULIWA
9. Neno la Mungu kupitia kwa Musa katika Kumbukumbu la Torati laonyesha nini juu ya kufahamu kwetu makusudi Yake?
9 Je! tudhani ni ajabu Mungu kujiwekea mwenyewe ujuzi huo kwa njia hii? Huko nyuma wakati Waisraeli walipokuwa wakiikaribia Nchi ya Ahadi, nabii Musa aliyaandika maneno haya yaliyoongozwa na Mungu wetu; lakini mambo yaliyofunuliwa 29:29: “Mambo ya siri ni ya [Yehova], Mungu wetu; lakini mambo yaliyofunuliwa ni yetu sisi na watoto wetu milele; ili tuyafanye maneno yote ya sheria hii.” Naam, Mungu hutufunulia mambo yote tunayohitaji kweli ndio tujue kumtumikia Yehova Mungu kwa uaminifu, na tunayohitaji ili kututia nguvu katika tumaini letu na kusadiki kwetu. Lakini anaweza pia kuficha mambo ikiwa kufanya hivyo kutatimiza kusudi lake vizuri zaidi, bila kudhuru wala kupungukia watumishi wake.
10. (a) Maneno ya Yesu aliyosema kabla ya kupaa kwake mbinguni yafunua nini juu ya kujua kwetu nyakati au tarehe fulani? (b) Wengine kati ya wanafunzi wa kwanza walipokosea kuhesabu wakati wa matukio, mtume Paulo aliwaandikia nini?
10 Musa Mkuu, Kristo Yesu aliwaambia pia wanafunzi wake, muda mfupi kabla hajapaa mbinguni hivi: “Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.” Hiyo ilikuwa kujibu ulizo lao juu ya kuurudisha ufalme, jambo walilotaka kuona kwa shauku. Ndipo alipoendelea kusema: “Lakini mtapokea [nini? Si ujuzi wa zile ‘nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe,’ bali] nguvu, [ikiisha kuwajilia juu yenu roho takatifu].” (Matendo 1:6-8; 3:20-23) Mungu angewatia nguvu na aliwatia watimize kazi na utumishi waliogawiwa kupatana na mapenzi yake aliyowafunulia wafanye. Walakini, yako mambo ambayo hawakujua na, baadaye, wanafunzi wengine walielekea kuamua-amua matukio fulani yaliyoahidiwa, wakijaribu kwa njia hiyo kuyaharakisha. (Linganisha 2 Wathesalonike 2:1-5.) Lakini mambo yote waliyohitaji kujua hasa ili wawe na imani yenye nguvu, wasadiki na wawe na ushujaa, na watende kwa hekima, Mungu aliwapa.
11. Je! wanafunzi walijua tarehe barabara ya uharibifu wa Yerusalemu, au nini?
11 Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya uharibifu wa Yerusalemu katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Kristo Yesu alifunulia wanafunzi wake hali ambazo zingetangulia na kuongoza kwenye uharibifu wa mji huo usioaminika, mahali pa kati pa ibada ya Kiyahudi ya wakati huo. Kwa kuona hali hizo zenye kufanyiza “ishara” hiyo, wanafunzi wake wangejua “uharibifu wake [Yerusalemu] “umekaribia. (Luka 21:10-20) Aliwaambia kwamba “kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatimie.” (Marko 13:30) Kwa hiyo iliwapasa waangalie jambo hilo wakati uo huo, lilikuwa jambo la kizazi chao. Lakini hawakuambiwa wakati barabara ambapo lingetukia.
12. (a) Wakristo katika Yerusalemu waliwezaje kuokoka kabla ya mji kuharibiwa pasipo kujua tarehe? (b) Kulikuwako jaribu gani kwa wale waliokimbia mara mazingiwa ya Yerusalemu yalipoondolewa?
12 Wakati ulifika wakaona sehemu ya ishara yenye kuhusu kuzingirwa kwa Yerusalemu na majeshi ya Rumi yenye kupiga kambi. Hali (kuondoka kwa muda kusikotazamiwa kwa vikosi vya Kirumi) ziliwaruhusu baada ya hapo waukimbie mji uliohukumiwa maangamizi watafute kimbilio katika majimbo yenye milima. Hawakujua bado wakati uharibifu halisi ungetokea. Kwa kweli, karibu miaka minne ilikwisha kati ya wakati wa kukimbia kwao na uharibifu wa Yerusalemu. Ingalikuwa vyepesi kwao wakati huo kulegea katika kukesha kwao au kudhani kwamba walikuwa wameielewa vibaya ishara na, kwa sababu hiyo, wangalikosa kutii onyo la Yesu: “Ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani, na walio katikati yake wakimbilie nje, na walio katika mashamba wasiungie.”—Luka 21:20, 21.
13. (a) Ni unabii gani wa Yesu wa wakati uliotimizwa hasa katika uharibifu wa Yerusalemu? (b) Ijapokuwa hakutoa tarehe barabara, je! onyo hilo la wakati lilikuwa lenye kufaidika kwa Wakristo?
13 Jambo moja ni hakika: Kizazi chao kiliona utimizo wa mambo aliyoonya Mwana wa Mungu. Waliosikia, waliokesha, walifaulu kuokoka msiba mkuu uliokumba Yerusalemu. Lakini historia yaonyesha kwamba mamia ya maelfu ya watu wengine hawakuokoka. Wao walikuwa wamelala wasione maana ya hali zilizokuwako na haraka ya siku walizokuwa wakiishi. Wakati Rumi ulipopeleka tena majeshi yake yakaufyatukia Yerusalemu na kuubana mwaka wa 70 W.K., mji ulitekwa ukiwa na jungu zima la maelfu ya wageni waliokuwa wamehudhuria sikukuu ya Kupitwa ya mwaka huo. Kati ya hao na wakaaji wa humo, mamia ya maelfu walikufa kwa kipindi cha karibu miezi mitano tu. Walikuwa wamekosa kuonyesha imani katika onyo la kimungu lililotolewa kupitia kwa Mwana wa Mungu; ‘hawakutambua majira ya kujiliwa kwao.’—Luka 19:41-44.
14, 15. Tuna ushuhuda gani kwamba onyo ambalo Yesu aliwapa wanafunzi wake wakati huo linatimizwa ulimwenguni pote katika wakati wetu?
14 Leo twaishi karne kumi na tisa kutoka kipindi hicho cha maana sana. Lakini wakati wetu ni wenye hatari zaidi. Akiandika karibu na mwisho wa karne ya kwanza, yaani makumi mengi ya miaka baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu, mtume Yohana alisimulia mambo yale yale ambayo Yesu alikuwa ametoa kama “ishara” kwa wanafunzi wake katika unabii wake uliohusu uharibifu wa Yerusalemu. Lakini Ufunuo, uliopokewa na Yohana kutoka kwa Yesu, ulihusu mambo ya wakati utakaokuja, mambo yasiyokuwa yametokea bado. (Ufu. 1:1) Na yale aliyoandika Yohana yaonyesha kwamba “ishara” aliyotoa Yesu ingehusu dunia nzima, vita, njaa kuu, bei za juu za chakula, magonjwa ya kipuku yakipata sehemu kubwa za watu wa mahali pengi pa dunia yote. (Ufu. 6:3-8) Baada ya hapo ataja ‘dhiki kubwa’ ambayo “mkutano mkubwa” wa watumishi wa Mungu utapitia ukiwa hai na salama, watu wa mataifa yote, makabila yote na lugha zote. (Ufu. 7:9-15) Dhiki hiyo ilikuwa sehemu ya mambo ambayo hayajaja bado.
15 Huu “ufunuo wa Yesu Kristo” basi waonyesha kwamba unabii wa Yesu, ulioandikwa katika Mathayo 24, Marko 13 na Luka 21, juu ya “dhiki kubwa” haukuhusu karne ya kwanza tu. Waonyesha kwamba dhiki iliyoupata Yerusalemu ilikuwa utimizo mdogo tu wa unabii huo na kwamba utimizo wake mkubwa wa dunia nzima utafanya dhiki ya Yerusalemu ionekane kitu kidogo sana zikilinganishwa. Kama vile kizazi kilichoishi na kusikia onyo la Yesu katika karne ya kwanza ndicho kizazi kilichoona utimizo wa maneno yake, ndivyo kizazi hiki—kizazi kinachoona utimizo mkubwa wa “ishara” yake inayojulisha siku za mwisho za taratibu hii ya mambo—kitapatwa na dhiki ya dunia nzima inayokaribia.—Mt. 24:34.
16. Kwa kuwa hatukuambiwa siku wala hata mwaka wa kutokea “dhiki kubwa,” je! kuna sababu ya kuwa baridi?
16 Basi, je! Mungu ametufunulia nini kuhusu hilo? Bila shaka hakutuacha bila uongozi. Kwa unabii mbalimbali kama ule ulioangaliwa sasa hivi anatuwezesha kujua tu wapi katika kipindi cha wakati. Utimizo wa neno lake la unabii watusadikisha kwamba Mungu hasinzii wala si mkawivu, na kama vile mtume Petro alivyosema kuhusu wenye kutenda kwa uovu, “hukumu yao tangu zamani haikawii, wala uvunjifu wao hausinzii.” (2 Pet. 2:3) Tuna habari na ushuhuda wa kutosha kutusadikisha kwamba tunaishi katika “wakati wa mwisho” wa taratibu ya mambo iliyopo isiyo na haki. Hata hivyo, yako mambo zaidi ambayo Mungu hajatufunulia. Mojawapo la mambo hayo ni wakati wa kutokea kwa “dhiki kubwa” iliyofananishwa na dhiki iliyoupata Yerusalemu, dhiki itakayotimia katika dunia nzima.
NYAKATI AMBAZO MUNGU HAJAFUNUA
17. Twajua kwamba tumo mwishoni mwa miaka elfu sita ya historia ya kibinadamu, lakini hili lina uhusiano gani na siku ya Mungu ya kupumzika?
17 Ziko sababu za kutoweza kwetu kujua. Kwanza, ingawa tarehe za Biblia zaonyesha wazi kwamba tumefikia miaka elfu sita tangu wakati wa kuumbwa kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu, hazielezi ni muda gani uliopita baada ya tukio hilo ndipo siku ya sita ya kuumba ikamalizika na kipindi cha saba au “siku” ya saba ya kuumba, siku kuu ya Mungu ya kupumzika, ikaanza. Mwanzo sura ya pili, mstari wa 3, wasema kwamba Yehova aliibariki akaitakasa “siku” hiyo, na kwa hiyo linaelekea kuwa jambo la akili kuwaza kwamba katika siku iyo hiyo taratibu mbovu ya kale itaondolewa isimamishwe taratibu mpya yenye haki ya Mungu kupitia kwa utawala wa miaka elfu wa Mwana wa Mungu. Hivyo kuna sababu ya kuamini kwamba kipindi hicho cha miaka elfu ndicho kitakachokuwa sehemu ya kumalizia ya siku hiyo kuu ya kupumzika na ndipo dunia na wakaaji wake watakaporudishiwa hali ya ukamilifu. Hiyo itawezesha Mungu kusema juu ya siku hiyo ya saba na matokeo yake—kama alivyosema juu ya siku nyingine za kuumba—kwamba ‘ilikuwa njema.’—Mwa. 1:4, 10, 12, 18, 21, 25, 31.
18, 19. (a) Kulitukia nini, baada ya kuumbwa kwa Adamu, kabla ya kuanza siku ya Mungu ya kupumzika? (b) Wakati wa kuumbwa kwake, Adamu alikuwa tofauti sana namna gani na kitoto kichanga kilichozaliwa hivi karibuni?
18 Lakini siku kuu hiyo haikuanza mara moja baada ya Adamu kuumbwa. Matukio mengine yalitukia baada ya kuumbwa kwa Adamu lakini kabla ya kumalizika kwa siku ya sita ya kuumba. Mojawapo la matukio hayo ni lenye maana kuu kwetu sote. Hilo ndilo kuumbwa kwa mwanamke wa kwanza, Hawa. Bila hivyo hakuna ye yote kati yetu angalikuwa hai leo, kwa maana, kama mtume Paulo atajavyo katika 1 Wakorintho 11:12, “kama mwanamke alitoka katika mwanamume, vile vile mwanamume naye huzaliwa na mwanamke,” nasi sote tulihitaji mama wa kibinadamu ndio tukazaliwa.
19 Ni muda gani uliopita kati ya kuumbwa kwa mwanamume na kuumbwa kwa mwanamke? Biblia haifunui hilo. Pengine ulikuwa wakati mfupi kiasi. Adamu aliumbwa—si akiwa mtoto wala kijana mwenye kubalehe—bali kama mtu mzima, mwanamume aliyekomaa kabisa, kimwili na katika akili pia. Haikuwa lazima atambae kwanza ajifunze kutembea, wala kubwabwaja kitoto ndio aweze kusema. Aliumbwa akiwa na uwezo huo mbalimbali na angeweza kupashana habari na Muumba wake wa kimbinguni na angeweza kufanya kazi ya kusitawisha na kuyatunza makao ya bustani. Angeweza kufahamu maagizo ya kimungu na vilevile katazo lililohusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwa. 2:15-17) Katika pande hizo, basi, angalikuwa katika hali ya kupokea mke wakati wo wote.
20. Hata hivyo, Adamu angeweza kulinganishwa na kitoto kilichozaliwa hivi karibuni katika mambo gani wakati wa kuumbwa kwake?
20 Ni kweli, lakini Adamu alikuwa kama kitoto kichanga kilichozaliwa karibuni katika mambo fulani alipoumbwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu, ingawa alikuwa mtu mzima, siku alipoumbwa ili ku wa ndiyo siku yake ya kwanza kuishi. Kila kitu alichoona—kila mti, ua, mmea, kila kijito, ziwa la maji, mto, kila kiumbe kati ya ndege, wanyama na samaki—alikuwa akikiona kwa mara ya kwanza. Ndivyo ilivyokuwa kwa kila alilofanya. Alipotembea hiyo ilikuwa hatua yake ya kwanza; na ndivyo na ujuzi wa kukimbia, kupanda mahali, kugusa, kunusa, kuonja, kula—yote hayo yalikuwa mambo mapya kabisa kwake. Lo! bila shaka alitaka kudadisi sana alipochunguza kazi zenye kusisimua za Yehova Mungu akafahamiana na makao yake ya bustani! Je! angeruhusiwa muda gani wa kumaliza udadisi wake kabla hajachukua madaraka zaidi kama kichwa cha jamaa?
21, 22. Ni sababu gani zinazowezesha kwamba Adamu alikuwa katika Edeni kwa muda fulani wa kutosha kabla ya kuumbwa kwa Hawa?
21 Haielekei kuwa makao hayo ya Edeni yalikuwa mahali padogo sana. Palikuwa na namna zote za miti, kulingana na Mwanzo sura ya pili. Na kulikuwa na “mto katika Edeni wa kuitilia bustani maji,” mto uliokuwa mkubwa kuweza kujitenga na kufanyiza vyanzo vya mito minne mikubwa, na mingine yayo bado yatiririka leo. (Mwa. 2:8-10) Ingemchukua Adamu wakati wa kupeleleza yote ili alifahamu eneo hilo alilogawiwa atunze na kulima.
22 “Lakini,” huenda mtu akauliza, “isingependeza kama angalipaswa kufanya mambo hayo yote mapya na mwanadamu mwenzake, mke, moja kwa moja na kwa njia hiyo ajifunze pamoja naye?” Huenda ikawa, lakini je! isingefaa zaidi kama alipaswa kupata maarifa na ujuzi mwingi kabla ya hapo? Halafu, akipata mwenzi, angekuwa katika hali ya kuweza kujibu maulizo yake na kumweleza mambo, kwa njia hiyo amfanye mkewe azidishe heshima yake kwake kama kichwa chake. (Efe. 5:22, 23) Onyo la Mungu la moja kwa moja kwa Adamu juu ya matokeo ya kula kwa uasi katika mti uliokatazwa lilimfanya Adamu awe nabii wa Mungu kwa mwenzi ambaye Yeye angemwumbia mwanamume baadaye.—Mwa. 2:16, 17.
23, 24. Kwa habari ya wakati, kutaja kwa Adamu majina ya wanyama wote kwaonyesha nini?
23 Habari ya pekee ambayo Biblia hutuambia ni kwamba, kabla Mungu hajaumba Hawa, alianza kumletea mwanamume viumbe vyote alivyokuwa amefanya na “Adamu akawapa majina yao kila mnyama wa kufugwa, na ndege wa angani, na kila mnyama wa mwituni; lakini hakuonekana wa kumsaidia Adamu aliyefanana naye.” (Mwa. 2:18-20) Hayo ni maneno machache tu yanayosimulia hilo; lakini lilichukua muda gani?
24 Ufupi wa masimulizi ya Mwanzo kwa hakika haupaswi kutufanya tudhani Mungu alikusanya tu wanyama wote na ndege wote wakawa kundi kubwa kisha akawapitisha kwa Adamu huku yeye akiwaita majina upesi upesi, mmoja kwa mmoja. Ni kweli kwamba huenda ikawa alipaswa kujishughulisha na aina za jamii za msingi si namna zote za viumbe zilizotokea katika aina hizo za jamii. Lakini hata iwe hivyo, hatuwezi kukataa uwezekano wa kwamba pengine wanyama walimkaribia Adamu kiasi cha kutosha aweze kuwachunguza kwa muda, akitazama sana tabia zao za silika na umbo lao, kisha kuchagua jina la kufaa sana kila mmoja, Mungu ‘alipowaleta’ viumbe hao kwa Adamu. Hii ingeweza kumaanisha wakati mwingi ulipita. Na tuangalie kwamba, mwishowe wakati Adamu alipomwona mke wake aliyeumbwa karibuni, maneno yake ya kwanza yalikuwa: “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu.” Hiyo pia ingeweza kuonyesha kwamba alikuwa amengoja muda fulani kabla hajapokea mwanadamu mfano wake mwenye kupendeza.
25. Ni shauri gani tunaloweza kukata juu ya wakati uliopita kati ya mwanzo wa historia ya wanadamu na kuumbwa kwa Hawa, pamoja na kupumzika kwa Mungu?
25 Basi, hiyo yamaanisha nini? Hivi tu: Kwamba sababu hizo, pamoja na uwezekano wote wa wakati ambao pengine ulipita, zinatuzuia tusiseme kwa hakika ni wakati gani uliopita kati ya kuumbwa kwa Adamu na kuumbwa kwa mwanamke wa kwanza. Hatujui kama ulikuwa wakati mfupi kama mwezi au miezi michache, mwaka au hata zaidi. Lakini lazima wakati wo wote uliopita uongezwe kwa wakati uliopita tangu Adamu alipoumbwa ili tujue tu wapi katika “siku” ya saba ya Mungu, siku yake kuu ya kupumzika. Kwa hiyo kufikia kwetu miaka elfu sita tangu mwanadamu alipotokea ni jambo moja. Kufikia miaka elfu sita katika “siku” ya saba ya Mungu ya kuumba ni jambo jingine kabisa. Nasi hatujui tumo katika wakati gani wa siku hiyo.
26, 27. Kulingana na yale ambayo tumezungumza, je! tarehe hazina maana kwetu?
26 Walakini, hiyo haimaanishi kwamba tarehe si za maana kwetu. Ni jambo la asili kwetu kupendezwa nazo, kwa maana Mungu ameona inafaa kuzifanya sehemu ya maana ya Neno lake aliloliongoza kwa roho yake. Juu ya manabii wa kale, mtume Petro asema kwamba “wakatafuta ni wakati upi, na wakati wa namna gani ulioonywa na [roho] . . . [iliyotangulia] kuyashuhudia mateso yatakayompata Kristo, na utukufu utakaokuwako baada ya hayo.”—1 Pet. 1:10, 11.
27 Sisi leo tunataka sana kujua kwa haki tumo sasa katika “wakati” upi, naye Mungu atueleza habari hiyo tuhitajiyo. Manabii wa Mungu wa kale walikuwa na imani kamili kwamba mambo yote aliyokuwa amesema Mungu yangetimia. Ingawa hatujui mambo fulani au nyakati, tunaweza kuwa na imani iyo hiyo imara na twapaswa kuwa nayo katika kutobadilika kwa kusudi la Mungu. Mwana wa Mungu ametupa sababu yenye nguvu tukae macho tuone kutimizwa kwa kusudi hilo, kama ionyeshavyo makala inayofuata.
[Picha katika ukurasa wa 539]
AHADI ZA YEHOVA HUTIMIZWA KULINGANA NA WAKATI WAKE HASA ULIOWEKWA
Masihi alitokea kulingana na wakati hasa uliotabiriwa
Baada ya miaka 70 Yehova Babeli alifungulisha Waisraeli Babeli wakairudishe nchi ya Yuda
Baada ya miaka 400 ya kuteswa, Waisraeli walifunguliwa Misri kwa wakati barabara