Ili Upate Uzima wa Milele Ulioahidiwa,—Onyesha Imani!
1. Kwa kuwa Ibilisi ana “wakati mchache,” kwa sababu gani sasa watendaji wa mapenzi ya Mungu wanatakiwa kwa haraka zaidi waonyeshe imani?
“WAKATI mchache” ambapo Shetani Ibilisi na jeshi lake la mashetani wamezuiwa hapa duniani sasa wakaribia kumalizika. (Ufu. 12:7-12) Kwa hiyo aweza kutazamiwa azidishe vita yake juu ya “waliosalia” wa “uzao” wa “mwanamke” wa mbinguni wa Mungu na juu ya “mkutano mkubwa” wa watangazaji wenzao wa ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Kwa hiyo linakuwa jambo la muhimu zaidi sana watendaji hawa wa mapenzi ya Mungu waonyeshe imani ili wavumilie kwa uaminifu washambuliwapo na adui.
2, 3. Ijapokuwa wakati wa Shetani uliobaki ni mfupi, yatupasa sisi tulio malengo ya mashambulio ya Shetani tufuate shauri gani ambalo Paulo alitolea Wakristo Waebrania?
2 Wote wanaofanyiwa vita sasa na Shetani wanatiwa moyo waendelee kuwa waaminifu kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mpaka adui watakaposhindwa. Vita hiyo inakaribia kukomeshwa, hasa kwa maana sasa miaka zaidi ya 56 imepita tangu Joka wa mfano na jeshi lake la mashetani walipotupwa chini kutoka mbinguni wakaja katika ujirani wa dunia yetu, wakiwa huru kwa “wakati mchache tu.” Ijapokuwa wakati ni mfupi, lazima bado tufuate shauri la mtume Paulo, lililoandikwa katika Waebrania 10:36, 37, NW:
3 “Mnahitaji uvumilivu, kusudi, mkiisha kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi. Kwa maana bado ‘kitambo kidogo sana,’ na ‘yeye anayekuja atafika wala hatakawia.’”
4. Mungu ataonyeshaje ukweli wa ahadi yake ya kuletea waabudu wake faraja ya wakati unaofaa?
4 Kulingana na maneno hayo yaliyotajwa na mtume Paulo kutoka Habakuki 2:3 na Hagai 2:6, Yehova ndiye “anayekuja” ambaye “atafika wala hatakawia.” Kwa kuwa ni Shujaa asiyeshindika, atashinda wote wale wanaofanya vita juu ya waabudu wake ambao wamesumbuliwa muda mrefu. Ataonyesha ukweli wa ahadi yake ya kuletea waabudu wake wanaotaabika faraja ya milele, kwa ushindi wake mtukufu katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni.
5. Kwa sababu gani Shetani na jeshi lake la mashetani wanalazimika sasa kutumia mawakili wa kidunia wenye kuonekana, naye “mnyama,” Mamlaka ya Ulimwengu ya Saba, na “sanamu” ya mnyama ni nini?
5 Joka, Shetani Ibilisi, na jeshi lake la mashetani wamezuiwa wasivae miili yenye kuonekana wakikusudia kufanya vita juu ya mashahidi Wakristo wa Yehova wa leo. Kwa hiyo, wanalazimika kutumia mawakili wa kidunia, walimwengu, matengenezo ya kilimwengu na serikali za kisiasa wanazoziongoza bila kuonekana. Wanasiasa wanaofanya vita hiyo ndio waliomo katika taratibu ya ulimwenguni pote ya kisiasa ambayo Ufunuo 13:1-10 wafananisha na “mnyama” mkali. Hiyo yatia ndani Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika, Mamlaka ya Saba ya Ulimwengu inayotajwa katika unabii wa Biblia. Kwa utimizo wa unabii wa Biblia, Mamlaka hii ya Saba ya Ulimwengu ilisaidia kuunda “sanamu” ya ibada ya “mnyama” wa kisiasa. (Ufu. 13:11-15) Kwa zaidi ya miaka 56 sasa, “sanamu” hiyo imevuta ulimwengu. “Sanamu” ndilo tengenezo la mataifa yote la amani na usalama wa ulimwengu, lililoundwa kwanza likiwa Ushirika wa Mataifa na sasa lajulikana kama Umoja wa Mataifa.
6. Ni “chapa” gani ya mfano ambayo wazalendo wenye kuabudu “mnyama” wanapata, nayo “chapa” hiyo ya hesabu yamaanisha nini?
6 Wazalendo wanaotetea enzi kuu za kitaifa na tawala za kisiasa za kibinadamu juu ya dunia wanaabudu “mnyama” huyo wa kisiasa. Wanatumainia pia “sanamu” ya “mnyama” huyo badala ya kutumaini utawala wa enzi kuu ya Yehova unaosimamiwa na Kristo. Wanaunga mkono mipango hiyo ya utawala wa ulimwengu kwa moyo wote kwa kutukuza taifa. Hiyo inafanya waipate “chapa” inayoonyesha wazi kwamba hawatumikii faida za ufalme wa Mungu, bali za wanadamu hao wenye kujisimamia wenyewe. Hawaoni aibu kuwa na uhusiano na hesabu yenye maana, 666, inayomtambulisha “mnyama” wa kisiasa. Katika Biblia sita ni hesabu inayotumiwa kumaanisha kutokamilika kwa kibinadamu, kupungukiwa kwa kibinadamu. Kwa hiyo, 600 kuongeza 60 kuongeza 6 kwaonyesha kutokamilika na kupungukiwa kwa kibinadamu kwa njia kubwa sana, hasa katika utawala wa kibinadamu juu ya dunia. Leo tunaweza kuona wazi zaidi kuliko zamani kwamba utawala wa kisiasa wa wanadamu umeshindwa ukaleta fadhaa, kwa sababu ya kutokamilika, kutofaa na kupotoka. Umeonekana kupungukiwa mbele za Mungu.—Ufu. 13:16-18.
7. Wazalendo wa kisiasa wanajaribu kulazimisha kila mtu mwingineo ajiunge nao kufanya nini, na hiyo inaleta jaribu la uaminifu kwa nani?
7 Wazalendo wenye kuabudu “mnyama” na “sanamu” yake wanavaa kwa kiburi “hesabu ya jina lake [666].” Wanakaza kila mtu mwingineo ajiunge nao kumwabudu “mnyama” na hivyo apate alama ya kuwa mali ya serikali ya kisiasa ya kibinadamu, si ya Mungu. Wanaleta mateso ya namna mbalimbali juu ya mashahidi Wakristo wa Yehova. Kwa sababu gani? Kwa sababu wanakataa kushiriki kuabudu vitu vya kuundwa na wanadamu. Hiyo inaleta jaribu kali la uaminifu kwa wote wanaounga mkono enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova na Uungu wake. Ndiyo sababu malaika aliyeonekana katika njozi ya mtume Yohana alisema: “Hapa ndipo penye subira [uvumilivu, NW] ya watakatifu, hao wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu.”—Ufu. 14:12.
8. Kwa hiyo sisi tuzishikao amri za Mungu na imani ya Yesu twafanya nini, na ingekuwaje kama tungepata “chapa” ya “mnyama”?
8 Sisi tushikao amri za Mungu twamtii kama Mtawala kuliko wanadamu, hata ikiwa tutateswa na watesi. Tunashikilia imani yetu kwamba Yesu ndiye Masihi au Kristo, nasi twamtangaza kuwa Mfalme mtiwa mafuta ambaye Yehova amemtawaza akamvika taji Majira ya Mataifa yalipokwisha mwaka wa 1914. Kwa sababu hiyo ya maana, twajiepusha tusishiriki katika siasa na mabishano makali ya “mnyama” na Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika, ambaye ndiye mteteaji wa “sanamu” ya “mnyama” tangu mwaka wa 1919, uliofuata vita. Tunajua tunaweza kupatwa na nini tukipata “chapa” ile, “yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake.” Kuipata kungemaanisha ‘kunywa katika mvinyo ya ghadhabu ya Mungu iliyotengenezwa, pasipo kuchanganywa na maji, katika kikombe cha hasira yake’ na ‘kuteswa kwa moto na kiberiti mbele ya malaika watakatifu, na mbele za Mwana-Kondoo [Yesu Kristo].’ Kufanya hivyo kungetuelekeza kwenye uharibifu wa milele, “mauti ya pili.” Tungetupwa katika ‘ziwa la mfano liwakalo moto na kiberiti.’ (Ufu. 14:9-11; 13:16, 17; 19:20; 21:8) Je! twataka tufanyiwe hilo? Aka!
9. (a) Hali ya sasa yatuhitaji tuwe na sifa gani? (b) Ni nini kinachotuchochea tuendelee kuwa waaminifu, na yatupasa tuwe na tumaini gani hakika juu ya Mungu?
9 Kwa kuwa sasa utukuzo mwingi mno wa taifa na ibada ya serikali za kisiasa imeenea ulimwenguni pote, wale “wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu” wanatakiwa wawe na uvumilivu. Lakini mapenzi ya Mungu kwetu sasa ni kwamba tutii amri zake na imani ya Yesu kwa uthabiti. Ni baada tu ya kufanya mapenzi ya Mungu katika njia hiyo tutakapopokea utimizo wa ahadi tuliyofanyiwa. Kwa kuwa sasa ni “kitambo kidogo sana” kilichobaki kabla “yeye anayekuja” hajafika bila kukawia, ungekuwa upumbavu tukiacha kuvumilia ili tujipatie faraja ya muda kabla Yehova hajafika kutulipia kisasi juu ya wale wanaotutatiza sana tunapofanya mapenzi Yake kwa uaminifu mpaka mwisho. Lakini ahadi ya Mungu inatuchochea tuendelee kufanya mapenzi ya Mungu kwa sababu tunampenda. Tumeonyeshwa kitu tulichoahidiwa, lakini twahitaji kuonyesha imani yenye nguvu juu ya Mtoa ahadi, kuamini kwamba ni mwaminifu kabisa kwa ahadi yake na vilevile aweza kututimizia ahadi hiyo.
KUPATA UZIMA WA MILELE KWA IMANI
10. (a) Kwa sababu gani Mungu anapendezwa kutupa thawabu ya kumwamini? (b) Tofauti na nafsi yenye kufura kwa kujitumainia, ni sifa gani itakayowezesha mwenye haki wa Mungu aishi?
10 Je! sisi tuna imani hiyo? Tunaihitaji itutie nguvu tuvumilie mpaka ahadi ya Mungu itakapotimizwa. Tukiwa na imani hiyo twamheshimu Mungu, kwa maana yaonyesha twamtumaini tukimheshimu kwamba ni mwaminifu kwa ahadi yake. Kwa hiyo tunapomwamini Mungu tunampendeza. Yeye anafurahi kuthawabisha wenye imani hiyo yenye kudumu. (Ebr. 11:6) Mtume Paulo anataja maneno zaidi ya Mungu katika unabii wa Habakuki anapotukumbusha jinsi imani ilivyo ya lazima ili tuweze kuendeleza ukamilifu wetu na kuonyesha twastahili kupata uzima wa milele katika taratibu mpya yenye haki iliyoahidiwa. Katika unabii huo Mungu kwanza ataja mtu mwenye kufura kwa kiburi, kujifikiria makuu na kujitumainia, asimwamini Yehova. Yeye si nafsi nyofu kwa Mungu mmoja wa kweli aliye hai. Baada ya kuona nafsi ya namna hiyo, Yehova anena maneno yaliyotajwa na Paulo: “Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani.” (Ebr. 10:38; Hab. 2:4) Imani hiyo inavuta “mwenye haki” awe mwaminifu, mnyofu.
11, 12. (a) Ili tupate uzima wa milele ulioahidiwa, yatupasa tuonyeshe imani kadiri gani? (b) Baada ya Paulo kusimulia kifupi matendo hodari ya imani yaliyofanywa na watu wa zamani, anatuonyesha mfano gani ulio bora kupita yote?
11 Bila shaka, katika 2 Wakorintho 5:7 Paulo asema: “Twaenenda kwa imani, si kwa kuona.” Hiyo yamaanisha kwamba twaishi tukimwamini Mungu. Lakini, ili tuvumilie na kupata uzima wa milele kwa kutimiziwa ahadi ya Mungu, lazima tuonyeshe imani mpaka mwisho wa maisha yetu katika taratibu hii mbovu ya mambo, ambayo Shetani Ibilisi ndiye mtawala wake. (1 Yohana 2:25; Yohana 12:31) yatupasa tuonyeshe imani ya kadiri ile ile iliyoonyeshwa na “wazee wetu.” Walihakikisha imani yao mpaka kufa kwenyewe, ingawa hawakutimiziwa waliloahidiwa. Matendo yao hodari ya imani ambayo ni mfano kwetu yanaelezwa kifupi na mtume Paulo katika sura inayofuata ya barua yake, Waebrania sura ya kumi na moja. Baada ya kusimulia wanaume na wanawake wengi sana wenye imani walioshuhudiwa vizuri na Mungu, Paulo atuonyesha mfano bora zaidi wa imani, akisema:
12 “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu.”—Ebr. 12:1-3.
13. Katika hiki “kitambo kidogo sana” kinachokwisha, kwa sababu gani yatupasa sisi hasa tumtazame sana Mfano wetu bora, na yatupasa tukumbuke onyo gani la Paulo katika Waebrania 10:38?
13 Sasa hasa yatufaa tumtazame sana Mfano wetu Mkamilifu, Yesu Kristo, maana kufikia hapo, zaidi ya kuketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu, amekwisha tawazwa akawa Mfalme wa Kimasihi. Hata katika hiki “kitambo kidogo sana” kinachopita haraka, ambapo Yehova hajafika akiwa Mlipiza Kisasi, yawezekana tukapoteza imani, kutenda dhambi inayotuzinga kwa wepesi. Karne kumi na tisa zilizopita Paulo alitumia wakati kuonya Waebrania waliogeuzwa kuwa Wakristo juu ya hatari hiyo, kwa kutumia maneno zaidi ya unabii wa Habakuki, akisema: “Naye akisita-sita [akirudi nyuma, NW], roho yangu haina furaha naye.”—Ebr. 10:38.
14. Habakuki 2:4 inafuata mpango gani inapotofautisha watu wawili mbalimbali, lakini Paulo anabadilije mpango huo katika Waebrania 10:38?
14 Kulingana na tafsiri ya Kigiriki cha zamani, katika unabii wa Habakuki, Yehova asema: “Mtu ye yote akirudi nyuma, nafsi Yangu haina raha katika yeye. Lakini mwenye haki ataishi kwa kuniamini Mimi.” (Hab. 2:4, tafsiri ya Thomson) Mtu anayekosa imani na kurudi nyuma achukiwa na Yehova. Anatofautishwa na Mkristo anayeendelea tu kumwamini Yehova na kupata uzima wa milele. Paulo anabadili mpango wa sehemu zile mbili za Habakuki 2:4 anapotaja maneno yaliyomo. Anatanguliza ile sehemu ya kwanza.
15. Hivyo Paulo atupa onyo gani, nalo linafaa sana kwa sababu ya jaribu gani linalokaribia mbele yetu?
15 Paulo anafanya hivyo ili kutuonya sisi tulio na imani ya Kikristo, maana hata sasa kuna hatari ya kwamba wengine kati yetu huenda tukarudi nyuma na kuanguka. “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (l Kor. 10:12) Kadiri ulimwengu unaoongozwa na Shetani uzidiyyo kutawala kwa nguvu, ndivyo mkazo unavyozidi kutupata. Tuonapo jaribu kubwa sana la mwisho la uaminifu wetu likikaribia mbele yetu katika “dhiki kubwa,” huenda tukaamua kuliepuka. Huenda tukakosa kumwamini na kumtumaini Mungu. Kwa hiyo twarudi nyuma. Twaacha kuvumilia majaribu.
16. Mtu asiyemwamini Mungu anatendaje kwa harara?
16 Kwa kufaa. sana tafsiri Vulgate ya Kirumi yasema ifuatavyo katika Habakuki 2:4: “Tazama, yeye asiyeamini, nafsi yake haitakuwa haki ndani yake mwenyewe: lakini mwenye haki ataishi katika imani yake.” (Douay English Version) The New American Bible ya Kikatoliki yaonyesha kwamba Mkristo ni ‘mwenye harara’ kuacha imani yake kwa sababu ya magumu yanayoongezeka anayoona yakiwa pale pale mbele yake, hata anavunja ukamilifu wake kwa Mungu. Yasema hivi: “Mtu mwenye harara hana ukamilifu; lakini mtu mwenye haki, kwa sababu ya imani yake, ataishi.”
17. Twaweza kusema nini juu ya kama mtu anayeendelea kusonga mbele kwa imani akielekea “dhiki kubwa” ni ‘mwenye harara’?
17 Mkristo anayeendelea kusonga mbele akiwa na imani kuelekea “dhiki kubwa” si ‘mwenye harara’ anapofanya hivyo. Mtu mwenye harara kweli kweli, mwenye kufura kwa kujitumainia mwenyewe, ndiye yule anayekosa kumwamini Mungu Mwenye Nguvu Zote na kuacha kusonga mbele. Huyo anaacha akiwa amekaribia sana kupata thawabu, utimizo wa ahadi ya Mungu kwa waaminifu. Yehova Mungu hana furaha na wenye kuacha.
18. Katika Waebrania 10:39, mtume Paulo anaambia jamii yenye uaminifu ifuate mwendo gani?
18 Kwa kuwa huu ndio wakati wenye misukosuko zaidi katika historia yote ya watu wa Yehova waliojitoa, tutafanya nini? Yatupasa tukaze nia kufanya nini? Tusiwe waoga kamwe na kurudi nyuma! Kwa fadhili zisizostahilika za Mungu, mwendo unaofaa tuufuate unaonyeshwa na mtume Paulo asemapo yafuatayo kwa niaba ya jamaa yenye uaminifu “Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa [nafsi ] zetu.”—Ebr. 10:39.
19. Ikiwa tunasema hatutaki kurudi nyuma, tutafanya nini kuhusu mikutano na “uhuru wa kusema”?
19 Huu ndio wakati wetu wa kuamua. Je! tutamwamini Mungu bila kuyumba-yumba na kukubaliana na mtume Paulo kwa kukata maneno hivi: “Sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea”? Tukisema hatumo kati ya Wakristo hao wasioamini, hatutaacha “kukusanyika pamoja,” kama ilivyo desturi ya wasioamini na kurudi nyuma, bali, tutakusanyika pamoja hata mapangoni, ikiwa lazima, ili tutiane moyo, “na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” Haitupasi kutupa uhuru wetu wa kusema, “kwa maana una thawabu kuu,” bali tutaendelea kwa ujasiri kutangaza kwamba serikali.ya kitheokrasi ya Yehova inayosimamiwa wa Kristo ndiyo tumaini moja tu la wanadamu wote.—Ebr. 10:25-35; Mt. 24:14; Marko 13:10.
20. Ikiwa twataka uzima wa milele, tunajitangaza kwamba twapendelea mwendo gani wenye kujenga?
20 Sisi hatutaki uharibifu, bali uzima wa milele, sivyo? Kwa hiyo, badala ya kunena mambo yasiyojenga, twanena yanayojenga tukisema: “Sisi . . . tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa [nafsi] zetu. Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana. Maana kwa hiyo wazee wetu [kutia na Ibrahimu] walishuhudiwa.”—Ebr. 10:39 mpaka 12:2.
21. Kuamini ahadi ya Mungu kwatupa nguvu za kufanya nini, nasi tunakuwa na taraja gani?
21 Tunapoamini ahadi ya Mungu, asiyeweza kusema uongo, tunapata nguvu za kuvumilia. Imani na uvumilivu zinakwenda pamoja, kwa maana imeandikwa katika Ufunuo 13:10: “Hapa ndipo penye subira [uvumilivu, NW] na imani ya watakatifu.” Mpaka sasa huenda tukawa tumevumilia muda mrefu tukingojea ahadi ya Mungu itimizwe, lakini taraja letu ni imara, lenye uhakikisho, taraja linalofanya tufikie hatua ya kusadiki kabisa Mungu hatatukatisha tamaa.
22. Twaamini nini juu ya mambo yasiyoonekana yaliyoahidiwa na Mungu, naye atatupa thawabu gani tufurahie utimizo wa ahadi?
22 Pengine hatujayaona bado mambo yaliyoahidiwa na Mungu, lakini twajua ni ya kweli maana yameonyeshwa na uwezo wa Mungu Mwenye Nguvu Zote. Lazima turithi uzima ili tuweze kuingia katika utimizo wa ahadi ya Mungu; yatupasa tuhifadhiwe hai nafsi zetu. Njia ya pekee tunavyoweza kupata zawadi hiyo ya uzima ni kuwa na imani isiyokwisha. Tunataka sana tuje kufurahi milele baada ya Mungu kutimiza ahadi yake. Basi, na lipotelee mbali wazo au elekeo lo lote la kurudi nyuma kwa hofu na kutoamini! Sisi tutaonyesha imani yenye kuhakikishwa kwa matendo! Naye Yehova Mungu Mpaji wa Uzima atatupa thawabu kwa kuhifadhi nafsi zetu hai milele.—1 Yohana 2:25.
23. Mungu atatimizaje ahadi yake kwa wanaoendelea kutenda mapenzi yake kwa uaminifu?
23 Kwa hiyo, pasipo kushindwa, “Mungu apaye uvumilivu” atatimiza ahadi yake kwa wenye kuvumilia kwa uaminifu wakitenda mapenzi yake. (Rum. 15:5, NW) Atatupa kwa furaha baraka na mapendeleo ya milele ya ufalme wake ulioahidiwa tangu zamani, utakaoongozwa na Mwanawe Yesu Kristo. Hivyo, hatutakuwa tumehubiri bure ufalme huo “katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote” kabla ya “mwisho” kuja.—Mt. 24:14, NW.
—Kutoka The Watchtower, Dec. 15, 1976.
[Picha katika ukurasa wa 234]
Watakaoendelea kuonyesha imani ndio watakaookoka mwisho wa taratibu hii peke yao, na kupata uzima wa milele kama Mungu alivyoahidi