Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● “Bwana” anayetajwa katika Warumi 10:12 ni nani, ni Bwana Yesu Kristo au ni Bwana Yehova?
Warumi 10:12 inasema hivi: “Kwa maana hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao.” Maneno yanayozunguka mstari huo hayaonyeshi kwa uhakika ni nani anayetajwa kuwa “Bwana.”
Karne zote zilizopita wanafunzi wa Biblia hawajafikia mapatano juu ya kama Paulo alikuwa akimtaja Bwana Yesu Kristo au Bwana Yehova. Yesu Kristo ndiye anayetajwa kuwa Bwana katika Warumi 10:9, na vilevile katika mtajo wa Isaya 28:16 unaopatikana katika Warumi 10:11, unaosema “kila amwaminiye hatatahayarika.” Kwa hiyo ikiwa Warumi 10:11 inapasa kuhusianishwa moja kwa moja na Bwana anayetajwa katika Warumi 10:12, Bwana anayetajwa ni Yesu Kristo.
Kwa upande mwingine, katika Warumi 10:9 Paulo anasema ‘uamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu.’ Hiyo inaonyesha kwamba kumwamini Yehova Mungu kunahitajiwa pia ili kupata wokovu. Tena, Warumi 10:13 (NW), ambao ni mtajo kutoka Yoeli 2:32, inasema: “Kwa maana ‘kila mtu anayeliita jina la Yehova ataokolewa.’ “Kwa hiyo, ikiwa kumwita Bwana anayetajwa katika Warumi 10:12 ni sawa na kumwita anayetajwa katika Warumi 10:13, Yehova Mungu ndiye Bwana anayetajwa na Paulo. Basi, hapo wazo hilo lingekuwa sawa na lile linalotajwa katika Warumi 3:29: “Je! Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu? Siye Mungu wa Mataifa pia? Naam, ni Mungu wa Mataifa pia.”