Jambo Kuu Linaloelezwa Katika Habari Njema Ni Ufalme wa Mungu
“Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mt. 6:33.
1. Habari njema zinahusu nini hasa, na kwa sababu gani?
HABARI njema zinazotoka katika Biblia zinahusu ufalme wa Mungu hasa. Kwa sababu gani? Kwa sababu mambo ambayo Mungu anakusudia kufanyia wanadamu yanautegemea Ufalme huo. Kitu ambacho mwanadamu anahitaji leo ni serikali nzuri—serikali yenye kumpa uongozi unaofaa bila kumnyang’anya uhuru wala hiari ya kutumia akili yake mwenyewe anapotaka kufanya mambo.
2. Kwa sababu gani serikali inayoongozwa na Muumba ni bora kuliko ya wanadamu?
2 Serikali yenye kuongozwa na Mungu inahitajiwa kabisa ili wanadamu waweze kupata uzima na furaha. Mwanadamu ameonyesha vya kutosha kwamba hawezi kufaulu akijiongoza mwenyewe kwa utawala wa namna yo yote anaoweza kutunga. Nabii aliyeongozwa na Mungu aliandika hivi: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yer. 10:23) Lakini Muumba anayajua mambo yale yale ambayo wanadamu, viumbe vyake, wanahitaji. Anayajua maoni yao ya moyoni, matakwa yao, mapendo yao, tamaa zao. (Mt. 6:7, 8, 32) Yeye peke yake ndiye anayeweza kuleta hali ya kutosheka kabisa katika maisha yao. “[Wewe Mungu] waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake,” yasema Biblia. Atafanya hivyo kwa kuutumia ufalme wake.—Zab. 145:16.
3. (a) Ufalme una uhusiano gani na enzi kuu ya Mungu? (b) Eleza jinsi washiriki wa Ufalme wanavyochaguliwa na jinsi unavyofanyika.
3 Ufalme wa Kimasihi wa Mungu ni serikali iliyopangwa na kusimamishwa na Yehova Mungu, aliye Mwenye Enzi Kuu peke yake katika Ulimwengu Wote. Ufalme huo unatolea enzi kuu yake usaidizi na kuinyenyekea. (1 Kor. 15:27, 28) Ndicho chombo cha kuonyeshea enzi kuu ya Mungu na utawala wake juu ya dunia. Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, yule Masihi, ndiye kiongozi wa ufalme huo, naye sasa ni mtu wa kiroho mbinguni, asiyeweza kufa. Yeye ndiye “mng’ao wa utukufu wake [Mungu] na chapa ya nafsi yake.” (Ebr. 1:3) Chini yake watakuwako wafalme wenzake 144,000 ‘walionunuliwa’ kati ya wanadamu, wakachaguliwa kwa uangalifu katika kipindi cha zaidi ya miaka 1,900. (Ufu. 14:1-5) Kristo anasemekana hivi: “Ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi.” (Ufu. 5:9, 10) Ufalme huo utaitawala dunia muda wa miaka elfu ili kuwaingiza wakaaji wake katika uhusiano unaofaa pamoja na Mungu.—Ufu. 20:4-6.
MAMBO AMBAYO UFALME WA MUNGU UTAFANYIA WATU
4. Ufalme utasaidiaje watu watakaokuwa chini yake?
4 Nabii wa Mungu anatamka hivi: “Hukumu zako [Yehova] zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki.” (Isa. 26:9) Mpango utafanywa kupitia kwa Ufalme ili kila mtu atakayekuwa duniani asaidiwe sana kibinafsi aijue njia inayofaa ya kuishi. Watiifu wote wataongozwa na Mfalme “kwenye chemchemi za maji yenye uhai.”-—Ufu. 7:17.
5. Ni kwa njia gani serikali zinashindwa kuwapa watu msaada wanaohitaji sasa?
5 Je! watu kwa ujumla wana uangalizi na uongozi huo sasa? Hapana, watu hawasaidiwi sana mmoja mmoja na serikali zao. Ziko sheria za ulinzi na uongozi, zilizotungwa na wanadamu na zinazofikilizwa nao. Lakini watu hawasitawishi utii wa sheria kwa moyo, hawaitii kwa sababu ni ya haki. Serikali zinazidi kudharauliwa kisha adili za watu zinaharibika kwa sababu wenye vyeo vikubwa hawatumii haki, tena wanazoea kutenda watu isivyo haki na kupotoka.
6. Ni uhitaji gani mwingine ulio wa maana sana ambao Ufalme unatimiza?
6 Vilevile, leo tumaini linahitajiwa sana, yaani, tumaini lenye msingi. Mtume Paulo alitaja “tumaini kwa Mungu” ambalo yeye na Wayahudi pia walikuwa nalo, kwamba “kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Tumaini ni tazamio lenye furaha la kupata kitu ambacho mtu anatarajia. Ulimwengu hauna tumaini kubwa la kuwapa walio hai, wala hauna lo lote la kuwapa waliokufa. Ufufuo ndilo tumaini lililo halisi na la pekee kwa wafu. Ndio mpango wa kuwapa nafasi hata wale ambao wametumia vibaya maisha yao wafanye mabadiliko na kupata uzima wa milele. Mamilioni ya watu watafufuliwa chini ya utawala wa ufalme wa Mungu, wapate kujifunza haki na kuishi. Yesu alisema: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka . . . kwa ufufuo.”—Yohana 5:28, 29; Ufu. 20:11-13.
7. Maneno ya Yesu yanayohusu Paradiso yatatimizwaje?
7 Akiwa mmoja wa watu hao, mtenda maovu aliyekufa kando ya Yesu aliahidiwa hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43, ZSB) “Paradiso” maana yake ni “bustani” au “uwanja mkubwa wenye starehe,” kama lile eneo zuri ambalo Mungu alimfanyia Adamu, yule mwanamume mkamilifu, likawa maskani yenye kumfaa. (Mwa. 2:8, 9) Chini ya utawala wa Ufalme dunia nzima itakuwa ‘mahali patukufu pa kuweka miguu’ ya Mungu, napo patampendeza mwanadamu. (Isa. 66:1; 60:13) Zaidi ya hilo, kwa kutawala dunia yake mwenyewe kupitia kwa Ufalme huo, Mungu atahakikisha kwamba mazingira yake yamesawazika vizuri tena, na kufuta mambo ambayo mwanadamu ametokeza karibu miaka 6,000 kwa kufanya jitihada mbaya na kuitumia isivyofaa. Dunia na hali yake ya hewa, majani yake, wanyama wake, na mwanadamu, itasawazishwa iwe na maisha yenye kufurahika—na vyote hivyo vitakuwa na hali yenye kumletea Muumba sifa.—Zab.148.
MSAADA WA KIMWILI, WA ADILI NA WA MOYONI
8. (a) Zaidi ya kuwa na usimamizi wa kifalme, ni utumishi gani mwingine utakaofanywa na wenzi wa Kristo 144,000? (b) Watakuwa makuhani wa namna gani? (Ebr. 4:15)
8 Basi tunaweza kuona kwamba ufalme wa Mungu utatufanyia mambo mengi kuliko yale tunayotazamia kufanyiwa na serikali ya kawaida. Ufalme wa Mungu utatimiza mazuri hayo kwa sababu wafalme wake watakuwa ukuhani wa kimbinguni pia—lakini si utawala wa jamii ya mapadre duniani, wenye kuungamiwa dhambi na kutawala kwa ukali na ushirikina, huku wakilemea sana watu kwa kuwaingiza katika gharama nyingi. Basi, wafalme hao 144,000 wanaitwa “ukuhani wa kifalme,” wakiwa chini ya Kuhani Mkuu wao, Yesu Kristo. (1 Pet. 2:9) Ukuhani huo hautakuwa ukitafuta faida zao wenyewe wala hautatafuta mali, kwa maana watakuwa makuhani wa kimbinguni na waigaji wa Kuhani Mkuu wao, mwenye rehema. Watakuwa na daraka la kusimamia kazi ya kuwapa watu elimu ya kiroho. Wakati huo hakutakuwa na dini zenye udanganyifu duniani, hakutakuwa na matengenezo ya kisiasa yenye kukaza watu, hakutakuwa na wafanya biashara wenye kunyonya watu. Matengenezo hayo yenye kuharibu watu yatakuwa yamekwisha haribiwa yenyewe.—Ufu. 11:18.
9. Matokeo ya huo “ukuhani wa kifalme” yatakuwa nini?
9 Watu watakapokuwa wakifanya maendeleo kiroho, wakitumia kanuni za haki katika maisha yao ya kila siku, watainuliwa na uwezo wa baraza ya mbinguni ya wafalme-makuhani wafikie ukamilifu. Baada ya hapo, mtu hatasema tena kwamba, “lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” (Rum. 7:19) Katika hali ya ukamilifu, kila mwanadamu atakuwa na mamlaka kamili ya kutumia uwezo wake wote na nguvu za akili, naye atakuwa kikweli katika ‘mfano na sura ya Mungu,’ akionyesha utukufu wake. —Mwa. 1:26, 27; Rum. 3:23.
10. Je! huo “ukuhani wa kifalme” utaweza kuharibika thamani, kama ukuhani mbalimbali wa zamani zilizopita? Kwa sababu gani?
10 Tunawezaje kuwa na hakika kwamba tunaweza kuutumaini ufalme huo wa makuhani? Je! baadaye ufalme huo utaharibika thamani yake, kama serikali na ukuhani mbalimbali wa zamani zilizopita? Hapana. Mungu hafanyi jambo bila kuwa na msingi wa haki. “Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chako,” aliandika mtunga zaburi. (Zab. 89:14; Kut. 34:6, 7) Kwa hiyo, alipokuwa akiupanga ‘ukuhani wake wa kifalme,’ alitumia karne nyingi kuchagua washiriki mmoja mmoja wa ukuhani huo, kuwazoeza, kuwajaribu aone wanafaa na kuwakamilisha.
MWANA WA MUNGU WA MBINGUNI AWA MWILI
11. Eleza jinsi maisha ya Mfalme wa Ufalme huo yalivyokuwa mpaka alipokuwa mwanadamu mkamilifu, mtu mzima.
11 Aliye wa kwanza kabisa ndiye Mfalme, Kichwa cha “ukuhani wa kifalme.” Yeye ndiye kiumbe cha kwanza cha Mungu, ‘Mwana pekee’ wa Mungu. (1 Yohana 4:9; Ufu. 3:14) Biblia haisemi po pote kwamba huyo ni sehemu ya uitwao “Utatu,” wala haisemi yumo katika cheo kinacholingana na cha Yehova Mungu. Alimwita Yehova ‘Baba yangu na Mungu wangu.’ (Yohana 20:17) Mwana huyo, Yesu Kristo, alikubali alipokuwa duniani kwamba alikuwa amefurahi kukaa mbinguni pamoja na Baba yake kabla hajawa mwanadamu. (Yohana 8:56-58) Muumba, Yehova Mungu, hakutatizwa kuhamisha uhai wa Mwanawe na kuuingiza katika tumbo la uzazi la msichana bikira jina lake Mariamu. Kwa hiyo, ingawa Yesu alikuwa na Baba wa kimbinguni, alizaliwa na mwanamke akiwa mtoto mkamilifu wa kibinadamu, si mtu wa kiroho wa mbinguni kama alivyokuwa amekuwa. (Gal. 4:4; Luka 1:35) Alikua kabisa, akawa mwanamume mkamilifu—sawa na Adamu mkamilifu, aliyetenda dhambi baadaye na kuzaa wanadamu wote.—Yohana 1:14; 1 Kor. 15:45.
12. Mwendo wa Kristo ulionyeshaje unyenyekevu wake na upendo wa Yehova?
12 Kwa habari ya kushuka kwa Mwana wa Mungu kutoka maisha ya juu ya kiroho awe mwanadamu kwa sababu ya kumnyenyekea sana Baba yake na kupenda wanadamu, Biblia inasema hivi: “Alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.” (Flp. 2:7, 8) Baba alikuwa na upendo mwingi kwa kumtoa Mwanawe hivyo awe dhabihu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
JINSI KUTAABIKA KWA YESU KULIVYOSAIDIA WANADAMU
13. Kwa sababu gani Kristo alihitajiwa apatwe na mateso na kifo?
13 Kwa sababu gani kukawa na uhitaji wa Mwana wa Mungu apatwe na majaribu yote hayo, pamoja na kifo? Kwanza, alipaswa kupatwa nayo ili kutimiza kusudi la Mungu la kuwa na serikali ya Ufalme yenye haki, ya kuonyesha enzi kuu yake. Vilevile, kifo cha Yesu kilihitajiwa kabisa ili wanadamu wote wapate wokovu na uzima. Jinsi gani?
14. (a) Mwendo wa Yesu duniani ulituhakikishia nini kabisa? (b) Mtume Paulo anaelezaje maisha ya Yesu na matokeo yake?
14 Kwanza, mwendo ambao Yesu Kristo alifuata kulingana na mapenzi ya Mungu unatukuza haki ya Mungu na bidii yake nyingi, na kuhakikisha kabisa kwamba dunia itakuwa na serikali isiyotikisika wala isiyoharibika tabia. Unawekea imani yetu msingi imara. Hiyo ni kwa sababu Yesu alipaswa kupatwa na jaribu kali kupita majaribu yote ili astahili kuwa Mfalme na Kuhani Mkuu wa mbinguni. Juu ya jambo hilo, mtume Paulo alisema hivi:
“Yeye, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii; kisha ametajwa na Mungu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki [aliyekuwa kuhani wakati wa Ibrahimu, kabla agano la Torati halijafanywa, naye aliwekwa katika cheo chake moja kwa moja na Mungu]”—Ebr. 5:7-10.
15. Kristo alimpelekea Mungu dua kwa kulia sana na kutoa machozi akitaka kupata nini? (b) Alijifunzaje kutii, nayo matokeo yakawa nini?
15 Yesu aliendeleza kabisa ukamilifu wake. Kusudi lake la ‘kumlilia sana Mungu’ halikuwa kuepuka kufia wanadamu kama dhabihu, bali alikusudia kuepuka kufa kwa sababu ya kumchukiza Mungu kwa tendo lo lote la kutoaminika au kushindwa kwa upande wake. Alitaka ushindi katika mwendo wake. “Alijifunza kutii.” Alikuwa amekuwa mtii mbinguni akiwa chini ya hali zenye kufaa kabisa. Lakini hapa duniani alipatwa na mateso na taabu, hata akapatwa na hali zenye kumvunja nguvu kwa sababu ya kumtii Mungu. Yesu alikuwa mkamilifu na mwenye haki, wala hakuwa na kikosa tangu alipozaliwa, lakini mwishoni mwa mwendo wake alikamilishwa kwa njia tukufu zaidi, akawa ndiye Mfalme-Kuhani wa kweli, mwenye kustahili kabisa, na aliyejaribiwa.
16. Jaribu na mateso ya Yesu duniani yalisaidiaje kuokoa wanadamu?
16 Kujaribiwa kwa Yesu, kutaabika na kufa kwake kulisaidiaje kuokoa wanadamu? Kwa mara nyingine, mtume anajibu hivi:
“Ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake. Na kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.”—Ebr. 2:17, 18.
WANADAMU WALINUNULIWA NA KRI5TO
17-19. (a) Wanadamu walikuwa katika hali gani mbaya? (Rum. 7:14: Zab. 49:6-9) (b) Yesu alikuwaje njia ya kuondolea wanadamu hali yao yenye msiba?
17 Wakati Adamu alipomwasi Mungu, alipata kuwa adui ya Mungu, kwa hiyo akapoteza uzima wake na kufanya wazao wake wazaliwe wakiwa wenye dhambi— wakiwa wameuzwa katika utumwa kwa dhambi na mauti. (Mwa. 3:17-19; Zab. 51:5) Basi, watoto hao hawakuwa watenda dhambi wa makusudi. Wangeweza kukombolewa. (Rum. 8:20) Yesu Kristo, akiwa Kuhani, alipaswa kutoa dhabihu yenye thamani na ubora uliotakiwa ili kulipia dhambi. Hakuna mwana wa Adamu ambaye angeweza kufanya hivyo kwa kutoa pesa, hata kwa kutoa uhai wake—bei ilikuwa juu mno, kwa maana kilichodaiwa ni kitu cha kulingana na Adamu, yaani, uhai mkamilifu wa kibinadamu. Kristo aliutoa “ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote,” uliohitajiwa sana. (1 Tim. 2:5, 6, NW) Alikuja kutimiza mambo yaliyokuwa yamefananishwa mapema na Torati pamoja na dhabihu zake hafifu za wanyama.
18 Maandishi yanaonyesha kwamba Yesu alisema yafuatayo alipomfikia Mungu wakati wa ubatizo wake: “Dhabihu na toleo hukutaka, lakini mwili (mkamilifu wa kibinadamu] uliniwekea tayari; sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo; ndipo niliposema, Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo (yaani, kitabu cha kukunja cha Torati, hasa walichoandikiwa wafalme, kama katika Kumbukumbu la Torati 17:19, 20] nimeandikiwa) niyafanye mapenzi yako, Mungu.”—Ebr. 10:5-7; Zab. 40:7, 8.
19 Kwa hiyo, Mungu amefanya vitu vyote tutakavyopokea, pamoja na matumaini yetu yote, vimtegemee Yesu Kristo. Mambo ambayo Mfalme mkuu huyo amefanya na yale atakayofanya kwa faida yetu yameendelea kuzungumzwa katika makala inayofuata.