Wewe Unampenda Yehova kwa Shauku?
UPENDO una “nyuso” nyingi. Kijana mwanamume mwenye shauku nyingi huenda akawa anapenda msichana fulani. Kuna ule upendo wa mama kwa mtoto wake. Na kuna ule upendo unaounganisha Wakristo pamoja katika udugu wenye kuzunguka dunia nzima.
Wote huo ni “upendo,” lakini Wagiriki wana maneno mbali mbali ya kutaja namna hizo tofauti-tofauti za upendo. Éros ni upendo unaoshirikishwa na mahaba Storgé ni upendo unaotegemea uhusiano wa damu. Na agápe, yaani, upendo usio wa kichoyo unaotegemea kanuni, ndio upendo ambao Wakristo wa kweli duniani pote wanao kati ya wao kwa wao.—Yohana 13:34, 35.
Upendo Mwororo Wenye Shauku
Lakini, wakati walipotaka kukazia upendo kwa njia yenye uchangamshi na shauku nyingi, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walilitumia neno philia. Neno hilo lina maana ya ushikamano wa kibinafsi ulio thabiti, wenye uchangamfu, kama ule unaokuwa kati ya rafiki za kweli. Yehova ana upendo huo wa pekee wenye shauku kwa Mwana wake aliye mzaliwa pekee. Hivyo Yesu alisema hivi juu yake mwenyewe: “Mwana hawezi kufanya jambo hata moja la kujianzia yeye mwenyewe, ila lile tu analoona Baba akifanya. Kwa maana mambo yo yote ambayo Huyo anafanya, mambo hayo Mwana pia anafanya katika namna iyo hiyo. Kwa maana Baba ana upendo wenye shauku kwa Mwana na anamwonyesha mambo yote ambayo yeye mwenyewe anafanya.” Na, vivyo hivyo, Yesu alisema hivi juu ya wafuasi wake wa kweli: “Baba mwenyewe ana upendo wenye shauku kwenu ninyi, kwa sababu ninyi mmekuwa na upendo wenye shauku kwangu mimi na mmeamini kwamba mimi nilitokea nikiwa mwakilishi wa Baba.”—Yohana 5:19, 20; 16:27, NW.
Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, “upendo wenye shauku” unamaanisha namna ya upendo wenye uchangamfu na wa kibinafsi. Jambo hilo linaonekana wazi kutokana na uhakika wa kwamba mara nyingi wakati neno hilo linapotafsiriwa linaambatanishwa na neno “-ororo.” Kwa mfano, mtume Paulo anawapa Wakristo onyo hili la upole: “Katika upendo wa kidugu iweni na upendo mwororo wenye shauku kwa mmoja na mwenzake.” (Warumi 12:10, NW) Tena, mwanafunzi Yakobo anautaja uvumilivu wa Ayubu na matokeo ambayo Yehova alitokeza kuthibitisha “kwamba Yehova ni mwororo sana katika upendo wenye shauku na ni mwenye rehema.”—Yakobo 5:11, NW.
Je! Inawezekana Kuwa na Upendo Wenye Shauku kwa Yehova?
Kwa hiyo Yehova anaweza kuwa na upendo mwororo wenye shauku kwa wanadamu washika-ukamilifu, wajapokuwa ni watu wasiokamilika. Lakini kwa kuwa upendo wenye shauku unamaanisha kupenda mtu kwa ukaribu na kwa uchangamfu, je! inawezekana wanadamu wasiokamilika wawe na upendo wenye shauku kwa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, Yehova?
Ndivyo, inawezekana. Mfano wa kutokeza wa mtu aliyekuwa na upendo wenye shauku na uchangamfu kwa Yehova ni Daudi. Hilo linaweza kuonekana kutokana na zaburi zake nyingi. Yeye aliuthamini sana uangalizi wenye upendo ambao Yehova aliuonyesha kama Mchungaji.—Zaburi 18:1; 23:1-6.
Yehova anaweza kuwa karibu sana, halisi sana, kwetu sisi hivi kwamba tunaweza kumwonyesha yeye upendo wa kibinafsi wenye shauku. Kwa kweli, amri ya kwanza iliyo kubwa zaidi ya zote inaonyesha wazi kwamba inatupasa tuwe na upendo huo wenye shauku, wa ukaribu na uchangamfu kwa Mfanyi wetu. Kulingana na amri hiyo, inatupasa sisi ‘tumpende Yehova kwa moyo wetu wote, kwa nafsi yetu yote, kwa akili zetu zote na kwa nguvu zetu zote.’—Marko 12:29, 30, NW.
Kusitawisha Upendo Wenye Shauku na Uchangamfu kwa Yehova
Basi, tunaweza kusitawishaje upendo huo wenye shauku na uchangamfu kwa Yehova? Ni kwa kukuza hali ya kuthamini inayozidi kuongezeka nyakati zote juu ya namna yeye alivyo Baba wa kimbingu mwenye upendo na shauku. Tunaweza kufanya hivyo kwa kutumia wakati tusome Neno lake, Biblia, kwa ukawaida. Hasa tunaweza kupata faida zaidi kwa kusoma visehemu kama Zaburi, zile Gospeli (Injili) na barua za mitume.
Msaada mwingine mkubwa katika kusitawisha upendo wenye shauku na uchangamfu kwa Yehova ni kuikuza roho ya kuthamini na kushukuru kwa ajili ya baraka nyingi anazoleta. Vifikirie vitu vyote vizuri kuwa vinakuja kutoka kwake, kwa maana, kwa kweli, “kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga.” Maonyo ya upole yanayotolewa na Maandiko ili Mungu apigiwe asante ni mengi sana, na hasa yanapatikana katika kitabu cha Zaburi na katika barua za Paulo. Mfano mzuri sana wa maonyo hayo ni maneno haya ya mtume: “Katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo [toeni] shukrani sikuzote kwa Mungu na Baba yetu kwa ajili ya vitu vyote.”—Yakobo 1:17, UV; Waefeso 5:20, NW.
Inayotusaidia pia tukuze upendo wetu wenye shauku kwa Yehova Mungu ni sala—maombi na dua zenye kutoka katika moyo mweupe na za unyenyekevu ambazo tunapelekea Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo. Tunapokuwa katika sala tunakaa sana tukitaja sifa njema za Yehova, wema anaotufanyia na uhitaji wa tegemeo letu kwake. Na tunapokuwa katika sala tunamwomba sana pia asamehe dhambi zetu, kama Daudi alivyofanya katika Zaburi 51. Ni wazi kwamba kwa sababu ya kufanya hivyo tunamkaribia zaidi Yehova kisha tunapata nguvu za kumpenda kwa shauku.
Namna Kumpenda Yehova kwa Shauku Kunavyotusaidia Sisi
Tukisitawisha upendo huo wa kibinafsi wenye shauku na uchangamfu kwa Yehova Mungu, tumpende kweli kweli kwa moyo wetu wote, nafsi yote, akili zote na nguvu zote, ndipo itakuwaje? Kufanya hivyo kutatusaidia tutembee katika njia inayopendeza Mungu na pia kutatuepusha na maumivu mengi na uchungu wa moyoni. Inaelekea sana kuwa kwamba Wakristo wale wanaojikuta katika mashaka kwa kuvunja sheria za Mungu za uadilifu kwa uzito wanakuwa wameshindwa kusitawisha uhusiano huo wa kuwa na uchangamfu kumwelekea Baba wa kimbingu.
Kwa mfano, kulikuwa na Mkristo kijana ambaye hakuwa ameuzidi sana umri wa miaka kumi na tisa, aliyekuwa na pendeleo la utumishi wa wakati wote. Lakini yeye alianza kufuata “matendo ya mwili” bila kujali sana naye akalazimika kupewa adhabu. (Wagalatia 5:19-21) Wakati alipoonyeshwa kwa mkazo uzito wa kosa lake, alitubu kwa moyo mweupe. Hata hivyo yeye alikuwa amekosa kujali kile ambacho angalipaswa kukumbuka zaidi ya mambo yote, yaani, sifa mbaya ambayo mwendo wake wa kupotoka uliletea jina la Yehova. Kama kijana huyo wa kiume angalikuwa na uhusiano wa kibinafsi na wenye uchangamfu pamoja na Baba yake wa kimbingu, inaelekea sana kwamba uhusiano huo ungalikuwa kizuizi ili asifanye alilofanya.
Yesu alimwuliza Petro kama alikuwa na upendo wenye shauku kwa Bwana wake, si upendo wa kikawaida tu. Wakati Petro alipojibu kwamba alikuwa nao, Yesu alisema, “lisha kondoo zangu wadogo.” (Yohana 21:15-17, NW) Ndivyo ilivyo na kuwa kwetu na upendo wenye shauku kwa Yehova. Upendo huo wenye shauku utatusaidia tuhangaikie kumfurahisha Mungu kwa kushika amri zake. Utatufanya tuhangaikie kutokumwudhi yeye, kutokuumiza moyo wake. Kama vile mtume Paulo anavyotukumbusha, sisi tukirudi nyuma tusite kufanya mapenzi ya Yehova, Yeye hatakuwa na raha yo yote nasi. Kwa uhakika hatutaki tupatwe na jambo hilo, au tunataka? (Waebrania 10:38, 39) Ni jambo bora zaidi kuwa na imani na kumpenda kwa shauku na uchangamfu Mungu wetu mwenye upendo!
Basi, acheni tusitawishe hali ya kumpenda Yehova Mungu kwa shauku na uchangamfu. Tunaweza kufanya hivyo kwa kusoma Neno lake, kwa kufikiria wema wake tukiwa na roho ya kupiga asante, kwa kudumu katika sala na kwa kutafuta kumfurahisha yeye kwa mwenendo wetu na huduma yetu yenye juhudi katika kutangaza jina na ufalme wake.