Utapigaje Asante kwa Ajili ya Fadhili Zake za Upendo?
1, 2. (a) Uhai wetu ni wenye thamani gani, lakini Daudi alisema nini katika Zaburi 63:3 juu ya uhai? (b) Ilikuwaje hivyo? (Ayubu 14:1, 2; Yak. 4:14)
NI KITU gani chenye thamani kupita uhai wako? Bila uhai huwezi kufurahia mali zo zote wala kufaidika nazo. Unapofikiria hilo, angalia kwamba mtunga zaburi alimwimbia Yehova. Mungu akasema: “Fadhili zako ni njema kuliko uhai.”—Zab. 63:3.
2 Daudi alikuwa akisema kwamba ingekuwa afadhali afe kuliko kupoteza upendeleo wa Yehova. Mambo yote ambayo Daudi angeweza kuwa nayo au kufurahia katika umilele ujao yalitegemea Mungu. Vilevile, Daudi alizijua nyakati nyingi wakati Yehova alipokuwa amemhurumia na kumsaidia kwa ushikamanifu. Huo wote ulikuwa ushuhuda wa fadhili za upendo za Mungu. Kwa hiyo Daudi aliziona fadhili hizo za upendo kuwa za maana zaidi kuliko kuishi kwa muda akiwa mwanadamu. (1 Nya. 29:14, 15) Ndivyo nawe unavyoona? Je! fadhili za upendo, au upendo mshikamanifu, wa Yule awezaye kukupa uzima wa milele si zenye thamani zaidi kuliko maisha yenye kufikia mwisho, ambayo ‘yapo leo na kesho yamekwenda’?
3. Daudi alichukua hatua gani aitikie fadhili za upendo za Yehova, na yafaa tujiulizeje?
3 Hata hivyo, Daudi hakuona tu ubora wa fadhili za upendo za Yehova na bas! Angalia alivyoitikia: “Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai; midomo yangu itakusifu. Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai.” (Zab. 63:3, 4) Naam, kuthamini sana fadhili hizo za upendo kulimfanya amsifu Mungu na kumpigia asante nyingi. Kama makala iliyotangulia ilivyozungumza, sisi mmoja mmoja tuna sababu nyingi za kumpigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo. Kwa hiyo, yatupasa tuwe na kawaida ya kumpigia asante na kumsifu katika maisha zetu. Ndivyo unavyofanya? Siku nzima au zaidi zapita bila ya wewe kumfikiria Mungu na kusema habari zake? Au mara nyingi unasema habari za Yehova, unamsifu bila kuagizwa kwa sababu ya jinsi alivyo na mambo ambayo amefanya? Je! waona kwamba kila siku waiga nia ya Zaburi 107:21, 22?
4. Ni kwa njia gani ni lazima tuzitangaze habari njema kuhusu jambo hili?
4 Bila shaka, njia moja ya kumpigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo ni kueleza wale ambao hawajaanza kumwabudu habari zake. (Matendo 14:1-3; 20:24) Ujumbe wa habari njema waweza kuokoa uhai wao. Basi, ni vizuri kwamba twapendezwa na kuhubiri habari njema kote kote.—Rum. 10:9-15.
5. (a) Kwa sababu gani huenda tukawa tunatolea watu ushuhuda wa mambo yenye sifa mbaya tu? (b) Hata hivyo, kwa sababu gani baadhi ya habari hizo ni za maana?
5 Wakristo wa kweli wanajua kwamba watu wengi wamejifunza baadhi ya mafundisho ya uongo na yaliyopotolewa juu ya Mungu na Biblia. Kwa hiyo, huenda bila kujua tukawa sikuzote tukieleza watu mambo yenye sifa mbaya tu tunapowapa ushuhuda. Jiulize ni mara ngapi unapotumia wakati wako wote ukieleza mambo ambayo Biblia haifundishi—kwamba haifundishi Mungu ni mwenye nafsi tatu wala moto wa mateso, kwamba mwanadamu hana nafsi isiyokufa na kwamba dunia haitateketezwa kwa moto. (Yohana 14:28; Eze. 18:4; Mhu. 9:5, 10; 1:4) Ni kweli kwamba watu ambao tunatolea ushuhuda wanahitaji msaada wasahihishe imani zao zenye makosa. Na huenda tukawasaidia watofautishe kati ya dini ya kweli na ya uongo kwa kuwaonyesha wazi makosa. Lakini yatupasa tuwe waangalifu tusiwe tukiongea nyakati zote habari za mambo yenye sifa mbaya.
6. Kwa sababu gani yatupasa kutia mambo mengi yenye sifa njema katika ungamo letu la hadharani?
6 Twapaswa kutia mambo mengi yanayohusu Yehova katika ‘ungamo letu la hadharani,’ kwa maana tunatoa “dhabihu ya sifa.” (Ebr. 13:15, NW; linganisha Zaburi 107:21, 22.) Kwa mfano, twaweza kukazia jinsi Yehova ALIVYO. Twaweza kuonyesha kwamba ‘yeye peke yake ndiye Aliye Juu Zaidi.’ (Zab. 83:18) Twaweza kueleza kwamba twaweza kupata uzima wa milele kwa kumjua sana yeye na Mwanawe. (Yohana 17:3) Tena twaweza kukazia baadhi ya sifa zake bora zinazoweza kufanya watu wamkaribie—rehema yake, hekima isiyopitika, ufahamu, ukarimu, uaminifu na bila shaka, fadhili zake za upendo.—Kum. 32:4; Yak. 1:17; Zab. 84:11.
7. Twaweza kukaziaje fadhili za upendo za Mungu, na matokeo yatakuwa nini?
7 Kila mmoja wetu apaswa kuchunguza “ungamo la hadharani” lake mwenyewe aone anavyoweza kukazia zaidi mambo hayo yenye sifa njema. Kwa mfano, unapoongoza funzo la kawaida la Biblia na jamaa yako au wengine, je! waweza kukazia fadhili za upendo za Mungu kwa njia fulani? Unapozungumza kisa fulani juu ya Biblia au kusudi la Mungu, unaweza kueleza kinaonyesha nini juu ya Mungu wetu, kwa ufupi tu. Au waweza kumwuliza mwanafunzi linalozungumzwa linamsaidia yeye afahamu nini juu ya Yehova. Kufanya hivyo kutamkaribisha zaidi mwanafunzi na Yehova, kumwonyeshe zaidi kwamba Mungu ni halisi na ahusiana naye, atake kujifunza mengi zaidi juu ya Mungu bora huyu na kumsifu.—Zab. 147:1, 11.
KUPIGA ASANTE KATIKA MAZUNGUMZO YETU
8. Ni nyakati gani nyingine twaweza kumpigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo?
8 Nyakati za kusema habari za Yehova na fadhili zake za upendo si tunapojaribu kufundisha watu kweli za Biblia tu. Namna gani mazungumzo ya kila siku? Yesu alisema: “Kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.” (Mt. 12:34) Ikiwa kweli twathamini fadhili za upendo za Mungu, yatupasa tuonyeshe hivyo kila siku tunaponena. Ndivyo alivyofanya mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Ni neno jema kumshukuru [Yehova], na kuliimbia jina lako, Ee Uliye juu. Kuzitangaza rehema zako [fadhili zako za upendo, NW] asubuhi, na uaminifu wako wakati wa usiku.”—Zab. 92:1, 2.
9. (a) Maoni ya watu wengi ni nini juu ya kumtaja Mungu? (b) Hilo latofautianaje na nia yetu? (Zab. 107:31, 32)
9 Pengine umepata kuona kwamba watu wengi, hata wanakanisa wanaodai wanamwabudu Mungu, hawana nia ya kusema habari zake wala makusudi yake. Tena hawataki kabisa kuonyesha wanahusiana na Mungu; kufanya hivyo kwaonekana kuwa si jambo la ki-siku-hizi na kwaaibisha mtu. Kwa ufupi, huenda ikawa watu hao wanakuwa na maelekeo hayo maana hawana uhusiano wa kipekee na Mungu. Lakini, kwa sababu nia hiyo ya kutotaka kuongea habari za Mungu imeenea kote, twaweza kujiuliza, ‘Je! mimi nimevutwa na nia ya ulimwengu ya kutotaka kuingia katika mazungumzo yanayohusu Mungu au kuonyesha katika mazungumzo kwamba mimi humfikiria katika maisha yangu na mawazo yangu?’ Bila shaka Yehova ni sehemu ya maisha zetu na apaswa kuwa sehemu ya mawazo yetu. Kwa kawaida twatafuta baraka na uongozi wake. Kwa hiyo haitupasi kusita kuongea habari zake, kumtaja katika mazungumzo yetu na kuonyesha twapendezwa na matendo na makusudi yake.
10. Ni mashauri gani ya Maandiko yanayotupasisha tuseme habari za Mungu kwa kawaida?
10 Bila shaka, yatupasa tuepuke kujionyesha kuwa wenye haki. Kumbuka, si vigumu watu kuona uanadini wa kuigizwa tu au wa kujifanya. Yesu alilaumu viongozi wa dini Wayahudi kwa sababu ya kujionyesha kuwa watawa ati ndiyo waonekane nakusikika. (Mt. 6:1-5) Hata hivyo Biblia yatusihi tumsifu Yehova na kumpigia asante daima. Kwa hiyo, ingawa tunatii shauri la Mathayo 6:1-5 na tunajiangalia watu wasidhani tunajionyesha kuwa wenye haki, twasema habari zake. Twaweza kwa unyenyekevu na imani kutaja matendo na njia zake, zinazotia ndani jinsi ameshughulika nasi au jinsi tunavyohusiana naye.
11. Tuna nafasi gani za kuingiza habari za Mungu katika mazungumzo yetu kupatana na Zaburi 34:1?
11 Mchana pengine wewe huongea mambo mengi na jamaa yako, rafiki Wakristo na wengine shuleni, kazini au katika ujirani. Pengine nafasi inatokea ya kuongea habari za Mungu kwa hali ya unyofu na ya kikawaida. Je! unaongea habari za safari ya kwenda kujiburudisha pwani au milimani na kufurahia kuumba kwa Yehova? Kwa kuwa unathamini uzuri wa vitu vya asili na utulivu wa vitu ambavyo amefanya, mbona usitaje hayo?
12. Twaweza kuongeaje habari za Mungu na watu ambao si waabudu wa kweli?
12 Hata ikiwa unazungumza na asiyeamini, pengine waweza kutumia busara uongee habari za Mungu, kwa mfano utaje kifupi furaha unayopata kutokana na vitu ambavyo Muumba wako amefanya. (Matendo 4:24; 14:15) Hakuna mtu anayepaswa kushangaa ati wewe huongea habari za Mungu katika mazungumzo yako ya kawaida, kwa maana je! humfikirii katika mambo unayofanya au unayoepuka kufanya? Huenda mtu akaongea nawe jinsi unavyozoeza watoto wako, kwa kuona kwamba umefaulu. Je! unaweza kumjibu kwa kutia ndani maneno machache ya kumpigia Mungu asante kwa ajili ya mashauri yake yanayohekimisha mtu afanye hivyo? (Zab. 19:7) Pengine mfanya kazi mwenzako asema watumia likizo lako kuhudhuria kusanyiko la Kikristo badala ya kutumia lote kwa ajili ya “anasa”. Waweza kujibu kwa unyofu kwamba, wafurahia kujifunza mengi zaidi juu ya fadhili za upendo na mapenzi ya Mfanyi wako. (Zab. 100:3-5) Huenda maelezo mafupi hayo yakawa na matokeo mema, pengine kufanya aanze kumfikiria Mungu. Lakini hatumtaji Mungu kwa sababu tu msikilizaji aweza kusaidika. Twaongea juu ya Mungu na matendo yake kwa sababu hayo yamo mioyoni mwetu na hivyo katika ndimi zetu pia.—Zab. 45:1.
13. (a) Kwa sababu gani lapaswa kuwa jambo jepesi zaidi kumtaja Mungu tunapoongea na waabudu wenzetu? (b) Ni nini baadhi ya njia za kufanya hivyo?
13 Ikiwa nyakati zinazofaa twamtaja Mungu mara nyingi tunapoongea na wasioamini, yafaa sana tufanye hivyo mara kwa mara tunapoongea na wale wanaomtumikia Mungu. Tunajiona huru zaidi kuongea na Wakristo wenzetu juu ya utendaji wetu, mipango yetu, maoni yetu, na mambo kadha wa kadha. Kwa hiyo je! katika mazungumzo hayo haitupasi tuelekee kumtaja Mungu na matendo yake, kama isemavyo Zaburi 92:1, 2? Pengine Jumba la Ufalme linatengenezwa. Yakupasa ushukuru kwa sababu Mungu anabariki kundi. Pengine tumepokea kitabu kipya cha kutusaidia kufahamu Biblia. Ukikiona kwa unyofu kama ushuhuda wa fadhili za upendo za Yehova, mbona usitaje hilo katika mazungumzo. Namna gani maelezo mapya yaliyomo, yenye kupendeza? Zungumza mambo hayo na ndugu zako kwa furaha, kwa unyenyekevu unaokuepusha usijionyeshe kuwa mwenye haki. Kuingiza mambo ya kiroho hapa na pale katika mazungumzo kutajenga wote.
KUWA MACHO KUONA SABABU ZA KUSHUKURU
14. Yatupasa tusitawishe maoni gani juu ya wema wa Mungu?
14 Ingekuwaje kama mtu angekupa chombo chenye mchanga na visehemu-sehemu vya chuma? Ingekuwa vigumu kuokota vipande hivyo vya chuma. Lakini ungeweza kuviokota vyepesi kwa kutumia sumaku. Moyo uliojawa na kumshukuru Yehova ni kama sumaku hiyo. Tukiwa na moyo wa namna hiyo, kila siku twaweza kuchagua vyepesi mifano mingi sana ya fadhili na ukarimu wake ambazo ni zenye thamani nyingi zaidi kuliko chuma, kuliko hata dhahabu Tukiwa macho kuona shuhuda za wema wa Mungu, itakuwa vyepesi kumsifu na kumpigia asante ya mambo hayo.—Mit. 3:3, 4, 13-18.
15. Twaweza kumpigia Yehova asante kwa sababu ya mambo kama yapi? (Efe. 5:20)
15 Kuumba kwa Yehova tunakoona kila siku kumejawa na vitu vinavyoweza kutukumbusha misaada aliyofadhili nayo wanadamu wote. Labda utaona vipaka viwili vikiangushana-angushana majanini. Bila shaka utachekelea mchezo wao. Je! hilo lakufanya umfikirie Yehova na jinsi anavyopendezwa na kuumba kwake? Biblia yasema yeye ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11, NW) Kwa hiyo unapotazama vipaka, visimba au wanyama wengine wakicheza, je! utakumbuka kwamba Mungu apenda furaha na ucheshi? Namna gani ladha nzuri ya kipande cha tunda katika mchana wenye joto? (Zab. 145:8, 15-17) Kwa habari ya harufu zenye kufurahisha, je! wakumbuka manukato ya maua fulani au harufu ya majani ya ng’ombe yaliyokatwa karibuni? Unapofurahia vitu hivyo, je! haifai kumpigia, Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za kutupa milango ya maarifa na vitu vizuri namna hiyo vya kufurahia?
16. Tukiwa macho kuuona wema wa Mungu na kuutaja, huenda hilo likawa na matokeo gani juu ya wengine?
16 Jamaa moja kaskazini mwa New York ilikuwa ikila wakati mwana wa miaka minane aliposema hivi: “Mama, si ni vizuri kwamba Yehova alituwekea uso upande wa mbele tuweze kula.” Ingawa kivulana huyo alikuwa akiongea kwa sababu ya ujana, bila shaka hakuwa akichukua mambo kikawaida tu. Maelezo yake ya unyofu yalisaidia wote waliokuwa karibu yake wakamfikiria Yehova na kuthamini zaidi vitu alivyofanya. Maelezo yetu juu ya fadhili za upendo anazotupa Mungu tunapomtumikia yaweza kuwa na matokeo ayo hayo.
KUFANYA MAENDELEO KATIKA NYIMBO NA SALA
17 Njia nyingine ya kumpigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo ni kuimba. Kuimba kumekuwa sehemu ya ibada ya kweli muda mrefu. (Kut. 15:1-21: Zab. 1-150; 2 Nya. 29:27; Ufu. 15:3, 4) Katika hekalu la Yerusalemu Walawi fulani walipendelewa kupiga muziki huku wengine wakiimba. Twastahili kuangalia jitihada walizofanya, na kusudi lao. Biblia yasema kwamba walipaswa “wamfanyie ukumbusho, na shukrani na sifa. [Yehova], Mungu wa Israeli.” Kwa sababu gani? “Kwa kuwa fadhili zake ni za milele.”—1 Nya. 16:4, 41, 42; 9:33.
17, 18. (a) Waisraeli walitumiaje nyimbo kupiga asante? (b) Marko 14:26 yaonyesha Yesu na mitume walifanya nini? (Matendo 16:25)
18 Katika habari hii, umepata kufikiri kwamba Yesu na mitume walikuwa waimbaji? Walikuwa, na walifurahia hilo. Marko 14:26 yatuambia kwamba usiku wao wa mwisho kuwa pamoja duniani waliimba sifa. Ilikuwa desturi ya Wayahudi kuimba Zaburi 113 mpaka 118 wakati wa chakula cha Kupitwa. Kwa hiyo inawezekana kwamba Yesu na mitume wake kumi na mmoja waaminifu walimalizia chakula hicho kwa kuimba Zaburi 118, inayoanza na kumalizika kwa kusema: “Mshukuruni [Yehova] kwa kuwa ni mwema. kwa maana fadhili zake ni za milele.”
19. Nia yetu yapaswa kuwa nini juu ya kuimba kundini? (Efe. 5:18, 19)
19 Leo pia Wakristo wana nafasi ya kumsifu na kumpigia Yehova asante kwa kuimbia fadhili zake za upendo. Je! Hivyo ndivyo wewe unavyoziona nyimbo zenye vichwa vya Biblia unazoimba katika mikutano ya kwenu ya Mashahidi wa Yehova? Au wakati wa kuimba unafanya mambo mengine? Au midomo yako ndiyo inayoyataja maneno huku akili zako zikifikiria mambo mengine? Ni vyepesi hilo kutukia. Lakini, jinsi lilivyo jambo zuri kuziona nyimbo za Kikristo kama njia ya kumpigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo!
20. (a) Sala yapaswa kutumiwaje kumpigia Mungu asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo? (Kol. 1:9-12) (b) Kulingana na Danieli 6:10, ni kwa njia gani Danieli ametuwekea mfano mwema katika jambo hilo?
20 Sala ni njia nyingine tunavyoweza kumpigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo. Inaelekea wewe wasali kwa kawaida. Lakini je! ungeweza kufanya maendeleo ya kumpigia Mungu asante na kumsifu katika sala? Ni vyepesi sana kuingia katika mazoea ya kumwomba tu vitu vyetu wenyewe, vya jamaa yetu, vya kundi letu na vya wengine. Ikiwa wewe ni mzazi, bila shaka watoto wako wanapokuomba mashauri na msaada unafurahi. Lakini ungeonaje kama mtoto wako angesema hivi: “Baba, ningependa kukuambia kwamba sisi watoto twakupenda sana. Wewe u imara, nasi twakuheshimia hilo, lakini u mwenye upendo pia. Wewe ndiwe rafiki yetu mkubwa zaidi.” Ikiwa wajua jinsi ungefurahia kusikia maneno hayo manyofu, wadhani Mungu huonaje tunapotia asante na sifa katika sala zetu? Nabii Danieli alituwekea mfano mwema. Biblia yataja wazi kwamba alimsifu Mungu katika sala.—Dan. 6:10.
21. Twaweza kuepukaje kutaja mambo ya ujumla tu Katika sala zetu?
21 Ni vizuri kutaja waziwazi katika sala zetu wema ambao Mungu ametuonyesha. Je! umepata kumsikia mtoto akisali na kumpigia Mungu asante kwa ajili ya ice cream ya chocolate, kwa ajili ya kufurahia kusafiri katika mashua au likizo lake la shule? Je! sisi nasi hatuwezi kutaja mambo waziwazi badala ya kumpigia Mungu asante bila kutaja ni kwa ajili ya mambo gani? Ikiwa umeona jambo jema katika kazi ya kuhubiri, mpigie Mungu asante waziwazi. Ikiwa ulipokea zawadi, inaelekea ulimpigia asante mtu aliyekupa. Lakini namna gani kumpigia asante Yule ambaye amefanya vitu vyote? Umepata kufahamu mashauri ya Biblia juu ya tatizo kubwa? Piga asante katika sala. Na unapopendelewa kuwakilisha wengine katika sala utaje mifano halisi ya baraka ya Mungu ambayo nyote mwapigia asante.—Zab. 42:8.
22. Kwa kurudia, ni kwa njia gani twaweza kumpigia Yehova asante kwa ajili ya fadhili zake za upendo, nasi tutakuwa tukionyesha nia gani?
22 Bila shaka ziko shuhuda nyingi za fadhili za upendo ambazo Mungu ametuonyesha tukiwa watumishi wake anaokubali. Twaweza kuziona kila siku tukiwa macho. (Zab. 107:43) Na kila mmoja wetu aweza kushukuru kwa kutaja habari za Mungu wetu. Jinsi gani? Wakati gani? Tunapohubiri na kufundisha watu. Katika mazungumzo yetu ya kawaida tunapokuwa na Wakristo wenzetu na watu wengine. Na katika nyimbo na sala. Naam, ingawa tunangoja bado wakati ambao kuumba kote kutaungana kumsifu Yehova kama isemavyo Zaburi 150, sisi mmoja mmoja twaweza kushiriki kabisa kufanya hilo sasa hivi. Hivyo tutaonyesha nia za Daudi zinazotajwa katika Zaburi 59:16, 17: “Nami nitaziimba nguvu zako asubuhi, nitaziimba fadhili zako kwa furaha . . . Ee nguvu zangu, nitakuimbia kwa furaha, maana Mungu ndiye aliye ngome yangu. Mungu wa fadhili zangu.”
—Kutoka The Watchtower, Feb. 15, 1977