Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 7/15 kur. 321-325
  • Mshukuru Yehova kwa Ajili ya Fadhili Zake za Upendo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mshukuru Yehova kwa Ajili ya Fadhili Zake za Upendo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIFA YENYE THAMANI NYINGI
  • MUNGU MWENYE KUFADHILI WOTE
  • KWA WATU WAKE KAMA JAMII
  • Acha “Sheria ya Fadhili Zenye Upendo” Ilinde Ulimi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Kufaidika na Fadhili-upendo za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Utapigaje Asante kwa Ajili ya Fadhili Zake za Upendo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Fadhili
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 7/15 kur. 321-325

Mshukuru Yehova kwa Ajili ya Fadhili Zake za Upendo

“Ee watu na wampe Yehova shukrani kwa ajili ya fadhili zake za upendo na kazi zake za ajabu.”​—Zab. 107:8, NW.

1, 2. (a) Nyakati za huzuni, twahitaji sana kitu gani? (b) Mara nyingi ni nini hukosekana kwa habari hii katika ulimwengu wa leo? (2 Tim. 3:1, 2)

JINSI lilivyo jambo zuri kuwa na mtu wa kushikamana nawe nyakati za magumu! Bila shaka ziko nyakati ambazo umeingia katika hali zilizokushusha moyo au zikakutaabisha, pengine kwa sababu ya makosa au udhaifu wako mwenyewe. Jinsi ulivyoshukuru mtu fulani alipojitoa bila choyo akakusamehe kosa lako kwa fadhili na kuja kukusaidia akakuondolea huzuni.

2 Ni kama vile mithali ya Biblia isemavyo: “Mwenzi wa kweli anapenda wakati wote, naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya wakati ambapo kuna taabu.” (Mit. 17:17, NW) Jambo linalosikitisha ni kwamba, mifano hiyo ya kujitoa kuonyesha fadhili bila choyo haionekani sana leo. Nyakati nyingine mtu aweza kuudhiwa sana na watu wale wale aliodhani walikuwa rafikize. (Mit. 18:24) Kwa upande mwingine, wako watu wengi wasioshukuru wanapotendewa fadhili hizo za kujitolea. Waume wengi wenye wake wenye kujitoa sana hawawashukuru mara nyingi wanapowatendea kwa upendo, kwa sababu wanaona hiyo ndiyo kazi yao, na ndivyo pia wake wengi wanavyoona waume zao wenye kujitoa. Lakini lo! jinsi inavyofurahisha shukrani zinapotolewa kwa ajili ya fadhili hizo za kujitoa!

3. Mtunga zaburi aonyeshaje rafiki mkubwa zaidi tuwezaye kuwa naye?

3 Fadhili zote za upendo zinazoonyeshwa na wanadamu ni ndogo sana zikilinganishwa na zinazoonyeshwa na Yule ambaye urafiki wake wapaswa kutafutwa na kuthaminiwa zaidi ya mwingine wote. Mtunga zaburi alimwimbia Huyo akasema: “Enyi watu, mpigieni Yehova​—⁠asante, kwa maana yeye ni mwema: kwa maana fadhili zake za upendo ni za mpaka wakati usiojulikana.”​—Zab. 107:1, NW.

SIFA YENYE THAMANI NYINGI

4, 5. (a) Ni nini linalomaanishwa na maneno “fadhili za upendo”? (b) Ni kwa njia gani fadhili za upendo ni alama ya kuonyesha jinsi Yehova alivyo? (Zab. 86:15)

4 Ni nini ‘fadhili hizi za upendo’ za Yehova zinazotajwa katika Zaburi 107? Sifa hiyo yatia ndani kupendezwa sana na wengine. “Fadhili za upendo” ni maneno yanayotafsiri neno la Kiebrania hheʹsedh, ambalo lamaanisha fadhili au kufikiria mtu kwa sababu ya upendo. Lakini mengi zaidi yatiwa ndani. Mtaalamu R. E. Perry asema kwamba hheʹsedh “lamaanisha nia ya ama Mungu ama mwanadamu inayotokana na uhusiano wa wote wawili,” tena ‘ “lamaanisha ‘fadhili’ au ‘msaada’ unaopokewa kutoka kwa mkuu. . . . Wazo kuu la [hheʹsedh] ni ‘upendo mshikamanifu.’” Kwa hiyo ushikamanifu unahusika katika fadhili za upendo za Mungu. Hivyo Revised Standard Version yamtaja Sulemani akieleza kwamba Mungu “alionyesha Daudi baba yangu upendo mwingi na thabiti [au, “fadhili za upendo”].”​—2 Nya. 1:8; linganisha 2 Samweli 9:1-7.

5 Basi, Yehova haonyeshi fadhili za upendo mara kwa mara tu, kama vile mfalme kigeugeu wa kibinadamu anavyoweza kuonyesha mtu upendeleo. Bali, anazionyesha daima kwa ushikamanifu. Yehova aithamini sana sifa hiyo, anafurahia hasa kufadhili watu mmoja mmoja walio waaminifu. Yapaswa pia ithaminiwe sana na wale wanaoipokea. Ilifaa sana Daudi akaandika hivi: “Ee Mungu, jinsi zilivyo na thamani fadhili zako! Wanadamu huukimbilia uvuli wa mbawa zako.”​—Zab. 36:7

6. Kwa sababu gani yatupasa tujichunguze tuone tunavyoitikia fadhili za upendo za Yehova?

6 Kawaida ya vitu vilivyoumbwa ni kwamba, kila tendo lalingana na kitu kingine chenye uwezo wa kulizuia. Lakini, hiyo haionyeshi bila shaka ndivyo mambo ya kiroho yalivyo. Kila mmoja wetu aweza kuuliza: Mimi naitikiaje maonyesho ya Mungu ya fadhili za upendo? Huenda wengi wakaona ni vigumu kujibu ulizo hilo, kwa maana huenda “fadhili za upendo” zikaelekea kuwa kitu kisichoonekana wala kugusika. Hata hivyo, je! umepata kufikiria mifano halisi ya jinsi umefaidiwa na fadhili za upendo za Mungu? Ukiifikiria, waweza kushukuru zaidi kwa ajili ya fadhili hizi za upendo, kumkaribia zaidi Mungu.

MUNGU MWENYE KUFADHILI WOTE

7. Je! Mungu ameweka kikomo cha kufadhili wale walio naye katika uhusiano anaoukubali?

7 Ingawa Yehova huonyesha wale ambao wameingia naye katika uhusiano anaoukubali upendo mshikamanifu, hiyo haionyeshi bila shaka hafadhili wale wasiohusiana naye. Mwana wa Mungu alipokuwa duniani alisema: “Aliye juu ni mwema kwa wasiomshukuru. na waovu. Basi iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma.” (Luka 6:35, 36) Mtume Paulo alifaa kuambia waabudu sanamu katika Listra kwamba Mungu “hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.” (Matendo 14:17)Hizo zote ni fadhili za Mungu zisizostahilika, wonyesho wa rehema​—yake kuu kwa wanadamu wote.

8. (a) Kuumba kunatupaje sababu ya kumpigia Yehova asante? (Zab. 33:5) (b) Tuna sababu gani zenye nguvu zaidi?

8 Ni jambo jepesi kuviona tulivyo navyo kama vitu vya kikawaida tu. Jiulize hivi: Ungemwelezaje mtu aliyezaliwa kipofu rangi ya anga au uzuri wa ua? Ikiwa mtu alizaliwa kiziwi, je! ungeweza kumweleza jinsi mtu anavyojisikia anaposikia, anapoweza kuwasikia ndege, kuzungumza, kusikiliza muziki wenye kufurahisha? Ni baraka kweli kweli kuweza kuona na kusikia, na karibu sote twaweza. Lakini ni mara ngapi tunapompigia Mungu, Muumba, asante ya mambo hayo? (Mit. 20:12; Kut. 4:11) Hata hivyo ziko sababu zenye nguvu. Sababu hizo zapatikana katika kazi za ajabu zinazotuwezesha kuingia naye katika uhusiano anaoukubali. Licha ya kupata fadhili zake anazoonyesha wanadamu wote kwa ujumla, tukifanya hivyo aweza kutuonyesha upendo wake mshikamanifu, fadhili zake za upendo anazoonyesha “wanadamu” ambao wanamtumikia kwa shukrani.​—Zab. 107:8.

9. Hali ya Mataifa ilikuwa imekuwaje katika Efeso, na wengine wao wakawaje Wakristo?

9 Mtume Paulo aliandika kwamba wakati mmoja Wakristo wa Mataifa katika Efeso wa kale walikuwa ‘hawana Kristo wakiwa wamefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Walikuwa hawana tumaini, hawana Mungu duniani.’ (Efe. 2:11, 12) Kwa kuwa yalikuwa mapenzi ya Mungu Wayahudi na Mataifa pia wapate nafasi ya kumkubali Kristo, walipelekewa ujumbe wa upatanisho. (Efe. 2:16; Kol. 1:21, 22; 2 Kor. 5:18-21) Hiyo ilikuwa sababu kubwa ajabu ya kuwafanya wampigie Mungu asante kwa ajili ya rehema yake.

10. Vivyo hivyo, kwa sababu gani wewe unaweza kupiga asante kwa ajili ya fadhili za Mungu zisizostahilika?

10 Je! wewe hupaswi kufanya hivyo? Fikiria mamilioni ya watu duniani ambao bado wamepofushwa na mafundisho yenye makosa ya kidini. (2 Kor. 4:3, 4; Mt. 15:8, 9, 14) Ijapokuwa wewe pia huenda ukawa ulikuwa ‘huna tumaini, huna Mungu duniani,’ sasa waijua kweli ya Neno la Mungu na unaweza kumtumikia. Je! wewe humpigia Mungu asante kwa sababu amekuruhusu ujifunze kweli ukawa rafiki yake?

11. Yehova alionyeshaje Mataifa mmoja mmoja katika Efeso fadhili nyingi?

11 Na tuelekeze fikira zaidi juu ya watu mmoja mmoja. Wakati kweli ilipofikia Waefeso hao, pengine wengi wao walikuwa kama watu wa Korintho wa zamani. ‘waasherati, waabudu sanamu wazinzi, wanaume waliowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wevi, wenye pupa, walevi, watukanaji na wanyang’anyi.’ (1 Kor. 6:9-11, NW) Lakini wangeweza kurehemiwa kwa sababu Yehova alikuwa amemtuma Mwanawe atoe dhabihu kama msingi wa kusamehe watu dhambi. Hivyo Paulo alikumbusha Waefeso habari za “msamaha wa makosa yetu, kulingana na wingi wa fadhili zake zisizostahilika.” (Efe. 1:7, NW) Je! nia ya Mungu kuwasamehe dhambi zao haikuwa wonyesho mzuri sana wa fadhili zisizostahilika? Namna gani sisi?

12, 13. (a) Kila mmoja wetu ajua alitenda nini wakati uliopita, kama inavyoonyeshwa na Tito 3:3-5? (b) Basi, tuna sababu gani ya kipekee kumpigia Yehova asante?

12 Kila mmoja wetu ajua mambo aliyotenda wakati uliopita. Licha ya dhambi nyingi sana tusizokumbuka, inaelekea twajua dhambi nyingi tulizotenda tukahitaji msamaha. Twapaswa kuvutwa moyoni tuwaze hivi: Mungu ni mwenye nia ya kutusamehe kwa sababu ya upendo wake. Yaonyesha atufadhili kwa sababu tumeikubali dhabihu ya Kristo tukaonyesha imani. Wazia kama ungekuwa na suti mpya unayopenda sana, lakini uimwagie kitu mara ya kwanza kuivaa. Ungeipeleka upesi kwenye duka la kusafishia mavazi, ukitumaini kwamba doa hilo laweza kuondolewa. Kisha ungerudi kuichukua suti. Kumbe! Doa halipo tena! Je! usingefurahi, naam, usingepiga asante? Basi, je! tuoneje kwa vile ambavyo Yehova ametusamehe dhambi zilizotutia madoa wakati uliopita, akatuonyesha sana fadhili zake zisizostahilika?​—Zab. 103:3, 12-14; Hes. 14:19.

13 Bila shaka tuna sababu ya kumpigia Mungu asante na kumsifu kwa ajili ya fadhili hizo zisizostahilika. Lakini, kwa kuwa tumekuwa miongoni mwa watu wake, tukawa waabudu wake Wakristo, ziko njia nyingi ambazo ametuonyesha ushikamanifu, akaja kutusaidia kwa fadhili zake za ajabu za upendo.

KWA WATU WAKE KAMA JAMII

14. Ni kwa njia gani nyingine twaweza kufahamu sababu ambazo yatupasa kumpigia Yehova asante?

14 Waabudu wa Yehova wameona muda mrefu maonyesho ya upendo mshikamanifu wa Mungu katika shughuli zake nao. Kwa kuchunguza baadhi ya mifano ya Biblia ya maonyesho hayo, inaelekea utasaidika ufahamu sababu zaidi ulizo nazo za kumpigia asante.

15. Yehova alikomboaje Waisraeli utumwani Misri?

15 Kitabu cha Kutoka chasimulia jinsi Yehova alivyotoa watu wake utumwani Misri akawapeleka ufuo wa magharibi wa Bahari ya Shamu. Ndipo alipotenganisha maji kwa mwujiza hata mamilioni ya Waisraeli na wenzao wakaweza kuvuka wakiwa salama. Wamisri walipojaribu kuzuia Yehova asikomboe watu wake, aliyatumia maji yale yale kuwaharibu wote, pamoja na Farao hodari. (Kut. 14:21-30; Zab. 136:1, 10-15) Kama ungalikuwako pamoja na watu wa Mungu ungalionaje?

16. Israeli waliitikiaje kwa njia ifaayo?

16 Waliposalimika katika ufuo ule mwingine, Musa na wana wa Israeli walimpigia Yehova asante kwa wimbo, wakisema: “Ni nani aliye kama wewe, mwenye kujihakikisha kuwa hodari katika utakatifu? . . . Wewe katika fadhili zako za upendo umeongoza watu ambao umewapata tena;bila shaka wewe utawaongoza kwa nguvu zako kwenye kao lako takatifu.” (Kut. 15:11-13, NW) Mungu alipowakomboa walisadiki kwamba angeendelea kufanya hivyo hata katika Nchi ya Ahadi. (Kut. 15:17) Tendo hilo la Mungu halikuonyesha uwezo wake tu, bali pia lilionyesha fadhili zake za upendo, ambazo kwa ajili yazo walimpigia asante wakamsifu.

17. Twaweza kupata ulinganifu gani katika shughuli za kisasa za Mungu na watu wake?

17 Je! wewe waitikia kwa njia iyo hiyo? Pengine waona wakati huu Mungu hajachukua hatua za ukombozi. Lakini namna gani mifano mingi ya kisasa ambapo waabudu wa kweli wameondolewa vizuizi au mateso? Unapopata habari hizo je! unapendezwa kivivu tu kisha unaanza tena shughuli za maisha ya kila siku? Kwa mfano, baada ya Mashahidi wa Yehova kufundisha na kukutana kwa siri miaka mingi kwa sababu ya kupigwa marufuku na serikali, sasa wako huru kuendesha elimu yao ya Biblia katika Spania, Ureno na Ugiriki. Je! hiyo si sababu ya kufurahi? Je! si ushuhuda wa fadhili za upendo za Yehova? Mungu angaliweza kuacha hali ziendelee zilivyokuwa. Lakini yalikuwa mapenzi yake kuwe na mabadiliko hayo. Je! wewe waitikia kama Waisraeli, ukimpigia Yehova asante na kumsifu kwa sababu ya vionyesho hivyo vya fadhili zake za upendo? Je! umetajia wengine waziwazi habari za ukombozi huo, ukaimba sifa kwa ajili ya fadhili za upendo za Mungu?​—Kol. 3:16.

18. Wengi wetu tumeonyeshwaje fadhili za upendo, mmoja mmoja? (Zab. 22:4, 7, 8)

18 Tena, pengine umepatwa na mambo ambayo yakupasa umpigie Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo. Kwa mfano, je! umedhihakiwa kwa sababu ya kutetea kanuni za Kikristo? Labda ni kwa sababu hukujitia katika mazoea ya udanganyifu kazini pako, ukakataa kupunja shuleni au ukakataa kushiriki kupiga porojo pamoja na jirani zako. (Efe. 6:5-8; Ebr. 13:18; 1 Tim. 5:13) Au pengine umekazwa upotoe ibada yako. (Dan. 3:16-18; Ufu. 18:4, 5) Hukufurahi kutendwa au kupingwa hivyo. Lakini labda baadaye hayo yalikwisha. Pengine wapinzani wamechoka au wakaanza kukuheshimu kwa sababu ya kushikamana na kanuni za Biblia. Lakini jambo la maana ni kwamba ulitetea suala la enzi kuu ya Mungu kwa kufanya yaliyo haki machoni pa Yehova, naye akakusaidia uendelee kuwa imara mpaka faraja ilipokuja. Je! hilo si onyesho la fadhili zake za upendo ambalo wapaswa kumpigia asante na kumsifu?​—Zab. 22:22, 25; 23:6.

19. Wakati Mfalme Daudi alipofaulu mwishowe kuagiza Sanduku la Agano liletwe Yerusalemu, jambo hilo lilifanya sifa gani itolewe?

19 Biblia ina mifano mingi ya kweli ya fadhili za upendo za Mungu. Mara nyingi hizo zilikuwa nyakati alipofanya watu wasaidie ibada ya kweli. Wakati mmoja ulihusu sanduku takatifu lililoitwa Sanduku la Agano lililowakilisha kuwapo kwa Yehova katika Israeli. (Kut. 25:10-22) Baada ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi Sanduku liliendelea kuwapo miaka mingi, si katika hema yake Shilo, bali katika Kiriath-yearimu. Daudi alitaka kulileta Yerusalemu ambako alikalia kiti cha enzi cha Yehova. Alijaribu kufanya hivyo mara ya kwanza akashindwa. (1 Nya. 13:1-14) Mwishowe, alilileta Sanduku, likiwa limechukuliwa vizuri na Walawi, mpaka Yerusalemu. (1 Nya. 15:1-28) Wakati huo maalum ulifanya sifa ifuatayo itolewe: “Mshukuruni [Yehova] kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake ni za milele.”​—1 Nya. 16:1, 8, 34-36.

20. Ni nini pia linaloweza kutambuliwa kuwa ushuhuda wa fadhili za upendo leo?

20 Je! wewe unaitikia ivyo hivyo wakati hatua ya maendeleo inapoinua ibada ya kweli? (Isa. 2:2, 3) Pengine msaada mpya umetolewa ili watu zaidi wajifunze habari za Yehova. Pengine ni kitabu kipya kinachotumiwa kufundisha watu kweli za Biblia. Au pengine ni toleo la pekee la Mnara wa Mlinzi au Amkeni! linalokusudiwa kusadikisha aina fulani ya watu kwamba wanapaswa kumtumikia Mungu. Au huenda kukawa na mpango wenye maendeleo unaohusu wazee wa kiroho katika kundi. Je! unajikuta ukiitikia kama Daudi, ukimshukuru Yehova kwa ajili ya fadhili za upendo zilizowezesha kuwe na hatua hizo za maendeleo katika ibada ya kweli? Bila shaka kuna sababu za kutosha kufanya hivyo.

21. Ni ujenzi gani ambao waabudu wa kweli waliutambua kuwa mfano wa fadhili za upendo za Mungu mwaka 536 K.W.K.?

21 Unapofikiria hali yako mwenyewe, angalia mfano mmoja zaidi wa Biblia. Huko nyuma katika mwezi mfupi wa pili (Aprili-Mei), 536 K.W.K.,Wayahudi waliokuwa wametoka uhamishoni Babeli walianza kujenga upya hekalu la Yehova Yerusalemu. Hawakuwa wamejitoa wenyewe Babeli wala sio waliofikiria kwanza kujenga upya hekalu. Sifa ilimwendea Yehova. (Ezra 1:1, 5) Je! wangeudharau mpango wa ujenzi? Twasoma hivi: “Hata wajenzi walipouweka msingi wa hekalu, . . . [Makuhani na Walawi wenye kutazama] wakaimbiana’ wakimhimidi [Yehova], na kumshuku wakasema, Kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake kwa Israeli ni za milele. Kisha watu wote wakapaza sauti zao, na kupiga kelele, walipomhimidi [Yehova], kwa sababu msingi wa nyumba ya [Yehova] umekwisha kuwekwa.”​—Ezra 3:10, 11.

22. Ni ulinganifu gani unaoweza kupatikana katika mambo ambayo sisi wenyewe tumeonyeshwa, na hilo limetuongoza tuitikieje? (Ezra 3:1; Zab. 149:1)

22 Sasa, namna gani leo? Pengine hapo kwanza kundi lenu lilikuwa likikodi mahali pa kukutania, lakini sasa mmejenga Jumba la Ufalme. Au pengine kundi lenu limepanua au likang’arisha Jumba la Ufalme. Au pengine mahudhurio ya mikutano yanaongezeka, na jamaa mpya za watu wenye kupendezwa zinafika katika jumba lenu. Au pengine wengi kundini wamechochewa washiriki katika utumishi wa painia msaidizi. Katika mambo hayo, je! wewe huona uongozi wa Yehova, na kutambua kwamba yeye ndiye amefanya yatukie, akamimina roho na baraka zake? Naam, je! wewe wajua kwamba mambo hayo yaliyotimizwa ni maonyesho ya fadhili nyingi za upendo za Yehova? Je! yanakufurahisha wewe pia?

23. Twaweza kufikia mkataa gani juu ya jinsi Mungu anavyoshughulika nasi? Lakini ni mambo gani katika shauri hili ambayo yastahili bado kuangaliwa?

23 Bila shaka Wakristo wana sababu nyingi za kumpigia Yehova asante na kumsifu kwa ajili ya fadhili zake za upendo: Kwa ajili ya kuzionyesha kuhusu kusudi alilotangaza linalofaidi wanadamu wote wanaoishi katika kazi zake za kuumba. Kwa ajili ya kutuonyesha sisi mmoja mmoja. Na kwa ajili ya fadhili za upendo ambazo tumepata tukiwa kati ya watu wa Mungu. Lakini, ni kwa njia gani hasa utampigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo? Hayo ni mambo ya kufikiria katika mazungumzo yanayofuata.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki