“Mpendane Ninyi kwa Ninyi”
KWA MSOMAJI
Labda utafurahia kusoma sura ya 12 ya Warumi kabla ya kuchunguza habari hizi.
LISA alikuwa msichana mwasi sana—akawa akitembea-tembea na watu wabaya na kutumia dawa za kulevya. Aliiba dawa za kutuliza maumivu za baba yake asiyeamini na kuandikia rafiki zake barua za kumdharau mama yake Mkristo aliyejaribu kumsahihisha.
Mwishowe, mama ya Lisa aliwaomba wazee wa kundi lao la Mashahidi wa Yehova wakutane na msichana wake. Lisa alionaje? “Mimi nilidhani wangenionyesha ubaya wangu tu. Baba, asiyependezwa na Biblia, aliniambia niende tu nikakutane nao kisha niwaambie waache kunifuata-fuata!”
Ikawaje? Lisa aeleza hivi: “Badala ya kunifanyia ukali, walinionyesha upole mwingi. Acha nishangae! Waliniambia mama alinishauri mara nyingi kwa sababu alinipenda. Hawakusema mambo niliyodhani wangesema. Walinihurumia sana kuhusu mambo hayo.
Niliacha mashirika yangu na kubadili tabia yangu kwa sababu ya upendo nilioonyeshwa na wazee.”
Ni wazi kwamba wazee hao walimsadikisha msichana huyo kwamba walimpenda. Walifuata ‘roho’ ya shauri la Paulo katika Warumi sura ya 12: “Pendo na lisiwe na unafiki; . . . Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi.”—Mistari 9 na 10.
Lakini sisi pia tunawezaje kuonyesha roho hiyo ya fadhili na upendo? Biblia inatuhimiza tufanye hivyo kadiri gani? Hayo ni maulizo ya maana sana, kwa sababu Yesu alisema kwamba alama yenye kutambulisha wanafunzi wake wa kweli ingekuwa kupendana kwao.—Yohana 13:34, 35.
‘KUPENDANA’ NI NINI?
Ni jambo la maana kujua kwamba ‘kupendana’ ambako Paulo alihimiza waamini wenzake wawe nako katika Warumi 12:10 si uungwana wa kijuu-juu tu. Neno la Kigiriki philóstorgos lililotafsiriwa hapo kama ‘kupendana’ lina maana ya urafiki wenye uchangamfu mwingi sana. Wanafunzi wa Biblia wanasema kwamba ni namna ya upendo unaoonyeshwa mara kwa mara kati ya watoto na wazazi. Je! hilo halipatani na maneno ya Yesu kwamba Wakristo wa kweli wangepata ‘ndugu waume, ndugu wake, mama, na watoto’ ndani ya kundi?—Marko 10:29, 30.
Vilevile, Yesu alituwekea mfano mwema. Yeye aliiga kwa ukamili sifa za Baba yake, Yehova, ambaye ni “mwingi wa rehema, mwenye huruma.” (Yak. 5:11) Mtume Paulo, aliyemwiga Yesu Kristo, alionyesha upendo huo alipokuwa akishughulika na waamini wenzake. Katika 1 Wathesalonike 2:7 anasema kwamba ‘alikuwa mpole’ kwao kama vile mama “mlezi” atunzavyo watoto wake, na kweli huo ni mfano wa upole. Inaonekana jambo hilo liliwafanya wampende Paulo. Wakati wazee wa Efeso walipokuwa wakimwaga mara ya mwisho, walilia “wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu.” (Matendo 20:17, 36, 37) Hawakumwaga kama vile askari wanavyoweza kumwaga jemadari mkali anayewakagua. Walimwaga kama vile watu wa ‘jamaa’ moja wanavyoagana; walikuwa ndugu.—Mt. 23:8.
Wanaume na wanawake wengi Wakristo wanajua kwamba ili maneno “ndugu” na “dada” wanayotumia yawe na maana, inawapasa wajitahidi kuongeza upendo wanaoonyesha waamini wenzao. Wanafahamu kwamba ili ‘pendo liwe bila unafiki,’ lazima upendo uongezeke kikweli. Lakini huenda wengine wakauliza, hilo linawezekanaje? Tunawezaje kuongeza upendano wa kidugu?
“VIUNGO, KILA MMOJA KWA MWENZAKE”
Mapema katika Warumi sura ya 12 mtume anaeleza kwamba washiriki wa kundi la Kikristo ni mali ya mtu na mwenzake. Wanategemeana—wanahitajiana. (Mstari 5) Halafu anahakikisha hilo kwa kutaja karama mbalimbali ambazo ndugu mbalimbali wamepewa katika kundi, kwa maana “viungo vyote havitendi kazi moja.” Zote zikijumlishwa, kundi linakuwa chombo kamili ambacho Yehova anaweza kutumia kuendesha kazi yake duniani.—Mistari 4, 6-8.
Huenda ukauliza ni jinsi gani mambo hayo yanahusu kupendana kwetu? Tusipofahamu jinsi tunavyohitajiana labda tutashindwa kukuza sifa za moyoni ambazo Paulo anatusihi tuwe nazo. Lakini, tukiufahamu uhitaji uliopo, wa kusaidiana na kufanya mapenzi ya Yehova, tunaongozwa tupendane. Tunaongozwa tuwathamini ndugu zetu na kujisikia kwamba sisi ni jamaa moja.
Lakini yako mambo yanayotuzuia tusijisikie kwamba tunategemeana na tuna udugu. Paulo anakataza sana mawili kati ya mambo hayo—majisifu na kiburi: “Namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia.” (Mstari 3) Tafsiri ya Phillip inasema hivi katika mstari wa 16: “Msiwe vipenda-wakuu bali pendezweni kihalisi na watu wa vivi hivi.”
Kupenda watu wakubwa peke yao ni namna ya kiburi, ni kujitakia ukuu. Kufanya hivyo kunabagua vyeo vya watu, kupendelea watu kulingana na vyeo walivyo navyo, kudharau wasio na elimu nyingi. Mambo hayo yote yanazuia mtu asiwe na maoni ya kimungu ya kuwahitaji ndugu zake na kuwatunza. Kwa kweli, wakati magumu makubwa au mateso yatakapotokea, utasaidiwa na nani? Je! hutasaidiwa na wanaompenda Mungu na Kristo kikweli, bila kujali wana vyeo gani?
Lakini zaidi ya kuwa vipenda-wakuu peke yao, au kupendelea watu, tunawezaje kupendana kikweli?
‘KATIKA KUONYESHA HESHIMA, WEKENI MFANO’
Paulo alitoa uongozi mwingine wenye maana, mara tu baada ya kututia moyo tupendane, akaandika hivi: “Katika kuonyeshana heshima wekeni mfano.” (Mstari 10, NW [Kiingereza]) Sio wazee peke yao walioandikiwa amri hiyo, kwa maana Paulo aliandika barua yake “kwa wote walioko Rumi, wapendwao na Mungu.” (Rum. 1:7) Kwa hiyo wote wanapaswa kuheshimiwa, nao wanapaswa kuheshimu wengine.
Tunaheshimu ndugu yetu kwa kumstahi sana bila kumchukua vivi hivi tu. Akisema jambo ambalo ni la maana kwake, hatutamsikiliza ili tuwe waungwana tu kisha tuyapuze maoni yake, bali tutayafikiria kwa unyofu anayoyasema.
Vivyo hivyo, dada kundini wanapaswa waheshimiwe. Hiyo ni tofauti kabisa na maoni ya walimwengu leo ambao kawaida yao ni kutawala wanawake kwa kutumia nguvu za mwili na kufanya madai. Ndugu Mkristo anafahamu kwamba anaweza kuwa mwanamume na bado awe mpole, anaweza kuweka mfano wa kuwa imara lakini awe mpole pia.—1 Pet. 3:7.
Kanuni ya kuonyesha heshima inahusu watoto pia. Kwa mfano, katika Jumba la Ufalme, je! watoto wanachukuliwa kuwa Wakristo vijana au wanaonekana kuwa ‘migogoro’ inayosumbua watu?
Mwangalizi mmoja mwenye kusafiri alikuwa ametembelea kundi moja la mashambani akamwona kivulana wa miaka minane ambaye hakuwa na Biblia lakini akasikiliza sana hotuba yake. Baada ya mkutano, mwangalizi alikwenda kuongea na kijana huyo wa jamaa iliyoanza kupendezwa karibuni. Alimwambia kijana amfuate nje, akachukua Biblia nyuma ya gari lake na kumpa kama zawadi. Kivulana alishangazwa sana, si na zawadi hiyo tu, bali na jinsi mwangalizi alivyotaka ajifunze na kufanya maendeleo.
Baada ya miaka 20, kivulana huyo ambaye sasa ni mzee, ametumia Biblia nyingi hata zikawa kuukuu, lakini hajasahau upendo alioonyeshwa na mwangalizi huyo. Tunapopendezwa na watu wa umri wote na kuwaheshimu, upendo unaongezeka.
‘MKAE KATIKA AMANI NA WATU WOTE’
Lakini, ili kuendelea kuonyesha upendo, ni jambo la maana tuwe na sifa nyingine ambayo Paulo alikazia katika Warumi sura ya 12, yaani, sifa ya kutafuta amani. Kwa kuwa mtume anamwagiza Mkristo ‘akae katika amani na watu wote,’ inampasa hata zaidi ajitahidi kuendeleza amani na ndugu zake. (Mstari 18) Huenda mtu akaudhiwa sana na ndugu yake katika jambo fulani, labda linalohusu porojo au kutotegemeka katika biashara. Hata baada ya kuwaona wakitugu aliwasamehe, cha kumpenda na kusema “Siwezi kamwe kumwamini tena.”
“Kamwe” ni neno kali. Sote tunaweza kufurahi sana kwamba Yesu hakuwakasirikia wanafunzi wake waliomwacha akiwa hatarini kabisa na kusema: “Siwezi kamwe kuwaamini watu hao tena!” Bali, baada ya kuwaona wakitubu aliwasamehe, akawapenda hata akawaheshimu. (Yohana 20:19-23; Matendo 2:4, 14) Tunapofikiria huruma ya Yesu, je! haitupasi kuwa na nia ya kusamehe wenzetu na kuwaamini?
Lakini hata tunapojisikia tukitaka kuonyesha upendo, tunawezaje kuonyesha upendo unaohitajiwa hasa katika hali fulani?
JINSI YA KUJUA KITU CHA KUTOA
Huenda tukataka kusaidia ndugu yetu kwa sababu tunapendezwa sana kuona akiwa katika hali njema kiroho, lakini ni njia gani bora ya kufuata? Kwa sababu gani ndugu na dada wengine wanajua sana jinsi ya kuonyesha upendo? Bila shaka, wamejifunza jinsi ya kutumia shauri la Paulo katika Warumi 12:15: “Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao.”
Ni sifa gani inayoelezwa hapa? Ni sifa ya kujitia katika hali za wengine. Maana yake si kuhurumia wengine tu. Bali, inahusu pia kujisikia vile wanavyojisikia. Mtu anapoona maumivu nasi tunayaona pia, au anapoona wasiwasi au furaha nasi tunakuwa ivyo hivyo, tunakuwa katika hali bora ya kujua uhitaji wake wakati huo. Tena, sisi pia tunaweza kumweleza tunavyojisikia.
Kwa mfano, tuseme ndugu mwenye jamaa kubwa amefutwa kazi. Bila shaka maneno ya kuonyesha huruma si mabaya. Lakini mtu mwenye huruma hatasema maneno ya huruma tu, bali atachukua hatua halisi. Je! kazini kwake kuna nafasi ya kazi? Je! jamaa ya ndugu huyo mwingine inahitaji kupelekwa kwa gari kwenye mikutano ya Kikristo? Hivyo, kuhurumia sana wengine kwa kujitia katika hali zao kunaleta upendano.—1 Yohana 3:18.
Kwa hiyo, tunaporudia kuangalia sifa nzuri ambazo Paulo anaeleza katika Warumi sura ya 12, hatuoni amri ya kupendana tu, bali pia tunaliona kusudi la kufanya hivyo na tunasaidika tuongeze upendo kikweli. Tunapoyafikiria sana mambo haya—
kufahamu kwamba tunategemeana,
kuonyeshana heshima,
kuendeleza amani na watu wote,
kuzidi kujitia katika hali za wengine na kuchukua hatua inayofaa—
je! hayatutii moyo tuwe na upendano wa kidugu na kuhurumiana? Bila shaka, kanuni izo hizo zinaweza kukuza upendo kati ya watu wote, kati ya wenzi wa ndoa, wazazi na watoto, au wengineo.
Tena, ni hakika kwamba upendo huo unaweza kubadili maisha ya watu, na kuleta jamii yenye hali tofauti. Hilo limeonyeshwa katika Neno la Mungu na linaonekana kutokana na yanayotukia sasa hivi katika Majumba ya Ufalme duniani pote. ‘Jamaa’ ya mataifa yote ya Mashahidi wa
Yehova inakutia moyo uchunguze kina cha udugu wao. Wakati huu ambao watu wanakosa kupenda watu wa kwao, upendano wa Wakristo wa kweli unang’aa kama taa yenye mwangaza mwingi, nao unahakikisha kwamba Baba yetu aliye Mmoja ni mwenye hekima na upendo.