Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 7/15 kur. 330-332
  • Yesu Anyenyekea Kifalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yesu Anyenyekea Kifalme
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Habari Zinazolingana
  • Fidia
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Mambo Ambayo Mfalme Anatufanyia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Jambo Kuu Linaloelezwa Katika Habari Njema Ni Ufalme wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Kuondoa Doa la Dhambi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 7/15 kur. 330-332

Yesu Anyenyekea Kifalme

MOJAWAPO sifa kubwa sana za Yesu Kristo ni unyenyekevu. Aliacha kwa moyo wa kupenda cheo chake kikubwa mbinguni awe mwanadamu “mdogo punde kuliko malaika.” (Ebr. 2:7; Flp. 2:5-7) Halafu, alipokuwa duniani, hakutafuta kutumikiwa na watu bali yeye alitumikia wengine kwa unyenyekevu. (Mt. 20:28) Hata hivyo, wakati ujao atanyenyekea kifalme akiwa “MFALME WA WAFALME, NA BWANA WA MABWANA.” (Ufu. 19:16) Unyenyekevu huo unatajwa katika 1 Wakorintho 15:24, tunaposoma hivi: “Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake.” Ili kuthamini yanayohusika, lazima tuangalie sababu Yehova amekusudia Mwanawe atawale kama Mfalme.

Wakati Yehova Mungu alipoumba wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, aliwataka wakae katika upendo wake wakiwa na umoja kamili naye. Alikuwa amewaumba kwa njia ambayo wangeweza kuishi milele kama wangeendelea kuwa na uhusiano mwema naye kwa kutii kila jambo. Kwa kuasi sheria ya Mungu, Adamu na Hawa walijitenganisha na Mfanyi wao wakapoteza uhusiano wa kiroho waliohitaji kuendelea kuishi. Baada ya kuharibu ukamilifu wake, Adamu alipoteza pia uwezo wa kuzaa watoto wakamilifu. Biblia yasema, “Kwa hiyo, kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Rum. 5:12) Kwa kuwa dhambi maana yake ni kukosa shabaha ya kumtii Mungu kabisa, taifa lote la kibinadamu lilipata kufarakana na Muumba kwa njia hiyo.

Lakini, hayakuwa mapenzi ya Mungu hali hiyo iendelee kuwapo. Hiyo ni wazi kutokana na aliyoandika mtume Paulo juu ya utawala wa Kristo, katika 1 Wakorintho 15:25, 26: “Sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.” Ili mauti ibatilishwe lazima udhaifu wote na kutokamilika kwa wanadamu kuondolewe. Ndivyo ilivyo kwa sababu, kama Biblia isemavyo, “uchungu wa mauti ni dhambi.” (1 Kor. 15:56) Kulingana na Ufunuo 20:4, “miaka elfu” imewekwa kando ili Kristo pamoja na kundi la watawala wenzake wabatilishe mauti kwa kurudishia wanadamu ukamilifu.

Mpango wa kukomboa wanadamu katika utumwa wa dhambi na mauti umeonyeshwa kwa njia ya mfano katika Ufunuo 22:1, 2. Hapo mtume Yohana aeleza aliyofunuliwa na malaika katika njozi: “Akanionyesha mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo. . . . Na upande huu na upande huu wa ule mto, ulikuwapo mti wa uzima, uzaao matunda, aina kumi na mbili, wenye kutoa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo ni ya kuwaponya mataifa.”

Biblia yaeleza wazi kwamba madoa ya dhambi yaweza kuondolewa kwa kutegemea dhabihu ya Yesu peke yake. Mtume Yohana aliongozwa na Mungu kuandika hivi: “Damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.” (1 Yohana 1:7) Kwa hiyo “mto wa maji ya uzima,” wenye miti kando kando ya kingo zake, wafananisha mpango wa Mungu wa uzima, kutia na faida zenye kulipia dhambi za dhabihu ya Mwanawe. Kwa kuwa “maji ya uzima” na miti yafananisha mpango wa Mungu wa uzima, kutumia mpango huo bila shaka kwahusu kuziamini faida zenye kulipia dhambi za damu ya Yesu.​—Ufu. 22:17.

Lazima imani hiyo ionyeshwe kwa matendo, kwa maana, kama Biblia ionyeshavyo: “Imani pasipo matendo imekufa.” (Yak. 2:26) Ni matendo gani yanayohitajiwa? Ni kutii uongozi wa ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo na watawala wenzake. Wakati watu mmoja mmoja watakapokuwa wakinyenyekea utawala wa Ufalme wa Kristo wa miaka elfu kwa kushikamana nao, huku faida zenye kulipia dhambi za dhabihu yake zikitumiwa kwa ajili yao, watakua mpaka wakamilike.

Maelezo ya mfano juu ya mpango wa Mungu wa uzima yaonyesha kwamba wanadamu watainuliwa kidogo kidogo mpaka wakamilike. Miti iliyo kando ya “mto wa maji ya uzima” huzaa matunda yake kila mwezi. Kama mpango wa Mungu wa uzima ungepaswa kutumiwa mara moja tu, ni wazi kwamba kusingekuwa na uhitaji wa matunda hayo yenye kuendeleza uhai kuzaliwa bila kukoma.

Tena, Yesu Kristo na watawala wenzake watatumia wajumbe wa kidunia ili kusaidia wanadamu. Watakuwako wanaume wenye kufuata kabisa yaliyo haki na wenye kupenda kabisa watu wengine. Kati yao watakuwako wanaume waaminifu wa ukoo wa babu za Yesu. Kwa kuwa Yesu Kristo atawafufua, watakuwa watoto wake.​—Zab. 45:16.

Ni wazi basi kwamba Mungu alikusudia kuwe na ufalme wa Kimasihi kwa sababu tu taifa la kibinadamu liliingizwa katika dhambi na mauti. Dalili zote za dhambi zitakapoondolewa, ufalme wa Kimasihi hautahitajiwa tena utawale kwa njia hiyo. Lakini, hautakoma papo hapo; ufalme huo ‘hautaangamizwa,’ kwa maana matunda ya kazi njema zake yatadumu milele. (Dan. 7:14) Inaelekea kwamba hivyo ndivyo Maandiko yanavyomaanisha yanaposema utawala wa Kristo “hauna mwisho.”​—Isa. 9:7; Luka 1:33; Ufu. 11:15.

Yesu Kristo atakuwa ametimiza daraka alilogawiwa la kukamilisha wanadamu mwishoni mwa utawala wake wa miaka elfu. Ndipo kwa unyenyekevu wa kweli atakapomrudishia Baba yake mamlaka aliyotumia juu ya wanadamu akiwa “MFALME WA WAFALME NA BWANA WA MABWANA.” Hivyo ndivyo maneno ya 1 Wakorintho 15:28 yatakavyotimizwa: “Vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake [Mwana], ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote.” Watawala wenzake na wajumbe wa kidunia wa Ufalme watafuata mfano wake na kuacha vyeo vyao vya furaha na unyenyekevu. Wakati huo wanadamu wote watakuwa na vyeo vinavyolingana mbele za Mungu, bila udhaifu wala kutokamilika.

Twapaswa kuongozwa na ujuzi huo tufanyeje hata sasa? Wapaswa kutukazia kwamba katika kundi la Kikristo vyeo sivyo vya maana sana. Mambo ya maana kweli kweli ni vile mtu alivyo, na uhusiano unaokubaliwa alio nao pamoja na Mungu, si madaraka au mamlaka aliyokabidhiwa. Katika kundi la Kikristo hamna “watu mashuhuri”; hata wazee au waangalizi ni watumishi au watumwa tu wa ndugu zao. (Mt. 20:25-27) Zaidi ya hilo, inaelekea kwamba mpango wa wazee au waangalizi uliopo leo au utakaokuwapo wakati wa utawala wa Kristo wa miaka elfu ni wa muda tu, na labda hautaendelea kuwapo baada ya wanadamu kuwa wakamilifu mbele za Yehova Mungu. Hakika, kufahamu mambo hivyo kunatia mkazo unapopaswa kuwa​—juu ya Mwenye Enzi Kuu, Yehova Mungu.

Kwa hiyo, na tumwige Yesu Kristo kwa kuendelea kuwa wanyenyekevu mbele za Mfanyi wetu, tukikumbuka sikuzote kwamba kuwa naye katika uhusiano anaoukubali ni mali yenye kudumu. (Mit. 22:4) Tukifanya hivyo, huenda tukawa na pendeleo la kuwa kati ya wale watakaoona Yesu akinyenyekea kifalme​—akimrudishia Mungu, Baba yake, ufalme.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki